Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Janeth Maurice Massaburi (33 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JANETH M. MASSABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa huruma, si mwepesi wa hasira mwingi wa rehema ambaye yeye ndiye amenipa kibali kuwa katika Bunge hili leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipekee naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wetu mpendwa wa Jamhuri ya Muuungano wa Tanzania kwa kuniamini na kuniteua kuwa Mbunge katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Spika pamoja na ninyi Wenyeviti wote. Kwa kipekee vilevile niwashukuru Wabunge wote kwa mapokezi mazuri na upendo waliouonesha kwangu. Naomba Mwenyezi Mungu azidi kuwabariki Wabunge wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tuzidi kuwatetea wananchi wengi wa Tanzania walio wanyonge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikishukuru chama changu, Chama cha Mapinduzi, chama chenye kuleta matumaini kwa Watanzania hasa wanyonge kwa kunilea vyema na kunishauri, na hapa nilipo ni Chama changu cha Mapinduzi ndiye mlezi thabiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kuishukuru familia yangu, wazazi wangu, watoto wangu, shemeji zangu, majirani ndugu na marafiki kwa kunilea na kunipa moyo na hasa wakati mgumu nilipoondokewa na rafiki yangu mpenzi wangu Didas Massaburi. Mwenyezi Mungu azidi kumpokea katika makao yake ya milele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango huu mimi nimeona kuna mambo mazuri mengi, lakini si maana kwamba yote ni mazuri tu na ndiyo maana kuna miaka mitano ya kujisahisha na ndiyo maana kuna bajeti za kila mwaka, penye mapungufu unajaza, unatoa wazo la kuleta manufaa.

Katika mpango wa miaka mitano (2016/2017 - 2020/ 2021) wametenga kanda tano maalum za kiuchumi. Kuna eneo maalum la uwekezaji la Bagamoyo hilo liko Mkoa wa Pwani, lengo kuu ni kujenga bandari ya kisasa ambayo itaruhusu meli kubwa na eneo hili litakuwa lango kuu la biashara za kikanda na kimataifa, lakini kutakuwa pia na viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kituo cha viwanda cha Kurasini Dar es Salaam. Mradi huu pia utaimarisha ushirikiano wa kibiashara kati ya Tanzania na mataifa mengine kupitia uwekezaji katika miundombinu ya kubiashara na ujenzi wa viwanda; huo kumbuka ni Mkoa wa Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu kuna maeneo maalumu ya uwekezaji ya Mkoa wa Kigoma. Lengo kuu la mradi ni kuwa na eneo maalumu wa uwekezaji llitakalokuwa na bandari huru (free port). Kutakuwa na mitaa ya viwanda, kongani za kitalii na kituo cha biashara. Hili limetengwa kutumia vizuri fursa za kijiografia ambayo itaweza kuhudumia nchi za Kongo, Burundi, Rwanda na Zambia. Kumbuka ni Mkoa gani huo? Ni Kigoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna eneo la uwekezaji Mkoa wa Mtwara eneo hili pia kutakuwa na uwekezaji jumla ya hekta 110 ambazo zimetengwa maalum kwa lengo la kujenga bandari huru ambapo kuna kampuni ambazo zinaendelea kufanya utafiti katika eneo lile na vilevile watajenga viwanda, Mkoa wa Mtwara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tano ni Mkoa wa Ruvuma, kuna uwekezaji wa jumla ya hekta 2030 kwa ajili ya ujenzi wa viwanda vikubwa (heavy industries) vitakavyotumia malighafi ya gesi na chuma. Viwanda vya kuongeza thamani na mazao ya kilimo kama korosho na viwanda vya vito vinatoka Mtwara hii ni Mikoa mitano Pwani, Dar es Salaam, Kigoma Mtwara na Ruvuma hii Mikoa yote inatoka Kanda ya Ziwa? Mikoa inatoka Chato? Tusipotoshe wananchi wetu, Watanzania wana akili sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna vipaumbele kwa mwaka wa fedha 2018/2019. Miradi mikubwa ambayo naona inasemwana sana, mradi wa Stiegler’s Gorge naona umekuwa ni mjadala mkubwa. Hata hivyo hiki ni chanzo cha nishati ya umeme. Tumesema Tanzania ya viwanda bila umeme hatuwezi kuwa na viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile kuna reli. Nakumbuka mimi katika Bunge la mwaka 2005 mpaka 2010 kulikuwa na mjadala wa Bunge kuhusu reli, barabara zinaharibika magari makubwa yanatumia barabara kila mwaka kuna fedha za kutengeneza barabara. Sasa sisi tunashauri Serikali inatekeleza, imekuwa kazi! Shirika la ndege… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kukupa pole kwa kuugua pia tunamshukuru Mungu kwa uponyaji wako. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mungu kwa zawadi ya uhai na kutupatia Viongozi wazuri wenye nia njema ya kuleta maendeleo kwa Watanzania. Nampongeza sana Rais na Wasaidizi wake Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amekuwa ni kielelezo chenye kuleta mabadiliko ya utendaji kazi wenye kuleta tija kwa jamii na Watanzania wote kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kusimamia shughuli zote za Serikali kwa umakini na umahiri mkubwa. Nawapongeza pia Mawaziri, Manaibu, Makatibu Wakuu na Watendaji wote wanaowasaidia katika utendaji wao wa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi, naomba kuchangia mambo yafuatayo ambayo yamekuwa ni kero au changamoto kwa jamii katika maeneo husika:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara za Mkoa wa Dar es Salaam. Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mwaka 2015 alipokuwa kwenye kampeni katika Mkoa wa Dar es Salaam, Jimbo la Segerea kwenye mkutano Vingunguti aliahidi kujenga barabara ya Segerea Seminari kuelekea Majumba Sita kupitia Kituo cha Polisi cha Stakishari kwa kiwango cha lami na kujenga daraja, lakini mpaka sasa hakuna dalili yoyote hata ya kukarabati ili wananchi wapite kwa amani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ni mbovu watu wanapita ndani ya mto wakati wakielekea maeneo ya Ukonga kutafuta huduma mbalimbali kama Airport, Hospitali ya Ukonga ya Rugambwa, Mahakama ya Mwanzo Ukonga na maeneo mengine ya huduma. Eneo la Segerea Shell Oilcom (Kona ya Segerea Seminari) inahitaji mfereji wa kupitisha maji ya mvua kwa haraka ili kunusuru ile barabara isikatike kwa mvua inayoendelea maana hali ni mbaya katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu afya, naiomba Serikali kupitia Wizara ya Afya itoe fedha za bajeti kwa wakati ili kukidhi mahitaji katika sekta ya afya kwa muda unaohitajika. Kuchelewesha kutoa fedha kwa wakati husika kunasababisha maafa na kurudisha nyuma jitihada nzuri za Serikali za kuboresha sekta ya afya. Kwa mfano, Kitengo cha Moyo Muhimbili (Jakaya Kikwete Cardiac Institute), Kitengo cha Mifupa (MOI), Wodi ya Wazazi wanalala wawili kitanda kimoja na hii inasababisha maambukizi kwa watoto wachanga na kusababisha vifo. Hospitali zote za Rufaa na vituo vyote vya afya, naiomba Serikali kupitia sekta hii nyeti ya afya fedha zake zipewe kipaumbele, Wizara ya Fedha itilie maanani suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza Madaktari wetu wanafanya kazi nzuri sana na ya kizalendo kwa kutoa huduma kwa kiwango cha Kimataifa hasa pale (Jakaya Kikwete Cardiac Institute) na Kitengo cha Mifupa (MOI) na pia Hospitali ya Kansa Ocean Road, Benjamin Mkapa Dodoma na Madaktari wote na Wauguzi nawapongeza wote sekta ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JANETH M. MASSABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tena nichukue fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuniamini na kuniteua kuwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pamoja na pongezi naomba nichangie Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2018/2019 kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu miundombinu ya barabara, naomba niipongeze Serikali kwa hatua mbalimbali za kuboresha barabara zetu hapa nchini. Hata hivyo kuna dosari kadhaa ambazo zinatakiwa kupatiwa ufumbuzi wa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano barabara za Mkoa wa Dar es Salaam, barabara ya Tabata Dampo kuelekea Tabata Segerea - Kinyerezi - Malamba Mawili - Msigani mpaka Mbezi, barabara hii imekuwa kero kubwa na adha ya foleni hasa nyakati za kuanzia saa 12.00 asubuhi mpaka saa 4; na saa 10.00 jioni hadi saa 3.00 usiku, na ikizingatiwa barabara ndiyo lango la kubebea mitambo mikubwa ya Mradi wa Gesi Kinyerezi. Kwa sababu hizo na nyingine tunaiomba Serikali ipanue barabara hiyo kutokana na idadi kubwa ya watu na watumiaji wengine kama mradi wa Kinyerezi (Mradi wa Gesi).

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Segerea Sheli kuelekea Seminari hadi Majumba Sita, tumeiomba Serikali iweke barabara hii kwenye mpango wa dharura wa muda mfupi na pia iwekwe kwenye mpango wa kujenga barabara hiyo na Daraja la Seminari ili wananchi waweze kutumia barabara hiyo kwa manufaa. Barabara hii Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John Pombe Magufuli, wakati wa Kampeni ya Uchaguzi Mkuu 2015 akiwa Vingunguti aliahidi kuwa barabara ya Segerea Shelil (Oil Com)kupitia Segerea Seminari hadi Majumba Sita ijengwe kwa kiwango cha lami na daraja lake. Kwa muda huu yafanyike matengenezo ya dharura hasa pale eneo la Sheli (Oil Com) ambapo njia inapitika kwa shida sana. Wakazi wa eneo hilo wamekata tamaa. Kwa kuanzia angalau kifusi cha mawe ili kunyanyua barabara maana pamechimbika sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu barabara kuu na barbara za mitaa; barabara nyingi hazifanyiwi matengenezo kwa wakati, hali hii inasababisha Serikali yetu ya CCM ilaumiwe. Naomba Serikali iweke kitengo madhubuti kitakachofanana na kuendana na kasi ya Mheshimiwa John Pombe Magufuli Rais wetu ili kitengo hiki cha ukaguzi wa barabara kuu na barabara za mitaani kiweze kutambua tatizo mapema kuliko tatizo litolewe na vyombo vya habari. Hali hiyo huwa inaleta fedheha kubwa, ikizingatiwa kuna viongozi na watendaji katika ngazi za kata na kadhalika walitakiwa kujua tatizo kabla. Kitengo cha ukaguzi kiongezewe vitendea kazi kama magari na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la maji Dar es Salaam. ninaipongeza Serikali kwa kuboresha upatikanaji wa maji katika Mkoa wa Dar es Salaam kwa asilimia 70; wananchi wa Dar es Salaam wamefurahi sana kwa kupata maji. Hata hivyo tunaiomba Serikali iharakishe upatikanaji wa maji katika maeneo ambayo hutegemea chanzo kingine cha maji, kwa mfano wananchi wa Kipera – Pugu, Majohe, Chanika, Msongola, Kitunda, Chamazi na maeneo ya Mwinuko ambao hawapati maji ya uhakika. Tunaomba kasi iongezwe zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu elimu ya ufundi na ujuzi, Serikali iangalie kwa upana zaidi kwa kuanzisha vyuo vingi vya ufundi ili viweze kutengeneza rasilimali watu wenye ujuzi wa fani mbalimbali kama mafundi wa mitambo midogo midogo, mafundi wa kutengeneza vifaa vya umeme, vifaa vya ujenzi; vifaa ambavyo soko lake litatokana na matumizi yetu ya kila siku sisi Watanzania. Kwa mfano kutengeneza vifaa vya ngozi (viatu, mikanda, mabegi, vifaa vya umeme aina zote za majumbani, vifaa vya ujenzi pamoja na vifaa (vipuri) vya mitambo midogomidogo pamoja na ujuzi wa aina nyingine ambazo zinaweza kuleta mabadiliko makubwa ya kiteknolojia na kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili la mafunzo ya ufundi na ujuzi itasaidia kuruhusu vijana wengi wanaomaliza darasa la saba, kidato cha nne na kidato cha sita, kupata mafunzo na baada ya hapo kupelekwa kwenye viwanda husika. Serikali si vibaya ikafuata mfumo uliotumika katika nchi ya Singapore ya kufanya mapinduzi ya kuwafundisha vijana wao wengi mafunzo ya ufundi na ujuzi kwa kuanzisha vyuo vingi vya ufundi na ujuzi mbalimbali na walitilie nguvu katika masuala ya vifaa vya umeme.

Mheshimwia Mwenyekiti, naunga mkono hoja pamoja na maoni yangu, nawasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kuwapongeza Waziri wa Habari, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, watendaji wote walio chini ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kazi nzuri waliyoifanya katika kuhakikisha sekta zilizoko katika Wizara hiyo zinasonga mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo kuna changamoto kadhaa ambazo zinatakiwa kufanyiwa maboresho. Changamoto hizo ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi cha karibu miaka 30 iliyopita kumekuwa na ulegevu kwa kiasi fulani kwa Serikali yetu kwa kutokuwa karibu na vijana (rika la miaka 12-35), kundi ambalo linahitaji kuelewa, kuelimishwa na kuthaminiwa kwa kuwa vijana ndio nguvu kazi ya nchi yoyote duniani hususan Tanzania. Kwa kuwatumia vizuri vijana wetu watasaidia kuongeza uchumi wa nchi na pia watajiajiri wao wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wasanii wetu wanahitaji elimu ya ujana, mila zetu, utamaduni wa Mtanzania, staha, heshima, nidhamu, utu, utaifa na uzalendo kwa nchi yetu. Haya yote yanahitaji fedha za bajeti katika Baraza la Michezo (BASATA) ili zitumike kwa kuwapatia elimu, mafunzo, warsha, semina, hamasa, matangazo mbalimbali ambayo yatasaidia kuwaelimisha wasanii/vijana wa Kitanzania kuelewa na kujiheshimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali ijipange upya katika kutambua na kusimamia vijana wasanii wa aina mbalimbali yaani music, ngoma za jadi, wachoraji, waimbaji injili, muziki wa dansi, waigizaji, wanamichezo na wengine wanaojihusisha na sanaa. Kwani wasanii wana mchango mkubwa katika ustawi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu enzi ya kutafuta uhuru wa nchi yetu ya Tanzania. Kwani wasanii wetu walikuwa bega kwa bega katika kutafuta Uhuru wa Tanganyika kwa kuimba na kucheza ngoma za kudai uhuru wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naomba tena Serikali kutoa fedha za bajeti za kutosha kwa ajili ya kuelimisha wasanii kwani mtoto umleavyo ndivyo akuavyo. Tukiri eneo hili tulilisahau likajilea lenyewe. Tukumbuke vijana ni kundi lenye nguvu na pia wana muda mwingi wa kuishi hapa duniani, tulilee na kulielekeza vema. Msanii Diamond anaiwakilisha Tanzania anahitaji kuelimishwa na kulelewa vema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga hoja mkono kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Spika, Pongezi kwa Serikali na Wizara hii, VAT kwa bidhaa za maziwa hususani (UHT Milk) tunaomba itolewe.

