Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Emmanuel Peter Cherehani (15 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana na Mheshimiwa Naibu Spika wetu. Kwanza nikumshukuru Mwenyezi Mungu Muumba wa Mbingu na Dunia kwa uhai na niendelee kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa fedha nyingi ambazo anatupa hasa kwenye Majimbo yetu. Pia, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa Kassim kwa kazi nzuri aliyoifanya juzi kukimbia na kuwahi kwa wahanga wenzetu waliopata tatizo pale Kagera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, ninampongeze Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri aliyoifanya kwa kutoa mapendekezo kwa kijana wetu Majaliwa aliyeokoa wananchi wenzetu ya kwenda kwenye mafunzo ya Kijeshi ya Uokoaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme tu kidogo kwamba tumekuwa tukiwapa support vijana hasa wanapo - support kwenye matukio mazito kama hayo, ninaiomba Wizara ya Mambo ya Ndani iendelee kutoa mafunzo kwa wavuvi wote nchini hasa walioko kwenye bahari zetu ili wajue namna nzuri ya kuokoa hasa katika kipindi kigumu cha majanga kwenye bahari, mito na maziwa yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijikite kwenye hoja yangu, naendelea ku-declare interest yangu kwenye suala la kilimo. Kilimo chetu bado kinategemea mvua. Mvua leo hii tunakaribia miaka miwili na huu ni mwaka wa tatu tunapata mvua chini ya wastani, kitu ambacho ni hatari sana kwenye uchumi wa Taifa letu. Kwenye taarifa ya Waziri wa fedha Ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, kwanza nimpongeze kwa Bajeti nzuri aliyotupa kwenye kilimo kutoka Bilioni 254 sasa wakulima tumepata kwa mara ya kwanza toka uhuru Bilioni 90, na pointi, hongera sana, sisi kazi yetu tuendelee kukuombea sana kwa Mungu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu kubwa ambayo mimi najikita ni kwenye Kilimo cha Umwagiliaji. Kuna mradi mkubwa sana wa maji kwenye nchi hii wa Ziwa Victoria. Mradi huu unatoka katika Mkoa wa Mwanza eneo la Iherere lakini bomba hili limepita zaidi ya kilometa 245 kwenda Tabora Mjini. Bomba hili linapita Solwa, Misugwi, Kahama, limeenda Shinyanga Mjini, limeenda Kishapu. Sasa hivi limeenda Nzega, Tabora na Igunga lakini tuulizane, bomba hili kote linakopita linapita kwenye mashamba ya wananchi ya wakulima wetu ambao wanategemea mvua, Serikali na Wizara yetu ya Kilimo pamoja na Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali na Wizara yetu ya Kilimo pamoja na Wizara ya Maji wanashindwaje kukaa pamoja kwenye maeneo ambako linapita bomba wakachimba Mabwawa makubwa ya maji wakachepusha maji kupitia kwenye bomba hili. Wakulima wetu walioko Jirani na bomba hili waendeshe kilimo cha umwagiliaji. Leo hii niseme tu hata kwa Ndugu yangu Waziri wa Kilimo pale bomba linapita kwenye barabara nzuri kwenye mbuga ya wakulima wanaolima mpunga lakini ukipita pale unashuhudia kabisa wakulima wa mpunga unakauka hakuna maji, lakini pale limepita bomba kubwa la maji. Kwa nini wananchi hawa wasichimbiwe Mabwawa makubwa ili maji ya umwagiliaji waweze kulima kiangazi, waweze kulima kipindi chochote, leo hii wanategemea mvua? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwenye mpango wako huu hatujaona kujikita kwenye mradi mkubwa wa Mabwawa ya umwagiliaji, maji haya ni mengi sana, lakini wananchi hawa wanaopelekewa maji haya ya kunywa wakati mwingine wanashindwa kulipia bill kwa sababu…

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimependa mchango wa Mheshimiwa Cherehani jirani yangu. Wiki iliyopita nafikiri siku tatu zilizopita, nilichangia kuhusu design ya miradi ya kimkakati katika nchi yetu. Hapa nauona msisitizo mwingine kwamba tunapo-design miradi yetu tuiangalie miradi strategically and comprehensively ili kutibu matatizo mengi zaidi kuliko kutibu tatizo moja. Kwa hivyo tatizo letu la kukosa mvua na kupungua kwa chakula lingeweza kutatuliwa na mradi wa kupeleka maji kutoka Ziwa Victoria, kwa kuweka hata mabomba mawili moja ya maji ambayo yako treated na moja la maji ambayo hayako treated. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante Doktari. Mheshimiwa Cherehani

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante taarifa hii naipokea kwa sababu kweli maeneo haya hata kama ni Kamati ya Wizara ya Maji itakapotembelea maeneo haya nenda pale Solwa kwa Ndugu yangu Mheshimiwa Ahmed, wananchi wale unakuta hata bwawa la kunyweshea mifugo yao hakuna, lakini bomba la maji limepita, nenda pale Kishapu, hakuna hata eneo la kunyweshea, zao la pamba linapokosa mvua linazidi kupukutika na kushuka uzalishaji lakini hakuna bwawa lililochimbwa kwa ajili ya kuchepusha maji haya wananchi waweze kufaidika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nenda pale Msalala kwa Ndugu yangu Mheshimiwa Kassim Idd hakuna Bwawa lolote lililochimbwa kwa ajili ya kunyweshea maji, leo ninaenda Igunga kwa Ndugu yangu Mheshimiwa Ngassa eneo hili lote lilitakiwa liwe na maji, mabwawa yachimbwe yajazwe maji, lakini leo hii hata kwenye tumbaku ambako mwaka huu tuna uzalishaji wa zaidi ya tani 140,000, Serikali na wakulima wetu wanaelekea kupata zaidi ya Bilioni 600 lakini hakuna mabwawa, sasa mbegu zinakauka lakini angalia fedha zinazoingia. Mimi ningeendelea kuiomba Serikali mahali ambako tunakoeleza uzalishaji mkubwa waweke nguvu kuhakikisha Taifa linapata mapato makubwa tuweze kumsaidia Mheshimiwa Rais.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tutamsaidiaje Mheshimiwa Rais? Mheshimiwa Rais anatutafutia fedha, anatupa fedha nyingi lakini fedha nyingi tunashindwaje kuzipeleka mahali ambako tunaweza tukapata fedha? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata mwananchi tu wa kawaida leo anashindwa kulipia bill ya maji kwa sababu hana vyanzo vya kuweza kupata mapato. Madhara yake pamoja na kumpelekea maji ya Ziwa Victoria anaamua kwenda kutafuta maji ya kisima lakini tungempelekea bwawa akalima bustani yake, akalima mahindi yake vizuri, akalima mpunga wake vizuri, tayari pale atauza kwa muda wowote halafu ataenda kulipia bill zake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye tumbaku tunatarajia kuzalisha tumbaku nyingi sana mwaka huu, lakini tunayo changamoto moja na bahati nzuri nimemwona Waziri wangu wa Kilimo na Naibu wako hapa. Tuna mfumo wa makundi ya watu kumi kwenye sekta ya tumbaku. Makundi haya yanafaidisha sana wakulima wazembe lakini pia wakulima waliopo serious na kilimo wanaenda kudumbukia, kwa sababu makundi ya watu kumi mpaka walipe deni lao ndipo waweze kulipwa fedha na wengine. Sasa unakuta kwenye kikundi cha watu kumi kuna wakulima watano wamelaza deni lao. Sasa wanaposhindwa kulipa hawa watano inabidi wawalipie madeni yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwaenyekiti, kwenye Chama cha Ushirika chenye watu 20 watu 15 wamelaza madeni chama kimekufa na hawawezi kukopesheka. Mimi niendelee kushauri kwenye eneo hili, kwa sababu Serikali yetu iko makini na nampongeza Mheshimiwa Waziri yuko vizuri. Tungeomba sasa wakulima wenyewe mmoja mmoja uje utaratibu mzuri waweze kukopeshwa wenyewe kulingana na dhamana zao ili tuweze kuongeza uchumi kwenye maeneo yetu mbalimbali na wakulima waweze kupata mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tuende kwenye Bodi ya Tumbaku. Bodi ya Tumbaku ndiyo inayosimamia uzalishaji wote huu. Uzalishaji ambao ni Mabilioni ya fedha yanaenda kwenye Serikali yetu lakini niombe waendelee kuipelekea fedha. Bodi ya Tumbaku bado ni changamoto, niseme tu hata Mkurugenzi wa Bodi hii ya Tumbaku hana gari. Anasubiria gari inayoenda field ndiyo aje afanye shughuki zake. Niombe bodi hizi za mazao ambazo ziko kwenye mazao ya kimkakati ziweze kupewa fedha za kutosha kuweza kuwa hudumia wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nikuombe radhi sauti yangu sio rafiki kulingana na hali ya hewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa nafasi hii ya pekee ya upendeleo ya kuweza kujadili kwa mara ya kwanza Wizara ya Kilimo. Nimpongeze sana pia Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais wetu Samia Suluhu Hassan, kwa upande wa kilimo ametusaidia sana sisi wakulima. Kwa mara ya kwanza katika nchi ya Tanzania tumeweza wakulima wa pamba kupewa mbegu zenye thamani ya bilioni 16 bure bila kukatwa chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye upande huohuo wa pamba Mheshimiwa Rais ametoa dawa zenye thamani ya za zaidi ya bilioni 36 kwa nchi nzima, mikoa yote, ya zao la pamba bure, haijawahi kutokea. Kwa hiyo, niendelee kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na Naibu Waziri wa Kilimo, pamoja na Makatibu Wakuu na watumishi wote kwa kazi nzuri wanayoitendea nchi yao, wanayowatendea wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimshukuru sana Mrajisi Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Tanzania, Dkt. Benson Ndiege. Kwa mara ya kwanza mwaka jana alipeleka magari saba kwa warajisi wasaidizi wa mikoa, amepeleka pikipiki 135 kwa Maafisa Ushirika. Hii yote ni kwaajili ya kuboresha wakulima, kwaajili ya kuboresha sekta za wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nataka niende moja kwa moja kwenye mchango wangu. Cha kwanza kabisa pamoja na mazuri yote wanayoyafanya Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri na viongozi wote, bado tuna changamoto kwenye Sheria ya Ushirika. Sheria ya Ushirika bado inahitaji marekebisho makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia bajeti ya Mheshimiwa Waziri yote sijaona mahali ambapo anaweza akaileta Sheria ya Ushirika Bungeni iweze kujadiliwa, iweze kupitiwa pamoja na Sera ya Ushirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunajivunia Mheshimiwa Bashe kuwepo pale na umahiri wake wa kazi, lakini bado uwezo wa utendaji wake wa kazi unaweza ukapotea kwa sababu, bado sheria ya ushirika si pana. Tunaomba sana hili suala la ushirika na Sheria ya Ushirika iletwe Bungeni ili tuifanyie marekebisho na tuweze kuiboresha ili iwe na makucha kwa ajili ya kushughulikia wabadhirifu wa fedha na mali za wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ugawaji wa pembejeo kama kwenye bajeti ilivyoandikwa; nataka nijikite kwenye mfumo mzima wa usajili wa wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli, Serikali inajitahidi sana kupeleka mbegu pamoja na dawa, lakini tuna changamoto ya kutowatambua tunaowahudumia. Tunatumia makisio ya tunaowahudumia lakini bado hatujawatambua tunaowahudumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Wizara imetoa pikipiki 6,000 kwaajili ya kwenda kwa wakulima wetu, lakini leo hii ukitaka uwaulize hata maafisa ugani wanahudumia wakulima wangapi hawawezi kukwambia. Mimi nilikuwa nashauri, na hata kwenye bajeti sijaiona; tupate mkakati mzuri wa kuwatambua wakulima, wa kuwajua wakulima mahali walipo na kuhakikisha kwamba mkulima wa Imala Makoye anayelima pamba yuko maeneo gani? Analima eka ngapi? Anazalisha kiasi gani? Pamoja na kwamba, tunapima udongo, lakini suala la kujua na kutambua mahitaji yake ni suala la msingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoa mfano hata sisi kwenye zao la tumbaku, kwenye zao la tumbaku mkulima huwezi kumpelekea bidhaa kama haumtambui. Pembejeo zote zinazotoka kwenye sekta ya tubaku zinakuja zinamlenga mkulima moja kwa moja kwa sababu tayari yuko kwenye usajili; ana namba yake, ana kitambulisho chake na anajua anacholima leo analima nini na anazalisha kiasi gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tukirudi kwenye zao la pamba ndio maana hata pembejeo zinazoenda kwenye zao la pamba matokeo yake tunakutananazo sokoni kwenye magulio kwa sababu, tunawapelekea watu tusiowafahamu. Tumeangalia kwenye bajeti sijaona kitengo ambacho kimeandaa kuwahudumia na kuwezesha bodi za mazao ziweze kuwa na nguvu. Tumeangalia bodi za mazao hazijatengewa fedha, tunaomba suala hili liangaliwe vizuri. Tuna Bodi ya Pamba; Bodi za Pamba, Tumbaku pamoja na Korosho zinafanya kazi nzuri sana, lakini hatuoni fedha gani zinapelekwa kushughulikia kuwezesha hizi bodi za mazao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mfano tosha sisi kwenye upande wa masoko ya tumbaku. Masoko ya tumbaku ili tuweze kupata madaraja classifier ni Mteuzi Mfawidhi wa Bodi ya Tumbaku. Na Mteuzi Mfawidhi wa Bodi ya Tumbaku wakati mwingine hana usafiri wa kwenda sokoni, usafiri anaotumia anabebwa na gari la mnunuzi ambaye wanaenda kushindana kwenye bei ya mkulima, nai atatendewa haki? Sidhani kama mkulima anaweza akapata haki wakati mwenye kutenda haki amepewa lifti na mnunuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba hili suala la fedha na bajeti kwa upande wa bodi zetu za mazao liweze kuimarishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa upande wa Jimbo la Ushetu. Nilitaka nimuombe Mheshimiwa Waziri, upande wa Ushetu tunazalisha sana mazao ya tumbaku, pamba, mahindi, tmpunga, karanga pamoja na dengu. Ningeomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha bajeti yake, kwa sababu Halmashauri ya Ushetu hatuna maghala na hivyo tunapoteza mazao mengi sana kwa sababu ya kukosa maghala na tumeshatenga eneo la zaidi ya ekari 600 kwa ajili ya kujenga maghala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kwa sababu tunazalisha mpunga na tunalisha nchi za mazaiwa makuu, Mkoa mzima wa Shinyanga pia unalishwa na Halmashauri ya Ushetu. Nchi za Kongo zinanunua mazao yao Ushetu, nchi ya Rwanda inanunua mazao yake Ushetu na wenzetu wa Burundi na Uganda wananunua mazao Ushetu. Tunaomba Mheshimiwa Waziri tuletewe maghala katika Halmashauri ya Ushetu, lakini pia tunahitaji eneo la umwagiliaji. Tumetenga zaidi ya ekari 3,500 kwa ajili ya umwagiliaji kwa kilimo cha mpunga. Tunaomba hili Mheshimiwa Waziri atakapokuja aje nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nijikite pia kwenye suala la utafiti. Tuna taasisi ya utafiti wa zao la tumbaku inayoitwa TORITA, sijaona fedha zinazopelekwa kwenye utafiti hasa kwenye upande wa TORITA, inatafiti sana suala la mbegu. Tuna changamoto kubwa sana ya mbegu za zao la tumbaku. Mbegu tunazozitumia kwenye zao la tumbaku wanao-supply ni wanunuzi wenyewe. Sasa tunaomba, kwa sababu tuna taasisi ya utafiti ambayo inasimamia zao la tumbaku, tunaomba fedha ziweze kuelekezwa kwenye taasisi ili mbegu za tumbaku zizalishwe hapa nchini, wakulima wengi wazalishwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa kuingiza kampuni nyingine ya ununuzi wa tumbaku na kuwasha kiwanda cha TLTC. Hili tumpongeze sana Mheshimiwa Waziri, wakulima wetu walikuwa na hali ngumu sana ya wapi wauze tumbaku. Na mwaka huu ameahidi kununua zaidi ya kilo milioni 10, na msimu unaukuja ataongeza kilo milioni 30. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe tu, nchi za wenzetu, kwa mfano Malawi wanazalisha zaidi ya kilo milioni 230 kwa mwaka na bei yao ni kuanzia dola tatu mpaka dola nane. Zimbabwe wanazalisha zaidi ya milioni 200 mpaka milioni 300 na bei yao ni kuanzia dola tatu mpaka dola nane, iweje sisi Tanzania tumekuwa kisiwa? Wastani wetu wa bei ni dola 1.4, umezipanga sana ni dola 2.2. Niombe kwamba, Waziri kupitia Wizara yake ya Kilimo ateuwe wataalamu na Bodi ya Tumbaku waende kwenye nchi za wenzetu hizi ili kuona wanatumia mfumo gani kupanda kutoka dola tatu mpaka dola nane ilhali sisi tunahangaika na wastani wa dola moja? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiendani na gharama za uzalishaji. Gharama za uzalishaji na bei ya pembejeo imepanda kwa kiasi kikubwa sana lakini bei ya tumbaku inazidi kuporomoka. Ningeomba sana hili Mheshimiwa Waziri aliangalie sana kwa sababu bodi zipo na viongozi wa ushirika wapo, waweze kutembelea kwenye nchi jirani waweze kuona wenzetu wanatumia mfumo gani kuweza kupata bei nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa nafasi ya pekee aliyonijalia kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu, pia nimshukuru sana Rais wetu Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi pamoja na Kamati Kuu ya Chama cha Mapinduzi kwa hekima na busara ya pekee kabisa ya kuweza kupeleka jina langu mbele ya wapiga kura wa Ushetu na niwashukuru sana wapiga kura wa Ushetu kwa kutupa kura nyingi za kishindo kwa kuweza kushinda kwa asilimia 96.69. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru sana Kamati kwa mapendekezo haya nilikuwa nayapitia pitia pamoja na ugeni wangu, lakini mimi ni mkulima nina-declare interest yangu na niwashukuru Wabunge wengi kwenye eneo la wakulima wamelijadili kwa mapana na nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu amekuwa dira na mwanga kwenye ushirika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikikumbuka jinsi Waziri Mkuu alivyopambana kuhakikisha ushirika unasimama, ameweza kurudisha mali nyingi za ushirika, amerudisha majengo mengi ya ushirika, amerudisha ginnery nyingi za ushirika, lakini kwenye mpango huu sijaona suala la ushirika linaguswa. Niseme tu kwamba pamoja na Wizara ya Fedha kufanya mambo mazuri, lakini wajikite sana katika kuhakikisha vyama hivi ambavyo vimerudishiwa mali za ushirika viweze kusimama na ginnery zote ziweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya mali zilizorudishwa nikisema upande KNCU mali zote zilirudishwa nimefanya ziara kwenye maeneo hayo nikiwa kama kiongozi wa ushirika, mali nyingi zimerejeshwa lakini zinachakaa kwa sababu zinashindwa kuendelezwa na zinatakiwa ziendelezwe hasa viwanda zipewe fedha, vifufuliwe mazao ya wakulima yanunuliwe. Nimetembelea kiwanda cha KNCU ni kikubwa sana lakini ukienda wakulima wanalia hali ya kahawa yao hainunuliwi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba, katika mapendekezo haya, kwa upande wa Wizara ya Fedha waweze kupeleka fedha kwenye viwanda. Wapeleke fedha kwenye viwanda vya SHIRECU; SHIRECU wanunue pamba; wapeleke fedha Nyanza. Kuna ginnery ambazo ukizikuta ni nzima, zinachohitaji ni kuwa boosted kidogo tu. Mfano, kuna ginnery ya Kasamwa iko vizuri sana, inahitaji ipelekewe fedha, iingizwe kwenye Mpango iweze kufufuliwa, wananchi wa eneo la Kasamwa watauza pamba yao kwa bei nzuri kupitia ushirika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikupe mfano na niipongeze Wizara ya Kilimo mwaka 2019 na mwaka 2020 wameweza kufufua viwanda vitatu; kiwanda cha Chato, Kiwanda cha Mbongwe na Kiwanda cha KOM lilichopo Kahama. Tumeweza kuingia sokoni na Wizara ya Fedha kupitia Benki ya TADB ya Kilimo wamepeleka fedha. Tumeingiza ushindani na tumeweza kununua pamba kwa bei ya shlingi 1,050 hadi shilingi 1,750 kwa wakulima. (Makofi)

