Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Nusrat Shaaban Hanje (25 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa muda nizungumze.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, kabla sijazungumza kwa sababu na mimi ni mara yangu ya kwanza kuzungumza katika Bunge hili la Kumi na Mbili, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa uzima na kunijaalia kila kitu mpaka hapa nilipofika. Pia niwashukuru wazazi wangu na familia yangu na watu wangu wote ambao wako karibu na wananifahamu wanajua nini kinafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijachangia hotuba ya Mheshimiwa Rais ya kuzindua Bunge la Kumi na Mbili iliyotolewa Novemba 2020, niseme kabisa nimesikilizia hotuba hiyo nikitokea gereza la Isanga ambako nilikuwa mahabusu pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitachangia katika maeneo mawili, eneo la kwanza nitachangia katika ukurasa 13 wa hotuba ya Mheshimiwa Rais ya mwaka 2020 ambako amezungumza na nitaanzia na hilo kwa sababu amezungumza kwenye hotuba yake kwamba ndiyo jambo la kwanza na la umuhimu ambalo anafikiri katika Serikali yake kwa muda wa miaka mitano atashughulika nalo ambalo ni kulinda na kudumisha amani ya nchi umoja, uhuru na mshikamano pamoja na kuyalinda Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar. Kwa uzito wa hoja hiyo na mimi naomba nichangie kwenye hoja hiyo kwa yafuatayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nia ya dhati ya kulinda amani ya nchi, kwa sababu wote tunafahamu kwamba amani ni tunda la haki, kwa hiyo, kimsingi unapozungumza kwamba Serikali imejipanga kulinda amani ya nchi lakini pia kulinda mshikamano wa nchi huwezi ku-ignore vitu vidogo vidogo ambavyo vinaonekana kama tunazungumza vitu vingine na tunatenda vitu vingine. Ninasema hivi kwa sababu naona hapa kama vile hawa wanazungumza hawa wanajibu lakini kimsingi kuna mambo ya msingi ambayo wote tunakumbuka, mimi nitasema deep down kila mtu anajua kwamba there was something very wrong kwenye uchaguzi wa 2020.

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Kuhusu Utaratibu.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, kila mtu anajua moyoni kwake kulikuwa kuna mambo ambayo si ya kawaida mpaka watu ambao si wanasiasa walikuwa wanajua, watu wanaofuatilia demokrasia ya nchi yetu, watu wanaofuatilia taratibu za uchaguzi kwenye nchi yetu walikuwa wanajua kuna shida kubwa imetokea kwenye uchaguzi wa 2020. That is the fact kwa sababu fact hazibishaniwi. Kwa hiyo, sitaenda into details nini kilitokea kwa sababu kila mtu anafahamu nini kilitokea Zanzibar, watu waliwekwa ndani, kesi zaidi ya 20 na kimsingi mpaka sasa kuna kesi mbili tu na sitaenda kwenye details kwa sababu najua kuna kanuni zinanizuia kuzungumza masuala ya kimahakama.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Nusrat, naomba ukae.

Mheshimiwa Ali King, kanuni inayovunjwa.

KUHUSU UTARATIBU

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, Kanuni ya 70 (1) mpaka 9 inaeleza kuhusu kusema ukweli au kuhusu kusema uongo. Mheshimiwa aliyekaa kitako, Mheshimiwa Nusrat Hanje anazungumza kwamba vyombo vyote ambavyo vilikuwa vinashughulikia uchaguzi huu vimethibitisha kwamba uchaguzi haukuwa mzuri au haukuwa huru na haki kwa mujibu wa maneno ambayo ameyatumia.

Mimi namthibitishia kwamba vyombo hivyo vyote vilivyoruhusiwa na kujihusisha na uchaguzi ikiwemo Tume ya Uchaguzi na observers wote walithibitisha kwamba uchaguzi ulikuwa uko sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Tume ya Uchaguzi ndiyo iliyotoa matokeo ya uchaguzi kwa sababu uchaguzi ulikuwa huru. Ma-observers wa Umoja wa Afrika, EISA ya South Africa, Umoja wa Ulaya na East Africa wote hawa walisema uchaguzi ulikuwa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa afute kauli yake au athibitishe chombo gani ambacho kilikuwa kina authority ambacho kimethibitisha uchaguzi haukuwa sawa. Nashukuru. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, alikuwa anachangia Mheshimiwa Nusrat Hanje, kwa mchango wake akasimama Mheshimiwa Ali King kuonesha kwamba anachokizungumza au anachochangia Mheshimiwa Nusrat kinavunja Kanuni ya 70 ambayo inakataza Waheshimiwa Wabunge wanapotoa michango yao kusema uongo Bungeni.

Mheshimiwa Ali King ameeleza yeye kwa kuvitaja ama kwa kuzitaja taasisi alizoona kwamba zilionesha kwamba uchaguzi huo ni huru. Wakati wote tukimsikiliza Mheshimiwa Nusrat nilikuwa najaribu kusikiliza hoja yake ni ipi kwa sababu ameeleza mambo ambayo yako jumla hajasema mahsusi, kwa hiyo nilikuwa nasikiliza hoja yake nijue inaelekea wapi.

Kwa hiyo, pengine atakuwa pia na mifano kama ambavyo ziko taasisi, ama viko vyombo ambavyo vimesema uchaguzi ulikuwa huru na wa haki. Kwa hiyo, pengine viko vyombo vya habari, ama taarifa, ama taasisi zilizosema haukuwa! Kwa hiyo, mnipe fursa nisikilize mchango wake halafu nijue hoja yake inaishia wapi kwa sababu kwa sasa inanipa vigumu kidogo kutoa mwongozo mahususi. (Makofi)

Mheshimiwa Nusrat, ushauri wa jumla umesikiliza Waheshimiwa Wabunge wakichangia pande zote, hata wa huku umewasikiliza wakichangia hoja ambazo hauna uthibitisho mahususi zinatakiwa kusemwa kwa namna ambayo hutaambiwa ulete ushahidi, kwa hiyo, huo ni ushauri wa jumla, malizia ushauri wako.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi nilizungumza nikasema deep down ndani ya moyo wako kila mtu anajua kulikuwa kuna shida mahali kwenye uchaguzi wa 2020, kila mtu atajitafakari yeye na Mungu wake anajua hicho ndio nilichokizungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia labda nishauri jambo moja ambalo ndio hoja ilikuwa hiyo, kama ni kweli umeshinda kihalali na umeshinda, kimsingi sitaki kwenda kwenye uchaguzi kwa sababu Taifa linasonga mbele na kimsingi Watanzania wana matumaini makubwa na pengine namba ndogo ambayo imepatikana na watu ambao wataleta chachu fulani kwenye Bunge hili. Kwa hiyo, wacha tu mwiba utokee ulipoingilia.

MBUNGE FULANI: Taarifa.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, wacha tu mwiba utokee ulipoingilia. Kwa hiyo, kimsingi, nashauri kama kuna kesi ambazo zilitokana na uchaguzi…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nishauri, Mheshimiwa Rais kwa sababu ya hotuba yake…

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge mniruhusu hapa mbele nina majina mengi kwa hiyo hapana! Mheshimiwa Halima tafadhali! Kuhusu taarifa sitaziruhusu ili majina yaweze kuisha hapa, isipokuwa kama mtu anavunja kanuni hilo halivumiliki na Bunge kwa sababu muda tulionao ni mfupi na majina ni mengi. Mheshimiwa Nusrat. (Makofi)

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, natoa ushauri kwa Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mawaziri ambao wanahusika na masuala ya kisheria na kimahakama.

