Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Condester Michael Sichalwe (31 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kukushukuru sana wewe kwa kunipa nafasi hii. Pia nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye amenijalia kibali kusimama mahali hapa. Vilevile nakishukuru Chama changu cha Mapinduzi kwa heshima na imani ambayo walinipa. Pia nawashukuru sana wapiga kura wangu wa Momba kwa kuniamini na kunituma mahali hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia niendelee kuwashukuru sana wazazi wangu kwa kunilea na ushirikiano mkubwa ambao walinipa kipindi cha uchaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Rais kwa asilimia 101. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Rais huyu na kusema kwamba ni miongoni mwa viumbe ambao wamemkopesha Mungu kwa kiasi kikubwa sana. Maandiko matakatifu yanasema kwamba anayemsaidia mnyonge na maskini anakuwa amemkopesha Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli katika kipindi chake cha miaka mitano amefanya mambo mengi ambayo amewagusa wanyonge na maskini wengi sana na watu ambao walikuwa hawana watu wa kuwasemea, yeye amekuwa ni msemaji wao. Kwa hiyo, ninaamini hata katika vipindi vyake vigumu ambavyo atapitia, Mungu atazikumbuka na kuzitakabali hizo sadaka zake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, ni kwa sababu ya muda, nilitamani kuchangia kwa kirefu kuhusiana na eneo la biashara. Kwenye eneo la biashara nitaenda kuongelea zaidi kwenye masuala ya mipaka. Sehemu nyingi ambazo ni za border kumeonekana kuwa na mwamko mzuri sana wa biashara. Nikitolea mfano kwa border ya Namanga na Tunduma, ni sehemu ambazo zina wafanyakazi ambao wamesoma na kuajiriwa wachache sana kuliko wafanyabiashara wanaokuwepo pale. Hivyo, inapelekea kuwepo kwa maendeleo mbalimbali ya kijamii, pia hata vijana na watu mbalimbali kuendelea kupata riziki na watu wengi kupata ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye ukurasa wa 26 nataka ku- quote kipengele kidogo tu kwa sehemu, Mheshimiwa Rais anasema hivi; “…na kwa bahati nzuri tangu mwaka jana tumeanza kutekeleza mpango wetu wa kuboresha mazingira ya biashara nchini, yaani blueprint for regulatory reforms to improve the business environment in Tanzania.”

Mheshimiwa Spika, nataka kusema hivi, nitolee mfano wa mpaka wa Zambia na Tanzania ambapo kidogo angalau nimekuwepo kwa hizi nchi za Kusini mwa Afrika na Afrika ya Kati. Naomba kuishauri Serikali na kuiomba, kama mawazo haya yanaweza yakawa chanya na yakasikilizwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Serikali iweze ku-expand mipaka yake. Pamoja na kuipongeza kwamba imepiga hatua sana katika kujenga hizi One Stop Border, mfano border ya Namanga na Tunduma, zimejengwa katika kipindi cha miaka mitano, lakini ipo hasara kubwa sana ambayo Serikali inapata kwenye hii mipaka. Bado biashara nyingi ambazo ni haramu, biashara za magendo, kutoroshwa kwa mazao vinaendelea kufanyika kwenye hii mipaka kiasi kwamba kama Serikali ingeamua ku-expand ile mipaka tungeweza kuzuia biashara haramu nyingi na biashara nyingi za magendo ambazo zinafanyika kwenye hii mipaka, ikasababisha Taifa likaendelea kukusanya fedha ya kutosha ambayo itaendelea kutusaidia.

Mheshimiwa Spika, nikitolea mfano mpaka wa Zambia na Tanzania, ndiyo mpaka ambao unabeba karibu nchi zote ambazo ziko Kusini mwa Afrika. Mfano, tunapoongelea mji mmoja wa Livingstone pale Zambia, ndiyo mji ambao unapokea mpaka wa Botswana, Namibia na Zimbabwe. Kwa hiyo, nitolee mfano labda bidhaa za magendo zinapotaka kupitia lile jengo la SADC zinapitaje?

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano wa kwenye Jimbo langu na hapa ninaiomba Serikali ikiwapendeza tupewe geti. Kwenye mfano huu naeleza, unapotoka pale Livingstone, kwenye zile nchi tatu, tuchukulie amekuja na biashara za magendo, anataka kukwepa kodi ya Serikali… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi ya kuchangia. Kwanza kabisa, niendelee kukupongeza wewe kwamba katika kipindi chote ambacho mimi nimekuwa nikikufuatilia kuanzia ukiwa Naibu Spika na mpaka sasa hivi umekuwa Spika, kiukweli nafurahishwa na namna ambavyo unaendesha Bunge hili. Mimi niseme kwamba ni miongoni mwa Maspika bora kabisa Afrika ambao wanapaswa kuigwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niendelee kumpongeza Mheshimiwa Rais na niendelee kusema kwamba hata yeye amekuwa ni record breaker. Ni miongoni mwa Marais ambao wameingia kwenye historia, hakuna Taifa lolote kwa sasa ambalo unapotaja jina la Dkt. John Pombe Magufuli hawamjui. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kuchangia Mpango wa Miaka Mitano na Mpango wa Mwaka Mmoja kwenye eneo la biashara na niendelee kuongelea kwenye eneo la mipaka. Mimi natamani kuishauri Serikali, kama ambavyo ulisema hapo kwamba sisi Wabunge wawakilishi wa wananchi ndiyo watu wa kwanza kabisa na sahihi wa kuishauri Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali bado haijautendea haki mpaka wa lango la SADC. Napoiongelea nchi ya Kenya ina mipaka zaidi ya minne, kuna mpaka wa Sirari, Namanga, Holili, Tarakea na ule ambapo ukipita Tanga unaenda Mombasa, bado yote ile ni Kenya. Nchi moja tu ina mipaka karibu mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuishauri Serikali kwa kusema kwamba, there is no way Zambia itakuja kupata bahari. Dunia imeumbwa na itaondoka Tanzania ndiyo yenye bahari. Kwa vyovyote vile nchi zote ambazo ziko Kusini mwa Afrika zinategemea bandari ya Tanzania kutoa vitu vyao kutoka kwenye nchi za Ulaya na bado wanatarajia kupita Zambia kwa ajili ya kupeleka kwenye nchi nyingine. Kwa hiyo, naweza nikasema kwenye lile geti moja tu la pale Tunduma ni mpaka ndani ya mpaka. Unaonekana tunapakana na Zambia, lakini nyuma tumebeba nchi nyingi. Je, Serikali haioni sababu ya kupanua mpaka ule ili tuendelee kunufaika nao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi natokea sehemu zile za Tunduma. Kumekuwa na wimbi kubwa sana la ndugu zetu kutoka vijijini, hata kwenye Kijiji changu ambacho mimi natoka, wapo wafanyabisahara pale wanasukuma baiskeli tu kwa ajili ya kupokea mizigo, lakini unapokuwa Tunduma hakuna biashara yoyote kubwa ya nyumba za kupanga kwa sababu hata Mtanzania wa kawaida ambaye hajui kusoma na kuandika kwa biashara ndogo ambayo anaifanya pale kwenye mpaka ana uwezo wa kujenga na kuishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wanaendelea kulalamika kwamba hakuna ajira. Je, hatuoni sababu ya kuboresha mipaka na sehemu nyingine hata wale wa darasa la saba mipaka itakapotanuliwa watakuja kupokea mizigo ya wageni, watajipatia riziki kwa sababu Mungu hakutuumba watu wote tukafanana ndiyo maana kuna Rais, Waziri, mwalimu wa shule ya msingi na kuna msukuma mkokoteni. Kwa hiyo, tutumie fursa tulizonazo kwa ajili ya kutatua matatizo. Bora kidogo cha halali kuliko kikubwa cha haramu, hata Maandiko Matakatifu yanasema, aliyenacho huongezewa asiyekuwanacho hunyang’anywa hata kile alichokuwanacho, lakini sisi tunavyo hatuvitumii sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitolee mfano ule ambao nilitaka kutoa nilipoishia, ni kwa namna gani biashara za magendo zinavyotoka zile nchi za Kusini mwa Afrika na hata nchi za Afrika ya Kati mfano Kongo. Kwa mfano, nikiongelea vipodozi, vipodozi vya kutoka Kongo vimekatazwa kuingia hapa nchini Tanzania inachukuliwa ni magendo, lakini ukipita huko Dar-Es-Salaam na sehemu nyingine, bado unakuta carolite zinauzwa, zinapitaje kama pale patrol inafanyika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi natoka Jimbo la Momba. Unapokuwa pale Livingstone, Zambia, mtu anapotoka na bidhaa Namibia, Zimbabwe au Botswana, anapoingia Lusaka unafika mji mmoja unaitwa Mpika, pale kuna njia mbili njiapanda. Whether uamue kwenda Ndola ambapo uende border ya Kasumbalesa kule mtu achukue vile vipodozi. Anapokuwa pale Mpika ana uwezo wa kuamua kupita barabara ya Tunduma atokee pale lilipo lango la SADC au aamue kupita mahali kunaitwa Kasama kutokea Mbara Road anaingia upande wa Jimbo la Momba ambapo kutokea inapoanzia Tanzania kuingia tarmac ya Zambia ni kilometa moja tu na nusu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niliyesimama hapa ni living testimony, natoka kwenye kata ya mpakani, kipindi chote nikiwa nasoma Mbeya Day, inapofika kuanzia mwezi wa kumi na mbili, wa kwanza, barabara hazipitiki tunapaswa kwenda kupita Zambia ili tuweze kufika Tunduma, mazao na mifugo mingi inatoroshwa kwa kutumia njia hiyo kwa sababu iko wazi, hakuna utaratibu wowote pale. Serikali kama mnasikiliza ushauri tunaona ipo sababu, iko nia na manufaa ambayo tutayapata pale ambapo tutaongeza geti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuendelea kuongezea, kuna soko kubwa la kimataifa ambalo limejengwa ndani ya Jimbo la Momba kwenye Kata moja inaitwa Ndalambo, Kakozi. Ni soko la kimataifa zaidi ya shilingi bilioni 8 Serikali imeweka pale. Kwanza, Serikali yenyewe iliona kwamba ni soko la kimataifa la mazao na mifugo lijengwe kwenye mpaka. Sasa kama limejengwa kwenye mpaka soko hili litachochewa na nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutataka tena kutoa mazao ambayo yanatoka Rukwa, Jimbo la Momba yaende yakapite Tunduma? Hizi halmashauri nyingine zinakuwaje? Zinawezaje kujitegemea kama haziwezi kusimama, mazao yote yanatoka yanaenda Tunduma na hili soko? Pia lilipo soko ndipo ilipo barabara ambayo inapita kwenda kwa baba yangu Mheshimiwa Kandege kwenda kwenye bandari ya Kalemii. Kwa nini kusiwe kuna sababu ya kupata geti? Tunaiomba na kuishauri Serikali tupate geti mahali hapo ili tuweze kuzuia biashara zote haramu na za magendo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuongezea, kumetokea migogoro mingi sana ya ardhi, kutokana na kwamba tuko mpakani Congolese na Zambians wengi wanawatumia Watanzania hawa kwa ajili ya kuja kumiliki ardhi kwa sababu ni kwenye mpaka. Tunaiomba sana Wizara yenye dhamana husika jambo hili muliangalie kwa karibu sana. Tunaomba Wizara ya Ardhi ifuatilie hati zote ambapo watu wanaonekana wanapata hati ndani ya Halmashauri ya Momba na muda mwingine ni wafanyabiashara hawa wanavaa uhusika wa Tanzania lakini wanawalinda hawa watu ni wahamiaji. Sheria ya Ardhi ya Tanzania inamkataza mtu yeyote asiyekuwa Mtanzania kumiliki ardhi. Kama anataka kumiliki kama mwekezaji ziko sheria ambazo zina mwongozo mtu huyo ni kwa namna gani anaweza kumiliki ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuongezea hapohapo kwenye suala la ardhi. Sisi watu wa Halmashauri ya Momba na halmashauri nyingine ambao wanapitia changamoto kama hii, hatutamani kuona tunafika kwenye matatizo ambayo ndugu zetu wa Kiteto na Morogoro wanayo. Limetokea wimbi kubwa la wawekezaji ndani ya Jimbo la Momba kutokana na ule mwamko wa lile soko kuwepo na ule mpaka, kuja kumiliki ardhi kinyume na taratibu. Kaka yangu Mheshimiwa Kunambi alisema pale, tunaomba ardhi ambayo inaonekana iko sehemu ambayo ni muhimu, kwa mfano sehemu kama hizi za mipaka, kwa kuwa wananchi wa maeneo haya wengi wao wanakuwa ni watu wa kipato kidogo, Serikali iingilie kati iyapime yale maeneo. Itusaidie kuyapima siku zijazo yatatusaidia kwa sababu tunajua tu lazima mpaka utafunguka, biashara nyingi zitafanyika na ardhi itapanda thamani mahali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wawekezaji hawa cha kwanza wanamiliki ardhi kinyume na taratibu. Mtu anamiliki ardhi eka 800, lakini amepata hati ambayo amepewa na Kijiji au mtu anamiliki ardhi zaidi ya eka 100, kutoka eka 50 mpaka eka 100 alipaswa angalau apewe na halmashauri, lakini anasema ana hati ya Kijiji. Wanamiliki ardhi kinyume na taratibu lakini hawaziendelezi ardhi hizi pia hawalipi kodi ya ardhi. Wao ndiyo watu wa kwanza kuchukua sheria mkononi na kuanza kuwaweka watu ndani. Wao wameshavunja sheria tatu, lakini wanawaweka watu ndani.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: AHsante sana Mheshimiwa Condester Michael Sichalwe.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Hoja Kuhusu Bei ya Kuuza na Kununulia Mahindi
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, kulingana na hoja ambayo mtoa hoja aliitoa jana ni kwamba Serikali haijatoa katazo lakini imetoa maelekezo ambayo yanawafanya wakulima au wafanyabiashara wapate changamoto ya kutoa mazao nje ya nchi. Changamoto hiyo ikasababisha bei za mahindi kushuka. Ukatuagiza kwamba twende kwenye vituo vyetu tukaulize kama NFRA wameshaanza kununua mahindi.

Mheshimiwa Spika, hali iliyopo sasa hivi ni kwamba NFRA mpaka sasa hivi bado hawajaanza kununua mahindi kwenye vituo. Hoja yetu iko hapa; wazo la Serikali ni jema lakini masharti waliyoyaweka yanafanya wafanyabiashara wasiweze ku-export mazao hayo kwa wakati, hata NFRA kwenye hivyo vituo vilivyopo si rafiki kumfanya mkulima aweze kuuza mazao. Hivyo basi mazingira yanakuwa magumu kwa wakulima wetu, kwa hiyo sisi tulikuwa tunaomba tutoe hoja ili Wabunge tunaotoka kwenye maeneo hayo tujadili ili tuweze kuishauri Serikali.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

SPIKA: Ngoja kwanza. Mheshimiwa Condester Sichalwe, hoja ya kutolewa mahindi nje ya nchi ama kuuza nje ya nchi imekuja kama sehemu ya kupungua kwa bei ya mahindi, maana yake kama yananunuliwa humu ndani kwa bei inayofaa hiyo hoja haipo.

Waheshimiwa Wabunge, kwa maelezo ya jana, na ndiyo maana nasema mwenye hoja; wewe kwa maelezo uliyotoa sasa hivi hapa nataka niulize jambo moja halafu ndio nijue cha kufanya. Kama mahindi yatanunuliwa kwa bei iliyopo na NFRA ile bei si ni sawa? Maana ndiyo majibu yalikyokuwepo hapa jana. Hoja ilikuwa ni kwamba NFRA ilikuwa haijaanza kununua mahindi kwa bei hiyo kwa sababu bei aliyotoa mtoa hoja ilikuwa shilingi mia nane sijui mia ngapi ndiyo ikaonekana bei inakuwa chini kuliko ile aliyotaja Waziri?

MHE.CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, naomba kukujibu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama bei hiyo ambayo Serikali wametoa bado mahindi yataendelea kushuka kwa sababu mbili zifuatazo: -

i. NFRA ukipeleka mahindi, wanavyo vigezo vyao vingi unaweza kupeleka tani mia tano wakachukua tani kumi. Hivyo kufanya wakulima hawa wasipate mahali pa kuuza mahindi lakini wachuuzi wa kawaida wenyewe wanachukua mahindi maadam ni mahindi na wananchi wanapata nafasi ya kununua.

SPIKA: Haya, nani anataka kutoa taarifa? Mheshimiwa Yahaya ngoja. Mheshimiwa Condester Sichalwe toa hoja.

MHE.CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nomba kutoa hoja Wabunge wote waunge mkono. (Makofi)

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Seriakli za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi. Kwanza nianze kabisa kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa nchi hii kwa namna ambavyo anafanya kazi vizuri na kwa namna ambavyo anaendelea kupambana kuhakikisha hata sisi ambao tunatoka Majimbo ya Vijijini tunapata pesa. Tunapata pesa kwenye miradi ya maendeleo, tunapata pesa ambazo zinaendelea kuwasaidia wananchi kwenye shughuli mbalimbali, hata wananchi wa Momba nitumie fursa hii kusema tulivyokuwa jana si ndivyo tulivyo leo.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya PAC ambayo kwenye kitabu hiki kimesheheni mambo mengi sana. Katika kipindi ambapo nilipata nafasi ya kusikiliza uwasilishaji wa CAG katika Taasisi mbalimbali ambazo zilikuja kututembelea kuna baadhi ya mambo nikajifunza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimegundua kwamba Mheshimiwa Rais anafanya kazi kubwa sana kwa kujitoa kwa huruma, kwa weledi na kutamani kuisaidia jamii yake na kama Mama amedhamiria kuona ule uchungu wa Mama kwa ajili ya kuwasidia Watanzania, lakini kuna baadhi ya mambo nikaona kwamba mimi ni Mbunge natokana na Chama cha Mapinduzi, Serikali ya Chama cha Mapinduzi haina wapinzani, wapinzani ni baadhi ya watendaji wa Serikali ambao siyo waaminifu kwa dhamana ambayo wamepewa ndani ya Serikali, wao ndiyo wanawaumiza Watanzania wenzao kwa nafasi ambazo wamepewa lakini wao ndiyo wanamfanya Mheshimiwa Rais apate do ana Watanzania wakati mwingine wamlaumu ilihali walipaswa kulaumiwa wao.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kuchangia ripoti ya Kamati yangu ya PAC nikaangalia kwenye ripoti ya Kamati ya watu wa LAAC, asilimia 10 ya Halmashauri, Serikali ilidhamiria kuwasaidia wananchi wa kawaida vijana ambao hawawezi wakakopesheka, wakina mama na maskini watu wenye ulemavu ili waweze kusaidika, lakini angalia shilingi bilioni 5.6 hazikuweza kupelekwa kwenye huo Mfuko, shilingi bilioni 1.7 hazikuweza kupelekwa kwenye huo Mfuko kwenye baadhi ya Halmashauri. Jambo la kusikitisha shilingi bilioni 88.42 hazikuweza kurejeshwa kwenye huo Mfuko! Bilioni 88 hivi kwanini hizi pesa hata zisingepelekwa hata kwenye zahanati? Watanzania wanakufa huko vijijini, kuna vijiji havina zahanati, hakuna vituo vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumemsikia jana Waziri wa Afya akiwa anaongelea vyanzo vya kupata pesa kwa ajili ya kuwezesha Mfuko wa Bima kwa Wote, hizo pesa si zingeweza kuwasaidia Watanzania. Kwa hiyo, nikagundua Serikali ya Chama cha Mapinduzi haina mpinzani wapinzani ni baadhi ya watu waliopo ndani ya Serikali wameshindwa kutumia nafasi zao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wakati anapokea hotuba ya CAG kama ambavyo ameongea Mjumbe mwenzangu wa Kamati, aliongea kwa uchungu sana. Nae kama Kiongozi wa State na yeye kama Mheshimiwa Rais wetu yeye mwenyewe alionyesha kuchukizwa na baadhi ya mikataba ambayo inafanywa na watu wasiokuwa waaminifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye shirika moja hapa la TRC kwenye SGR, naomba nisome kidogo tu. Kwenye SGR kwenye kipengele kidogo ambacho kinasema dosari mbalimbali zilizobainishwa katika ununuzi wa vichwa na mabehewa ya treni. TRC ilikataa zabuni mara mbili kwa ajili ya manunuzi ya vichwa vya treni ya umeme na mabehewa ya abiria ambapo mzabuni aliye na bei ya dola za Kimarekani 263,460,514 alikataliwa kufanya manunuzi yasiyo na ushindani kwa dola za kimarekani ikapelekea kufika dola za Kimarekani 478,507,468 iliyosababisha ongezeko la gharama dola za Kimarekani 215,046 ambapo ni sawa na pesa za Kitanzania bilioni 550.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa na-convert hapa kwenye vituo vya afya ni vituo vya afya 1,100 maana yake Jimbo langu lote la Momba lingekuwa limeshapata vituo vyote vya afya, Mkoa mzima wa Songwe na Mikoa mingine yote ambayo ipo hapa Tanzania ingekuwa imepata kwa sababu tu kuna mtu hakufuata utaratibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa najiuliza swali huu utaratibu je, ni Mheshimiwa Rais ndiyo anawatuma wafanye hivi? hawa ni watu wasio waaminifu ambao wamepewa dhamana, wameaminiwa na wanajificha kwenye kichaka cha dhamana ambazo wamepewa wanasahau kwamba wanaumiza Watanzania wenzao. Kwa nini wasifuate utaratibu, Kanuni na Miongozo kama ambavyo CAG mwenyewe anasema kwamba yapo baadhi ya mambo ambayo tunayapata ni watu kwa kutokufuata utaratibu, Kanuni na maagizo ndiyo yanatupelekea hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea hapo hapo kwa SGR, katika mkataba wa manunuzi wa locomotive na mabehewa ya abiria yaliyotumika, TRC ilitelekeza mkataba wa bila dhamana ya tendaji kazi hali iliyosababisha hasara ya Euro 5,520,400 ambayo ni sawa sawa na bilioni 13.7 za Kitanzania, nikaweka kwenye vituo vya afya ni vituo vya afya 28.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ilitokana na Mkandarasi kushindwa kutekeleza mkataba na TRC kushindwa kutoza gharama zilizotokana na uvunjifu wa masharti ya mkataba. Anaendelea anasema Mkandarasi alidai sababu hizo zilikiuka kanuni hivyo vitu kama hivyo. Mheshimiwa Rais siku anapokea hotuba yake ya CAG aliongelea mambo kama haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea tena…

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. CONDESTER MICHAEL SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Reli TRC, Mheshimiwa Waziri utapewa nafasi ya kujibu, shirika la Reli la Tanzania …..

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Condester naomba usubiri kuna taarifa usuburi, Mheshimiwa Naibu Waziri.

TAARIFA

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka tu kumkumbusha msemaji Dada yangu ambae anaongea vizuri sana, kwanza kwa hoja ya kwanza aliyoizungumza na cancellation kwamba unapobadilisha Mkandarasi wa kwanza na wa pili na bei ikitofautiana kuna factor nyingi. Moja kuna teknolojia, mbili kuna wakati ulipofikia awamu ya kwanza na awamu ya pili. Pia kwenye hoja yake hii ya pili anayoizungumza sasa hivi ambayo kimsingi alikuwa ameshaanza kuizungumza vizuri, tunazungumza hapa tulikuwa tumeshazunzumza haikufanyika ni kwa sababu hakukuwa na performance iliyo-guarantee ndiyo maana hakupewa, kwa hiyo hakukuwa na hasara iliyotokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri Taifa likafahamu kwa sababu isije ikajengeka hoja kwamba ilifanyika manunuzi tukapata hasara bilioni 13, haikufanyika na sababu mojawapo kwa nini haikufanyika na haikufika mwishoni ni kwa sababu hapakuwa na hiyo performance guarantee, kwa hiyo nilitaka kuiweka vizuri hiyo statement. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Condester unaipokea hiyo taarifa?

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei. Mimi ni Mjumbe wa Kamati na Management ya TRC ilikuja ikahojiwa nilikuwepo kwenye Kamati na Hansard zipo, kwa hiyo najua ninachokifanya na hiki ninachokisoma mimi ni taarifa ya CAG siyo mimi, siyo taarifa yangu kutoka Momba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea. Shirika la Reli Tanzania - TRC lilimwomba Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Nchini Uturuki kufanya uchunguzi wa kina due diligence kuhusiana na kampuni ya Eurowagon juu ya ununuzi wa vichwa viwili na mabehewa 30 ya abiria ili waendelee kufanya hii shughuli. Jambo la kusikitisha ni TRC waliendelea na shughuli hii pamoja na Mheshimiwa Balozi kuwafanyia due diligence kuwaambia kwamba kampuni hii haifai lakini wakaendelea kufanya. Sasa swali tunajiuliza Mheshimiwa Balozi yupo nchini kule, anatumia pesa zetu za kodi na yupo kwa ajili ya hiyo kazi, anataka kulisadia Taifa lakini bado waliokuwa wamemwomba wakakataa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imagine tunaenda wapi, imagine yaani mtu kateuliwa na Mheshimiwa Rais, halafu hawataki, hawa ndiyo wapinzani wa Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Ninaendelea anasema kampuni hao Eurowagon haikuwasilisha dhamana ya utendaji kazi (performance security) licha ya kukumbushwa mara kadhaa na Shirika la Reli Tanzania (TRC), Shirika la Reli Tanzania liliendelea kutekeleza mkataba huo pasipokuwa na dhamana ya utendaji imagine na hivyo kupelekea hasara, anasema Shirika la Reli Tanzania TRC haikutoza Euro 2,260,000 hivyo kupelekea hasara ya Euro 5,520,400 hapa nime-convert ni bilioni 14 za kitanzania sawa na vituo 24 ya afya Watanzania wangekuwa wamevipata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema nini, wapo viongozi wa juu ambao nia yao ni njema wanataka kulisaidia Taifa, mpango wao ni mzuri ndiyo huo ambao Mheshimiwa Rais alionao mzuri. Lakini wapo wachache ambao wameaminiwa ni wataalam Mheshimiwa Rais amewaamini, ni wabobezi wa kufanya hayo mambo, badala watumie utaalam wao kulisaidia Taifa, kutusaidia Watanzania ambao labda sisi hatujui, wanatumia dhamana yao na utaalam wao vibaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana hawa watu pia wamesomeshwa kwa mkopo wa Serikali, hawa nikuambie ni wahujumu uchumi kama wahujumu wengine tu ambapo zipo sheria ambazo watu wakikosa makosa kidogo tu wanachukuliwa hatua, kwanini hawa hawachukuliwi hatua, kwa nini? CAG kwa nini kaandika hiki? Kwa nini alileta kwenye Kamati jambo kama hili? Walikuja kwenye Kamati kwanza taarifa yao yenyewe ambayo ilikuwa imeletwa na CAG walikuwa wanaikataa, na GAG mwenyewe alikuwa anawashangaa, as if hawakuwa na exit meeting walipokutana na CAG! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hilo inatosha kwamba watu wasiendelee kumwangusha Mheshimiwa Rais anapowaamini kwenye mikataba na wasifikirie Watanzania ni wajinga sana, wasiendelee kutuhujumu sana maana wanalitesa sana Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo kwamba Taifa hili halina fedha, hicho kidogo tunachopata tungeweza kuki-utilize vizuri, tukakifanyia kazi vizuri, tungefika mbali, lakini watu wachache wasiokuwa na nia njema na mapenzi ya Taifa hili wanaendelea kulihujumu Taifa hili, kujinufaisha peke yao, kwa manufaa yao peke yao na kuendelea kututesa jambo ambalo siyo sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais ana nia njema ya kutumikia Taifa hili. Yule mama ni mtu mzima, anapambana na hata unaiona sura yake ya kusaidia watu. Hata siku moja mwanamke hajawahi kuwa tapeli, mwanamke hajawahi kuacha kuwasaidia watu kwenye nyumba yake, lakini hawa aliowaamini ndio wanaomfanya Mheshimiwa Rais apate doa na Mheshimiwa Rais ana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Condester, ahsante sana, kengele ya pili imelia.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wangu umeisha?

MWENYEKITI: Ndiyo, ni kengele ya pili.

MHE.CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia tu hoja moja, kuhusiana na suala la BoT, kama ambavyo wameongea wenzangu; aliongea Mjumbe mwenzangu wa Kamati. BoT ni taasisi kubwa, sisi wote ni Watanzania, na kila mtoto wa kawaida wa Tanzania anatamani afanye kazi kwenye sehemu nzuri. BoT wanapaswa kurejea ile procedure yote ambayo walipatikana wale watu, kwa sababu kila mtoto aliyepo Tanzania ana haki ya kupata kazi kwenye taasisi kubwa kama zile. BoT wamevunja sheria, wao kwa ajili ya kujinufaisha wenyewe, baadhi ya watu wameona watoto wao ndio wanaofaa sana kwenye hii nchi na ndiyo maana wakavunja utaratibu na wakaenda ndivyo sivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba Watanzania watendewe haki sawa na Watanzania wote. Sisi fahari yetu ni Utanzania wetu. Babu zetu waliokufa kwenye ardhi hii, sisi wote lazima tunufaike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuweza kuchangia. Kwanza kabisa nianze kwa kuishukuru na kuipongeza Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi kwa mambo ambayo waliweza kutufanyia katika Jimbo la Momba katika Awamu ya Tano, na mambo ambayo wanaendelea kutufanyia katika Awamu hii ya Sita; tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kumpongeza dada yangu, Mheshimiwa Ummy Mwalimu, kwamba tuna imani sana na wewe kwenye Wizara husika ambayo umepewa kuisimamia, lakini pia kuendelea kuwapongeza kaka zangu, Manaibu hodari sana ambao wanamsaidia dada yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mbele ya Bunge lako Tukufu, naomba niwasilishe baadhi ya changamoto za wananchi wa Jimbo la Momba kama ifuatavyo. Nitaongelea kwenye miundombinu ya barabara pamoja na madaraja; miundombinu ya elimu; miundombinu ya vituo vya afya pamoja na zahanati na muda ukiwa Rafiki nitamalizia na namna gani kuendelea kuwawezesha akinamama wa vijijini katika ubunifu wao mbalimbali walionao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Momba ndilo jimbo ambalo tuseme kwa Mkoa wetu wa Songwe linaongoza kwa kiasi kikubwa sana kulima mpunga, maharage pamoja na mahindi. Na tunaweza kusema ndilo jimbo ambalo linalisha Mkoa mzima wa Songwe kwa mbegu, au tuseme kwa zao la mchele. Lakini pamoja na nchi ambazo ni Jirani kama Kongo na Zambia, wanategemea sana mchele pamoja na maharage kutoka kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa basi, kutokana na mambo ambayo Waheshimiwa wenzangu ambao wametangulia kueleza hapa. Ufinyu mkubwa uliopo kwenye bajeti ya TARURA ni wazi kwamba hata nitakapoeleza changamoto nyingi ambazo zinalipata Jimbo la Momba sitaweza kumaliza. Kiukweli Jimbo la Momba ni miongoni mwa majimbo ambayo yana changamoto kubwa sana ya miundombinu ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata sasa ambavyo ninaongea hapa ni kweli ziko kata ambazo ziko pia visiwani, zimebaki kwasababu hakuna madaraja, barabara siyo rafiki, hawawezi wakatoka kwenda kijiji kingine, hawaweze wakatoka kwenda kata nyingine, wanaendelea kusubiri mpaka mvua zitakapokauka ndipo waendelee kupitia kutoka sehemu moja kwenda nyingine. Hali hiyo imeendelea kusababisha kudorora sana kwa mapato ya halmashauri yetu, pamoja na kwamba jimbo linaendelea kuhudumia na nchi nyingine ambazo zipo mpakani.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu kwa Serikali; kwa kuwa network ya barabara ambazo ziko ndani ya Jimbo la Momba ni barabara 57 zenye urefu wa kilometa 647.21, ninajua kwa ufinyu wa TARURA barabara hizi haziwezi kutekelezeka. Niende kwenye uhalisia; tunaomba tuombe barabara chache za kimkakati ambazo kuwepo kwa barabara hizi Serikali itakapotuwezesha, kunaweza kukachangia kwamba halmashauri ikaongeza mapato yake, lakini pia ikavutia maana zitakuwa ni barabara za kimkakati. Lakini pia inaweza ikafanya hata wafanyakazi ambao wanafanya kazi katika maeneo hayo, yakawavutia kuendelea kubaki hapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya kwanza ambayo nianze kuiombea ni barabara ya Makamba – Ikana. Na barabara hii sababu ya kuiombea barabara hii ni kwamba ndiyo barabara ambayo inaunganisha Jimbo la Momba kwa ukanda wa juu na wa chini na soko la kimataifa la mifugo na mazao limejengwa katika Tarafa ya Ndalambo ambalo tunalitegemea sana katika kupandisha mapato ya halmashauri na kuliongezea Taifa mapato yake kwa kuwa tutaendelea kusambaza kwa wingi na kwa ubora kwenye nchi zetu ambazo ziko Jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii tutakapokuwa tumeipata barabara hii, itakuwa imerahisisha Tarafa za Msangana na Kamsamba ambazo zina jumla ya kata nane, kwa hiyo watapandisha mazao yao kwa urahisi kwa ajili ya kwenda kufika kwenye soko la mifugo na mazao ambalo lipo Kakozi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara nyingine ninayoiomba ni barabara ya Chindi – Msangano ambapo kuwepo hapo kuna daraja kubwa ambalo limetenganisha Halmashauri ya Wilaya ya Momba pamoja na Halmashauri ya Mji wa Tunduma. Kwa hiyo kama barabara hii itafunguka, na tutakapopata daraja katika eneo hilo, itatusaidia sana wananchi kuendelea kuwa na options mbalimbali kwa ajili ya kupeleka mazao mengine au na shughuli nyingine za kiuchumi kwenye Mji wa Tunduma ambao tunautegemea kama mji ambao uko mjini kwa ajili ya kuendelea kupata mahitaji mbalimbali, ikiwa na hospitali ya wilaya iko kwenye Mji wa Tunduma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara nyingine ninayoiombea ni barabara ya Ivuna – Chole. Barabara hii inaunganisha Halmashauri ya Wilaya ya Momba pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Songwe. Na wananchi ambao wapo katika Kata ya Mkomba wanatenganishwa na daraja kubwa. Mwenyewe kipindi cha mvua nikienda kufanya ziara ni lazima nibebwe mgongoni kwasababu baiskeli haiwezi kupita, pikipiki haiwezi kupita, gari haliwezi kupita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini barabara nyingine ambayo naomba ushughulikiwe ni barabara ya Kakozi – Ilonga. Barabara hii ndiyo ambayo inaunganisha Mkoa wa Songwe pamoja na Mkoa wa Rukwa. Barabara hii pia Mheshimiwa baba yangu Mheshimiwa Kandege naye ninajua itamsaidia sana kuja kutumia lile soko la mifugo na mazao kwa sababu ataleta mazao yake pale. Vilevile barabara hiyo ndiyo ambayo inapita mpaka kufika kwenye Bandari ya Kalemii.