Mheshimiwa Spika, Serikali iwekeze kwenye taaluma ya maziwa Vyuoni kama Shahada na Stashahada ili tupatiwe Wataalamu na kuongeza ujuzi katika Sekta hii ya maziwa.

Mheshimiwa Spika, Kwa sasa Afrika ya Mashariki Chuo pekee kinachotoa taaluma hii ya maziwa ni Egerton University ya nchini Kenya.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ndiye aliyenipa zawadi ya uhai na ametujaalia sisi sote kujumuika hapa leo na kuweza kujadili mambo yaliyo mbele yetu kwa maslahi ya nchi yetu. Vilevile namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumjaalia afya njema Mheshimiwa Spika wetu kwa kumuwezesha kurudi salama. Tunamshukuru Mungu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Makamu wa Rais, Rais wa Zanzibar, Mawaziri wote na Naibu Mawaziri wote, Makatibu Wakuu na Watendaji wote wa Serikali bila kusahau Wakuu wa Mikoa ambao wote kwa pamoja wamefanya kazi njema ambayo matunda yameonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Jaffo, Waziri wa TAMISEMI na Naibu Mawaziri wake kwa kazi nzuri wanayoitekeleza. Tumewaona mara kwa mara wakikimbia huku na huku, na mara nyingine wamepata ajali njiani, kwa kweli tunampongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nichukue fura hii kumshukuru na kumpongeza Waziri husika wa TAMISEMI ambaye ni Rais wetu mpendwa, Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa aliyoifanya kwa kipindi hiki cha miaka miwili na nusu. Amefanya mambo mengi makubwa ambayo yamewashangaza Watanzania ambao wengi walikuwa wanabeza na wengi tukikumbuka walikuwa wanambeza sana Rais wetu wa Awamu ya Nne kwa kutokuchukua maamuzi mengine ingawa yeye pia ndiye aliyeweka mfumo mzuri, lakini pia yeye ndiye aliyetuchagulia Rais Magufuli. Yeye na wenzake walikuwa makini; akamchagua Mheshimiwa Magufuli ambaye leo amekuwa Rais wetu wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo mengi yamefanyika katika nchi hii. Kwanza wananchi wengi katika nchi hii wamebadilika kifikra na kimtazamo. Kumekuwa na miradi mikubwa ambayo imetekelezwa kwa kiwango kikubwa sana na mingine pia inaendelea kutekelezwa chini ya uongozi wa Rais wetu. Pia kumekuwa na mabadiliko ya kiutendaji kwa watumishi wa Serikali na taasisi za umma. Nidhamu ya kazi kwa watumishi na huduma nzuri zinafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitaje mambo machache tu ambayo yamefanyika kwa kipindi cha miaka miwili na nusu.

Moja, kumekuwa na nidhamu kazini kwa watumishi wa umma na uwajibikaji; pili, mapambano dhidi ya dawa za kulevya na udhibiti wa uingizaji wa dawa za kulevya. Mapambano dhidi ya ufisadi na uhujumu uchumi, udhibiti wa mapato ya Serikali na matumizi yake; mapato ya Serikali yameongezeka, kudhibiti rasilimali za taifa kama madini na kadhalika, ununuzi wa ndege sita na tatu zimeshawasili hapa nchini na wengi tumehudumiwa na wanaobeza na wao wanapanda hizo ndege.

Pia huduma ya maji imeboreshwa mijini na vijijini, sisi watu wa Dar es Salaam ni maajabu maana tulikuwa tunalalamika, lakini siku hizi changamoto sasa ni maji kupasuka huko mitaani, maji yanapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna uhamasishaji wa ujenzi wa viwanda vya madawa nchini na viwanda vingine…

T A A R I F A . . .

MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei hiyo taarifa kwa sababu kwa asilimia kubwa maji yameboreshwa. Kuna maeneo ya Kimbiji na Chanyika ambayo yanategemea mradi unaotoka kule Kigamboni, lakini kwa asilimia 70 maji Dar es Salaam yanapatikana (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma za afya zimeboreshwa, lakini kumbuka Roma haijajengwa kwa siku moja. Uhamasishaji wa ujenzi wa viwanda vya dawa kama nilivyosema, mradi wa umeme wa Rufiji (Stieglers Gorge) unaendelea, ulinzi na usalama umeimarishwa nchini, mauaji ya Kibiti yamekomeshwa. Amekaribisha wafanyakazi kushirikiana na Serikali kuondoa vikwazo mbalimbali ili kuleta tija kwa Tanzania. (Makofi)

T A A R I F A . . .

MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, inauma sana, muda mfupi mambo mengi yamefanyika. Hiyo sipokei kwa sababu naangalia data.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara zimejengwa, madaraja, flyover mmeziona Dar es Salaam, mji unabadilika unakuwa wa kisasa, mradi wa mabasi awamu ya pili, tatu unaendelea; ujenzi wa kiwanja cha michezo Dodoma unazinduliwa na kadhalika Ni mengi, ngoja niishie hapo maana itauma sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo yote yaliyofanyika hapa nchini ambayo yanastahili pongezi, na dunia imeshangaa, mwenye macho haambiwi tazama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo kumekuwa na changamoto kadhaa ambazo zinapaswa kutiliwa mkazo au kufanyiwa kazi. Katika nchi zilizoendelea kiuchumi duniani ikiwemo nchi ya Marekani, suala la ulinzi limetiliwa mkazo na limetiliwa kipaumbele kuliko sekta nyingine kwa sababu jinsi uchumi unavyokua ndivyo uhalifu pia unavyokua. Kwa sababu hiyo hata nchi yetu ya Tanzania uchumi unakua lakini na mbinu mbalimbali za kihalifu nazo zinakua. Naiomba Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi iongeze bajeti ya kutosha kwa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama ili ziweze kukidhi mahitaji ya vikosi vyetu au kwa vyombo vyetu vya usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na changamoto mbalimbali kama makazi ya askari, magari, mafuta na vifaa mbalimbali. Mafunzo ya ndani na nje ya nchi, kwa hiyo naiomba Serikali yangu itilie maanani katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kidogo niongelee Jeshi la Zimamoto. Tunaposema uchumi wa viwanda ujue viwanda ni rafiki wa moto kwa hiyo tunaomba pia bajeti katika eneo hilo iongezwe bila kusahau Jeshi la Zimamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposema elimu bure ujenzi wa shule mbalimbali, umeme vijijini, ujenzi wa mradi wa umeme wa Rufiji (Stieglers Gorge) na kadhalika, bila usalama haya yote hayawezi kutekelezwa. Kwa hiyo naiomba Serikali itilie maanani katika masuala ya ulinzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuongelea habari ya hospitali na naomba niipongeze Wizara ya Afya kwa kazi nzuri wanayoifanya, pamoja na kwamba pongezi ambazo nilishazitoa hapo nyuma. Katika Kitengo cha Moyo cha Jakaya Kikwete (JKCI), Kitengo cha Mifupa (MOI), Kitengo cha Dharura na Kitengo cha Akina Mama (Wodi ya Wazazi;) naomba fedha zipelekwe kwa wakati ili ziweze kukidhi na kuzuia maafa zaidi ambayo yanaweza kutokea katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuwe na ukaguzi wa maeneo wakati wa kufanya usafi siku za Jumamosi kwa sababu siku hiyo akina mama wengi katika Mkoa wa Dar es Salaam ambao wanafanya biashara ya kuuza maandazi na vitafunwa, chapati na kadhalika, muda wao wa kufanya biashara ni asubuhi mpaka hapo saa tatu. Sasa kule muda huo unakuwa umepigwa marufuku, hakuna kufanya biashara mpaka saa nne, na ikifika saa nne muda wa kunywa kifungua kinywa utakuwa umeshakwisha, kwa hiyo akina mama hawa wanaathirika sana.

Naomba Serikali husika, najua kero hii itakuwa si Dar es Salaam tu, hata mikoa mingine, iangalie eneo hili ili kuinusuru hali ya akina mama ambao wamekopeshana hela ndogo ndogo kutoka kwenye VICOBA vyao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naomba Serikali iongeze vyuo vingi vya ufundi ili kuwaweka vijana wetu tayari kwa ajili ya kuajiriwa katika maeneo ya viwanda. Bila kuwatayarisha vijana kutakuwa na changamoto kubwa katika kupata sifa ya kuajiriwa katika viwanda. Baada ya kusema hayo, nawashukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuongea; nitaongea kwa uchache sana. Sichoki na sichoki tena katika kumshukuru Mheshimiwa Rais wetu wa Awamu ya Tano kwa kazi nzuri anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watakumbuka ndugu zangu, huko nyuma sisi tunaokwenda Mara tulikuwa tunapita Nairobi, Sirari ndiyo tunaingia Mara; wanaokwenda Kagera walikuwa wanapita Nairobi, Kampala huko ndiyo wanaingia kule Bukoba. Lakini chini ya uongozi tukimkumbuka Mheshimiwa Rais wetu ambaye alikuwa Waziri wa Ujenzi, hakulala, alikuwa analala kwenye mahema huko. Mheshimiwa Rais amejitoa muhanga katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia siachi kumshukuru na kumpongeza, amefufua Shirika la Ndege, huko nyuma tulikuwa tunapiga kelele nchi haina ndege, nchi inaliwa, yeye amekuja ameleta ndege kwa mkupuo. Tunasema watalii wamepungua nchi hii hatuna alama, ameleta ndege ili tutangaze nchi yetu katika utalii. Mheshimiwa huyu amefungua barabara ukihesabu toka miezi miwili iliyopita hawezi kukaa wiki moja bila kufanya kazi, haijawahi kutokea Rais wa namna hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, tusichoke kumuunga mkono. Kwanza ametupa heshima katika Chama chetu cha Mapinduzi, nawashangaa Wabunge wa Chama cha Mapinduzi ambao wanabeza mafanikio. Wengine wana hasira, kama hasira zako peleka nyumbani, lakini Chama cha Mapinduzi chini ya utekelezaji wa Ilani amefanya. Umpende usimpende, ndio Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza Mawaziri wake, wote wamemwelewa. Maana yake nikianza kumchambua Waziri wa Ujenzi, nikichambua Mawaziri wengine ambao bajeti zao zimepita, wote kila mtu anafanya kazi kwa bidii na umakini. Naibu Mawaziri wanakimbizana utafikiri panya, huyu katokea huku, huyu kaenda huku, mwingine analia, mwingine anabeba ndoo, wote wana lengo moja katika kujenga nyumba moja ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze Waheshimiwa Wabunge wa Upinzani, juzi wameunga mkono bajeti ya afya kwa asilimia mia, hongereni sana. Kwa sababu wanaelewa ukweli na sisi kama kwa wenzetu wamefanya kitu kizuri kwa kupongeza Serikali ya CCM basi na sisi tuwapongeze. Tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kero ndogondogo ambazo najua zitafanyiwa kazi, lakini kuna baadhi ya ma- engineer hawako makini. Kuna barabara za ndani za Mkoa wa Dar es Salaam, ni mbovu.

Waheshimiwa Wabunge, kusifia nitarudia bado naendelea! Maana yake hiyo inawachoma wengi!