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi uchaguzi umeisha tujenge Taifa si ndio hivyo tunazungumza hivyo, sasa twende ili tusonge mbele. Kuna watu mpaka leo bado wanasumbuliwa mahakamani na kesi za uchaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba kama kuna watu wanahusika na hayo mambo waachieni watu wakafanye maisha yao, kwa nini bado wanaenda mahakamani mpaka Mheshimiwa Salome Makamba bado ana kesi ya uchaguzi, tuna kesi zipatazo 20 Mainland na Visiwani. Sasa watu wa ACT kule kuna vitu walifanya huko na nini kesi zimepunguzwa mpaka zimebaki mbili ya Nassoro Mazrui na mwenzake yule Ally Omar Shekha. Kwa hiyo, kimsingi nashauri hivyo hatuna haja waache basi watu waendelee na mambo yao unawashikilia watu kwenye kesi za uchaguzi ambao unajua uchaguzi wenyewe yaani mtu unamchukulia mkewe halafu unataka kumuua, come on! (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye jambo la pili ambalo nataka kumalizia ni kuhusiana na masuala ya mahakama. Kwenye hotuba ya mwaka 2015 ya kufungua Bunge kwa maana ya Bunge la Kumi na Moja na Bunge la Kumi na Mbili, Mheshimiwa Rais alizungumzia suala zima la mahakama na ni miongoni mwa watu ambao nimeishi kwa vitendo na ninashuhudia vitu ambavyo vinafanyika kwenye mahakama zetu na kwenye magereza zetu. Kimsingi kuna tatizo kubwa sana na yeye alizungumza na akashauri kwamba wajaribu kurekebisha mifumo ya uendeshaji kesi ili kusiwe na mrundikano wa watu wengi sana kwenye magereza zetu. Kimsingi huwezi kutenganisha magereza, wafungwa, mahabusu na mahakama. Kwa hiyo, tukizungumza mahakama maana yake haya mambo yote yanahusika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka tunapozungumza tishio la COVID na mrundikano wa watu ambao wana kesi za upelelezi za miaka zaidi ya kumi kwenye magereza ni jambo la hatari kiafya. Mheshimiwa Waziri wa Afya yupo anasikia, kule kuna changamoto kubwa na niseme, Bunge likiwa hapa watu wale wadada zetu wale wengine wanafanya shughuli zao nyingine wanakuja, wakija hapa kila siku wanakamatwa wanapelekwa hapo, mimi nimekaa hapo Isanga, wanakuja pale tunaitaga kontena jipya mpaka wanatenga cell maalum ya watu wanaoletwa ambao wanaondoka na kuja ambayo unajua huyu wiki ijayo atakuja tena kwa sababu atakamatwa tena uzururaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, labda nishauri kuna vitu vya kurekebisha, Mheshimiwa Rais sijui kama wale wanaomshauri au pia Waziri kuna jambo moja la digital platform ya kuendesha kesi, siyo lazima watu wahudhurie mahakamani, lakini pia itasaidia kupunguza mlolongo wa kesi, kwa sababu kulikuwa kuna malalamiko kwenye kipindi cha corona watu walikuwa hawaendi kabisa mahakamani kwa sababu kila mtu alikuwa anajua mikusanyiko ilikuwa haitakiwi. Walijaribu kidogo kuendesha kesi kwa kupitia digital platform zoom, Jaji huko aliko kesi zinaamuliwa, nafikiri waongezewe uwezo wafanye kazi ili tupunguze milolongo na mrundikano wa kesi kwenye magereza zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nimalizie…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa, huwezi kuanza na jambo jipya.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa nafasi. Naomba nianze kwa kutoa masikitiko yangu kwa Waheshimiwa Wabunge vijana ambao wako kwenye Bunge hili ambao kimsingi zaidi ya asilimia 60 ni vijana. Natoa masikitiko yangu kwa sababu kama vijana, tunao wajibu kama ambavyo kila kizazi kina wajibu wake, kama vijana tunao wajibu wa kulisaidia Taifa hili kwa sababu tuna Tanzania moja tu, sasa haiwezekani vijana tuko zaidi ya asilimia 60 kwenye Bunge hili lakini tunashindwa kutoa msaada kwa ajili ya kusaidia Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitoe wito kwa vijana ambao wengine wameshachangia, lakini najua wanaweza kuchangia tena kwa maandishi wakashauri yaliyo bora na mema kwa ajili ya Taifa hili. Ambao bado, nawashauri, hatuna Tanzania nyingine, tuna Tanzania hii moja, tutoe michango yenye tija kusaidia Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia kwenye Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano na Mpango wa Mwaka Mmoja…

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nusrat, nasikia kuna taarifa mahali. Hebu ngoja tuelewane kidogo. Subiri kwanza Mheshimiwa Saashisha.

Mheshimiwa Nusrat, takwimu za kuwatuhumu vijana wote humu ndani, unamaanisha hakuna kijana aliyesimama akatoa mchango! Yaani wataanzia kutoa mchango baada ya wewe kutoa mchango? Maana umeisema kwa namna kana kwamba vijana wote waliochangia, hakuna wazo walilotoa kabisa. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Afute kauli.

MWENYEKITI: Hiyo haikai sawasawa. Nanyi mnakumbuka takwimu alizozitoa Mheshimiwa Spika humu ndani. Mimi nilisikiliza michango yote, nami huhudhuria Bunge kila siku, Wabunge vijana wanafanya kazi nzuri.

MBUNGE FULANI: Alikuwa gerezani, arudishwe ndani.

MWENYEKITI: Wanaishauri Serikali, wametoa mawazo ya kuboresha maisha ya vijana. Wameeleza kuhusu mikopo, kuwekeza kwenye mitandao, kilimo na kuhusu Benki ya Vijana. Tunataka nini jamani? Mheshimiwa Nusrat, ongezea pale ambapo wenzako wamechangia. Lile ambalo wenzako hawajaliona, changia wewe, lakini usioneshe kana kwamba hakuna kijana anayetoa mchango humu ndani isipokuwa wewe. Hapana, hiyo haikai sawasawa. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Anawaza kufukuzwa kwenye chama.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nusrat endelea. (Makofi)

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Labda ningefika mpaka mwisho ndiyo mngejua namaanisha nini.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ni-recognize kwa waliyozungumza, kwa sababu kimsingi hakuna tupu iliyo tupu kabisa. Kwa hiyo, kuna waliyoyazungumza.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti,…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hanje, ngoja kwanza. Hebu tutulie kidogo.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, nimesimama.

MBUNGE FULANI: Kutachafuka humu ndani! Vijana tumeongea, tumefanya kazi kubwa! Kutachafuka humu!

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, nimesimama, kwa hiyo, mkae. (Kicheko)

Waheshimiwa Wabunge, tuelewane jambo moja. Nimeeleza hapa kwa kirefu nikiwa nimekaa. Nimelazimika kusimama kwa sababu Bunge hili watu wanaotakiwa kusimamia utaratibu ni wale wanaosimamia vikao. Na mimi nimeeleza vizuri; michango ya vijana waliopita, wa vyama vyote ambao wameshachangia, wamefanya kazi nzuri. (Makofi/Kicheko)

Hiyo michango waliyoitoa ni ya muhimu yote. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Sana!

MWENYEKITI: Hakuna kijana aliyesimama hapa ambaye hajatoa mchango wa muhimu kwenye mapendekezo haya ya Mpango. Kwa muktadha huo, ndiyo maana nimemwambia Mheshimiwa Nusrat, naye ni kijana, aanzie pale ambapo wenzake wameishia, achangie mchango wake. Yale ambayo wanaona…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Mtulie kidogo, mkitajwa majina, mnakuwa wa kwanza. Mtulie msikilize. Nikiwa nimesimama hakuna mtu anaruhusiwa kuzungumza. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Kweli! (Makofi)

MWENYEKITI: Tuelewane vizuri; na tuheshimiane. Nikiwa nimesimama, Bunge linatakiwa kutulia.

MBUNGE FULANI: Sawa.

MWENYEKITI: It is only me who should be speaking because I have the right to speak. (Makofi/Kicheko)

Kwa hiyo, nikiwa nazungumza, kila mtu anapaswa kunyamaza. Ndiyo kanuni zetu zinavyosema. Tusome Kanuni, tuzielewe ili humu ndani tuheshimiane kama tunavyoitana Waheshimiwa. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo, hoja ya kwamba hakuna tupu, tupu kabisa, hakuna Mbunge yeyote aliyemtupu humu ndani. Kila Mbunge analo jambo ambalo wale waliomtuma wanaamini atalifanya humu ndani. Ndiyo maana kanuni zinamlinda kila Mbunge anapopata fursa ya kuchangia. Nami ni kazi yangu kumlinda kila Mbunge kwa mujibu wa kanuni zetu. (Makofi)

Bunge letu hili, alishasema Mheshimiwa Spika wakati linaanza, tukiamua kuliletea dharau, tunajidharau wenyewe. Tukiamua kuliheshimu, tunalitafutia heshima sisi wenyewe. Kwa hiyo, humu ndani tuheshimiane kama ambavyo sisi tumeamua kuheshimiana na wale waliotutuma wanatuita Waheshimiwa. Kila Mbunge anao mchango wake, hakuna Mbunge aliye tupu humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Nusrat.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nizungumze, kwa sababu mipango ilikuwa imepangwa kwa miaka 15 kwa miaka mitano mitano, for the last ten years, ripoti za CAG zinaonyesha kuna failure kubwa sana katika utekelezaji wa mipango. Bajeti zinapangwa, mambo hayaendi kwa sababu…

MHE. JAQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, haijawahi kutokea Mbunge akaweka mapendekezo au akazungumza…

MHE. JAQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nusrat kuna taarifa. Mheshimiwa Jaqueline Msongozi.