Kwa hiyo, itasaidia wananchi wa Jimbo la Momba na Majimbo mengine ambayo yapo kwenye Mkoa wa Songwe na kwenye Halmashauri zingine wanaweza wakaitumia kwa ajili ya kufikisha mazao yao au vitu vyovyote kwenye bandari hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe ushauri kidogo kwa Serikali namna gani inaweza ikatusaidia kuongeza pato kidogo kwa TARURA. Nitolee mfano wa wananchi wangu wa Jimbo la Momba. Wananchi wa Jimbo la Momba kwa asilimia ni wachache sana ambao wana simu za smartphone, kwa hiyo, mtu anaponunua kifurushi anapewa dakika za maongezi, SMS za ku-chat pamoja na MB lakini kwa sababu ni watu wa kupiga tu hata ku-chat kwa SMS za kawaida hawa-chat, inapofikia kile kifurushi kina-expire anakuwa ametumia dakika lakini MB pamoja na SMS zinakuwa zimebaki lakini mtu yule anakuwa ameshalipia na kodi ya Serikali amekatwa kwenye ule muda wa maongezi. Mnaonaje kama TAMISEMI wataamua kwamba kile ambacho kinakuwa kimebaki kwa sababu ni cha mwananchi na alikilipia kwa pesa yake halali akatolea na kodi kwa nini isirudi ili ije kwa ajili ya kusaidia vitu kama hivi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata kwa Waheshimiwa Wabunge tuna experience kitu hiki, umenunua dakika, SMS na MB unatumia kidogo vinabaki vinaenda wapi? Kwa hiyo, tunayafaidisha makampuni ya simu ambayo yameshatuchaji na tunawaachia bure, hivi viki-expire tuwekeane mwongozo vinarudi kwa Serikali kwa sababu itakuwa ni changizo halali la mwananchi huyu. Kwa hiyo, mimi naona inaweza kutusaidia kukusanya na kuboresha barabara na katika hilo dada yangu Mheshimiwa Ummy mtukumbuke huko Momba, ahsante sana. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kwenye miundombinu ya elimu, kutokana na Jimbo la Momba kuwa na changamoto nyingi za barabara imepelekea mazingira ya walimu wengi ambao wanafanya kazi ndani ya Jimbo la Momba yanakuwa si Rafiki. Walimu hawa kuna wakati wanakuwa wananung’unika, hawana motisha ya kufanya kazi vizuri. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa fursa. Kwanza kabisa nianze kwa kusema kwa kuwa muda ni mfupi namwomba baba yangu Mheshimiwa Waziri Simbachawene pamoja na Naibu Waziri, wapate nafasi ya kutembelea Jimbo la Momba ili kwa haya ambayo nitayaainisha kutokana na muda mfupi, sitaweza kupata nafasi ya kuelezea kwa kina, watakuja kujionea kwa uhalisia wenyewe nitakachokiongea hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto ya kwanza ambayo nataka kueleza hapa ambayo inawapata Jeshi la Polisi na wanashindwa kutekeleza majukumu yao vizuri kwa wananchi wa Jimbo la Momba, jambo la kwanza ni usafiri. Jimbo la Momba ni Jimbo ambalo ni pana sana, lina square meter za mraba 5,856; vijiji 72 na vitongoji 302. Unaweza kuona ni kwa kiasi gani Askari hawa wanawezaje kufanya kazi; kutoka kijiji kimoja kwenda kingine wakati mwingine ni zaidi ya kilomita 100. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, uhalifu unapotokea mfano labda Kijiji cha Itumba, Kata ya Nzoka mpaka Askari huyu afike eneo la tukio kwenda kuwasaidia wananchi hawa, nasi tuko kwenye Jimbo la mpakani, unakuta wahalifu hawa wameshakimbia, wameondoka, wametokomea Zambia. Kwa hiyo, tunaomba sana Serikali na Wizara hii itutazame, tupatiwe gari ili Askari hawa waweze kufanya kazi yao vizuri. Wakati mwingine hata lambalamba tu wanatusumbua sana. Hatuwezi hata ku-deal na lambalamba.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Taarifa Mheshimiwa.

SPIKA: Endelea wa taarifa. Mheshimiwa Condester, kuna taarifa unapewa. Upande gani?

T A A R I F A

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, nataka nimpe taarifa mzungumzaji kwamba hali iliyoko kule Momba ni sawa sawa na Nyang’hwale, tuna magari mawili Landcruiser lakini hayana matairi. (Kicheko)

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa hiyo, lakini sisi hatuna kabisa hiyo gari.

SPIKA: Pokea taarifa hiyo Mheshimiwa.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, hatuna kabisa hilo gari, hata pikipiki hakuna; hata baiskeli hakuna.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, Jimbo la Momba, yaani Halmashauri ya Wilaya ya Momba ndiyo Jimbo ambalo linabeba Makao Makuu ya Wilaya ya Momba, Majimbo mawili ya uchaguzi…

SPIKA: Kwa hiyo, Mheshimiwa Amar Hussein afadhali wewe una magari hayana matairi, mwenzako hata baiskeli hana. Sijui yupi zaidi sasa hapo. Endelea Mheshimiwa. (Kicheko)

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, jambo la pili, ni kuhusiana na kwamba Jimbo la Momba yaani Halmashauri ya Momba ndio jimbo ambalo Makao yake Makuu inabeba Wilaya ya Momba, lakini hatuna kituo cha polisi ambacho kinafanana na hadhi ya wilaya. Tuna outpost mbili tu ambayo ni kituo kidogo cha Kamsamba ambacho kina askari nane, kituo kidogo ambacho kipo Chitete ambako ndio makao makuu, kina askari wanne, yaani hata ukipata ya Uchaguzi jamani askari huyu hana baiskeli, hana pikipiki anakwenda kumkamata nani.

Mimi kuna wakati nimefanya kampeni na lambalamba, maana yake nimekuta lambalamba anafanya mkutano wake na hawezi kuja kunisikiliza, wananchi wanafanya pale, kwa hiyo ikabidi tuwaombe kwa sababu hatuwezi kuwapigia Jeshi la Polisi watakuja na nini, watembee kilomita 50.

SPIKA: Mheshimiwa Condester, lambalamba ndio nini?

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, lambalamba ni mkusanyiko. Ulinde dakika zangu Mheshimiwa Spika tafadhali, nitakapotoa ufafanuzi wa lambalamba.

Mheshimiwa Spika, lambalamba ni hawa wanajiita, sijui tusemeje! Sijui waganga wa kienyeji, kwa hiyo wakifika kwenye Kijiji wanahamasisha kwamba tumtafute mchawi na kitu kama hicho. Sasa vile vinaleta mgongano kwenye jamii, kwa hiyo utakuta wakati mwingine wananchi wanataka hata wakaague shule. Nimefika mahali nimewaambia Serikali haitambui uchawi, wananchi wanasema hapana si tunataka Mbunge ambaye anayetutetea, tunaumwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunaomba sana, naamini kungekuwa na gari na kungekuwa na Kituo cha Polisi kizuri, kina Afisa mwenye nyota tatu, akapewa askari wa kutosha wangeweza kufanya patrol na kuzunguka, wananchi katika hali ya kawaida tunaogopa sana askari. Kwa hiyo kuona askari wanapitapita, wanalinda wanaona kwamba kuna usalama wa kutosha.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine hatuna askari wa kike, nafikiri kwa sababu hatuna kituo ambacho kina hadhi ya wilaya ili Afisa mwenye nyota tatu akikaa pale kuna mwongozo wa Jeshi la Polisi ambao wanabidi awe na askari wa idadi fulani. Sasa tunajiuliuza sisi wananchi wa Jimbo la Momba sisi wote ni wanaume? Hapana, sasa tunakaguliwa na nani kama askari wote hawa ni wanaume? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, hakuna nyumba za maaskari na wakati mwingine hata Kituo cha Polisi chenyewe huwezi ku-identify kama ni Kituo cha Polisi. Askari hawa wanalala wapi, wanajichanganya huko, wanapanga huko mitaani. Sasa kama ilivyo kuna imani za kishirikina, wakati mwingine wanaweza kuamini hata askari mwenyewe ni mchawi. Kwa hiyo akachomewa nyumba, kwa sababu kule watu wanakatana mapanga kwa hizi imani za kishirikina.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo namwomba baba yangu Mheshimiwa Simbachawene afike kule tu, kwa sababu muda hautoshi nisije nikasitishwa hapa, ili akajionee, tukatembee nimfikishe kule Katumba, nimpeleke kule Chole, Siliwiti na kule Kichangani Kamsamba. Akishaenda kuona tu, baada ya mwezi mmoja ataniletea askari hata 40 na atanipa gari.

Mheshimiwa Spika, ahsante san ana naunga mkono hoja. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kutoa mchango wangu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ni mwingi wa rehema na huruma zake kuendelea kunipa kibali na nafasi kusimama tena kwenye Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nami niwasilishe maombi yangu kwa Serikali ikiwa ni pamoja na kuishauri Serikali. Kupitia Jimbo langu natoa mchango huu kwa kuwa najua utakuwa unabeba taswira na azma nzima ya Taifa, natokea kwenye eneo la mpakani, tumekulia eneo hilo na kuona kwamba zipo fursa nyingi za ajira, biashara, maendeleo na vitu mbalimbali kutokana na watu ambao wanatoka mpakani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni nini naomba kuishauri Serikali kupitia Wizara hii ambapo wao ndiyo wanatoa fedha na kusimamia rasilimali nyingi za Watanzania. Kuna haja kubwa ya kutazama na kurudia kupitia tena kuona vile ambavyo tunaweza tukaendelea kuimarisha na kuwekeza kwa kiwango kikubwa mpakani.

Mheshimiwa Spika, nataka kutolea mfano wa baadhi ya maeneo ambapo kuna border post (mipaka) za Holili, Namanga na Tunduma yenyewe nitolee mfano, wakazi ambao wanatoka Tunduma hawalimi, hawavui, hawafugi, hawafanyi chochote, kikubwa ambacho wanakifanya pale ni biashara. Sababu ambayo imechochea kuwepo na msukumo mzuri wa biashara Tunduma ni uwepo wa lile gate ambapo kuna mpaka kati ya nchi ya Zambia na Tanzania ambayo nyuma yake inazibeba nchi zote za SADC. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo ipo kwa bandari ya Dar es Salaam kuna ma-gate zaidi ya moja, Serikali inaonaje kuongeza ma-gate kwenye sehemu nyingi za mpakani ambazo zinapelekea kuwepo na mrundikano wa watu, lakini wakati mwingine huduma hizi za forodha kushindwa kutolewa kama inavyostahiki na wakati mwingine Serikali kupoteza mapato? Kama ilivyo Tunduma na sehemu zingine kama Namanga kumetokea uwepo wa wimbi kubwa la watu, watu wengi kupata ajira bila kujali elimu, umri au itikadi ya kitu chochote, imeonekana watu wengi wanapata sana ajira.

Mheshimiwa Spika, mfano watu ambao wanatoka Tuduma ajira zipo kwa wingi kwa watu ambao hawajasoma, kwa watu ambao wamesoma, wafanyabiashara kutoka kila pembe ya nchi hii wameenda kujikita pale wanafanya biashara. Waliofungua hoteli, vituo vya mafuta na huduma za kubadilisha fedha za kigeni, wote hawa wanajipatia riziki.

Je, Serikali haioni kwamba ni wakati muafaka kwenda kutuwekea gate kwenye Jimbo la Momba ambalo pia litaenda kusabababisha Watanzania wengine na watu wengine ambao watataka kuwekeza ndani ya nchi yetu kuendelea kupata huduma kama ambazo wanapata katika sehemu zingine za mipaka? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini naomba kuwepo na gate kwenye Jimbo la Momba. Naishukuru sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi imetujengea Soko la Kimataifa la Mifugo na Mazao mahali pale. Eneo ambalo limejengwa soko kutoka linapoanzia Jimbo la Tunduma mpaka unapolimaliza Jimbo la Momba ni zaidi ya kilometa 80 lote ni eneo la mpaka. Ina maana kwamba cha kwanza hata ardhi ambayo inayopatikana maeneo yale itakapopimwa itaonekana ni ardhi ambayo ina fursa kwa kuwekeza kwa sababu kila Mtanzania na watu mbalimbali watatamani kwenda kuwekeza pale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwenye eneo lile kuna njia za kutumia gari zaidi ya kumi ambazo zinatoka kutoka nchi ya Tanzaia kuingia nchi Zambia. Je, Serikali haioni watakapoweka gate pale itasababisha Wizara ya Ulinzi kuongeza usalama wa eneo lile? Pale Tunduma au sehemu zingine zinapotoa bidhaa kutoka Bandari ya Dar es Salaam wakati mwingine wanapitisha kinyume na taratibu kwa sababu njia zile zipo nyingi. Je, Serikali haioni kwamba tutakapopata gate itatuongezea fursa nyingi, watu watapata ajira lakini pia wawekezaji ambao watataka kufungua hoteli na vituo vya mafuta, shughuli za kibenki zitaongezeka mahali pale na mimi naamini hata ajira ambazo tunaendela kuzi-promote na kuzisema kwa Watanzania hawa zitapatikana. Kwa sababu mama lishe watatokea pale, kwa sababu pale kuna mnada wa mifugo watu mbalimbali wataendelea kujipatia riziki mahali pale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ninaendelea kuona kwamba ipo namna, tuma watu wa SADC na COMESA waende kuutembelea mpaka ule, wakague na wajiridhishe uwezekano wa kuongeza geti pale. Kama ambavyo tunaendelea ku-promote kuongeza bandari nyingine hata kule Bagamoyo ili kuendelea kutoa huduma nzuri kwa ajili ya bandari yetu ya Dar es Salaam ipo haja pia kwenye mpaka kati ya nchi yetu na Zambia kuongeza geti kwa sababu lipo moja tu pale Tunduma. Wakati mwingine wafanyabiashara wanakaa muda mrefu pale zaidi ya wiki mbili kwa sababu kumeonekana kuwa na mrundikano na huduma hazifiki inavyotakikana hivyo inapelekea hata kupoteza mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kuiomba hata Wizara ya Mama yangu Mheshimiwa Jenista kwamba…

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa Mheshimiwa Condester.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nataka kumpa taarifa Mbunge wa Jimbo mdogo kuliko wote humu ndani kwa akina mama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, anachokizungumza Mbunge hapa ni jambo kubwa na la maana. Kwa mfano, sisi kule Mara yaani mtu atoke Serengeti mpakani wa Masai arudi apite Kirumi aende Tarime border ndiyo aende kutoa mzigo wake. Hivi nani anaweza kusafiri umbali mrefu hivi ili kupeleka hela Serikalini? Kwa nini Serikali sasa isifanye kama anavyozungumza ikague mipaka ya nchi yetu nchi yote ione wapi pa kwenda kuweka wafanyakazi ili watu tuendelee kupata fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, juzi amezungumza hapa Mheshimiwa Tarimba kwamba kwa mwezi mmoja wenye siku 30 na siku nne, yaani siku 34 wafanyakazi wa Wizara ya Fedha wametumia shilingi bilioni 39. Sasa kwa nini wasidhibiti mipaka hiyo wakaweza kutafuta fedha nyingi ili waweze kupata mapato ya kutumia? (Makofi)

SPIKA: Taarifa inatosha.

Waheshimiwa Wabunge, kabla sijampa nafasi Mheshimiwa Condester, kuhusu hili suala la Wizara ya Fedha na matumizi yaliyofanyika kama Mheshimiwa Waziri Mkuu alivyowatembelea naomba kwa sasa tusiwahukumu kwa sababu bado ni jambo linalofanyiwa kazi halafu taarifa itapelekwa kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu labda baadaye tutakuja kupata taarifa halisi. Sasa kwa kuwa linafanyiwa kazi tukipitisha hukumu kabisa nadhani tutakuwa a little bit unfair. Kwa hiyo, naomba hilo tuliache kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Condester, unapokea taarifa?

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa ya Mheshimiwa Mbunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kuiomba Serikali kwamba kama vile Serikali ambavyo inatupia jicho la umakini pale Tunduma kwa sababu inajua inavyonufaika na zile nchi ambazo zipo SADC sasa watashindwaje kulichukua ombi hili na kulitekeleza? Kama mpaka wa Zambia na Tanzania nyuma umebeba mipaka mingine kwa nini tuwe na gate moja? Kwa nini tusingekuwa hata na mageti matatu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu tumeshapewa hela nyingi pale lilipo Soko la Mazao la Kimataifa basi kuna haja kubwa Serikali kutuwekea gate pale. Naamini Watanzania kutoka sehemu mbalimbali watanufaika, vijana wetu wa Kitanzania watapata ajira, mama zetu ambao wanatafuta riziki ndogo ndogo watajipatia pale kama ambavyo ipo Tunduma kwamba hata watu ambao siyo wasomi lakini ni matajiri wa kutosha kuliko hata wasomi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo mahali ambapo naendelea kuliombea liwepo gate ndiyo sehemu ambapo kuna barabara ambayo inaenda mpaka kwenye ile Bandari ya Karemii. Nchi ya Tanzania ilikuwa inapata changamoto kubwa sana…

T A A R I F A

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri wa Fedha, nimekuona.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwa ridhaa yako, naomba nimpe taarifa mchangiaji, Mbunge anayeongea ujengaji wa hoja wa kwake ni wa viwango vya Wabunge wazoefu sana. Kwa kweli ndiyo maana Jimbo la Momba walimpitisha kwa kishindo na waendelee kumchagua. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, kwa jinsi alivyojenga hoja, naomba nitoe taarifa kwamba Wizara pamoja na Mamlaka ya Mapato tutatembelea lile gate analolisema na tupate mfano ule aliousema ili tuweze kuzungukia na mageti mengine ili tuweze kutengeneza utaratibu wa kukusanya fedha na kuwawezesha wananachi wetu waweze kufanya shughuli zao kwa uangalifu. (Makofi/Vigelegele)

SPIKA: Mheshimiwa Condester ziara hiyo itafanyika, lakini kwa ruhusa ya Spika. Endelea Mheshimiwa. (Kicheko)

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nashindwa hata cha kusema, natamani hata kutoendelea kuchangia kwa sababu pale tukapojengewa gate ndani ya Jimbo la Momba hata siku nikifa nitahisi kwamba Mwenyezi Mungu kile alichonituma kuwatendea ndugu zangu wa Jimbo la Momba kitakuwa kimetia kwa sababu nitakuwa Mbunge wa kwanza kabisa kuwafanya ndugu zangu wa Jimbo la Momba kuishi kwenye mazingira ya biashara. Katika vijiji vyetu vyote 72 tulivyonavyo hatuna mji hata mmoja vyote ni kijijini hata mahali ambapo natokea, kwa hiyo, mtakuwa mmetusaidia sana kupata mjini ndani ya Jimbo la Momba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naendelea kuishukuru sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi na nisema kwa kauli hiyo nawashukuru sana wapiga kura wa Jimbo la Momba ambao kwa mara ya kwanza walimsimamisha Mbunge mwanamke na mdogo kwa umri na wakanipa heshima na wakaniamini. Kwa kauli yao walikuwa wakisema tunamtaka mtoto mdogo na mama ambaye tukimtuma anatumika. (Makofi/ Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia 205. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi, nianze kutoa mchango wangu kwanza kabisa kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu kwa namna ambavyo ameendelea kujitoa na kwa namna ambavyo ameendelea kuhakikisha anawafikishia Watanzania huduma mahali popote pale walipo. Lakini pia niendelee kuendelea kuwaomba wale ambao Mheshimiwa Rais amewaamini kama wasaidizi wake, Baraza la Mawaziri Wasaidizi mikoani na wilaya wahakikishe angalau wanakwenda na speed ya mama ili wasiendelee kumwangusha ili Watanzania wapate kile ambacho mama amekusudia kiweze kuwafikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe mchango wangu katika maeneo matatu kama muda utakuwa rafiki, nichangie kwenye eneo la Kilimo, Nishati lakini kwenye eneo la Teknolojia namna ambavyo tukitumia teknolojia vizuri inaweza kutusaidia ku-speed up maendeleo lakini pia ambavyo inaweza kusaidia kutoa ajira kwa vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza kwenye eneo la kilimo, nitachangia katika maeneo mawili. Suala la kwanza ni kwenye pembejeo kama ambavyo waliotangulia wamesema. Kwa kuwa sisi Tanzania siyo kisiwa, tulipopata janga la Corona Nchi nyingine zilipokuwa zimeathirika automatically na sisi Tanzania tuliathirika hata kama sisi hatukujifungia ndani tuliendelea kufanya kazi. Nchi nyingi ambazo zinazalisha mbolea pamoja na pembejeo zingine zilipata changamoto hizo, kwa ambazo zimepata changamoto hizo imesababisha hata vitendea kazi vya kilimo huko especially mbolea imekuwa ni changamoto. Kwa hiyo, tuiombe sana Serikali ambayo ni Serikali ya Chama cha Mapinduzi, Serikali Sikivu sana. Kwa sababu tuna wiki mbili tu tayari tumeshafika kwenye msimu wa kilimo, tunaomba Serikali itoe fedha ya dharula kwa ajili ya ruzuku ya mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili tunaomba kwenye Mpango ambao utakuja baada ya kutoa mawazo yetu 2022/2023, tunaomba viwanda vyetu vya ndani ambavyo vinazalisha mbolea viwezeshwe. Viwanda hivi vikiwezeshwa vitakuja kutusaidia kwenye nyakati kama hivi, hakuna mahali panapoonesha kwenye mpango kwamba baadhi ya viwanda vyetu vitaweza kuwezeshwa ili mbolea ambayo itatoka na kuzalishwa ndani Nchi yetu iweze kuwasaidia wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye jambo la pili kwenye kilimo nichangie kuhusiana na masoko na hapa naomba niende kabisa soko la DRC Congo. Kwa kuwa mama ameonekana kuwa ni Mwanadiplomasia mzuri na katika kipindi kifupi hiki ameonesha namna ambayo ameionesha dunia kwamba tunaweza tukashirikiana na mataifa mengine. Tumuombe sana Mheshimiwa Rais, atusaidie kukaa na Nchi ya Zambia waweze kutuondolea vile vikwazo ambavyo wafanyabiashara ambao wanategemea soko la Congo wanavipitia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitaka kutoa takwimu ya namna ambavyo soko la Congo linaitegemea Nchi ya Tanzania kwa ajili ya kuwasambazia chakula, unaweza kuona hata zile bilioni 50 ambazo tulipoiomba Serikali tulipoleta hoja hapa waliweza kutusaidia, tusingeweza kwenda kuitumia kwa ajili ya kununua mahindi kwa Watanzania, soko la Congo peke yake lilikuwa linatosha wafanyabiashara kununua mahindi ya kutosha na kupeleka Congo au kusindika unga wa mahindi na kusambaza kule. Soko la Congo linatamani Watanzania sisi tuwa-supply tani za unga kuanzia laki moja na hamsini mpaka laki nne. Na inaweze hapo tunaongelea Congo Lubumbashi peke yake labda Katanga na Kolowezi lakini hapo hatuongelei Congo Kinshasa, hatuongelei Goma ni hiyo Congo Lubumbashi peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikiwa vikwazo hivi vitaendelea, vinaendela kuwanyima nguvu wananchi ambao wanazalisha mazao ya nafaka especially wale ambao wanatokea Nyanda za Juu Kusini mikoa yote saba. Kwa hiyo, tunaomba sana Serikali itafuta namna nzuri ambayo itakaa na Nchi ya Zambia waelewane vile vikwazo ambavyo wafanyabiashara wanapata na kwenye biashara nyingine viweze kuondoka ili tuweze kutumia kwa sababu mizigo mingi ambayo inatoka Tanzania inakwenda kama transit. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa kumalizia niongelee suala la teknolojia. Suala la teknolojia, teknolojia ni kama muda hauwezi kushindana na muda, wewe unapotaka kushindana na muda wewe utapitwa na wakati. Unaweza ukaona, sasa hivi hata Bunge letu vitu vingi tunaendesha kwa kutumia kishkwambi, lakini unaweza ukaona Nchi ambazo zimeendelea teknolojia hii ilipaswa itumike kwenye Bunge la Nane, Bunge la Tisa au Bunge la Kumi. Lakini tupo Bunge la Kumi na Mbili mwaka 2021 ndiyo tunatumia teknolojia hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hapa kwenye teknolojia nataka niongelee kuna kitu kinaitwa Block Chain Technology na kwenye Block Chain Technology nataka nitoe takwimu ndogo tu ikiwa kama Nchi zetu zitatamani kuendana na kasi ya teknolojia iliyopo duniani, tusiwe tunachelewa kupokea teknolojia, mambo ambayo tunapaswa kuyafanya sasa hivi tunakuja kuyafanya baada ya miaka kumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu turudi miaka kumi iliyopita nyuma mwaka 2010. Mwaka 2010 wakati teknolojia ya Block Chain Technology inakuja, ndani ya Block Chain Technology kuna vitu vingi, watu wa kada mbalimbali wanaweze wakatumia Block Chain Technology lakini hapa niongelee suala la fedha ambalo naamini kila mtanzania tunafanya kazi ili tuweze kupata fedha. Ndani ya Block Chain Technology kuna kitu kinaitwa Digital Currency, Crypto Currency yaani BitCoin. Mwaka 2010 bitcoin ilikuwa inauzwa chini ya dola 5, ilikuwa inauzwa 0.5 USD ambapo mwaka 2010 dola ya Kimarekani ukilinganisha na fedha yetu ya Tanzania ilikuwa inakwenda kwenye 1,490 – 1500.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa tafsiri yake kama Serikali ingesema sisi tumeilewa hii idea hebu tujaribu tu tuchukue bilioni 1 tuwekeze hapa kama vile ambavyo wananunua hisa na nimegundua inawezekana hata IMF hizi Benki za Dunia wanavyotukopesha wao wanawekeza kwenye vitu kama hivi halafu sisi ndiyo wanakuja kutukopesha tunabaki tunalipa madeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Serikali ingeamua kuchukua bilioni moja ikanunua bitcoin ambayo ilikuwa ni Dola 0.5 ya Kimarekani ukizidisha na thamani ya dola kipindi kile unapata kama 750 maana yake bilioni 1 ukigawanya kwa hiyo fedha unakuja kupata bitcoin laki moja ama elfu thelathini na tano hivi. Ukizidisha na bei ya sasa ya bitcoin, bei ya bitcoin ya sasa ni dola za Kimarekani 66,000 ambapo almost na fedha ya Kitanzania kama Milioni mia moja na hamsini na.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yaani tafsiri yake kama Serikali sasa hivi ingeamua kuziuza hizo bitcoin laki moja na thelathini na tano n.k. tungekuwa na uwezo wa kulipa hilo deni la Taifa ambalo tunadaiwa sasa hivi hizo trilioni 70 na. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu bei ya bitcoin sasa hivi ukizidisha na kama Serikali ingenunua bitcoin kipindi hicho inakuja karibu trilion 90. Kwa hiyo, unaweza kuona namna gani hatuwekezi kwenye teknolojia tunapitwa, 2010 na sasa tulipo siyo muda mrefu. Unaopomuongelea Mwekezaji kama Mark Zuckerberg’s ambaye ndiyo mwanzilishi wa Facebook na sasa hivi hi WhatsApp kama kuna Watanzania 10 tu wangekwenda kununua hiza kwenye kampuni yake hata wakawa na share mojamoja sasa hivi ndiyo trillionaire.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuangalie namna gani tunaweza tukawekeza kwenye teknolojia na ni maombi yangu na mapendekezo yangu, vijana wengi wa Kitanzania waliopo huko na nilipata nafasi kufanya research kwenye nchi za West Africa mwaka 2016/2017. Kipindi kile Nchi za Nigeria zilikuwa zina burn sana mambo haya ya cryptocurrency lakini sasa hivi tunavyoongea muda huu hata ukiongea na Ubalozi wa Tanzania nchini Nigeria. Nigeria wamepitisha cryptocurrency bitcoin ni miongoni mwa fedha ambayo inatumika na wameweka katika mfumo mzuri hata kwa kutumia local network za Nchi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hata Mnigeria asiyejua kusoma ambaye hana uwezo hawezi kutumia internet anaweza akafanya, kwa hiyo ni kitu ambacho katika mpango huu tunaomba kuona Tanzania waisome teknolojia ya Block Chain Technology ili waweze kuiwekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ni kwenye nishati. Kwa kweli sisi Wabunge ambao tunatokea vijijini kwenye umeme, kwa kweli kauli hii ambayo Serikali inasema sana umeme mpaka kwenye vitongoji inatutesa huko vijijini. Sera ya Serikali inasema kwenye kila Kijiji kilometa moja ya nguzo ambazo ziweze kupita. Lakini unagundua...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. CONDESTER M. SICHWALE: Dakika moja tu.

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. CONDESTER M. SICHWALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini unagundua kwamba umeme haupiti kwenye nyumba kama inavyotakikana kwa hiyo wananchi wanajiulia hiyo umeme kwa kila Kitongoji imekuwaje? Na vijiji vingine ni vikubwa ina vitongoji vikubwa kwa hiyo, bado hii kauli inatupa mkanganyiko wananchi wakisikia umeme kwa kila Kitongoji lakini ukienda uhalisia kule umeme kwa kila Kitongoji hakuna.