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara za ndani za Mkoa wa Dar es Salaam ni mbovu. Kwa mfano, ukiangalia Barabara ya Segerea Seminari kuelekea Majumba Sita kupitia Kituo cha Polisi pale Stakishari, barabara ni mbovu, lakini hiyo barabara Mheshimiwa Rais aliahidi akiwa kwenye mkutano pale Vingunguti, tunamwomba Mheshimiwa Waziri aiangalie barabara hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Kinyerezi kwenda Malamba Mawili, tunaomba kasi iongezeke. Barabara tumeona imeharibika, Daraja la Kivule lile tunaomba pia kasi na umakini uongezeke; tunaomba ma- engineer wenye umakini waongezwe katika Mkoa wa Dar es Salaam maana kuna wengine hawako makini. Leo sipendi kuwataja watu, lakini kuna watu wanakera, tunaomba umakini katika kuangalia barabara zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile naomba Uwanja wa Ndege wa Musoma ujengwe.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpongeza Waziri wa Maji, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na watenddji wote walioshiriki katika kutekeleza miradi ya maji hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie kwa kueleza changamoto zilizoko katika sekta ya maji na umwagiliaji. Kumekuwa na matukio mengi ya maafa yanayosababishwa na mafuriko ya mvua nyingi hali ambayo husababisha uharibifu wa mali na hata vifo vingi kwa wananchi wetu vilivyotokana na mafuriko ya mvua hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Idara hii ya Umwagiliaji inakuwepo kipindi chote cha awamu zote na utawala na kumekuwa na matamko na ahadi mbalimbali kwa kuahidi kujenga mabwawa na miundombinu ya kilimo cha umwagiliaji hapa nchini, lakini hakuna matokeo ya kuridhisha katika sekta hii ya umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua kwamba jiografia ya nchi yetu ya Tanzania imejaaliwa na Mwenyezi Mungu kuwa na mabonde mengi ya kuvuna maji, mito, maziwa, milima mingi na rasilimali ya mvua, vyote hivi vikitumika ipasavyo tunaweza kutatua changamoto kadhaa kama za kilimo cha umwagiliaji na kutenga maeneo ya malisho kwa ajili ya wafugaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na upotevu mkubwa wa maji ya mvua ambayo hutiririka mabondeni kuelekea kwenye makazi na mashamba ya watu, hali hiyo husababisha maafa na uharibifu mkubwa wa mali na hata vifo vingi kutokana na mafuriko na mvua nyingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokanana maafa hayo mara nyingi Serikali hulazimika kutoa misaada mbalimbali kwa dharura kwa ajili ya wahanga hao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ingewekeza kwenye kujenga miundombinu ya umwagiliaji kwa kujenga mabwawa kwa ajili ya kilimo cha kisasa cha umwagiliaji na kujenga miundombinu kwa ajili ya malisho ya wafugaji. Kwa kuwekeza katika sekta hii ya umwagiliaji kutasaidia kutatua tatizo la ajira kwa vijana na akinamama. Vilevile kutasaidia kupunguza mafuriko ya mara kwa mara kwa kuwa maji mengi ya mvua yatavunwa kwa ajili ya umwagiliaji na malisho, hivyo ugomvi baina ya wakulima na wafugaji utakuwa umekwisha. Maana mapigano yanasababishwa na ukosefu wa malisho kwa mifugo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali ihamasishe wananchi jinsi ya kuvuna maji ya mvua na hasa katika taasisi za umma kama shule, taasisi za kiserikali na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali itenge fedha kwa ajili ya kuwekeza katika kujenga miradi mikubwa ya mabwawa kwa ajili ya malisho ya mifugo yote hapa nchini. Awamu ya Tano inasthili sifa kubwa kwa mageuzi makubwa katika sekta ya maji, kazi kubwa inaendelea na inaonekana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Waziri wa Ujenzi, Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu, watendaji wote katika Wizara hii kwa kazi kubwa waliyoifanya chini ya uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Tanzania kwa jitihada za makusudi za kubadilisha maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie mambo machache yafuatayo nikianza na viwanja vya ndege, barabara za Mkoa wa Dar es Salaam na usafiri wa ndege za ATCL.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege kuhakikisha vifaa vyote muhimu vinavyohitajika kwa ajili ya usalama wa anga na usalama wa ndege wakati inatua kwenye viwanja, kwa kuweka alama, taa ambazo rubani wa ndege anaweza kuziona wakati kunapokuwa na ukungu mkubwa kwenye viwanja vya ndege ili kuepusha athari kubwa (usalama kwanza).

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na upungufu wa viwanja vya ndege ambavyo havikidhi viwango vitakavyowezesha ndege kubwa kuweza kutua katika viwanja hivyo kwa sababu mbalimbali kama kiwanja cha ndege cha Musoma, kiwanja cha ndege cha Mugumu – Serengeti (kwa ajili ya hifadhi), kiwanja cha ndege cha Iringa na kiwanja cha ndege cha Singida.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuboresha viwanja hivi kutasaidia maeneo hayo kujiimarisha kiuchumi na kiusalama, kutokana na kiwanja cha Musoma na Mugumu ni eneo la kiutalii na ndiyo kuna Makumbusho ya Muasisi wa nchi yetu Baba wa Taifa Mwalimu J. K. Nyerere. Hivyo, wageni wengi kutoka nchi jirani na watalii wengi kupitia Musoma kwenda Serengeti National Park.

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanja cha Iringa ni muhimu sana kuboreshwa kutokana na uhitaji wa uharaka wa watumiaji pia ni kiwanja ambacho kiko karibu na kiwanja cha ndege cha Dodoma ambacho inapotokea dharura mfano ndege kupungukiwa na mafuta inaweza kutua kiwanja cha karibu cha Iringa na Singida.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu barabara za Mkoa wa Dar es Salaam; katika sekta ya barabara kumekuwa na changamoto nyingi katika barabara za mitaani, hali hii imesababisha adha na kero kubwa kwa wakazi wa Mkoa huo. Barabara ya Tabata kuelekea Segerea - Kinyerezi - Malamba Mawili - Msigani mpaka Mbezi kumekuwa na ongezeko kubwa la watu wanaohamia, kwa sababu hiyo kumekuwa na changamoto ya foleni kubwa ya magari ambayo huchukua masaa mawili mpaka matatu hali hiyo husababisha watu kuamka mapema sana kuwahi foleni isiwakute muda wa saa 11.30 alfajiri ndiyo muda mzuri wa kuwahi kwenda mjini ili kuepuka adha hiyo. Tunaomba Serikali itafute utaratibu wa kuipanua barabara hiyo ili iweze kusaidia kutatua kero hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahadi ya Mheshimiwa Rais ya barabara ya Segerea Seminary kuelekea Majumba Sita kupitia Kituo cha Polisi cha Stakishari Mheshimiwa Rais wa Tanzania aliahidi kuijenga kwa kiwango cha lami na daraja wakati akiwa kwenye mkutano wa kampeni mwaka 2015 katika viwanja vya Vingunguti. Naiomba Serikali itimize ahadi hiyo maana hali ya barabara hiyo ni mbaya sana, wananchi wanalalamika kwa kukosa barabara ya uhakika.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Waziri wa Ulinzi na JKT, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, Mkuu wa Majeshi, Mkuu wa JKT, Makamanda wote wa vikosi, Maofisa, Askari, Taasisi zote zilizo chini ya Jeshi na Watendaji wote walioshiriki na kufanikisha kazi nzuri katika jeshi la letu. Nichukue fursa hii kuwapa pole kwa vifo vya wanajeshi wetu waliopoteza maisha wakiwa katika ulinzi wa amani nchini DRC, Mwenyezi Mungu awape pumziko la amani na milele. Amina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Wananchi wa Tanzania limekuwa ni msaada mkubwa na tegemeo la Watanzania, jeshi letu limeshiriki katika ukombozi wa Kusini mwa Bara la Afrika, (Zimbabwe, Msumbiji, Angola, Namibia), Afrika Kusini na kadhalika. JWTZ limeshiriki kumpiga Nduli Idd Amin Dada aliyevamia nchi yetu Mkoani Kagera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo ya ulinzi wa nchi yetu JWTZ limeshiriki katika shughuli mbalimbali za kijamii na hata kusaidia kuwaokoa wananchi pale wanapopatwa na majanga mbalimbali kama, matukio ya Lindi na Mtwara mwaka 1990, kuzama kwa meli ya MV Bukoba, kuzama kwa meli ya MV Spice Island 1-Zanzibar, ajali ya Treni-Dodoma, mafuriko ya Kilombero, madaktari wa kijeshi kutibu raia (dharura), mlipuko wa mabomu ya Mbagala na Gongo la Mboto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jeshi limetumika kufanya kazi kwa ufanisi na uadilifu mkubwa na kwa wakati. JWTZ limeshiriki kusomba mbolea kupeleka mikoani, JWTZ limeshiriki pia kusomba vitabu kuvigawa mikoani. Jeshi limeshiriki kusaidia kuokoa wananchi pale wanapopatwa na ajali za barabarani , majanga ya moto na mafuriko mbalimbali. JWTZ limekuwa ni tegemezi la Watanzania na hata nchi za Bara la Afrika lina heshima na kuthamini mchango wa jeshi letu, kwa sababu zote hizo na nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali itenge fedha nyingi zaidi kwa majeshi yetu ili waweze kukidhi mahitaji yanayoendana na hali ya sasa na matishio ya kigaidi kwa kutenga fedha za mafunzo yanayoendana na teknolojia za kisasa kwa kuwapelekea vijana wetu nje ya nchi kupatiwa mafunzo na mbinu mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kununua vifaa na mitambo ambayo inaweza kung’amua au kutambua viashiria vya hatari kabla ya mashambulizi (mfano DRC) ugaidi. Ziara za Kimataifa kwa makamanda za mara kwa mara ili kujifunza mambo mapya ya kiulinzi, kujenga makazi ya Askari wote kwa kuomba mkopo wa nyumba wa muda mrefu na kwa riba nafuu ili kukidhi mahitaji ya Askari wetu, ambao ndiyo tegemeo la Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, JKT ipewe fedha kwa ajili ya kuanzisha mashamba makubwa kwa kilimo cha alizeti, ufuta, mchikichi na mazao ambayo yanatoa mafuta na kufanya hivyo kutasaidia kuondoa tatizo la upungufu wa mafuta ya kula hapa nchini. JKT ina rasilimali ardhi kubwa, watu na uongozi imara utakaoweza kufanikisha kilimo hicho. Kwa kufanya hivyo kutasaidia JKT kuingiza fedha zitakazotokana na mauzo ya mbegu za mafuta au kuanzisha viwanda vya kusindika mafuta ya kula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono asilimia 120.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwapongeza viongozi na watendaji wote walioko katika Wizara hii kwa kazi nzuri waliyofanya wakiongozwa na Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Makatibu Wakuu, hakika nawapa pongezi kubwa kwa bidii na uzalendo mlionao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo, kuna changamoto kubwa zinatakiwa kupatiwa ufumbuzi/ majibu ili kuleta tija na iweze kupatikana kwa nchi na wananchi kwa ujumla. Changamoto hizo ni kama ifuatavyo; Vyuo vya Ufundi - VETA na uwekezaji mkubwa, Serikali kutumia mitaala kwa lugha ya kiswahili kwa vyuo vya ufundi/VETA kwa ajili ya vijana wanaomaliza darasa la saba, vyuo vya kati kutobadilishwa kuwa vyuo vikuu na elimu ya watu waliyoikosa (elimu ya watu wazima).

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vyuo vya Ufundi (VETA) kumekuwa na speed ndogo katika uwekezaji na ujenzi wa vyuo vya ufundi katika nchi yetu na kuzingatia kuwa eneo hili ndilo linalobeba vijana wengi ambao ndiyo nguvu kazi ya Taifa lolote duniani. Kutowekeza katika vyuo vya ufundi
kutasababisha wimbi la vijana kutojishughulisha na kazi na hasa vijana wengi kukimbilia kufanya biashara za kimachinga ambazo ni za kubahatisha na pia kujiunga na makundi ya hovyo/ulevi, kushiriki kwenye mitandao yenye kuharibu maadili yetu ya Kitanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali iwekeze kwa kiwango kikubwa katika ujenzi wa Vyuo vya Ufundi (VETA) majengo, walimu, vifaa vya kujifunzia, wataalam wa fani ambazo zitakidhi soko la ndani na nchi jirani zinazotuzunguka, mitambo na teknolojia zinazoendana na wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutumia mitaala ya kiswahili kwa Vyuo vya Ufundi (VETA) kwa ajili ya vijana wa darasa la saba kumekuwa na ufanisi mzuri kwa vijana wetu waliomaliza darasa la saba ambao hujishughulisha na kazi ya ufundi kutengeneza magari, mafundi wa umeme wa magari, mafundi welding, mafundi waashi, mafundi mchundo, mafundi wa umeme wa majumbani, mafundi wa computer na kadhalika. Hawa wote kwa asilimia kubwa ni vijana waliomaliza darasa la saba na form form.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia hayo yote ni vema Serikali ikatumia mitaala ya kiswahili kwa Vyuo vya Ufundi na VETA ili itumike kwa vijana wetu wa standard seven na form four ambao wote hawa ndiyo nguvu kazi kubwa inayojihusisha na fani za aina mbalimbali za ufundi. Kwa mafunzo hayo, vijana wataweza kuongeza tija na ufundi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vyuo vya kati kubadilishwa kuwa vyuo vikuu; kumekuwa na ongezeko la kubadilisha vyuo vya kati na kuwa vyuo vikuu hali hii inadhoofisha vyuo vya kati ambavyo ndivyo vyenye kulenga kutengeneza ajira kwa vijana wengi. Naomba Serikali isitishe suala la kubadilisha vyuo vya kati kuwa vyuo vikuu na badala yake vyuo hivyo viimarishwe kwa kiwango kikubwa na miundombinu ya ufundi, wataalam, wakufunzi na kadhalika, uwekezaji wa vyuo hivyo kwa kuzingatia soko la ndani kama inavyofanyika nchi ya Singapore.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi ya Singapore inawekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta ya elimu ya ufundi kwa kulenga soko la ajira kwa vijana na kuangalia soko la ndani na nje (nchi jirani). Nchi hiyo inatengeneza vifaa vingi vya kielektroniki kama vifaa vya umeme vya aina zote. Hii imesaidia vijana wengi kwa asilimia 95, vijana wako viwandani wanazalisha bidhaa mbalimbali.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwapongeza Waziri wa Kilimo, Naibu Waziri wa Kilimo, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na watendaji wote walioshiriki katika kutenda na kusimamia shughuli zote zinazohusika na kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo, kuna changamoto ambazo zinatakiwa kupatiwa ufumbuzi wa haraka ili kukidhi mahitaji ya Watanzania kwa kuzalisha mazao ya chakula na biashara kwa kupunguza uagizaji wa mafuta ya kula na sukari kutoka nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, iwapo nchi yetu itazalisha mazao ya mbegu za mafuta ya kula na sukari kwa kiwango kikubwa, kwa Serikali kuwekeza kwenye kilimo cha miwa na mbegu za mafuta kuongeza mashamba na kushiriki. Jeshi la Magereza, Jeshi la Kujenga Taifa na wawekezaji kutoka nje ya nchi na Watanzania wenyewe kwa kuweka mazingira mazuri ya kilimo, kuweka miundombinu ya umwagiliaji kama kuvuna maji ya mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kushirikisha nguvu kazi ya vyombo vya ulinzi itasaidia vijana wetu kushiriki kikamilifu katika kuzalisha mazao mbalimbali na pia itasaidia vijana kupata ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mazao makuu ambayo ni ya kiuchumi hapa nchini yanapaswa kuwekewa mkakati wa kudumu na endelevu kwa kuweka misingi imara. Kilimo cha kisasa cha umwagiliaji hakikwepeki katika zama za sasa.

