Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Emmanuel Peter Cherehani (6 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana na Mheshimiwa Naibu Spika wetu. Kwanza nikumshukuru Mwenyezi Mungu Muumba wa Mbingu na Dunia kwa uhai na niendelee kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa fedha nyingi ambazo anatupa hasa kwenye Majimbo yetu. Pia, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa Kassim kwa kazi nzuri aliyoifanya juzi kukimbia na kuwahi kwa wahanga wenzetu waliopata tatizo pale Kagera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, ninampongeze Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri aliyoifanya kwa kutoa mapendekezo kwa kijana wetu Majaliwa aliyeokoa wananchi wenzetu ya kwenda kwenye mafunzo ya Kijeshi ya Uokoaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme tu kidogo kwamba tumekuwa tukiwapa support vijana hasa wanapo - support kwenye matukio mazito kama hayo, ninaiomba Wizara ya Mambo ya Ndani iendelee kutoa mafunzo kwa wavuvi wote nchini hasa walioko kwenye bahari zetu ili wajue namna nzuri ya kuokoa hasa katika kipindi kigumu cha majanga kwenye bahari, mito na maziwa yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijikite kwenye hoja yangu, naendelea ku-declare interest yangu kwenye suala la kilimo. Kilimo chetu bado kinategemea mvua. Mvua leo hii tunakaribia miaka miwili na huu ni mwaka wa tatu tunapata mvua chini ya wastani, kitu ambacho ni hatari sana kwenye uchumi wa Taifa letu. Kwenye taarifa ya Waziri wa fedha Ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, kwanza nimpongeze kwa Bajeti nzuri aliyotupa kwenye kilimo kutoka Bilioni 254 sasa wakulima tumepata kwa mara ya kwanza toka uhuru Bilioni 90, na pointi, hongera sana, sisi kazi yetu tuendelee kukuombea sana kwa Mungu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu kubwa ambayo mimi najikita ni kwenye Kilimo cha Umwagiliaji. Kuna mradi mkubwa sana wa maji kwenye nchi hii wa Ziwa Victoria. Mradi huu unatoka katika Mkoa wa Mwanza eneo la Iherere lakini bomba hili limepita zaidi ya kilometa 245 kwenda Tabora Mjini. Bomba hili linapita Solwa, Misugwi, Kahama, limeenda Shinyanga Mjini, limeenda Kishapu. Sasa hivi limeenda Nzega, Tabora na Igunga lakini tuulizane, bomba hili kote linakopita linapita kwenye mashamba ya wananchi ya wakulima wetu ambao wanategemea mvua, Serikali na Wizara yetu ya Kilimo pamoja na Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali na Wizara yetu ya Kilimo pamoja na Wizara ya Maji wanashindwaje kukaa pamoja kwenye maeneo ambako linapita bomba wakachimba Mabwawa makubwa ya maji wakachepusha maji kupitia kwenye bomba hili. Wakulima wetu walioko Jirani na bomba hili waendeshe kilimo cha umwagiliaji. Leo hii niseme tu hata kwa Ndugu yangu Waziri wa Kilimo pale bomba linapita kwenye barabara nzuri kwenye mbuga ya wakulima wanaolima mpunga lakini ukipita pale unashuhudia kabisa wakulima wa mpunga unakauka hakuna maji, lakini pale limepita bomba kubwa la maji. Kwa nini wananchi hawa wasichimbiwe Mabwawa makubwa ili maji ya umwagiliaji waweze kulima kiangazi, waweze kulima kipindi chochote, leo hii wanategemea mvua? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwenye mpango wako huu hatujaona kujikita kwenye mradi mkubwa wa Mabwawa ya umwagiliaji, maji haya ni mengi sana, lakini wananchi hawa wanaopelekewa maji haya ya kunywa wakati mwingine wanashindwa kulipia bill kwa sababu…

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimependa mchango wa Mheshimiwa Cherehani jirani yangu. Wiki iliyopita nafikiri siku tatu zilizopita, nilichangia kuhusu design ya miradi ya kimkakati katika nchi yetu. Hapa nauona msisitizo mwingine kwamba tunapo-design miradi yetu tuiangalie miradi strategically and comprehensively ili kutibu matatizo mengi zaidi kuliko kutibu tatizo moja. Kwa hivyo tatizo letu la kukosa mvua na kupungua kwa chakula lingeweza kutatuliwa na mradi wa kupeleka maji kutoka Ziwa Victoria, kwa kuweka hata mabomba mawili moja ya maji ambayo yako treated na moja la maji ambayo hayako treated. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante Doktari. Mheshimiwa Cherehani