Kwa hiyo, naomba ginnery ya Kasamwa, Manawa, Sola, Funze, Luguru, hizi ginnery ziangaliwe kwa jicho la karibu sana, zifufuliwe na wanaushirika waweze kupata faida kubwa, ushindani uongezeke. Ushindani unapoongezeka na watu wakapata bei nzuri, wakulima hawa wataenda kununua cement, mabati, nondo na wataendelea kuchangia mapato ya Serikali kupitia bidhaa hizo na watajenga nyumba nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa zao la Tumbaku, nataka nichangie kidogo kwa sababu nami pia ni mkulima wa Tumbaku. Mwaka 2012/2013 zao hili liliweza kuingiza fedha za kigeni zaidi ya Dola milioni 320 kwenye nchi hii; lakini wataalamu wetu hawa ambao wamesoma na wamesomeshwa na Serikali wameshindwa kulisimamia hili zao na mpaka leo limeshuka hadi kilo milioni 37. Shilingi milioni 420 ukizi-convert kwa leo tulikuwa tunaenda kwenye zaidi shilingi bilioni 700.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa, nikwambie tu, tozo zimekuwa nyingi mpaka zimewakatisha tamaa wanunuzi wetu. Nikikumbuka hata kampuni ya TOTC ilikuwa inanunua kwa zaidi ya vyama 70, ambapo imeondoka na imeacha hawa wakulima hawana mahali pa kuuzia. Sasa naiomba Wizara ya Fedha, kiwanda hiki kipo Morogoro, ni kikubwa sana, kinazalisha na kusaga zaidi ya tani 120,000 kwa mwaka. Toka mwaka juzi, 2019 kimeachwa, kampuni imeshaondoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiki kiwanda kama kingeweza kufanya kazi, Serikali ikaongea na kampuni hii ikaweza kurudi, wakulima hawa wakauza tumbaku zao, soko likapanda, kiwanda kikafanya kazi, ajira zikaongezeka, nina imani hata mazao yetu ya wakulima yanaweza yakanunuliwa vizuri na bei ikaongezeka kwa wakulima wetu. Kwa hiyo, naomba kushauri kwamba tozo zipungue.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hata leo, pamoja na tozo nyingine ambazo zipo, bado upande wa wakulima tumeletewa Withholding Tax ya 2%. Wabunge wote wameongelea suala la pembejeo kwamba lipewe ruzuku na 2% ukiziunganisha kwenye makampuni ambazo zimekatwa, wakulima hawa wamekatwa zaidi ya dola 700 na kitu na hii ndiyo ilikuwa faida ya wakulima. Sasa leo hii bei ya mbolea imepanda. Fedha hizi ambazo wakulima walitakiwa waende kununua mbolea zimekatwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikikueleza, sisi kwenye upande wa wakulima huwa gharama za uendeshaji na gharama za uzalishaji. Sasa haya makato yamekuja katikati ya msimu ambao mkulima anatakiwa achukue fedha yake, haijaingizwa kwenye gharama ya uendeshaji. Mkulima ambaye amefanya kazi miezi kumi na mbili, kilimo kinaanza mwezi wa Saba, halafu soko anakuja kuanza mwezi wa Tano msimu unaokuja; anajiandaa sasa fedha yake na yeye angalau hata shilingi 500,000 aipate kwa mwaka, imekuja kukatwa. Sasa fedha ya kununua mbolea hana na bei imepanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nashauri maeneo haya, wakulima wetu wanateseka sana, hali ni ngumu sana. Fedha hizi zirejeshwe kwa wakulima kwa msimu huu. Hata kama ni makato sasa yanakuja, yaingizwe kwenye utaratibu ambao hata wakulima tutaziingiza kwenye gharama za uzalishaji, tutaziingiza kwenye gharama za uendeshaji, lakini leo hii hazipo kabisa kwenye mjengeko wa bei. Tunaweza tukalalamikia ruzuku lakini matatizo mengine yanasababishwa na wataalamu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara ya Kilimo pamoja na Wizara ya Fedha wakae karibu, wapeane taarifa, watembee njia moja ili kupunguza adha kwa wakulima wetu. Tunahitaji mkulima naye afufuke, alime.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi Mheshimiwa Waziri wa Fedha kuna jambo alilisema na nilimpongeza sana kwamba tuna matajiri wasiopungua 5,000. Sasa hao matajiri tunahitaji pia wawemo humu.

MWENYEKITI: Mabilionea.

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mabilionea 5,000. Sasa tunahitaji mabilionea hawa na wakulima wawemo; wapunguziwe tozo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukirudi kwenye suala la pembejeo, ni kweli zimepanda kwa kiasi kikubwa sana. Sasa pembejeo imepanda, lakini bado tunaenda kuwanyang’anya na kile kidogo walichokusanya wakulima. Dola 708,000 ni zaidi ya shilingi bilioni moja ambazo zimechukuliwa kwa wakulima wetu ambao walitakiwa wanunue cash na msimu umeshaingia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Bunge lako Tukufu, fedha hizi ningerudia kwamba zirejeshwe kwa wakulima, kama ni tozo, basi tujipange kwa msimu ujao tuweze kuwapelekea na tuweze kuwafundisha wakulima wetu na tuwape elimu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekititi, la mwisho, mfumo. Wakulima hawa hatujawaingiza kwenye mfumo wa usajili. Tunalalamika lakini wataalamu wetu wako kule. Wakulima wetu nchi hii wasajiliwe, waingie kwenye mfumo, tuwatambue mmoja mmoja, tujue namna ya kuwahudumia. Tukifanya hivyo hatutateseka. Bila hivyo, tutaendelea kusema kuna Bwana Shamba na Maafisa Kilimo; watambulike kwenye mfumo. Tukifanya hivyo, hata namna ya kuwafikia na kuwajua walipo na wataalamu wetu ambao watalipwa mshahara na Serikali, tutajua kwamba huyu leo amehudumia wakulima wangapi na wako maeneo gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa nafasi hii ya pekee kuendelea kuweza kusimama kwenye Bunge lako hili Tukufu. Pia nikupongeze wewe mwenyewe kwa ushindi mnono ulioupata na namna unavyoliendesha Bunge hili kwa hekima na busara na kutambua nafasi za Wabunge wako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri ya bajeti aliyoitoa. Kwa kweli, iligusa kila mahali, imegusa uhitaji wa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa jinsi anavyoipambania nchi yake, kwa jinsi ambavyo halali anatafuta fedha kwa ajili ya kuhakikisha wananchi wake wanafaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nimpongeze sana kwa upande wa Jimbo la Ushetu, katuletea shilingi 3,200,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya wilaya, katuletea Shilingi 1,590,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa, katuletea Milioni 500 kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Ulewe. Kweli mama anapambana sana. (Makofi)

Mheshimia Spika, Jimbo la Ushetu, liko sehemu ya Wilaya ya Kahama, na Jimbo la Ushetu lina changamoto kubwa sana ya maji. Nikuambie kutoka Ushetu kwenda Kahama ambako mradi mkubwa wa maji wa Ziwa Victoria upo ni kama kilomita 12 tu, lakini wananchi hawa na Kata zao hawana maji kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa ya Ushetu ni maji, pamoja na kazi nzuri wanayoifanya Wizara ya Maji, nakuendelea kuleta watafiti wa maji katika Jimbo la Ushetu, changamoto iliyopo ni maji hayapatikani na wanapochimba wanakutana na vumbi pale chini. Kwa hiyo, ningeomba maji ya Ziwa Victoria yaweze kuletwa kwa wananchi wa Ushetu.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, nadhani unapotoa taarifa utafuata ile miongozo ya taarifa unayoweza kutoa na siyo kwamba unataka kuchangia, Mheshimiwa Iddi Kassim.

T A A R I F A

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante, nataka nimpe taarifa mchangia kwamba mwezi wa kumi mwaka jana Wizara ilitenga kiasi cha Shilingi 99, 225,000 kwa ajili ya upembuzi yakinifu, mpaka sasa tunazungumza ni kwamba bado hata ule mchakato wa kumpata consultant haujakamilika.