MHE. JAQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nataka tu nimpe taarifa mzungumzaji anayezungumza, kwanza afute kauli yake aliyoongea kwanza, halafu ndiyo aendelee na mchango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha. (Kicheko/Makofi)

(Hapa baadhi ya Wabunge walzungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, nimeshatoa maelezo ya namna ya kwenda kuanzia hapa tulipo. Mheshimiwa Nusrat.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nilikuwa nazungumza kwamba, tunafeli kwa sababu hatuna sheria. Ibara ya 63(3)(c) inaruhusu Bunge kutunga sheria ya kusimamia mipango kwa ajili ya kusaidia uwajibikaji na kusaidia mipango kufanya kazi. Mpaka sasa for the last ten years hatujawahi kuletewa Muswada. By then mimi nimekuja lakini hakuna Muswada uliowahi kuletwa hapa Bungeni (If I am not right, kuna wakongwe watasema) kwa ajili ya kusaidia ufanikishaji na usimamiaji wa mipango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani kila siku tunapanga, tunarudi hapa kwenye kilimo. Tunaona kabisa tumetoka hatua moja, tumeenda hatua mbili mbele, tumerudi nane nyuma. Tunarudi tunasema tunapanga tena. Bajeti haiendi mathalan…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. NUSRAT S. HANJE: … bajeti ya maendeleo imetekelezwa kwa asilimia 17.55.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nusrat kuna taarifa. Mheshimiwa Ndaisaba.

MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kumpatia taarifa Mheshimiwa Nusrat. Katika maelezo yake amesema kwamba tunafeli kwa sababu hatuna sheria ya kusimamia mipango. Naomba nimfahamishe kwamba kila jambo linalotungwa; bajeti ya Serikali, lina sheria mama na lina-fall kwenye specific category ambayo ina sheria zake. Ukienda kwenye kilimo kuna sheria, kwenye maji kuna sheria, kwenye barabara kuna sheria. Sheria zile ndizo zinazoratibu utekelezaji wa mipango ya Serikali

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hiyo sheria nyingine anayotaka iibuke sheria juu ya sheria ni ya namna gani? Naomba apokee taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nusrat unaipokea taarifa hiyo?

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei hiyo taarifa kwa sababu nimezungumza kitu kingine na amezungumza kitu kingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Wabunge sasa hicho nilichokizungumza kama vijana tungeweza kusimama pamoja tukashauri Serikali ilete Muswada kwa ajili ya kuhakikisha mipango tunayoipanga, itekelezwe ili tuepuke budget reallocation, tuepuke kutokupeleka bajeti kama zinavyopangwa kwenye Bunge la Bajeti, wanapanga bajeti hazipelekwi, Mpango wa Maendeleo…

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. NUSRAT S. HANJE: … bajeti ya maendeleo kwenye kilimo imepelekwa asilimia 17.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. NUSRAT S. HANJE: …asilimia 82 haijapelekwa…

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, kwa Mheshimiwa Nusrat hii itakuwa taarifa ya mwisho. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Hussein Amar.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, mchangiaji anayeongea ni kana kwamba sisi wazee ama wenye umri mkubwa, hatustahiki kuchangia Mpango wa Maendeleo. Tumeletwa na wananchi na wametuamini pamoja na umri wetu kuja kuchangia maendeleo na kufikisha mipango yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa, vijana wanataka kuleta ubaguzi wakati tumeongoza kwenye kura kwa asilimia nyingi pamoja na umri wetu mkubwa. (Makofi)

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, tumsikilize. Mheshimiwa Nusrat, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mzee wangu shikamoo! (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaheshimu wazee wote, lakini tunafahamu hata Wamasai wapo humu ndani, morani; huwezi kufananisha age. Yaani hiyo age conflict. Ila nawaheshimu sana wazee wangu. Mpo! (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nazungumza kwamba bajeti ya maendeleo kwenye kilimo haijaenda kwa asilimia 82. Tuna shida ya mbegu kwenye Taifa, tuna tatizo la mbegu kwenye Taifa, lakini Serikali imetenga mashamba tisa ya kuzalisha mbegu. Ni shamba moja tu ambalo linazalisha mbegu, linafanya kazi mwaka mzima. Mashamba mengine yote nane yanategemea kilimo kwa kudra za Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwenye jambo moja. Mheshimiwa Spika juzi alivyokuwa kwenye kiti alitoa mfano akasema anatamani tupate kitu cha ziada kuwasaidia vijana wetu, anachukia kuwaona wako kwenye pool table. Naomba ku-declare interest, mimi ni Mwalimu. Kama nchi, tuna tatizo kwenye elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika elimu, watoto wetu wanakosa vitu vitatu vya msingi na Waziri wa Elimu yupo asikilize. Elimu yetu haina career guidance, haina personal development. Leo tunazungumza soft skills, wasomi wengi wanaotoka vyuo vikuu, inawezekana nikiwemo mimi na wengi wetu humu na wengine wako nje, tunakosa vitu vya msingi. Tunafundishwa kwenye Civics Communication Skills, tunafundishwa self-esteem, self-confidence na nini, lakini tunashindwa ku-connect na maisha halisi. Ndiyo maana kuna motivation speakers. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kaka yangu Mheshimiwa Eric Shigongo yule pale anaelewa, ndiyo maana leo kuna motivation speakers wengi kwa sababu tunashindwa, yaani hatuwezi ku-connect maisha ya shule na nini kipo mtaani, ndiyo maana watu hawawezi kujiongeza. Falsafa ya Kuanzia sokoni, watu walitakiwa wajifunze shule, siyo wanamaliza shule, ndiyo wanatoka wanakuja kuambiwa kwenye biashara tuanzie sokoni. No!

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna kitu kingine cha msingi tunakosa. Leo Waheshimiwa Wabunge wanakalishwa chini wanafundishwa investment, shule wanasoma pesa, lakini hawasomi financial management; elimu yetu inakosa financial management; tunasoma Book Keeping na Commerce (makabati), haina reality kwenye ukweli. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naweza nikatoa mchango wangu pia kwenye maandishi kuhusiana na elimu; nishauri kwa sababu kila mtu ana akili (everybody is genius), lakini if you judge a fish by its ability to climb a tree, anaishi maisha yake yote hajui kama yeye ana akili. Kwa hiyo, naweza nikashauri hiyo kwa sababu natamani kuona tunafika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, naishia hapo. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwanza kwasababu ni mara yangu ya kwanza tangu tumepata janga kubwa la Taifa kuzungumza hapa nitoe pole kwa Watanzania wote kwa msiba mkubwa tulioupata wa kuondokewa na Mheshimiwa Rais, lakini pia nitoe pole kwa Mheshimiwa Rais mteule Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuondokewa na Mheshimiwa Rais ambaye yeye alikuwa msaidizi wake wa kwanza na wa karibu sana.

Mheshimiwa Spika, lakini pia nimpongeze Mheshimiwa Rais mteule Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mwanamke wa kwanza Afrika Mashariki kwa kuwa Rais.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Philip Mpango kwa kuteuliwa kwa mujibu wa Katiba kuwa Makamu wa Rais wa Tanzania, lakini pia niwapongeze Waheshimiwa Wabunge kwa kuendelea kuwa pamoja na nchi yetu kutokana na kipindi ambacho tumepitia cha mpito na mambo magumu ambayo tumepitia.

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie na nitachangia kwenye Sekta za uzalishaji na nitajikita katika sekta ya kilimo, kwasababu Kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa letu na tunajua tumekuwa tukitumia kauli hiyo tangu tunasoma; lakini pia practicability yaani utekelezaji wa maendeleo ya Taifa tunategemea sana kilimo kwa sababu kama tunazungumza Tanzania ya Viwanda na kama mwelekeo wa Serikali maana yake hatuwezi kuzungumza viwanda bila kilimo.