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante taarifa hii naipokea kwa sababu kweli maeneo haya hata kama ni Kamati ya Wizara ya Maji itakapotembelea maeneo haya nenda pale Solwa kwa Ndugu yangu Mheshimiwa Ahmed, wananchi wale unakuta hata bwawa la kunyweshea mifugo yao hakuna, lakini bomba la maji limepita, nenda pale Kishapu, hakuna hata eneo la kunyweshea, zao la pamba linapokosa mvua linazidi kupukutika na kushuka uzalishaji lakini hakuna bwawa lililochimbwa kwa ajili ya kuchepusha maji haya wananchi waweze kufaidika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nenda pale Msalala kwa Ndugu yangu Mheshimiwa Kassim Idd hakuna Bwawa lolote lililochimbwa kwa ajili ya kunyweshea maji, leo ninaenda Igunga kwa Ndugu yangu Mheshimiwa Ngassa eneo hili lote lilitakiwa liwe na maji, mabwawa yachimbwe yajazwe maji, lakini leo hii hata kwenye tumbaku ambako mwaka huu tuna uzalishaji wa zaidi ya tani 140,000, Serikali na wakulima wetu wanaelekea kupata zaidi ya Bilioni 600 lakini hakuna mabwawa, sasa mbegu zinakauka lakini angalia fedha zinazoingia. Mimi ningeendelea kuiomba Serikali mahali ambako tunakoeleza uzalishaji mkubwa waweke nguvu kuhakikisha Taifa linapata mapato makubwa tuweze kumsaidia Mheshimiwa Rais.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tutamsaidiaje Mheshimiwa Rais? Mheshimiwa Rais anatutafutia fedha, anatupa fedha nyingi lakini fedha nyingi tunashindwaje kuzipeleka mahali ambako tunaweza tukapata fedha? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata mwananchi tu wa kawaida leo anashindwa kulipia bill ya maji kwa sababu hana vyanzo vya kuweza kupata mapato. Madhara yake pamoja na kumpelekea maji ya Ziwa Victoria anaamua kwenda kutafuta maji ya kisima lakini tungempelekea bwawa akalima bustani yake, akalima mahindi yake vizuri, akalima mpunga wake vizuri, tayari pale atauza kwa muda wowote halafu ataenda kulipia bill zake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye tumbaku tunatarajia kuzalisha tumbaku nyingi sana mwaka huu, lakini tunayo changamoto moja na bahati nzuri nimemwona Waziri wangu wa Kilimo na Naibu wako hapa. Tuna mfumo wa makundi ya watu kumi kwenye sekta ya tumbaku. Makundi haya yanafaidisha sana wakulima wazembe lakini pia wakulima waliopo serious na kilimo wanaenda kudumbukia, kwa sababu makundi ya watu kumi mpaka walipe deni lao ndipo waweze kulipwa fedha na wengine. Sasa unakuta kwenye kikundi cha watu kumi kuna wakulima watano wamelaza deni lao. Sasa wanaposhindwa kulipa hawa watano inabidi wawalipie madeni yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwaenyekiti, kwenye Chama cha Ushirika chenye watu 20 watu 15 wamelaza madeni chama kimekufa na hawawezi kukopesheka. Mimi niendelee kushauri kwenye eneo hili, kwa sababu Serikali yetu iko makini na nampongeza Mheshimiwa Waziri yuko vizuri. Tungeomba sasa wakulima wenyewe mmoja mmoja uje utaratibu mzuri waweze kukopeshwa wenyewe kulingana na dhamana zao ili tuweze kuongeza uchumi kwenye maeneo yetu mbalimbali na wakulima waweze kupata mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tuende kwenye Bodi ya Tumbaku. Bodi ya Tumbaku ndiyo inayosimamia uzalishaji wote huu. Uzalishaji ambao ni Mabilioni ya fedha yanaenda kwenye Serikali yetu lakini niombe waendelee kuipelekea fedha. Bodi ya Tumbaku bado ni changamoto, niseme tu hata Mkurugenzi wa Bodi hii ya Tumbaku hana gari. Anasubiria gari inayoenda field ndiyo aje afanye shughuki zake. Niombe bodi hizi za mazao ambazo ziko kwenye mazao ya kimkakati ziweze kupewa fedha za kutosha kuweza kuwa hudumia wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nikuombe radhi sauti yangu sio rafiki kulingana na hali ya hewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa nafasi hii ya pekee ya upendeleo ya kuweza kujadili kwa mara ya kwanza Wizara ya Kilimo. Nimpongeze sana pia Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais wetu Samia Suluhu Hassan, kwa upande wa kilimo ametusaidia sana sisi wakulima. Kwa mara ya kwanza katika nchi ya Tanzania tumeweza wakulima wa pamba kupewa mbegu zenye thamani ya bilioni 16 bure bila kukatwa chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye upande huohuo wa pamba Mheshimiwa Rais ametoa dawa zenye thamani ya za zaidi ya bilioni 36 kwa nchi nzima, mikoa yote, ya zao la pamba bure, haijawahi kutokea. Kwa hiyo, niendelee kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na Naibu Waziri wa Kilimo, pamoja na Makatibu Wakuu na watumishi wote kwa kazi nzuri wanayoitendea nchi yao, wanayowatendea wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimshukuru sana Mrajisi Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Tanzania, Dkt. Benson Ndiege. Kwa mara ya kwanza mwaka jana alipeleka magari saba kwa warajisi wasaidizi wa mikoa, amepeleka pikipiki 135 kwa Maafisa Ushirika. Hii yote ni kwaajili ya kuboresha wakulima, kwaajili ya kuboresha sekta za wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nataka niende moja kwa moja kwenye mchango wangu. Cha kwanza kabisa pamoja na mazuri yote wanayoyafanya Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri na viongozi wote, bado tuna changamoto kwenye Sheria ya Ushirika. Sheria ya Ushirika bado inahitaji marekebisho makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia bajeti ya Mheshimiwa Waziri yote sijaona mahali ambapo anaweza akaileta Sheria ya Ushirika Bungeni iweze kujadiliwa, iweze kupitiwa pamoja na Sera ya Ushirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunajivunia Mheshimiwa Bashe kuwepo pale na umahiri wake wa kazi, lakini bado uwezo wa utendaji wake wa kazi unaweza ukapotea kwa sababu, bado sheria ya ushirika si pana. Tunaomba sana hili suala la ushirika na Sheria ya Ushirika iletwe Bungeni ili tuifanyie marekebisho na tuweze kuiboresha ili iwe na makucha kwa ajili ya kushughulikia wabadhirifu wa fedha na mali za wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ugawaji wa pembejeo kama kwenye bajeti ilivyoandikwa; nataka nijikite kwenye mfumo mzima wa usajili wa wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli, Serikali inajitahidi sana kupeleka mbegu pamoja na dawa, lakini tuna changamoto ya kutowatambua tunaowahudumia. Tunatumia makisio ya tunaowahudumia lakini bado hatujawatambua tunaowahudumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Wizara imetoa pikipiki 6,000 kwaajili ya kwenda kwa wakulima wetu, lakini leo hii ukitaka uwaulize hata maafisa ugani wanahudumia wakulima wangapi hawawezi kukwambia. Mimi nilikuwa nashauri, na hata kwenye bajeti sijaiona; tupate mkakati mzuri wa kuwatambua wakulima, wa kuwajua wakulima mahali walipo na kuhakikisha kwamba mkulima wa Imala Makoye anayelima pamba yuko maeneo gani? Analima eka ngapi? Anazalisha kiasi gani? Pamoja na kwamba, tunapima udongo, lakini suala la kujua na kutambua mahitaji yake ni suala la msingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoa mfano hata sisi kwenye zao la tumbaku, kwenye zao la tumbaku mkulima huwezi kumpelekea bidhaa kama haumtambui. Pembejeo zote zinazotoka kwenye sekta ya tubaku zinakuja zinamlenga mkulima moja kwa moja kwa sababu tayari yuko kwenye usajili; ana namba