SPIKA: Hizo Shilingi Milioni 99 ni kwa ajili ya Jimbo lake la Ushetu?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, la Jimbo la Ushetu.

SPIKA: Mheshimiwa Mbunge wa Ushetu, unapokea taarifa hiyo?

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, taarifa hii naipokea kwa mikono miwili na kwa sababu hiyo, kuna watu walikuja pale kipindi cha nyuma pale baada ya kuuliza sana tukaambiwa kwamba ujazo wa maji ya Ziwa Victoria kwa upande hayawezi kupata uelekeo wa Jimbo la Ushetu, ni jambo la kushangaza, lakini maji hayo ya Ziwa Victoria ambayo yamechukuliwa kutoka Kahama yameenda Nzega, yameenda Tabora, yanaendelea kwenda maeneo mengine zaidi ya kilomita 200, yashindweje kuja kwa wananchi wa Ushetu ambao wanahangaika na kununua maji? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, toka uhuru kuna Kata hazijawahi kupata hata maji ya kisima, mfano Kata ya Bukomela, Kinamapula, Kata ya Ulewe, Kata ya Ubagwe, Kata ya Ulowa, Kata ya Ushetu, Kata ya Mapamba, Kata ya Ukune. Pamoja na hali ngumu ya maisha ya kupanda kwa vitu hawa wananchi wananunua maji dumu moja Shilingi 500. Hebu niambie maji yamepanda bei, mafuta yamepanda bei, mafuta ya kula yamepanda bei, sukari imepanda bei, lakini wananchi hawa bado wanahangaikia maji ya kunywa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningeomba suala hili Serikali ilifanyie kazi kwa udharura wake, wananchi hawa wanapakana sana na vijiji vilivyoko katika Wilaya ya Kahama, katika Jimbo la Kahama Mjini. Maji ya Ziwa Victoria yapo, wanashindwa kupeleka maji ya Ziwa Victoria kwa wananchi hawa waweze kufaidika? Wanashindwaje kufanya upembuzi yakinifu kwa haraka na fedha zipo kwa ajili ya Jimbo la Ushetu na wananchi wake? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakuomba sana hili nakujua uchapakazi wako, Mama Samia namjua uchapakazi wake, Waziri Mkuu namjua uchapakazi wake, Mheshimiwa Waziri wa Maji na Naibu wake pamoja na watumishi wote wa Wizara ya Maji nawajua uchapakazi wao, naomba suala hili walifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Ushetu ni jimbo ambalo pia ni la wakulima kwa kiasi cha asilimia 90, ni kati ya wazalishaji wakubwa sana wa mazao ya mahindi, mpunga pamoja na tumbaku lakini changamoto ni miundombinu.

Mheshimiwa Spika, eneo la Ushetu, lina wafanyabiashara wanaokuja kununua mahindi yao, wananunua mpunga wao hasa katika barabara muhimu sana ambayo tunaomba sana hii barabara itengewe fedha haraka. Barabara inayotoka Masumbwe, kilomita 124.01 inayopita Mwawomba, inayopita Nyankende, inayopita Ulewe, barabara inayopita Ubagwe na inapita Ulowa na inaunganisha Mikoa ya Shinyanga, Geita pamoja na Tabora mpaka eneo la Uyowa. Kwanini barabara hii isianze angalau kutengewa fedha za dharura ifanyiwe matengenezo ya dharura? (Makofi)

MHE NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Nicodemas Maganga.

T A A R I F A

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nataka tu nimpe taarifa mchangiaji kwamba barabara anayoizungumzia, inaunganisha mikoa mitatu, kwa hiyo, ni ya muhimu sana hiyo barabara maana inatoka Masumbwi, Mkoa wa Geita, inakuja Ushetu ambao ni Mkoa wa Shinyanga, inakuja Mkoa wa Tabora. Kwa hiyo, tunaitegemea sana hiyo barabara Serikali ione kila namna iweze kurekebishwa hiyo barabara.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, niwakumbushe tena masharti ya taarifa. Hapa mbele mtaanza kusikia mtu akiaambiwa hiyo siyo taarifa. Mheshimiwa Cherehani, malizia mchango wako.

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, nashukuru lakini pia taarifa hizi ziendelee kuzipokea kwa sababu wananchi hawa sasa tunaelekea kwenye masoko, masoko ya tumbaku, ambapo magari ya wanunuzi wanahitaji watumie hizo barabara kupeleka tumbaku sokoni. Barabara ya kilomita 47 ambayo inatoka Kata ya Ulewe, inapita Kata ya Bulungwa, inaenda moja kwa moja Kahama Mjini maeneo yetu ambapo wakulima wetu wanafanyia masoko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado kuna kilomita 30 zinazotoka Kata ya Ulowa, kupita Kata ya Ushetu mpaka Uyogo. Barabara hizi magari yanaanguka sana ya wananunuzi, inafika mahali wanunuzi hawa wanaongeza gharama za uendeshaji kwa sababu ya magari yao kukaa muda mrefu kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba sana eneo hili barabara hizi muhimu kwa wananchi wa Jimbo la Ushetu na wananchi wote wanaozunguka maeneo hayo ziweze kutengewa fedha za matengenezo ya dharura. Nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuweza kuzipandisha barabara hizi hadhi, kuzipeleka kuwa ni za TANROAD, ziweze sasa kufanyiwa matengenezo ya dharura, maeneo yote ambayo hayapitiki ili wakulima hawa waweze kusafirisha mazao yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la mwisho ambalo nataka nijikite kulichangia ni suala la ushirika. Nimpongeza sana Waziri wa Kilimo kwa kazi nzuri anayoifanya kwenye ushirika. Nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kutoa pikipiki zaidi ya 6,000 kwa Maafisa Ugani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba suala hili tulipe kipaumbele sana hasa kwenye upande wa vyama vya ushirika. Tunahitaji wakulima wetu inapopanda bei ya pamba kwenye soko la dunia, inahitaji pia waweze kufaidika wakulima wetu. Wakati mwingine inapopanda bei ya pamba wanashindwa kufaidika wakulima wetu kwa sababu mara nyingi fedha hizi tunazolipa ziweze kulipwa moja kwa moja kwenye akaunti za wakulima wenyewe badala ya kupeleka kwenye AMCOS. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu fedha zinapopelekwa kwenye AMCOS unakuta mkulima wa pamba ameshapeleka pamba yake, amelipwa, amepewa receipt, lakini mnunuzi anapokuja kupeleka fedha anakuta pamba iko kwenye godauni imejaa, bei imepanda kutoka 1,400 kwenda mpaka 1,700, mfano 1,750 mkulima afaidike na bei hii. Sasa mkulima angelikuwa analipwa kwenye akaunti moja kwa moja, mnunuzi angekuwa anapeleka fedha moja kwenye akaunti ya mkulima. Kwa hiyo, mkulima angekuwa anafaidika sana na kupanda kwa bei. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba suala hili liangaliwe sana, namuamini sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo najua atalifanyia kazi, ninamwamini sana Waheshimiwa Waziri Mkuu najua atalifanyia kazi na nimpongeza tu Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi nzuri alizofanya kwenye ushirika, amefanya kazi nzuri sana, amerudisha mali nyingi sana za ushirika, amerudisha mali nyingi, magodauni mengi, viwanda vingi, ningeoma sasa viwanda hivi viweze kufufuliwa wananchi hawa waweze kufaidika na mali ambazo zimerudishwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu mali hizi zimerudishwa lakini bado hazijaanza kuwafaidisha wana ushirika wetu, kwa sababu bado hati nyingi zimeshikiliwa na benki na ningeomba benki zitumie busara sana, kwa sababu wanashikilia hizi hati kwa sababu vyama vinadaiwa lakini wameshikilia hati sasa vyama vinashindwa kujiendesha vyama vinashindwa kutumia hivi viwanda, kwa hiyo mali zinachakaa sasa kwa nini wasikae chini wakubaliane utaratibu wa kulipa madeni yale halafu viwanda hivi vifufuliwe viendelee kufanya kazi badala ya kuendea kuvizuia matokeo yake mali zinachakaa umeshikilia hati, lakini hivi viwanda vinaendelea kuchoka na kupunguza thamani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba Mheshimiwa Waziri wa Kilimo najua hili analiweza lipo ndani ya uwezo wake afuatilie hivi viwanda vyote ambavyo vimeshikiliwa hati zake na mabenki ili wakae wazungumze namna nzuri ya kuweza kufanyakazi na kuanza kurejesha ile mikopo taratibu huku wakiendelea kufanyakazi huku kuendelea kuimarisha viwanda na wakulima wanaendelea kufaidika na ushirika wao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kukushukuru sana lakini niendelee kurudisha shukrani zangu pia kwa mawaziri wanafanyakazi nzuri sana, naendelea kuunga mkono hoja kwa asilimia 100. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa moyo wake wa kujitoa kuwatumikia Watanzania.

Pili, naomba nimshukuru Mheshimiwa Waziri wa Maji kwa uzalendo wake wa kusimamia vizuri Wizara ya Maji kwa uwajibikaji uliotukuka.

Mheshimiwa Spika, hoja ya kufikisha maji ya Ziwa Victoria pale Ushetu ni ya msingi sana kwa sababu utaalam umedhihirisha bayana kuwa Ushetu haina chanzo mbadala baada ya jitihada za kuchimba maji chini ya ardhi kushindikana.

Mheshimiwa Spika, suluhisho pekee la kutatua changamoto ya muda mrefu ya ukosefu wa maji kwa wananchi wa Ushetu ni maji ya Ziwa Victoria kutoka bomba la KASHWASA kuanzia Kahama. Kwa kuwa Serikali kupitia Wizara ya Maji tayari imefikisha maji ya Ziwa Victoria kupitia bomba la KASHWASA katika miji ya Ngudu - Kwimba, Muhunze - Kishapu, Kagongwa, Isaka, Nzega, Igunga na sasa maji yatafika Tinde, Shelui - Singida na Miji ya Sikonge na Urambo, hakuna sababu ya msingi ya maji ya KASHWASA kufika Ushetu ambapo kata ya kwanza kufaidi maji hayo ipo kilometa 12 tu kutoka bomba la KASHWASA ikilinganishwa na kilometa nyingi zilizojengwa kwenda maeneo yaliyotajwa.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu iundwe timu maalum ya wataalam wa ndani ikijumuisha RUWASA na KASHWASA ili ifanye tathmini na uchambuzi wa kina kuhusu mradi wa kufikisha maji Ushetu na kusanifu mradi kwa ujumla. Aidha, nashauri ujenzi wa mradi huo ufanye kwa force account kama ilivyofanyika katika miradi mingine mikubwa. Pia nashauri kama hali ya kifedha haitaruhusu kutekeleza mradi wote, ujenzi ufanywe kwa awamu ukianzia na kata iliyo karibu na Kahama.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru lakini niendelee kukupongeza kwa nafasi hiyo ya pekee na unaonesha ujasiri mkubwa sana kwamba hatukukosea kukuchagua, hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kibali cha pekee kusimama tena mbele ya Bunge lako Tukufu kwa ajili ya mchango mkubwa sana wa Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwanza kabisa niendelee kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anazowafanyia wananchi wa Ushetu. Nina mwaka mmoja nikiwa Mbunge Bungeni lakini fedha zilizokuja Ushetu kwa mwaka mmoja ni zaidi ya Bilioni 17 zimeletwa na Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye afya tu peke yake tumepokea zaidi ya bilioni 4.9, kwenye Kilimo ndio usiseme bilioni 21 ikiwemo na suala la ruzuku ya pembejeo, lakini kwenye elimu ni zaidi ya bilioni 5.8, ukienda kwenye maji na juzi tumepewa fedha nyingine za BOOST zaidi ya bilioni mbili, lazima tumshukuru Mheshimiwa Rais amefanya kazi kubwa sana. Pia lazima tumshukuru Mheshimiwa Rais hata wakati anaingia madarakani, mfano tu kwenye Benki ya Kilimo (TADB) ilikuwa na mtaji usiopungua bilioni 60 na ndio ilikuwa inawakopesha wakulima, lakini mwaka 2021 Mheshimiwa Rais alipeleka fedha zaidi ya bilioni 208 kwenye Benki ya Kilimo. Benki ya Kilimo hiyo hiyo mwaka 2022 iliweza kupeleka fedha kwa wakulima, kwenye viwanda zaidi ya shilingi bilioni 268, ina maana ni zaidi ya asilimia 102, ni kazi ya Mheshimiwa Rais, ni kazi ya Rais wetu kafanya kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuomba tu, tunaongelea sana wakulima na ni asilimia 60 ya Watanzania wako vijijini wanalima. Niendelee kumpongeza sana Mheshimiwa Rais na Wizara ya Kilimo, lakini tuendelee kuipelekea fedha TADB Benki yetu ya Kilimo kwa sababu inahitaji mtaji mkubwa. Wakulima wengi wako vijijini hawana mitaji hawana mikopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikukumbushe tu kwenye azimio letu la mwaka jana Novemba, 2022, tuliazimia benki hii iwe inapewa bilioni 100 kila mwaka kwa ajili ya kuongeza mtaji wake na kwenye Azimio namba saba, naomba kwa ridhaa yako niweze kusoma kipengele kidogo; “Kwa kuwa pamoja na jitihada za Serikali kuipa kiasi kikubwa cha bilioni
208 mwaka 2021, kuna ahadi ya Serikali ambayo kama ingewezeshwa benki hii ingekuwa na mtaji wa jumla ya bilioni 706.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kukuomba benki hii ipelekewe fedha ili iendelee kuwakopesha wakulima wadogo wadogo, iendelee kukopesha vyama vya ushirika na ndio iliyotoa mfano mkubwa sana kupeleka fedha kwenye vyama vya ushirika. Vyama vingi vya Ushirika mwaka huu vimenunua pamba na vimeleta ushindani sana kwenye nchi yetu. Kwa nini sasa bilioni 100 hii isiendelee kupelekwa kila mwaka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kukuomba Mheshimiwa Mwenyekiti na Bunge lako Tukufu benki hii ipelekewe fedha. Nishukuru sana hata kwenye taarifa ya CAG tumeona na ndio benki iliyofanya vizuri zaidi hata kwenye taarifa za ukaguzi. Kwa hiyo niendelee kuipongeza Menejimenti ya TADB pamoja na Mkurugenzi wake wamefanya kazi kubwa sana, kikubwa tuendelee kuisimamia ili iendelee kuwasaidia sana wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la umeme; Kahama ni mji mkubwa sana na unaokua kwa kasi sana, lakini una changamoto kubwa sana ya umeme pamoja na halmashauri zake, hakuna umeme wa uhakika, unakatikakatika kwa muda wote na ndio mji unaokusanya fedha nyingi pamoja na halmashauri zake Ushetu pamoja na Msalala, lakini ukiambiwa mpaka leo hali ya umeme ni mbaya mno. Hata upande wa REA nikiongelea kwenye Jimbo la Ushetu, kata zangu 10 hazina umeme kabisa wa uhakika, umeme ni wa kusuasua na kinachosikitisha sana ni Mkandarasi, haiwezekani Wilaya ya Kahama yenye halmashauri tatu inapelekewa Mkandarasi mmoja. Mkandarasi huyo huyo awepo Msalala, Mkandarasi huyo huyo aweke Ushetu, Mkandarasi huyo huyo awe Kahama Manispaa, haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Kata yangu ya Mapamba, Ulewe, Ubagwe, Ulowa, Idahina, Chambo, Mpunze, Gulungwa, Nyamilangano pamoja na Bhutibu mpaka tunavyoongea havina hata ile kilometa moja moja, ni kidogo mno, ni maeneo makubwa yamesimamishiwa nguzo tu. Kwa hiyo ningeomba suala hili umeme uende lakini maeneo ambayo miji yake inakua kwa kasi Wakandarasi kwani kuna shida gani ya kupeleka Ushetu kuwa na Mkandarasi wake, Msalala kukawa na Mkandarasi pamoja na Manispaa kukawa na mkandarasi wake. Malalamiko mengine ya wananchi tunayasababisha sisi kwa sababu huwezi kupeleka Mkandarasi mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la TARURA hiyo hiyo Kahama ina Meneja mmoja wa TARURA na Halmashauri zake tatu. Meneja huyo Ofisi yake iko Kahama Manispaa lakini huko huko aende kuzungukia kata 20 za Ushetu na vijiji 112 na vitongoji 560, barabara haziwezi kufunguka. Huyo huyo aende Msalala kwenye kata 18, huyo huyo abaki Mjini kwenye Manispaa ya Kahama kwenye kata 20, Meneja mmoja wa TARURA. Tulikuwa na Meneja wetu kwenye halmashauri zetu, lakini wakaondolewa wakarudishwa makao makuu wakapewa kazi ya ku-survey tu, meneja akabaki mmoja tu, haiwezekani!