Mheshimiwa Spika, na kwa Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamekuwa wana champion hoja ya kilimo, kwabababu utakumbuka hata mzungumzaji aliyepita amezungumza pia kilimo, na ninajua Waheshimiwa Wabunge wengi sisi kama nchi wengi tunajua tunalima kwa namna tofauti tofauti, lakini pia tunajua umuhimu; wake, kama ambavyo Mwenyekiti wa Kamati ametoka kuzungumza. Kwamba tunahitaji malighafi kwa ajili ya viwanda vyetu kwasababu tunategemea malighafi za ndani sasa hauwezi kuzungumza malighafi za ndani bila kuzungumza kilimo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa pekee sana kwa mujibu wa ripoti ya CAG na mambo ambayo amechambua kwenye ripoti yake, ukiangalia mpango wa kwanza na wa pili kwasababu tunazungumza Mpango wa Tatu lakini wakati tuko sasa hivi lazima tukumbuke tulikotoka kwa hiyo, kwenye suala zima la kilimo kuna mambo kadhaa ambayo CAG katika ukaguzi wake ameyaona.

Mheshimiwa Spika, mathalani nitayazungumzia hayo huwezi kuzungumza kilimo bila kuzungumza mbegu, sasa kama Taifa tulikubaliana kwamba tutakuwa na mashamba tisa ya kuzalisha mbegu lakini ukweli ni kwamba kwa mujibu wa ripoti ya CAG mpaka sasa ni shamba moja tu ambalo linafanyakazi mwaka mzima lakini mashamba mengine nane yanategemea msimu wa mvua kwa hiyo yako kwa mujibu wa msimu. Sasa hatuwezi tukazungumza kwamba tunataka tufanye kilimo kiwe sekta ambayo ni stable wakati hatuzungumzi tunapataje mbegu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunahitaji mashamba yote tisa ambayo yametengwa kwaajili ya kuzalisha mbegu nchini yafanye kazi yote mwaka mzima bila kusubiri msimu wa mvua kwasababu ripoti ya CAG inasema tunategemea shamba moja ambalo linafanyakazi mwaka mzima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwenye nchi ambayo asilimia kubwa tuna water bodies tuna maji kwa asilimia kubwa sana kwenye nchi yetu ardhi ya Tanzania hatuwezi tukawa tunategemea mvua watu wanatushangaa kwasababu kuna vitu tu haviko sawa kwenye scheme za umwagiliaji kwasababu ili uweze kufanya uzalishaji kwa kutumia umwagiliaji lazima utengeneze scheme za umwagiliaji zifanye kazi ili uweze kufanya kilimo especially cha kuzalisha mbegu kwasababu mashamba tisa kama nchi ni mashamba machache sana ambayo tunaweza tukatengeneza utaratibu mzuri na tukayahudumia mwaka mzima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kama nchi ripoti ya CAG inatuambia ni 39% tu ya pembejeo za kilimo zimegawiwa yaani ugavi kwenye pembejeo za kilimo ni 39% tu. Sasa unategemea Taifa lizalishe malighafi kwaajili ya viwanda vyake kwa Tanzania ya viwanda halafu unafanya ugavi wa pembejeo za kilimo kwa 39% tu. Kuna jambo Wizara na Waheshimiwa Wabunge kuna jambo lazima tukubaliane kwamba kama tumeamua kwamba tunatengeneza Tanzania ya viwanda ni lazima tukubaliane suala zima la kilimo ndiyo msingi na ni lazima wote ikiwezekana tuzungumze kuhusu kilimo. Kwasababu ndiyo tutapata malighafi kwaajili ya viwanda vyetu lakini ndiyo sehemu ambayo itatusaidia sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwasababu sasa hivi mwenyekiti wa kamati amezungumza kwamba sasa hivi tunalima kilimo cha kujikimu yaani watu wanalima sana ni kwaajili ya kuendeleza maisha kwamba wapate chakula waishi lakini kwa ardhi ukubwa wa ardhi ambao tunao kwenye Taifa letu lakini water bodies ambazo tunazo kwenye Taifa letu, resourcefully ya wasomi na watu ambao wana profession za mambo ya agriculture Taifa letu limebarikiwa sana tunatakiwa tutoke huku tuende sehemu nyingine zaidi kwenye kuboresha kilimo chetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa ripoti ya CAG inatuambia ni 1% tu ya wakulima wamepatiwa mafunzo na mbinu bora za kilimo sasa asilimia moja tu wamepatiwa mafunzo ya mbinu bora za kilimo. Kuna jambo hapa haliko sawa, na hii ni kwa mujibu wa ripoti ya CAG na wapo maana yake watu wanaelewa nini tunachokizungumza. Bahati nzuri nina imani kubwa sana na Mheshimiwa Naibu Waziri pale kwasababu mara nyingi ndiyo tumekuwa tunamuuliza hata yeye maswali na yeye anajibu na anafuatilia Mheshimiwa Hussein Bashe. Kwa hiyo, kwasababu lengo letu ni kujenga na hii nchi ni ya kwetu maana yake hakuna mtu atatoka huku aje kutuambia tunajengaje nchi yetu hapa ni sehemu ambayo ni lazima tuweke nguvu Mheshimiwa Waziri yupo na Mheshimiwa Naibu Waziri pia yupo na Mheshimiwa Naibu Waziri pia yupo tuangalie tunafanyaje kwenye suala zima la kilimo na kimsingi mimi ni wa Singida kwetu tunalima alizeti, na tunalima kweli kweli alizeti kwa hiyo, ni declare interest kwamba mimi pia ni mkulima Pamoja na kwamba tunalima kwa simu. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kwenye upande wa pili nitoe mapendekezo labda nini kifanyike kwaajili ya kuhakikisha kwamba pengine utekelezaji wetu wa mipango ukiangalia mpango wa kwanza na mpango wa pili ni lazima tukubali kwamba kuna sehemu inawezekana haiko sawa ndiyo maana unakuta tunapanga bajeti za sekta za uzalishaji halafu hazitekelezwi kama tunavyopanga kama Bunge linavyopanga.

Mheshimiwa Spika, labda nitoe mapendekezo yafuatayo, pendekezo langu la kwanza napendekeza kuwe kuna sheria maalum kwasababu ni miaka 10 imepita mpango wa kwanza na Mpango wa Pili tunajadili Mpango wa Tatu phase ya mwisho ya miaka mitano ili itimie 15 tunaianza. Kwa hiyo, na nikiangalia hata nikisoma documentation na nini na Waheshimiwa Wabunge ambao ni wazoefu nyinyi mtalizungumza hili vizuri hatuna sheria mpaka sasa hivi ya kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kama tunakaa tunajadili na tumekuwa tunajadili kuhusu mpango sisi wengine tumekuja juzi siyo wenyeji sana lakini kama tunapanga vitu ambavyo hatuvitungii sheria ya utekelezaji maana yake baadaye tunashindwa kujibana yaani tunashindwa kwamba tutabanana wapi kwasababu kama kutafanyika bajeti reallocation hakuna sheria ya kutu-guide kwamba sasa tumepanga mpango huu tunatumia sheria gani kusimamia utekelezaji wa mipango hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nishauri uletwe muswada wa sheria Bungeni tutunge sheria ya kusimamia utekelezaji wa mipango tunayoipanga kama Wabunge, kwasababu sisi ni watu wazima tuna akili zetu na kuna watu ni wasomi sana hapa na kuna watu wana mawazo mazuri sana lakini hatuna sheria ya kutu-guide kwamba sasa tunatekelezaje mipango tuliyojiwekea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili naweza kushauri ni kwamba sisi kama Wabunge sasa hivi tuko kwenye Bunge la Bajeti tunapanga bajeti na kuna bajeti ambazo tunajua kabisa kwamba Bunge hili ndiyo linatoa muelekeo wa Taifa kwenye masuala la bajeti. Lakini kama tunapanga bajeti za miradi ya maendeleo halafu hazitekelezwi katika kiwango ambacho Bunge limepanga maana yake ni kama vile kuna kukosekana nguvu kwa upande mmoja. Kwa hiyo, nishauri tunapokaa kama bunge tukapanga bajeti zinazokwenda kwenye miradi ya maendeleo tunaomba bajeti zitekelezwe kadri ambavyo Bunge hili limepanga kwasababu hiki ni chombo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hiki ni chombo ambacho kinakaa na tunatumia fedha na tunatumia muda kupanga kwa hiyo hatuwezekani tukiwa tunapanga halafu bajeti hazitekelezwi kama ilivyo na kimsingi sheria ndiyo itatusaidia kwasababu hata bajeti reallocation haitakuwa sana kwasababu kama sheria itatulazimisha kwamba kusifanyike bajeti reallocation especially kwenye miradi mikubwa ya maendeleo ambayo tutajiwekea kufanya kama Taifa.

