United Republic of Tanzania
Parliament of Tanzania
Timu ya Mpira wa Miguu ya Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (Ndugai Boys), Aprili 26, 2019 ilimenyana na Timu ya Baraza la wawakilishi na kutoka sare ya magoli 2 – 2.
Mechi hiyo ilichezwa katika Uwanja wa Jamhuri wa Jijini Dodoma ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 55 ya Mungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Magoli ya Ndugai Boys yalipachikwa na Mhe. Venance Mwamoto na Yona Kirumbi huku kwa upande wa Baraza la Wawakilishi magoli hayo yalifungwa na Mhe. Juma Ally na Mhe. Hamza Hassan.
Akizungumza kuhusu mechi hiyo Waziri Mkuu, Mhe. Kassim Majaliwa ambaye alikuwepo Uwanjani hapo kushuhudia mchezo huo alisema kuwa mechi hiyo ilikuwa nzuri na ni njia mojawapo ya kudumisha muungano.
Pia aliahidi kuwa, mechi kama hiyo itachezwa tena mwakani huko Zanzibar wakati wa maadhimisho ya miaka 56 ya Muungano.
Akizungumza mara baada ya mchezo huo, Spika wa Bunge, Mhe. Job Ndugai aliipongeza Ndugai Boys kwa kucheza vizuri na kwa kuwa waliwabana ipasavyo wapinzani wao.
Kwa upande wake Spika wa Baraza la Wawakilishi, Mhe. Zuberi Ali Maulid aliwapongeza wachezaji wote kwa mchezo mzuri na kusema kuwa wanaisubiria Ndugai Boys katika mchezo mwingine utakaofanyika Zanzibar hapo mwakani.