yake, ana kitambulisho chake na anajua anacholima leo analima nini na anazalisha kiasi gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tukirudi kwenye zao la pamba ndio maana hata pembejeo zinazoenda kwenye zao la pamba matokeo yake tunakutananazo sokoni kwenye magulio kwa sababu, tunawapelekea watu tusiowafahamu. Tumeangalia kwenye bajeti sijaona kitengo ambacho kimeandaa kuwahudumia na kuwezesha bodi za mazao ziweze kuwa na nguvu. Tumeangalia bodi za mazao hazijatengewa fedha, tunaomba suala hili liangaliwe vizuri. Tuna Bodi ya Pamba; Bodi za Pamba, Tumbaku pamoja na Korosho zinafanya kazi nzuri sana, lakini hatuoni fedha gani zinapelekwa kushughulikia kuwezesha hizi bodi za mazao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mfano tosha sisi kwenye upande wa masoko ya tumbaku. Masoko ya tumbaku ili tuweze kupata madaraja classifier ni Mteuzi Mfawidhi wa Bodi ya Tumbaku. Na Mteuzi Mfawidhi wa Bodi ya Tumbaku wakati mwingine hana usafiri wa kwenda sokoni, usafiri anaotumia anabebwa na gari la mnunuzi ambaye wanaenda kushindana kwenye bei ya mkulima, nai atatendewa haki? Sidhani kama mkulima anaweza akapata haki wakati mwenye kutenda haki amepewa lifti na mnunuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba hili suala la fedha na bajeti kwa upande wa bodi zetu za mazao liweze kuimarishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa upande wa Jimbo la Ushetu. Nilitaka nimuombe Mheshimiwa Waziri, upande wa Ushetu tunazalisha sana mazao ya tumbaku, pamba, mahindi, tmpunga, karanga pamoja na dengu. Ningeomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha bajeti yake, kwa sababu Halmashauri ya Ushetu hatuna maghala na hivyo tunapoteza mazao mengi sana kwa sababu ya kukosa maghala na tumeshatenga eneo la zaidi ya ekari 600 kwa ajili ya kujenga maghala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kwa sababu tunazalisha mpunga na tunalisha nchi za mazaiwa makuu, Mkoa mzima wa Shinyanga pia unalishwa na Halmashauri ya Ushetu. Nchi za Kongo zinanunua mazao yao Ushetu, nchi ya Rwanda inanunua mazao yake Ushetu na wenzetu wa Burundi na Uganda wananunua mazao Ushetu. Tunaomba Mheshimiwa Waziri tuletewe maghala katika Halmashauri ya Ushetu, lakini pia tunahitaji eneo la umwagiliaji. Tumetenga zaidi ya ekari 3,500 kwa ajili ya umwagiliaji kwa kilimo cha mpunga. Tunaomba hili Mheshimiwa Waziri atakapokuja aje nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nijikite pia kwenye suala la utafiti. Tuna taasisi ya utafiti wa zao la tumbaku inayoitwa TORITA, sijaona fedha zinazopelekwa kwenye utafiti hasa kwenye upande wa TORITA, inatafiti sana suala la mbegu. Tuna changamoto kubwa sana ya mbegu za zao la tumbaku. Mbegu tunazozitumia kwenye zao la tumbaku wanao-supply ni wanunuzi wenyewe. Sasa tunaomba, kwa sababu tuna taasisi ya utafiti ambayo inasimamia zao la tumbaku, tunaomba fedha ziweze kuelekezwa kwenye taasisi ili mbegu za tumbaku zizalishwe hapa nchini, wakulima wengi wazalishwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa kuingiza kampuni nyingine ya ununuzi wa tumbaku na kuwasha kiwanda cha TLTC. Hili tumpongeze sana Mheshimiwa Waziri, wakulima wetu walikuwa na hali ngumu sana ya wapi wauze tumbaku. Na mwaka huu ameahidi kununua zaidi ya kilo milioni 10, na msimu unaukuja ataongeza kilo milioni 30. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe tu, nchi za wenzetu, kwa mfano Malawi wanazalisha zaidi ya kilo milioni 230 kwa mwaka na bei yao ni kuanzia dola tatu mpaka dola nane. Zimbabwe wanazalisha zaidi ya milioni 200 mpaka milioni 300 na bei yao ni kuanzia dola tatu mpaka dola nane, iweje sisi Tanzania tumekuwa kisiwa? Wastani wetu wa bei ni dola 1.4, umezipanga sana ni dola 2.2. Niombe kwamba, Waziri kupitia Wizara yake ya Kilimo ateuwe wataalamu na Bodi ya Tumbaku waende kwenye nchi za wenzetu hizi ili kuona wanatumia mfumo gani kupanda kutoka dola tatu mpaka dola nane ilhali sisi tunahangaika na wastani wa dola moja? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiendani na gharama za uzalishaji. Gharama za uzalishaji na bei ya pembejeo imepanda kwa kiasi kikubwa sana lakini bei ya tumbaku inazidi kuporomoka. Ningeomba sana hili Mheshimiwa Waziri aliangalie sana kwa sababu bodi zipo na viongozi wa ushirika wapo, waweze kutembelea kwenye nchi jirani waweze kuona wenzetu wanatumia mfumo gani kuweza kupata bei nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa nafasi ya pekee aliyonijalia kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu, pia nimshukuru sana Rais wetu Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi pamoja na Kamati Kuu ya Chama cha Mapinduzi kwa hekima na busara ya pekee kabisa ya kuweza kupeleka jina langu mbele ya wapiga kura wa Ushetu na niwashukuru sana wapiga kura wa Ushetu kwa kutupa kura nyingi za kishindo kwa kuweza kushinda kwa asilimia 96.69. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru sana Kamati kwa mapendekezo haya nilikuwa nayapitia pitia pamoja na ugeni wangu, lakini mimi ni mkulima nina-declare interest yangu na niwashukuru Wabunge wengi kwenye eneo la wakulima wamelijadili kwa mapana na nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu amekuwa dira na mwanga kwenye ushirika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikikumbuka jinsi Waziri Mkuu alivyopambana kuhakikisha ushirika unasimama, ameweza kurudisha mali nyingi za ushirika, amerudisha majengo mengi ya ushirika, amerudisha ginnery nyingi za ushirika, lakini kwenye mpango huu sijaona suala la ushirika linaguswa. Niseme tu kwamba pamoja na Wizara ya Fedha kufanya mambo mazuri, lakini wajikite sana katika kuhakikisha vyama hivi ambavyo vimerudishiwa mali za ushirika viweze kusimama na ginnery zote ziweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya mali zilizorudishwa nikisema upande KNCU mali zote zilirudishwa nimefanya ziara kwenye maeneo hayo nikiwa kama kiongozi wa ushirika, mali nyingi zimerejeshwa lakini zinachakaa kwa sababu zinashindwa kuendelezwa na zinatakiwa ziendelezwe hasa viwanda zipewe fedha, vifufuliwe mazao ya wakulima yanunuliwe. Nimetembelea kiwanda cha KNCU ni kikubwa sana lakini ukienda wakulima wanalia hali ya kahawa yao hainunuliwi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba, katika mapendekezo haya, kwa upande wa Wizara ya Fedha waweze kupeleka fedha kwenye viwanda. Wapeleke fedha kwenye viwanda vya SHIRECU; SHIRECU wanunue pamba; wapeleke fedha Nyanza. Kuna ginnery ambazo ukizikuta ni nzima, zinachohitaji ni kuwa boosted kidogo tu. Mfano, kuna ginnery ya Kasamwa iko vizuri sana, inahitaji ipelekewe fedha, iingizwe kwenye Mpango iweze kufufuliwa, wananchi wa eneo la Kasamwa watauza pamba yao kwa bei nzuri kupitia ushirika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikupe mfano na niipongeze Wizara ya Kilimo mwaka 2019 na mwaka 2020 wameweza kufufua viwanda vitatu; kiwanda cha Chato, Kiwanda cha Mbongwe na Kiwanda cha KOM lilichopo Kahama. Tumeweza kuingia sokoni na Wizara ya Fedha kupitia Benki ya TADB ya Kilimo wamepeleka fedha. Tumeingiza ushindani na tumeweza kununua pamba kwa bei ya shlingi 1,050 hadi shilingi 1,750 kwa wakulima. (Makofi)