Kwa hiyo, tunaomba sana Serikali iliangalie jambo hili ikiwezekana umeme kwenye kila Kijiji angalau nguzo kilometa tatu. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi kwanza kabisa nianze kukupongeza wewe kwa namna ambavyo umeliendesha Bunge hili na kuendelea kuwapa Wabunge nguvu zaidi na kuendelea kuliheshima Bunge, kwa dhati ya moyo wangu ninakupongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu kwanza kabisa niseme naunga hoja taarifa zote za Kamati ambazo ziko hapa mezani ambazo ni Kamati ya PAC, LAAC pamoja na PIC ambayo Mimi ni Mjumbe huko. Nitachangia katika maeneo mawili, nitachangia kwenye asilimia Kumi za Halmashauri pamoja na Benki ya Kilimo.

Mheshimiwa Spika, nikianza na asilimia Kumi ya mapato ya Halmashauri naona kabisa nia ya dhati kabisa ya Serikali kwanini waliweka kuwepo na asilimia Kumi hii ya Halmashauri. Lengo kubwa ilikuwa ni kuhakikisha wanampa mwananchi huyu nguvu kumuwezesha katika uchumi wake ikiwa ni sambamba ya kuendelea kumpa madaraka ya yeye kuendelea kujisimamia kama ambavyo Serikali yoyote inapaswa kufanya duniani kote.

Mheshimiwa Spika, kabla sijaendelea na mchango wangu nataka kum-quote kidogo ambaye alishakuwa Rais wa Marekani Thomas Jefferson, anasema hivi, ‘‘The purpose of the Government is to enable the people of a Nation to live in safety and happiness. Government exists for the interests of the governed, not for the Governors’’. Akiwa na maana kwamba Serikali yoyote duniani maslahi yake kwanza ni kuwaridhisha wale ambao wanawatawala na siyo wale ambao watawaliwa. Tafsiri yake, viongozi wote wa Serikali na wasimamizi wote ambao wamepata dhamana cha kwanza kabisa jukumu lao ni kuhakikisha wanalinda maslahi ya wananchi ambayo sisi wao tunawatumikia au kwa lugha nyingine kama ni Serikali ambao tuseme wanawatawala.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo nataka nirejee kwenye Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi, nitasoma mambo kadhaa. Kwenye sura ya Sita ya Ilani ya Chama Cha Mapinduzi, ukurasa wa 161 ukienda kwenye ukurasa wa 174 unasema hivi, kwa kutambua umuhimu wa kuendelea kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi katika hali iliyoshirikishi, Chama cha Mapinduzi katika kipindi cha miaka ijayo imetarajia kufanya yafuatayo: -

(i) Kuimarisha mifumo ya taasisi na uwezo wa Viongozi na Watendaji wa Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kwenda Vijijini kusikiliza na kushughulikia kero na malalamiko ya wananchi kwa wakati na haki na uadilifu. Aidha, kupokea na kusikiliza na kuwahudumia wananchi wanaotembelea ofisi hizo kwa weledi hekima na busara;

(ii) Kufanya mapitio ya Sheria za Tawala za Mikoa na Sheria za Serikali za Mitaa ili kuendana na uboreshaji wa mifumo ya utoaji huduma kwa wananchi;

(iii) Kuimarisha makusanyo ya mapato ya ndani ya Halmashauri kwa kubuni vyanzo vipya vya mapato na kuimarisha makusanyo ya mapato katika vyanzo vilivyopo ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi;

(iv) Kuimarisha Serikali za Mitaa ili ziendelee kuwa chombo cha kuwapa wananchi uwezo na sauti ya kuamua kushiriki kwa karibu katika shughuli za maendeleo, mwisho na mengine yanaendelea;

(v) Kusimamia kikamilifu suala la utawala bora ndiyo hapa ambapo watu wamekula hela hapa, narudia, kusimamia kikamilifu suala la utawala bora, uadilifu, uwajibikaji na matumizi sahihi ya rasimali za umma pamoja na miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika mamlaka hizo, itekelezwe kwa kiwango kinachokusudiwa kuhakikisha kuwa ubora wa miradi unalingana na thamani ya fedha iliyotumika.

Mheshimiwa spika, kwenye ripoti ya CAG inaonesha kwamba kwenye asilimia kumi zipo halmashauri kwamba kwenye asilimia kumi zipo asilimia 155 nchini hazikuweza kurudisha yale marejesho, bilioni 47.5. Bilioni 47.5 zote hizi cha kwanza, zimepora mamlaka ya wananchi ambazo ilani ya Chama cha Mapinduzi inasema; ‘kwamba mtawala yeyote anapokuwepo kwenye madaraka lazima ahakikishe anawapa nguvu wale ambao wao wamemuweka madarakani’. Hizi bilioni 47.5 zimepotea ziko kwenye mifuko ya watu, (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa sio najiuliza na ni wazo langu katika maazimio ambayo wenyeviti wa Kamati wanaweza wakachukua. Nikaona tu; kwa mfano TAMISEMI wangeamua kwamba waweke dirisha maalum linaloshughulikia mikop tu, labda tuchukulie kwamba afisa maendeleo wao wamekuwa na shughuli nyingi na hawana huo utaalam wa kusimamia hizi fedha. Hizi fedha ambazo zimepotea bilioni 47.5 ni katika kipindi cha mwaka mmoja tu 2021/2022, bilioni 47.5.

Mheshimiwa Spika, nikachukulia mfano, wako vijana wengi mtaani ambao hawajaariwa ambao ni bankers, accountant, pamoja na wachumi. Tufanye kama TAMISEMI, ingeamua kuajiri kwa kutumia fedha hizi hizi ambazo ni za Serikali, zimeliwa toka kwenye mifuko ya watu au zimepotea kwa uzembe ambao unasababisha na wataalam wetu kutokuvaa, kuzimiliki zile fedha kwamba ni fedha za Serikali.

Mheshimiwa Spika, mimi nikawa najiuliza, kwenye mabenki yetu, CRDB, NMB na benki zingine zilizopo hapa hapa nchini, hao ambao ni wataalam wa kusasanya mikopo wametoka nje wapi? Si wamesoma hapa hapa ni ma-banker wamesoma hapa hapa nchini kwetu mbona wana huo utaalam wa kukusanya mikopo? Kuna mwananchi yeyote amekopa hela benki anaweza akala fedha? Sasa kwanini sisi Serikali isitenge dirisha kuwaajiri wataalam, wahasibu, wachumi, ma-banker wakasaidia kutoa elimu, kukusanya fedha hizi na fedha hizi zirudi?

Mheshimiwa Spika, nikaweka hesabu ya kawaida tu kwa mfano TAMISEMI, waamua kumuajiri graduate ambaye amemaliza degree yake ya uchumi, uhasibu whatever ambaye anaweza kusimamia vizuri mikopo, waanze kwa kumlipa mshahara wa Shilingi laki saba, wakaajiri watu watatu kwenye halmashauri 84, nikapata kwamba wakiwaajiri watoto watatu kwa mwezi watakuwa wanawalipa milioni 2,100,000, ukichukua milioni 2,100,000 katika halmashauri 184 tutapata milioni 386,400,000. Nikaweka kwamba tufanya kwa miaka mitano ya majaribio, hii ambayo tunatekeleza ilani utakuta hawa vijana umewalipa bilioni 1.932; lakini unaona kwa mwaka mmoja hela zimepotea bilioni 47.5. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tafsiri yake tungeweze kuajiri vijana watatu tu, ambao ni uhasibu, banker na mchumi wanakaa yaani wao kitengo chao ni special kusimamia mikopo tu ya asilimia 10, katika kipindi cha miaka hiyo mitano ambayo tumeweka tungeweza kuwalipa bilioni mbili. Tafsiri yake ni kwamba tungeweza kuokoa hela.

Mheshimiwa Spika, lakini bado nikapiga hesabu, ukiwaajiri vijana hao kwenye halmashauri 184 utaajiri vijana wakitanzania wasiopungua 520. Kwa hiyo pia tungekuwa tume-solve changamoto ya ajiri. Hata hivyo, kama wangesimamia kwa ufanisi, zile hela zingekuwa zinazunguka; maana yake kama mwaka huu watu walikopeshwa bilioni moja, mwaka huu halmashauri ikakusanya tena bilioni moja vikundi vitapata, nikatolea tu mfano, mfano nikachukulia halmashauri yangu. Labda halmashauri yangu sisi labda mwaka huu wa fedha tulipata bilioni 1.7, kwa hiyo ni milioni 170; tukivigawia vikundi vitano wangeweze kupata milioni 34 kwenye kila kikundi. Tafsiri yake milioni 34 hii ingekuja na mwaka mwingine siwangekusanya? Milioni 34 ingekuja na vikundi vingine na wakati huo mapato yaongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hayo ni mapendekezo yangu kwa wenyeviti wa kamati, kwamba ipo haja ya kuona hili. Lakini wakati tunaendelea kuona ipo hoja ya kuona hivi hawa waliohusika na jambo washughulikiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni kuhusiana na benki ya kilimo. Benki ya kilimo, pamoja kwamba mwaka wa nyuma kuna kiwango cha pesa ambazo walipewa kama bilioni 208, lakini walikuwa wanaomba waongezewe mtaji angalau bilioni 760. Ni kweli, mimi ninatamani waongezewe hicho kiwango cha fedha ili kuleta tija kwa wananchi wetu ambao ni wakulima; na tukiangalia nchi hii kwa kiwango kikubwa wazalishaji wakubwa ni wakulima.

Mheshimiwa Spika, pia nataka niseme, watu hawa wa Benki ya Kilimo pamoja na kwamba mnataka kuongezewa fedha na Waziri wa Kilimo upo hapa, pamoja hatukushauri tunakusimamia muda huu, tunaomba kuona mnapotaka kuwaongezea fedha hizi tuwape, zikalete tija kweli kwa wananchi, zifike kule kwa wananchi ambao tunawakusudia. Ni kweli tunaona kuna benki ya kilimo, lakini kuna wakati jamani kule vijijini hatuona sana tija hii ya benki ya kilimo mwananchi wa kawaida hakopesheki, mwananchi wa kawaida kule kijijini hapati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe mfano mzuri tu pamoja naongelea Benki ya Kilimo. Miezi miwili iliyopita tulipata ruzuku ya mbolea, tukaambiwa Wabunge tukatoe taarifa kwamba Serikali inatuletea mbolea, ni kweli mbolea imekuja. Cha kushanga sasa hivi tunavyoongea tumebakiwa na wiki mbili tu msimu wa mvua urudi wananchi vijijini waanze kulima mpaka sasa mbolea hazijafika vijijini, mpaka muda huu mbolea bado na sehemu zingine mbolea imeenda ya aina moja tu.

Mheshimiwa Spika, sasa tunajiuliza wakati mwingine mnapotuomba Wabunge tuwasaidie kuwapikishia hiki tuona na tija ili wakati mwingine tunapokuja hapa; kwamba kama tuliwasaidia kuwapitishia hizi fedha au ndio mnaomba tuwapendekezee kama sisi Bunge maazimio yetu, tuone na mambo ambayo yanafanana na mambo hayo. Kama ni Benki ya Kilimo imewezeshwa imfikie kweli mkulima, lisionekane tu lipo kundi la mapapa hawa ambao wao tu ndio wana-grub na kuchukua wao tu lakini mwananchi wa kawaida yule ambaye ndiye mzalishaji halisi, yule ambaye mpaka sasa hivi analima kwa jembe la mkono, yeye ambaye sasa hivi kununua mfuko mmoja tu wa DAP ni changamoto, amekopeshwa, mwananchi huyu ambaye bado hata mbegu yenyewe kununua ni shughuli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi tunategemea Benki ya Kilimo ndiye huyu tumkusudie apate. Wakati mwingine ukiwauliza watu wa Wizara wanasema Benki ya Kilimo kazi yake si kufungua matawi huko vijijini na sehemu zingine zingine kwenye wilaya kwa sababu hawafanyi transaction.

Mheshimiwa Spika, mimi ninajiuliza, kwani Mheshimiwa Rais, Mama Samia anaishi kwenye halmashauri zote 184? Si anaishi Ikulu hapa Chamwino na Dar es Salaam? Lakini mbona miradi yote akitoa inafikia halmashauri zote 184? Kote anapeleka. Kwa hiyo, kaeni na benki Dar es Salaam, whatever, wekeni kwenye kanda lakini tunachotaka huduma zifike. Whether mtatafuta mawakala wakufikisha hizi huduma kwa wananchi or mtaunda vikundi, lakini tunataka mkulima wa kawaida, yaani tunaongelea mkulima wa kawaida.

Mheshimiwa Spika, na katika hili nimuombe Mheshimiwa Waziri Bashe, twende nikakukutanishe na wakulima wa kawaida huko vijijini ili tunapoongea muwasilize wenyewe kwa masikio yao, hawapati mikopo.

Mheshimiwa Spika, naunga hoja zote za kamati ambazo ziko mezani, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii naomba kupitia Bunge lako Tukufu kwa heshima na taadhima niombe sana Serikali yangu Sikivu ya Chama Cha Mapinduzi ninaomba kwenu sana sana tunaiomba Serikali yetu tuwatazame wakulima walioko vijijini.

Mheshimiwa Spika, kwa kusema hayo simaanishi kwamba labda wakulima ambao wako mjini hawastahili kuombwa lakini Serikali yangu ya Chama Cha Mapinduzi wakulima hawa ambao wako vijijini ndiyo ambao wamekuwa ni waaminifu kwetu mno katika kutupa kura na sehemu zingine hawaamini hata vyama vya upinzani wanaelewa ni CCM tu. Kwa hiyo, fadhila ya kuwalipa wakulima hawa ni sisi kuwatazama wakulima hawa jamani Benki ya Kilimo haiwafikii huko vijijini Benki ya Kilimo haiwafikii ndiyo maana wamegubikwa na wimbi la hawa watu ambao wanaitwa AMCOS. AMCOS mmewapa watu wa vijijini wawasaidie spidi ya watu wa vijijini hawafanani kabisa na spidi ya watu wa AMCOS, AMCOS ni waongo samahani Waheshimiwa wengine wametumia lugha na kusema ni matapeli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwenyewe nimehusika katika kusimamia kuendelea kuwaombea mkopo wapiga kura wangu wa Jimbo la Momba ambao walikuwa wameomba AMCOS nimepiga simu kwa mameneja kadhaa wa Branchi husika za wilaya mpaka kwa mameneja wa kanda kwa ajili ya kuendelea kuomba mkopo wananchi wameahidiwa kupewa mkopo kuanzia mwezi wa 12 mpaka sasa wanaendelea kuomba kilimo kinaanza kulimwa kuanzia mwezi wa 11 mpaka wa 12 watalima nini? Hivyo Serikali yangu naomba kwa kuwa iko Benki ya Kilimo ambayo riba yake ni nafuu kwa wapiga kura hawa waaminifu wa Chama Cha Mapinduzi ambao tukienda tunapiga magoti na kugaragara kwao kuwaambia Serikali ya Chama Cha Mapinduzi ni Sikivu basi tuwape kitu ambacho kinafanana na uelewa wao ambao ni Benki ya Kilimo na inatoa riba nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ukisikia mchele mzuri ambao unalimwa Kamsamba unalimwa ndani ya Jimbo la Momba achilia tu kwamba tunalima na kusambaza kwenye mikoa mingine ambayo iko hapa Tanzania lakini mchele ambao tunalima ndani ya Jimbo la Momba tunasambaza mpaka nchi ambazo ziko SADC. Lakini cha kushangaza ndani ya Jimbo la Momba ikiwa kama lilivyo jimbo lenyewe tuna bonde kubwa kabisa ambalo linabeba na mto wa Momba lakini cha kusikitisha tuna skimu moja tu ya umwagiliaji na ambayo na yenyewe haifanyi kama ambavyo inatakikana. Skimu ya umwagiliaji ya Naming’ong’o.

Mheshimiwa Spika, lakini Pamoja na hayo Serikali imeshawahi kutoa kwenye skimu nyingine ya umwagiliaji ambayo iko Iyendo, Kata ya Kapele Zaidi ya pesa milioni 800 na Wizara ya Kilimo wakaunda Tume kwa ajili ya kwenda kukagua skimu hii lakini mpaka sasa tunavyoongea hatujawahi kupewa hata majibu na hatujui nini kinaendelea kuanzia niko Form four na mpaka sasa ni Mbunge, jamani Serikali tunaomba wananchi hawa na wapiga kura hawa ni waadilifu na ni wachapakazi tunaomba tuwawezeshe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini skimu ya umwagiliaji Naming’ong’o kaka angu Bashe nimekufuata mara kadhaa hii skimu Serikali imetoa hela nyingi Zaidi ya bilioni 4.7 ina matatizo kadhaa farm layout kuna shida designing na drawings zina changamoto leveling farm roads mwenyewe nimeitembelea ile skimu mara kadhaa mara nyingi nimeitembelea hakuna mifereji ambayo inaonyesha inatoa maji na inaingiza maji, zile njia zote za kupitishia maji kwenye skimu zimejaa matope basi tunaomba mtupe excavator ili hata wataalamu ambao wako kule tuweze kukwangua wenyewe ile mifereji tunaomba sana.

Mheshimiwa Spika, lakini bonde hili lina zaidi karibu hekta 100,000 za kulima mpunga pamoja na mazao mengine ya umwagiliaji na mbogamboga. Lakini cha kushangaza ndiyo skimu hizo ambayo hata iliyopo yenyewe ni mbovu tunaomba kabisa tupate skimu ya umwagiliaji Kamsamba tupate skimu ya umwagiliaji Msangano, tupate skimu ya umwagiliaji Kasinde, tupate skimu ya umwagiliaji kubwa zaidi kwenye Mto Tesa tunaomba mtuongezee. Kwa sababu mazao yote ambayo tunayazalisha pale kwenye Jimbo la Momba ni tija kwa Mkoa ni tija kwa mikoa mingine lakini Taifa linakusanya mapato ya kutosha kwenye zile nchi za Jirani ambazo tunazitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimekuwepo Zambia muda mrefu wanatumia mchele wa kutoka Tanzania tu na kama Jimbo la Momba ndiyo tuko pale mpakani Kongo wanatumia mchele wa Tanzania tu lakini hata nchi zingine ambazo ziko huko Kusini wanatumia mchele wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini siyo hayo tu kama ambavyo ameongea Mheshimiwa Deus Sangu tunalima pia mahindi yamkini tungeweza kulima hata mara tatu kwa mwaka lakini tutafanyaje mkopo hatupewi tumepewa matapeli AMCOS. Umwagiliaji hakuna sasa huyu mkulima huyu tunamtazamaje aliyepo vijijini? Tunamtazamaje.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho tunaishukuru sana Serikali kwa kutupa soko la mifugo na mazao pale Kakozi lakini tuna vijiji 72 na jiografia jamani ni ngumu. Jiografia ya Jimbo la Momba ni changamoto wapo Waheshimiwa Wabunge ambao wamefika hapo wanaijua ile vijiji 72 ghala moja tu. Mtu aliyoko kule Kamsamba Usoche ili atoe mazao yake kabla yajafikisha kule juu Kakozi hayo maghala hakuna tuna maghala mawili tu na lingine hili halijakamilika liko toka kipindi hicho. Tunaiomba Serikali tunaomba kuongezewa maghala hata kama hayatafika 72 kwenye kila Kijiji lakini angalau basi yafike hata 26 kwa kuanzia tunaiomba sana Serikali ili tuweze kupandisha mazao yetu kufika pale Kakozi.

Mheshimiwa Spika, na jambo lingine la kumalizia tunaomba Wizara ya Kilimo kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi tuwekewe mkakati mzuri namna gani hawa wakulima hawa wapimiwe ardhi zao ili wawe wanakopesheka na kwenye benki wenyewe wakienda peke yake ardhi ni potential tuko mpakani tunaishia tu kugawa ardhi kwa wazambia na Watanzania kwa sababu hakuna muundombinu mzuri ambao Serikali imeweka kwa wapiga kura hawa, naunga mkono. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi. Kwanza niseme naunga mkono hoja zote za Kamati ambazo zimewasilishwa Mezani; Kamati ya Bajeti pamoja na Kamati ya Mambo ya Nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaelekeza mchango wangu kwenye Wizara ya Mambo ya Nje. Hapa nataka kuchangia kwenye diplomasia ya uchumi. Mwenyekiti wa Kamati alipokuwa akiwasilisha hoja yake, alisema kwamba tunapotaka kutekeleza diplomasia ya uchumi kwenye Wilaya zetu, hususan kwenye Halmashauri pamoja na tawala za mikoa, watendaji wetu wa Serikali hawana uelewa kuhusiana na diplomasia ya uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii naona ni kwa sababu, zipo hata jumuiya za kikanda ambazo sisi ni wanachama huko, kumekuwa na utaratibu wa Serikali kutokurudi kutupa taarifa ya jumuiya hizo. Kwamba, kwa wakati huo malengo yale ambayo sisi tulijiunga kwenye hizo jumuiya, mpaka sasa hivi tunaendelea kunufaika na nini; na mpaka sasa hivi nini kinapaswa kuboreshwa? Wachukue maoni ya wadau? Tunapoongelea diplomasia ya uchumi ni pamoja na hizo jumuiya ambazo ndiyo zinatufanya tuwe washirika pamoja na wenzetu tunapotaka kutekeleza hiyo diplomasia ya uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kurejea kidogo kutoka kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, kwenye Sura ya 7, Ukurasa wa 182, ule ukurasa wa 184 inapoongelea diplomasia ya uchumi, nitasoma kipengele kimoja tu. Kinasema kwamba, “Kulinda uchumi na maslahi mapana ya Taifa kwa kutumia jiografia ya nchi kimkakati na ushawishi wa kihistoria, hususan kwenye ukanda wa Kusini.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi katika miaka mitano ambayo tunatekeleza, inapoongelea kwenye suala la mambo ya diplomasia ya uchumi inatambua kwamba ni lazima tutumie hizi jumuiya za kikanda, lakini na historia zetu za kiuchumi huko nyuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nataka kuongelea sana sana kwenye hii jumuiya. Mwaka 1996 tulikuwepo kwenye COMESA, mwaka 2000 tukajitoa kwenye COMESA. Swali ambalo nataka kujiuliza hapa, sasa hivi ni miaka 20 imepita toka sisi tujitoe kwenye umoja huu ambao ulikuwa unaunganisha nchi za Kusini mwa Afrika pamoja na nchi ambazo ziko Mashariki ya Afrika. Ziko baadhi ya nchi ambazo ziko kwenye SADC, lakini haziko kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki, lakini nchi hizi zinapatikana COMESA tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, nchi kama Misri na Ethipia; hivi kwa mfano, unamuachaje Misri awe ni mshirika wako katika kutekeleza diplomasia ya uchumi, ikiwa Misri mwenyewe ndiye anatujengea Bwawa la Mwalimu Nyerere? Egypt wao ndio wanatujengea Bwawa la Mwalimu Nyerere? Je, zipo fursa ngapi za kiuchumi ambazo sisi tulipaswa tupate kutoka kwenye nchi ya Misri? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi ya Misri ndio watu ambao tunawauzia bidhaa za ngozi. Kwa hiyo, unaweza ukaona kwamba, Serikali haijawahi kuja na ripoti miaka 23 iliyopita, sisi tulivyojitoa COMESA kipindi kile kwamba, labda ada ilikuwa kubwa, tulikuwa tunalinda bandari zetu kwamba tungekuwa wanachama, watu wangepitisha mizigo yao bure; tulikuwa tunalinda viwanda vyetu vya ndani, lakini sasa hivi zama zimebadilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunajitoa COMESA mwaka 2000 tuchukulie process zilianza mwaka 1999, tayari tulikuwa tuko karne ya 20, sasa hivi tunaongelea kuanzia mwaka 2000 na sasa hivi tuko karne ya 21 teknolojia imebadilika, mambo ya uchumi yamebadilika na uongozi umebadilika. Tumetoka kipindi kile akiwa Rais ni Hayati Mheshimiwa Mkapa, sasa hivi tuko na Mama Samia ambaye yeye ni mwanadiplomasia wa kwanza. Je, hatuoni tunaendelea kumpa kazi ya ziada ya kwenda kuanza kuongea na watu wa Misri na watu wa Ethiopia ili tukaenao mezani, tukubaliane baadhi ya mambo wakati tunayo platform ambayo ni COMESA ingetusaidia kuweza kushirikiana na wenzetu kuwa pamoja?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati nauliza swali la msingi hapo juzi, Serikali walijibu kwamba, kwa sababu tuko EAC na tuko SADC hatuoni umuhimu wa sisi kuwepo tena COMESA. Sidhani kama hili ni sawa kwa sababu, hizi nchi ambazo ziko East African Community na hizi nchi ambazo ziko SADC na hizi ambazo ziko COMESA peke yake haziko kwenye nchi zote hizi mbili, tunazikuta wapi tukitaka kushirikiana?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema tanataka kuweka umoja wa Afrika ili tuwe na sehemu moja ya kufanya biashara; je, tunapotaka kutekeleza haya, kama tunayo platform ambayo sasa hivi inaweza ikatuunganisha na nchi zaidi ya 20 na sisi tukawa huko ni wanachama, wafanyabiashara wetu wakanufaika, wafanyabiashara wetu wakasaidika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naona ipo haja Serikali iwe inakaa inatuletea ripoti. Hata sasa hivi tuko East African Community, lakini bado ziko changamoto nyingi sana ambazo wafanyabiashara wetu wanaendelea kupitia. Tuko SADC sasa hivi, lakini kulifikia soko la Congo tu pamoja na kwamba, Congo ni mwanachama mwenzetu kwenye SADC, lakini tunapata changamoto nyingi. Wakati mwingine unakutana na wafanyabiashara mpaka wanashauri kwamba labda tungekuwepo COMESA ingetusaidia kupunguza hizi changamoto kwa sababu, lengo la COMESA lilikuwa ni kuwepo na ushirika wa kiuchumi, kuwepo na soko moja ili kuondoa hizo changamoto za kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa naona kwamba, Serikali iende ikafanye tathmini itujie na majibu, katika miaka 23 ambayo tunayo mpaka tulipofikia sasa hivi, ipo haja ya sisi kurudi COMESA. Hata kama hawataona haja ya kurudi COMESA, waje watusaidie kuainisha tutambue. Pia takwimu hizo zitusaidie kwenda kule kwenye Halmashauri zetu na kwenye mikoa yetu kwa wananchi wa kawaida ambao tunataka watekeleze diplomasia ya uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoongelea mambo haya ya jumuiya, imeonekana diplomasia ya uchumi ni ya watu wa kaliba fulani, waliosoma tu, watu ambao wako juu, wakati watekelezaji wakubwa ni wakulima, wananchi wa kawaida. Wangefahamishwa haya mambo, yamkini wangejua kwamba, kama nchi yetu iko SADC tunanufaika na vitu gani? Kama nchi yetu iko kwenye umoja wa Afrika Mashariki tunanufaika na vitu gani? Wananchi hawana uelewa kabisa katika mambo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuongezea, hapo tunaposema tuendelee kufanya tathamini zetu na Serikali iwe inatuletea taarifa kutoka kwenye jumuiya tulizonazo, mfano mzuri unaweza ukaona kwamba, unapoenda kwenye ule ukanda wa Ziwa tanganyika tumejenga bandari zaidi ya tano. Kuna Bandari ya Katanga, Bandari ya Kipili, Bandari ya Kabwe, na Bandari mpya ya Karema. Tulipokuwa tunauliza swali hapa, ni namna gani Serikali itatusaidia kuondoa changamoto ambazo tunazipata kupitia Zambia kuingia nchi ya Congo? Serikali ilikuwa inatujibu kwamba, tumeshajenga bandari na ni mkakati ambao utatufanya sisi tuingie DRC moja kwa moja bila kupitia nchi yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu tuna uelewa kidogo, mimi nikamfuata Mheshimiwa Waziri wa Uchukuzi nikamwambia Mheshimiwa Waziri majibu haya ambayo mnatupa, nafikiri Serikali haijafanya tathmini. Uende wewe na timu yako ukatembelee zile bandari ambazo zimejengwa kwenye Ziwa Tanganyika na uende upande wa pili ambao ni wa Congo, ili ukaone kama jambo hilo linatekelezeka ndani ya mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri alipoenda, amekuja kutupa taarifa. Unagundua kabisa kwamba ni kitu ambacho hakitafanyika mwaka huu wala hakitafanyika mwakani ili sisi tuweze kupitia Ziwa Tanganyika kuweza kufika Congo, especially, kufika Lubumbashi ambayo ndiyo miongoni mwa majimbo ambayo yanafanya vizuri sana kibiashara ambapo hata sisi Watanzania wengi wana-target kupeleka mazao yao huko. Ni kitu ambacho sio cha sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wao kwa kwenda kufanya tathmini, na kufanya takwimu ikatusaidia wao kuja na njia mbadala wajue tukitaka kuingia Congo kuna namna ambavyo hatuwezi kuikimbia Zambia. Aidha, sisi turudi COMESA ili kurahisisha kuondokana na hizo changamoto au kutafuta njia nyingine mbadala namna gani sisi tuisaidie nchi ya Congo kujenga barabara kwao ili tuweze kupita kutoka Ziwa Tanganyika kwenda moja kwa moja. Hayo yote yamefahamikaje? ni baada ya viongozi wetu wa Serikali kwenda kufanya tathmini na kuleta ripoti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, siyo mambo ya kuendelea kukaa. Kama tulishajitoa COMESA sasa hivi tuko wakati mwingine, vita ya uchumi ni kubwa, kila mtu analiangalia soko la Congo. Nasi kwa kutumia soko la Congo tu peke yake linaweza likatuongezea mapato kwa kiwango kikubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru. Ni Condester Sichalwe. Ahsante kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa nianze kwa kuipongeza Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi na kuishukuru. Kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Momba, nashukuru sana kwa miradi yote ambayo tulipewa pesa ndani ya Jimbo la Momba. Yawezekana hatujafika pale mahali tunapotaka, lakini tunasema asiyeweza kushukuru kwa kidogo, hawezi kushukuru hata akipewa kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitumie fursa hii kuwashukuru Watanzania; pamoja na changamoto yote ya mfumuko wa bei tunayoipitia, wanaendelea kupambana kuhakikisha wanaijenga nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka leo hoja yangu niielekeze katika kuishauri Serikali na kuiomba. Nimesoma vizuri sana Taarifa ya Kamati ya Viwanda na Biashara, lakini kuna kipengele ambacho natamani kuona Serikali inawasaidia wananchi wa chini kabisa; mwanachi yule aliyeko kijijini ambaye hajui hata kusoma na kuandika, anaweza akatumia uwezo wake na maarifa yake ambayo Mwenyezi Mungu amemsadia katika kuzalisha viwanda vidogo vidogo na kufanya biashara ndogo ndogo ambazo zinawasadia kulea watoto wao na kuwasomesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inapotupelekea Vituo vya Afya na Zahanati, wanafanya hizo biashara ndogo ili waweze kupata fedha ya kununua dawa kwenye vituo vyetu. Pamoja na kwamba Serikali imetoa elimu bila malipo, kuna kununua daftari, uniform za watoto na michango mingine elekezi ambayo imewekwa kwenye shule zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapotoa mchango huu, nataka nijielekeze kwenye Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa wa Miaka Mitano ambao unaanzia mwaka 2021/ 2022 mpaka 2025/2026 wenye dhima ya kujenga uchumi shindani wa viwanda kwa maendeleo ya watu. Tafsiri yake ni kwamba tunapotaka kujenga viwanda, vifanane na maendeleo ya watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuongelea Local Industry na Consumers Industry; na hapa nataka kuongelea pombe za kienyeji. Pombe za kienyeji kwenye makabila mbalimbali na mikoa mbalimbali; kila makabila wana pombe zao za kienyeji. Kuna pombe ya ulanzi inatengenezwa kule Iringa, kuna mbege kule Kilimanjaro, dengelua, ntulu kule Singida kwa kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu, pombe ya mnazi kwenye mikoa huko ya Pwani; pia kuna kindi, kimpumu na pombe nyingine ambazo Serikali imezizuia, mfano gongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuishauri Wizara ya Viwanda na Biashara, kwanza kabisa iiunde bodi kama ambavyo Wizara ya Kilimo imefanya, imeunda Bodi ya CPB ambayo inasimamia mazao ya nafaka na mazao yote mchanganyiko. Mfano sijui mpunga, mahindi, dengu na mazao yote. Wizara ya Kilimo imeunda bodi maalum.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumwambia Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara, pombe hizi ambazo naweza nikasema Serikali haijazipa kipaumbele na imezidharau, wakati mwingine wanasema mataputapu. Ukionekana wewe unakunywa kindi, kimpumu au gongo, hujielewi, huna akili kabisa. Ila ukionekana unakunywa bia ambazo watu wa TBL wanatengeneza, unaonekana ni wa kisasa. Hata ukienda kwenye Balozi zetu huko kuna ile inaitwa Cartas, wanawatengea kabisa fungu kununua zile pombe za bei ghali ya shilingi 300,000 , ya shilingi 400,000 , lakini zote ukizionja ladha yake haina tofauti na gongo. Tunajiuliza, swali ni kwamba, ni sababu hizi zina jina la Kizungu na gongo ina jina la Kibantu?