Kilimo kiendane na dhana ya Tanzania ya viwanda kwa vitendo, kila Wizara inahusika na kushabihiana na Tanzania ya viwanda.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Spika, pamoja na hatua nzuri zilizochukuliwa katika kutatua changamoto zilizoko katika sekta ya uvuvi na mifugo, kuna changamoto nyingi ambazo zinahitaji kupatiwa ufumbuzi wa haraka. Naomba nichangie changamoto chache kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, sekta ya uvuvi itaendelea iwapo itapata msukumo kwa kuwekeza kwa kiwango kikubwa kama kuwekeza kwa wataalam ambao wataendana na teknolojia ya uvuvi wa kisasa, ununuzi wa vifaa vya kisasa vya uvuvi na uhifadhi wa samaki, elimu, semina za mara kwa mara kwa wavuvi wadogo wadogo. Viongozi wa Serikali watumie lugha ya kuelimisha wavuvi kuliko kutumia nguvu zaidi, hali wakijua uelewa wa watu uko tofauti. Ndiyo maana Baba wa Taifa alitumia kampeni ya kuelimisha na kuhamasisha watu katika mambo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, vilevile Serikali iweke mazingira ya kujenga mabwawa ya kufugia samaki kwa kila Halmashauri ili wananchi waweze kupata lishe na pia kufanya biashara na kuongeza ajira kwa vijana. Kwa kufanya hivyo kunaweza kupunguza malalamiko ya uvuvi. Pia Kanda ya Ziwa itumike kujenga mabwawa ya ufugaji wa samaki kando kando ya Ziwa Victoria, kwa kiwango kikubwa bila kusahau kuwaelimisha wavuvi wadogo wadogo. Uvuvi wa bahari kuu ndiyo mkombozi wa kuingiza fedha za kigeni. Vilevile nguvu iongezwe kupata makampuni makubwa ya kuvua samaki katika bahari ya kina kirefu (Deep Sea Fishing).

Mheshimiwa Spika, sekta ya mifugo ndiyo tegemeo la wanadamu karibu wote kwa maana ya kwamba kabla ya mtoto kuzaliwa, mama mjamzito hushauriwa kunywa maziwa, mtoto akizaliwa hunywa maziwa, mgonjwa hunywa maziwa, mzee chakula chake ni maziwa na sisi maziwa ndiyo chakula chetu cha kila siku. Serikali iangalie uwezekano wa kuwekeza katika sekta hii, kwa kuwa inawagusa wananchi wengi walio maskini sana, pia uelewa wao ni mdogo ingawa wana mifugo mingi. Ubora wa mifugo na unafuu wa kodi ambazo ni kikwazo kwa mazao ya mifugo kama nyama, maziwa, ngozi, jibini, mifupa, mbolea na kadhalika. Kupiga chapa ng’ombe kuangaliwe kwa kuweka alama eneo la masikioni kuliko kuweka pajani au tumboni. Hali hiyo huharibu ubora wa ngozi.

Mheshimiwa Spika, ombi langu ni kwamba Serikali ifanye uwekezaji mkubwa katika sekta ya mifugo na uvuvi ili kufanya mageuzi na mapinduzi katika sekta hizi bila kusahau sekta ya kilimo pia.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpongeza Waziri, Naibu Waziri, Katibu na Watendaji wote walioko katika Wizara hii. Pamoja na pongezi nina machache yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itenge fedha za kutosha kwa Balozi ambazo zinatumika nchi tatu mpaka tano ili Balozi aweze kuzitembelea na kutafuta fursa za kiuchumi kama utalii, viwanda na usalama na uwakilishi uwe wenye manufaa katika nchi hizo. Ofisi za Ubalozi zitengewe fedha za ukarabati wa ofisi za ubalozi na nyumba za watumishi katika Balozi husika ili ziendane na hadhi ya nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanja vya Ubalozi ambavyo havijajengwa vitengewe fedha kwa ajili ya ujenzi wa ofisi za Ubalozi na makazi ya Balozi zetu na watumishi wake. Kwa mfano, kiwanja cha Ubalozi Jijini London kimetelekezwa na kimejaa magugu na mbwa mwitu. Kila ofisi za Ubalozi wetu nje ya nchi ziwe na wataalam wa fani ambazo zitasaidia kuiuza nchi yetu kiutalii, kiutamaduni, lugha ya Kiswahili, kuvutia wawekezaji kuja Tanzania kujenga viwanda, Kujenga hospitali za kitalii kwenye website ya kila Ubalozi kuwe na vivutio vyote vilivyoko katika nchi yetu ili kila mtalii aamue ni eneo gani anapenda kwenda kutalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, kuna mazoea ya kuona vivutio vichache tu Serengeti National Park, Mlima Kilimanjaro, Ngorongoro Crater, Zanzibar lakini ukiangalia nchi yetu ina vivutio vingi sana kama, Kitulo National Park, Ruaha National Park, Manyara National Park, Mahale National Park, Maporomoko ya Kalambo (Rukwa), Gombe National Park, Saa Nane Island, Arusha National Park, Tarangire National Park, Udzungwa National Park, Kilimanjaro National Park, Serengeti National Park, Selou National Park, Majengo ya Kale Kilwa, Mafia, Bagamoyo, Olduvai George, Nyagoza Mtu wa Kale, Mapango ya Amboni Tanga, Kaburi la Baba wa Taifa Mwalimu Julius K. Nyerere – Butiama, Fukwe za Bahari, Utalii wa Water Sports (Bahari na Maziwa Victoria, Tanganyika na Nyasa - Matema Beach). Maeneo ya kale Mtwara Mikindani na Utamaduni wa Ngoma za asili na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba vivutio hivyo vyote na vingine ambavyo sikuvitaja viwekwe kwenye matangazo mbalimbali duniani na hasa ziwekwe kwenye website za kila Balozi zetu nje ya nchi. Balozi ziandae maonesho kwa lengo la kuitangaza nchi yetu ya Tanzania, katika sekta za utalii, kiutamaduni na kutumia fursa ya kijiografia ya nchi yetu kupakana na nchi zaidi ya tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Spika, napenda kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa tijihada kubwa inayofanyika katika kutatua changamoto za Watanzania katika sekta mbalimbali za huduma za jamii ambazo fedha zote zilizotolewa zinatoka katika Mfuko wa Hazina.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amekuwa ni kinara wa kuleta mabadiliko ya kiuchumi na kijamii kwa Watanzania kwa kuboresha huduma za kijamii kwa kuongeza mapato na udhibiti wake kwa kiwango cha kuridhisha. Mheshimiwa Rais amekuwa makini kwa kuteua wasaidizi wake makini kama Waziri wa Fedha, Naibu Waziri wa Fedha, Katibu Mkuu, Naibu Makatibu Wakuu watatu, Kamishna Mkuu wa TRA na watendaji wote walioko chini ya Wizara hii ya Fedha kwa jitihada kubwa walizozifanya katika kusimamia kikamilifu na juhudi kubwa katika kupanga na kutekeleza. Pamoja na pongezi, nina mambo machache kama changamoto kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, moja, ununuzi wa pamoja (bulk procurement), Serikali itafute uwezekano wa kuwa na matenki ya kuhifadhi mafuta kwa ajili ya usalama wa nchi (national reserve) kuliko kutegemea matenki ya makampuni binafsi. Mafuta hayo yanaweza kuhifadhiwa na taasisi ya Serikali kama GPSA.

Mheshimiwa Spika, pili, ni mafunzo kwa watendaji wa fani ya ununuzi na ugavi. Kuwe na bajeti ya kutosha kwa ajili ya mafunzo ya mara kwa mara kwa watumishi wa Serikali na taasisi zake katika fani ya ununuzi na mikataba (procurement and contract management course) kwa kuzingatia kwamba asilimia 90 ya matumizi ya Serikali ni manunuzi ya umma. Hivyo basi, watendaji wa fani hii wawe na weledi na uadilifu wa kutosha kwa kuwapatia mafunzo ya ndani na nchi na nje kwa kushirikiana na PCCB katika kutoa mafunzo.

Mheshimiwa Spika, tatu, ni kuhusu miradi kwa njia ya ubia (PPP). Kwa kuwa nchi yetu kwa sasa ina uhitaji mkubwa wa kufanya miradi mikubwa ya miundombinu ya aina mbalimbali kama barabara kubwa za kisasa, madaraja makubwa, vivuko, shopping malls, airport, hotel za kitalii, hospitali, viwanja vya michezo, viwanda, kilimo cha kisasa cha umwagiliaji na kdhalika, miundombinu hii inahitaji miradi ya ubia baina ya Serikali na makampuni binafsi ili kwa pamoja miradi hiyo iweze kuchochea uchumi wa nchi na watu binafsi.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu hiyo, bado kuna upungufu wa watalaam wa fani ya PPP na mikataba. Hivyo kuna uhitaji wa vijana wetu kwenda nje ya nchi kujifunza fani hiyo (PPP, Procurement and Contract Management) kwa kuzingatia nchi zilizobobea kwa miradi ya PPP kama China na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, nne, Maofisa wa Kodi TRA wanaofanya tathmini kwa wajasiriamali au wafanyabiashara wa ngazi zote kwa kukadiria bidhaa/biashara kwa kiwango cha juu sana kuliko faida ya biashara husika, TRA iangalie uwezekano wa kufanya tathmini kwa kuzingatia uhalisia wa biashara husika.

Mheshimiwa Spika, tano, vyanzo vipya vya mapato; TRA kupitia Wizara hii iangalie vyanzo vipya vya mapato hata kwa kwenda kujifunza kwa wenzetu nje ya nchi ili kuongeza wigo zaidi wa kuongeza mapato ya nchi. Ukiangalia nchi yetu inapokea meli nyingi zinazoingia hapa nchini. Mfano, ndege, magari makubwa, viwanda na mitambo mikubwa ambayo hutoa hewa chafu (air pollution). Eneo hili linaweza kuwa chanzo cha mapato kipya kwa kutoza kodi (carbon tax) kwa kuzingatia nchi kadhaa duniani, kutumia utaratibu wa kutoza kodi eneo hili. Nchi kama India, South Africa na kadhalika hutumia aina hiyo.

Mheshimiwa Spika, nashauri pia Serikali iwekeze kwenye kilimo cha kisasa cha umwagiliaji kwa mtazamo wa matokeo makubwa kwa muda mfupi, kwa kuzingatia mazao ya muda mfupi yenye kuleta tija. Kwa mfano, mazao ya mafuta ya alizeti, ufuta, pamba na mazao ya mahindi, ngano, maua, mchele na kadhalika. Maeneo kama haya yakifanyiwa uwekezaji kwa ubia kati ya Serikali na sekta binafsi itaweza kuchochea uchumi wa watu binafsi na Serikali. Pia itasaidia kuongeza mapato kwa kuzingatia mahitaji ya mafuta ya kula duniani ni makubwa sana; hata mahitaji ya ngano, mahindi, mchele na kadhalika ni makubwa pia.