Kwa hiyo, naomba ginnery ya Kasamwa, Manawa, Sola, Funze, Luguru, hizi ginnery ziangaliwe kwa jicho la karibu sana, zifufuliwe na wanaushirika waweze kupata faida kubwa, ushindani uongezeke. Ushindani unapoongezeka na watu wakapata bei nzuri, wakulima hawa wataenda kununua cement, mabati, nondo na wataendelea kuchangia mapato ya Serikali kupitia bidhaa hizo na watajenga nyumba nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa zao la Tumbaku, nataka nichangie kidogo kwa sababu nami pia ni mkulima wa Tumbaku. Mwaka 2012/2013 zao hili liliweza kuingiza fedha za kigeni zaidi ya Dola milioni 320 kwenye nchi hii; lakini wataalamu wetu hawa ambao wamesoma na wamesomeshwa na Serikali wameshindwa kulisimamia hili zao na mpaka leo limeshuka hadi kilo milioni 37. Shilingi milioni 420 ukizi-convert kwa leo tulikuwa tunaenda kwenye zaidi shilingi bilioni 700.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa, nikwambie tu, tozo zimekuwa nyingi mpaka zimewakatisha tamaa wanunuzi wetu. Nikikumbuka hata kampuni ya TOTC ilikuwa inanunua kwa zaidi ya vyama 70, ambapo imeondoka na imeacha hawa wakulima hawana mahali pa kuuzia. Sasa naiomba Wizara ya Fedha, kiwanda hiki kipo Morogoro, ni kikubwa sana, kinazalisha na kusaga zaidi ya tani 120,000 kwa mwaka. Toka mwaka juzi, 2019 kimeachwa, kampuni imeshaondoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiki kiwanda kama kingeweza kufanya kazi, Serikali ikaongea na kampuni hii ikaweza kurudi, wakulima hawa wakauza tumbaku zao, soko likapanda, kiwanda kikafanya kazi, ajira zikaongezeka, nina imani hata mazao yetu ya wakulima yanaweza yakanunuliwa vizuri na bei ikaongezeka kwa wakulima wetu. Kwa hiyo, naomba kushauri kwamba tozo zipungue.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hata leo, pamoja na tozo nyingine ambazo zipo, bado upande wa wakulima tumeletewa Withholding Tax ya 2%. Wabunge wote wameongelea suala la pembejeo kwamba lipewe ruzuku na 2% ukiziunganisha kwenye makampuni ambazo zimekatwa, wakulima hawa wamekatwa zaidi ya dola 700 na kitu na hii ndiyo ilikuwa faida ya wakulima. Sasa leo hii bei ya mbolea imepanda. Fedha hizi ambazo wakulima walitakiwa waende kununua mbolea zimekatwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikikueleza, sisi kwenye upande wa wakulima huwa gharama za uendeshaji na gharama za uzalishaji. Sasa haya makato yamekuja katikati ya msimu ambao mkulima anatakiwa achukue fedha yake, haijaingizwa kwenye gharama ya uendeshaji. Mkulima ambaye amefanya kazi miezi kumi na mbili, kilimo kinaanza mwezi wa Saba, halafu soko anakuja kuanza mwezi wa Tano msimu unaokuja; anajiandaa sasa fedha yake na yeye angalau hata shilingi 500,000 aipate kwa mwaka, imekuja kukatwa. Sasa fedha ya kununua mbolea hana na bei imepanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nashauri maeneo haya, wakulima wetu wanateseka sana, hali ni ngumu sana. Fedha hizi zirejeshwe kwa wakulima kwa msimu huu. Hata kama ni makato sasa yanakuja, yaingizwe kwenye utaratibu ambao hata wakulima tutaziingiza kwenye gharama za uzalishaji, tutaziingiza kwenye gharama za uendeshaji, lakini leo hii hazipo kabisa kwenye mjengeko wa bei. Tunaweza tukalalamikia ruzuku lakini matatizo mengine yanasababishwa na wataalamu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara ya Kilimo pamoja na Wizara ya Fedha wakae karibu, wapeane taarifa, watembee njia moja ili kupunguza adha kwa wakulima wetu. Tunahitaji mkulima naye afufuke, alime.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi Mheshimiwa Waziri wa Fedha kuna jambo alilisema na nilimpongeza sana kwamba tuna matajiri wasiopungua 5,000. Sasa hao matajiri tunahitaji pia wawemo humu.