Mheshimiwa Spika, lakini pia jambo la mwisho naweza kushauri kuwe na uwajibikaji na kimsingi watu wanajitahidi katika kufanya wajibu wao lakini kwenye masuala la fedha kuwe kuna uwajibikaji endapo tunapanga tunapangiana program za kufanya na project za kufanya basi watu kuwe kuna uwajibikaji mkubwa kwenye masuala ya fedha ili kuwe kuna accountability kuwe kuna patriotism ule uzalendo mtu anauona kwamba sasa mimi hili ni jukumu langu kufanya jambo hili.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwasasa nimechangia hapo. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie katika Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia na nitaomba niseme yafuatayo kwanza. Wanafunzi wanaweza kuwa 20% tu ya population yetu. Yaani students may be 20% of our population, but they are 100% of our future. Kwa sasa tunaweza tukaona wanafunzi kama sehemu tu, kwa sababu ni sehemu ndogo ya jamii yetu, lakini kwa maisha yetu yajayo, wanafunzi ndio watakuwa sisi, yaani watakuwa 100% ya population yetu. Maana yake kuna umuhimu mkubwa sana wa kuwekeza nguvu zetu na uwezo wetu wote kwenye mfumo wetu wa elimu Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Sera ya Elimu ya mwaka 2014 dhima yake ni kuwa na Mtanzania mwenye maarifa, ustadi, umahiri, uwezo, na mtazamo chanya katika kuchangia maendeleo ya Taifa. Sasa katika mambo haya ambayo tunasema ndiyo dhima ya elimu katika Sera ya Elimu ya mwaka 2014, hatuwezi kuyazungumza haya bila kutaja ubora na kuboresha mfumo wetu wa elimu.

Mheshimiwa Spika, nitazungumza kidogo kuhusu udhibiti ubora. Ripoti ya CAG inaonyesha kwamba kumekuwa na upungufu mkubwa sana wa udhibiti ubora kwa 8%, baadhi walishazungumza. Tumepeleka wadhibiti ubora 98 kati ya 1,306 ambayo ilikuwa ndiyo kusudio. Sasa kwa kutekeleza hili, maana yake hawa ndio wanaoenda kuangalia ubora wa elimu yetu. Sasa tumetekeleza kwa 6% tu, ni jambo ambalo linavunja moyo kiasi kubwa. Kwa hiyo, hata kama kuna mambo makubwa tunayapanga, lakini katika ufuatiliaji, tunawategemea watu ambao ni wadhibiti ubora kwa ajili ya kwenda kuangalia utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, hili siyo jambo la kihisani, ni suala ambalo liko kisheria. Katika Sheria ya Vyuo Vikuu ya Mwaka 2005 kifungu cha 27 inaeleza hayo, lakini pia katika Sheria ya Baraza la Elimu ya Ufundi ya Taifa (NACTE) ya Mwaka 1997 Kifungu (5) na (1) kinavitaka Vyuo Vikuu na Vyuo vya Ufundi kuwa na utaratibu na kujiwekea miongozo ya kudhibiti ubora ili kuhakikisha kwamba elimu yetu inayotolewa Tanzania kweli iaakisi 100% ya population yetu ya Taifa in the future, ambayo future hatuzungumzi miaka 3,000 ijayo.

Mheshimiwa Spika, hawa hawa wanafunzi baadaye watakuja kuwa Mawaziri na watakuja kuwa watendaji. Sasa ubora wa elimu yetu tunategemea hawa watu wakadhibiti, lakini tumeweza kwa 8% tu jinsi ambavyo hatuweki nguvu katika udhibiti ubora. Ni jambo ambalo linasikitisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nizungumze kidogo kuhusiana na mtaala. Kwanza ni-declare interest, mimi ni mwalimu professionally. Nimeona wivu kidogo, kuna wenzangu wameanza kuchangia wameitwa Walimu; kwa hiyo, kwenye record yako naomba iingie kwamba nami pia ni Mwalimu. (Makofi)

SPIKA: Mwalimu Nusrat Hanje. Nashukuru tumefahamu sasa. (Kicheko/Makofi)

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza elimu yetu ina tatizo kubwa sana. Kimsingi ninakusudia kuleta maelezo binafsi kwenye Bunge hili kushauri kama miongoni mwa watunga sheria kwenye Bunge hili Tukufu namna ambavyo elimu yetu inaweza kusaidia vijana wetu na hasa ambao tunategemea watakua 100% of our future. Elimu yetu inakosa mambo matatu ya msingi. Inakosa kitu kinaitwa Person Development. Juzi Ijumaa niliuliza swali kwenye Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia kuhusiana na kufanya topic ya life skills kuwa somo kuanzia Darasa la Tano mpaka Form Four na tutaangalia Form Five na Six tuone namna bora ya kujenga uwezo wa kibinadamu, uwezo na utashi wa kimtu, kwa sababu ndiyo dhima ya Sera ya Elimu ya Mwaka 2014, ambayo inataka kujenga Mtanzania mwenye maarifa, ustadi, umahiri na uwezo na mtazamo chanya katika kuchangia maendeleo ya Taifa. Sasa tunakosa kitu kinaitwa personal development. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushawahi kutoa tafakuri tunduizi hapo hapo kwenye kiti chako kwamba unashangaa kwamba Watanzania hatuna uaminifu? Kwa nini mtu anaaminiwa afanye kitu na anashindwa ku-perform kama ambavyo aliyemwamini amempa wajibu huo? Hilo siyo katika biashara tu, kuna vitu vingi ambavyo Watanzania; vijana wanaotoka vyuoni wanashindwa ku-perform.

Mheshimiwa Spika, leo watu kama Marehemu Ruge, kwa kweli tunatambua mchango wake mkubwa kwenye Taifa hili, anaonekana ni genius. Everybody is genius, but if you judge a fish by its ability to climb a tree it will live its whole life believing it is stupid. Yaani kila mtu ana akili, lakini kama tutamhukumu samaki kwe uwezo wake wa kupanda mti, hataweza kushindana na nyani. Nyani ana uwezo wa kupanda mti kuliko Samaki. Samaki anaweza kuogelea. Kwa hiyo, samaki ana uwezo wa kuogelea, kwa hiyo, anatakiwa apelekwe baharini na nyani apelekwe kwenye miti kwa sababu ndiyo ana uwezo huko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mfumo wetu wa elimu unawafanya watu baadhi wenye mawazo mbadala kwa sababu ya kujipa maarifa kwingine waonekane wana uwezo mkubwa. Tumeshasema, ili ulime kilimo cha biashara, ni lazima uanzie sokoni, ukajue soko linahitaji nini ndiyo ukalime. Huwezi kulima ndiyo ukatafute soko. Sasa mtu akizungumza hivi, anaonekana ni genius, lakini ni suala ambalo tunatakiwa tu-train vijana wetu kwenye Taifa, kwenye personal development; uwezo wa kuthubutu. Tuna tatizo la kubwa la uthubutu. Watu hawawezi kuthubutu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, nitaleta maelezo binafsi kuelezea kwa nini tunasema vitu vitatu vinakosekana katika elimu yetu? Jambo la pili ambalo linakosekana ni kitu kinaitwa financial literacy. Sisi walimu tunafundisha shuleni financial knowledge, ndiyo tunafundisha accounts, yaani mtu anafundishwa kufugua makabati; anatakiwa akajibu mtihani ili aonekane ana akili, afaulu aende darasa la mbele. Leo ninyi hapa Bungeni tulivyoapishwa tu, tuliletewa wataalamu wa fedha waje kutushauri how much do we spend? How much do we invest? How much do we save? How should we donate? Spirit ya donation watoto wanatakiwa wafundishwe kwenye nchi hii. Tunatakiwa tuanze ku-train vijana wetu wakiwa mashuleni financial literacy, siyo financial knowledge. Financial Knowledge inamfanya akajibu mitihani afaulu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la tatu, ambayo elimu yetu haitupatii, ni kitu kinaitwa Career Development, amezungumza Mheshimiwa Mpina, ambayo inamfanya kijana aliyepo shuleni ajue, akutane na watu ambao wanafanya kitu ambacho anatamani kukifanya. Siyo mimi nina kipaji cha kucheza mpira, lakini kwa sababu sijawa trained vizuri, mimi role model wangu anakuwa mwanasiasa, come on! Yaani tunatakiwa tuwa-connect vijana wetu na watu ambao wana- inspire kwenye maisha, tangu wakiwa shuleni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vitu tatu vya msingi, kama kuna mwalimu humu katika walimu uliowataja au wataalamu ma-professor ataniambia hivi vitu vinapatikana kwenye mfumo wetu wa elimu, basi nitakuwa nimekosea, lakini kwa sababu ninajua hivi vitu tunavisoma tukitoka; kuna watu wanaitwa motivational speakers mnawajua, ndiyo vitu wanavyovizungumza, ni hivi hivi kwa sababu wanajua mfumo wetu wa elimu hauwapi hivi vitu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfumo wetu wa elimu upo Paper Oriented. Duniani model ya elimu bora kabisa duniani, the best education system in the world ni ya Finland. Kuna watu wanazungumza kuhusu China; kwenye uchumi, sawa ni China kwa sababu tunaona performance outcome yake, lakini the best education system in the world ni ya Finland. Wameweza kufanikiwa kwa sababu watoto hawafanyi mitihani. Standardized testing; kuna watu wamefeli Form Four, lakini leo ndiyo billionaires. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna waliofaulu sana tunawajua sana ma-professor wapo hapa, tunakutana nao huko na nini, tunashukuru, tunawapongeza kwamba mmesoma na nini, lakini tunawajengea watoto wetu uelewa mbaya kuhusiana na nikifeli, maana yake sina uwezo. Yaani mfumo wa elimu unanilazimisha mimi hata kwa cram, hata kwa kuibia, ndiyo maana tuna watoto wanamaliza Darasa la Saba hajui kusoma na kuandika na utashangaa amefanya mtihani kafaulu. Vipi? Kumbe kuna watu wana vipaji vya kupiga chabo. Mnajuwa chabo!