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu, bodi hii itakapoundwa, inatasaidia kwenda kupima kiwango ambacho gongo inapotengenezwa. Je, mlishawahi kupima mkaona ni nini watu wa TBS wanaweza wakatusaidia kutoa makali ambayo yapo kwenye gongo yafanane na konyagi na pombe nyingine hizo ambazo mnaziona ni za kifahari ambazo matajiri wanakunywa, lakini wote wakinywa wanalewa?

Mheshimiwa Spika, nataka kusema kupitia Bunge hili Tukufu, pombe hizi za kienyeji ambazo tumezidharau, wapo wafanyabiashara wakubwa na mashuhuri ambao bibi zao, mama zao, shangazi zao, wamewasomesha kupitia hizi pombe za kienyeji. Wapo Wabunge humu ndani ya Bunge lako hili Tukufu ambao ni wasomi na ni maarufu na tunawajua na nianaamini hata kaka yangu Mwigulu huko kwao atakuwa amesomeshwa na pombe hizi za kienyeji.

Mheshimiwa Spika, pia huko nyuma mimi nilishawahi kusoma profile moja ya Kiongozi mkubwa sana hapa nchini ambaye alihojiwa na vyombo vya Kimataifa Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo na yupo hapa kwenye Bunge hili Tukufu akasema kwamba amesomeshwa na bibi yake kwa kutumia pombe za kienyeji. Yupo mahali hapa, nione kama hawezi kuthibitisha.

Mheshimiwa Spika, swali langu kwa Watanzania na Wabunge mliyopo humu ndani, ni nani hapa aniambie hawezi kutamani mtoto wake asome awe Profesa kama Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo? Ni nani aniambie? (Makofi/Kicheko)

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Condester, taarifa.

T A A R I F A

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekaa na Askofu hapa; kwa hiyo, kidogo ni changamoto. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka tu nimpe taarifa mchangiaji kwamba kule kwetu Kijiji ninachotoka kinaitwa Mgela, pale tumejenga mpaka Kilabu cha Pombe na tumekijenga vizuri na ni source kubwa ya mapato. Kwa hiyo, ni mchango wake mzuri sana. Ni kweli mimi nimesoma kwa pombe, kwa hiyo, mchango wake ni mzuri sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Condester.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa yake. Yupo Mbunge mwingine hapa, mama yangu anaitwa Mheshimiwa Tendega, naye amesoma mpaka Chuo Kikuu kupata digrii yake kwa wazazi wake kupika pombe za kienyeji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa msingi kwa Serikali, miradi mikubwa yote kama SGR, sijui Bwawa la Mwalim Nyerere, tunaipenda sana. Ndani ya Jimbo langu tuna miradi mikubwa mitatu ambayo ina-worth mabilioni ya pesa, lakini miradi hii mpaka sasa hivi tunavyoongea ina zaidi ya miaka mitano haijatekelezeka. Swali la kujiuliza: Je, wananchi hawa tunapoendelea kusubiri hii miradi mikubwa itekelezeke hawaumwi? Hawasomeshi Watoto? Hawaishi? Wakiumwa wanatibiwa na nini? Wanafanya shughuli hizi hizi, pombe za kienyeji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipofanya ziara na Naibu Waziri wa Utawala ambao wanasimamia TASAF, iko chini yao, alipojaribu kuwatembelea wamama ndani ya Jimbo la Momba; wamama ambao wanafanya vizuri kwenye TASAF wakipewa pesa, ni wale ambao wanatengeneza pombe za kienyeji.

Sasa mimi najiuliza, sisi kila siku hatuwezi kuthamini vilivyo vyetu. Kama ambavyo wamechangia Wabunge wengine hapa, sisi kila kitu ni ku-import, kila kitu ni ku-import; jamani hata pombe tu, hatuwezi kuwasaidia hawa watu ambao wanatengeneza ulanzi kule Iringa wapate ithibati?

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuipa ithibati kimpumu, kinde ambazo zinatengenezwa kule Momba? Hatuwezi kuwasaidia wamama na wabibi wa Kitanzania tupate wasomi wengi kama akina Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo? Mpaka sasa hizi tunaendelea kuongea suala la Liganga na Mchuchuma, tutasubiri miaka 50…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: …lakini pombe hizi wananchi wanakula, wanaishi, wanavaa, wanasomesha watoto wao. Mimi nawajua vijana wengi wa Kitanzania wanaendesha V8 huko, mama zao wamewasomesha kwa kupitia pombe za kienyeji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema Waziri wa Viwanda na Biashara atakaposimama hapa, aseme kuhusiana na pombe za kienyeji siyo kushika tu shilingi yako, nitaikwapua shilingi yako. Nitataka aseme neno kuhusiana na pombe za kienyeji wanakujaje? (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Sichalwe, nilikuongezea dakika mbili.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia hizo dakika mbili. Nimefanya utafiti wangu kuonyesha kwamba kuna soko.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Muda wake umeisha Mheshimiwa Matiko.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Sichalwe, mwache akupe taarifa kwa ufupi.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nitamalizia hoja yangu. Okay.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nataka kumpa taarifa Mheshimiwa Condester; mchango anaoutoa ni mzuri na valid kwa Watanzania wote. Kwa hiyo, napenda kumpa taarifa kwamba kuna kipindi Watanzania ambao wanazalisha mafuta kwa njia ambazo zilikuwa hazijarasimishwa, walikamatwa na Jeshi la Polisi na Waziri wa Kilimo akatoa tamko akasema Watanzania hao wasikamatwe, badala yake wasaidiwe ili waweze kujikwamua zaidi na kuweza kupimwa na kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa mchango wake huu, ni kweli na dhahiri unasaidia Watanzania wengi. Hata wakitaka kuchukua takwimu hapa, ni zaidi ya asilimia
70. Basi Serikali ichukue hawa Watanzania wanaofanya biashara ya pombe zilizotajwa hapa, wasikamatwe na kupelekwa Magerezani, na badala yake wawezeshwe kuhakikisha kwamba inakuwa ni pombe ya kiwango na inangia kwenye market. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Condester.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa taarifa, nimepokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutaka kuonesha kuthibitisha, wenzetu nchi za jirani wana-support watu ambao wanatengeneza pombe za kawaida. Nimekuja na sample za pombe za bei rahisi kabisa hapa.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Waheshimiwa muda wake umemalizika, namwachia amalizie.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, pombe kama hii inauzwa sijui shilingi 1,000 inatoka Malawi; pombe kama hii inauzwa sijui shilingi 8,000 inatoka Zambia…

(Hapa Mhe. Condester M. Sichalwe Alionesha chupa za pombe mbalimbali)

MBUNGE FULANI: Ni gongo hiyo!

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Zote hizi ni gongo, Shilingi 1,500 na zimeingia nchini kinyume na utaratibu. Hizi ni gongo zimepewa majina ya kizungu, owners kutoka Zambia; sijui lulars whisky kutoka Zambia; sijui Jambo gin, sijui K-Vant, sijui icelandan… (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi. Shukrani zangu ziambatane na pongezi za kukupongeza wewe binafsi, kwamba unawatia moyo wazazi wengi ambao wamewekeza kwa watoto wa kike. Wanawaambia wasome kwa bidii ili siku moja wawe ma-lecturer kama wewe; wanawaambia wasome kwa bidii ili siku moja wawe Wanasheria kama wewe; wawe wanasiasa kama wewe na ikiwekezekana waweze kushika Mhimili kama wewe ulivyo. Kwa hiyo, unatutia moyo sana mabinti wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kwanza kabisa kwa kuipongeza Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi. Kwa dhati ya moyo wangu kama mwakilishi wa wana-Momba, naishukuru sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi ambayo inaongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Hassan Suluhu kwa miradi yote ya maendeleo ambayo tumepewa ndani ya Jimbo la Momba. Ingekuwa naruhusiwa kupiga magoti hapa, ningepiga goti la heshima la kuonesha shukrani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu leo utajielekeza kwenye kuwasemea vijana wa Kitanzania, hususan kwenye suala la ajira. Ajira kwa vijana ni suala la usalama kama ambavyo tunavyoangalia usalama wa afya zetu na usalama wa chakula. Vijana ambao wanaajiriwa katika kipindi hiki, miaka 20 ijayo ndio viongozi wakubwa wa mhimili kama wewe, ndio atapatikana Mheshimiwa Rais hapo, Baraza la Mawaziri, na Wabunge kama sisi. Kwa hiyo, ni usalama wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na changamoto kubwa sana ya ajira nchini kwetu, lakini changamoto ya ajira siyo issue, ila ni namna ambavyo ajira hizi zinagawanywa; ni

namna ambavyo ajira hizi zinaenda zikiwa na usawa sawia, especially kwa sisi ambao tunatoka vijijini ambako hakuna fursa nyingi za biashara, hakuna makampuni binafsi ambayo tunajua kwamba watu wanaweza wakaajiriwa huko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niseme kwamba changamoto ya ajira inawezekana inasababishwa na jambo fulani. Kwenye uchumi kuna kitu kinaitwa demand and supply. Supply inapokuwa low au inapokuwa limited, demand ikiwa high inapelekea bei kupanda kwa kitu husika. Kwa hiyo, mahitaji yanapoongezeka, bei inapokuwa juu, lakini vitu hivi huwa vinaboreshwa, kwa sababu watu wanalipia gharama kubwa kupata hicho kitu.

Mheshimiwa Spika, sasa tuangalie kwenye ajira zetu, inawezekana changamoto ya ajira imetokana na kuwepo kwa teknolojia na kuongezeka sana. Teknolojia imechukua ajira nyingi za vijana, lakini pia nchi yetu imepiga hatua kwenye kuboresha elimu. Wasomi wameongezeka ukilinganisha na nyuma, lakini mambo yalivyoendelea sana, kwa mfano mambo ya artificial intelligence mambo ya Web3, mambo ya Blockchain, yamechukuwa ajira za vijana, lakini tunaongelea hicho kidogo ambacho kinapatikana chenye thamani, kinatakiwa kipatikanaje? Changamoto ndiyo inaanzia hapo.

Mheshimiwa Spika, mimi naona kwamba ipo misingi ya utawala bora iliachwa kwa namna ambavyo ajira hizi zinagawiwa. Kwenye misingi ya utawala bora, kuna vitu ambavyo unaambatana navyo. Lazima kuwe kuna uwazi, namna ambavyo ajira hizi zinapatikana, ni kwa uwazi? Zinagawiwa kwa uwazi? Ushirikishwaji; ajira hizi zinapokuwa zinagawanywa kunakuwa na ushirikishwaji kila mtu aweze kuona? Kuwajibika; watu wanawajibika wanapogawa hizi ajira kwenye Halmashauri zote na kwenye maeneo yote, na kwa watu ambao hawana watu wa wakuwasemea? Ufanisi; kuna ufanisi kwenye jambo hili? Je, kuna usawa na ujumuishi?

Je, watu ambao hawana watu wa kuwasemea, hawana ndugu zao viongozi, usawa umefanyika? Je, makubaliano yanayoelezeka, yapo makubaliano ambayo yakionekana kwamba hapa palifeli tukubaliane ili wakati mwingine iweje? Je, usikivu wa karibu wa Serikali, jambo hilo linafanyika? Lingine ni kufuata utawala wa sheria.

Mheshimiwa Spika, jambo hili likapelekea jamii kuanza kukosa Imani. Siyo kwamba labda inakosa imani na Rais wao, lakini inakosa imani na wale ambao watu Rais amewaamini, mamlaka zimewaamini, ambapo wao ndio wanachakata hizo ajira ziweze kuwafikia watu wote. Kwa nini wananchi wakapoteza imani? Kwa nini wananchi waache kuamini mfumo ambao unachakata ajira, waanze kutufuata sisi Wabunge? Kila Mbunge anafuatwa ili aweze kumsaidia mwananchi kuweza kupata ajira? Mimi mwenyewe kwenye simu yangu nini meseji zaidi ya 300; kila mtu ananiambia wewe ni mtu mkubwa. Mimi ni mtu mkubwa kuanzia lini? Mimi kazi yangu ni kuwasemea wananchi, kuyaleta mahitaji yao hapa kwa Serikali. Kwa nini wananchi wapoteze imani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wananchi watakapopoteza imani kwa vyombo ambavyo vinachakata ajira zetu, tutatengeneza jamii ambayo itakuwa na matabaka sana. Miaka 20 au 30 inayokuja tutakuwa na watu ambao wanaamimi kila mtu aliyeko madarakani ni mtoto wa kigogo, kitu ambacho siyo kweli. Sisi wengine ni watoto wa wakulima, mbona tuko hapa ndani! Kwa hiyo, ni lazima ajira hizi ziwe jumuishi, ajira hizi zizingatie utawala bora ili kila mtu aweze kupata. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini imani ni kitu cha muhimu? Hebu tuangalie, mimi kwa imani yangu kama Mkristo, tunaamini kwamba hata Mungu wakati anaumba ulimwengu, aliumba kwa imani. Nisome kwa Waraka wa Waebrania Sura ya 11 mstari wa kwanza mpaka wa tatu.

Biblia Takatifu, inasema hivi: “Basi imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasionekana. Maana kwa hiyo wazee wetu walishuhudiwa. Kwa imani twafahamu ya kuwa ulimwengu uliumbwa na kwa neno la Mungu, hata vitu vinavyoonekana havikufanywa kwa vitu vilivyo dhahiri.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Biblia yenyewe inasema kwamba imani ni kuwa na hakika na mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana. Kwa hiyo, wananchi wakianza kuamini kwamba sisi hatuwezi kutendewa haki, mbele tunaweza kutengeneza kizazi ambacho ni cha waasi. Mbele tukatengeneza watu ambao hawatawaamini tena viongozi walioko madarakani, kwa sababu watakuwa wanamwona kila aliye Spika ni kwa sababu alikuwa ni mtoto wa kigogo. Jaji Mkuu labda wa Mahakama, ni mtoto wa kigogo. Ni lazima tuweze ku-balance kama ambavyo wazee wetu wa zamani, kila mahali ambapo nchi hii ilitoka, alitoka kiongozi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiangalia Kanda ya Ziwa, alitoka Rais wa kwanza; tukiangalia sijui Rais wa Awamu ya Nne Dkt. Jakaya Kikwete, ametoka Pwani; tukiangalia sijui Mtwara kule, alitoka Rais. Pia nchi hii, wako Viongozi kama akina Kawawa, walitoka sehemu za kawaida. Kwa hiyo, ni lazima ajira hizi ziwa-spot vijana kutoka maeneo yote. Ni lazima Serikali ifike hatua itengeneze imani kwa Watanzania kwamba ajira hizi zinapotokea, wakikaa chini huko sirini ambapo sisi hatuoni, wawaaminishe Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu ni nini? Ushauri wangu ni mambo yafuatayo: Wapo vijana wengi wa Kitanzania ambao ni ma-programmer wazuri sana. Mimi mwenyewe by professional ni programmer. Tunaomba vijana hawa wa Kitanzania waitwe, wawasaidie kutengeneza system ambayo mtakapokuwa mkikaa sirini, mkiwaita vijana; kwa mfano, kama nafasi zilizotolewa ni 21, kama 100,000 wana sifa, system ile iwe ya wazi. Tuweze kuona kwamba kama watu 100,000 wana sifa, system iweze kuwachakata tuone. System yenyewe iwa-terminate kulingana na system ilivyo. Hii itafanya tusindelee kuona kwamba Serikali ni bias. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, imani hiyo hiyo kwa Watanzania ambayo imejengeka kwamba nafasi ambazo zinatolewa, zinatolewa kwa kujuana; mwaka 2022 ulivyotupeleka sisi Jeshini, kuna nafasi za Watendaji zilitolewa kwenye Halmashauri yangu. Kule ambapo nafasi zilikuwa zimetangazwa kulikuwa na watoto wengi ambao wanajitolea kwenye Halmashauri ya Momba. Yule mtu aliyetoka Tume, cha kushangaza, sisi hakuna hata mtoto mmoja aliyetoka Momba. Sasa kwa sababu tumejenga imani ya kwamba nafasi hizi zinatolewa kwa madili na janja janja na mbambamba nyingi, hata mimi mwenyewe Mbunge naamini yule mtu aliyetoka kule Tume alikuja na majina yake mfukoni, ndiyo maana hakutaka kuwapa nafasi watoto ambao walitoka kwenye Halmashauri ya Momba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, halafu jambo hili liliteta uchungu kwenye Jimbo la Momba…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, jambo hili liliumiza sana wazazi wa Momba kwamba ilikuwaje kwamba watoto hawa ambao Halmashauri ilikuwa imewaamini, wanajitolea na wanakusanya mapato TAMISEMI, halafu leo walipoingia kuhojiwa, eti watoto wao hawakuwa na sifa. Ni kitu ambacho hakiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye misingi ya utawala bora inasema, lazima kuwe na usawa na ujumuishi. Sasa hiyo usawa na utawala bora ulikuwepo wapi ambapo sisi hatukufanyiwa usawa na hatukujumuishwa? Hivyo naomba, hata kwenye ajira hizi ambazo zimetolewa, watoto wote wa Kitanzania, misingi ya utawala bora ifuatwe wakati watakapokuwa wanapewa ajira. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: …bila ya kujali ni mtoto wa kigogo, bila ya kujali ni mtoto wa nani, tunatamani kuona hata watoto wa masikini na wakulima wakishika nafasi kubwa kwenye nchi hii kama ilivyo kwenye viongozi wetu wa zamani. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, naunga mkoni hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi. Nianze kabisa kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na jopo lake. Hatuna mashaka na weledi wao ndio maana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amewaamini.

Mheshimiwa Spika, leo nitaongelea mambo mawili katika bidhaa za makundi mawili tu, bidhaa ambazo zinaingizwa ndani ya nchi yetu. Tumekuwa na kasumba ambayo imekuwa siyo nzuri sana inapokuja kwenye kuingiza bidhaa nchini. Kila kitu kwa asilimia kubwa tunaingiza. Nikawaza itafika wakati tutaingiza mpaka dhambi.

Mheshimiwa Spika, cha kwanza, nitaongelea mambo mawili. Jambo la kwanza natamani kuongelea kuhusiana na mradi wa chumvi. Wabunge wenzangu wengi wameongea vizuri kuhusiana na chumvi, wamefafanua vizuri sana. Nimwombe Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha, nilipouliza swali la msingi hapa kuhusiana na Kiwanda cha Chumvi Itumbula sikujibiwa kikamilifu. Tunaamini kiwanda kile cha chumvi hakitawasaidia tu wananchi wa Jimbo la Momba kupandisha mapato kwenye halmashauri yetu, lakini ni kiwanda ambacho chumvi inayozalishwa pale inaweza kusaidia Mikoa yote ya Nyanda za Juu Kusini na ambapo Wabunge wengine wametangulia kusema hapa kwamba, tuna uhitaji mkubwa sana wa chumvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bidhaa nyingine ambayo nataka kuongelea hapa ni uingizwaji wa pombe nchini kwetu. Katika imani zetu hapa, Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hatuna dini, lakini wananchi sisi ndio tuna dini. Sasa najiuliza kama wananchi tuna dini na kila mtu kwa imani yake, wapo tunaoamini pombe ni dhambi na wengine wanaamini pombe ni haramu.

Mheshimiwa Spika, kwanza niseme mimi sio mtumiaji wa pombe, lakini sina sababu ya kutokutetea maslahi ya watu ambao wanatumia pombe na kama zipo nchini kwetu zinatumika.

Mheshimiwa Spika, mara ya mwisho nilipokuja hapa nikazitetea pombe zetu za kienyeji, sikupewa majibu mazuri na Serikali na Mheshimiwa Simbachawene akaahidi vizuri sana hapa kwamba atalifanyia kazi na Mheshimiwa Waziri ni huyu huyu na Naibu Waziri ni huyu huyu.

Mheshimiwa Spika, leo nimekuja na pombe zenye thamani kubwa sana hapa, nataka Mheshimiwa Waziri aniambie hizi pombe ziko hapa nchini zinafanya nini na hizi pombe kwa namna zinavyouzwa bei ghali. Hapa nimekuja na pombe mpaka ya 270,000. Hizi pombe nimeenda kuzinunua kwenye hoteli kubwa hapa Dodoma pale Morena kwa Shabiby, ambapo naamini watu ambao wanakwenda sehemu ile ni Mawaziri wenyewe, Makatibu Wakuu wa Wizara, labda na Wabunge wenyewe na wafanyabiashara wakubwa wakubwa. Sasa swali, kama Serikali haina dini na pombe ni dhambi hizi pombe zinafanya nini hapa nchini?

(Hapa Mhe. Condester M. Sichwale aliweka juu mezani chupa za pombe mbalimbali)

MHE. CONDESTER M. SICHWALE: Mheshimiwa Spika, kuna smirnoff, nisaidie kutoa mama, green fish wanywa pombe wanajua, sijui kuna Hennessy, kuna Jack Daniels, kuna hennessy nyingine, hii inaitwa Gordonson. Haya naomba hizi za Tanzania, hizi ndio za kwetu za Tanzania zinazozalishwa hapa K-Vant na Konyagi. Swali langu hizi zote nimenunua Morena kwa Mheshimiwa Shabiby, zinagharimu zaidi ya Sh.500,000 hapa zilipo. Swali najiuliza hizi pombe zinafanya nini? Tafsiri yake wapo watu ambao wanatumia hizi.

Mheshimiwa Spika, nataka niwaulize Watanzania wenzangu walioko huko nje na Wabunge walioko huku, ni nani ambaye mtoto wake akienda kufanya kazi kwenye Kiwanda cha TBL atakataa, atasema ni dhambi. Tufanye sasa hivi awe ni Mkurugenzi Mkuu wa Kiwanda cha TBL, nani atazungumzia masuala ya dhambi hapa? Nataka kujua ni Watanzania wangapi ambao watoto wao wanafanya kazi kwenye Kiwanda cha Konyagi? Ni Watanzania wangapi ambao watoto wao wanafanya kwenye Kiwanda cha K-Vant wangapi, hawapati hiyo mishahara?

Mheshimiwa Spika, sasa najiuliza kwa nini pombe zetu mfano wa pombe ya gongo zinamwagwa, vijana wenzangu wakimbiza Mwenge kule Mtwara walimwaga pombe za Watanzania wapika gongo. Kwa nini tunadharau ubunifu wa Watanzania? Kwa nini tunadharau mawazo ambayo ni ya Watanzania. Sasa najiuliza, kwani viwanda maana yake nini? Viwanda si huwa vinaanza na wazo, mtu akipata wazo si ndio atengeneze bidhaa kwa hali ya kawaida.

Mheshimiwa Spika, hao China wanaotuletea makorokoro feki humu nchini kwetu wanafanyaje? China kila mtu hata mtoto wa miaka 10 ana kiwanda chao wanatengeneza ma-product mabovu ndio wanatuletea huku kwenye nchi zetu.” [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Spika, sasa sisi kama yupo Mtanzania ambaye anaweza akapata wazo la kutengeneza gongo mpaka watu wakalewa, jamani si Mtanzania huyu alipaswa apewe support. Sasa Serikali ubunifu ambao inautaka inataka ubunifu upi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, angalia pombe hizi zote ambazo unaziona, siku moja Mheshimiwa Waziri Bashe akiwa anaongea huko kwenye viwanda vyake vya miwa huko, anapongeza namna ambavyo wanzalisha sukari. Akawa anasema namna ambavyo wanazalisha Molasses wanauza kwenye nchi za nje ambazo wao ndio wanatuzalishia hizi wanatuletea sisi tunakunywa. Molasses inatengenezwa kwetu halafu wanasafirisha kwenda nje sisi tunarudi tukaanze kunywa pombe. Imani zetu Serikali zinasema pombe ni dhambi…

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, sasa hii dhambi inafanya nini hapa nchini kwetu?

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, Kiwanda cha Mtibwa mwaka huu fedha…

SPIKA: Mheshimiwa Condester.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, walizalisha molasses tani…

SPIKA: Mheshimiwa Condester.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, muda hautoshi jamani.

TAARIFA

SPIKA: Subiri kidogo kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Aida Khenani.

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru napenda kumpa taarifa mzungumzaji kwamba pamoja na uzuri wa hizo chupa hizo bidhaa alizoziweka mezani, hata watumiaji wengi hawajui imetengenezwa na vitu, lakini hiyo aina ya pombe inayotengenezwa Tanzania, inafahamika kwamba material yake yanatoka shambani na yanatoka wapi. Kwa hiyo ni suala la Serikali kuongeza kuwapa motisha wanaotengeneza. Ahsante. (Makofi)

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, napokea taarifa ya Mheshimiwa Aida. Yeye Mheshimiwa Aida…

SPIKA: Mheshimiwa Sichalwe subiri kidogo inabidi uitwe ndio uanze kuzungumza. Mheshimiwa Sichalwe unapokea taarifa hiyo.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, napokea na wewe kule Ilolo, Mafyati kule Mabatini una wapiga kura wengi ambao mimi nawafahamu na nawajua wanatengeneza pombe za kienyeji. Kwa hiyo mimi na wewe tuna wapiga kura ambao wanatengeneza pombe za kienyeji. Bahati mbaya inawezekana hawatengenezi gongo lakini Kimpumu, Kindi, Komoni, Isute, zote hizo ni pombe za kienyeji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa najiuliza tunapohubiri ubunifu, ubunifu upi ambao sisi kwenye nchi yetu tunauhubiri. Kuna wachangiaji wamepita hapa aliongea Mheshimiwa Tauhida Gallos jana, akasema kuna vijana wa kitanzania ambao wanaweza kutengeneza system ambayo mtu akiwa mbali ikaweza kuzima umeme nyumbani kwake. Najiuliza hivi vijana hawa wa Kitanzania waweze kutumia akili yote hiyo kuja na utaalam wote huo washindwe kutenganisha kati ya methanol na ethanol kwenye gongo. Maana yake ambacho kinazuiliwa hapa kwenye matumizi ya gongo eti ni methanol ambayo sisi tulitegemea.

Mheshimiwa Spika, nimeenda zaidi, nimewasiliana na Profesa wa…

TAARIFA

SPIKA: Haya achilia hapo hapo kwenye kuwasiliana utaanzia hapo, Mheshimiwa Agnes Hokororo.

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nataka kumpa mzungumzaji taarifa kwamba wakati wakulima wa korosho wanalalamikia bei ndogo ya korosho ghafi, matunda ya korosho kwa maana ya mabibo yana uwezo wa kutengeneza pombe bora tena yenye virutubisho, lakini huo ubunifu haujatumika kulifanya hilo bibo litengeneze pombe bora, ambayo itatumika na Watanzania. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Sichalwe unaipokea taarifa hiyo.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, napokea.

Mheshimiwa Spika, nimewasiliana na Profesa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam najiuliza kwenye nchi yetu kuna chuo kinachoaminika kama Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Profesa Kessy pamoja na watalaam wenzake Maprofesa wengine huko sijui Profesa Muhinzi, Profesa Athuman, wanasema wameshafanya utafiti kwenye suala la gongo na pombe zingine za kienyeji. Hakuna madhara makubwa ya kiafya. Serikali inachokikatalia kwenye gongo ni methanol iliyopo kwenye gongo, lakini wanasema iko mitambo ambayo wala sio shida kutenganisha…

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: …methanol na ethanol kwenye gongo ili iweze kufaa…

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Sasa kama watu wanasema eti gongo yetu sisi ina matatizo kwa sababu haijatenganishwa. Kwa hiyo Jack Daniel anakunywa nani? Jack Daniel kwenye nchi hii anakunwa nani? tumezikuta pale Morena. Mwananchi wa kawaida mwenye kipato cha Sh.2,500 anaenda Morena pale? Maana yake wanakunywa matajiri wa nchi hii…

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, sasa gongo haifai, Watanzania tabia ya sisi kudharau vitu vya kwetu ndio hiyo sababu tuna-import mpaka dhambi. (Makofi)

SPIKA: Haya Mheshimiwa Sichalwe, subiri kidogo, Mheshimiwa Musukuma.

TAARIFA

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nampa taarifa mzungumzaji, Mbunge wa Momba, kwa uzoefu mimi natumia hivyo vitu, wala msicheke tupo wengi tu na wala sio dhambi. Natumia hivyo vitu alivyoweka mezani na watu wengi wanaovipinga wanavipinga hasa wanapokuwa makazini, lakini wanapostaafu baada ya miezi miwili, mitatu, wateja wakubwa wa hizo pombe ulizoziweka kushoto Konyagi na K-Vant ni Maprofesa na Madaktari na nina research niliyoifanya mwaka jana. (Kicheko)

SPIKA: Haya ahsante sana.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, napokea taarifa.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, ameshapewa taarifa tatu zinamtosha, tumwache amalize hoja yake, Mheshimiwa…

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, unipendelee na muda kidogo ni ombi tu kwa faida ya Watanzania.

SPIKA: Nakupa sasa nafasi ili utulie, uchangie vizuri hoja yako.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana mama.

SPIKA: Unaipokea kwanza taarifa ya Mheshimiwa Musukuma.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nimepokea, natetea na wapigakura wako wa Jimbo la Mbeya. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimeeleza Kiwanda cha Manyara Sugar wana-export molasses tani 1,500 katika mwaka huu wa bajeti tulionao. Sasa ombi langu kwa Serikali ni hili, mimi natoka kwenye familia ya watu wenye dini, sinywi pombe, mlokole mzuri tu, lakini hizi pombe hapa zinafanya nini?

Mheshimiwa Spika, zipo Serikali duniani ambazo zenyewe zimejipambanua kwamba ni Serikali za kidini, mfano Falme za Kiarabu, ni watu ambao hatushangai, wao wanasema Serikali yao inaamini dini, lakini nawauliza watu ambao wameenda kwenye state zote za kule Falme za Kiarabu, Sharjah, Abu dhabi, Dubai hakuna mtu hakuti hizi pombe?

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, Kuhusu Utaratibu.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, kila Serikali inaamini dini, lakini hizi pombe zipo kwenye hizo nchi.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, Kuhusu Utaratibu.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, sasa sisi kwa nini…

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, Kuhusu Utaratibu.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, sasa sisi kwa nini tunakataa utaratibu…

KUHUSU UTARATIBU

SPIKA: Mheshimiwa Sichalwe kuna kanuni inavunjwa, yuko wapi anayesema kuhusu utaratibu.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Hussein.

SPIKA: Kanuni inayovunjwa Mheshimiwa.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, kwa kanuni ya 75, kanuni ambayo imevunjwa, huwa tunapita pale kwenye security, ukiwa hata una chupa moja ya maji wanaizuia. Je, hili suala linaruhusiwa kuingiza vifaa kama hivi Bungeni?

SPIKA: Sasa kuhusu utaratibu inabidi kanuni iwe inavunjwa na yule anayehusika, kwa hivyo wewe unaliza kama amevunja kanuni au hajavunja kwa kukaa na hizo pombe hapo, ndio swali lako?