MWENYEKITI: Mabilionea.

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mabilionea 5,000. Sasa tunahitaji mabilionea hawa na wakulima wawemo; wapunguziwe tozo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukirudi kwenye suala la pembejeo, ni kweli zimepanda kwa kiasi kikubwa sana. Sasa pembejeo imepanda, lakini bado tunaenda kuwanyang’anya na kile kidogo walichokusanya wakulima. Dola 708,000 ni zaidi ya shilingi bilioni moja ambazo zimechukuliwa kwa wakulima wetu ambao walitakiwa wanunue cash na msimu umeshaingia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Bunge lako Tukufu, fedha hizi ningerudia kwamba zirejeshwe kwa wakulima, kama ni tozo, basi tujipange kwa msimu ujao tuweze kuwapelekea na tuweze kuwafundisha wakulima wetu na tuwape elimu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekititi, la mwisho, mfumo. Wakulima hawa hatujawaingiza kwenye mfumo wa usajili. Tunalalamika lakini wataalamu wetu wako kule. Wakulima wetu nchi hii wasajiliwe, waingie kwenye mfumo, tuwatambue mmoja mmoja, tujue namna ya kuwahudumia. Tukifanya hivyo hatutateseka. Bila hivyo, tutaendelea kusema kuna Bwana Shamba na Maafisa Kilimo; watambulike kwenye mfumo. Tukifanya hivyo, hata namna ya kuwafikia na kuwajua walipo na wataalamu wetu ambao watalipwa mshahara na Serikali, tutajua kwamba huyu leo amehudumia wakulima wangapi na wako maeneo gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa nafasi hii ya pekee kuendelea kuweza kusimama kwenye Bunge lako hili Tukufu. Pia nikupongeze wewe mwenyewe kwa ushindi mnono ulioupata na namna unavyoliendesha Bunge hili kwa hekima na busara na kutambua nafasi za Wabunge wako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri ya bajeti aliyoitoa. Kwa kweli, iligusa kila mahali, imegusa uhitaji wa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa jinsi anavyoipambania nchi yake, kwa jinsi ambavyo halali anatafuta fedha kwa ajili ya kuhakikisha wananchi wake wanafaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nimpongeze sana kwa upande wa Jimbo la Ushetu, katuletea shilingi 3,200,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya wilaya, katuletea Shilingi 1,590,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa, katuletea Milioni 500 kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Ulewe. Kweli mama anapambana sana. (Makofi)

Mheshimia Spika, Jimbo la Ushetu, liko sehemu ya Wilaya ya Kahama, na Jimbo la Ushetu lina changamoto kubwa sana ya maji. Nikuambie kutoka Ushetu kwenda Kahama ambako mradi mkubwa wa maji wa Ziwa Victoria upo ni kama kilomita 12 tu, lakini wananchi hawa na Kata zao hawana maji kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa ya Ushetu ni maji, pamoja na kazi nzuri wanayoifanya Wizara ya Maji, nakuendelea kuleta watafiti wa maji katika Jimbo la Ushetu, changamoto iliyopo ni maji hayapatikani na wanapochimba wanakutana na vumbi pale chini. Kwa hiyo, ningeomba maji ya Ziwa Victoria yaweze kuletwa kwa wananchi wa Ushetu.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, nadhani unapotoa taarifa utafuata ile miongozo ya taarifa unayoweza kutoa na siyo kwamba unataka kuchangia, Mheshimiwa Iddi Kassim.

T A A R I F A

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante, nataka nimpe taarifa mchangia kwamba mwezi wa kumi mwaka jana Wizara ilitenga kiasi cha Shilingi 99, 225,000 kwa ajili ya upembuzi yakinifu, mpaka sasa tunazungumza ni kwamba bado hata ule mchakato wa kumpata consultant haujakamilika.

SPIKA: Hizo Shilingi Milioni 99 ni kwa ajili ya Jimbo lake la Ushetu?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, la Jimbo la Ushetu.

SPIKA: Mheshimiwa Mbunge wa Ushetu, unapokea taarifa hiyo?

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, taarifa hii naipokea kwa mikono miwili na kwa sababu hiyo, kuna watu walikuja pale kipindi cha nyuma pale baada ya kuuliza sana tukaambiwa kwamba ujazo wa maji ya Ziwa Victoria kwa upande hayawezi kupata uelekeo wa Jimbo la Ushetu, ni jambo la kushangaza, lakini maji hayo ya Ziwa Victoria ambayo yamechukuliwa kutoka Kahama yameenda Nzega, yameenda Tabora, yanaendelea kwenda maeneo mengine zaidi ya kilomita 200, yashindweje kuja kwa wananchi wa Ushetu ambao wanahangaika na kununua maji? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, toka uhuru kuna Kata hazijawahi kupata hata maji ya kisima, mfano Kata ya Bukomela, Kinamapula, Kata ya Ulewe, Kata ya Ubagwe, Kata ya Ulowa, Kata ya Ushetu, Kata ya Mapamba, Kata ya Ukune. Pamoja na hali ngumu ya maisha ya kupanda kwa vitu hawa wananchi wananunua maji dumu moja Shilingi 500. Hebu niambie maji yamepanda bei, mafuta yamepanda bei, mafuta ya kula yamepanda bei, sukari imepanda bei, lakini wananchi hawa bado wanahangaikia maji ya kunywa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningeomba suala hili Serikali ilifanyie kazi kwa udharura wake, wananchi hawa wanapakana sana na vijiji vilivyoko katika Wilaya ya Kahama, katika Jimbo la Kahama Mjini. Maji ya Ziwa Victoria yapo, wanashindwa kupeleka maji ya Ziwa Victoria kwa wananchi hawa waweze kufaidika? Wanashindwaje kufanya upembuzi yakinifu kwa haraka na fedha zipo kwa ajili ya Jimbo la Ushetu na wananchi wake? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakuomba sana hili nakujua uchapakazi wako, Mama Samia namjua uchapakazi wake, Waziri Mkuu namjua uchapakazi wake, Mheshimiwa Waziri wa Maji na Naibu wake pamoja na watumishi wote wa Wizara ya Maji nawajua uchapakazi wao, naomba suala hili walifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Ushetu ni jimbo ambalo pia ni la wakulima kwa kiasi cha asilimia 90, ni kati ya wazalishaji wakubwa sana wa mazao ya mahindi, mpunga pamoja na tumbaku lakini changamoto ni miundombinu.