Mheshimiwa Spika, pongezi kubwa kwa Wizara na TRA. Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia kuwapongeza Watendaji na Viongozi wote wa Wizara hii wakiongozwa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na vikosi vyote vilivyoko katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vijana wetu waendesha bodaboda hasa walioko Mkoa wa Dar es Salaam, kwa asilimia 90 hawana usikivu na utu wa kutosha kwa Jeshi la Polisi, kupitia Idara ya Usalama Barabarani kwa kutozingatia usalama wa raia wakati wawapo barabarani. Vijana wengi wa bodaboda huendesha wakati wakiwa wamekunywa pombe au kuvuta bangi. Hali hiyo husababisha ajali nyingi za bodaboda na hivyo kuua na kujeruhi wananchi wengi wasiokuwa na hatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Jeshi la Polisi kupitia Idara ya Usalama barabarani liangalie upya jinsi ya kuzuia ajali zilizokithiri katika Mkoa wa Dar es Salaam zinazofanywa na vijana waendesha bodaboda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuwapongeza Makamanda wa Usalama Barabarani katika Mkoa wa Dodoma kutokana na waendesha bodaboda kutii kwa kufuata Sheria za Usalama Barabarani. Vijana wa Dodoma tumewaona wakisimama kwa kuwapisha wananchi kuvuka kwa dakika mbili mpaka tatu. Kwa kitendo hicho sisi tunaotoka Mkoa wa Dar es Salaam imetushangaza kuona vyombo vya moto (pikipiki) kusimama kwa adabu na kuheshimu watu wasipatwe na ajali na kuacha ulemavu na hata vifo kwa raia wetu wasiokuwa na hatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali ifanye utaratibu wa kuwapatia fedha Idara ya Upelelezi kwa ajili ya mafunzo mbalimbali ikiwemo kuepuka kulaumiwa kwa baadhi ya Maafisa Upelelezi ambao wanalichafua Jeshi letu kwa kupokea rushwa kutoka kwa walalamikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na tabia ya baadhi ya Wapelelezi kutotenda haki kwa walalamikaji wakati wanapokwenda kushtaki katika Vituo vya Polisi. Wapelelezi hao hubadili kibao kwa walalamikaji na kutoa upendeleo kwa watuhumiwa. Hali hiyo inaashiria kuna mkono wa rushwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Jeshi litafute jinsi ya kukomesha tabia hiyo kwa baadhi ya Maofisa hao Wapelelezi. Pia Maofisa hao wapatiwe usafiri na fedha za mafuta na makazi bora ili waweze kutimiza wajibu wao wa kazi kwa ufanisi na tija. Kwa kuwapatia nyenzo au vitendea kazi kutaweza kuepusha vishawishi kwa wahalifu/watuhumiwa kwa kuwashawishi Maofisa hao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Kituo cha Polisi Segerea (jirani na Ofisi ya Mtendaji wa Kata ya Segerea) kijengwe au kimaliziwe na kupatiwa samani, gari na Askari wa kutosha ili waweze kuimarisha ulinzi katika eneo hilo la Segerea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, narudia kuwapongeza wote waliohusika na utekelezaji katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru kwa kuweza kunipa fursa hii. Pia nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa zawadi ya uhai na kuweza kusimama hapa katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara kupitia jeshi la polisi itupatie taarifa ya kifo cha Chacha Wangwe, tunaomba taarifa ya kifo cha Mchungaji Mtikila, tunaomba taarifa ya watalii waliomwagiwa tindikali kule Zanzibar, tunaomba taarifa ya Makanisa yaliyochomwa moto Zanzibar. Tukumbuke nchi yetu iko hapa kwa mkono wa Mwenyezi Mungu na tangu kuhasisiwa kwake tangu enzi ya Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, enzi ya Mzee Mwinyi, enzi ya Mzee Mkapa, enzi ya Mzee Kikwete na sasa hivi enzi ya ndugu yetu Dkt. John Pombe Magufuli. Hawa wote wamewekwa hapa kwa ruhusa na mkono wa Mwenyezi Mungu na ndiyo maana hata ukiangalia maisha yao ni ya kawaida sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba ndugu zangu tusitumie fursa ya viongozi wetu kukaa kimya na kuweza kuwatukana hovyo hovyo. Tulikuwa tukimtukana Mheshimiwa Kikwete sana, mpole tukamhujumu hata kwenye miradi yake, lakini Mwenyezi Mungu alikuwa amemsimamia alikuwa upande wake. Vilevile Rais wa Awamu ya Tano kuna mkono wa Mwenyezi Mungu na nasema watapambana lakini hawatashinda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumbukeni ndugu zangu tuliapa kuitetea na kuilinda katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa maana hiyo tulisema tutalinda Muungano kwa gharama yoyote. Tarehe 26 Aprili ni siku ambayo tunakumbuka Muungano wetu ulioasisiwa na ndiyo maana yale mazoezi na parade mlizoziona ndiyo gharama za kulinda Muungano. Kwa hiyo, tumesikia watu wanasema gharama zimekuwa kubwa tungejenga shule. Ile ni sehemu ya kulinda Muungano wetu ndiyo gharama zenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii nchi ni yetu sote humu ndani tuko kama mia tatu na kitu, lakini tukumbuke Watanzania wako zaidi ya milioni 60 sisi tunajiona kama tuna haki zaidi ya Watanzania walio wengi. Kuna wakulima, wavuvi, wamachinga, watu wasio na vyama, wenye dini, wapagani, kila mtu ana haki na hamasa ambazo zinatolewa kwa kutubagua sisi tunaomba zishindwe katika jina la Yesu na hazitafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kumpongeza IGP wetu na Makamanda wote wa Mikoa yote na Wakuu wa Mikoa kwa kazi nzuri sana wakiongozwa na Waziri, Naibu Waziri bila kumsahau Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama. Wamefanya kazi nzuri sana kuhakikisha nchi inakuwa salama, bila amani hatuwezi kulima, bila amani hamna kwenda shule, bila amani hakuna kustarehe, bila amani hamna kuzaliana, bila amani hamna kizazi endelevu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tusitanie amani kwa kutumia dini, kwa ku-convince watu kwamba dini fulani inaonewa, hakuna! Mbona wewe kama dini unabaguliwa mbona uko humu ndani? Tuko dini tofauti humu ndani, kama kungekuwa kuna ubaguzi tusingekuwepo. Tusitanie amani kwa sababu tuna dhamana ya kulinda uhuru wa nchi hii tuweze kurithisha na vizazi vijavyo. Tumeikuta nchi hii ikiwa na amani, kama mnatumika na maadui wa ndani na wa nje waambieni Tanzania haitaniwi, iko imara, hakuna utani katika masuala ya amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali iongeze bajeti ya kutosha katika vyombo vyetu vya ulinzi na usalama, tunaomba magari yaongezwe, tunaomba mafuta yaongezwe, tunaomba makazi yao yaboreshwe na kujengwa nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba maslahi ya askari; katika nchi nyingine nimetoa mfano kadhaa kule Marekani bajeti yao ya kwanza yenye kipaumbele ni ulinzi bila ulinzi yote hayawezi kutekelezeka, mbona wewe nyumbani kwako unafunga mlango, mbona unajenga geti, mbona unaweka walinzi, tusitaniane katika mambo ya ulinzi wa nchi na wala hatutishwi, sisi Wabunge wa Chama cha Mapinduzi hatutishwi na tupo imara. Mmetushika pabaya katika masuala ya amani hatutaniwi, sisi tutatoka kwenye Bunge hili na kizazi kitaendeleza ulinzi kwa sababu Mungu yuko pamoja na sisi kwa sababu Mungu ni wa amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee Jeshi la Zimamoto, kama alivyosema Mjumbe aliyemaliza kwa kweli limekuwa lina mwamko mdogo na hasa kwenye Wizara yenye dhamana ya kupanga bajeti katika jeshi hili. Tunaomba Jeshi la Zimamoto lipewe fedha za kutosha, sisi sote hapa majanga ya moto huwa yanatokea huko mtaani na majumbani kwetu, jeshi lipewe vifaa, magari ya kutosha, majengo yako marefu sana Dar es Salam, Dodoma Makao Makuu, jengo la Bunge hivi tuna vifaa vya kisasa vya kutosha kukabiliana na janga la moto, vifaa vya uokoaji au ikitokea majanga tunaita watu kutoka South Afrika? Naomba jeshi hili liimarishwe kama vilivyo vikosi vingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Idara ya Uhamiaji, naomba idara hii pia iongezewe bajeti ya kutosha kukabiliana na wahamiaji haramu, Dar es Salaam kule mkienda Kariakoo unakuta sura tofauti maana yake sisi Watanzania tunajuana. Nimwambie Mheshimiwa Waziri, wako wengi Dar es Salaam bila kutaja ni mataifa gani, mimi nakaa maeneo ya Segerea kule. Siku hizi kuna majirani wageni tunashangaa, tutumieni sisi Wajumbe wa Mabalozi wa CCM tunaweza kuwaambia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiongelee Jeshi la Magereza; Jeshi hili liongezewe bajeti ya kutosha ili wajenge makazi ya askari wapatiwe usafiri unakutana na askari magereza anaomba lifti, unakuta pale askari magereza amekaa kona anaomba lifti ni jambo la aibu mno. Anakuwa mnyonge, matokeo yake ndiyo huwa wanatukanwa hovyo hovyo. Naomba watoe pesa tuwekeze kama tunavyowekeza kwenye Stiegler’s Gorge, katika masuala ya ulinzi yapewe kipaumbele, miradi hii yote mikubwa haiwezi kutekelezwa kama hamna ulinzi wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudie kusema sisi tutakuwepo, tutaondoka watakuja wengine, lakini kizazi cha Watanzania cha sasa na cha kijacho kinatutegea sisi, ulimi wetu tuutumie vizuri, tukiongozwa na roho ya Mungu, tusitumie dini kudanganyana hapa, hata mpagani anaweza kuona ufalme wa mbingu wewe ambaye unasema unadini ukapelekwa motoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kwa kipekee kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi na juhudi kubwa anayoifanya ya kusimamia na kulinda rasilimali za nchi yetu ya Tanzania. Kwa kipindi cha miezi michache ya utekelezaji matokeo mazuri yameonekana. Hongera sana Mheshimiwa Rais, Mwenyezi Mungu akulinde wewe na Serikali yako.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpongeza Waziri wa Madini, Naibu Mawaziri, Katibu Mkuu, taasisi zote zilizo katika sekta hii ya madini na watendaji wote wa Wizara hii ambao wameshiriki katika kufanikisha kazi nzuri. Kipekee, niwapongeze Mheshimiwa Waziri wa Madini na Manaibu wake wamekuwa wakifanya kazi kwa bidii na kufuatilia kwa ukaribu sana maeneo mengi ya migodi na kutatua changamoto zilizoko katika sekta hii ya madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizo, naomba nichangie mambo au maoni machache kama ifuatavyo:-

(i) Serikali itafute uwezekano wa kuainisha aina zote za madini zinazopatikana hapa nchini na ionyeshe faida zake na masoko yake nje ya nchi. Pia kuwe na maonesho ya mara kwa mara ya uelewa na kuweza kuchukua fursa ambazo zinaweza kutoa ajira nyingi zaidi kwa vijana kwa kuuza vito na madini mengine ya ujenzi na malighafi na kadhalika.

(ii) Naomba Serikali itoe mafunzo ya vitendo kwa wachimbaji wadogo wadogo na wa kati ili waweze kuongeza ujuzi wa kuchenjua madini ya aina mbalimbali.

(iii) STAMICO ijengewe uwezo kwa kupatiwa fedha za kutosha ili iweze kujiendesha kwa ufanisi na tija.

(iv) Ufanyike uhakiki/sensa kwa wachimbaji wote wadogo wadogo ili Serikali na Shirikisho la FEMATA waweze kuwatambua kwa kuwapatia vitambulisho maalum. Hii itasaidia kuzuia watu wasio Watanzania kuvamia migodi yetu bila utaratibu wa kisheria na wakati mwingine baadhi yao hufanya uhalifu na kukimbilia nchi jirani bila kujulikana.

(v) Madini ya ujenzi kama kokoto, gypsum, madini ya kutengeneza marumaru (tiles), changa na kadhalika. Migodi ya aina hii inapaswa kusimamiwa kwa ukamilifu kama yalivyo madini mengine ikizingatiwa matumizi yake ni makubwa mno. Migodi hii hupoteza kiasi kikubwa cha fedha za Serikali kwa kutokuwa na utaratibu mzuri wa uchimbaji na usimamizi pia hata utozaji wa ushuru katika madini hayo.

(vi) Viongozi wa ngazi za aina zote wawe na lugha zinazoleta au kuashiria utaifa kuliko kutumia lugha kibaguzi kwa kutumia madini, mazao, vitega uchumi na kadhalika. Mara nyingine baadhi ya viongozi hutoa lugha ya kusema madini haya ni ya mkoa fulani hayawezi kuuzwa mkoa fulani au mazao fulani yauzwe kupitia bandari fulani. Lugha hizi zinabomoa nchi na ni hatari sana kwa kizazi kijacho.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja 100%.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE.JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwapongeze Mawaziri, Naibu Mawaziri na watendaji wote kwa kazi nzuri wanayoifanya chini ya uongozi wa Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, Awamu hii ya Tano ya utawala wa Jemedari wetu Mkuu, Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, ameudhihirishia ulimwengu inaumahiri na uhodari, maarifa na umakini mkubwa wa kufanya mageuzi ya kiutendaji kwa watumishi wa umma na kupiga vita rushwa na ufisadi, uzembe kazini na uwajibishwaji wa viongozi wazembe. Kwa sababu hiyo na nyinginezo, nashauri kuwe na mfumo endelevu kwa awamu zote za utawala wa nchi utaozingatia uwajibikaji na uwajibishwaji watumishi wa umma ambao hawazingatii viwango vilivyopangwa ili kuleta tija kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii itasaidia baada ya awamu hii muda wake wautawalakuisha. Nidhamu na mifumo hii iendelee bila kutupwa kapuni kama yalivyotupwa au kuachwa mambo mazuri ya Awamu ya Kwanza. Mazuri mengi ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Magufuli, Rais wa Tanzania hayapaswa kuachwa hata kidogo. Kizazi hiki kitahukumu iwapo Awamu zinazofuata zitasahau mazuri haya. Mungu ibariki Tanzania naviongozi wote, amina.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia 100.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Spika, naomba kumpongeza Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, taasisi zote zilizoko katika Wizara na watendaji wote kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Spika, sekta ya michezo na burudani, iwapo itasimamiwa vizuri kwa kutenga bajeti ya kutosha itasaidia kuongeza mapato ya Serikali kwa kiwango kikubwa lakini pia michezo inaitangaza nchi kiutalii duniani.

Mheshiimiwa Spika, kwa mfano, michezo kama mpira wa miguu, riadha, wasanii wa muziki, wasanii wa vichekesho (stand up comedy), ngoma za asili na wasanii wa maigizo (sinema); hawa wote ni chanzo kikubwa cha mapato yao wenyewe na hata Serikali inaweza kupata kodi yake kwa kiwango kikubwa iwapo kutakuwa na uwekezaji wa kisasa kwa sekta hii. Naiomba Serikali iwekeze kwa kiwango cha kutosha katika Sekta ya Michezo.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Spika, naipongeza Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na taasisi zake kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Spika, katika Nchi ya India kwa suala la usalama barabarani, wao ikifika saa tatu usiku huanza kuwakagua madereva wote ili kutambua kilevi kwa lengo la kuzuia vifo vingi vinavyotokana na ajali za barabarani wakati wa usiku. Kwa mfano huo wa Nchi ya India, naliomba Jeshi letu la Polisi liangalie uwezekano wa kuanzisha utaratibu huo wa ukaguzi wa kilevi kwa madereva wakati wa usiku ili kuzuia ajali nyakati za usiku ambazo nyingi zinasababisha vifo kutokana na ulevi wa madereva.

Mheshimiwa Spika, Madereva wa Serikali wadhibitiwe kwa kuendesha magari kwa kasi na kutoku-overtake sehemu za hatari.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Spika, naomba niwapongeze Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu, Watendaji na Taasisi zote zilizo chini ya Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, kuhusu mawasiliano, katika Jiji la Dodoma eneo la pembezoni Kata ya Mbalawala, Kijiji cha Lugala – Matangizi hakuna mawasiliano ya simu hali ambayo inasababisha wagonjwa kutopata huduma kwa haraka kutokana na umbali wa eneo hilo. Naomba wananchi hawa wapatiwe mawasiliano ya simu ili waondokane na changamoto hii.