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mameneja wetu warudishwe, kama tunahitaji twende vizuri kwenye bajeti zetu za upande wa TAMISEMI, Mameneja hawa warudishwe haraka kwenye halmashauri zetu. Hali ni mbaya na tunavyoongea leo hali ya Ushetu ni mbaya mno. Barabara inayotoka Kata ya Ulewe kufanya mawasiliano na Halmashauri ya Ushetu ili wananchi waende kutibiwa kwenye hospitali yao ya wilaya, hakuna barabara, imekatika, wananchi hawapiti kabisa. Pia Kata ya Ubagwe kwenye Daraja la Ubagwe kuja Ulowa kwenda kwenye Hospitali ya Halmashauri ya Ushetu, hakuna mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Naibu Waziri wa Ujenzi tuambatane naye kesho kwenda kushuhudia adha hii, kwa sababu mwaka jana hili nililisema kwenye bajeti ya Wizara ya Ujenzi kwamba barabara hizi zimeshatoka TARURA zimepelekwa TANROADS, zinahudumiwa na Mkoa, lakini hakuna fedha zilizotengwa za matengenezo. Sisi kama Wabunge tunatakiwa tulie kwa nani, tulalamike kwa nani, tumwambie nani ili tuweze kufikishiwa huduma zetu kwa wananchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasubiri mpaka tatizo litokee, wananchi waende na maji, akinamama wanaoenda kujifungua hospitalini waende na maji, ndio tukimbie sasa na magari yetu kwenda kuona tukio! Naomba niende na Naibu Waziri au Waziri wa Ujenzi akashuhudie kesho adha ambayo leo wanaipata wananchi wangu katika Jimbo la Ushetu. Barabara hazipitiki, naomba mwaka huu zitengewe fedha ili ziweze kutengenezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumzie suala la maliasili; jimbo langu ni kati ya majimbo yanayopakana na mapori mengi. Halmashauri yangu kupitia Baraza la Madiwani tulishakaa tukaomba wafugaji wetu watengewe eneo la malisho. Tumepeleka barua kwenye Ofisi ya Maliasili, tukapeleka barua TAMISEMI watutengee eneo kwa sababu ni maamuzi ya Baraza la Madiwani, lakini tunavyoongea ni mwaka wa pili hajaja hata Waziri kuja kushuhudia kwamba ni eneo gani, ni pori gani angalau walete wataalam litengwe kwa ajili ya malisho kwa sababu ni pori la halmashauri. Wafugaji wetu sasa hakuna mahali pa kuchungia, lakini wafugaji wetu hawa hawa wakiingia kwenye hayo mapori wanakamatwa na wanafilisiwa ng’ombe wao, hatuwezi kulikubali hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri twende tukashuhudie wananchi wangu eneo walilolitenga, angalau watoe ushauri kwamba pamoja na kwamba Baraza la Madiwani limetenga eneo hili, lakini ushauri wetu ulikuwa moja mbili, tatu, lakini hawataki hata kwenda. Naomba kupitia Bunge lako Tukufu, Mheshimiwa Waziri wa Maliasili twende akashuhudie wananchi ambapo wametenga eneo la malisho tuwasaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo naomba niliseme, tuna wananchi wenzetu ambao wanahangaika na mikaa, sijajua kwa nini Wizara ya Maliasili inabaki kupitia TFS kukamata tu wananchi, kukamata sio suluhu. Tumeanza kukamata wananchi hao na kuwaweka na kuwachomea baiskeli, kuchoma mkaa toka uhuru. Hivi hatuna akili ya kubuni kwamba twende na utaratibu gani sasa? Hivi kwa nini Wizara ya Kilimo imekuja na hoja ya kutenga mashamba ya block farm kwa ajili ya wakulima ambao hawana mitaji. Sasa maliasili inashindwaje kutenga maeneo ambayo yatakuwa special kwa wananchi wadogo wadogo ambao wanajishughulisha na biashara ya mkaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu hawa watengewe maeneo wakapande miti ili waweze kuvuna miti yao badala ya kuwakamata. Wamewakamata miaka mingapi toka uhuru, leo miaka 61 tunakamata wamepata nini? Wameacha kuchoma mikaa? Si wako barabarani na baiskeli kila siku. Kwa nini gharama ambayo wanatumia kukimbizana nao kwenye magari wasiitumie sasa kuwa…

MWENYEKITI: Naomba umalizie mchango wako, sekunde tatu.

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe tu, kwanza naunga mkono hoja, lakini niwapongeze sana Wizara ya Fedha kwa kutupelekea fedha nyingi kwenye sehemu ya Kilimo, lakini suala la maliasili na suala la Waziri wa Ujenzi, naomba tuondoke naye akashuhudie hali iliyopo katika Jimbo la Ushetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, ahsante nakushukuru sana kwa kweli wewe ni msikivu na unasikiliza sana Wabunge wako.

Mheshimiwa Spika, nilitajka tu nimalizie mchango wangu kwa Mheshimiwa Waziri. Kwanza niendelee kuiomba Wizara ya Maji iangalie visima ambavyo wanachimba nchi nzima waviwekee miundombinu kwa ajili ya kuwafikia wananchi. Kwa mfano ukiangalia kuna Kata ya Masaka ambako ndio kwa mwenyekiti wangu wa kamati, kule kuna visima vizuri kabisa lakini miundombinu haipo.

Mheshimiwa Spika, kuna suala jingine la Mbauti. Miradi mingi ya maji ambayo wanaijenga Wizara ya Maji wanawasahau wafugaji, ningeendelea kuwaomba; ndiyo maana kuna kitu, kama inawezekana hawajagundua Wizara ya Maji, kuna migogoro inakuwa inaibuka kule kwenye miradi mikubwa ya maji. Wafugaji wanazunguka kutafuta maji lakini kwenye kijiji chao kuna miradi mikubwa ya maji.

Mheshimiwa Spika, sasa ningeomba Wizara ya Maji na Wizara ya Mifugo wakae wakubaliane kwenye mradi mkuu wa maji ulipojengwa kuwepo na kitu kinaitwa Mbauti kwa ajili ya kunyweshea wafugaji. Waunganishwe kwenye eneo la mradi wawekewe kama ushirika hivi wawe pamoja halafu wafungiwe na mita yao. Wafugaji hawana shida badala ya kuendelea kuhangaika kuhamahama, wanaondoka kwenye miradi mikubwa ya maji badala yake inaweza kuwasaidia wasiendee kuzunguka kuzurua. Hii kelele wakati mwingine ya wafugaji na wakulima tunaweza tukaipunguza kupitia Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Spika, ningeomba Mheshimiwa Waziri aliangalie hili. Tumeliona hata kipindi cha ziara tulipokuwa kwenye kamati, limekuwa ni kero, wafugaji wanalalamika na madhara yake wanaharibu miundombinu ya maji ambayo ni hatari sana.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri aweke mbauti pale wafungue mita, wajikusanye wao wasajiriwe; tena ifike mbali Mheshimiwa Waziri na Waziri wa Mifugo wawasajiri wale wakulima kama wanavyofanya Wizara zingine. Wale wafugaji wakiwasajiri pale wana uhakika kabisa kwamba watafanya kazi vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, la mwisho ni uvunaji wa maji ya mvua; ningeomba tuwe na center ya uvunaji wa maji ya mvua kwa sababu maeneo mengi maji ya mvua yanapotea. Wakifanya hivyo kelele nyingi za ndugu zetu wakulima tutaziondoa kwa sababu maji yanapotea yanaenda kwenye mto wananchi wanapata shida.

Mheshimiwa Spika, mimi nikushukuru sana naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nina imani kwa sababu ni wa mwisho nitapata hata dakika 15. Cha kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehema kwa nafasi hii ya kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kwa ajili ya kutoa mchango wangu kwenye bajeti kuu ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kwanza niendelee kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa niaba ya wakulima hapa nchini hasa wakulima wa tumbaku, wakulima ambao walifkia hatua ya kukata tamaa. Lakini kwa uwepo wa Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan; wanunuzi walikuwa wameshaondoka nchini; hivi tunavyoongea leo wanunuzi wa tumbaku Tanzania ni wengi. Bei ya tumbaku sasa imepanda kutoka dola 1.4 leo wastani wa bei ya tumbaku inayozunguka kwa wakulima wetu katika mikoa yote inayolima tumbaku ni wastani wa dola 2.5.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kukuomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha, niendelee kukuomba sana wakulima wa tumbaku wanahitaji waione dola 4 kwenye bei yao, wakulima wa tumbaku wanataka waone bei inazidi kuongezeka. Tunaomba uendelee kutupunguzia kodi ambazo zinabana wanunuzi wa tumbaku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Fedha kazi unayoifanya ni nzuri sana, bajeti yako imekaa vizuri, hotuba yako ilishiba vizuri sana. Ombi langu hili; mwaka jana kwenye bajeti nilikuomba sana tuondolee kodi kwenye Hanson cross ili wakulima wa tumbaku waweze kupata faida kubwa. Tuondolee kodi kwenye ushuru wa duty twine ili wakulima wa tumbaku waweze kupata faida kubwa. Waondolee wanunuzi ushuru wa mionzi wanapata shida kubwa sana. Tunahitaji ushuru uendelee kupungua kwa sababu Mheshimiwa Rais anahitaji wakulima waende kulima, wakulima waweze kupata faida kubwa sana. Kwa hiyo niendelee kukupongeza Mheshimiwa Waziri ulianya kazi kubwa sana bajeti yako imeshiba vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kumshukuru Mheshimiwa Rais. Kwenye Jimbo la Ushetu leo tunavyoongea tulikuwa na barabara zetu ambazo zilikuwa hazijafunguka. Mheshimiwa Rais wakati anaingia madarakani tulikuwa na mtandao wa barabara kilometa 400 tu lakini leo mtandao wa barabara katika Jimbo la Ushetu ni zaidi ya kilometa 1029 ni kazi kubwa imefanywa na Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Wilaya ilikuwa haifanyi kazi, leo tumewekewa x-ray tuna vifaa vyote vimejaa, watalamu wetu kwenye Hospitali ya Halmashauri ya Ushetu inafanyika, operation zinafanyika pale pale. Wananchi wa Ushetu sasa hawaendi tena katika Manispaa ya Kahama kazi inafanyika vizuri katika Halmashauri yao ya Ushetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kumwomba tu Mheshimiwa Waziri. Tuliahidiwa Kituo cha Afya Ulowa, Mheshimiwa Waziri Mkuu alipofanya ziara katika Kata ya Ulowa aliahidi ujenzi wa kituo cha afya tangu mwaka 2017, leo miaka zaidi ya mitano hakuna kituo cha afya hakijajengwa, Mheshimiwa Waziri tupelekee fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuiomba Serikali walituahidi kilometa 54 za lami, nashuhudia tu Waheshimiwa Wabunge wenzangu wana-sign mikataba, mikataba inazinduliwa kwenye majimbo ya wenzangu. Mheshimiwa Waziri hebu nipelekee fedha na mimi kwenye kilometa 54, kwenye hii barabara ambayo iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Aliahidi marehemu Magufuli sasa barabara ile bado haijaanza kujengwa. Tuombe basi angalau kwenye bajeti hii tukazindue, tukasaini na wewe uwepo kwenye uzinduzi wa barabara inayotoka Kahama inapita Nyandekwa, inapita Ukune, inapita Kisuke, inapita Nyambilangano inaenda Uyogo inaunganisha mpaka kwenye Jimbo la Kaliua kwa ndugu yangu Mbunge wa Kaliua. Tuwekee na sisi historia kwenye Jimbo la Ushetu tupate angalau hata lami ya kipindi cha utawala wa Mheshimiwa Rais pamoja na wewe ukiwa Waziri wa Fedha ya kuweza kupigia picha wananchi wa Ushetu, tunakuomba sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kumshukuru sana Mheshimiwa Rais mwaka jana ametupa zaidi ya 2,080,000,000 madarasa yamejengwa vizuri; lakini ametupa shule mpya mbili zaidi ya milioni 800 shule zimejengwa na zimeshakamilika zinafanya kazi. Niendelee kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuomba, tuna kilio kwa wakulima wa pamba. Hali ya wakulima wa pamba bei inazidi kuporomoka niendelee kukuomba kuwepo na mfuko wa pembejeo. Kuwepo na mfumo wa kinga ya mazao hasa mazao ya kimkakati kipindi bei ya masoko inapokuwa imetikisika. Leo hii wakulima wa pamba wametumia gharama kubwa kuzalisha zao lao, wamelima pamba nyingi, wamehamasika hasa baada ya kupelekewa mbegu za pamba kwa bei ya ruzuku. Tunaomba sasa, kama mtikisiko wa bei ya pamba inapokuwa mkubwa hivi kwenye mazao yetu ya kimkakati tuwe na maandalizi, tusisubiri mpaka tukio litukute halafu ndipo tuanze maandalizi. Leo hii bei ni 1,060 mpaka inaenda mpaka shilingi 1,000 lakini wakulima wanalia wanasikitika bei ya pamba imeporomoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuombe sasa, kama mwaka mmoja korosho ilishuka bei Serikali yetu iliweka mkakati wa kuzinunua korosho zote na bei iliongezeka na Serikali ikaja kuuza. Mafuta yalipanda bei Mheshimiwa Rais akaamua kuweka bilioni 100 kwa kila mwezi; lakini pembejeo pia mmeweka ruzuku kwa nini sasa mtikisiko huu wa bei msijifungie wataalamu ambao Mheshimiwa Rais akaamini mkaweka ruzuku ili wakulima wetu wa pamba waweze kupata bei nzuri? Kwa sababu wamehamasika kulima pamba vizuri. Sasa wanapopata beii ndogo imeshuka, tunawashusha tena wanashuka chini hawawezi kulima pamba mwakani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niendelee kuomba Mheshimiwa Waziri wa Kilimo kwa sababu uko hapa lichukue hili kwa ajili ya kuweka kinga ya mazao tuwe na mfuko wa kinga ya mazao ya kimkakati tunapoingia kwenye mtikisiko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wa tumbaku wanahitaji kulipwa fedha zao kwa dola. Tunapata taarifa kwamba wakulima wa tumbaku inawezekana wakalipwa shilingi kitu ambacho ni hatari sana. Wakulima kwenye mkataba wetu wa halmashauri ya tumbaku malipo yanafanyika kwa dola, makato ya bei yao wamekatwa kwa dola iweje sasa malipo yaende kwa shilingi? Na Mheshimiwa Waziri wa Fedha wakati anahutubia hapa kwenye mpango wa bajeti yake amesema Serikali ina akiba ya dola zaidi ya 1,177,000…