Mheshimiwa Spika, eneo la Ushetu, lina wafanyabiashara wanaokuja kununua mahindi yao, wananunua mpunga wao hasa katika barabara muhimu sana ambayo tunaomba sana hii barabara itengewe fedha haraka. Barabara inayotoka Masumbwe, kilomita 124.01 inayopita Mwawomba, inayopita Nyankende, inayopita Ulewe, barabara inayopita Ubagwe na inapita Ulowa na inaunganisha Mikoa ya Shinyanga, Geita pamoja na Tabora mpaka eneo la Uyowa. Kwanini barabara hii isianze angalau kutengewa fedha za dharura ifanyiwe matengenezo ya dharura? (Makofi)

MHE NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Nicodemas Maganga.

T A A R I F A

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nataka tu nimpe taarifa mchangiaji kwamba barabara anayoizungumzia, inaunganisha mikoa mitatu, kwa hiyo, ni ya muhimu sana hiyo barabara maana inatoka Masumbwi, Mkoa wa Geita, inakuja Ushetu ambao ni Mkoa wa Shinyanga, inakuja Mkoa wa Tabora. Kwa hiyo, tunaitegemea sana hiyo barabara Serikali ione kila namna iweze kurekebishwa hiyo barabara.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, niwakumbushe tena masharti ya taarifa. Hapa mbele mtaanza kusikia mtu akiaambiwa hiyo siyo taarifa. Mheshimiwa Cherehani, malizia mchango wako.