Mheshimiwa Spika, kuhusu barabara ya Seminari, mnamo mwaka 2015 wakati Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akiwa mgombea wa Urais aliwaahidi wananchi wa Jimbo la Segerea kuwa barabara ya Segerea - Seminari - Majumbasita (km 3) itajengwa kwa kiwango cha lami. Hata hivyo, barabara hiyo haina hata dalili ya kutengenezwa kwa kiwango cha lami. Naomba Serikali itekeleze ahadi hiyo ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, mwisho, nirudie kuwashukuru sana watendaji wote kwa kazi nzuri wanayoifanya.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe pongezi kwa Waziri na wasaidizi wote wa Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, vikwazo ambavyo vinazuia maeneo yote EPZ kutoanzisha viwanda hapa nchini vitatuliwe. Mfano, eneo la EPZ Morogoro hatua za haraka zichukuliwe kwa kushirikisha Wizara ya Ardhi na TAMISEMI na kutoa maamuzi kwa haraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda vidogovidogo, SIDO ipewe uwezo mkubwa zaidi kwa kutengewa fedha za mafunzo kwa vitendo na kuwakopesha vijana mitambo midogo na ya kati na kuanzisha viwanda vidogovidogo kwa vijana kwa wilaya zote hapa nchini. Hii itasaidia kupunguza tatizo la ajira kwa vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Dodoma uwekezwe kwa viwanda vingi vya mvinyo kutokana na zabibu ya Dodoma kukubalika katika soko la dunia.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa100%.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kulipongeza Jeshi letu kwa kazi nzuri wanayoifanya katika maeneo tofauti ndani na nje ya nchi. Katika nchi zilizoendelea duniani, nchi kama Marekani, bajeti ya ulinzi wa nchi hiyo ndiyo inayopewa kipaumbele cha kwanza katika bajeti ya nchi hiyo duniani. Kwa kuzingatia kuwa bila ulinzi na utulivu wa nchi maendeleo endelevu hayawezi kutokea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu ya Tano, malengo yake ya msingi ni kuifikisha Tanzania kwenye uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025 na ikizingatiwa kwa sasa kuna miradi mikubwa ya kimkakati ambayo itachochea uchumi wetu kwa haraka zaidi. Miradi hiyo ni kama ujenzi wa Bwawa la Kufua Umeme Rufiji, Mradi wa Reli wa SGR, ununuzi wa ndege mpya (ATC) na Mradi wa Bomba la Mafuta kutoka Uganda - Hoima - Tanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hizo na nyinginezo, naomba Serikali ingeangalia upya upangaji wa bajeti kwa kuzingatia uhalisia na bajeti hiyo iongezwe maradufu. Jinsi maendeleo yanavyoendelea ndivyo wahalifu na wapinga maendeleo waongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi linahitaji fedha zaidi ili kujumuisha kiteknolojia (kiulinzi), mafunzo mbalimbali, kununua vifaa vya kisasa, mitambo ya kung’amua uhalifu, mafunzo ya ndani na nje ya nchi, ujenzi wa nyumba za askari, kuazisha viwanda, maslahi ya wanajeshi na mambo mengine ya kijeshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, JKT iongezewe fedha ili iweze kuzalisha zaidi kwa kuanzisha viwanda vidogo vidogo katika makambi yake. Hii itasaidia kuwapatia ajira vijana wetu wanaohitimu mafunzo ya JKT.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi liendelee kuongeza ulinzi kwa maeneo nyeti ya Serikali na pia Jeshi liimarishe zaidi ulinzi kwa viongozi wetu wakuu wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nirudi kumpongeza sana Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wetu wa Tanzania, CDF, Makamanda wote na Wizara ya Ulinzi kwa kazi njema ya kulinda nchi yetu. Mungu libariki Jeshi la Wannachi wa Tanzania. Amina. Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja 100%.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuchangia katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya uhai ambayo amenijalia na kuniruhusu leo hii kusimama na kutoa mchango wangu kwa maslahi ya taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii pia kumpongeza Waziri, Mheshimiwa Ummy, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Watendaji wote wa Wizara na madaktari na wauguzi wote nchini kwa kazi nzuri na njema na takatifu wanayoifanya kuhakikisha afya za Watanzania zinaimarika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwenyezi Mungu aliumba mbingu na nchi, naomba ninukuu Biblia, Kitabu cha Mwanzo, kinasema: “Mungu akasema, iwe nuru; ikawa nuru. Mungu akaiona nuru, ya kuwa ni njema; Mungu akatenga nuru na giza”. Mwisho wa kunukuu. Maana yake ni nini? Mwenyezi Mungu alifanya tathmini ya uumbaji wake hatua kwa hatua. Hata alipomuumba mwanadamu, alimuumba mwanaume kisha akatathmini akamuumba mwanamke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Watanzania wenzangu tufanye tathmini ya kazi kubwa inayoifanywa Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Mheshimwa Dkt. John Pombe Magufuli akisaidiwa na Mawaziri, Makatibu Wakuu, watendaji na madaktari na wauguzi hapa nchini. Mabadiliko makubwa yamefanyika kusema ukweli, mnyonge mnyongeni haki yake mpeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini asilimia kubwa hata na ndugu zetu hapa wanaamini na wanatambua amefanya kazi kubwa lakini haya huwa wanafanya tathmini wakiwa wamejifungia kwenye vyumba vyao. Hapa ni kawaida kwa sababu hata kwa Mungu pia kuna viumbe ambao hawamuungi mkono Mwenyezi Mungu, ni kawaida hiyo.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. JANETH M. MASABURI: Hebu nyamazeni pale.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. JANETH M. MASABURI: Mmeipata hiyo, katika kipindi hiki cha uongozi Awamu ya Tano chini ya jemedari wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ameidhihirishia ulimwengu na hata mataifa yanapongeza juhudi na kazi kubwa anayofanya, ni lazima tuseme. (Makofi)

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, Taasisi ya Jakaya Kikwete imefanya kazi kubwa sana chini ya uongozi wa Dkt. Janab, Dkt. Kisenge na madaktari wengine ambapo kwa sasa kwa asilimia 85 huduma za moyo zinafanyika nchini. Mtakumbuka siku za nyuma Watanzania wengi walikuwa wanachangiwa kwenda kupata matibabu nchini India, sasa hivi hiyo ni historia ni lazima tupongeze Serikali hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali ya Muhimbili inaendelea kufanya kazi vizuri na wameboresha maeneo mengi hata kule ndani ukienda utatambua ni hospitali ya taifa. Taasisi ya Mifupa (MOI), inafanya vizuri. Taasisi ya Ocean Road inafanya vizuri. Hospitali ya Mlonganzila inafanya vizuri. Hospitali ya Benjamin Mkapa inafanya vizuri na hasa katika magonjwa ya figo. Hivi karibuni tumeambiwa kwamba hata viongozi na baadhi ya Mabalozi wamekuja kutibiwa katika hospitali zetu, haijapata kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nauliza ni lini tutawapa tuzo madaktari wetu, tuwatambue kwa kazi njema wanayofanya. Tusingoje mtu akifaa ndiyo tunaanza kusema maneno mengi. Tuwatambue kwa kazi njema wanazofanya za kuokoa uhai na hasa madaktari bingwa, tuna madaktari wengi sana wanaofanya vizuri. Nitatoa mfano, tuna Profesa Janab, Profesa Mseru na madaktari bingwa wengine, Dkt. Magandi, tuna wataalam wengi sana hapa tunaomba tuwatambue hata kwa kuwapa tuzo. Mheshimiwa Ummy nakuomba Wizara ifanye mchakato wa kuwatambua madaktari na wauguzi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuboresha hospitali za Wilaya. Hivi karibuni tumepata taarifa wamejenga vituo vya afya 352 katika kipindi kifupi sana, haijawahi kutokea na itaendelea kuwauma sana. Hospitali mpya za Wilaya 67 zimejengwa katika Mikoa ya Simiyu, Geita, kazi nzuri imefanyika katika sekta ya afya. Kwa sababu inauma na mnatambua kwamba kazi njema imefanyika na majibu tunayo, Chama cha Mapinduzi kimeendelea kuielekeza Serikali kutimiza haja ya Watanzania na hasa walio wanyonge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia kutambua kwamba kinga ni bora kuliko tiba. Taasisi ya Chakula na Lishe kama itawezekana iundiwe Wizara yake au itengewe fedha za kutosha ili kuweza kuhamasisha wananchi wajue jinsi ya kula chakula bora, kufanya mazoezi ili kuzuia magonjwa mengi ambayo siyo ya lazima. Magonjwa haya yanailazimu Serikali kutumia fedha nyingi sana. Kwa hiyo, kinga ni bora kuliko tiba, nakuomba Mheshimiwa Waziri hili ni jambo la muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati fulani nilibahatika kwenda China katika Mji wa Shanghai, nilikuta kuna wazee wanakaribia miaka 80 mpaka 90 lakini wako mtaani wanafanya kazi na wana nguvu. Hiyo yote inatokana na ulaji wenye kuzingatia ubora wa chakula na mazoezi. Hiyo inasaidia hata kupunguza gharama za matibabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwaambia Waheshimiwa Wabunge tufanye mazoezi na wenye Gym wengine hapa wanapiga debe. Pia tuzingatie kula kwa wakati chakula bora na kulala mapema, yote ni katika kuzuia maradhi mengine yasiyokuwa na lazima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia kuwapongeza madaktari wote nchini. Kusema ukweli wanafanya kazi njema na kazi ya Mungu, wanafanya kazi ya wito. Mimi nasema daktari hana tofauti na Mchungaji, Askofu au Shekhe, wanafanya kazi ya kumsaidia Mwenyezi Mungu. Kwa hiyo, naiomba Serikali iwaangalie, kuwaheshimu, kuwajali na kuwathamini madaktari wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nikupongeza Mheshimiwa Waziri na timu yako, Mwenyezi Mungu azidi kukulinda. Nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kukuteua mwanamke hodari na Naibu wako mmefanya kazi nzuri ya kutuongoza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Spika, pongezi kubwa kwa Serikali ya Awamu ya Tano. Niongelee utafiti. Bila utafiti wa magonjwa ya mazao, bila utafiti wa mbegu bora, bila utafiti wa masoko ya chakula na mazao ya biashara, bila utafiti wa wataalam wa kilimo ili kutambua ni wataalam wangapi waliopo na wako wapi na wanaleta tija gani katika maeno ya wakulima hapa nchini haya yote yasipozingatiwa na umakini mkubwa, na kikubwa bila kutenga bajeti ya kutosha katika maeneo yote hayo. Narudia tena kuiomba Serikali kutenga fedha za kutosha kwenye bajeti katika maeneo hayo na mengine ya kitaalam ambayo yanakuwa ni kikwazo na kurudisha nyuma sekta hii nyeti ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, maafisa ugani; maafisa ugani ni wachache na hata wale waliopo hawaonekani. Hii ni kutokana na ukosefu wa vitendeakazi kama magari, pikipiki, vifaa vya kunyunyizia dawa ya kuulia wadudu waharibifu wa mazao n.k kwenye maeneo ya kata mbali mbali hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, kilimo cha muhogo; kilimo cha zao la muhogo ni chepesi na ni rahisi zaidi na kinastahimili ukame, lakini pia kina tija kubwa kwa wakulima wengi, hasa wadogo wadogo na wa kati. Hata hivyo pia kuna wawekezaji wakubwa na wa kati wameanzisha viwanda vya kuchakata zao hili la muhogo kama kule Mkoa wa Lindi na Handeni (Tanga) ili viwanda hivi viweze kuzalisha kwa kiasi kikubwa zao hili la muhogo na ikizingatia kuwa wawekezaji hawa wametumia fedha nyingi kwa kuja hapa nchini kuwekeza kwenye ujenzi wa viwanda kama ilivyo malengo ya Serikali ya Awamu ya Tano (Serikali ya Viwanda). Wawekezaji hawa pia wangepewa maeneo makubwa ya kulima kilimo cha muhogo kama walivyopewa maeneo wawekezaji wa kilimo cha miwa ambao wanazalisha miwa na kisha kusindika (sukari), viwanda vya kuchakata mpunga na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, wawekezaji hawa wanalima mashamba yao na pia wananunua mazao mengine kwa wakulima wadogo wadogo (outgrowers).

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo naiomba Serikali iwapatie maeneo makubwa wawekezaji wenye viwanda vya kuchakata mazao ya kilimo kama muhogo na mazao mengine ambao wamewekeza kwa kujenga viwanda hapa nchini. Kwa mfano kiwanda cha kuchakata zao la muhogo mkoani Lindi wanahitaji eneo kubwa la kulima zao hili. Wamepewa kiasi kidogo ili kuwapa moyo na kuvutia wawekezaji wengi, ni vyema wakapatiwa eneo la ziada ili kukidhi haja na tija kwa kiwanda na wakulima wengi Tanzania kwa mkoa wa Lindi na mikoa mingine ambayo inalima mihogo. Kiwanda cha Lindi ni muhimu sana, kiongezewe eneo.

Mheshimiwa Spika, kilimo cha umwagiliaji. Kilimo cha umwagiliaji ndiyo suluhisho la kumkomboa mkulima wa Kitanzania na kupata ziada kuuza mazao nje ya nchi. Nchi ifanye jitihada kubwa kujenga miundombinu ya kukinga maji ya mvua ambayo yatasaidia kunywesha mifugo, kufuga samaki, kumwagilia mazao ya kilimo na matumizi ya nyumbani. Je, eneo hili la kukinga maji ya mvua kwa kutengeneza mabwawa makubwa ya kuhifadhi maji ya mvua na kuweka miundombinu ya kutiririsha maji hayo kwenye maeneo ya kilimo yanahitaji fedha za kigeni na wataalam kutoka nje ya nchi?

Mheshimiwa Spika, Ombi. Wizara ya Fedha itenge fedha za kutosha kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji. Wataalam wetu katika Wizara ya Kilimo watambue unyeti wa Wizara hii na kwa uchumi wa nchi yetu, na watekeleze kwa kuhakikisha wanashirikisha na Wizara nyingine kama Wizara ya Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya TAMISEMI, Wizara ya Viwanda na Biashara,Wizara Afya, Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano) n.k.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuwapongeza Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu watendaji wote na taasisi zilizoko kwenye Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja, vivutio vyote vya utalii hapa Tanzania viwekwe kwenye website kwa kila Ofisi za Balozi zetu zilizoko nje ya nchi. Pili, kivutio kikubwa katika nchi yetu ni amani kwa hiyo ni jambo jema kutangaza nchi yetu kuwa ni nchi ya amani na ni mahali patulivu kwa kupumzika na kufanya utalii kwa utulivu mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia utalii, Wizara hii ishirikiane na Wizara nyingine kama Wizara ya Madini, Wizara ya Kilimo, Wizara Viwanda na Biashara na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki kwa pamoja tuweze kutumia Balozi zetu kutangaza rasilimali zetu kama utalii, madini, mazao, Kiswahili, amani yetu na mengine ambayo yatainua uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lugha mbalimbali zitumike kutangaza utalii kupitia channel yetu ya utalii, lugha kama Kichina, Kiarabu, Kijerumani, Kifaransa, Kihindi, Kirusi na kadhalika ili dunia yote iweze kuona na kuifahamu Tanzania kuwa ina vivutio na ni eneo zuri duniani na ni ya pili duniani kwa vivutio vya asili.