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali yetu iweje leo dola…

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Emmanuel, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kakoso.

TAARIFA

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru sana kunipa nafasi ya kumpongeza ndugu yangu Cherehani na kutoa taarifa juu ya anachokizungumzia. Zao la tumbaku limekuwa na uhimilivu wa kuuzwa kwa bei nzuri kwa sababu ya makubaliano yado la, pembejeo zinakopwa kwa dola, mauzo yote yanafanyika kwa dola. Sasa tunapofikia hatua ya kutaka kuuza kwa shilingi ni kuwaua wakulima naomba sana dola iendelee kuliko mapendekezo yalivyo kwa sasa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Cherehani, taarifa unaipokea?

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hii kwa sababu wakulima wana matumaini, wana imani kubwa na Mheshimiwa Rais, wana imani kubwa na Waziri wa Kilimo lakini wana imani kubwa na Serikali yao ya Chama cha Mapinduzi. Kwa hivyo tunaomba wakulima wetu wa Tumbaku waendelee kulipwa kwa dola kama utaratibu ambao tumejiwekea kwenye Halmashauri ya Tumbaku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kukuomba, Mheshimiwa Waziri wa Fedha yupo hapa, kuhusu Kahama. Kahama ningeomba tuitenge kuwa lango la biashara kwa Kanda wa Ziwa pamoja na nchi za maziwa makuu kwa sababu ninavyoongea tu mawasiliano katika Manispaa ya Kahama ni makubwa. Nikikutajia tu hapa na wewe unaweza ukajua kwamba kweli Kahama inastahili kuwa lango la kibiashara kwa sababu wakulima wetu na viongozi wetu na wananchi wetu sio lazima waende Kariakoo kuhemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inatakiwa sasa kanda ya ziwa na sisi tuwe na ukanda wetu tutengeneze Kariakoo katika ukanda wa maziwa makuu. Ukiangalia mwaka 2019 Manispaa ya Kahama ilikusanya bilioni saba, mwaka 2021 walikusanya mapato katika Manispaa ya Kahama bilioni 9.6, mwaka 2022 walikusanya bilioni 9.6 na mwaka 2023 Kahama wamekusanya zaidi ya bilioni 10 kwa miaka mitatu Kahama imekusanya zaidi ya bilioni 35. Iweje sasa tusiitenge kuwa ni lango la kibiashara? Kuna eneo limetengwa Dodoma ukienda wafanyabiashara wamejaa pale wengi zaidi ya 1,500. Biashara zilizosajiliwa tu Kahama ni zaidi ya 8,558.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia tu magari ya nchi jirani yanayopita Kahama kwa siku ni zaidi ya 446 mpaka 600, na yanayolala pale Kahama ni zaidi ya magari 200. Kwa nini tusifanye Mji wa Kahama kama lango la kibiashara kwa ukanda wa maziwa makuu ili makusanyo ya kodi na mtandao wa kodi kwenye Serikali yetu uwe mkubwa? Kwa sababu tunaangalia wananchi wengi wanakwenda kuhemea mpaka wafike Kariakoo, mpaka waende Dar es Salaam. Wananchi pia na wafanyabiashara wanaposafiri kwa muda mrefu gharama za uendeshaji inaongezeka na biashara zina bei zao zinaongezeka lakini wanapoishia Ukanda huu wa Kahama, ina maana biashara yetu, wafanyabiashara na wakulima wanaweza wakaendelea na vitu vyao hapa karibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niendelee kukuomba Mheshimiwa Waziri…

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Cherehani, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Tabasam.

TAARIFA

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mchangiaji Mheshimiwa Cherehani kwamba Mji wa Kahama pamoja na biashara kubwa zinazokuwepo pale Kahama sasa hivi wapo maafisa wa TRA ambao si waadilifu na wanadharau mpaka kauli za viongozi wa Taifa kwamba habari ya kudai kodi za miaka mitano nyuma hizo ni kauli za kisiasa. Kahama ndiyo yanayofanyika, wanataka kuuwa ule Mji wa Kahama, naomba uendelee Mheshimiwa Mchangiaji.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Cherehani, taarifa unaipokea?

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa wananchi wa Kahama wanalalamika, wafanyabiashara wanalia na akina mamantilie wanateseka. Na kwa kuwa Rais wetu ni msikivu na Waziri wa Fedha uko hapa, ninaomba tenga muda, kaa na wafanyabiashara wa Kahama wasikilize ni wachangiaji wazuri sana wa mapato ya Serikali. Kama ni madeni yaliyoko kwa wafanyabiashara waiteni mzungumze nao, waiteni muwasikilize, walipe kidogokidogo. Na, nikupongeze juzi ulisema wafanyabiashara wasifungiwe biashara zao, akina mamantilie wasifungiwe biashara zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta mamantilie anauza nyanya, anauza biashara yake ya hoteli anafungiwa anawekewa seal sasa baada ya siku mbili, tatu ndio wanaenda kumfungulia. Hebu niambie zile nyanya zinakuwa na hali gani? Kama ni kanyama ka kuku kale katakuwa na hali gani? itakuwa imeshaharibika mama amekopa kwenye halmashauri, akina mama wamekopa benki. Tunaomba Serikali ipo ilifanyie kazi, biashara Mji wa Kahama uendelee kukua kwa kuwa ni tegemeo kwenye ukanda wa maziwa makuu nchi za maziwa makuu pamoja na mikoa yetu ya Kanda ya Ziwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naunga mkono hoja nishukuru sana Mheshimiwa Mwenyekiti na Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya uhai na kuweza kuendelea kutusimamia na kuendelea kumsaidia Mheshimiwa Rais. Pia nikushukuru sana wewe binafsi kwa jinsi ambavyo unaendesha Bunge kwa hekima kwa busara. Nimshukuru sana vile vile Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa bajeti kubwa ambayo amevunja rekodi kati ya Marais wote waliowahi kuitawala nchi yetu, bajeti yake imejikita sana kuwasaidia wananchi wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kusamehe kodi kwa wafanyabiashara ambao sasa wamepewa wigo mpana wa kuendelea kufanya shughuli zao na kuwahudumia wananchi wetu. Kipekee sana nimshukuru Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu na Naibu wake, niseme kwamba amevunja rekodi hasa kwenye suala la kubana matumizi ya magari na amevunja rekodi kusimamia haya magari. Kwenye hotuba yake kama alivyosema ni kweli unakuta gari nyingi zinazunguka barabarani wakati mabosi wao wamepanda ndege kwenda Dar es Salaam, wamepanda ndege kutoka Dar es Salaam kwenda Bukoba, wamepanda ndege kutoka Bukoba kuja Dodoma, halafu magari sasa yanawafuata kule gharama zake zinakuwa kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa hili, ningeomba sasa fedha hizi ambazo wanaenda kuziokoa, Mheshimiwa Waziri zielekezwe mahospitalini, zielekezwe kuwahudumia akinamama hospitalini. Fedha hizi zikienda hospitalini zitawasaidia sana akinamama wanaoenda kujifungua. Bado akinamama wanaambiwa kwenda na gloves hospitalini, bado akinamama wanaambiwa kwenda kununua dawa zingine, hatujajua na naomba hili niweze kulisema hapa hadharani, akinamama wanapoenda hospitalini wanaandikiwa vitu vingi vya kwenda navyo, sasa tunataka tujue ni vitu gani akinamama wanatakiwa aende navyo, akinamama hao hospitalini wanahangaika sana, akinamama hao hospitalini wanateseka sana. Pia watoto wadogo hopitalini wanapoenda wanateseka sana na kunakuwa na changamoto moja ambayo tunakutana nayo sisi hasa kwenye majimbo ya vijijini ni gharama gani ambapo mama anatakiwa afanye operation ni kiasi gani anatakiwa alipe. Kwa sababu katika maeneo mengi unakuta akinamama wanapofanyiwa operation gharama zinakuwa kubwa, wengine wanafanyiwa operation mpaka kwa 150,000, wengine operation mpaka kwa 400,000, wengine anafanyiwa operation mpaka kwa 500,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna issue ambayo naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha aiangalie vizuri, anafika mama hospitalini anaambiwa apumzike mpaka mfumo ukae sawa, mfumo umegoma, daktari ana-chat na simu, nurse ana-chat na simu, eti kwanza mfumo umegoma, sasa tujiulize ndugu zangu Wabunge tuko hapa, hivi uchungu unasubiri mfumo? Tuambizane hivi mtoto anapotaka kuzaliwa anasubiri mfumo? Ningeomba suala hili Mheshimiwa Waziri aliangalie, akinamama wanateseka, akinamama wanapewa rufaa kwenye hospitali zetu, kwenye zahanati zetu, wanaenda kwenye hospitali za rufaa, kwenye vituo vya afya, mtu anapopewa rufaa hali yake siyo nzuri, anafika pale anaambiwa mfumo haujakaa vizuri. Niombe, akinamama wanapoteza maisha katika hili suala la mfumo, tunaomba tuliangalie, anapofika mama kwa udharura wake ashughulikiwe kwanza wakati mfumo wao wanauandaa badala ya kuambiwa kaa hapo mfumo haujakaa sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati Waziri wa Fedha, Dkt. Gwajima alitangaza suala hili kwamba vifo vinavyotokana na akinamama wajawazito na watoto lazima wajiridhishe Wizara ya Afya, lakini cha ajabu maneno haya yanaishia kwenye mtandao tu, hakuna anayeshuka chini kwenda kulifuatilia hili. Naomba hili suala lifanyiwe kazi hasa katika majimbo ya vijijini, ni changamoto kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia juzi kwenye hotuba ya Waziri wa Fedha, ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ameondoa tozo kwenye vifungashio vya pamba, akaondoa tozo kwenye vifungashio vya korosho, lakini hajaondoa tozo kabisa kwenye vifungashio vya zao la tumbaku, zao ambalo linaingiza fedha nyingi za kigeni hapa nchini. Mwaka huu tu zao la tumbaku pekee fedha ambazo zinakopwa benki ni zaidi ya dola milioni 86 ambazo zinaenda kuwahudumia wakulima na Mheshimiwa Rais ameweka ruzuku, lakini kuna tozo ambazo ziko kwenye vifungashio hasa magunia, kuna asilimia 35 ambayo ni ya import duty, ni gharama kubwa sana kwenye magunia haya ambayo wakulima wanaenda kutumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna VAT 18%, ukiipiga kwa magunia tu kwa bei ya dola 720 kwa pensheni cross inaingia kwenye dola 1146.96 kabla ya gharama za usafirishaji bado gharama za bandarini ukijumlisha gharama yake na gunia inakuwa na bei kubwa sana, lakini magunia haya yanaenda kutumiwa na wakulima wetu, magunia haya wanaenda kufungia tumbaku wakulima wetu na ndiyo wanazitumia wakulima wetu kuvunia tumbaku na mwisho wa siku tumbaku hii ndiyo inayoingiza fedha nyingi za kigeni.