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, swali langu ni hilo kwamba je amevunja kanuni au la?

SPIKA: Ahsante sana. Amefuata utaratibu kuingiza pombe humu ndani, kwa hiyo hajavunja kanuni yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Condester Sichalwe.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, mimi sitaki kutenda dhambi, kushika tu pombe inawezekana ni dhambi. Baba yangu namheshimu sana, yale aliyofanya nyuma yanatosha, busara yangu na hekima yangu asiitumie vibaya, mimi ni mtoto mdogo namheshimu kama baba yangu mzazi. Mimi sio kichaa, yaani Spika na usomi wake wote huo halafu mimi nikurupuke kufanya hivi vitu.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Spika, niendelee kusema kwamba, nataka kusema nini? Nataka kusema tunapoongelea viwanda vinaanza na mawazo ya mtu wa chini, vinaanza na mtu wa kawaida, tuheshimu mawazo ambayo yanatolewa na Watanzania wenzetu, tuheshimu mawazo ambayo yanatolewa na watu wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hizi K-Vant na hizi Konyagi ni pombe za Watanzania. Sasa hivi Serikali ya South Africa itokee itangaze kwamba inatangaza ajira 100,000 kwa watu wakafanye kazi kwenye viwanda vya wine, Watanzania lukuki watamiminika kwenda pale.

Mheshimiwa Spika, tukienda huko duniani wine za South Africa ndio zinaheshimika wakati zabibu inalimwa hapa Dodoma na Dodoma wine inauzwa shilingi 10,000. Halafu Mheshimiwa Waziri wakati alikuwa anajaribu kuongelea sehemu ambazo wamepata masoko huko sijui mpaka pilipili, mbona alikuwa haongei kama K-Vant na yenyewe ni most selling pombe kwenye huko nchi za East African Community? Si ni bidhaa ya Watanzania. Kwa nini hawajivunii na hizi bidhaa, mbona hivi wanapitisha bandarini, TBS wao wanafanya kazi ya kupima hivi tu, ila TBS kwenda kukaa kushirikiana mawazo na watu wa chini kwamba huyu mtu asiyejua kusoma na kuandika anawezaje kutengeneza kindi, komoni, kimpumu watu wakalewa wanashindwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naona Serikali imeweka nguvu tu kwenye kukataza gongo. Ziko baadhi ya pombe nyingi sana pia za kienyeji kwenye jamii zetu zina madhara. Kwa mfano kule kwa Profesa Mkenda, kuna hii pombe moja huku inaitwa vimolari hivyo vimolari kule Rombo inasemekana vinauwa nguvu za kiume vya wanaume wetu huko Rombo. Sasa najiuliza hayo mawazo ndio yalibidi yachukuliwe, yaani kama iko pombe ambayo Mtanzania anaweza akapata wazo, akatengeneza mpaka zikauwa nguvu za kiume za mtu huyu, si ilitakiwa ndio hiyo pombe itumike kuwafanya hawa wanaume ambao wanawaingilia watu kinyume na maumbile ili wasiteseke, kwa sababu tayari ni maarifa hayo. Sasa wanataka maarifa gani?

Mheshimiwa Spika, hizi pombe kwa sababu zimetoka Ulaya na zimepewa majina mazuri sijui smirnoff sijui kitu gani, hiyo ndio heshima, lakini ujuzi wetu wa ndani unadharauliwa.

Mheshimiwa Spika, ifike muda…

SPIKA: Dakika moja malizia.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, ifike muda sisi tuache kasumba, kasumba hapa ndio inayotuponza, kasumba hapa ndio inatuletea shida. Kama soko la ndani linaonesha kuna wanywaji wa pombe wanatumia pombe. Niombe Serikali iwatumie vijana wa Kitanzania, Maprofesa na wasomi ambao wanasema wapo tayari kufanya research, kumsaidia mwananchi wa kawaida kuboresha pombe yake. Zile pombe ambazo zinakaa siku tatu hazina kazi tena haziwezi kupakiwa. Nilishakuja na vipombe vidogovidogo hapa vya Sh.3,000, tumsaidie mwananchi huyu aweze ku-pack, viweze kuuzwa kwenye nchi zetu za Jirani. Huko ndio kuinua uchumi. Tunapoongelea uchumi wa viwanda inabidi uanze na mtu mmoja mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mama Samia peke yake na matajiri hawa wachache, hawawezi wakajenga hii nchi, nchi hii itajengwa na Watanzania wenyewe kwa kuzingatia shughuli zao za kawaida ambazo wanafanya. Ni nani huko kijijini ukiacha kulima na kufuga biashara ambazo wananchi wa kawaida wanafanya ni nini, si ni pombe za kienyeji?

Mheshimiwa Spika, ninayo orodha ya Maprofesa wakubwa hapa nchini hapa, wakubwa wengine mpaka ni aibu kutaja, ukitaja watu watabaki wameshika mdomo, ambao wamesoma kwa kutumia pombe za kienyeji ukiacha gongo. Pia hizo gongo wanakunywa, tabia ya kujifanya watu ni watakatifu, wakati watenda dhambi kama watu wengine wapo hapa, kuwajaji watu ni wa kwanza, lakini laiti Mungu angeleta karatasi zao hapa, tukafunua dhambi zao, watu wangeweza kukimbia na wasingeamini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri leo aje aseme ana mkakati gani. Kama hawataki pombe, ushauri wangu basi tuseme Tanzania ni nchi ambayo haihitaji pombe ili tujue moja. Hakuna pombe nchini kwetu na pombe za kienyeji zisithaminiwe na gongo ndipo ziendelee kuitwa haramu, lakini kama pombe zitaendelea kuingia, ni lazima tutambue ubunifu wa watanzania wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii. Kwanza kabisa nianze kuipongeza Serikali yetu na kuishukuru kwamba tunashukuru kwa kutusaidia kutujengea soko la Kimataifa la mifugo na mazao ambalo lipo pale Kakozi ambalo lipo mpakani kabisa kati ya nchi ya Tanzania na Zambia ni kilometa moja tu kutoka Tanzania kuingia Zambia. Soko hili liligharimu karibu, Serikali iliidhinisha pesa karibu bilioni 8.645 na mpaka sasa hivi tumepewa kiasi cha pesa bilioni 3.09. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe kwa kusema hivi kutokana kuwepo kwa soko hili la mifugo na mazao pale ni soko kubwa sana ambalo ninaamini kwamba Serikali wakati inaidhinisha kiwango hiki cha pesa na kutafuta mpango huu mzuri kwamba soko likajengwe pale ni mahsusi kabisa walizingatia kwamba ni kwa sababu tupo mpakani ina maana kwamba tutawahudumia Watanzania wa mikoa yote lakini pamoja na nchi zote ambazo zinatupaka kwenye lile eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa basi, ombi langu kwa Serikali, iko sababu kubwa sana Wizara hii iweze kufika kwenye lile soko ambapo tunaendelea na ujenzi japokuwa tunashukuru limeshakamilika kwa kiasi fulani na tumeshaanza kufanyia kazi. Ifike ili tuweze kushauriana muweze kuona miundombinu namna gani tumejipanga katika kuboresha kwenye hilo eneo la ufugaji na eneo lingine ambalo litakuwa linahusu Wizara ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo kwa kuwa soko hili ni kubwa kwa kiwango hiki, naiomba Serikali ipo haja na sababu ambayo tunaweza tutakapoweka kiwanda cha kusindika nyama mahali pale inaweza ikatunufaisha sana. Itatunufaisha sana kwa sababu karibu mikoa yote ya Katavi, Rukwa na mikoa mingine iliyoko karibu nasi ya Nyanda za Juu Kusini na mikoa mingine itaenda kwenda kutumia soko hili kwa sababu kua mnada kabisa wa kisasa ambao unatarajiwa kujengwa mahali pale, machinjio ya kisasa kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wasiwasi wangu tunaweza, wakati tutakuwa tunafanya shughuli hizi za ufugaji tukawa tunawanufaisha wenzetu wa nchi za jirani. Sasa twende kuongeza thamani kwenye haya mazao ambayo yatatokana na ufugaji. Kwa hiyo, tukipata kiwanda cha kusindika nyama mahali pale, kuna soko kubwa sana la nyama kwenye nchi ya Kongo, Zambia na nchi zote ambazo ziko kwenye zile nchi za SADC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo liko andiko ambalo nimeziandikia baadhi ya Wizara hapa kuona kwamba kama tuko mpakani na soko lile liko pale mpakani kuna hati hati ya kwamba chochote tutakachokuwa tunazalisha pale kinaweza kikawa kinaenda nchi ya Zambia kinyume na utaratibu. Kwa hiyo, nimeiandikia andiko Wizara ya Fedha, Kilimo, Viwanda na Biashara, Uwekezaji, Mifugo yenyewe na Wizara ya Ulinzi na Usalama kwamba ninaiomba Serikali yangu Sikivu wkae wajadiliane waone kuna umuhimu wa sisi kutupatia geti pale ili tuweze kulinda mapato yote ambayo hayatapaswa kutoka pale kwa sababu soko litakapoanza kufanya vizuri na muingiliano wa watu utakuwa mwingi. Kwa sababu kuna njia zaidi ya 10 ambazo zinaizunguka lile soko ambazo zinatoka pale sokoni kuingia nchi ya Zambia na wakati mwingine huwa tuanzitumia hizo njia kupita ambapo wakati mwingine inakuwa ni kipindi cha Masika, barabara hazipitiki. Kwa hiyo, sitatamani kuona tunaenda kuzinufaisha nchi za wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie kwa kuwasemea watu wa Momba kwenye suala la mifugo. Kwenye sensa ambayo ilikuwa imefanyika mwaka 2012 tulionekana tulikuwa na ng’ombe 128,218, mbuzi 78,522, kondoo 10,071 na kuku 155,233 na kwa ajili ya muda pamoja na mifugo mingine. Kwa miaka ya karibuni ambayo imeongezeka sasa tumeonekana kuwa na ongezeko la mifugo hii karibu mara tano kwa sababu tumepokea wenzetu wengi wa Jamii ya wafugaji, Wasukuma na Wamaasai ambao wamekuwepo maeneo yale. Sasa, kutokana na ongezeko hilo, kumeonekana uhitaji mkubwa sana wa kuhitaji malambo pamoja na majosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na lambo ambalo lilikuwa limeanza kujengwa kwenye Kata ya Mkomba ambapo Shirika hili la Debit kwenye mwaka 2016/2017 liliweza kutupatia kiwango cha pesa milioni 150 ambapo lambo hili lilikuwa linapaswa kukamilika kwa thamani ya milioni 800. Ombi langu kwa Serikali, kama mnaweza kufika, kupitia na kuliona lambo hili ili tuweze kuwasaidia wafugaji hawa wasiendelee kunung’unika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo yapo baadhi ya malambo ambayo yalikuwa yanatumika, lakini hayana ubora na yanahitaji kurekebishwa kwa sababu ongezeko la wafugaji limekuwa kubwa mara tano kama ambavyo nimesema. Naomba ukarabati wa malambo yafauatayo; lambo ambalo liko Kata ya Ivuna, Mkomba, Mpapa, Chitete, Msangano. Pia ombi langu kwamba kama tunaweza tukapata majosho kwenye Tarafa ya Ndalambo ambayo pia kwenye Bonde la Mto wa Kasinde pamoja na Tesa kuna ongezeko kubwa sana la watu hawa ambao ni wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo kwenye suala la ufugaji tunaomba kuboreshewa vifaa vya uimarishaji ili kwa ajili ya kuboresha koo za mifugo ambazo ziko pale. Hii imeonekana ni changamoto lakini na vifaa vya hawa Maafisa Mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la uvuvi naomba niende tu moja kwa moja niziongelee changamoto ambazo zinawapata wavuvi ambao wako ndani ya Jiji la Momba. Wavuvi ambao wako ndani ya Jimbo la Momba wanaomba jambo moja kama sio matatu au manne. Tunaomba tupate engine za boti kwa sababu mpaka sasa tunaendelea kuvua kwa kutumia uvuvi wa kienyeji kwa kutumia tu mitumbwi. Kwa hiyo, tukipata engine hizi tutaweza kutengeneza maboti ambayo angalau yanaweza yakawa ni ya kisasa.

Mheshimiwea Mwenyekiti, pia tunaomba kupata mikopo kwa wavuvi. Pia tunaomba kupata soko zuri ambalo liweze kutusaidia kuweza kukusanya mapato ndani ya halmashauri pia kukusanya mapato kwenye Serikali Kuu. Kwa sababu, pamoja na kwamba tunavua kienyeji, tunaweza kuvua kuanzia tani 7,000 mpaka tani 100,000 na pamoja na kuvua huku, tunalitosheleza soko la Mbeya Mjini, Tunduma, Vwawa na Mlowo. Kwa hiyo, tutakapokuwa tumepata hivi vifaa tunaweza kuzalisha tani kubwa na kwa wingi lakini pia tutaongeza mapato ndani ya halmashauri yetu pamoja na mapato kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakuskuru kwa kunipatia nafsi. Kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Profesa Mkenda pamoja na timu yake, lakini pili ninaipongeza Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi ambayo inaongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia kwa namna ambavyo ameendelea kuboresha miundombinu kwenye elimu yetu hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, naomba niwapongeze walimu wote nchini kwa ngazi mbalimbali, kuanzia kindergarten, shule za msingi, sekondari mpaka vyuo vikuu. Hatuwezi kusema wala kujivuna wasomi tulioko Tanzania hii bila kuwashukuru na kuwaheshimu walimu wetu, hata wale ambao wamestaafu kwa namna ambavyo walijitolea kuhakikisha tunaelimishwa.

Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa naomba nitumie nafasi hii kuwapongeza na kuwashukuru walimu ambao wako ndani ya Jimbo la Momba. Kwa nini ninawapongeza walimu waliopo ndani ya Jimbo la Momba? Jimbo la Momba tuna vijiji 72 na vitongoji 302; yako baadhi ya maeneo hatuna zahanati kwenye baadhi ya vijiji lakini walimu hawa wameendelea kufanya kazi kwa kujituma na kujitoa pamoja hata kama hakuna huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, yapo maeneo ambayo kuna changamoto ya miundombinu ya barabara na kuna wakati mvua zikianza kunyesha njia haziwezi kupitika walimu wanaweza wakakaa zaidi ya miezi mitatu hawajaenda mjini, lakini walimu hawa wameendelea kufanya kazi kwa kujituma na kwa kujitoa.

Mheshimiwa Spika, ndani ya Jimbo la Momba vijiji 50 havina maji safi na salama lakini walimu hawa wameendelea kushirikiana kunywa maji na mifugo lakini wakiendelea kufundisha watoto wetu ndani ya jimbo la momba, wakiendelea kujitoa na kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, ndani ya Jimbo la Momba kuna maeneo hakuna umeme lakini walimu hawa wameendelea kujituma, yamkini wanaendelea kutumia vibatari mafuta ya taa na sola; kwa namna yoyote ile lakini wameendelea kuwa wazlendo kujitoa ndani ya jimbo la momba.

Mheshimiwa Spika, ombi langu nikuombe Profesa Mkenda, tutakapomaliza Bunge la Bajeti twende tukawatembelee walimu wa Jimbo la Momba, wanashida nyingi ambazo wanatamani mwalimu mwenzao uweze kujua. Kwa walimu wote wa Jimbo la Momba na wengine wote walioko vijijini ambao wanapitia changamoto lakini wanafundisha watoto kwa kujituma ninawapongeza wakiongozwa na DC wa wilaya yangu ambaye pia ni mwalimu.

Mheshimiwa Spika, ombi jingine, kwa kuwa sisi watu wa Momba tunalima kufuga na kuvuna, tunaomba tupate chuo ambacho kitafanana na shughuli zetu ambazo tunazifanya ili watoto wa Jimbo la Momba watakapotaka kusoma whether wajifunze kulima katika ubora unaotakiwa kuvua katika ubora unaotakiwa na kufuga katika ubora unaotakiwa.

Mheshimiwa Spika, ombi lingine; Mkoa wa Songwe hatuna Chuo Kikuu chochote ambacho kinatoa digrii. Tunayo kampasi ya Dar es salaam Institute of Technology, ina mazingira mazuri na maeneo makubwa. Tunaomba kuanzia pale muwape hadhi waanze kutoa degree tupate chuo kikuu ndani ya Mkoa wa Songwe tukitumia Dar es salaam Institute of Technology.

Mheshimiwa Spika, ombi lingine, tunayo shule ya sekondari Songwe Girls ambayo tunasema ni shule ya mkoa; shule hii haina tofauti na shule ya kata, na mwanzilishi wa shule hii alikuwa ni Mheshimiwa Dkt. Samia Hassan Suluhu. Tunaomba tumpe heshima Mheshimiwa wetu kwa kuiwekea miundombinu bora shule ile ili watoto waendelee kupata elimu ndani ya Mkoa wa Songwe.

Mheshimiwa Spika, sina mashaka na ufanisi wa Wizara ya Mheshimiwa Mkenda, anafanya vizuri sana, anasimamia vizuri sana sera ambazo zimewekwa kwa utaratibu kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, mimi nataka kushauri mambo kadhaa. Inawezekana hata sasa hivi tunavyotaka kubadirisha elimu ni kweli tuko sahihi lakini kwa nini tunaona kumekuwa na uhitaji mkubwa sana wa kubadilisha mitaala yetu?

Mheshimiwa Spika, niseme kwamba teknolojia tuliyonayo ndiyo inatusukuma kutuvuta kutupeleka hapo. Serikali haina makosa yoyote kuona kwamba kuna baadhi ya ajira zinaondoka kwa vijana kwa sababu ya kuongezeka kwa teknolojia, lakini Serikali itakuja kufanya makosa kama haitataka ku-adopt hizi teknolojia kuziwekea mpangilio mzuri kwenye nchi yetu ili wananchi na Watanzania wasione kwamba artificial intelligent imechukua ajira zao bali tuione kwamba artificial intelligent tuitumie kama fursa ya kuhakikisha vijana wa Kitanzania wanapata ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nikawa na wazo, nikaona Wizara ya Profesa Mkenda inaitwa Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia, Wizara ya Mheshimiwa Nape inaitwa Wizara ya Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari.

Mheshimiwa Spika, Profesa Mkenda huyu kwenye Wizara yake a-deal na mitihani ya darasa la nne, darasa la saba, form two, form four wapi, bado wanafunzi hawajagoma, bado hatujaomba tubadilishiwe elimu, bado Walimu hawajataka kuboreshewa mazingira yao; mambo kede kede kwenye Wizara hii. Ni wakati gani Profesa Mkenda atakuwa anahangaika na timu yake kujua kuna emerging technologies ambazo ziko duniani zinaweza zikawasaidia watanzania kujiajiri?

Mheshimiwa Spika, lakini ukiangalia Wizara ya Mheshimiwa Nape, Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari a-deal na wandishi wa Habari mikonge ya Habari, kule Momba kuna watu hawapati mawasiliano yote haya ni ya kwake saa ngapi tena atakumbuka na teknolojia ya Habari? teknolojia zinakuja kila wakati. Ushauri wangu kwa Serikali nilikuwa naomba yafuatayo;

Mheshimiwa Spika, kama itawapendeza, kama mtaona inafaa tupate Wizara mpya ya Teknolojia peke yake. Kipengele cha Mheshimiwa Profesa Mkenda kibaki Wizara ya Elimu na Sayansi, Teknolojia iondoke, kwenye Wizara ya Mheshimiwa Nape ibaki Wizara ya Habari na Mawasiliano, Teknolojia iondoke tupate Wizara ya Teknolojia. Ndani ya hiyo Wizara ya Teknolojia kuwe kuna taasisi zake. Kuwepo na taasisi ambayo itasimamia old technology kwa sababu bado ziko taasisi hapa nchini kwetu tunatumia teknolojia za kizamani. Pia iwepo taasisi ambayo itasimamia current technology ambayo tunatumia sasa hivi muda huu lakini kuwepo na taasisi ambayo itasimamia emerging technology na future technology ili Wizara hii ndio iweze kusambaza ujuzi mbalimbali kwenye Wizara ya Elimu, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Mifugo, Wizara ya Uvuvi na vitu mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa najiuliza, mfano leo mimi nimwalike Elon Musk aje hapa Tanzania nitampeleka kwenye Wizara ipi akapeleke ujuzi wake kwa ajili ya kujadiliana na Serikali yangu? Tunashindwa kujua, atakwenda kwa Mheshimiwa Mkenda kwa sababu ana teknolojia au ataenda kwa Mheshimiwa Nape kwa sababu ana teknolojia ya Habari?

Mheshimiwa Spika, tunaomba Serikali ichukulie teknolojia kama ni jambo la muhimu. Matajiri wote ambao tunawaongelea sasa hivi, mfano sasa hivi tunapomuongelea huyo Elon Musk ambaye anayo kampuni ya Spacex ambayo imefanya mambo makubwa kwa ajili ya kwenda huko angani, ni mwanateknolojia, ni mtu ambaye alizaliwa tu hapo Pretoria, South Africa, sasa hivi anaonekana ni mtu mashuhuri sana duniani. Aliununua mtandano wa twitter kwa zaidi ya dola za Kimarekani bilioni 44 kwa ajili ya teknolojia tu. Tukimwangalia mtu kama Mark Zuckerberg, wote hao waliwekeza kwenye teknolojia, tukimwangalia mtu kama Bill Gates, wote hawa ni matajiri ambao walitokana na teknolojia.

Mheshimiwa Spika, tunabadilisha mtaala hii, ni kweli, lakini ninaona baada ya miaka kumi bado tutarudi hapa kuona kwamba bado mitaala yetu tuliyobadilisha haifanani. Ninasema hivyo kwa sababu gani, hatuwezi kushindana na teknolojia, tutakuwa tunajidanganya kushindana na teknolojia ni kama kushindana na muda.

Mheshimiwa Spika, ni kwa sababu naongea katika hali ya Kibunge, lakini nilitamani ningewaonyesha pia watu kwamba teknolojia hii namna ambavyo inashabihiana zaidi hata na mambo ya kiroho. Wanaosoma vizuri Biblia wataelewa vizuri sana vita ya Urusi na Ukraine nini kinaendelea. Sasa hivi benki zinavyofungwa ni mambo ambayo kwenye Biblia yameandikwa. Sasa sisi kwa nini tusiendane na huo wakati?

Mheshimiwa Spika, vijana wa Kitanzania wanaona hakuna ajira kabisa lakini kama tukiamua kutumia artificial intelligent in a positive way tunaweza tukapata ajira nyingi zadi ya ajira ambazo zilikuwa zimeandikwa kwenye ilani ya Chama Cha Mapinduzi. Tunaweza tukapitiliza.

Mheshimiwa Spika, vijana wa Kitanzania wamekosa platform, wamekosa sera namna ya kuja kuonesha ujuzi wao. Wako vijana huko nje ni mahiri, ni wataalamu, wapeni nafasi, wapeni room, wajue wakija wata-fit kwenye taasisi ipi, wata- fit kwenye taasisi ya teknolojia ya zamani teknolojia ya sasa au teknolojia inayokuja? Vijana wa Kitanzania muwape nafasi waweze kutengeneza hata stimulation za teknolojia ambazo tunazitarajia. Zipo teknolojia za blockchain hatujazikumbatia, zinatoa ajira nyingi sana huko duniani. Sasa hivi kuna wakati unaweza ukaona benki zinabisha, hawataki kupokea digital currency. Mimi nataka uwaambia hivi wanajidanganya, watashindana na ukuta. Huko tunakoenda na majira yaliyopo na benki ambazo zinafungwa huko duniani, na kwa namna hali ilivyo tupende tusipende tunakuja na currency moja duniani; na tumeshaanza kuona wachumi wa dunia ambavyo Dola ya Marekani imeshaanza kuteteleka. Kwa hiyo niiombe Serikali…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika moja, malizia Mheshimiwa.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, hatua ya kumalizia ni kumuomba Profesa Mkenda atakapokuwa pia anahitimisha kwenye hitimisho lake aseme kidogo ni namna gani ambavyo ametumia artificial intelligent kutengeneza ajira nyingi ambazo ziko kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ukiacha hizi ajira ambazo vijana wa kitanzania tunagawana…

SPIKA: Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, niishukuru Serikali ya Chama Cha Mapinduzi inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mambo yote ambayo amefanya kwenye Wizara hii lakini pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri pamoja na timu nzima kwa ujumla kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya. Niipongeze na kuishukuru Serikali kwa baadhi ya minara ambayo tumepata ndani ya Jimbo la Momba kwenye Kata za Chululumo, Msangano, Nzoka na sehemu zingine. Tunaomba kueneelea kuboreshewa minara kwenye Kata za Kapelle, Tungwa, Mkomba lakini pamoja na Kata ya Chitete ikiwa ni sambamba na kuhakikisha mnatuchepushia Mkongo wa Taifa kufika makao makuu Chetete.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naomba kidogo niku-challenge Mheshimiwa Waziri in very positive way. Kwenye zile ajira ambazo ziko kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi wewe ndiye mtu kwenye Wizara hii umebeba ajira nyingi sana za vijana kama ukiamua tu ukiamua kutumia teknolojia in very positive way.

Mheshimiwa Naibu Spika, Juzi wakati nachangia kwenye Wizara ya Profesa Mkenda ambaye Wizara yake ni Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia lakini Wizara yako ni Wizara ya Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari tukaomba tungepata Wizara mpya ya Teknolojia ili tuweze kuendana na karne ya 21 ili tuweze kuendana na Fourth Industrial Revolution Mapinduzi ya Nne ya Viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna namna tunaweza tukakwepa jambo hili ndiko wakati unakotupeleka lakini nishukuru sana Chama changu cha Mapinduzi nataka kurejea; kwenye ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi kwenye sura ya nne ambayo inasema sayansi na teknolojia na ubunifu kwenye ukurasa wa 154.

Ilani yetu ambayo tuliinadi, inasema hivi “Chama cha Mapinduzi kinatambua kuwa uchumi wa kidijitali ni muhimu katika kuleta maendeleo kwa kuongeza ufanisi katika uzalishaji na utekelezaji wa shughuli mbalimbali na kutoa fursa za kuongeza vipato kwa wananchi na Taifa kwa ujumla. Uchumi huo umeonekana kuwa eneo muhimu katika kuchangia kukuza uchumi nchini kama ilivyofanyika katika nchi zingine za kipato cha kati. Aidha, uchumi wa kidijitali unalandana na mapinduzi ya nne ya viwanda yaani maana yake fourth industrial revolution yanayokuja na ambayo hayaepukiki. Hivyo basi, CCM itaendelea kusimamia Serikali kuhakikisha kuwa teknolojia mpya za kidijitali zinatumika kuongeza ufanisi katika sekta za uzalishaji na kuepuka madhara yanayoweza kutokea. Katika kipindi cha miaka mitano ijayo Chama cha Mapinduzi kinaelekeza yafuatayo: -”

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mambo manne, lakini naomba niende kwenye jambo moja la muhimu. Kuimarisha kituo cha utafiti hapa Mheshimiwa Waziri amekwama; kuimarisha kituo cha utafiti, ubunifu na uendelezaji wa TEHAMA ikiwemo kujenga uwezo wa kuongeza matumizi ya teknolojia mpya za kidijitali na artificial intelligence.