Mheshimiwa Naibu Spika, makapuni ya utalii ya ndani na nje yashirikiane kuitangaza nchi yetu kiutalii. Tuna upungufu katika sekta nyingi hasa zinazohusika na kutoa huduma mbalimbali ikiwemo eneo la hoteli. Huduma kwa mteja (customer care) mafunzo zaidi yatolewe kwa wafanyakazi wetu ili tuendane na ushindani wa kibiashara kwa nchi zilizotuzunguka kama Kenya, Rwanda na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kampeni kwa utalii wa ndani. Timu maalum ya Wizara na taasisi zake zifanye ziara maalum nje ya nchi na hasa maeneo ya Ulaya, Asia na Amerika kutangaza na kujifunza mbinu nzuri za kuongeza watalii kuja kwa wingi hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Spika, naomba kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kupitia Wizara hii ikiongozwa na Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Wakuu wa Taasisi zote zilizo katika Wizara hii kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Spika, Juhudi ziendelee za kutafuta vyanzo vingine tofauti vya kuzalisha umeme ambavyo viko hapa nchini. Vyanzo hivyo ni kama vile jotoardhi, umeme wa upepo, jua, maporomoka ya maji (hydropower) yaliyopo maeneo mbalimbali, urania na vinginevyo. Vyanzo hivi vitasaidia nchi yetu kuwa na uhakika wa umeme na wa kutosha vikisaidiana na miradi mikubwa inayoendelea kujengwa.

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Umeme wa Rufiji ndio mkombozi na chachu ya maendeleo hapa nchini. Nichukue fursa hii kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa uamuzi wa busara na wa kimapinduzi ambao utakumbukwa na vizazi vijavyo. Mradi huu utapunguza gharama za uzalishaji viwandani pamoja na kupunguza bei ya umeme kwa wananchi wetu maskini.

Mheshimiwa Spika, nawapongeza watendaji wetu wa kizalendo kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya ya kuhakikisha nchi yetu inasonga mbele wakiitikia wito wa kazi wa Jemedari wetu Mkuu, Kamanda wa maendeleo Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Tanzania; Mwenyezi Mungu awabariki Watendaji wote wa Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, katika Jiji la Dodoma, kuna maeneo ya pembezoni hakuna umeme. Ninaiomba Serikali kupitia REA iwapatie umeme wananchi wa maeneo ya Kata ya Mbalawala, Kijiji cha Lugala, Kitongoji cha Matangizi na maeneo jirani ili wananchi wale wanufaike na umeme kwani wanapata taabu kwenda Nala kusaga nafaka zao na mahitaji mengine yanayotokana na huduma ya umeme. Hali hii ni shida kwao.

Mheshimiwa Spika, Mwisho, kazi yenu ni njema sana, chapeni kazi na TANESCO & REA iendelee vyema, kazi zake zinaonekana.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja asilimia mia moja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana Serikali kwa hatua kubwa ya mageuzi ya kiuchumi na kijamii ambayo yameushangaza ulimwengu kwa kipindi hiki cha miaka mitatu na nusu tu chini ya uongozi wa Awamu ya Tano. Pia, niwapongeze Waziri wa Fedha, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Manaibu Katibu Wakuu na Watendaji wote wa Wizara ya Fedha na taasisi zake zote kwa kazi nzuri walizofanya kwa kipindi chote. Mwenyezi Mungu azidi kuwaongoza vema katika utendaji wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Tanzania kwa uzalendo mkubwa, upendo wake kwa Watanzania na nchi yake, kwa kuchukua hatua mbalimbali ambazo zinasaidia nchi yetu kusonga mbele kimaendeleo.

Mheshimiwa Rais wetu amekuwa jasiri, hodari na mbunifu mkubwa hasa kwa mambo ambayo yalishindikana kwa awamu zote za utawala wa nchi yetu. Ni Rais ambaye atakumbukwa na vizazi vya sasa na vizazi vijavyo, Mwenyezi Mungu azidi kumlinda na amjalie afya njema na neema tele.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizo, nina maoni/ushauri kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo; Serikali ijenge maghala ya kisasa na vihenge vya kuhifadhia chakula ili kuzuia uharibifu wa mazao ya wakulima ambayo mengi yanaharibika kwa kukosa hifadhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, masoko; kuwe na kitengo maalum cha kutafuta masoko nje ya nchi ya mazao mbalimbali na kipewe bajeti ya kutosha. Ukizingatia kuwa biashara ya mazao yetu ni lazima tuitangaze huko duniani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutenga maeneo makubwa ya kilimo; Serikali ichukue hatua ya makusudi ya kutenga maeneo makubwa ya kilimo na kuyatangaza ndani na nje ya nchi ili wawekezaji ambao wako tayari au wana nia ya kuwekeza kwenye kilimo, wachukue fursa hii. Watanzania pia washirikiane na wageni katika kuwekeza kwenye kilimo cha kisasa cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, mazao ya viungo; mazao kama karafuu, hiliki, pilipili manga, mdalasini, vanilla, mchaichai na viungo vingine. Mazao haya hayana utaratibu mzuri wa masoko, wakulima wa mazao haya wanahitaji mafunzo maalum ya jinsi ya kuendeleza kilimo chao na fursa ya mikopo kabla na baada ya mavuno ya mazao yao. Kwa mfano bei ya hiliki, karafuu, pilipili manga ni kati ya Sh.20,000 mpaka Sh.40,000, lakini walanguzi huenda kununua mti mmoja wa pilipili manga kwa Sh.50,000 ambapo mti mmoja hutoa kilogram 50. Hali hiyo inawanyonya wakulima wa viungo hapa nchini, tatizo ni kukosa huduma ya fedha kwa mazao ya muda mrefu, mazao haya yana soko kubwa nje ya nchi. Maeneo ya Morogoro, Muheza, Mbeya, Kigoma na kadhalika ndiyo kunakolimwa mazao hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Naomba kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa kibali kusimama katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kupongeza Wizara, nimpongeze Waziri wa TAMISEMI, Naibu Mawaziri wake, Katibu Mkuu, Mtendaji wa TARURA na Viongozi ambao wako chini ya Wizara ya TAMISEMI. Wizara ya TAMISEMI ndiyo inayotafsiri maisha ya Watanzania ya kila siku. Wizara hii ni kubwa sana ina majukumu mengi na ndiyo maana iko chini ya Ofisi ya Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia fursa hii kumpongeza Rais wetu kipenzi, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya. Tumeona mambo mengi ameyafanya na aliahidi kuendeleza miradi. Miradi inatekelezwa na miradi mingine tunaiona ameanzisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, amekuwa ni mbunifu wa mambo mengine tofauti, tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutoa vipaji tofauti tofauti kwa watu wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina machache ambayo nitayaongelea, kwanza kuhusu Kanuni zinazotoa asilimia 10 ya mikopo katika Halmashauri zetu. Kanuni zinazotumika kwa sasa hazimnufaishi sana mwananchi kwa sababu zimejikita katika Halmashauri husika. Mtu anapoomba mkopo yeye anaruhusiwa kufanya biashara kwenye Halmashauri hiyo hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano Dar es Salaam, watu wa Dar es Salaam hatuna mashamba tunategemea biashara na biashara kwa asilimia kubwa pale ni watu wanaoshughulika na biashara ndogo ndogo. Karibu asilimia 80 ya wana Dar es Salaam wana shughulika na biashara ndogo ndogo, lakini wana nia ya kufanya biashara katika kilimo, wanapotaka kuomba fedha kwa ajili ya kwenda kulima hawapewi kwa sababu Kanuni zinakataa. Kwa sababu, yeye anakopa Manispaa labda mfano Ilala au Ubungo lakini shamba lake liko Bagamoyo Kanuni zinamkataa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashangaa Serikali ni hiyo moja, Wizara ni moja, Halmashauri ya Bagamoyo, Halmashauri ya Ilala iko chini ya TAMISEMI. Sasa Kanuni hizi ni kikwazo sana kwa watu wetu kuweza kunufaika na mikopo na ndiyo maana hii mikopo marejesho yanakuwa hafifu kwa sababu watu wamekariri kufanya biashara ambazo hazina tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utakuta achukue mtaji aende kununua samaki ferry, biashara ya kuuza soksi, biashara ya kuuza handkerchief haziwezi kumtoa mtu, haziwezi kusaidia. Tutawafukuza tutawanyang’anya ndizi kila siku tusipobadilika na tusipobadilisha kanuni zetu, katika kutoa mikopo tutakuwa tunaimba wimbo usiokuwa na mwisho. Ninaiomba Wizara izingatie haya ibadilishe hizi Kanuni zetu

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee upungufu wa watumishi katika Halmashauri zetu na nitaongelea watumishi wale wenye fani ambazo zinachochea kipato au fani ambazo zitasaidia Halmashauri kupata kipato zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kuna fani ya Wahandisi, Wasanifu Majenzi, Wakadiriaji Majenzi, Mabwana Afya, Mabibi Afya, Wachumi na Wakaguzi wa Fedha. Fani hizi zikitumika vizuri zitasaidia kuleta mapato katika Halmashauri zetu, lakini ni wachache, hawapo ni wachache sana. Halmashauri ni kubwa huduma ni nyingi shughuli ni nyingi miradi ni mingi lakini watenda kazi ni wachache. Utakuta ndiyo maana majengo yanaanguka watu wanajenga kwa kukosa vibali kwa sababu watumishi ni wachache, mapato yanakosekana kwa sababu watu wanajenga, hawana usimamizi na ubora wa majengo nao unakuwa hafifu. Naiomba Serikali izingatie hayo katika masuala ya ajira katika kada hizi ambazo nimezisema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru Serikali imesema kwamba inaongeza ajira kwa walimu, madaktari, wauguzi lakini fani hizi kwa kweli tunaomba vijana wetu wachukuliwe. Wengi wamemaliza Vyuo Vikuu wapo, Waziri mhusika tunaomba mzingatie haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kuhusu kuwapanga wamachinga, naipongeza Serikali na Mheshimiwa Waziri juzi umechukua hatua za haraka tunakupongeza sana. Wewe ni mnyenyekevu katika level yako, lakini watu wenu kule kwenye Halmashauri na wale Mgambo na wasimamizi hawana utu. Ni lazima tuseme tunapata lawama sana, simu ni nyingi sana, lakini wewe tunakutambua wewe ni mnyenyekevu ni msikivu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini watu wa chini yako sio wanyenyekevu kwa wananchi? Waende kusikiliza wananchi hawa ndiyo waliotuweka madarakani, ni lazima twende tukasikilize shida zao na tuzitatue kwa kutumia utu na kuwaheshimu. Ninaomba sana mzingatie hayo kwa sababu tunapata vikwazo sana na tunajua mengi. Wabunge wanajua mambo mengi sana. Kwa hiyo, wewe unatusikiliza, Wabunge wanasikiliza watu wao lakini watekelezaji wa kule chini baadhi yao wanatukwamisha. Kumsaidia Mheshimiwa Rais ni kuwa mnyenyekevu kwa wananchi kule chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza baadhi ya Mikoa wananyenyekea sana wananchi lakini wengine wanatukwamisha ni lazima tuseme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilishuhudia mwananchi anabomolewa kibanda mvua inanyesha, ana Watoto, Mgambo sijui wamelogwa na nani mgambo wa Jiji, hawatekelezi kwa utu wanatuangusha sana. Naomba Serikali izingatie hayo, iwahudumie wananchi kwa kuzingatia utu wa mwanadamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wetu ni wasikivu hawana taabu watatii, lakini pia biashara ndogondogo kama magenge kule waruhusiwe kufanya kazi kwa kuzingatia usafi, kwa kuzingatia kupangwa, kwa sababu mtu hawezi kutoka kitongojini akaenda Buguruni kununua nyanya ya Shilingi Mbili. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa ahsante sana.

MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru lakini tusiwasahau Madiwani wetu wanafanya kazi nzuri sana. Posho zao na maslahi yao yaboreshwe. Nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. Nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kunipa kibali kusimama hapa leo.

Mheshimiwa Spika, kwa haraka haraka naomba nianze kwanza kuipongeza Wizara ya Mambo ya Ndani kwa ujumla na Jeshi la Polisi na hasa IGP Sirro. Juzi tumemwona Mheshimiwa Waziri na Afande IGP wakitoa tamko na tamko lao limeanza kufanyiwa kazi na kazi tumeiona. Angalau kwenye Sikukuu hii kumekuwa na utulivu kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Jeshi la Polisi kupitia usalama barabarani kumekuwa na madereva ambao ni watukutu na hasa madereva ambao wanaendesha mabasi yaendayo Mikoani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukifika saa 12 pale katika Kituo cha Magufuli, Dar es Salaam, jinsi magari yanavyoongozana, yanakimbia utafikiri Nyumbu wanatoka Serengeti kwenda Masai Mara; ni mbio bila huruma. Hawajali abiria wala magari. Vile vile kuna madereva wa magari ya Serikali, wanaendesha magari kwa kasi sana. Wamehatarisha maisha ya viongozi, na maisha ya wataalam wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, roho za watu haziuzwi dukani. Tunaomba kila mtu afuate taratibu. Kwa sababu dereva wa Serikali anaweza kusababisha kukatisha maisha hata ya masikini ambaye anategemewa na watu huko nyumbani. Tunaomba Jeshi la Polisi lifanye kazi yake, litoe semina kwa hawa madereva ambao hawajafuata taratibu za usalama barabarani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongee kidogo kuhusu hili suala la panya road, wamekuwepo siku nyingi na viongozi wameshatoa matamko mengi. Hata hivyo, kumbukumbu yangu inanieleza kwamba wamekuwepo kipindi kirefu huko nyuma, wanakuja wanaondoka, wanakuja wanaondoka.