Mimi ningeomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha hili suala la upande wa import duty kwenye magunia yetu vifungashio vya tumbaku viweze kupunguzwa viweze kuondolewa ili wakulima sasa tuwape favour ya kuongeza bei waweze kuona faida kwenye zao la tumbaku. Vile vile kuna tozo ya mionzi, tozo ya mionzi ni 0.2 kwa kilo kwa kila tumbaku inayosafirishwa nje ya nchi, lakini hawa watu mbaya zaidi hawako bandarini ofisi yao iko Arusha, ina maana mtu anaposafirisha tumbaku mpaka wapigiwe simu kutoka Arusha waende Dar es Salaam kutoa kibali, sasa inachelewesha usafirishaji na gharama yake inakuwa kubwa kinachofanyika sasa wanunuzi wanapunguza bei.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nimwombe na nimshauri Mheshimiwa Waziri, tuangalie cha kufanya, tukiondoa hii kodi ya mionzi, tukaamua kuwekeza kwenye mjengeko wa bei, kwanza tukiondoa wanunuzi wataongeza bei, tumbaku yetu inanunuliwa wastani wa dola moja mpaka dola 1.6, lakini wenzetu Nchi za Malawi, Zimbabwe na washindani wetu Zambia, bei yao sasa iko kwenye dola tatu, dola tano mpaka dola nane kwa sababu kodi hizi nyingi wameziondoa. Naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha, kodi hizi aziondoe, halafu aziweke kwenye mjengeko wa bei. Mfano tu kama uzalishaji tukaenda tani 60 mpaka tani 200, tukiweka dola mbili tu kwenye kila kilo, tuna uwezo wa kukusanya zaidi ya dola 800,000 kwa mwaka. Ukibadilisha kwa fedha kwa rate ya leo, tuko kwenye zaidi ya trilioni moja. Sasa hebu tuangalie asilimia 0.2, hatukusanyi fedha nyingi usumbufu kwa wanunuzi, matokeo yake wanunuzi wetu wanaendelea kupunguza uzalishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo linanisikitisha sana, zao la tumbaku linaingiza fedha nyingi sana, lakini juzi Waziri wa Afya amesema anaendelea kupiga marufuku matumizi ya tumbaku Tanzania na ni zao la kimkakati kwenye Serikali yetu. Hata kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi, ukurasa wa 41 linasema Serikali inahakikisha kufikia mwaka 2025, tutatoka kwenye tani 60,000 tutaenda kwenye tani 200,000, sasa tutafikaje kama wakulima tunaendelea kuwachanganya hivi? Waziri anasema anapiga marufuku matumizi ya tumbaku, kwenye ilani inasema inahitaji kuongeza uzalishaji, tuondoke na lipi? Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ambayo sasa ndiyo msahafu wetu wa Chama Cha Mapinduzi unasema tuongeze uzalishaji, lakini wengine tunasema tunapiga marufuku matumizi ya zao la tumbaku, wakulima hawa tunawachanganya na wanunuzi ambao wanaingia kutoka nchi za nje. Hivyo, ningeomba sasa tuangalie wapi ambao tunaweza tukasimama.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho ni riba za benki. Bado riba ya benki kwenye sekta ya tumbaku ni kubwa sana, bado ni asilimia saba kwa dola, ukizibadilisha leo ni zaidi ya asilimia 18 ya riba. Ningeomba mabenki yaendelee kupunguza riba, ni kweli juzi wametangaza ni asilimia tisa lakini asilimia tisa haiwafaidishi wakulima wadogo wadogo bado ni changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine masharti bado hawajayapunguza, unapunguza riba lakini masharti yanakuwa makubwa kwa wakulima wetu. Tungeomba sasa mabenki pamoja na kupunguza riba, wanaendelea kupunguza riba, lakini masharti yaendelee kupunguzwa ili wakulima wadogo wadogo waweze kukopa, wakulima wetu vijijini waweze kukopa, wafanyabiashara wadogo wadogo waweze kukopa na waendelee kufaidika, lakini tunaposema riba imepunguzwa lakini masharti yanaendelea kuwa magumu, haisaidii.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kukushukuru sana, kwa kweli suala la riba ya benki ni changamoto kubwa sana. Naomba sana sekta ya pamba inaingiza fedha nyingi pia na yenyewe naomba kodi zake ziendelee kuondolewa ili wakulima wetu wanaolima pamba waweze kufaidika na pamba. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kuunga mkono hoja, nawapongeza sana Waheshimiwa Mawaziri, wanaupiga mwingi na wanamshauri vizuri Mheshimiwa Rais, Ahsanteni sana, hongereni sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza namshukuru sana Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema kwa nafasi ya pekee ya kuweza kusimama mbele ya Bunge lako tukufu na kuweza kuchangia Wizara ambayo mimi naiita ni uti wa mgongo wa nchi yetu. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan kututeulia Mheshimiwa Bashe kuwa kwenye Wizara hii ya kilimo ambayo wananchi wengi, Watanzania wengi wanaitegemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana kwa kazi kubwa ambayo ameifanya; mawazo yake, amaimarisha wakulima na ushirika kwenye nchi yetu. Mimi niseme tu, mama yetu Samia Suluhu Hassan anafanya kazi kubwa, ametunukiwa udaktari wa heshima. Mheshimiwa Bashe anastahili na yeye atunukiwe udaktari wa heshima kwa kazi kubwa ambayo anaifanya kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia leo hii wananchi wa Ushetu wamekuwa wakipokea mahindi ya kutosha, hawakuhangaika na njaa, lakini wananchi wa Ushetu ambao ni wakulima wazuri sana wa zao la tumbaku wanafurahia masoko yanavyokimbia kwenye mjengeko wetu wa bei. Ukiangalia madaraja ambapo L10F ambayo ilikuwa inauzwa dola 2.9 leo chini ya utawala wa Mheshimiwa Rais na Waziri wetu Bashe ni dola 3.200, wananchi wanachekelea. L10 ambayo ilikuwa ni dola 2.2, leo ina dola 3.1. L1L ambayo ilikuwa ni 2.9 leo ina dola 3.70.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna daraja moja ambalo lilikuwa linapewa dola 0.9 lakini chini ya Utawala wa Mheshimiwa Rais, Comrade Mheshimiwa Bashe na Naibu wake, leo lina dola 3.039. Ni pongezi kubwa kwenye Wizara ya Kilimo na kwa Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi kwa Mheshimiwa Waziri, kwenye hotuba yako umesema Serikali imejipanga kutoa ruzuku ya mbolea kwa mazao yote nchini. Sasa wakulima wa tumbaku wanalalamika, hawapo kwenye ruzuku ya mbolea, hawajapata kwenye ruzuku ya mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima tu kwa msimu huu, mbolea zilizoenda kwa wakulima ni mifuko 802,000 ambapo kwa bei waliyouziwa ni 166,000 kwa mfuko mmoja wa kilo 50. Sasa tumeombe Mheshimiwa Waziri kama wangeuza kwa shilingi wangelipa kwa shilingi 70,000 inamaana wakulima wangebakiwa na bilioni 77 ambazo zingeenda kuwajengea maisha yao, wangeenda kufanya shughuli zao nyingi za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe Mheshimiwa Waziri kwa sababu uchapakazi wako ni mzuri ebu naomba hili muwafikilie hawa wakulima, wakulima hawa wametumia mbolea nyingi, wamechukua fedha nyingi kwenye mabenki ni zaidi ya bilioni 99 zimetumika kwenye kuwapelekea wakulima mbolea. Sasa wasipopata ruzuku pamoja na bei nzuri ya tumbaku bado tutakuwa hatujawasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe Mheshimiwa Waziri, nikuombe sana ndugu yangu na mimi term hii nitajipanga kushika shilingi tusipopata tamko la kuhusu mbolea za ruzuku. Niendelee kukuomba Mheshimiwa Waziri unapokuja na hili njoo wakulima hawa wa tumbaku nini hatma yao kuhusu ruzuku ya mbolea? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile suala jingine ni suala la tija kwenye uzalishaji. Tumekuwa tukishuhudia bajeti inaenda fedha nyingi kwenye eneo la kilimo lakini hatushuhudii nani anaenda kukagua uzalishaji wa tija kwenye mazao yetu. Tuangalie tu, tumekuwa wakaguzi wazuri wa miradi unaona Waziri ameenda kukagua barabara mpaka wakati mwingine wanaenda na nyundo kubomoa zile barabara kwamba haijajengwa vizuri. Tumeona viongozi wanaenda kukagua majengo lakini hatujaona wameenda kukagua uzalishaji wa tija kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie tunajiwekea mikakati kwamba labda zao la pamba tutazalisha kutoka kilo 200 kwa heka moja, tunaenda kilo 800 je, tunapoenda kufunga msimu uzalishaji umefikiwa? Angalia kwenye korosho nchi zote zilizojifunza mazao kwetu nchi ya Vietnam pamoja Ivory Coast wamejifunza uzalishaji kwenye nchi yetu ya Tanzania lakini angalieni wenzetu sasa hivi uzalishaji wao uko juu. Angalia Misri pamoja na Algeria kwenye pamba wanazalisha kilo moja kwa heka moja 800 mpaka 1,500. Uturuki ndiyo inaongoza ambayo ina kilo 1,500 kwa heka moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi pamoja na nguvu zote tunazozitumia bado tuko kwenye uzalishaji wa eka moja kilo 200, bado tuko chini. Tutapeleka fedha nyingi, tutapeleka fedha za kutosha lakini bado tutahitaji wakulima hawa wakaelimishwe namna bora lakini usimamizi uwe mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna wakuu wetu wa Mikoa tuwatumie vizuri Mheshimiwa Waziri nikuombe ebu tenga fungu wakabidhi kazi wakuu wa Mikoa na wakuu wa Wilaya ma-RC wako kule, ma–DC wako kule waende wakasimamie uzalishaji wa tija kwenye nchi yetu. Wakulima wetu walime kidogo wazalishe kwa wingi kwa sababu sasa hivi wanalima eneo kubwa lakini uzalishaji unakuwa ni changamoto. Kwa hiyo, nikuombe kwamba tunapoenda kwenye uzalishaji sasa hivi kuingia kwenye uzalishaji twende tukazalishe kwa tija tuwasaidie wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kumuomba Mheshimiwa Waziri, kwa upande wa wakulima wetu wa tumbaku kwa mwaka huu wana uwezo wa kupata zaidi ya dola milioni 350. Kwa sababu ya soko zuri la tumbaku kama alivyosema Mheshimiwa Almas Maige, ni kazi nzuri ambayo imefanywa. Mheshimiwa Waziri, kazi nzuri ambayo amefanya Mheshimiwa Rais milioni 350 wanazipata wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bodi inayosimamia zao hili halina fedha ni Mkurugenzi pekee ambaye zao lake linalouzwa kwa dola hana gari ya kutembelea. Lakini watumishi mishahara inayolipwa iko chini na wanaenda kuwasimami wanunuzi, makampuni ambayo mishahara yao ni minono sasa mwisho wa siku tunawashawishi kuingia kwenye vishawishi vingine nikuombe Mheshimiwa Waziri, liangalie hili Bodi ya Tumbaku hali ni mbaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bodi ya Tumbaku sasa kwenye masoko wanatumia gari moja na vyama vya ushirika. Mkurugenzi wa Bodi ya Tumbaku asingekaa na wakulima wakaamua kutoa magari kuisaidia bodi leo hii. Kwenye masoko angeendelea mkurugenzi wa bodi, wanunuzi wake na classifier wanakuwa gari moja na wanunuzi wa wanaoenda kuadhibu wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningekuomba Mheshiiwa Waziri hii bodi iangalieni kwa macho mawili, mkisubiri mpaka ichangiwe shilingi 30 kutoka kwa wakulima mtatengeneza mgogoro mwingine. Kwa muda huu nikuombe Mheshimiwa Waziri, kwa sababu ukiangalia bajeti unayotengewa na Mheshimiwa Rais ni kubwa sana nenda kaingalie Bodi ya Tumbaku namna nzuri ambayo utaweza kuisaidia ili inapoenda kusimamia masoko vijana hawa wanapoenda kupambana uzalishaji kama Serikali wakulima tu wanaingiza tu milioni 300 za dola? Nchi inapata shilingi ngapi kama mapato? Ukiangalia halmashauri zetu zinapata bilioni 17 kama halmashauri ushuru lakini sasa hawa wanaosimamia hili zao wana hali gari? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho mimi kwa sababu leo nampongeza tu Mheshimiwa Waziri, vyama vya ushiriki. Nimpongeze sana Mrajisi wa Vyama vya Ushirika Dkt. Benson Ndiege amefanya kazi nzuri. Sasa tunaenda vyama sita vikanunue pamba ningekuomba Mheshimiwa Waziri Simiyu, Nyanza naomba hawa pamoja na Shileku waingizeni kwenye mfumo wa kununua pamba. Tunataka competition iwe kubwa kwa wakulima wetu ushindani uwe mkubwa wakaende kuhudumia wakulima wetu kwa sababu bila vyama vya ushirika, bila muungano hivi hatuwezi angalia Nchi ya Kenya Mheshimiwa Waziri na Mwenyekiti wamekuja kujifunzia pia ushirika kwetu kwenye upande wa mikopo lakini angalia leo benki kubwa ambayo iko Kenya ni benki ya ushirika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ningekuomba Mheshimiwa Waziri, haya yanaangalie kwa mapana sana haswa suala la tija, tuongeze tija tuondokane, sasa kilo kwa kuzalisha eka moja kilo 200 basi twende kwenye kilo 800 mpaka 1,500 mkulima analima kidogo eneo dogo anazalisha kwa wingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana, ninaunga mkono hoja lakini suala la ruzuku ya mbolea kwa wakulima wa tumbaku hili ndilo linanifanya leo nikamate shilingi ya Waziri. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana wewe kwa kazi nzuri unazozifanya na kutusaidia sisi Wabunge wako lakini pia nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ambazo anazifanya kwenye Wizara ya Maji. Nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wake Pamoja na Makatibu Wakuu mmekuwa wasikivu sana. Kwa kweli tuwapongeze kwa dhati kabisa kutoka kwenye mioyo yetu.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tumpongeze sana Engineer Clement Kavigelo anafanya kazi nzuri; ndiye anaye-design miradi mikubwa ya maji hapa nchini, anafanya kazi nzuri sana. Kuna siku moja Wabunge walisema kwamba Chifu wa TARURA anastahili tuzo na huyu kijana anastahili tuzo, anafanya kazi kubwa, nina Imani kila Mbunge amemgusa.