Mheshimiwa Naibu Spika, yuko msanii wa Mheshimiwa Waziri pale Diamond, muulize ameshapeleka kazi zake kwenye NFT, bado. Vyote hivyo ni vitu vya muhimu. Ni msanii wetu ilibidi tulinde kazi zake NFT kazi zake ziende hapo ambapo kazi zake zisije kupata huko madhara. Block chain technology kwa research ndogo ambayo nimefanya hapa kwetu Tanzania kwa mambo madogo ambayo nimefuatilia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano unamuuliza mtu unajua nini kuhusiana na block chain technology, unajua nini kuhusiana na digital currencies, unajua nini kuhusiana na crypto currencies. Mtu anakuuliza kwa hiyo Mheshimiwa nikitaka kujiunga kwenye Bitcoin nafanyaje? Yaani swali hili does not make sense, yaani ni sawa mtu ananiuliza kwamba Mheshimiwa Mbunge najiungaje kwenye T-shilling? Yaani mtu anajiungaje kwenye T-shilling yaani Tanzania shilling hela yetu mtu anajiungaje? Digital currencies, block chain technology ni teknolojia kubwa sana ambayo Chama Cha Mapinduzi kwenye Ilani yetu imesema, tuboreshe Kitengo cha Utafiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipindi akiwa kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Ndugulile kwenye Wizara hii, nilishawahi kumfuata sana kuhusiana na mambo ya PayPal kila wakati nilikuwa nachangia. Akaniambia tunaendelea kufuatilia dada, tunafuatilia tunaongea na watu wa BOT. Siku moja nikamwona tena kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Ndugulile amekuja hapa anauliza mambo ya PayPal. Sasa nikashangaa huyu tena kaka yangu alikuwa ni Waziri, sasa tena amekuja kuuliza. Kwa hiyo unaweza ukaona utafiti huo Mheshimiwa Waziri angekua ametusaidia, amekaa vizuri na watu wa BOT. Tunatamani kuona teknolojia tunazozipata zisiende tofauti na kazi zetu ambazo tunazifanya na taratibu ambazo tumejiwekea kwenye nchi yetu, lakini tayari kama kungekuwa na utafiti tungejua namna ya ku-accept PayPal kama ni njia ya kulipa na kulipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi huko nje watu wetu hapa Tanzania wanalipa kwa PayPa,l hela zao zinapitia Kenya zinaishia huko, why not us? Yaani nini ambacho Kenya wanatuzidi ambacho sisi hatuna ambacho hatuwezi ku-adapt, nini ambacho South Africans they have sisi hatuwezi ku-adapt tukawa nacho.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu muda ni mdogo nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, block chain technology si teknolojia ya kuidharau, ni teknolojia ambayo ina mawanda mapana. Huko ndani kuna watu wa mambo ya sheria, mambo ya smart contract, huko ndani kuna mambo ya watu ambayo yanahusiana na mambo ya ardhi kuna vitu vingi. Huko ndani kuna mambo ya NFT ambayo ni mambo ya wasanii kwa ujumla na hata waigizaji wetu, yaani viko vitu vingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Mheshimiwa Waziri kiamua tu kuikumbatia block chain technology vizuri kwa lengo zuri, bila kuathiri mila na desturi zetu. Ndio namwambia Mheshimiwa Waziri inaweza ikawa ni Wizara ya mfano ambayo itatoa ajira nyingi sana ambayo imeandikwa kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi. Wapo maprofesa kadhaa kwenye nchi hii ambao wameandika maandiko kuhusiana na block chain technology. Kwa nini tusimwombe akae nao, lengo tunataka jamii ijue, mara nyingi wananchi wamechukulia hivi. Kwa mfano kuna siku moja kuna mtu akawa ananiuliza block chain technology ni nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, nikaona anafananisha, ni kama mtu umwambie mtoto mdogo unataka kuwa mwanasiasa? Aseme hapana, mimi sitaki, mambo ya kutukanana kwenye mikutano, mimi sitaki kuwa mwanasiasa, lakini siasa sio hivyo, siasa ndio tuko hapa sisi Wabunge tumekutana. Sisi ni wanasiasa, kwenye siasa ndiyo tunampata Mheshimiwa Rasi, kwenye siasa ndio tunampata Spika wa Bunge, kwenye siasa ndio tunampata Mheshimiwa Zungu, kwenye siasa ndio tunapata Baraza la Mawaziri, kwenye siasa hapa ndani tulipo Bunge ndio tunapitisha bajeti, ndio tunatunga sheria, ndio tunatetea mambo ya wananchi. Kwa hiyo yule mtu ameingolea siasa kwenye ka-negativity kadogo yaani tone yaani drop of water kwenye bahari, ndio ameongelea siasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mtu anaposema Bitcoin ni wizi, sijui ni pyramid yaani ni kama mtu aseme mimi sitaki internet kwa sababu wanaonyesha pornography. Si sawa, internet inafanya vitu vingapi? Hayo ni madhara madogo ambayo yanatokana na kuwepo kwa internet. Kwa kuwepo kwa block chain technology, ni teknolojia ambayo lazima itaambatana na challenges nyingi tu ambazo hatuwezi kuziepuka, lakini unapoongelea block chain technology na vitu viliko ndani yake ni jambo kubwa, ni jitu kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri aende basi hata kukaa na timu yake, apitie hata vitu vichache tu mambo ya coin market, yaani aingie tu hata kwenye ile website, coin market cup. Aangalie pale, zile currencies zote, hivi kweli watu wote wale wanaweza wakawa ni wajinga wamekaa. Mheshimiwa Waziri atamani hata kumfahamu who is Santos Nakamoto. Huko tunapoenda Biblia yenyewe imeandika hakuna namna tutakavyokwepa kuja na one currency. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiko huko tunakoenda hakuna namna benki zitakwepa hilo jambo ndiko tunakoenda. Kizazi chetu ndio hiki hiki Waziri anavyotuona, miaka 20 ijayo ndio tutapata Rais hapo, ndio tutapata Waziri Mkuu hapo ndio tutapata viongozi wakubwa hapo. Kwa hiyo, hiki tunachokishauri muda huu hatutamani kupitwa. Hebu aangalie sasa hivi tulivyopokea internet, angalia internet ambavyo inatusumbua. Tulichelewa kutunga sheria ambazo zitafanana na wakati tulionao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna watu kwenye mitandao ya kijamii wanaweza wakamtukana hata Mheshimiwa Rais, hatujawahi kuona hata mahali wanashtakiwa kwamba walimtukana na wapo, wana challenge. Tunaona watu wanatukana viongozi mbalimbali matusi mengine makubwa. Tunaona watu wanaandika vitu vya ajabu, wanaposti vitu vya ajabu ambavyo viko nje na utaratibu na mila na desturi zetu, lakini hatuna sheria ambazo zinawabana kwa sababu tuliacha internet ikatutangulia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: …kuliko sisi. Kwa hiyo nimwomba Mheshimiwa Waziri aboreshe utafiti kama ambavyo Ilani ya Chama Cha Mapinduzi inasema na kama itawapendeza kama Serikali…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa malizia sekunde, ahsante sana muda wako umekwisha.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa fursa na mimi kwanza nianze kwa kupongeza wasilisho kutoka kwa Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara. Na mimi naomba kutoa mchango wangu katika maeneo matatu kama muda utakuwa rafiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya kwanza kabisa nataka kutoa mchango wangu kwa kuishauri Serikali ni kwa namna gani iweze kutusaidia wananchi wa Tanzania kuendesha biashara zake, lakini kwa kuangalia na kasi halisi ya teknolojia ambayo iko duniani ili iweze kutusaidia kuendana na mataifa mengine na kukimbizana sawasawa na wenzetu ambavyo wanakimbizana huko kwenye mataifa ambayo yameendelea ambayo yanatumia teknolojia katika kufanya vizuri kwenye biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili ni kuomba ni kwa namna gani Serikali inaweza kuwekeza nguvu kubwa kwenye maeneo ya mipaka maana kuna fursa nyingi sana ikiwa ni pamoja na kufungua viwanda kwenye maeneo ya mipaka, lakini pia hata kuboresha mazingira mazuri ya biashara kwa sababu panapatikana ajira nyingi, kuanzia vijana, wazee, watu waliosoma na ambao hawajasoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na eneo la tatu, nitataka kuchangia na kuishauri Serikali kwamba vijijini akina mama wengi wameonekana ndio ambao wanatengeneza pombe za kienyeji na pombe hizi za kienyeji kwa kule vijijini zimeonekana zikipendwa sana. Basi kwa nini Serikali isitafute namna nzuri ya kuwasaidia akina mama hawa kuboresha ujuzi wao ili itusaidie kutoku-import pombe nyingi kutoka mataifa ya nje, tutumie ujuzi wa akina mama hawa ili kuendelea kutengeneza pombe zetu hapahapa kwa watu ambao ni watumiaji wa pombe waendelee kutumia vitu vyetu halisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye teknolojia za biashara ambazo ziko duniani, naomba kuanza na namna gani ambavyo toka dunia ilivyokuwa imeanza kuna mifumo mbalimbali ambayo ilikuwepo ya biashara. Mfumo wa kwanza wa biashara uliokuwepo ni mfumo wa barter trade. Barter trade ilikuwa inafanyika katika mfumo kwamba kulikuwa hakuna means of exchange, kwa hiyo, biashara zilikuwa zinafanyika kwa kubadilishana bidhaa na bidhaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini baada ya hapo, mfumo huo ulikuja ukapita baada ya dunia kuendelea tukaja kwenye metal au coin ambapo vito au dhahabu vilitumika kama means of exchange. Baada ya hapo dunia ikaondoka tukaingia kwenye paper (cash) ch currency, maana yake hapa tunaangalia Tanzanian Shilling, Kenyan Shilling, Zambian Kwacha, Nigerian Naira, Pula na pesa mbalimbali kutoka kwenye mataifa mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo tunaendelea tuko kwenye huu mfumo, lakini tukaja kwenye mfumo mwingine ambao tunaita credit card ambao hata sasa hivi bado tunatumia, kwamba watu hawataki kubebeshana pesa nyingi, lakini mtu unapokuwa na kadi unaweza ukafanya transaction mahali popote pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo wa nne uliofuata ambao sasa dunia ipo na ndipo mahali ambapo dunia inatengeneza pesa nyingi sana, ndipo mahali ambapo hata matajiri wengi ambao wamepata kutokea katika kipindi cha miaka 15, ninapowaongelea Bill Gates, Alibaba, wametokana na mfumo huu wa teknolojia ambao umegawanyika katika phases mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa naongelea fourth industrial revolution ambayo ndani yake kuna block chain technology. Kwenye block chain technology kuna teknolojia nyingi; watu wa sheria wanaweza wakaitumia block chain technology, watu wa ardhi wanaweza wakaitumia block chain technology, lakini hapa nataka niongelee kwenye mambo ya fedha namna gani block chain technology inatumika, na zaidi ya hapo nataka kuongelea kwenye digital currency.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kwenye digital currency, hii ni teknolojia ambayo ni kubwa sana lakini kwa bahati mbaya tafsiri ambazo tunazipata sanasana kwenye Nchi kama Tanzania na nyingine za Afrika, tunashindwa kuitafsiri vizuri teknolojia hii. Na hakuna namna tunaweza tukaizuia teknolojia hii isije kufanya kazi, na tayari huko duniani kuna watu ambao wametokea matajiri wengi sana kwa kupitia block chain technology ambayo ndani kuna digital currency.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kwenye digital currency nataka kuziongelea baadhi ya currencies. Mfano naziongelea bitcoin, ethereum, theta, bitcoin cash, litecoin na ripple, na zipo coin mbalimbali. Lakini hapa nataka kuiongelea zaidi coin ya bitcoin. Coin hii mpaka sasa Tanzania hatufahamu kwa upana namna bitcoin inavyofanya kazi, na Watanzania wengi wamekuwa wakiendelea kupoteza fedha zao kwa sababu wanadanganywa, hawajui. Lakini kama Serikali ingekuwa imeamua kulivalia njuga jambo hili wakaamua kuwekeza kwenye elimu kuna vijana wengi wa Kitanzania ambao wanaulewa mkubwa na wimbi kubwa sana la vijana ambao wapo wengine wanafanya na wanatengeneza hela, lakini pia Serikali inapoteza mapato yake kwa kiasi kikubwa sana kupitia hili eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano leo nikiongelea, jana bei ya bitcoin ilikuwa milioni 92 za Kitanzania, nachukulia mfano mtu kwa mfano South Africa kuna ATM ya bitcoin, Kenya kuna ATM ya bitcoin lakini sasa hivi tuchukulie mtu anatuma hela kutoka South Africa anamtumia Mtanzania aliopo hapa, hakuna namna yoyote ambayo BOT wanafuatilia transactions hizi kwa sababu mambo yote yanafanyika online, mambo yote yanafanyika kwenye internet.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hata ilipotokea wakati ambapo Serikali iliamua kuzifunga zile bureau nyingi ambazo zilikuwa zipo Arusha na sehemu zingine, bureau nyingi ziliamua kuhamia kwenye online kwa mfano Serikali haijui kuna kitu kinaitwa remitano, Serikali haijui local bitcoin, Serikali haijui kuna kitu kinaitwa e-wallet huko kwote Watanzania wapo ambao wanatengeneza hela na wanatengeneza hela wakati mwingine naweza kusema hata hela zinaingia nchini kinyume na taratibu kwa sababu hakuna connection kati ya teknolojia, Serikali na taasisi za fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ombi langu kwa sababu ya ku-serve muda, Serikali tuamue kujifunza hata kwa nchi za wenzetu, tunaweza kujiuliza South Africa wanafanyaje mpaka wana ATM ya bitcoin, Kenya wanafanyaje mpaka wana ATM ya bitcoin? Kwa nini wanaweka zile ATM, wananufaika na nini.

MWENYEKITI: Malizia sentensi yako ya mwisho.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa hiyo kwa kumalizia ni kwamba tunaiomba Serikali iwekeze sana mahali hapa kwa sababu wimbi kubwa la vijana ambao wanatumia teknolojia wanaweza wakapata ajira kwa kupitia mahali hapa na Watanzania wengi wasiendelee kupotoshwa na kuibiwa kama ambavyo lilikuja hata wimbi la D9 watu wengi wakaibiwa ni kwa sababu Serikali ilikuwa haijaweka mikono yake namna gani ikusanye mapato na namna gani iwalinde Watanzania hawa. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi. Kwanza nianze kusema tunaipongeza sana Serikali kwa vile ambavyo wameandaa bajeti yao kwa kuzingatia maoni mengi ya Wabunge na wamewatendea haki kwa sababu kazi za Mbunge ni pamoja na kuishauri Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie fursa hii kumshukuru na kumpongeza sana mama kwa namna ambavyo anaendelea kusikiliza na kupokea michango ya vijana wa Tanzania. Tarehe 22 mwezi wa Tano nilisimama kwenye Bunge hili Tukufu na kuchangia kuhusiana na mambo ya blockchain technology, cryptocurrency na digital currency na tarehe 13 mwezi huu mama aliweza kutoa kauli na kuwaomba BOT waweze kuendelea kufuatilia teknolojia hii kujifunza ili nasi tusiweze kupitwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, wito huu wa mama umepelekea kufanya aingie kwenye orodha ya marais wachache ambao wameonyesha kuongea kitu kikubwa sana duniani na kuunga teknolojia mpya ambayo inaweza ikaleta uchumi mkubwa lakini kuongeza ajira kwa vijana lakini na kuchochea uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ajili ya kufupisha muda naomba niendelee kuiomba Serikali na kuishauri kwamba, BOT whether taasisi zozote za kifedha kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha na Mipango, watakapokuwa wanaunda Kamati zao tunaomba ushirikishi kwa vijana wa Kitanzania ambao wanauelewa ili waweze kuwasaidia, lakini elimu iendelee kutolewa kwa sababu elimu ni bure itawafanya Watanzania hawa waweze kuelewa na wasiendelee kudanganywa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hilo naomba, wakati tunaendela kusubiri BOT waendelee kuamua na kujifunza kwamba uko mfumo ambao unatumika kwenye hizi online business, unaitwa PayPal. Ikiwa kama BOT imekubali kwamba Watanzania hawa waweze kulipa kwa kutumia PayPal, lakini wao hawawezi kupokea malipo kwa kutumia PayPal, tunaomba basi BOT tena waone namna gani watawasaidia hawa vijana wa Kitanzania ambao wanalazimika kutoa hela nje ya nchi, lakini wao hawawezi kupokea na wanalazimika kutumia nchi za jirani kulipwa na hivyo kupoteza mapato yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe ushauri wangu mwingine kwa Serikali kuhusiana na teknolojia ya miundombinu. Hapa nataka kuongelea nanofiber technology, kwa ajili ya muda nitafupisha tu, kwamba, teknolojia hii ina faida nyingi sana na ina faida nyingi sana especially kwa barabara ambazo zinatusumbua vijijini sisi Wabunge ambao tunatokea vijijini. Hata hivyo, teknolojia hii inaweza ikatumika hata mjini nanofiber technology wataalam wanasema kwanza ina PSI 11,000, kwa hiyo ina maana kwamba ina uwezo wa kuhimili kiwango ambacho lami haiwezi kuhimili.

Mheshimiwa Naibu Spika, lami jua linapowaka magari makubwa yanapopita inatengeneza vitu kama mbonyeo. Kwa hiyo inapelekea Serikali kupoteza hela nyingi inapokuwa ina-maintain zile barabara, lakini nanofiber technology, Serikali itakapoamua kuitumia inaendana na mazingira yote hata kwenye zile mbuga zetu za wanyama ambako hatuwezi kuweka lami kwa sababu tunaogopa teknolojia ambayo tunatumia sasa ina emission, lakini teknolojia hii iko vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii nanofiber technology ina uwezo wa ku-save gharama ambazo zinatumika kujengea lami za sasa kuanzia asilimia 25 mpaka asilimia 50. Kwa hiyo unaweza ukaona ni kwa kiasi gani Serikali itakapoamua kutumia teknolojia inaweza ika-save mapato yake, sitaweza kuendelea nitaandika andiko kwa ajili ya muda ili niseme vitu vingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine naomba kuchangia kwenye suala la miradi hii ya kimkakati na nifupishe. Kwenye hii miradi ya kimkakati naomba niongelee mradi wa kimkakati ambao uko ndani ya Jimbo la Mwomba mradi wa chumvi. Kwenye soko letu la Tanzania inaonyesha kwamba kiwango cha chumvi ambacho Tanzania inahitaji ni tani milioni moja na laki tatu na kuendelea, lakini viwanda vyetu vya ndani kwa mfano Uvinza; viwanda vilivyoko Pwani au viwanda viliko huko Lindi vina uwezo wa kutengeneza tani za chumvi 270,000 tu. Kwa hiyo Serikali inapelekea Serikali kuangiza chumvi nyingi kutoka Nchi za Kenya na zingine ili tuweze kutosheleza soko la ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu kwa Serikali ikiwa miradi hii ya kimkakati tuliileta kwa lengo tu kwamba iweze kuzisaidia halmashauri kuongeza mapato yake, lakini iweze kutoa ajira kwa Watanzania na tuweze kuimarisha viwanda vyetu vya ndani, tunaomba Serikali irudi na kupitia tena kuangalia miradi hii ya kimkakati ikiwa ni pamoja na hiki Kiwanda cha Chumvi ambacho kipo Ivuna kwenye Jimbo la Momba. Wakati kiwanda hiki kinaendeshwa na TRC kilikuwa na uwezo wa kuzalisha tani mpaka 25,000, lakini toka kiwanda hiki kimerudi kwenye mradi wa kimkakati kinazalisha chini ya tani 100. Kwa hiyo tunaomba Serikali ipitie tena ili tuweze kunufaika na miradi hii ya kimkakati, iweze kwenda kutimiza lengo ambalo lilikusudiwa kwa Watanzania hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi. Niseme kwanza naunga mkono hoja za Kamati zote mbili ambazo zimewasilishwa kwenye Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu kwa nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia kwa namna ambavyo ametupatia pesa nyingi kwenye Majimbo yetu na wananchi wamenufaika, wanashukuru sana. Pamoja na pongezi hizo naomba nami nitoe mchango wangu kwenye maeneo mawili kama siyo matatu kama muda utakuwa rafiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwanza kabisa nataka kuongelea kuhusiana na TASAF. Kwenye majimbo ambayo ni ya kijijini haifanyi vizuri sana kama ambavyo Serikali ina picha halisi. Wanufaika wengi wa TASAF kule Vijijini kiukweli siyo wale ambao walipaswa waingie kwenye Mfuko wa TASAF. Watu wengi ambao ni wazee na wengine ni walemavu hawana hata uwezo wa kukopeshwa kwenye ile asilimia mbili yao ambayo inapatika asilimia kumi kwenye Halmashauri wameachwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine niwaombe sana Viongozi wa Serikali, Mawaziri pamoja na Naibu Mawaziri wakubali tufanye ziara za kushtukiza twende kule ili wajionee uhalisia namna gani ambavyo wananchi wanalalamika. Tumeona wakati mwingine wakitembelea kwenye maeneo yetu wanapata ule msururu wanazongwazongwa hawapati picha halisi. Wakati mwingine wanapewa taarifa ambazo siyo sahihi kulingana na uhalisia ambao upo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TASAF wananchi wengi ambao wanapaswa kunufaika ambao kweli hawapati mlo na wengine hawawezi kujiendeleza kabisa hawajapata na wengine ambao ni watendaji hawafiki kwenye yale maeneo ili kuchukua takwimu halisi, wanawaachia Wenyeviti wa Vijiji, wanawaachia Wenyeviti wa Mitaa na wengine pia ni binadamu wanaingia kwenye tamaa wanawaingiza ndugu zao ilihali hawakuwa wanufaika na TASAF.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia kwenye TASAF, sehemu nyingine nyingi ambazo tumeona kwenye TASAF, ile miradi ya maendeleo ambayo imeubuliwa imeisaidia jamii kwa ujumla hata ambao hawakupaswa kunufaika na TASAF. Zipo baadhi ya halmashauri za vijijini watalaam wake hawana utalaam wa namna gani ya kuandaa haya maandiko ili wayalete TASAF Makao Makuu waweze kunufaika na miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ni kuhusiana na TARURA. Nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu tena kwa namna ambavyo alimpatia kila Mbunge wa Jimbo bilioni 1.5 ili ziweze kwenda kumsaidia kwenye miundombinu. Kwa upande wangu kwenye Jimbo langu tumeanza kuona mwanga kutoka kwenye bilioni 1.5 hii. Ombi langu na ushauri kwa Serikali, wakati natoa ombi nisisahau kumpongeza Chief wa TARURA Injinia Seif kwa kweli amekuwa ni mtu mwema sana anawasaidia Wabunge wengi na nimesikia watu wengine wakimsemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la TARURA tunaiomba Serikali kupitia Wizara yenye dhamana wawapunguzie TARURA mambo mengi wanapokuwa wamepata hela, kuwawekea vitu vingi mara sijui zabuni, vitu gani, inafika wakati wanaanza kutekeleza miradi hii wakati mvua zimekuja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano sasa hivi kuna mafuriko, mkandarasi ameanza kulima barabara mwezi wa Pili, tarehe Mosi, leo tunavyoongea tarehe 14 Februari, barabara zote zimekwishasombwa na maji. Kwa hiyo, tunaomba pesa zinapotoka immediately watu wa TARURA waanze kufanya kazi mapema iwezekanavyo ili wafanye kipindi ambacho ni cha kiangazi, itatusaidia barabara zile zinapopitiwa na magari, zinapopitiwa na watu zinajishindilia lakini sasa hivi barabara zinaanza kutengenezwa mwezi wa Kumi na Mbili unapowauliza ni corrugations nyingi ambapo taratibu nyingi zinafanya hata zile pesa ambazo tumepewa na Mheshimiwa Rais zimepoteza thamani yake kwa sababu pale walipolima maji yamechukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia, tunashukuru Serikali kwa kutujengea madarasa mengi lakini pia na watoto wakapata madawati. Walimu walisahaulika kwenye eneo hili, Walimu hawajapata fenicha, wamepata ofisi lakini hawana mahali pa kukaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusiana na upungufu wa Walimu kwenye madarasa ambayo tumeyapata, naiomba Serikali, kama Serikali Kuu imekubali kwamba itawalipa Madiwani posho zao, tunaomba zile halmashauri ambazo hazina uwezo kwa sababu sisi wengine tunatoka kwenye halmashauri ambazo hazina uwezo, kwa hiyo hawataweza kuwaajiri watoto wao kupitia mapato yao ya ndani, tuombe hii iwe replaced na Madiwani kama watapata posho kutoka Serikali Kuu, kile ambacho walikuwa wanapata Madiwani basi wale vijana wenzetu ambao wako mtaani wamekaa zaidi ya miaka minne hadi mitano na watoto wamekaa bila kusoma basi tunawaomba vija hao wakachukue hizo nafasi hata wakilipwa shilingi laki nne ninaamini zitawasaidia sana. Ahsante sana. (Makofi)
Hoja ya Dharura kuhusu Mikopo ya Elimu ya Juu Nchini
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi nami niweze kuunga hoja iliyopo mezani. Wakati naanza kuchangia mchango wangu naomba nirejee maneno ya Baba wa Taifa, Taifa la Afrika ya Kusini, ambaye ameshawahi kusema hapo, “Education is a most powerful weapon which, you can use to change the world.” Akimaanisha kwamba, elimu ndio silaha peke yake ambayo unaweza ukaitumia kuibadilisha dunia. Kwa muktadha wake huu ni nini?

Mheshimiwa Spika, sisi pia Watanzania pamoja na vizazi vyetu na hawa watoto ambao tunatarajia kuwasomesha, tunatarajia ya kwamba elimu ndio silaha mojawapo ambayo wao wanaweza wakaitumia kuibadilisha jamii yetu, lakini pia kuwa washindani kwenye soko la dunia huko tuliko. Tukiangalia hapa kwenye takwimu za sensa ambazo tumepewa jana pale na Mheshimiwa Rais, Milioni 61 ya Watanzania na hiyo Laki Saba, ukiangalia kwa uhalisia utagundua idadi kubwa ya Watanzania ni Watanzania ambao wana kipato cha kawaida kabisa. Maana yake asilimia kubwa ni wakulima, asilimia kubwa wanafanya shughuli ndogondogo kwa ajili ya kuendesha maisha yao ikiwa ni pamoja na kusomesha watoto wao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ikiwa Watanzania hawa ni wa kawaida kabisa ambapo mtoto huyu hapati mkopo kabisa wa Chuo Kikuu, anapata mkopo chini ya kiwango au anaenda inafika hatua ameshadahiliwa kuanza masomo mpaka sasa hivi vyuo vimefunguliwa ni wiki ya pili, watoto bado hawajapata mikopo. Unajiuliza mzazi huyu ambae alikuwa akimsomesha mtoto wake kwa kuungaunga kwenye shule hizi za Kata kwa maisha magumu, sasa hivi ni wiki ya pili, mtoto labda amechaguliwa Dar-es-Salaam anatoka Mwanza Vijijini, mtoto amechaguliwa kwenda kusoma vyuo vilivyoko Mwanza ametoka huko Momba Vijijini, amefika na nini? Atalipia malazi nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wamemtaka atoe hela ya udahili ili aanze masomo. Mtoto huyu ambae Serikali imefuta ada kutoka O-Level mpaka sasa hivi A-Level, mzazi anapata wapi hela ya kumsaidia mtoto huyu kumdahili? Ada ni zaidi ya Milioni Mbili, mzazi ni mkulima wa kawaida ambaye analima magunia mawili au anachoma mahindi barabarani, anafanya usafi Mama ni house girl, Baba anaranda, anapata wapi ameachwa kwenye mkopo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninao ushauri katika jambo hili. Kwanza tunaomba Bodi ya Mikopo (HESLB) ivunjwe na ipitiwe tena. Ipo haja ya HESLB inapaswa kuchunguzwa kwanza, yapo malalamishi mengi sana ambayo wanufaika wa mikopo huko nyuma bado wanayalalamikia.

Mheshimiwa Spika, kupitia Bunge hili Tukufu naomba niseme wazi ninaishukuru sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi, mimi ni mnufaika ambaye nilikopeshwa mkopo na kupitia Bunge hili mwezi wa Kumi uliopita nimemaliza mkopo wangu. Kwa hiyo, tafsiri yake kile changu ambacho mimi Serikali iliniwezesha, mtoto wa mkulima wa kawaida kutoka Momba, nikasoma na niko hapa na inawezekana isingekuwa mkopo ningekuwa nimeshaolewa saa hizi nina wajukuu hata Wanne kwa hiyo, tafsiri yake inawezekana hata watoto wengine sasa hivi wakikosa mkopo wataingia kwenye mazingira magumu, wataendelea kuteseka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, HESLB ivunjwe, ichunguzwe, ipitiwe upya tena, lakini yale marejesho ambayo watu wengine ambao wanarejesha wanaonekana wanabambikiziwa yapitiwe tena pia, tuweze kuangalia Je, yale marejesho yanayorejeshwa hayawezi kuwasaidia watoto wapya ambao wanaingia? Je, hiki kiwango ambacho tulikipitisha hapa Bungeni hakiwasaidii watoto wapya ambao wanatakiwa kunufaika na mkopo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu mwingine ni kuwa, wako watoto wengi ambao wanafika chuo mwaka wa pili na wa tatu, wanashindwa kufanya mitihani yao kwa kukosa ada. Ninaomba Wizara ifungue dirisha, Wabunge tukiwaletea watoto hawa na sisi wakati mwingine ni binadamu, tunasaidia misiba, tunasaidia wagonjwa, inafika wakati tunashindwa. Mtoto yuko mwaka wa tatu, ameshindwa kufanya mtihani, ameomba mkopo zaidi ya mara tatu ameshindwa, mwaka wa tatu mtoto anaacha masomo?

Mheshimiwa Spika, tu-assume labda wewe mwaka wa tatu ungeachishwa masomo sasa hivi tungekuwa hatuna Spika hapo ulipokaa. Mwaka wa tatu ungeachishwa masomo tungekuwa hatuna Waziri Mkuu hapa ndani. Tunawaomba Bodi ya Mikopo mfungue dirisha, mtoto anapokuwa mwaka wa tatu ameshindwa kufanya mtihani wake kwa ajili ya kukosa ada laki nne, laki tano, tunaomba jamani watoto hawa muwape nafasi waweze kumaliza mitihani yao, waweze kufanya mitihani waende wakahangaike huko barabarani. Tuje hapa tujadili mambo mengine kwamba ajira ni changamoto, lakini kama tunasema education is the best weapon in the world, let us give them the weapon, acha tuwape silaha wakapambane huko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunawaomba sana watoto wasiache kufanya mitihani eti kwa sababu amekosa Laki Tano, amekosa Laki Sita. Hata sisi ni Wabunge wakati mwingine tunashindwa, siwezi mtoto afanye…

SPIKA: Ahsante sana dakika zako zimeisha Mheshimiwa.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
Naunga mkono hoja iliyoko mezani.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii adhimu ili nami niweze kuchangia. Kwanza kabisa, nitakuwa sijaitendea haki nafsi yangu kama sitampongeza na kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Nchi hii Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan. Tuseme ukweli, mama wa watu; mnyonge mnyongeni, lakini haki yake mpeni, anajitahidi. Ombi langu tu kwa wale ambao amewaamini, wasiendelee kumwangusha, wamsaidie ili aweze kutimiza kusudi lake la kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia mambo mawili tu, kwa kuwa muda siyo rafiki. Jambo la kwanza kabisa, nataka kuwaongelea wananchi wa nchi hii, wale ambao ni wa kawaida, wanyonge, masikini, wakulima na wote ambao wanafanya shughuli zao ndogo ndogo, wanazalisha mambo ambayo yako ndani ya nchi yetu, ni pamoja pia na wafugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wa nchi hii wanajitahidi sana na wanajituma sana katika kuzalisha mazao yao ambayo Mwenyezi Mungu amewasaidia wazalishe, na wengine wanatumia mpaka jembe la mkono katika kuzalisha, lakini ambacho nakiona, tunapaswa tuwekeze nguvu kubwa sana kwenye masoko. Kwenye uchumi wanasema, demand inapokuwa high, supply ikawa low au constant inapelelea price kuwa high. Tafsiri yake ni nini? Kama supply itakuwa constant au itakuwa low, demand ikawa high, maana yake wananchi hawa chochote watakachokuwa wanakizalisha kwa sababu wanazalisha katika supply hiyo hiyo, lakini demand inapokuwa kubwa kwenye masoko, itakuwa inaleta motisha ya wao kuendelea kuzalisha sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mapendekezo ya mpango, nimesoma ukurasa wa 125 ambao unasema kuhusu huduma za biashara na masoko. Waziri wa Fedha na Mipango anasema, kuimarisha miundo mbinu ya masoko, lakini kipengele cha pili anasema, kuimarisha mfumo wa kilimo cha mikataba na upatikanaji wa mikopo ya kilimo yenye riba nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi kipo kipengele ambacho kinazisisitiza balozi zetu kuhakikisha zinatutafutia masoko huko nje. Je, balozi zetu zimesimamaje kuhakikisha zinawatafutia wakulima wa nchi hii masoko ya kutosha ili hata kama supply yetu itakuwa limited, demand iwe high ili wananchi hawa waendelee kupata kwa kiwango kikubwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia zipo baadhi ya balozi ambazo tukiwasiliananazo, wanasema changamoto kubwa ambayo wanaipata ni wakulima wetu kushindwa ku-supply kuanzia mwezi wa Kwanza mpaka wa Kumi na Mbili (continuously). Wanashindwa kwa sababu gani? Wanazalisha kwa kiwango cha chini. Kama wanazalisha kwa kiwango cha chini, tafsiri yake ni nini? Hawajawezeshwa. Hapa tunaposema kwenye mikopo yenye riba nafuu, ndipo tunaposema Benki ya Kilimo ihusike na pia Wizara ambazo zimepewa dhamana kwa ajili ya kuziomba benki ambazo zinaweza zikatoa mikopo ya riba nafuu iweze kuwasaidia wakulima wa nchi hii pamoja na wafugaji ambao pia watataka kuwezeshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nataka kusoma kidogo kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri kwenye ukurasa wa 15(xv) kinachoongelea miradi ya maji. Mheshimiwa Waziri anasema hivi, “hadi kufikia Juni, 2022 miradi ya maji kwa vijijini ilifikia asilimia 74.5 ukilinganisha na mwaka ya nyuma Juni, 2021 ilikuwa ni asilimia 72.3; na mijini asilimia 86.5 mwaka wa nyuma asilimia 86.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilivyosoma hapa kwa kweli asilimia 74 ya miradi ya maji ambayo anasema hivi: “kuboresha upatikanaji wa huduma ya maji ambapo hadi kufikia Juni, 2022 imefikia wastani wa asilimia 74 kutoka mwaka wa nyuma asilimia 72.3.” Tafsiri yake nini? Maana yake ukitembea katika vijiji 100, vijiji 70 vina huduma ya maji. Nilipoona hii ripoti nikajiuliza, kwa hiyo, ni sisi Momba tu ndio tumesahaulika ama! Nikaanza kuuliza baadhi ya Wabunge wenzangu ambao na wenyewe wanatoka kwenye majimbo ya vijijini kama jimbo langu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeuliza Wabunge zaidi ya 20 hapa, hakuna Mbunge hata mmoja ambaye ameniambia yeye kwenye jimbo lake amefikisha hata asilimia 50 ya upatikanaji wa maji. Swali langu, sisi tunajenga nyumba moja, tuko hapa kuwatumikia Watanzania, hata Mama Samia sera yake anasema anataka kumtua mwanamke ndoo kichwani, nia yake ni ya dhati na nzuri zaidi kwa ajili ya kutaka kuwasaidia akina mama wa nchi hii pamoja watu wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhalisia huu siyo wa kweli. Nitolee tu mfano wa jimbo langu, mimi nina vijiji 72. Katika vijiji 72, yaani leo nimeona niwasiliane na Madiwani wote waseme; katika vijiji 72 ziko baadhi ya Kata hazina mradi wa maji kabisa. Sasa nikajiuliza, hiyo asilimia 74 inatoka wapi? Wako pia Wabunge wengine hizo asilimia hazijafika? Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwenye ukurasa wa saba…

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, ni mchango mzuri sana wa Mheshimiwa Mbunge, nataka kumpa tu taarifa hayo anayoyasema ni ya kweli kabisa kwamba takwimu hizo zinashangaza na mimi kama Mbunge ninayetokea Dar es salaam upande wa Jimbo la Kibamba, maji ni changamoto, katika kata nyingi hakuna, kwa hiyo ni mchango mzuri na ni kweli kabisa anachokisema. (Makofi)

MWENYEKITI: Nyie wa Dar es Salaam huwa mkisimama na mkaungana na wa vijijini kuna muda hatuwaelewi sana. Hivi na nyie wa Dar es Salaam mna changamoto kweli kama za Momba? (Makofi)

Mheshimiwa malizia sekunde 30.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Katika vijiji 72 ni vijiji 16 tu ambavyo vina maji na vijiji 56 havina maji. Sasa najiuliza hii takwimu inatoka wapi? Sisi tunajenga nyumba moja, tuwatendee Watanzania haki. Tulienda kuomba kura kwa kutumia ilani hii na kwenye ilani hii ukurasa wa saba, samahani kidogo tu nisome mama yangu. Katika miongoni mwa vitu ambavyo ni vipaumbele ambavyo sisi tulipewa ilani tukanadi kama Wabunge wa Chama cha Mapinduzi inasema hivi; “Kuongeza kasi ya usambazaji wa maji safi na salama ili kutosheleza mahitaji kwa zaidi ya 85% vijijini na zaidi ya 95% mijini.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naamini kwa sababu wanaona tumeshafika mwaka wa pili na ilani inasema 85%, wameamua waseme 74% hii ili ionekane wametekeleza, hapana sio kweli. Kupitia Bunge hili, namwomba Mheshimiwa Aweso, nataka nikafanye naye ziara kwenye jimbo langu, vijiji 10 ili kweli na vyombo vya habari vimchukue nione kama kweli atakuja na hiyo takwimu ya 76%, kwamba kweli kuna maji. Hapana sio kweli. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi hii na naunga mkono hoja iliyopo mezani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nianze kwa kuishukuru Serikali yetu ya Chama Cha Mapinduzi ambayo inaongozwa na Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Pia nitumie nafasi hii kuwaomba Watanzania wote tuendelee kumwombea Mheshimiwa Rais wetu ili Mungu amwezeshe kumpa maono, maarifa, busara na hekima ili ajue namna bora na ambayo inastahili katika kuwaongoza Watanzania. Kwa sababu kama Mwenyezi Mungu anaweza kutupa fumbo tusiweze kuijua kesho yetu tunapolala, ni imani yangu Mwenyezi Mungu naweza kumsaidia kumpa maono yaliyo matakatifu na maono mazuri Mheshimiwa Rais ya namna ya kuwaongoza Watanzania kuwafikisha pale wanapopataka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nishukuru kwa ajili ya hatua ya kwanza ya ujenzi wa hospitali yetu ya wilaya lakini Kituo cha Afya Msangano pamoja na KLituo cha Afya cha Nkulu. Naomba nijielekeze kwenye hoja yangu ya leo, kutoa changamoto zangu ambazo zinawakumba wananchi wa Jimbo la Momba, kupitia Bunge lako Tukufu naomba niseme kwamba huduma ya afya kwa wananchi wa Jimbo la Momba kiukweli hairidhishi na ni hafifu.