Mheshimiwa Spika, Chuo Kikuu tulikuwa tunasema kudesa. Kuna watu wana uwezo wa kudesa, anafaulu, lakini hana uwezo. Yaani the output, material ambayo inatoka chuoni haiwezi kuwa challenged kwa sababu iko very low. Yaani ile output ya kutoka vyuoni bado kuna shida kwa sababu tupo Paper Oriented.

Mheshimiwa Spika, bado kuna tatizo kubwa sana la…

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mwenye taarifa endelea, Mheshimiwa Saashisha.

T A A R I F A

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, kwanza nataka nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge anavyochangia madini ya kutosha hapo, lakini nilitaka nimpe taarifa tu kwenye eneo aliosema la career development kwamba kwenye hoja yake sasa ni vizuri career development ikaingizwa kwenye kozi za ile tunasema ni seven, four, two, three plus. Ile mwaka wa mwisho, career development ifundishwe hapo.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu msemaji anayeendelea kuzungumza, kama hayatafundishwa, wanafunzi wanafika chuoni ndiyo wanaanza kujadiliana, anayemaliza Form Six, wewe unataka kwenda kusoma nini? Mwanasheria; au mwingine baba yake kwa sababu alifanya vizuri kwenye Hesabu, anamwambia kasome Hesabu, lakini kuna kitu kinaitwa core curriculum. Kama haya mambo yote yakiunganishwa na hii career development, hata watoto wanapomaliza kwenye ile seven ya mwisho, wafundishwe kwamba wewe kwa namna ulivyo, tunavyokuona, tunadhani uende hivi na utashi ulionao kwa kuzingatia mawazo ya watoto.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilitaka nimwongeze tu kwamba career development ni sehemu muhimu sana ya kubadilisha na ku-transform mindset za wasomi wa nchi hii. Ahsante. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Nusrat, unapokea ushauri huo?

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, napokea. Kimsingi nampongeza pia aliyezungumza. Pia, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa sababu wakati nauliza swali alisimama mwenyewe akasema kwamba atafungua mjadala kwa ajili ya wadau kutoa maoni yao. Nafikiri hayo pia ni sehemu ya maoni ambayo tutayatoa. Kwa hiyo, naipokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie katika eneo moja. Wakati tunarekebisha mitaala yetu tukumbuke kwamba kuna wale vijana ambao wanamaliza shule ya msingi wanashindwa kuendelea na Sekondari na kuna wale wanaomaliza form four wanashindwa kuendelea na elimu ya juu zaidi; wale kwenye mtaala wetu tuwawekee utaratibu ambao katika stadi za kazi wanazosoma shule wakafundishwe vitu kutokana na uchumi wa maeneo yao husika.

Mheshimiwa Spika, mathalani, maeneo ambayo kuna migodi… (Makofi)

(Hapa sauti ya Mhe.Nusrat S. Hanje ilikauka)

SPIKA: Pole sana Mwalimu. Hakuna maji karibu hapo! (Kicheko)

MBUNGE FULANI: Amefunga.

SPIKA: Amefunga loh! Pole sana. (Kicheko)