Mheshimiwa Spika, mimi nijikite pia kwenye miradi yangu. Nishukuru sana, Mheshimiwa Waziri amenipatia fedha kwenye Kata yangu ya Chona Kijiji cha Itumbili milioni 500, mradi wa maji unaendelea vizuri. lakini pia umenipa fedha 1,200,000,000 Kata ya Sabasabini, mradi wa maji unaendelea vizuri na wananchi wanakunywa maji.

Ombi langu, niendele kukuomba Mheshimiwa Waziri, kuna vijiji ambavyo vinazunguka maradi wa maji ambavyo vinahitaji kupatiwa maji. Kwa mfano Kijiji cha Bungungu kiko jirani na tenki la maji lakini hakina maji. Kuna Kijiji cha Lusonzo nacho kipo jirani na tenki la maji lakini hakina maji. Niendelee kukuomba Mheshimiwa Waziri kwamba wananchi hawa tuwasaidie. Hawa ni walinzi wa miradi yetu, tu sipowasaidia maji madhara yake nina imani Mheshimiwa Waziri wewe mwenyewe ni shahidi, yanaweza ikawa makubwa sana.

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna Kata yangu ya Igwamanoni na kwenyewe kuna mradi wa milioni 450 umenipatia maji, wananchi wa Igwamanoni Pamoja na Ilamba wanakunywa. Lakini kuna vijiji vyake ambavyo havipati maji kabisa, viko pale. Kijiji changu cha Kipangu na Nyakashagala, Kitongo pamoja na Luhaga bado havijapatiwa maji. Sasa faida ya mradi huu wa maji bado haujawafikia wananchi kwenye kata kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Spika, lakini kubwa sana, Mheshimiwa Waziri wewe mweyewe ni shahidi, hali ya Ushetu ni mbaya sana. Zaidi ya kata 11 mmepeleka magari ya kuchimba; nimpongeze sana Menaja wa RUWUSA Mkoa wa Shinyanga ndugu yangu Julieth, amepeleka magari yeye mwenyewe ni shahidi; lakini kinachokutana pale hakuna maji. Kata ya Ulowa ambayo ina wakazi zaidi ya 35,000 hakuna maji. Kuna Kata za Ubagwe, K Ulewe, Uyogo, Bukomela, Kinamapula, Mapamba, Ushetu pamoja na Chona ambako pia anatoka Mwenyekiti wangu wa Mkoa wa Chama Cha Mapinduzi, hakuna maji. Mheshimiwa Waziri hata kile kisima cha pump angalau tungelikuwa angalau na visima vya pump navyo hakuna kwa sababu maji hakuna kabisa. Kwa hiyo ningekuomba Mheshimiwa Waziri unapokuja kuhitimisha naomba nijue hatma ya wananchi wangu wa Jimbo la Ushetu.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze, juzi alinitumia wataalamu wake wa RUWASA pamoja na KASHIWASA wameenda ku-design mradi wa Ziwa Victoria ambapo umechelewa kwa muda mrefu kwa wananchi wa Ushetu. Ulitakiwa uwe umeshafika muda mrefu, niombe Mheshimiwa Waziri aandike historia kwa wananchi wa Ushetu; ni kilomita 20 tu kutoka Kahama Mjini. Pia kuna Kata ya Igunda pamoja na kata ya Ukune, hizo ni kilomita saba kwa wananchi wanaokunywa maji ya Ziwa Victoria wao hawana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ni kipindi ambacho kama Mbunge napata wakati mgumu sana, na Mheshimiwa Waziri ni Mbunge mwenzangu anajua hali. Majimbo sita ya Mkoa wa Shinyanga, Jimbo la Ushetu tu peke yake ambalo halina mradi wa Ziwa Victoria, kata 11 hata visima vya pump hakuna, vinateseka, vinahangaika. Mradi wa maji wa Nyamilangano kidogo kidogo uliozinduliwa na Mwenge mwaka jana, ambao ulitumia Zaidi ya milioni kama 700, kidogo inasaidia, ambao tunaomba na wenyewe upanuliwe sasa kwenye vijiji vinavyozuunguka Halmashauri ya Kata ya Nyamilangano, Makao Makuu ya Halmashauri ili kule ambako mji unaendelea kupanuka tuweze kupata.

Mheshimiwa Spika, lakini jingine Mheshimiwa Waziri niendelee kukusihi tu kwamba shida ya maji katika Jimbo la Ushetu ni maji ya mradi wa Ziwa Victoria. Najua umeweka upembuzi pale vijana wako wamefanya kazi;akini naogopa kushika shilingi kwa kazi nzuri unazozifanya naona aibu lakini naomba tu unapohitimisha nipate jambo la kufanya kwa wananchi wa Ushetu.

Mheshimiwa Spika, kingine…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungunzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa fedha nyingi katika ujenzi wa barabara Ushetu hasa barabara ya Uyogo - Ulowa kilometa 30 ambayo ilikuwa ni kero kubwa sana kwa wananchi wa Ushetu na wakulima wa tumbaku sasa imetengenezwa na wananchi wamenituma kuja kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Spika, ombi la wananchi wa Ushetu ni ujenzi wa lami kwa barabara yao ya kilometa 54 kutoka Uyogo Nyandekwa hadi Nyandekwa hadi Kahama itengewe fedha ili ujenzi uanze, hii ni ahadi ya viongozi wetu wakuu wa nchi pia hata katika Ilani ya CCM imewekwa pia tunaomba kutengewa fedha kwa barabara ya Mwambomba inayopita Idahina - Nyakende - Ulewe - Ubagwe - Ulowa kilometa 224 na barabara ya Bugomba A - Butibu hadi Nyamilangano kilometa 47. Barabara hizi ni kiungo muhimu sana kwa wananchi wa Ushetu sasa zianze kutengenezwa na zitengewe fedha. Hali ya barabara hizo ni mbaya sana, kuna baadhi ya maeneo hazipitiki kabisa. Naomba Mheshimiwa Waziri barabara hizi zitengewe fedha.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, niendelee kukushukuru sana lakini pia mimi niendelee kukuombea sana kwa Mwenyezi Mungu jambo lako ambalo liko mbele yako uweze kufanikiwa na upate ushindi mkubwa kuiwakilisha Tanzania; na kama mwana mama uendelee kuandika historia kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Spika,mimi niendelee kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu mama Samia Suluhu Hassan kwa niaba ya wanachi wa Jimbo la Ushetu kwa kutujali kwenye suala la umeme. Wakati Mheshimiwa Rais anaingia madarakani Ushetu ilikuwa na kata saba tu zilizokuwa zimeshafikiwa na umeme. Leo Mheshimiwa Rais yuko madarakani kata zote 20 zimeshafikiwa na mtandao wa umeme. Lakini pia kwenye vijiji wakati Mheshimiwa Rais anaingia madarakani tulikuwa na vijiji ambavyo vimefikiwa na umeme vilikuwa vijiji 20 lakini leo tunavyoongea vijiji 71 kwenye Jimbo la Ushetu tayari vimefikiwa na umeme. Niendelee kumpongeza Mheshimiwa Rais lakini pia kipekee niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri ndugu yangu Januari Makamba, Ushetu sasa inaendelea kuneemeka, Ushetu sasa inaendelea kung’aa. Niendelee kukuomba; vijiji ambavyo vimebaki kwa wananchi wa Ushetu sasa ni vijiji 41 ambavyo havijafikiwa na umeme kabisa. Niendelee kukuomba uendelee kumbana mkandarasi. Mkandarasi wako anaenda taratibu sana.

Mheshimiwa Spika, jiografia ya eneo la Ushetu na Halmashauri ya Ushetu ni kubwa sana akaze buti. Ukiangalia tu majimbo yetu yote matatu na Halmashauri tatu ukijisemea Kahama Manispaa, Msalala pamoja na Ushetu akimbize. Hata kipindi fulani niliuliza swali hapo nyuma la nyongeza kwamba Mkandarasi anaenda kwa kusua sua msukumeni sasa akimbize. Tunaona mabadiliko sio kama ilivyokuwa mwanzo,na Imani kazi imefanyika akimbize. Vijiji vinahitaji umeme, shule zinahitaji umeme, hospitali zinahitaji umeme na zahanati zetu kwenye vijiji vyetu ambazo amezijenga Mheshimiwa Rais zinahitaji umeme. Akimbize akamilishe hivyo vijiji 41viweze kufikiwa umeme.

Mheshimiwa Spika, lakini nimeona jana amesema kila jimbo angalau kupata vitongoji 15 kwa ajili ya kuwapatia umeme. Ndugu yangu Januari nikuombe Mheshimiwa Waziri, Ushetu ina vitongoji 561, sasa unaposema tu vitongoji 15 unaacha kipi na unachukua kipi? Tumia hekima yako tumia busara yako. Najua wewe ni kijana unahitaji kesho kubwa pambana ili wananchi wangu wa Ushetu na vitongoji angalau viongezeke kwa sababu ya wingi.

Mheshimiwa Spika, unajua tunatofautiana vitongoji unakuta kuna Halmashauri nyingine ina vitongoji 200 nyingine 300; lakini angalia vitongoji 561 na kitongoji kimoja ukubwa wake unaweza ukadhani ni vijiji viwili kwa hiyo niombe hili Mheshimiwa Waziri ulichukue utalifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, niendelee kumuomba Mheshimiwa Waziri aiangalie Kahama kwa macho mawili. Mwaka jana tulilia sana, tulisema hapa na Mheshimiwa Idd pamoja na Profesa Kishimba. Kahama ilivyo inahitaji mkoa wa ki-TANESCO. Kwa nini Kahama usiipe mkoa wa ki-TANESCO kwa upande wa Umeme. Ukingalia wenzio TRA tayari wana Mkoa wa ki-TRA kwa sababu ya makusanyo yaliyopo pale Kahama. Ukiangalia NSSF wana Mkoa wa ki-NSSF kwa sababu ya makusanyo yaliyopo pale Kahama. Ukiangalia hata kwenye upande wa kilimo wenzetu wa tumbaku wana mkoa wa ki-tumbaku Kahama kwa sababu ya kazi na ukubwa wa eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, hali ya umeme ya Kahama ni mbaya. Kahama ambayo ina viwanda zaidi ya 422 umeme unakatika kwa wiki, umeme unamaliza wiki haupatikani Kahama. Kahama ambayo inawafanyabiashara, eneo lillotengwa na Manispaa ya Kahama; kuna eneo maarufu linaitwa Dodoma lina vijana waliojiajiri zaidi ya 1,700 umeme vijana wanashinda wamekaa umekatika Kahama. Hii Kahama ambayo ina benki zaidi ya 12 umeme unakatika katika. Kahama ambayo ina hoteli nyingi, ina wageni wengi, ina mzunguko mkubwa, ina kusanya kwa mwezi zaidi ya bilioni nne na milioni mia tano umeme ni wa kusua sua. Kahama ambayo kwa miezi mitatu imeweza kukusanya zaidi ya bilioni 13; Kahama imekusanya bilioni 13 kwa miezi mitatu lakini umeme bado ni wa kusuasua. Yaani Kahama biashara ya generator ni kubwa kuliko biashara ya umeme unavyopatikana.

Mheshimiwa Spika, nimuombe Mheshimiwa Waziri aiangalie Kahama kwa jicho, aiangalie Kahama na ukubwa wake. Wananchi wa Kahama wanalalamika hakuna umeme, wafanyabiashara wa Kahama wanalalamika hakuna umeme…

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Cherehani, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Stella Fiyao.

TAARIFA

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa Mheshimiwa Taarifa kwamba, tatizo lililoko Kahama ndio tatizo lililoko Songwe ambalo ndilo lango Kuu la SADC. Umeme unakatika kila mara wananchi tunakosa majibu.

SPIKA: Mheshimiwa Cherehani, unaipokea taarifa hiyo?

EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa ya Mheshimiwa Mbunge kwa sababu inaongezea nguvu kwenye miji mikubwa inayokusanya fedha nyingi kwenye mapato makubwa, Serikali ipeleke umeme igeuze na ibadilishe maeneo yale ambayo yana makusanyo makubwa ya fedha yapewe nguvu na yapewe mikoa.

Mheshimiwa Spika, nimuombe Mheshimiwa Waziri, maeneo ambayo anapata nguvu, anapata fedha nyingi aelekeze nguvu; Serikali ya Mheshimiwa Rais inahitaji fedha; na jana Mheshimiwa Waziri ametuonesha; mimi sijafika kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere, mimi jana nimeliona pale Dodoma, nimeliona, ukigeuka huku unaona Mtumbwi, ukigeuka huku unaona unasogelewa na Samaki. Sasa kwa nini ashindwe kufanya miji inayokua kwa kasi aibadilishie kukatikakatika kwa umeme iwe historia?

Mheshimiwa Spika, mimi nalia na Kahama, eneo la Kahama ukiliwekea mkoa Msalala ambayo ina madini, ina vijana ambao wanahangaika, ina wachimbaji wakubwa itaneemeka na hawatasumbuka na umeme. Kahama ukiipa mkoa, Ushetu wakulima wetu watawekeza viwanda. Ndiyo maana hata juzi wawekezaji wetu wanunuzi wakubwa wa tumbaku wameshindwa kuwekeza kwa sababu hakuna umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, mimi niendelee kukuomba, na niendelee kukupongeza sana, kazi unayoifanya ni kubwa sana, lakini hebu angalia kwa macho mawili miji inayokuwa kwa kasi ipe mkoa. RCC Mkoa wa Shinyanga imeshakaa ikamaliza na ikatoa mapendekezo, leo ni zaidi ya miaka mitatu mmekaa tu. Fanyeni ziara muone jiografia ya maeneo. maeneo mengine Mheshimiwa Waziri wamefanya kazi vizuri sana, wanadhibiti mapato. Lakini wanashindwaje kwenda kujiridhisha maeneo ambayo yanakusanya? Kama kwa mwezi mmoja tu, mfano mwezi wa pili Kahama imekusanya bilioni 8,323,140,550.36 kwenye makusanyo ya umeme wilaya hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nimpongeze Tumaini Chonya ambaye ni meneja wa Wilaya, yule bwana halali, anafanya kazi. Akipigiwa simu Msalala anakimbia, Ushetu anakimbia, na sisi tukiwa kwenye mkutano wa hadhara wananchi wakilalamika tu tunamuunganisha hapo tunaweka loud speaker, analalamika, anasema anachopata ni sawa na wilaya nyingine kama zilivyo. Sasa hauwezi kuilinganisha Wilaya ya Kahama na wilaya nyingine halafu ukailinganisha matumizi na kuipelekea hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Waziri utakapokuja kuhitimisha suala la Kahama liwe na majibu ya kipekee. Tunahitaji Kahama ipate mkoa. Na kama RCC imekwishapitisha ninyi wizara mnashindwa nini? Niendelee kumuomba Mheshimiwa Waziri; kuna kata zangu hazina umeme. Kata ya Igwamanoni…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Emmanuel, kengele ya pili imeshagonga, malizia sentensi.