Mheshimiwa Spika, tuna changamoto nyingi sana ambazo zinatukumba ndani ya Jimbo la Momba. Cha kwanza ni upungufu wa dawa kwenye zahanati zetu na kwenye vituo vya afya. Ukiangalia hatuna hospitali ya wilaya lakini hata Hospitali ya Mkoa ambayo tunaitegemea labda tunaweza tukaitumia kwa ajili ya rufaa iweze kutusaidia, bado pia ina changamoto.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ni vifaa tib ana vile vile ukosefu wa watumishi, watumishi kuwa wachache, imepelekea hata mtumishi anapopata likizo yake ambayo ni stahili yake, analazimika kufunga zahanati ili aende kwenye likizo yake na wananchi wanakosa huduma na wakati mwingine inaleta ugomvi na wananchi kuona kwamba walistahili kuendelea kuhudumiwa, lakini mtumishi hayupo ili hali huyu mtumishi ilikuwa ni haki yake kwenda likizo.

Mheshimiwa Spika, pia changamoto hizi ambazo zimeendelea kutupata zimepelekea hata wakati mwingine kuwepo na mchafuko kuzidi kwa imani za kishirikina kwenye jamii zetu, kwa sababu wananchi wanapokosa dawa kwenye zahanati kwenye kituo cha afya na ukiangalia sisi wengine majimbo yetu ni ya vijijini mtu atoke Siliwiti, Mkomba kuja kufuata huduma kwenye Kituo cha Afya cha Kamsamba, pikipiki tu inabidi atumie Sh.40,000.

Mheshimiwa Spika, mwananchi kutoka Kamsamba kwenda Vwawa inabidi atumie nauli zaidi ya Sh.15,000 na wakati mwingine ni kipindi cha mvua barabara hazipitiki. Kwa hiyo kutokana na kwamba mwananchi anaona suala la afya halina mbadala anaona atumie njia yoyote ile kwa ajili ya kutafuta afya. Ninao mfano mzuri wa Katibu wetu wa Chama Cha Mapinduzi, alipata ajali pamoja na Mwenezi mwaka jana mwezi Mei, wakavunjika miguu mara mbili, lakini kutokana na kwamba kwenye Kituo cha Afya cha Kamsamba hakuna hata x-ray ambayo angeweza kupimwa kuona inabidi apate huduma ipi akalazimika kwenda kwa waganga wa jadi na mpaka sasa hivi Katibu huyu hajapona. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa swali kama huyu tu ndio kiongozi ambaye wananchi wanamwona, kwa hiyo unaweza ukaona namna gani ambavyo kutokuwepo na vifaa tiba na dawa kwenye zahanati zetu na kwenye vituo vyetu vya afya, vinawafanya wananchi waendelee kutafuta njia nyingine mbadala ya kutafuta afya zao. Ombi langu kwa Serikali, tunaomba sana zahanati zetu ambazo zipo katika Jimbo la Momba, zipate dawa za kutosha, vifaa tiba tuweze kuvipata, whether tutapata kutoka kwenye Wizara ya Afya au Wizara Afya wataongea na TAMISEMI vyovyote vile itakavyokuwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni matumaini yangu kwamba, wananchi wa Jimbo la Momba watapata afya stahiki ili tuweze kupambana, kuendelea kujenga Jimbo letu. Pamoja na kukosekana dawa pamoja na vifaa tiba kwenye zahanati zetu na vituo vya afya, bado hata kwenye Hospitali yetu ya Mkoa wa Songwe ambayo ndio tunaitegemea kama hospitali ya rufaa kwa ajili ya kutusaidia, huduma zipo lakini haziwezi kufanyika kwa ufanisi kama inavyotakiwa, hakuna vifaa tiba kwenye suala la mifupa, hakuna Madaktari Bingwa wa watoto, hakuna Daktari Bingwa wa upasuaji, hakuna Madaktari Bingwa wa magonjwa ya ndani, hakuna Wauguzi wa kutosha, lakini hata vifaa ambavyo vinabidi viwasaidie watu ambao wana changamoto ya mifupa hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye zahanati zetu unaweza ukakuta mgonjwa anakwenda hakuna hata kipimo cha kumpima BP imepelekea wananchi hawa wanapata BP mpaka wana-paralyze, wazee wako wengi kule kila wakati kushinda kwa waganga wa jadi wakifikiri wamelogwa, lambalamba wanatusumbua kila wakati kwa sababu kila mtu anasema huyu kaniloga, huyu kaniloga, lakini kama dawa zingekuwepo za kutosha, watumishi wapo wa kutosha, wakawahudumia wananchi hawa inavyotakiwa sidhani kama kuna mtu yeyote angeenda kutafuta njia mbadala huko mahali pengine ambapo hapafai. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa watu wa Wizara ya Afya, kipo kitengo kwenye Wizara ya Afya ambacho kinawatambua hawa watu wa Tiba Asili. Tunawaomba wale watu walioko kule ambao wanatoa hizi tiba asili Mheshimiwa Waziri, watoe wito wa namna ya kuwasajili ili tuwajue ambao Serikali imewaona ndio wanafaa, wanatambulika na watu na NIMR ambao wao wanafanya utafiti kwamba hizi tiba asili ndizo zinafaa, huko mitaani ni ugomvi kila mtu kaniloga, kila mtu kaniloga, watu wanauwana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi ni nani atajua huyu kaniloga halafu nimwache, umeona, mtu anajua fulani kamloga na yeye anaona mimi siwezi kumloga anaenda kumkata mapanga usiku. Kwa hiyo kutokana na huduma mbovu za afya ambazo zipo kwenye jamii zetu zinafanya hivyo vitendo viendee kushamiri, lakini huduma za afya zikiboreshwa na zikiwa nzuri, mtu akaenda hospitali amevunjika mguu, akapata huduma, sidhani kama atawaza kwenda kumtafuta mganga wa jadi, mganga wa jadi atakuwa wa nini? Unaweza Mbunge ukaenda kufanya mkutano wa hadhara, lambalamba akapata wafuasi kuliko hata wewe kiongozi ambaye unaenda kuwaambia mambo mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lambalamba amejaza watu kwa sababu gani? Kwa sababu anatoa matunguli, wewe hapo unaumwa mguu kwa sababu huyu alikuloga, wewe hapa ulivunjika mguu hauponi kwa sababu hivi. Sasa huyu ataponaje wala hata hajapimwa, usikute hata mfupa umeoza. Sasa hivi kwenye Hospitali yetu ya Mkoa wa Songwe tunaye mwananchi ambaye amekaa zaidi ya miezi sita, alivunjika mguu ameenda kwa waganga wa jadi, amekaa huko hajapona, mfupa sasa hivi unaoza, lakini kungekuwa na x-ray kwenye vituo vyetu vya afyam akapata huduma inayostahili, kusingekuwa na hii migongano kwa ajili ya kuendelea kufanya jamii zetu ziende…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi. Kwanza nianze kabisa kuipongeza Serikali yetu ya Chama Cha Mapinduzi ambayo inaongozwa na Dkt. Samia Hassan Suluhu ambaye ni mwanadiplomasia namba moja. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri lakini pia nimongeze Mheshimiwa Naibu Waziri, baba yangu Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk.

Pia nimpongeze mama yangu Mulamula Mwenyezi Mungu akutangulie ili uweze kupata hiyo nafasi. Mungu akusaidie ili uweze kuipeperusha vyema Tanzania yetu na mimi nikiwa mkubwa nitakuwa kama wewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu nitachangia kwenye diplomasia ya uchumi ambayo ni kipaumbele namba moja kwenye Wizara. Kabla sijaongelea kwenye hilo suala la diplomasia ya uchumi, naomba nimkumbushe Mheshimiwa Waziri kwamba bajeti iliyopita nilichangia kidogo kuhusiana na vikwazo vya wafanyabiashara ambao wanaliendea soko la Zambia, lakini wakifanya shughuli zao Zambia pamoja na kuliendea soko la Kongo kupitia Nchi ya Zambia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutatamani Mheshimiwa Waziri aseme neno, je. bado anaendelea kujua kwamba wafanyabiashara hawa wanaendelea kupitia vikwazo? W iki moja iliyopita walimfuata Mwenyekiti wa Kamati Mheshimiwa Nyongo kwa ajili ya kuendelea kuelezea changamoto zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye diplomasia ya uchumi kama ambavyo Wizara wenyewe wamesema kwamba ndio kipaumbele chao namba moja, lakini na maoni ya kamati wamesema kwamba diplomasia ya uchumi bado haijaeleweka kwa ufasaha kwa wananchi na hata kwa viongozi ambao wanasimamia sekta hizo, wakataja kwa mfano. Nitataka nisimamie zaidi kwenye maoni ya Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli diplomasia ya uchumi kwa wananchi wetu wa kawaida, bado hawajui diplomasia ya uchumi ni nini. Watu wengi wanafikiria diplomasia ya uchumi ni wale watu ambao wanapita kwenye red carpet na wale wavaa suti za dark blue pamoja na white color, lakini tunaamini kwamba diplomasia ya uchumi hapa ndio kwenye eneo ambalo limebeba ajira nyingi sana na zinaweza zikasaidia kukuza uchumi wetu kwa kiwango kikubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitolee mfano, mwaka jana kama sio mwaka juzi, tulipewa soko kubwa sana kwenye nchi ya China kupeleka soya, lakini unaweza ukashangaa kwamba ilifika wakati sisi hatuwezi kupata soya hapa. Ilipelekea Watanzania wakawa wanachukua soya nyingi kutoka Zambia, yaani pale mpakani Tunduma ilikuwa ndio biashara, kila mtu anatafuta soya kutoka Zambia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nikawa najiuliza sisi hapa kwetu tuna halmashauri 184, nikachukulia mfano tuchukue tu halmashauri 100 tu za wakulima mfano kule kwetu Momba, mia tu. Tungewapa target kwamba wazalishe tani za soya milioni moja halmashauri mia, maana yake kila halmashauri ingeweza kuzalisha soya tani elfu kumi ambayo ni kitu kinawezekana, lakini hatukuwahi kupata hilo soko kabisa na soya nyingi kwa kiwango kikubwa zilikuwa zinatoka Zambia na waliokuwa wanaenda kuchukua Zambia ni Watanzania hawa hawa. Tafsiri yake ni nini? Ni kwamba sisi tunasaidia kuwakuzia uchumi Zambia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maandiko kidogo ambayo nilipata nafasi nikasoma kuhusiana na diplomasia ya uchumi namna ambavyo inaelezea, kwamba watu wenye uwezo wafanyabiashara, lakini na hata watu wa kawaida wa chini ambavyo diplomasia hii ya uchumi inawalenga. Inasema hivi diplomasia ya uchumi ni mbinu na mkakati unaotumiwa na nchi na mashirika ya kimataifa katika kukuza maslahi yao ya kiuchumi nje na mipaka yao. Lengo la diplomasia ya uchumi ni kuimarisha ushirikiano wa uchumi kibiashara, uwekezaji na ushirikiano wa kiufundi kati ya nchi na kuboresha hali ya uchumi kitaifa. Diplomasia ya uchumi inahusisha shughuli kadhaa ikiwa ni pamoja na uendelezaji wa biashara na uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inaendelea: Nchi zinatumia diplomasia ya uchumi kukuza biashara na uwekezaji kwa kuvutia wawekezaji na kujenga mazingira mazuri ya biashara. Hivyo, wafanyabiashara kusaini mikataba ya biashara na makubaliano na wawekezaji kushirikiana katika masuala ya kifedha na kibenki. Aidha, ushirikiano wa kiufundi, diplomasia ya uchumi inahusisha pia kubadilishana maarifa na teknolojia. Nchi zinaweza kuweka mikataba ya ushirikiano wa kiufundi katika maeneo ya kilimo hapa kwenye kilimo ndio tunajiongelea sisi watu wa Momba na halmashauri zingine ambazo wanalima, afya, nishati, miundombinu na teknolojia ya Habari. Kwenye teknolojia ya habari ndio kwenye mambo ya block chain technology na mawasiliano. Hii inaweza kuimarisha teknolojia na ujuzi na inachangia katika maendeleo ya uchumi wa nchi zinazoshirikiana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameendelea wanasema, katika diplomasia ya uchumi nchi zinaweza kutuma wawakilishi wa Serikali kama mabalozi wa uchumi au wajumbe wa biashara kwenye nchi zingine. Hao hufanya mazungumzo na kuwakilisha Serikali…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante sana.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, namalizia tu kidogo. Fursa za biashara na ushirikiano wa kiuchumi. Diplomasia ya uchumi kwa kumalizia anasema, malengo ya diplomasia ya uchumi ni pamoja na kuongeza mauzo ya nje na bidhaa na huduma za nchi. Kujenga mtandao wa biashara wa washirika wa kimataifa, kuvutia wawekezaji wa kigeni, kukuza viwanda vya ndani. Sasa tutakuzaje viwanda vya ndani kama hatumshirikishi mwananchi wa kawaida huyu anayefanya shughuli ndogo ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia, niombe kwamba, Wizara ilikuwa inasema inatoa elimu mbalimbali kwenye mambo ya diplomasia ya uchumi kwenye magazeti, redio na vitu kadha wa kadha. Niombe elimu hii iende kule kwenye Baraza letu la Madiwani. Wizara ya Mambo ya Nje waweke dirisha kwenye Wizara ya TAMISEMI ambao wao wanazijua halmashauri na uwezo wao. Wanajua vipato vya halmashauri ipi ina mapato kidogo, halmashauri ipi inafanya kazi gani.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Tunaomba Wizara ya Mambo ya Nje watusaidie katika hili ili diplomasia ya uchumi iende kwa wanachi wa kawaida kabisa, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi, Mwenyezi Mungu akubariki. Kwanza kabisa nianze kuipongeza Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi ambayo inaongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuweka jitihada kubwa katika Wizara hii ili iendelee kutuongezea mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa mambo yote ambayo ameyafanya kwenye Wizara alikotoka huko, kuhakikisha mpaka Yanga wamefikia hiyo hatua ambayo wameifikia, tunaamini pia ni jitihada zako zimeonekana huko. Yupo msanii mmoja alishawahi kuimba huko nyuma kwamba, “Hiki ni kisiki cha mpingo, wenye shoka wameshindwa, unakuja na panga unajisumbua.”
Sasa tunaamini kwamba Mheshimiwa Waziri, wewe umekuja kwenye hii Wizara yenye kisiki cha mpingo, uje na msumeno ili uweze kutoa hicho kisiki cha migogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaomba tu kuchangia katika maeneo mawili. Moja ni ushauri. Ushauri wangu kwanza niombe Wizara hii kwa kushirikiana na Wizara nyingine zile ambazo zinaunda ile Kamati ya Mawaziri Nane kwamba tuangalie hata nchi nyingine ambazo zimeendelea, mfano, South Africa wame-specialize kwenye mambo kadhaa. Kwa mfano ukienda Durban ni sehemu inayohusika na viwanda tu. Ukienda Johannesburg ni sehemu ambayo inahusika na biashara na sisi tuangalie kwamba yako baadhi ya maeneo ambapo tutenge maeneo iwe ni special kwa ajili ya wafugaji wetu ili pia mifugo isiingie hifadhini na pia isiwaingilie wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, iko mikoa hapa inajulikana kabisa kwamba ni mikoa ambayo inategemewa na nchi hii kwa ajili ya kuzalisha chakula. Mfano Songea, Iringa, Njombe, Songwe, Mbeya, Katavi na Rukwa, lakini hata Mkoa wa Morogoro. Sasa pia mikoa hii ambapo inaendelea kugubikwa na wafugaji pia tunashindwa hata kuitambua mifugo yetu tuwaweke sehemu moja ili ile azma ya Mheshimiwa Ulega ya kutaka kuwapandia majani sehemu moja, itakuwa ni rahisi kuitambua mifugo hii na tuweze kuwahudumia vizuri lakini itawasaidia sana watu wa maliasili mifugo hii isiendelee kuingia hifadhini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, mimi nina maombi hapa kutoka kwa wananchi wa Jimbo la Momba. Kwa ridhaa yako naomba mhudumu apite aweze kumpelekea Mheshimiwa Waziri. Mheshimiwa Waziri sisi watu wa Jimbo la Momba miaka ya 1974 kipindi kile cha Sogea cha Mwalimu Nyerere, wazazi wetu kutoka huko vijijini nikimaanisha babu zetu, waliambiwa watoke kwenye vijiji vya mbali wakae sehemu za karibu ili huduma za kijamii ziweze kuwapata kwa pamoja, kukiwa kuna lengo zuri na wakaachia mapori yao ya kutosha ili wakae kwenye vijiji kwa pamoja waweze kupata huduma za kijamii kwa pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wazazi hawa, babu zetu hawa, waliamua kuachia hayo maeneo kwa nia njema kwa Serikali na maeneo hayo yakawa ni maeneo ya hifadhi. Sasa kipindi hicho cha mwaka 1974, watu hawa walikuwa wanakadiriwa kuwa chini ya watu 20,000. Sasa hivi tunavyoongea kwenye sensa ambayo imefanyika mwaka jana 2022, wananchi wa Jimbo la Momba tuko zaidi ya 270,000. Sasa tumeongezeka, katika vijiji hivyo 72 kuna maeneo machache tu wanaomba wapate kipande kidogo cha ardhi Mheshimiwa Waziri ili waendelee kuendesha shughuli zao za kilimo kwa sababu sisi shughuli yetu kubwa ni kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba kwa moyo wa unyenyekevu na uadilifu mkubwa, kwenye Kitongoji cha Kanyara ambacho kijiji chake ni Tontera kwenye Kata ya Chilulumo kwenye Kitongoji cha Mbaro kwenye Kijiji cha Mlomba Kata ya Chitete, kwenye Kitongoji cha Moravian Kijiji cha Itumbula Kata ya Ivuna, kwenye Kitongoji cha Mbao na Chiula kwenye Kijiji cha Ntungwa na Mkomba ambapo Kata yake ni Mkomba. Wananchi hawa wote wamezungukwa na hifadhi. Wananchi hawa wote wamezaliana hawana mahali pa kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tunatambua kwamba nia ya Serikali ni njema, nia ya Serikali ni nzuri kwamba ni lazima tutunze maeneo yetu ili vizazi na vizazi vije kurithi. Sasa kama msipotaka kutupa hata kipande kidogo cha ardhi, hawa babu zetu ambao waliamua kuyaachia maeneo haya wakaamua ku-sacrifice kwa ajili ya sisi kizazi chetu, tusipopewa sisi tutaenda wapi? Wananchi hawa wasipokumbukwa ili wapate kipande kidogo; na hawaombi ekari 1,000, hawaombi ekari 500, wanaomba ekari chache tu ili waweze kuendelea kuendesha shughuli zao. Mtakapoendelea kutuacha hatuna mahali pa kwenda, sisi tutageuka kuwa watumwa ndani ya ardhi yetu wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tunavyoongea miaka 30 iliyopita Bunge lilikuwa kule Msekwa ndiko Wabunge walikuwa wanakaa, lakini baada ya mahitaji kuongezeka sasa hivi tuko mahali hapa. Maana yake kulionekana kuna uhitaji wa kuongezewa Bunge ili kuwe na uwakilishi. Kwa hiyo, sisi mkituweka kwenye kundi la kutufunga kwamba tunatunza kwa ajili ya vizazi vijavyo, maana yake mnakihukumu kizazi cha sasa kwa ajili ya kizazi kinachokuja. Sasa hawa wananchi ambao babu zao waliamua kutunza kwa ajili ya wajukuu zao, baba zetu wamevumilia sasa tumezaliwa kizazi kama hiki cha kwangu. Vijana hawana mahali pa kulima, vijana hawana mahali wanaweza wakajenga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa dhati ya moyo wangu nikuombe sana sana Mheshimiwa Waziri na ikikupendeza nikuombe sana tunaomba uje ufanye ziara kwenye Jimbo la Momba kwa masikio yako ili angalau uweze kusikia namna ambavyo wananchi hawa wanaendelea kuomba. Tunakuomba sana, tunakuomba mno na kwa unyenyekevu mkubwa, kama ambavyo wananchi wa maeneo mengine wamefurahishwa. Wananchi wa Mara ambavyo Mheshimiwa Rais aliwaona akawakumbuka akaona iko haja ya kurekebisha tena mipaka ya uhifadhi. Hata sisi tunaomba mipaka ya uhifadhi ije irekebishwe ili wananchi hawa kwa moyo wa unyenyekevu waweze kupata sehemu ya kuendesha shughuli zao. Mimi nakuomba sana na ninarudia tena kuomba sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama bajeti hii itapita sisi hatukupata tena eneo la kulima, hata yale ambayo tulikuwa tumeendelea kuwaahidi wananchi kwamba watapata afadhali, tutaonekana ni waongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Hoja Kuhusu Bei ya Kuuza na Kununulia Mahindi
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru tena kwa nafasi, nimesikiliza maoni yote ya Waheshimiwa Wabunge ambao wametoa na kwa upande wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, Wabunge tuseme tuko hapa siyo kwa lengo la kupinga maoni ambayo Serikali imetoa na mpango wote ambao wameutoa. Waraka ambao Mheshimiwa Waziri aliutoa tarehe 23 Mei, 2023 kuelezea namna na mchakato ambavyo tunapaswa kutoa mazao nje ya nchi, mimi niseme unaonekana una tija kwa Serikali, una tija kwa wananchi wetu, lakini changamoto iko hapa tu, ametoa jambo hili ghafla sana, jambo hili amelitoa siyo rafiki kwa mazingira yetu.

Mheshimiwa Spika, kwenye Waraka wake ukisoma kwenye para ya kwanza roman number three amesema hivi “wafanyabiashara na wanunuzi hao wanatakiwa kuwa na nyaraka zote muhimu ikiwemo na utambulisho wa mlipa kodi - TIN, certificate of clearance, leseni ya biashara ambayo ni export license, namba za NIDA na wamiliki wa makampuni.

Mheshimiwa Spika, kwenye TASAF peke yake tukiwa hapa ndani watu wanakosa TASAF kwa ajili ya kukosa namba za NIDA. Iwe leo, yaani leo ndani ya mwezi mmoja mtu ataweza kupata namba za NIDA ili aweze kufanya hilo jambo, siyo uhalisia. Jambo ambalo Mheshimiwa Waziri amelileta ni rafiki lakini haliendani na mazingira.

Mheshimiwa Spika, biashara ya mazao ni biashara ya msimu, sasa hivi tunavyoongea Zambia imefunga mipaka yake kupeleka mazao ya chakula nchini DRC. Tafsiri yake sisi huku kwetu ni opportunity. Kwa hiyo, kama Mheshimiwa Waziri ame-raise haya mambo mapema hivi safari hii hatuwezi ku-meet hiyo demand ya soko la Congo.

Mheshimiwa Spika, ombi letu kwa Serikali tunaomba mambo haya yaanzishwe mwakani mwezi wa kwanza au kama Mheshimiwa Waziri yuko tayari jambo hili liendelee awe rafiki yeye kupitia Wizara yake aseme mambo yote haya kila kinachotakiwa mwananchi huyu au Mtanzania huyu anaweza akayapata ndani ya wiki moja ili aweze kuendana na hiyo demand ya wakati huo, yaani yeye Mheshimiwa Waziri awe kiungo kwenye hizo Taasisi nyingine.

Mheshimiwa Spika, kwa ridhaa yako naomba Mheshimiwa Waziri apelekewe hii document kwenye para la pili roman six ambapo anaongelea lazima upate export permit pamoja na phytosanitary certificates. Wameweka link hapa ya Wizara ya Kilimo ambayo unapaswa ku-apply kupitia mfumo.