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, nashukuru lakini pia taarifa hizi ziendelee kuzipokea kwa sababu wananchi hawa sasa tunaelekea kwenye masoko, masoko ya tumbaku, ambapo magari ya wanunuzi wanahitaji watumie hizo barabara kupeleka tumbaku sokoni. Barabara ya kilomita 47 ambayo inatoka Kata ya Ulewe, inapita Kata ya Bulungwa, inaenda moja kwa moja Kahama Mjini maeneo yetu ambapo wakulima wetu wanafanyia masoko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado kuna kilomita 30 zinazotoka Kata ya Ulowa, kupita Kata ya Ushetu mpaka Uyogo. Barabara hizi magari yanaanguka sana ya wananunuzi, inafika mahali wanunuzi hawa wanaongeza gharama za uendeshaji kwa sababu ya magari yao kukaa muda mrefu kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba sana eneo hili barabara hizi muhimu kwa wananchi wa Jimbo la Ushetu na wananchi wote wanaozunguka maeneo hayo ziweze kutengewa fedha za matengenezo ya dharura. Nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuweza kuzipandisha barabara hizi hadhi, kuzipeleka kuwa ni za TANROAD, ziweze sasa kufanyiwa matengenezo ya dharura, maeneo yote ambayo hayapitiki ili wakulima hawa waweze kusafirisha mazao yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la mwisho ambalo nataka nijikite kulichangia ni suala la ushirika. Nimpongeza sana Waziri wa Kilimo kwa kazi nzuri anayoifanya kwenye ushirika. Nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kutoa pikipiki zaidi ya 6,000 kwa Maafisa Ugani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba suala hili tulipe kipaumbele sana hasa kwenye upande wa vyama vya ushirika. Tunahitaji wakulima wetu inapopanda bei ya pamba kwenye soko la dunia, inahitaji pia waweze kufaidika wakulima wetu. Wakati mwingine inapopanda bei ya pamba wanashindwa kufaidika wakulima wetu kwa sababu mara nyingi fedha hizi tunazolipa ziweze kulipwa moja kwa moja kwenye akaunti za wakulima wenyewe badala ya kupeleka kwenye AMCOS. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu fedha zinapopelekwa kwenye AMCOS unakuta mkulima wa pamba ameshapeleka pamba yake, amelipwa, amepewa receipt, lakini mnunuzi anapokuja kupeleka fedha anakuta pamba iko kwenye godauni imejaa, bei imepanda kutoka 1,400 kwenda mpaka 1,700, mfano 1,750 mkulima afaidike na bei hii. Sasa mkulima angelikuwa analipwa kwenye akaunti moja kwa moja, mnunuzi angekuwa anapeleka fedha moja kwenye akaunti ya mkulima. Kwa hiyo, mkulima angekuwa anafaidika sana na kupanda kwa bei. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba suala hili liangaliwe sana, namuamini sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo najua atalifanyia kazi, ninamwamini sana Waheshimiwa Waziri Mkuu najua atalifanyia kazi na nimpongeza tu Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi nzuri alizofanya kwenye ushirika, amefanya kazi nzuri sana, amerudisha mali nyingi sana za ushirika, amerudisha mali nyingi, magodauni mengi, viwanda vingi, ningeoma sasa viwanda hivi viweze kufufuliwa wananchi hawa waweze kufaidika na mali ambazo zimerudishwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu mali hizi zimerudishwa lakini bado hazijaanza kuwafaidisha wana ushirika wetu, kwa sababu bado hati nyingi zimeshikiliwa na benki na ningeomba benki zitumie busara sana, kwa sababu wanashikilia hizi hati kwa sababu vyama vinadaiwa lakini wameshikilia hati sasa vyama vinashindwa kujiendesha vyama vinashindwa kutumia hivi viwanda, kwa hiyo mali zinachakaa sasa kwa nini wasikae chini wakubaliane utaratibu wa kulipa madeni yale halafu viwanda hivi vifufuliwe viendelee kufanya kazi badala ya kuendea kuvizuia matokeo yake mali zinachakaa umeshikilia hati, lakini hivi viwanda vinaendelea kuchoka na kupunguza thamani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba Mheshimiwa Waziri wa Kilimo najua hili analiweza lipo ndani ya uwezo wake afuatilie hivi viwanda vyote ambavyo vimeshikiliwa hati zake na mabenki ili wakae wazungumze namna nzuri ya kuweza kufanyakazi na kuanza kurejesha ile mikopo taratibu huku wakiendelea kufanyakazi huku kuendelea kuimarisha viwanda na wakulima wanaendelea kufaidika na ushirika wao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kukushukuru sana lakini niendelee kurudisha shukrani zangu pia kwa mawaziri wanafanyakazi nzuri sana, naendelea kuunga mkono hoja kwa asilimia 100. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru lakini niendelee kukupongeza kwa nafasi hiyo ya pekee na unaonesha ujasiri mkubwa sana kwamba hatukukosea kukuchagua, hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kibali cha pekee kusimama tena mbele ya Bunge lako Tukufu kwa ajili ya mchango mkubwa sana wa Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwanza kabisa niendelee kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anazowafanyia wananchi wa Ushetu. Nina mwaka mmoja nikiwa Mbunge Bungeni lakini fedha zilizokuja Ushetu kwa mwaka mmoja ni zaidi ya Bilioni 17 zimeletwa na Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye afya tu peke yake tumepokea zaidi ya bilioni 4.9, kwenye Kilimo ndio usiseme bilioni 21 ikiwemo na suala la ruzuku ya pembejeo, lakini kwenye elimu ni zaidi ya bilioni 5.8, ukienda kwenye maji na juzi tumepewa fedha nyingine za BOOST zaidi ya bilioni mbili, lazima tumshukuru Mheshimiwa Rais amefanya kazi kubwa sana. Pia lazima tumshukuru Mheshimiwa Rais hata wakati anaingia madarakani, mfano tu kwenye Benki ya Kilimo (TADB) ilikuwa na mtaji usiopungua bilioni 60 na ndio ilikuwa inawakopesha wakulima, lakini mwaka 2021 Mheshimiwa Rais alipeleka fedha zaidi ya bilioni 208 kwenye Benki ya Kilimo. Benki ya Kilimo hiyo hiyo mwaka 2022 iliweza kupeleka fedha kwa wakulima, kwenye viwanda zaidi ya shilingi bilioni 268, ina maana ni zaidi ya asilimia 102, ni kazi ya Mheshimiwa Rais, ni kazi ya Rais wetu kafanya kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuomba tu, tunaongelea sana wakulima na ni asilimia 60 ya Watanzania wako vijijini wanalima. Niendelee kumpongeza sana Mheshimiwa Rais na Wizara ya Kilimo, lakini tuendelee kuipelekea fedha TADB Benki yetu ya Kilimo kwa sababu inahitaji mtaji mkubwa. Wakulima wengi wako vijijini hawana mitaji hawana mikopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikukumbushe tu kwenye azimio letu la mwaka jana Novemba, 2022, tuliazimia benki hii iwe inapewa bilioni 100 kila mwaka kwa ajili ya kuongeza mtaji wake na kwenye Azimio namba saba, naomba kwa ridhaa yako niweze kusoma kipengele kidogo; “Kwa kuwa pamoja na jitihada za Serikali kuipa kiasi kikubwa cha bilioni
208 mwaka 2021, kuna ahadi ya Serikali ambayo kama ingewezeshwa benki hii ingekuwa na mtaji wa jumla ya bilioni 706.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kukuomba benki hii ipelekewe fedha ili iendelee kuwakopesha wakulima wadogo wadogo, iendelee kukopesha vyama vya ushirika na ndio iliyotoa mfano mkubwa sana kupeleka fedha kwenye vyama vya ushirika. Vyama vingi vya Ushirika mwaka huu vimenunua pamba na vimeleta ushindani sana kwenye nchi yetu. Kwa nini sasa bilioni 100 hii isiendelee kupelekwa kila mwaka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kukuomba Mheshimiwa Mwenyekiti na Bunge lako Tukufu benki hii ipelekewe fedha. Nishukuru sana hata kwenye taarifa ya CAG tumeona na ndio benki iliyofanya vizuri zaidi hata kwenye taarifa za ukaguzi. Kwa hiyo niendelee kuipongeza Menejimenti ya TADB pamoja na Mkurugenzi wake wamefanya kazi kubwa sana, kikubwa tuendelee kuisimamia ili iendelee kuwasaidia sana wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la umeme; Kahama ni mji mkubwa sana na unaokua kwa kasi sana, lakini una changamoto kubwa sana ya umeme pamoja na halmashauri zake, hakuna umeme wa uhakika, unakatikakatika kwa muda wote na ndio mji unaokusanya fedha nyingi pamoja na halmashauri zake Ushetu pamoja na Msalala, lakini ukiambiwa mpaka leo hali ya umeme ni mbaya mno. Hata upande wa REA nikiongelea kwenye Jimbo la Ushetu, kata zangu 10 hazina umeme kabisa wa uhakika, umeme ni wa kusuasua na kinachosikitisha sana ni Mkandarasi, haiwezekani Wilaya ya Kahama yenye halmashauri tatu inapelekewa Mkandarasi mmoja. Mkandarasi huyo huyo awepo Msalala, Mkandarasi huyo huyo aweke Ushetu, Mkandarasi huyo huyo awe Kahama Manispaa, haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Kata yangu ya Mapamba, Ulewe, Ubagwe, Ulowa, Idahina, Chambo, Mpunze, Gulungwa, Nyamilangano pamoja na Bhutibu mpaka tunavyoongea havina hata ile kilometa moja moja, ni kidogo mno, ni maeneo makubwa yamesimamishiwa nguzo tu. Kwa hiyo ningeomba suala hili umeme uende lakini maeneo ambayo miji yake inakua kwa kasi Wakandarasi kwani kuna shida gani ya kupeleka Ushetu kuwa na Mkandarasi wake, Msalala kukawa na Mkandarasi pamoja na Manispaa kukawa na mkandarasi wake. Malalamiko mengine ya wananchi tunayasababisha sisi kwa sababu huwezi kupeleka Mkandarasi mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la TARURA hiyo hiyo Kahama ina Meneja mmoja wa TARURA na Halmashauri zake tatu. Meneja huyo Ofisi yake iko Kahama Manispaa lakini huko huko aende kuzungukia kata 20 za Ushetu na vijiji 112 na vitongoji 560, barabara haziwezi kufunguka. Huyo huyo aende Msalala kwenye kata 18, huyo huyo abaki Mjini kwenye Manispaa ya Kahama kwenye kata 20, Meneja mmoja wa TARURA. Tulikuwa na Meneja wetu kwenye halmashauri zetu, lakini wakaondolewa wakarudishwa makao makuu wakapewa kazi ya ku-survey tu, meneja akabaki mmoja tu, haiwezekani!