Mheshimiwa Spika, naomba Serikali tuweke mifumo ambayo itasaidia malezi kwa vijana wetu. Wanapomaliza darasa la saba wanakosa kazi, wanaenda kukaa kwenye magenge yale wanaita vijiwe. Kwenye vijiwe kule wanavuta bangi. Ukivuta bangi unaondoa uoga, unakuwa mkatili, wanakwenda kuwararua wazazi wao ambao hawana hatia.

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali itenge makambi ya kilimo kwa ajili ya vijana wa Mkoa wa Dar es Salaam, hawa nguvu zao wakazitumie kwenye kilimo. Serikali iandae masoko, iweze kuwasimamia hawa vijana waweze kupata fedha, tusiwaache bure. Ukiwaacha bure, watakuwa wanapata walimu wa kuwafundisha maovu. Naomba sana Serikali itusikilize katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongee kuhusu Jeshi la Zimamoto. Jeshi hili limekuwa halina wataalam wazamiaji. Mfano mmoja, juzi kulitokea maafa kule Bagamoyo, kuna kijana alizama kwenye dimbwi la maji pale Msata, wakaitwa Jeshi la Zimamoto, walikosa watu wa kwenda kuwaokoa. Wakaita watu wa private, wakawalipa shilingi milioni moja wakaenda kuokoa, wakakuta yule mtu ameshafariki. Naiomba Serikali itoe mafunzo kwa Askari wetu wa Zimamoto, itenge fedha za kutosha katika Jeshi hili ndani na nje, lakini pia iwape motisha ili wawe na mvuto katika kufanya kazi katika Jeshi hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaomba vitendea kazi. Hawana magari ya kutosha, vifaa hakuna vya kutosha, lakini maendeleo yanakuja kwa kasi, majengo makubwa yanakuja, kuna viwanda, kuna reli, kote kule kuna tahadhari zinatakiwa kwa ajili ya hili Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ili wapate vifaa waweze kusaidia hapo itakapotokea hayo majanga.

Mhshimiwa Spika, nije kwenye Jeshi la Magereza. Nalipongeza Jeshi la Magereza kwa sababu kwa sasa limejitegemea kwa asilimia 80 kwa chakula, kutoka zero mpaka asilimia 80 kwa chakula, nalipongeza sana. Naomba Serikali iwaongeze ili waweze kujitegemea kwa asilimia 100 ili kuipunguzia Serikali katika kupanga bajeti za kila mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee NIDA.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Spika, naomba niongelee NIDA, dakika moja tu. (Makofi)

SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kabla siajaanza kuchangia naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu, ambaye amenipa kibali cha kuweza kusimama hapa katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudie kumshukuru Mungu, kwa sababu kabla sijaanza kazi hii ya ubunge tulikula kiapo kwa kutumia Biblia na wenzangu Waislam, ndugu zangu walitumia Quran Tukufu. Kwa hiyo tunapokwenda kufanya kazi kwa kumtumia Mwenyezi Mungu, twende kufanya kazi kwa kumheshimu na kumwogopa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii pia kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoifanya yeye na wasaidizi wake Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Mawaziri wote, Watendaji wote wa Serikali pamoja na Wabunge, wamefanya kazi kubwa sana kwa kuhakikisha kazi na maendeleo yanaendelea katika nchi yetu. Mheshimiwa Rais, aliahidi kwamba atafanya kazi na slogan yake ni “Kazi Iendelee” baada ya kurithi kazi aliyoiacha marehemu Dkt. John Magufuli. Mheshimiwa Rais, aliahidi ukweli na amefanya kazi, amepambana sana, tumetembelea miradi mingi, tumeona mambo makubwa yanayofanyika, Mama amefanya kazi kubwa sana tena ya kijasiri. Waheshimiwa Wabunge na Waheshimiwa wananchi, tunaomba tumuunge mkono Mheshimiwa Rais, ana nia njema sana katika nchi hii. Tumpe nguvu, tumwombee kwa Mwenyezi Mungu, aweze kutimiza ahadi zake alizoahidi kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, amani na usalama katika ngazi ya familia. Suala la maadili na malezi ya watoto wetu yanashabihiana na amani na usalama katika ngazi ya familia. Sisi wazazi na walezi tulitetereka katika kulea watoto, tumeachia wadada wa kazi kulea watoto, tumeachia watoto majirani kutunza watoto sisi tunahangaika na kutafuta pesa. Matokeo yake watoto wamejilea wenyewe, watoto wetu wamebakwa, watoto wamelatiwa, watoto wamejifunza tabia tofauti kinyume na maadili, sasa tunalia, tufanye nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile mfumo wa elimu yetu hauko sawa katika kulea watoto au kufundisha watoto kuanzia ngazi ya shule za awali. Serikali iwekeze kwenye shule za awali kwa kuweka walezi wazuri ambao watamtengeneza mtoto, huyu mtoto ambaye anakuja kuwa kiongozi katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tukumbuke kisa cha Sodoma na Gomora. Naomba kunukuu hii Sodoma na Gomora kitabu cha Biblia utasoma mwanzo 19, mstari wa 23
– 26 inasema, nanukuu: “Jua lilipokuwa limechomoza juu ya nchi ya Lutu alipoingia Sowayi ndipo bwana akanyesha juu ya Sodoma na juu ya Gomora kiberiti na moto toka mbinguni kwa bwana, akaangusha miji hiyo ya bonde lote na wote waliokaa katika miji hiyo na yote yaliyomea katika nchi ile lakini mkewe Lutu akatazama nyuma yake akawa nguzo ya chumvi.” mwisho wa kunukuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna wake wengi wa Lutu katika nchi hii ambao wanataka tugeuke nguzo ya chumvi ambao wanatetea suala la ushoga, lakini tunasema alipo shoga kuna basha, lakini wanaoonekana wengi hapa ni mashoga, mabasha wako wapi? Basha huwezi kumtambua kirahisi na mabasha ndiyo wenye pesa. Namuunga mkono dada yangu Dkt. Thea anasema waasiwe, tunasema kabla hajaasiwa na kukuhumiwa kwanza wachapwe viboko hadharani, kama nilivyoona kule Wahindi na kama nilivyo waona Waganda na wale Wamasai walivyo mchapa yule mtu aliyewasaliti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo nawakumbusha tena kuna habari za gharika kuu, uwasi wa mwanadamu kwa Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu alinyesha mvua siku 40 usiku na mchana akaifuta ile nchi yote chini ya uongozi wa Nabii wake Nuhu. Hiki kitu kinachoongelewa siyo mzaha, tumeongelea miradi mingi inafanyika katika nchi hii, matrilioni ya fedha yanatumika katika nchi hii, tuna madini, tuna maziwa, tuna bahari, tuna rasilimali nyingi katika nchi hii. Nchi hii ilipendelewa na Mwenyezi Mungu, lakini tuwekeze kwa watoto waadilifu. Haya tunayosema kuna majizi, wala rushwa, yote inatokana na ukosefu wa malezi tangu mtoto mdogo. Mtoto mdogo kuanzia kuzaliwa mpaka miaka sita anaiga kila kitu. Ukimtengeneza ataiga kitu kizuri, usipomtengeneza ataiga kitu kibaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, twende Serikali tukawekeze kwenye malezi ya watoto. China wamewekeza kwenye malezi ya watoto wao, Singapore wamewekeza kwenye malezi, kuna nchi zimejifungia kutengeneza kizazi kitakachoweza kushika nchi. Tunaweza kukataa ndoa za jinsia moja maana yake unakataa uumbaji wa Mwenyezi Mungu, zaeni mkaongezeke, watu wanazuia watu wasizaliane, wingi wa watu ni tishio, China wako wengi wanatisha dunia, India inatisha dunia kwa sababu ya wingi wa watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuja kudanganywa na uzazi wa mpango. Ule ni uongo wa kutuzuia tusizae ili tuendelee kuwa dhaifu. Ahadi ya Mwenyezi Mungu, ni kuzaa, utazaaje unatengeneza wanaume kuwa wanawake? Sisi wanawake ambao tunashika mimba miezi tisa unaambiwa umezaa mtoto gani? Wa kiume, zamani ulikuwa unaulizwa umezaa mtoto gani? Mwanajeshi, leo unaenda kutoa litoto linakuwa nyoronyoro, litoto langu kama lile mimi naweza kulipoteza tu, siwezi kuona vitu vya namna hiyo, haiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siwezi kuwa na mtoto msenge halafu bado namchekeachekea, nitahama hata kama mji, kama nipo Dar es Salaam nitahama, siwezi kukaa na mtoto msenge. Tunaongea kwa lugha laini laini inakera sana, inanikera, inaniudhi na nawapongeza Viongozi wa Dini wameongelea kwa nguvu sana. Nampongeza Waziri Nape nimemwona juzi ameongea, lakini kila Mbunge sauti yako ni sauti ya Mungu, usiposema utahukumiwa na Mwenyezi Mungu, utakuwa umemsaliti Mwenyezi Mungu, kuungana na wale watu wa Sodoma na Gomora. Hatuwezi kufanya kazi kubwa katika kuendeleza nchi hii tukaanza kufumbia macho masuala haya. (Makofi)

MHE. ISSA J. MTEMVU: Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Issa J. Mtemvu, taarifa.

TAARIFA

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mzungumzaji anaendelea kuzungumza vizuri. Kwenye eneo la maadili hilo nilitaka nimkumbushe tu, si tu wazazi kule nyumbani, si tu Serikali kutengeneza mifumo ambayo itatuwezesha kujifungia ndani na kutengeneza msingi mzuri wa malezi kwa Watoto, lakini inasemekana hata ndani ya Bunge kuna hao unaowazungumza, hata ndani ya Bunge inasemekana, kwa hiyo Mheshimiwa Mwenyekiti, sina uhakika yanasemwa tu kwa hiyo ndiyo maana tunapata ugumu wa kulea.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Issa unachangia hiyo taarifa na kuzungumza. Mheshimiwa Janeth Masaburi, taarifa unaipokea?

MHE. JANETH M. MASABURI: Hii taarifa naipokea. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa sababu nitakuwa mwongo mbele za Mwenyezi Mungu. Wenye tabia hiyo waache, tunawajua, wengine viongozi, hatutaki kusema sana, tunamwogopa Mungu si mwanadamu, haya ya dunia ni ya kupita tu. Leo niko hapa kwenye hiki kiti kesho sipo na kesho nipo labda nimekufa, lakini Mungu apewe sifa yake, Mungu ahidimiwe Mungu ndiye mwenye kutukuzwa na Mungu ndiye mwenye kuogopwa. Sisi wanadamu siyo kitu, tuko duniani kesho tunapita lakini kizazi lazima tukiendeleze kwa sababu ni ahadi ya Mwenyezi Mungu. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutasifia ndiyo lakini kwa nini watu wanafanya hivyo na hizo NGO kubwa naona zina…

MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante sana, muda wako umekwisha, tunakushukuru sana. (Makofi)

MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa ruhusa ya kusimama leo, kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa kibali na pumzi yake ya bure na kuweza kuchangia katika masuala ya ulinzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Samia Suluhu Hassan na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, amefanya kazi kubwa tumetembelea vikosi tumekuta amefanya kazi kama alivyoahidi kwamba kazi inaendelea, lakini sisi tulikuja tuliona kazi zinaendelea maana ni nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Waziri, Katibu Mkuu wa Wizara hii ya Ulinzi kwa kazi kubwa pia wanayoifanya. Lakini kipekee nimpongeze Mkuu wa Majeshi Jenerali Mabeho, Mnadhimu Mkuu, Makamanda wote kwa kazi nzuri na njema wanayoifanya katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona mara nyingi panapotokea maafa wanajeshi wamekuwa mstari wa mbele katika kwenda kusaidia wananchi. Lakini pia tulipata simanzi mwaka jana kwa kuondokewa na Rais wetu mpendwa wa Awamu ya Tano Dkt. John Magufuli, lakini Jeshi la Wananchi lilisimama imara likahakikisha nchi imetulia na mpaka sasa wananchi wana amani katika nchi yao, hongereni sana majeshi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nalipongeza tena Jeshi tumetembelea Makao Makuu ya Ulinzi pale Kikombo tumekuta vitu vya ajabu, hatukutegemea kuona kama kuna wakandarasi wa kiwango cha juu cha aina ile. Ukipata nafasi nenda katembelee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi tulikuwa tunauliza hili jengo limejengwa na Mchina, Mjapani kama tulivyozoea, lakini jengo lile limejengwa na wataalam wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania. Lakini limetumia fedha kidogo lakini kwa ubora na hadhi ya hali ya juu, limeokoa shilingi bilioni 69; nani kama Jeshi la Wananchi wa Tanzania? (Makofi)

WABUNGE FULANI: Hamna.

MHE. JANETH M. MASABURI: Hongereni sana makamanda. Hawa ni wazalendo, ni waadilifu iwapo Serikali itawajengea uwezo wataweza kufanya vitu vikubwa sana katika nchi hii. Kuna mambo mengine ambayo tunaweza kuyasema kuna mengine hayasemeki, wanahitaji fedha. Kuna mazao ya kila aina ambayo wakipata kiwango kikubwa cha fedha, tutaweza kuuza katika nchi za jirani, tutaweza kuwaongezea uwezo Jeshi letu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee kuhusu suala la…

SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. JANETH M. MASABURI: Mama yangu weee. (Kicheko)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Spika, leo hunipi kidogo dakika moja basi niongee kimoja tu. Leo nihurumie, najua umenikubalia.

Mheshimiwa Spika, ninaomba barabara zilizopo pembezoni za Mkoa wa Ruvuma kwa ajili ya doria ya ulinzi ziwekewe lami zitengenezwe, kwa sababu nchi jirani wana barabara lakini huku wanajeshi wetu wanapata ugumu sana kwa sababu hatuna barabara ambazo zitasaidia doria katika mambo ya ulinzi. (Makofi)

Mwisho naomba bajeti iongezwe, bajeti ya ulinzi ni ndogo bajeti ya vyombo vya ulinzi vyote ziongezwe. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana. (Makofi)