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, Kata yangu ya Igunda, Kata ya Igwamanoni, Kata ya Chona ni maeneo ambayo vijiji vyake vingi havijapata umeme. Mheshimiwa Waziri, naomba aangalie Mkandarasi, amsukume kwenye kata zangu hizi ili ziweze kupelekewa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, naunga mkono hoja.
Azimio la Bunge la Kuridhia Kufutwa kwa Hifadhi ya Taifa ya Kigosi ili Kuruhusu Kuanzishwa kwa Hifadhi ya Msitu wa Kigosi na Azimio la Bunge la Kuridhia Kurekebisha Mpaka wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Niendelee kukushukuru sana wewe kwa kazi nzuri ambazo unatuongoza. Leo ni takribani miezi minne ukiendelea kuongoza mhimili huu mkubwa, kazi inafanyika vizuri.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri anayoifanya, namna anavyoshughulikia migogoro ya hifadhi zetu. Kashughulikia mgogoro wa Ngorongoro, wananchi wamesafirishwa kwa uhakika kabisa na sasa hivi wanafurahia maisha mapya bila kelele yoyote, na Mheshimiwa Rais anashughulikia migogoro ya nchi kwa uhakika kabisa. Tuendelee kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu.

Mheshimiwa Spika, nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri, kwa kweli unastahili maua yako, pamoja na Naibu Waziri, Makatibu Wakuu na Wizara yote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwapongeze sana Makamishna wa Uhifadhi wa TANAPA na TFS; kazi nzuri wanaendelea kufanya. Wanatambua nafasi ya kazi ambayo mmewapa.

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba hili suala wananchi walikuwa wamelisubiri kwa kasi kubwa sana, na hatimaye limeweza kufika. Nikupongeze Mheshimiwa Mary Masanja, ulifika kwa wananchi wa Ushetu, uliongea nao, uliwasikiliza na uliwaahidi. Na leo wanaona matunda mazuri ya Mheshimiwa Rais; ni kazi nzuri ambayo imefanyika.

Mheshimiwa Spika, niendelee kukuomba tu Mheshimiwa Mchengerwa, Waziri wetu, kwa sababu sasa tunakwenda kulirudisha pori hili kwenye uhifadhi wa wananchi wetu, kutoka Hifadhi ya Taifa ya Kigosi sasa inakwenda kuwa Hifadhi ya Kigosi; nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, tuna wananchi wetu wafugaji, wanaorina asali, wavuvi pamoja na wachimbaji, sasa wanakwenda kufaidika na rasilimali hizi.

Mheshimiwa Spika, tuna tatizo moja naomba tulifanyie kazi; tuwasajili wafugaji na warina asali, tuweze kuwatambua; wachimbaji wadogo tuweze kuwatambua. Lakini pia na wenzetu ambao wanaingia pale kuvua samaki na wenyewe waweze kutambulika ili tujue kazi hii sasa wanapoingia kwenye kurina asali tuweze kujua, ili tunapojua sasa kwamba idadi yao ni wangapi, inatusaidia sana namna ya usimamizi mzuri kwenye hifadhi.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais kafanya kazi kubwa sana. Ukiangalia leo katika Jimbo la Ushetu peke yake, Kata zinazokwenda kufaidika na eneo hili, kuna Kata kubwa sana ya Ulowa, inakwenda kufaidika; Kata za Ubagwe, Ulewe, Idahina, Nyankende na Bulungwa. Wote hawa wanazungukwa na pori hili ambalo sasa wanakwenda kufaidika wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, lakini bado kuna Wilaya zetu za Bukombe, Kaliua, Mbogwe kwa ndugu yangu, Waziri, Mheshimiwa Doto Biteko. Wananchi hawa wote wanazunguka pori hili. Ni kazi nzuri, kubwa sana Mheshimiwa Rais ameifanya. Mheshimiwa Rais ni msikivu, pamoja na kwamba ametuma Mawaziri wote wamezunguka maeneo haya, lakini anaporudishiwa ripoti anaifanyia kazi hapohapo na kutoa matokeo. Sasa haya ni matokeo ya Mheshimiwa Rais jinsi anavyosimamia rasilimali za nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee kukupongeza sana wewe, lakini niipongeze sana Serikali, niwapongeze sana Kamati, Kamati imefanya kazi kubwa sana; hongereni sana Kamati. Kazi iliyofanyika ni kubwa, imeishauri Serikali kwa uhakika bila upendeleo, na leo wananchi wetu migogoro inakwenda kuondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee kuiomba Wizara, endeleeni pia kushughulikia na migogoro ya maeneo mengine, endeleeni pia kushughulikia na mipaka ya maeneo mengine. Ili Mheshimiwa Rais anapoelekea 2025 tuendelee kumpa maua yake, aendelee kubeba kura zake, tuendelee kumtendea haki. Kazi anayoifanya leo Mheshimiwa Rais ni matokeo atakuja kuyapata maua yake 2025, ni kazi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo niendelee kupongeza kazi nzuri imefanyika, wananchi wa Ushetu sasa wanakwenda kufurahi, kufaidika. Kama Mbunge naahidi kuongeza nguvu kuhakikisha tunaendelea kuwapa elimu ili waendelee kui-support Serikali katika tukio hili.

Mheshimiwa Spika, nikupongeze tena; naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, ahsante, nikushukuru sana wewe, lakini pia tumshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kibali cha pekee cha kutufanya leo tuendelee kukutana hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, cha kwanza niendelee kumshukuru sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa nafasi ya pekee hasa tukio la jana ambalo mimi naona limevunja rekodi kwa mara ya kwanza kuweza kukutana na Makatibu Mahsusi, ni mwanamke ambaye anajua uhitaji wa wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia niendelee kumshukuru sana Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Pindi Chana pamoja na dada yangu Naibu Waziri Mary Masanja na Katibu Mkuu Dkt. Francis Michael kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya katika nchi hii wanamsaidia ipasavyo Mheshimiwa Rais, wanaisaidia na wanaitendea haki Wizara ya Maliasili na Utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nijikite kwenye mada hasa kwenye maslahi ya hawa ndugu zetu wa maliasili, hawa Jeshi la wenzetu Jeshi la Maliasili, Jeshi la Uhifadhi Wanyamapori, hawa watu ningemuomba Mheshimiwa Waziri waangaliwe sana ni askari ambao iwe mvua ya kwao, liwe jua la kwao, wanyama wakali porini ni wa kwao, majangili ni wa kwao. Kwa hiyo, ningeomba Serikali iwaangalie kwa mapana sana hasa suala la marupurupu na namna gani ya kuweza kukaa nao karibu, wanafanyakazi ngumu sana.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naangalia kwenye taarifa kwenye ripoti ya Mheshimiwa Waziri eneo la uhifadhi lipo zaidi ya kilometa 307,800 ni zaidi ya asilimia 32 ya eneo la nchi lakini wanaolinda na kuzungukia hili eneo ni maaskari wa uhifadhi. (Makofi)

Kwa hiyo, ningemuomba Mheshimiwa Waziri pamoja na mambo mengine mazuri wanayoyafanya hawa watu lazima waangaliwe sana kwenye suala la marupurupu. Ninajua sana hata watakapoangaliwa suala la marupurupu hawa ni askari ambao wanalinda rasilimali za nchi. Kwa hiyo, mimi ningeomba Mheshimiwa Waziri hili liangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri nilikuwa na suala la watu wa TFS sijajua hawa watu wanaochoma mkaa wanakosea wapi. Ukiona mwananchi amepakia gunia lake la mkaa anasafirisha kwenda kuuza, ukifuatilia wakati mwingine, aidha, ana mgonjwa au mke wake anaumwa au kafanyiwa operation hospitalini. Anataka akatafute fedha ya dharura aidha ya kwenda kulipia matitabu au kwenda kumkomboa mke wake hospitalini aweze kurudi nyumbani. (Makofi)

Kwa hiyo, ningeomba anakutana na wenzetu hawa maaskari ambao ni watanzania wenzetu anakamatwa ananyang’anywa hata baiskeli ananyang’anywa hata gunia lake la mkaa na ametembea labda kilometa 20, anarudi kwa mguu. Ningeomba wizara iangalie utaratibu rafiki wa kuweza kuwaelimisha hawa watu, wawaelimishe hawa watu namna nzuri ya kuvuna mkaa wao. Wakati mwingine hata hajakata mti, amechimba mizizi kule kwenye shamba lake, akaikausha vizuri ili angalau aweze kuhudumia. Aidha, ameondoka kabisa nyumbani, ameacha hakuna hata unga hamna hata chakula angalau akauze gunia lake la mkaa au debe lake la mkaa aweze kurudi na unga, aweze kurudi angalau na mahindi kwa ajili ya kuhudumia watoto wake lakini madhara yake anakumbana na hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ningeomba tuwabadilishe wenzetu askari hasa TFS wawe angalau na muda wa kuwapa elimu hawa watu tusiendelee ku-copy toka zamani, mimi nikiangalia hata asilimia kubwa ya Wabunge humu tunatumia mkaa huwezi kula tu na hata huyu aliyeenda kumkamata nyumbani kaacha gunia la mkaa, ugali aliokula umepikwa kutumia mkaa, sasa inakuwaje tena anageuka kuwa mwiba kwa wenzetu hawa. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Ni kweli.

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, ningeomba sasa huyu mwenye gunia moja hawezi kwenda Wilayani akatafute kibali. Mfano, nikiongelea Jimbo la Ushetu kutoka kule ukapate kibali zaidi ya kilometa 40 aende akatafute kibali cha gunia moja halafu arudi kwa ajili ya kusafirisha, huku ana tatizo nyumbani, huku hana chakula, mimi ningeomba wenzetu wa TFS wajikite kwenye kutoa elimu, lakini wajikite kwenye kuwafundisha hawa vijana waweze kuwa na mashamba yao ya miti kwa ajili ya kwamba sasa pandeni miti yetu hapa na utaratibu unakuwa ni bora zaidi kuliko wanavyofanya sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niongelee eneo la Ushetu, tuna mgogoro ambao naona umedumu kwa muda mrefu, mgogoro wa pori letu la halmashauri, Usungwa Forest Reserve pamoja na Kigozi – Muyoyozi ambao toka tarehe 31 Disemba, 2019 kuna timu ilikuja kwa ajili ya kutatua huu mgogoro, lakini haikutoka na matokeo wala haikutoa jibu na mbaya zaidi haikukutana na Madiwani wala Mwenyekiti wa Halmashauri hata Mkurugenzi wa Halmashauri haikukutana naye.

Mheshimiwa Spika, mimi ningeomba Mheshimiwa Waziri anapokuja kuhitimisha aje anisaidie ni lini tutaenda kushughulikia mgogoro wa wananchi hawa wa Ushetu ambao wanaoteseka hasa wananchi waliopo katika Kata ya Nyankende, Kata ya Ulewe, Kata ya Idahina, Kata ya Ulowa, Kata ya Ubagwe na Kata ya Sabasabini ni maeneo ambayo wananchi wake wanateseka na mgogoro huu ambao umedumu kwa muda mrefu. Niombe sana ndugu zangu waziri kwa sababu uwezo wako wa kazi ni mkubwa, tuje tukashughulikie huu mgogoro ili tuuondoe kati ya Usungwa Forest Reserve ambayo ilikuwa ni bonde la Halmashauri ya Ushetu lenye GN number 442 ya mwaka 1959 lakini kwenye mgao wa mwaka 2020 wakati Kigozi inapanda kuwa TANAPA ukaingizwa huko sasa ni mgogoro ambao unawatesa sana wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ningekuomba Mheshimiwa Waziri kwasababu uwezo wako wa kazi ni mzuri na Naibu Waziri na Katibu Mkuu mje sasa mtuambie ni lini tutaambatana pamoja kwenda kukaa na wananchi na wazee wa eneo hili maeneo yote haya ambao ni wazaliwa wa eneo hili ili tuone namna gani tunatatua. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Sawa.

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, lingine nilikuwa nashauri ndugu zangu wa maliasili, tunajua tunachangamoto nyingi, lakini kubwa sana ninawaomba Mheshimiwa Waziri fanya ziara kwenye maeneo haya ukifanya ziara kwenye maeneo haya kutana na wazee, kutana na Madiwani kwenye haya maeneo yote ya migogoro watakusaidia sana nakumbuka hata hawa mawaziri wanane ambao waliteuliwa kwa ajili ya kuzungukia kutatua hii migogoro hawajawahi kukanyaga Ushetu, hatujawahi kuona Ushetu wanakuja kututatulia hii migogoro. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba ndugu zangu mnapokuja kushughulikia hii migogoro mje na Ushetu mkutane na Madiwani na maeneo mengine mkikutana mkakaa na Madiwani, Madiwani wa maeneo husika na Wenyeviti wa Vitongoji wana mambo mengi ambayo wanaweza wakawaelezea na namna nzuri ya kuweza kusimamia sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri utakapokuja unisaidie sana ili wananchi wangu wasiendelee kuteseka na suala la mkaa tuje na utaratibu mzuri ambao tutawasaidia wananchi wetu namna nzuri ya kuboresha na namna nzuri ambayo itafanya sasa wawe wapandaji wazuri wa miti na kujenga uoto mzuri wa asili wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana na nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri anayoifanya kwenye nchi hii. Ninajua kila Mbunge kwenye eneo lake barabara zinajengwa, hospitali zinajengwa, kila kitu kinafanyika. Mheshimiwa Rais anafanya kazi, hata kwenye gharama ya mafuta katoa shilingi bilioni 100. shilingi bilioni 100 ukiziweka humu tunaweza tukakosa hata mahali pa kukanyaga. Mama anaupiga mwingi, kwa kweli tumshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)