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mameneja wetu warudishwe, kama tunahitaji twende vizuri kwenye bajeti zetu za upande wa TAMISEMI, Mameneja hawa warudishwe haraka kwenye halmashauri zetu. Hali ni mbaya na tunavyoongea leo hali ya Ushetu ni mbaya mno. Barabara inayotoka Kata ya Ulewe kufanya mawasiliano na Halmashauri ya Ushetu ili wananchi waende kutibiwa kwenye hospitali yao ya wilaya, hakuna barabara, imekatika, wananchi hawapiti kabisa. Pia Kata ya Ubagwe kwenye Daraja la Ubagwe kuja Ulowa kwenda kwenye Hospitali ya Halmashauri ya Ushetu, hakuna mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Naibu Waziri wa Ujenzi tuambatane naye kesho kwenda kushuhudia adha hii, kwa sababu mwaka jana hili nililisema kwenye bajeti ya Wizara ya Ujenzi kwamba barabara hizi zimeshatoka TARURA zimepelekwa TANROADS, zinahudumiwa na Mkoa, lakini hakuna fedha zilizotengwa za matengenezo. Sisi kama Wabunge tunatakiwa tulie kwa nani, tulalamike kwa nani, tumwambie nani ili tuweze kufikishiwa huduma zetu kwa wananchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasubiri mpaka tatizo litokee, wananchi waende na maji, akinamama wanaoenda kujifungua hospitalini waende na maji, ndio tukimbie sasa na magari yetu kwenda kuona tukio! Naomba niende na Naibu Waziri au Waziri wa Ujenzi akashuhudie kesho adha ambayo leo wanaipata wananchi wangu katika Jimbo la Ushetu. Barabara hazipitiki, naomba mwaka huu zitengewe fedha ili ziweze kutengenezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumzie suala la maliasili; jimbo langu ni kati ya majimbo yanayopakana na mapori mengi. Halmashauri yangu kupitia Baraza la Madiwani tulishakaa tukaomba wafugaji wetu watengewe eneo la malisho. Tumepeleka barua kwenye Ofisi ya Maliasili, tukapeleka barua TAMISEMI watutengee eneo kwa sababu ni maamuzi ya Baraza la Madiwani, lakini tunavyoongea ni mwaka wa pili hajaja hata Waziri kuja kushuhudia kwamba ni eneo gani, ni pori gani angalau walete wataalam litengwe kwa ajili ya malisho kwa sababu ni pori la halmashauri. Wafugaji wetu sasa hakuna mahali pa kuchungia, lakini wafugaji wetu hawa hawa wakiingia kwenye hayo mapori wanakamatwa na wanafilisiwa ng’ombe wao, hatuwezi kulikubali hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri twende tukashuhudie wananchi wangu eneo walilolitenga, angalau watoe ushauri kwamba pamoja na kwamba Baraza la Madiwani limetenga eneo hili, lakini ushauri wetu ulikuwa moja mbili, tatu, lakini hawataki hata kwenda. Naomba kupitia Bunge lako Tukufu, Mheshimiwa Waziri wa Maliasili twende akashuhudie wananchi ambapo wametenga eneo la malisho tuwasaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo naomba niliseme, tuna wananchi wenzetu ambao wanahangaika na mikaa, sijajua kwa nini Wizara ya Maliasili inabaki kupitia TFS kukamata tu wananchi, kukamata sio suluhu. Tumeanza kukamata wananchi hao na kuwaweka na kuwachomea baiskeli, kuchoma mkaa toka uhuru. Hivi hatuna akili ya kubuni kwamba twende na utaratibu gani sasa? Hivi kwa nini Wizara ya Kilimo imekuja na hoja ya kutenga mashamba ya block farm kwa ajili ya wakulima ambao hawana mitaji. Sasa maliasili inashindwaje kutenga maeneo ambayo yatakuwa special kwa wananchi wadogo wadogo ambao wanajishughulisha na biashara ya mkaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu hawa watengewe maeneo wakapande miti ili waweze kuvuna miti yao badala ya kuwakamata. Wamewakamata miaka mingapi toka uhuru, leo miaka 61 tunakamata wamepata nini? Wameacha kuchoma mikaa? Si wako barabarani na baiskeli kila siku. Kwa nini gharama ambayo wanatumia kukimbizana nao kwenye magari wasiitumie sasa kuwa…

MWENYEKITI: Naomba umalizie mchango wako, sekunde tatu.

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe tu, kwanza naunga mkono hoja, lakini niwapongeze sana Wizara ya Fedha kwa kutupelekea fedha nyingi kwenye sehemu ya Kilimo, lakini suala la maliasili na suala la Waziri wa Ujenzi, naomba tuondoke naye akashuhudie hali iliyopo katika Jimbo la Ushetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa moyo wake wa kujitoa kuwatumikia Watanzania.

Pili, naomba nimshukuru Mheshimiwa Waziri wa Maji kwa uzalendo wake wa kusimamia vizuri Wizara ya Maji kwa uwajibikaji uliotukuka.

Mheshimiwa Spika, hoja ya kufikisha maji ya Ziwa Victoria pale Ushetu ni ya msingi sana kwa sababu utaalam umedhihirisha bayana kuwa Ushetu haina chanzo mbadala baada ya jitihada za kuchimba maji chini ya ardhi kushindikana.

Mheshimiwa Spika, suluhisho pekee la kutatua changamoto ya muda mrefu ya ukosefu wa maji kwa wananchi wa Ushetu ni maji ya Ziwa Victoria kutoka bomba la KASHWASA kuanzia Kahama. Kwa kuwa Serikali kupitia Wizara ya Maji tayari imefikisha maji ya Ziwa Victoria kupitia bomba la KASHWASA katika miji ya Ngudu - Kwimba, Muhunze - Kishapu, Kagongwa, Isaka, Nzega, Igunga na sasa maji yatafika Tinde, Shelui - Singida na Miji ya Sikonge na Urambo, hakuna sababu ya msingi ya maji ya KASHWASA kufika Ushetu ambapo kata ya kwanza kufaidi maji hayo ipo kilometa 12 tu kutoka bomba la KASHWASA ikilinganishwa na kilometa nyingi zilizojengwa kwenda maeneo yaliyotajwa.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu iundwe timu maalum ya wataalam wa ndani ikijumuisha RUWASA na KASHWASA ili ifanye tathmini na uchambuzi wa kina kuhusu mradi wa kufikisha maji Ushetu na kusanifu mradi kwa ujumla. Aidha, nashauri ujenzi wa mradi huo ufanye kwa force account kama ilivyofanyika katika miradi mingine mikubwa. Pia nashauri kama hali ya kifedha haitaruhusu kutekeleza mradi wote, ujenzi ufanywe kwa awamu ukianzia na kata iliyo karibu na Kahama.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.