Mheshimiwa Spika, mimi nimesoma IT degree yangu ya kwanza, ona vile system inavyoonyesha inaonyesha system iko under maintenance, sasa huyu mwananchi ata-apply kitu gani? Naomba mhudumu aje achukue ampelekee Mheshimiwa Waziri hili jambo labda yeye atufafanulie system yake inavyosema hivi inamaanisha nini? Inasemaje yaani huyu mwananchi wa kutoka Momba, kutoka kule Kalambo anapata nini hapa, hizo ndiyo permit ambazo tunaziongelea.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Haya sekunde 30 maliazia, kengele imeshagonga.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nia ya Serikali ni njema lakini ndani ya muda mfupi wameweka masharti lukuki ambayo hata hao wafanyabiashara wetu au Watanzania wetu ambao tunawazuia wafanyabiashara kutoka nje bado hayawa-favor. Kwa hiyo, tukuombe Bunge litoe Azimio ili Mheshimiwa Waziri alegeze masharti kwa lengo la kuwasaidia wakulima. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi. Kwanza kabisa nianze kuipongeza Serikali kupitia Wizara yake ya Kilimo, Mheshimiwa Waziri nakupongeza pamoja na crew yako yote bila kusahau Katibu Mkuu na Watendaji wote. Kwa dhati kabisa naomba nimpongeze Mkurugenzi wa TAHA Dada yangu Jackline Mkindi, kwa kweli tunakupongeza sana kwa namna ambavyo umeendelea kuwapa matumaini Wizara ya Kilimo, umeonesha mfano kwa akina mama ambao wanafanya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutumia Bunge hili niseme naomba urafiki wetu usiishie tu kule Arusha sasa hivi tuhamie Jimboni Momba tunatamani kukuona. Mheshimiwa Waziri kabla nielekeze mchango wangu kwenye mambo mawili kwenye Benki ya Kilimo pamoja na umwagiliaji naomba nitoe ushauri. Mheshimiwa Waziri hotuba yako ni njema sana na imeleta matumaini sana kwa wakulima wa nchi hii, kwa namna hata ulivyokuwa unawasilisha mwili wako ulivyokuwa unazungumza inaonesha umebeba matumaini kwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri katika hili ili bajeti yako iweze kutekelezeka vizuri, angalau kupungue siasa kidogo, ili siasa ipungue ili matumaini haya uliyowaonesha Watanzania wakati unawasilisha naomba tuanzie hapa. Sasa hivi bei elekezi ya Mahindi ambayo mmetangaza kwa kilo ni Shilingi 570 vyovyote vile, Mheshimiwa Waziri tumepata janga la mvua hapakuwa na mvua kabisa na hayo yalikuwa ni mabadiliko ya hali ya hewa, pia tulipata mfumuko wa bei kwenye mbolea, wananchi hawajalima na hata walipolima kwa kutumia uwezo wa Mwenyezi Mungu hawakuweza kwa sababu mazao yamekauka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka kukuambia huko vijijini mahindi ni bei ghali. Bei ya debe moja la mahindi linauzwa shilingi 10,000, shilingi 9,000 hadi sehemu nyingine shilingi 12,000, mwananchi huyu atanunua kutoka wapi? Tunaomba kama inawezekana kwa kuwa NFRA lengo lake kubwa ni kwa ajili ya usalama wa chakula, tunaomba bei ya mahindi kwenye maghala yetu kwa mkulima wa kawaida yauzwe kwa kilo shilingi 300, tukiwa na maana kwamba yakiuzwa shilingi 300, kilo 100 yatauzwa shilingi 30,000 sawa sawa na ile bei ambayo huwa wachuuzi wanaanza kwenda kununua kule vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitaka kula lazima uliwe! Kwa hiyo ambavyo Serikali huwa inaenda kuonekana wakati wa kununua tu sasa hivi tunaomba na yenyewe ikubali kuingiliwa, wananchi hawana kabisa mahindi huko vijijini hakuna, hata wakipika hizo pombe za kienyeji hawana uwezo wa kununua mahindi. Kwa hiyo, tunaomba bei ya mahindi ishuke kwenye maghala iwe Shilingi 300. Utajuaje kwamba itaenda kumnufaisha mwananchi wa kawaida kwa sababu tunajua wafanyabiashara watachukua hiyo nafasi kwa ajili ya kujinufaisha, wale wanajeshi wako uliokuwa umewaleta pale juzi wanawajua vizuri wananchi wa kawaida wale Maafisa Ugani, wanawajua vizuri kabisa kwamba huyu ni Bibi hana uwezo na huyu ni mfanyabiashara, yule Bibi ambaye anataka kununua kuanzia gunia moja, debe mbili hadi gunia 10 tunaomba mahindi yauzwe kwa kilo moja Shilingi 300. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na muda kutokuwa rafiki kwenye suala la umwagaliaji, nimeshawasilisha maandiko yangu kwa watendaji wako. Yapo mabonde kadhaa kwenye jimbo langu ambapo pia mwaka 2021 nilikwambia; tunalo Bonde la Msangano ambalo likiwezeshwa kwenye umwagiliaji litahudumia vijiji zaidi 10. Pia tunalo Bonde la Kamsamba ambalo likiwezeshwa litahudumia kata zaidi ya nne pamoja vijiji zaidi 15. Vile vile tunalo Bonde la Kapele pamoja na bwawa ambalo linabeba Bonde la Kasinde pamoja na Mto Tesa, litahudumia kata zaidi ya sita pamoja na vijiji zaidi ya 15. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoongelea lango la SADC tunamaanisha Wilaya ya Momba. Wilaya hii ina majimbo mawili; Tunduma na Momba. Sisi Momba ndiyo tunalima, Tunduma hawalimi. Sasa Mheshimiwa Waziri itakuwaje usituwezeshe sisi huku ambao ndio tunaanza kupokea kwenye lango la SADC kwenye umwagiliaji? How comes mtu unaweza usitengeneze sebule ukaenda kutengeneza chumbani, mgeni akija atajuaje? Kwa hiyo, tuanzie hapa ambayo ndiyo mapokeo ya lango la SADC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchele wote ambao unauona upo pale Tunduma unatoka Kamsamba na mchele wa Kamsamba unauzika sehemu yoyote. Kwa hiyo, tunaomba sana; Zambians wanakula mchele wetu, Kongo wanakula mchele wetu. Tunaomba kuwezesha kwenye mabonde yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo namwomba Mheshimiwa Waziri hili tusaidiane. Ataongea vizuri na watu wa TAMISEMI, tunaelewa dhati kabisa ya moyo wake ya kwamba anataka kuwasimamia wale Maafisa Ugani, lakini how comes mzazi awe na mtoto ambaye amemzaa, na ana uwezo, anaweza kumhudumia, lakini awe anakulia nyumba ya pili? Maafisa Ugani warudi kwenye Wizara yake. Hiyo D by D tunaona kabisa imeshindwa kufanya kazi. Haiwezekani hata kidogo… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa, malizia hiyo sentensi yako ya mwisho.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, namalizia. Kule kwenye Halmashauri zetu Maafisa Ugani wanatumwa kazi nyingine na wakati mwingine hata wakipewa magari wananyang’anywa. Sasa nani ambaye ataweza kusoma kama hali. Kwa hiyo, tunaomba Maafisa Ugani warudi kwenye Wizara yako ili tuone huo usimamazi unaotaka kuwasimamia sisi tuje kukubana hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi kwa ajili ya muda ninaipongeza Serikali pamoja na viongozi wote wa Wizara. Mchango wangu utajielekeza kwenye mapinduzi ya nne ya viwanda Forth Industrial Revolution nikimaanisha nataka kuongelea teknolojia ya Block Chain.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kabla nijielekeze kwenye mchango wangu naomba nitaje baadhi ya maeneo kwenye Jimbo langu ambayo hakuna mawasiliano ya simu. Kata ya Mkomba yote especially kwenye kijiji cha Ntungwa, kijiji cha Mfuto, Isunda, Lwasho, Kata yote ya Kapela na vijiji vyake Lwate, Ntanga, Ntungwa, Mang’ula pamoja na vijiji vingine kata ya Ivuna Kamsamba na Chiluluma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuchangia kwenye block chain nataka kuongelea kwenye hili eneo ambalo angalau Benki Kuu yetu imeshaanza kuruhusu mazungumzo na baadhi ya vijana wa kitanzania ambao wanafanya kazi kwenye hii teknolojia nataka niseme toka teknolojia hii imeingia kwenye mapinduzi haya ya nne ya viwanda zaidi ya vijana wa kitanzania 1,000,000 pamoja kwamba siyo rasmi wanajishughulisha na biashara hii na kwa miaka minne au mitano ambayo imepita zaidi ya bilioni 300 za kitanzania zimeshafanyiwa transaction lakini unaweza ukaona hakuna namna nzuri ambayo Serikali imeweka ili kuendelea ku-regulate hizi transaction ili iweze kuzichukulia kodi lakini pia ili kuilazimisha hii sekta na tuweze tufahamu tupate takwimu kwamba ni watanzania wangapi ambao wanajihusisha na hii teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hii Central Bank Digital Currency nataka nirejee waraka mmoja ambao umepita kama wiki mbili Benki Kuu walitoa, ambao ulikuwa unasema hivi Ministry and chamber welcomes discussion on CBDC and clip to asset Minister for Finance and Planning Dr. Mwigulu Nchemba has challenge an International Conference on Central Bank Digital Currencies and clip to assets to come up with a clear guidance and whatever countries should regulate or supervise clip to assess or discourage their use.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema kwamba hapa wanasema whether waone namna nzuri ambayo wanaweza waka-regulate au wakaamua kui-discourage nataka kusema ni ngumu sana kama Serikali kupitia Wizara hii ambayo inasimamia suala hili kama hawataruhusu kutengeneza chombo maalum ambacho watawaita vijana wa kitanzania ambao wanauelewa waweze kuwashauri waweze kuwasaidia ndipo ambapo watakuja na njia nzuri ya kuweza kuwasaidia namna ya ku-regulate kuwepo kwa hii Benki ya hii CBDC yaani tupate Central Bank ambayo itajishughulisha na mambo ya digital currencies. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, itakuwa ngumu kwa sababu gani? Kwa sababu hoja ya CBDC huko duniani ni kuwepo kwa beat coin (yaani ni kuwepo kwa zile digital currencies) hoja na idea na concept ambayo iko kwenye block chain ambayo iko kwenye digital currency especially kwenye beat coin ndiyo ambayo huko duniani iliibua hii CBDC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa itakuwa ngumu sana kui-regulate na kuipokea hii idea ikiwa kama tu kwanza Serikali haijawahi kumiliki hata coin exchanger yoyote hapa tunapoongea sidhani kama Serikali wanajua kuna kitu kinaitwa Binance, kuna kitu kinaitwa Remitano local bitcoin. Tulitamani kuona angalau kuwe hata na coin exchanger yoyote ya majaribio ambayo Serikali imefanya vijana hawa wa kitanzania wana-practice na wana-regulate sasa hatujawahi ku-regulate unafikiri Benki Kuu wataichukulia hii namna gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwenye Wizara hii ninawaomba mtoe room under Task Force yako ita vijana wa kitanzania wakupe ushauri hatupotezi chochote kama tutakubali kujifunza. Naomba nitolee mfano mimi nikiwa form two mwaka 2004 tulikuwa tunafundishwa kama siyo form two form three kuna topic moja ilikuwa inasema globalization. Tulikuwa tunaambiwa dunia kiganjani at that time kulikuwa hakuna smart phone unaposema dunia kiganjani tulikuwa hatujui tutamaanisha nini dunia kiganjani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sasa hivi tuna-practice dunia kiganjani bili tunalipia kwenye kiganja, Bunge tunaendesha kwenye kiganja habari ni kwenye kiganja. Kwa hiyo, hata hili jambo ili CBDC iweze kufanyakazi ni lazima kwanza Serikali iruhusu vijana wa kitanzania ni lazima Serikali iwekeze iweze kuleta coin exchange Serikali ifungue wallet ifanye majaribio kama ambavyo tunaweza tukasema hatuna vita Jeshini lakini tunatengeneza mabomu kwa kujihami tu kwamba likitokea lolote tufanye, kwa hiyo, tungeweza kufanya mazoezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mzuri Rais wa Salvador ambaye anaitwa Naibu Bukin tarehe 17 Mei Jumanne hii ya wiki hii ambayo tuliyonayo aliitisha mataifa 44 duniani akiziita baadhi ya Benki Kuu kwenye mataifa mbalimbali, lakini akiziita na baadhi ya taasisi za kifedha kwenda kushiriki akaunti yake ya twitter iko verified wataalam wanaweza wakamtembelea wakaona pale unaweza ukatembelea page yake Waziri ukaona alichokifanya na majadiliano yote aliyofanya. Rais huyu aliziita nchi mbalimbali Zambia ilikuwepo, Mauritius ilikuwepo, Bangladesh, Mozambique, Morocco, Sera Leone, Senegal, Nigeria, Jordan, Egypt na nchi mbalimbali kwanini sisi nchi yetu hakutokea hata mwakilishi hata mmoja tunapoteza hela nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tunaendelea kulalamika tunasema kwamba ajira ni ngumu kwa watanzania ni kweli ajira ni ngumu na tukiwa hapa Bungeni tunalalamika kila wakati kwamba mfumo wetu wa elimu hau-support watu kujiajiri, lakini tunashindwa kuendana na teknolojia.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Condester.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika moja tunashindwa kuendana na teknolojia tuliyonayo ili iweze kuwaajiri vijana wengi wa kitanzania na kupoteza mapato. Wito wangu kwa Serikali kwenye bajeti hii unda chombo kwenye Wizara yako Mheshimiwa Waziri Nape ili vijana wa kitanzania waweze kukushauri na tuweze kuitumia vizuri Block Chain Technology naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi, kwanza kabisa nianze kwa kusema naunga hoja iliyoko mezani.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kipekee kabisa nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo amejitahidi kuwa mwanadiplomasia namba moja kuhakikisha anaendelea kuiunganisha nchi yetu na nchi zingine ili kuleta maendeleo kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu utajielekeza kwenye diplomasia ya uchumi na kwenye diplomasia ya uchumi nitaongelea mambo mawili; nitaongelea masoko, lakini pia nitaongelea zile nchi ambazo zina masoko, lakini tunaendelea kupitia vikwazo vingi ambavyo tunatamani kuona Wizara hii iweze kutusaidia.

Mheshimiwa Naibu spika, lakini kabla ya kuanza kuchangia mchango wangu nataka mchango wangu ujielekeze kwa kuzingatia Ilani ya Chama cha Mapinduzi ambayo ina Sura 10; kwenye Sura ya Saba inaongelea kwenye Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye sura hiyo nataka nisome kwenye ukurasa wa 184 ambao Chama cha Mapinduzi kiliielekeza Serikali hii katika kipindi cha miaka mitano inapaswa kufanya nini. Katika kipindi cha miaka mitano Chama cha Mapinduzi kinaielekeza Serikali kwenye diplomasia ya uchumi kufanya mambo kadhaa yafuatayo:-

(a) Kukuza mahusiano ya kiuchumi na mataifa, Jumuiya za Kikanda na taasisi zingine za kimataifa.

(b) Kulinda uchumi na maslahi mapana ya Taifa kwa kutumia jiografia na nchi kimkakati una ushawishi wa historia hususan kwenye Ukanda wa Kusini.

(c) Kuhakikisha kuwa balozi zetu zinakuwa kiungo muhimu cha kukuza uwekezaji na upatikanaji wa masoko na bidhaa na huduma zetu.

(d) Kuweka mazingira wezeshi ya kuendelea kuratibu na kuhamasisha ushiriki wa Watanzania wanaoishi nje ya nchi (Diaspora) ili waweze kuzitangaza fursa zinazopatikana nchini na kushiriki kikamilifu katika kuchangia maendeleo hususan ya kiuchumi ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nataka ku-quote kidogo kwenye sera ya diplomasia ya uchumi inasemaje? Inasema hivi; diplomasia ya uchumi katika eneo hili pamoja na mambo mengine inapaswa kuwezesha wafanyabiashara kupata masoko na huduma na bidhaa zinazozalishwa na kutaka kukuza katika masoko ya nje katika jambo hili wanapaswa kuonesha ukubwa wa soko la bidhaa na huduma husika na taratibu za kuingia katika masoko hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ziko baadhi ya nchi ambazo zinatumia sana mazao ambayo tunazalisha hapa nchini kwetu ni pamoja labda na mchele ambao unatokana na mpunga, mahindi na mazao mbalimbali ya mikunde na zipo baadhi nchi nyingi tu kwenye ukanda wa SADC ambazo zinatumia mazao hayo. Lakini cha kusikitisha kwa kuangalia hiki kipengele ambacho kinasema balozi zihusike naweza kusema kwamba mwaka jana kulikuwa na mdororo sana wa bei za mahindi hapa nchini kwetu na ikapelekea Serikali kukopa bilioni 50 ili kununua mahindi yale kwa wakulima wetu, unaweza ukaona kwamba hili lilikuwa ni jukumu la Wizara hii wao kuendelea kuzitumia balozi zetu zilizopo nchi mbalimbali ili kuendelea kututafutia masoko kwenye nchi mbalimbali zipo nchi nyingi sana ambazo ziko hapa Afrika zinatamani kupata mahindi tukianza hata na nchi ya Congo yenyewe na nitaeleza hapo baadaye vikwazo kwenye point yangu namba mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini zipo nchi nyingine Kenya wanatumia mahindi kutoka kwetu, lakini pamoja na mazao mengine je, Wizara hii mmewajibika namna gani kuhakikisha mnaendelea kututafutia masoko, imagine hii bilioni 50 ingeweza kutumika kwenye mambo mengine, Serikali isingeweza kwenda kununua yenyewe kwa sababu mngekuwa mmefungua wigo wa wakulima wetu, wafanya biashara wetu kwenda kuuza mazao huko sehemu nyingine ikiwa Ilani yenyewe ya Chama cha Mapinduzi ambayo ni chama ambacho kimeweka Serikali madarakani kiliwapa jukumu hili kufanya katika kipindi hiki cha miaka mitano.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nataka kuongelea vikwazo vya kibiashara ambavyo nchi yetu inapata kuelekea kwenye masoko mengine na hapa nataka kuliongelea sana soko la DRC Congo; sasa hivi Congo amekuwa ni mwanachama katika East Africa ni mwanachama wa SADC lakini ni mwanachama wa COMESA, ukiangalia sisi tulijitoa kwenye COMESA kwa hiyo Congo anao wigo mpana sana wa kimasoko sasa sisi zipo baadhi ya vikwazo ambazo tunavipitia kutoka nchi ya Zambia, nataka kurejea kitu kidogo kwenye hi sehemu (b) inayosema; kulinda uchumi na maslahi mapata ya Taifa kwa kutumia jiografia ya nchi kimkakati na ushawishi wa kihistoria hususani kwenye Ukanda wa Kusini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushirikiano wetu na nchi ya Zambia ni wa kiasili kabisa, ni wa kibaiolojia hatukupaswa sisi Wizara yetu kuupuuza, angalia sasa hivi tumetafuta option nyingine ya kuzikwepa vikwazo vya Zambia kwa kupitia Ziwa Tanganyika, tumeziwezesha bandari zetu nyingi kule, tumetumia fedha nyingi sana kuhakikisha namna gani tunaingia kwenye Jimbo la Tanganyika, mimi nasema naunga mkono Serikali kutaka kwenda kufungua hata barabara upande ule kule wa Congo, lakini naweza kusema hii tuitumie kama fursa tu ya kutafuta namna gani tuweze ku-penetrant Congo katika Majimbo 26, lakini hatupaswi kuchukua kile kigezo ambacho tunaona kwamba Zambia wametuzingira, tunashindwa kuingia Lubumbashi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kutoka Dar es Salaam upite Tunduma ili uweze kuingia Lubumbashi ni rahisi sana kuliko kutoka Dar es Salaam, upite Tabora, uende ukaingie ufike kwenye zile bandari sijui Kasanga, Kabwe, Kalema ambayo imejengwa sasa hivi zaidi ya bilioni 49. Tulitakiwa tukae na nchi ya Zambia tujadiliane tuweke mambo sawa kule yale Majimbo kwa mfano lile Jimbo la Hot Katanga ambalo ndio Lubumbashi, Rwalaba ambapo ni Kolowezi tutumie hiyo njia ya Tunduma kufika kwa sababu ni rahisi sana, na huku tuangalie hayo majimbo kwa ajili ya kuingia kwenye Majimbo mengine ambayo yapo mengi kule Congo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tumechukulia kama jambo hili kwamba tunajaribu kui-escape Zambia hakuna namna tunaweza tukai-escape Zambia kwa sababu bado tutataka kuingia kwenye nchi nyingine hata kama isipokuwa Congo. Tukitaka kuingia Zimbabwe tutaingiaje, tukitaka kuingia Botswana tutaingiaje ni lazima tutapita Zambia. Kwa hiyo ushirikiano wetu na Zambia si jambo la kuepukika si jambo la kupuuza Wizara hii mmechukua jukumu gani kuhakikisha tunaendelea kuji-expand/kujipanua zaidi kuona namna gani ambapo tunafikia soko la Congo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeliona hili jambo kama ni la kupuuza wafanyabiashara, madereva watu mbalimbali wanateseka sana. Sasa hivi imekuwa yaani unapopitisha mahindi Zambia ni kama umepitisha madawa ya kulevya na jambo hili sio kwamba Serikali ya Zambia ndio imelizingatia sana kwamba inaizuia Tanzania, wakati mwingine ni vita ya kiuchumi ambayo inafanywa na nchi nyingine, mbona South Africa wameaanza kujenga reli ambayo inapita Angola, iingie Lubumbashi iende mpaka Kolowezi. Hii ni vita ya kiuchumi ambayo wapo wafanyabiashara wanaendelea kutuchonganisha sisi na Zambia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi hatuwezi kugombana na Zambia sisi na Zambia ni ndugu, sisi na Zambia ni washirika wazuri ni washirika wa kihistoria ambao undugu wetu hauwezi kuepukika. Kwa hiyo mimi nilikuwa naona kuna haja kubwa sana Wizara hii itafute namna nzuri ya kwenda kukaa na nchi ya Zambia ili kuondoa vikwazo ambavyo tunavipata, ili wafanyabiashara ambao wanataka kupitisha mizigo yao kuingia Congo kwa kupitia njia ya Lubumbashi wapite kiurahisi na yale maboresha ambayo yamefanyika kwenye bandari zetu ili kuingia Jimbo la Tanganyika na majimbo mengine ambayo yapo Congo tuitumie kama fursa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Sichalwe, nilikuongeza dakika tatu.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi. Kwanza naanza kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kutekeleza mambo ambayo tuliyapendekeza kwenye Mpango uliopita. Pia, nawapongeza Waheshimiwa Mawaziri kwa kuwasilisha Mpango wao nasi tuweze kuongeza mawazo yetu waone kama vile yanafaa kwa ajili ya kusaidia Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaongelea katika maeneno mawili. Chanzo cha mapato, ni namna gani ambavyo tunaweza tukatumia mawazo haya yakatusaida kama Taifa kwa ajili ya kuongeza mapato. Jambo la kwanza, najaribu kuangalia yale maeneo ambayo kutoka kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi hususani kwenye upande wa vijana, Ilani ya Chama Cha Mapinduzi inasema: “kutengeneza ajira zisizopungua milioni nane katika Sekta Rasmi na isiyokuwa rasmi kwa vijana.” Chanzo kimoja ambacho nitaongelea ndani ya nchi yetu ni pamoja na huduma za forodha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Huduma nyingi za kiforodha mfano Tunduma, Namanga, Holili, Kasumulu na maeneo mengine ambapo kuna Vituo vya Forodha, kumeonesha kuvutia sana wananchi wengi kwenda kufanya biashara maeneo hayo. Namwomba Mheshimiwa Dkt. Mwigulu kwamba 2021 ulikuja pale, ukatembelea kwenye lile eneo, tunaomba tupate Kituo cha Forodha. Licha tu ya kwamba itasaidia wana-Momba lakini vituo vingi vya Forodha vimeonekana kuwa chachu ya mapato kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia tu mfano wa Tunduma, angalia mapato ambayo yanapatikana pale. Pia kwenye hivi vituo vya Forodha, licha tu ya kupata mapato, hata katika hali ya ulinzi, tunaongeza ulinzi kwenye nchi yetu kwa sababu tunakuwa tunaendelea kuikagua vizuri ile mipaka na kuzuia hata mambo ya magendo. Nakuomba Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, uone tena, ukae na timu yako ya TRA mpitie lile eneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuongezea hapo hapo kwenye Kituo cha Forodha Tunduma, namwomba Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi. Hivi mnaonaje kwenda kuyapunguza yale magari yote ambayo yamejaza msongamano pale Tunduma na kusababisha jam zisizokuwa za lazima? Kwa nini baadhi ya magari yasivutwe kwenda mpaka kule kwa Kakozi? Si ni matumizi mabaya ya barabara? Barabara iko wazi tu, nyeupe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa tunasubiri huo mfumo wa njia nne, basi tunaweza tukayavuta yale magari tukapunguza jam Tunduma ili watu wakaendelea kuvusha magari yao vizuri bila kuathiri shughuli nyingine. Mji mdogo lakini unaweza ukatumia zaidi ya nusu saa kwa ajili ya kupita kilometa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nataka kuongelea chanzo cha mapato ambacho kinaweza kikasaidia vijana, ni kwenye eneo la teknolojia. Wakati nasoma hotuba ya Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo, kwenye ukarasa wake wa 51 pamoja na ukurasa wa 117 kwenye kipengele cha 3.3.2.2.1, nikajaribu kuangalia namna ambavyo yeye ameielezea teknolojia. Katika ulimwengu tulionao, matajiri duniani, kwa mfano nikiongelea nchi ya USA wana mabilionea 735. China wana mabilionea 607 na nchi nyingine huko duniani. Hata hivyo, matajiri wengi hawa wanatokana na utajiri ambao unatokana na teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili nimeandaa andiko fupi kwa kuangalia mwaka 2021 ambao toka nimeanza kuchangia mambo ya teknolojia mwaka 2022, naomba Mheshimiwa Prof. Kitila Mkumbo apate pamoja na wewe mwenyewe upitie uone. Nimekuja na orodha ya matajiri duniani kama kumi hivi ambapo utaona utajiri wao wote mabilionea hawa unatokana na mambo ya teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ngoja niwasome kidogo. Tajiri wa kwanza duniani mwaka huu wa 2023 ni Elon Musk ambaye ana utajiri wa dola za Kimarekani bilioni 240 ambao unatokana na kufanya biashara za teknolojia. Ana Kampuni ya SpaceX pamoja na Tesla. Tajiri wa pili ni Bernard Arnault lakini yeye anafanya mambo ya fashion.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tajiri wa tatu ni, Jeff Bezos ambaye yeye utajiri wake ni dola za kimarekani bilioni 154, ambaye ndiye mmiliki wa Taasisi ya Amazon, anafanya biashara za mtandaoni, tajiri wa nne ni Larry Ellison ambaye utajiri wake ni dola za kimarekani bilioni 146 naye ni mmiliki wa Kampuni ya Oracle Cooperation ni mambo ya teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tajiri wa tano kwa mwaka huu wa 2023 …

MWENYEKITI: Mheshimiwa Sichalwe pamoja na kuwajua hao matajiri, ungelisaidia Bunge utajiri wao walioupata kwenye teknolojia na walitumia mbinu zipi ili work the talks ambapo sasa hao matajiri hawasaidii kitu kama huelezi wamefanya nini ili Waziri aweze kuelewa, sawa.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

MWENYEKITI: Halafu sasa hao matajiri waache, tutaambizana baadaye jioni.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Nataka kusema nini hapa; orodha ya matajiri wote ambao tunawaona duniani hawa wote wametokana na kuwekeza kwenye teknolojia. Kwenye teknolojia ipi? Mapinduzi manne viwanda (forth industrial revolution) kwenye mambo ya blockchain technology, kwenye mambo ya digital currencies na kwenye mambo ya artificial intelligence. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo haja ya Serikali yetu kutafuta mazingira mazuri na wezeshi ya kuruhusu vijana wa kitanzania kuonesha uwezo wao wa kiteknolojia ili na wao tuweze kupata matajiri wengi kama hawa duniani. Miundombinu yetu mingi iliyopo hapa Tanzania, hai-support vijana wengi kwenye kujielekeza katika teknolojia. Pia hakuna mazingira wezeshi ambayo Serikali imewawekea vijana ili waweze kuonesha uwezo wao na ubunifu wao ili tuweze kupata akina Elon Musk wengi kama hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia watu wote hawa pamoja na kunikataza ndio hivyo hivyo. Mtu kama Mark Zuckerberg pamoja na mawazo yake ya ubunifu lakini unaona kabisa Serikali yao imewatengenezea mazingira ambayo wana-support ubunifu. Yeye ndie ambaye ndio mmiliki wa Mtandao wa Facebook, Instagram, WhatsApp, angalia mazingira gani ambayo wanapata, angalia ni mapokeo gani ambayo Serikali ina-support teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2021 tulipochangia sana kwenye mambo ya blockchain technology Mheshimiwa Rais ameshawahi kutoka hadharani na kuonesha ni namna gani ambavyo wataalam wanapaswa ku-support.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa hivi kutaka kujua kwa nini nchi yetu wakati mwingine, inatukwamisha kwenye ku-support mambo ya teknolojia, angalia mpaka sasa hivi tulishachangia sana hapa bungeni kuhusiana na kuruhusu Mfumo PayPal ili tuweze kulipa malipo ya PayPal kwenda nje ya nchi, lakini unaweza kukuta watanzania wengi ambao wanafanya biashara ili waweze kulipa kwa njia ya PayPal wao wanaruhusiwa kulipa lakini wao hawaruhisiwi kulipwa. Kwa mazingira kama hayo yanaonesha dhahiri kabisa kwamba nchi yetu bado haijatu-support hususan vijana kwenye mambo ya teknolojia. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, mazigira wezeshi ya ku- support teknolojia yawezeshwe ili tuweze kupata matajiri wengi kama hawa duniani, ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Sasa hayo ndio ilitakiwa uyaseme, sio kutaja majina ya matajiri.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ilikuwa ni kuwa-motivate Mawaziri pamoja na wewe mwenyewe.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi. Kwanza naanza kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kutekeleza mambo ambayo tuliyapendekeza kwenye Mpango uliopita. Pia, nawapongeza Waheshimiwa Mawaziri kwa kuwasilisha Mpango wao nasi tuweze kuongeza mawazo yetu waone kama vile yanafaa kwa ajili ya kusaidia Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaongelea katika maeneno mawili. Chanzo cha mapato, ni namna gani ambavyo tunaweza tukatumia mawazo haya yakatusaida kama Taifa kwa ajili ya kuongeza mapato. Jambo la kwanza, najaribu kuangalia yale maeneo ambayo kutoka kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi hususani kwenye upande wa vijana, Ilani ya Chama Cha Mapinduzi inasema: “kutengeneza ajira zisizopungua milioni nane katika Sekta Rasmi na isiyokuwa rasmi kwa vijana.” Chanzo kimoja ambacho nitaongelea ndani ya nchi yetu ni pamoja na huduma za forodha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Huduma nyingi za kiforodha mfano Tunduma, Namanga, Holili, Kasumulu na maeneo mengine ambapo kuna Vituo vya Forodha, kumeonesha kuvutia sana wananchi wengi kwenda kufanya biashara maeneo hayo. Namwomba Mheshimiwa Dkt. Mwigulu kwamba 2021 ulikuja pale, ukatembelea kwenye lile eneo, tunaomba tupate Kituo cha Forodha. Licha tu ya kwamba itasaidia wana-Momba lakini vituo vingi vya Forodha vimeonekana kuwa chachu ya mapato kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia tu mfano wa Tunduma, angalia mapato ambayo yanapatikana pale. Pia kwenye hivi vituo vya Forodha, licha tu ya kupata mapato, hata katika hali ya ulinzi, tunaongeza ulinzi kwenye nchi yetu kwa sababu tunakuwa tunaendelea kuikagua vizuri ile mipaka na kuzuia hata mambo ya magendo. Nakuomba Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, uone tena, ukae na timu yako ya TRA mpitie lile eneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuongezea hapo hapo kwenye Kituo cha Forodha Tunduma, namwomba Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi. Hivi mnaonaje kwenda kuyapunguza yale magari yote ambayo yamejaza msongamano pale Tunduma na kusababisha jam zisizokuwa za lazima? Kwa nini baadhi ya magari yasivutwe kwenda mpaka kule kwa Kakozi? Si ni matumizi mabaya ya barabara? Barabara iko wazi tu, nyeupe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa tunasubiri huo mfumo wa njia nne, basi tunaweza tukayavuta yale magari tukapunguza jam Tunduma ili watu wakaendelea kuvusha magari yao vizuri bila kuathiri shughuli nyingine. Mji mdogo lakini unaweza ukatumia zaidi ya nusu saa kwa ajili ya kupita kilometa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nataka kuongelea chanzo cha mapato ambacho kinaweza kikasaidia vijana, ni kwenye eneo la teknolojia. Wakati nasoma hotuba ya Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo, kwenye ukarasa wake wa 51 pamoja na ukurasa wa 117 kwenye kipengele cha 3.3.2.2.1, nikajaribu kuangalia namna ambavyo yeye ameielezea teknolojia. Katika ulimwengu tulionao, matajiri duniani, kwa mfano nikiongelea nchi ya USA wana mabilionea 735. China wana mabilionea 607 na nchi nyingine huko duniani. Hata hivyo, matajiri wengi hawa wanatokana na utajiri ambao unatokana na teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili nimeandaa andiko fupi kwa kuangalia mwaka 2021 ambao toka nimeanza kuchangia mambo ya teknolojia mwaka 2022, naomba Mheshimiwa Prof. Kitila Mkumbo apate pamoja na wewe mwenyewe upitie uone. Nimekuja na orodha ya matajiri duniani kama kumi hivi ambapo utaona utajiri wao wote mabilionea hawa unatokana na mambo ya teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ngoja niwasome kidogo. Tajiri wa kwanza duniani mwaka huu wa 2023 ni Elon Musk ambaye ana utajiri wa dola za Kimarekani bilioni 240 ambao unatokana na kufanya biashara za teknolojia. Ana Kampuni ya SpaceX pamoja na Tesla. Tajiri wa pili ni Bernard Arnault lakini yeye anafanya mambo ya fashion.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tajiri wa tatu ni, Jeff Bezos ambaye yeye utajiri wake ni dola za kimarekani bilioni 154, ambaye ndiye mmiliki wa Taasisi ya Amazon, anafanya biashara za mtandaoni, tajiri wa nne ni Larry Ellison ambaye utajiri wake ni dola za kimarekani bilioni 146 naye ni mmiliki wa Kampuni ya Oracle Cooperation ni mambo ya teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tajiri wa tano kwa mwaka huu wa 2023 …

MWENYEKITI: Mheshimiwa Sichalwe pamoja na kuwajua hao matajiri, ungelisaidia Bunge utajiri wao walioupata kwenye teknolojia na walitumia mbinu zipi ili work the talks ambapo sasa hao matajiri hawasaidii kitu kama huelezi wamefanya nini ili Waziri aweze kuelewa, sawa.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

MWENYEKITI: Halafu sasa hao matajiri waache, tutaambizana baadaye jioni.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Nataka kusema nini hapa; orodha ya matajiri wote ambao tunawaona duniani hawa wote wametokana na kuwekeza kwenye teknolojia. Kwenye teknolojia ipi? Mapinduzi manne viwanda (forth industrial revolution) kwenye mambo ya blockchain technology, kwenye mambo ya digital currencies na kwenye mambo ya artificial intelligence. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo haja ya Serikali yetu kutafuta mazingira mazuri na wezeshi ya kuruhusu vijana wa kitanzania kuonesha uwezo wao wa kiteknolojia ili na wao tuweze kupata matajiri wengi kama hawa duniani. Miundombinu yetu mingi iliyopo hapa Tanzania, hai-support vijana wengi kwenye kujielekeza katika teknolojia. Pia hakuna mazingira wezeshi ambayo Serikali imewawekea vijana ili waweze kuonesha uwezo wao na ubunifu wao ili tuweze kupata akina Elon Musk wengi kama hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia watu wote hawa pamoja na kunikataza ndio hivyo hivyo. Mtu kama Mark Zuckerberg pamoja na mawazo yake ya ubunifu lakini unaona kabisa Serikali yao imewatengenezea mazingira ambayo wana-support ubunifu. Yeye ndie ambaye ndio mmiliki wa Mtandao wa Facebook, Instagram, WhatsApp, angalia mazingira gani ambayo wanapata, angalia ni mapokeo gani ambayo Serikali ina-support teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2021 tulipochangia sana kwenye mambo ya blockchain technology Mheshimiwa Rais ameshawahi kutoka hadharani na kuonesha ni namna gani ambavyo wataalam wanapaswa ku-support.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa hivi kutaka kujua kwa nini nchi yetu wakati mwingine, inatukwamisha kwenye ku-support mambo ya teknolojia, angalia mpaka sasa hivi tulishachangia sana hapa bungeni kuhusiana na kuruhusu Mfumo PayPal ili tuweze kulipa malipo ya PayPal kwenda nje ya nchi, lakini unaweza kukuta watanzania wengi ambao wanafanya biashara ili waweze kulipa kwa njia ya PayPal wao wanaruhusiwa kulipa lakini wao hawaruhisiwi kulipwa. Kwa mazingira kama hayo yanaonesha dhahiri kabisa kwamba nchi yetu bado haijatu-support hususan vijana kwenye mambo ya teknolojia. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, mazigira wezeshi ya ku- support teknolojia yawezeshwe ili tuweze kupata matajiri wengi kama hawa duniani, ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Sasa hayo ndio ilitakiwa uyaseme, sio kutaja majina ya matajiri.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ilikuwa ni kuwa-motivate Mawaziri pamoja na wewe mwenyewe.