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba nimalizie taratibu taratibu. Maeneo ambayo labda kuna migodi, maziwa na mito ambapo tunategemea watu wa pale wengi ni wavuvi...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Naambiwa ya pili tayari. Basi sentensi moja tu.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, basi tunategemea pia wale wananchi na wanafunzi wanaopewa elimu katika maeneo husika, basi wakafundishwe kwa sababu wengi wakimaliza wanashindwa kuendelea na vyuo, wanarudi mtaani, halafu wanaanza kujifunza upya kuhusu kilimo, kuhusu uvuvi, kuhusu uchumi unaopatikana kwenye hilo eneo. Kwa hiyo, stadi za kazi zikafundishwe kutokana na uchumi wa eneo husika ili wale vijana wanaoshindwa kuendelea na vyuo waende kufanya shughuli za uzalishaji mali katika maeneo husika. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kwanza niungane na mzungumzaji aliyepita kuhusiana na mchango wa teknolojia na ukuaji wa teknohama katika ulimwengu. Pia, sisi kama Taifa, kama sehemu katika ulimwengu miongoni mwa washiriki katika maendeleo makubwa sana ya sayansi na teknolojia, hatuwezi kuishi kama kisiwa. Kwa hiyo, ni lazima kama nchi kwa pamoja tukubaliane kwamba tunapozungumza uchumi wa kidijitali, digital economy kwanza siyo terminology mpya, siyo neno jipya, pia siyo myth, yaani ni kitu ambacho kinaishi na kinafanyika kwa sababu nchi za wenzetu duniani sasa hivi wanazungumza kuhusu digital economy. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunazungumzia digital economy au uchumi wa kidijitali, hatuwezi kumaliza bila kuzungumzia miundombinu. Kwa hiyo, tunapongeza jitihada kwa sababu kimsingi sisi kama nchi mkiangalia hata namna ya utekelezaji wa mambo yetu, bado tuko kwenye makabrasha sana. Ndiyo maana hata Bunge hili ni miaka michache tu iliyopita ndiyo tumeingia kwenye teknolojia, hata tunatumia vishikwambi sasa hivi. Tuna mabunge mawili nafikiri ndiyo tumeanza kutumia vishikwambi. Kwa hiyo, maana yake ni lazima pia tukubali kwamba tulikuwa somewhere behind kwa sababu dunia ilishakwenda huko ambako sisi tuna-struggle kwenda ama tuko sasa hivi tunapambana kufika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napongeza kwa namna yao Wizara na Serikali kwa upande fulani wamejitahidi sana, kwa sababu mpaka sasa hivi wameshaunganisha Makao Makuu ya Mikoa 26 na Wilaya 42. Wamejitahidi, tunakwenda kwa maana ya connectivity, kwenye miundombinu ya kusaidia Watanzania kufikiwa na huduma za kimtandao. Pamoja na hayo, bado tuna changamoto kubwa sana, kwa sababu wananchi asilimia 68 maeneo wanayoishi wana uwezo wa kupata huduma za mtandao (internet), lakini ni asilimia 26 tu ndio ambao wanaweza kufikia (access) kupata huduma ya mtandao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua mpaka uwe na simu janja ndiyo unaweza ukatumia internet. Kwa hiyo, ni asilimia 26 tu. Wakati Serikali inajaribu kuweka miundombinu na kuhakikisha kwamba wananchi wanapata huduma ya kimtandao, bado wananchi wetu sisi kufikia kumiliki vifaa vyenye uwezo wa ku-access internet, bado ni asilimia ndogo sana. Kwa hiyo, hii inatuelekeza kwamba hata tunavyozungumza digital economy bado kuna sehemu tuko nyuma. Kwa sababu ili tuweze ku-access digital economy ni lazima wananchi wetu wawe wana vifaa vyenye uwezo wa kutumia hizo internet ambazo tunazizungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila mtu anafahamu kwamba simu janja gharama yake ni kubwa mno. Kwa hiyo, wananchi wengi unakuta wana simu ndogo tu ya kutumia, lakini kupata kifaa au kupata simu ambayo inaweza kumpa access ya kuweza kutumia internet, wengi bado hawana uwezo huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa Wizara na Serikali kwa namna yao waangalie namna gani wanaweza wakapunguza gharama ya vifaa hivi vyenye uwezo wa ku- access internet ili wananchi wetu wengi waweze ku-access internet, waweze kupata taarifa nyingi sana ambazo zinapatikana kwenye mitandao na faida kubwa inayopatikana kwenye suala zima la digital economy. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hata wale ambao wana vifaa vyenye uwezo wa ku-access internet, bado kuna gharama kubwa sana za data ambazo zinasababisha hata Serikali ikose mapato kwenye kiwango ambacho ilistahili kupata. Mpaka sasa kuna ongezeko kubwa sana la matumizi ya data asilimia 35, lakini Serikali inapata asilimia 16 tu kwenye pato la Taifa kutokana na matumizi ya data. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba najua kuna Tume inaitwa Tume ya TEHAMA, nafikiri miongoni mwa jukumu ambalo naweza kushauri, waongezewe, wapewe uwezekano wa ku-regulate, kuhakikisha kwamba makampuni ya simu yenye kupewa jukumu na TTCL kwa ajili ya kusaidia wananchi kupata internet, waweze ku-regulate. Kwa sababu unaweza kujiuliza kwa nini data ni asilimia 35, lakini asilimia 16 tu ndiyo tunayochangia kwenye pato la Taifa. Maana yake kuna tofauti katika utoaji wa huduma za data. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, maana yake ile Tume sasa ya TEHAMA itusaidie kuwa na segment at least ya kushauri na kuangalia namna wanaweza ku-regulate ili bei zisiwe tofauti sana. Kwa sababu, pamoja na kwamba ni huduma, tunajua pia wanafanya biashara, lakini isifike hatua kwamba wanawaumiza wananchi, wanashindwa ku-access.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili nami nina direct interest kwenye upande wa vijana, kwa sababu, ni ukweli usiopingika kwamba watumiaji wengi wa mitandao ni vijana. Mheshimiwa Jenista Mhagama anajua tatizo kubwa la ajira nchini, pengine vijana wengi wangekuwa na uwezo wa ku- access internet kwenye vifaa pamoja na data, wangekuwa na uwezo mkubwa pia hata wa kujiajiri. Nitakwenda moja kwa moja kwenye namna ambavyo kama Taifa, kama vijana tunaweza kupunguza tatizo la ajira na kusaidia vijana wetu kwenye kujiajiri na tukaishi kwa vitendo katika digital economy. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila mtu sasa hivi anafuatilia kwenye mitandao anaona kuna debate kubwa kuhusiana na namna ambavyo wasanii wetu wanatengeneza pesa kwenye viewers you tube. Tunaishi kwenye ulimwengu ambao ni tofauti sana, inawezekana vitu vingine watu wakashangaa kabisa. Ukiwa na viewers milioni moja katika YouTube una uwezo wa kupata USD 5,000. That is money na hauhitaji subscribers; unahitaji u-post content You Tube ili watu waka-view content yako ili you tube waweke matangazo kwenye channel yako upate pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa vijana wengi sasa hivi hawaelewi hiki kitu ndio maana mpaka sasa hivi wana-discuss kwamba, inawezekana kweli watu wanatengeneza viewers YouTube; kwamba Diamond katoa nyimbo siku mbili tu ina viewers milioni 10! That is money, that is money. Yaani hiyo ni pesa, kwasababu, YouTube wanaweka matangazo yao kwenye ile video. Wakishaweka hayo matangazo yao, wewe wanakulipa pesa.

Mheshimwia Mwenyekiti, mwaka 2018 kuna kijana mdogo wa miaka saba anaitwa Riyans’ Toys Review, ana- post midoli; ndio alikuwa anaongoza YouTube, analipwa milioni 22 USD. Sasa hivi nafikiri ana miaka 12 ama 10 hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tuna Jeffry Star analipwa dola milioni 200 net worth yake na alikuwa ame-bankrupt kabisa. Huyu content yake anatangaza bidhaa za urembo. Actually ni mwanaume, lakini anafanya mambo ya entertainments. Kwa hiyo, ana bidhaa za make up, anaimba music. Kwa hiyo, ana-post YouTube halafu anatengeneza subscribers.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna robots wanatengeneza subscribers YouTube. Wale subscribers wanakusaidia kuita watu waka-view content yako YouTube. Waki-view content yako YouTube wewe unapata pesa kwa sababu YouTube wanaweka tangazo kwenye account yako na you get paid, lakini kuna procedure za kufuata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wengi wa Kitanzania hawajui kwamba you can get paid by just posting your content. Hata Wizara ya Maliasili na Utalii…

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MWENYEKITI: Taarifa.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa taarifa tu mzungumzaji kwamba anachosema ni kweli asilimia 100. Wasanii wetu wa Tanzania hawajui ku-monetize, kugeuza viewers wao kupata fedha, matokeo yao wanafanyiwa na Wakenya. Kwa hiyo, fedha zinaenda Kenya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampa taarifa tu mzungumzaji. (Makofi)

MWENYEKITI: Haya Mheshimiwa Nusrat, taarifa hiyo umeipokea?

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeipokea. Tuseme tu kwenye hilo, hata Kiswahili, Wanaijeria wananunua online vitabu vya kufundisha a, e, i, o, u Dar es Salaam kwa shilingi 500/= wanaenda kufundisha watu Kiswahili YouTube na they get paid for that, nasi tumezaliwa na Kiswahili na tunakuwa nacho na tunakiangalia. We don’t know how to get money on it. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitoe kama changamoto; kwanza kwenye uwasilishaji wa juzi wa TCRA, Mheshimiwa Waziri na watu wako wa TCRA kweli mmeleta wasilisho zuri. Kwenye issue ya maudhui, pamoja na capacity building mnahitaji kufanya capacity building kwa vijana wengi ili tuache sasa, tutoke kwenye ku-complain watu waende waweke content. Kwa sababu, hawa waliotengeneza hizi pesa kwanza wengi ni watu ambao hawana hata kazi rasmi, ni watu wanaoishi tu nyumbani, unahitaji tu kuwa full time YouTube, unahitaji tu kuwa na kitu cha ku-post, kwa sababu money is the reward after solving somebody’s problem. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tajiri namba mbili anayelipwa pesa nyingi YouTube, ana-post video games, yeye ndio anacheza games; zile play station, anaji-record reaction yake wakati anacheza na ana-post na watu wanakuwa inspired, wanakwenda ku-view. Sasa hiyo ni pesa. Watu wa utalii wanahitaji kutangaza utalii. Sisi kama nchi tunahitaji kutangaza, lakini sijui kama Wizara ya Utalii wana YouTube Channel. We need YouTube Channel for that. Tunahitaji kuwa na YouTube Channel kutangaza nchi yetu. (Makofi/Kicheko)

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MWENYEKITI: Taarifa, Mheshimiwa Shangazi.

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda tu kumpa taarifa Mheshimiwa Nusrat kwa mchango wake mzuri kwa vijana wetu, lakini nimwambie tu kwamba kwa hapa Tanzania mwanamuziki Nassib Abdul Diamond Platnum analipwa kuanzia kati ya dola 75,000 mpaka 100,000 kupitia YouTube. (Makofi)

MWENYEKITI: Haya Mheshimiwa Nusrat, taarifa hiyo.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa maana ya nia njema ila namshauri pia Mheshimiwa Shangazi akaangalie vizuri kwa sababu hii ni updated na Diamond hayuko kwenye list. Hata hivyo is a good thing, kwa sababu kama anaweza aka-hit viewers wengi kwenye muda mfupi sana, maana hiyo ni opportunity kubwa sana.

MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MWENYEKITI: Ehe taarifa.

MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, anachokisema Mheshimiwa Nusrat ni sahihi kabisa. Regulator wa YouTube yuko Kenya, kwa hiyo, anatujengea hoja kwamba tunapoteza mapato mengi kwa sababu regulator wa YouTube Tanzania kwa hao wanaolipwa yuko Kenya. Kwa hiyo, tunatakiwa tuwe na regulator wetu sisi hapa Tanzania. (Makofi)

MWENYEKITI: Haya Mheshimiwa Nusrat na Mheshimiwa Waziri, umelisikia hilo? Endelea Mheshimiwa Nusrat.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru maana yake kama Wizara wanaona sasa kuna kazi ya kufanya. Lazima tuweke nguvu, tuweke teknolojia, tuweke utaalam, watu wakafanye tafiti watuletee ili tuone namna gani tutatengeneza pesa. Siyo tu kuweka miundombinu, tukajenge minara, hatuwezi kuishia kuzungumza minara, lazima tuzungumze tunanufaika vipi na hivi vitu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo yote, ili hivi vitu vyote tufanikiwe kwa sababu tunazungumza faida tutakayoipata baada ya miundombinu kukaa sawa, hatuwezi pia kuacha kuwa-recognise TTCL ambao mpaka sasa hivi wanaidai Wizara Dola za Kimarekani milioni 68. Kwa kweli mnawakwamisha sana TTCL, kwa sababu tunawategemea, ndiyo wanaosimamia, wanatumia mapato yao ya ndani kuendesha mfumo mzima na kuhakikisha kwamba Mkongo wa Taifa unafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunategemea hawa ndio wafike, kwa sababu tunaweza tukawa tuna ideas nzuri kweli watu wanapewa mafunzo waende waka-monetize YouTube Channels zao wapate pesa, lakini kama hatuna connectivity, hatuna miundombinu na hawana access ya kutumia internet bado tutakuwa tuko nyuma sana, bado tutakuwa tuna lag behind.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja la mwisho, pamoja na kwamba tumeweka kwenye data kwamba watu inabidi walipe ili kununua data wa-access internet, lakini kama Wizara tunaomba mwangalie upya kwenye machapisho ya kielimu na kwenye document za Kiserikali, hebu waondoe cost za downloading.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wanahitaji kupata information. Sasa ili ni-download kitabu ambacho kitanisaidia kupata maarifa ambacho pengine mwalimu anaenda kufundishia au mwanafunzi anajifundishia; wanafunzi wa vyuo vikuu mnajua, kuna amount unapata darasani na kuna amount unaenda kutafuta mwenyewe. Wako kwenye internet wanatafuta materials. Sasa kuna vitu vya msingi kama hivyo ambavyo tunaomba mwondoe downloading cost ili waweze ku-access kwa sababu ni muhimu kwao. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nichangie kwenye bajeti ya Wizara ya Kilimo. Kabla sijachangia naomba ni-declare interest mimi ni muumini wa matokeo, yaani mimi ni mtu ambaye naamini kwamba maneno matupu yanachosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, miaka na miaka tangu wazee wetu wako shuleni na pengine wengine wazee wetu baadhi walikuwa hawajazaliwa mpaka leo bado tunazungumza kwamba kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa. Nafikiri kauli hii ndio inayosababisha kutufikisha hapa leo. Unaweza kuvunja uti wa mgongo ukaendelea kuishi ila ukikosa oxygen utakufa.

Mheshimiwa Spika, nafikiri ipo haja ya kubadilisha kauli ya kilimo kwamba ni uti wa mgongo wa Taifa na tutafute kauli nyingine pengine inayofanana na kwamba kilimo ni oxygen ya uchumi wa Taifa. (Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa mmesikiliza hoja yake, hoja kubwa kweli hii. (Kicheko)

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kilimo kimesemwa ni uti wa mgongo wa Taifa, ndiyo maana bajeti ya Wizara ya Kilimo tangu mwaka 2016 mpaka 2021 imetekelezwa chini ya asilimia 50. Ukitafuta average ya utekelezaji wa bajeti mwaka ambao ilitekelezwa kwa kiwango kikubwa ni asilimia 42 mwaka 2018/2019, the rest ukitafuta average ni asilimia 19 tu. Kwa kuwa kilimo ni uti wa mgongo unaweza kuvunja uti wa mgongo ukaendelea kuishi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa ndio maana sasa hivi ukienda Nane Nane Dodoma unakuta kuna pilikapilika za maandalizi ya Nane Nane, kikishafika kilele cha Nane Nane watu wanafunga biashara zao unakuta mapori. Hii ni kwa kuwa kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa, vijana wetu ambao wako Chuo Kikuu cha Kilimo (SUA), wanakaa miaka yote darasani wanakwenda field miezi saba tu, kujifunza kuotesha mbegu, kuweka mbolea na kuotesha kila kitu mpaka mwisho kwenda kwenye masoko. Kwa kuwa kilimo ni uti wa mgongo Tanzania tuna eneo linalofaa kwa kilimo hekta milioni 44, lakini hekta milioni 29.4 zinafaa kwa kilimo cha umwagiliaji lakini mpaka sasa tumetumia hekta 561,383. Target ya Serikali ni kutumia hekta 1,200,000 ifikapo 2025 kwa sababu kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa, kwa hiyo unaweza kuvunja uti wa mgongo na ukaendelea kuishi.

Mheshimiwa Spika, kilimo chetu kina changamoto kubwa sana bado Tanzania tunalima kama Adamu na Hawa walivyolima Eden. Tunategemea mvua na kudra za Mwenyezi Mungu, katikati ya mabadiliko makubwa ya sayansi na teknolojia, katikati ya mabadiliko makubwa ya tabia nchi bado tunazungumza agriculture wakati dunia inazungumza agritecture. Dunia inakwenda kwa mabadiliko makubwa ya sayansi na teknolojia, kwa kuwa kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa, tunaendelea kuvunja uti wa mgongo tukitegemea tutafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya uchache wa muda niende kwenye kutoa ushauri tufanye nini. Jambo la kwanza, nashauri kilimo kisizungumzwe kama sekta ya maendeleo wala kisizungumzwe kama mfumo wa maisha life style kizungumzwe kama big money-making business. Kilimo kwa ujumla duniani ni dhahabu ya kijani, tuzungumze kama money-making business siyo desturi kwamba ni jambo la kimaendeleo, ndiyo maana tunafanya haya tunayofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, michango ya Waheshimiwa Wabunge inaonesha namna gani tunakwama sehemu. Hatuwezi kutatua tatizo hili kwa kuweka solution za pamoja ni lazima tuwe na solution za muda mfupi na za muda mrefu. Jambo la kwanza na la msingi, tuna watu ambao wako kwenye finger tips zetu, Maafisa Ugani, ni watu wako Waziri, nashauri tu-militarize sekta ya kilimo, tuibadilishe sekta ya kilimo iwe agricultural machinery. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukisoma bajeti ya mwaka jana ya Mheshimiwa Japhet Hasunga wakati yuko Waziri, vitu vilivyobadilika ni kipaumbele kilichokuwa cha tatu kinakuwa cha pili kilichokuwa cha nne kinakuwa cha sita. Mimi ni muumini wa mabadiliko, mimi ni muumini wa matokeo, tunataka matokeo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, kwa kunipa nafasi nichangie na mimi katika Wizara ya Michezo na nitachangia kwenye upande wa maendeleo ya sekta ya michezo nchini.

Mheshimiwa Spika, tukizungumza michezo kwenye Taifa sio tu ni sehemu ya kujenga afya ya mwili, lakini michezo pia ni sehemu ya kutangaza nchi, lakini pia michezo ni sehemu ya kuimarisha umoja na mshikamano wa nchi; lakini pia michezo ni ajira hasa hasa kwa vijana kwa sababu tunajua hata wanamichezo wapo ambao wamekuwa wakipunguza muda wao ili waonekane kama ni vijana kwa sababu inaonekana michezo pia ni kwa ajili ya vijana, hasa football na mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kwa nchi yetu TFF ndio wamekuwa wasimamizi kwenye upande wa mchezo wa mpira wa miguu Tanzania. Kwa hiyo, haitakuwa busara kama hatutazungumza yaliyopo kwenye TFF.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2017 Tanzania ilikuwa mwenyeji kwenye mashindano ya vijana Barani Afrika - AFCON ambako Mheshimiwa Rais, Hayati Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli aliatoa shilingi bilioni moja na mashirika mengine na taasisi walichanga kwa ajili ya kusaidia kufanikisha mashindano ya AFCON 2017. Lakini pia baada ya wageni kuja kulifanyika vitu vingi sana ambavyo kimsingi vilileta taharuki kwa TFF kiasi kwamba TAKUKURU waliingilia kati kwa ajili ya kwenda kuchunguza ubadhirifu wa fedha ambazo zilichangwa pamoja na fedha iliyotolewa na Mheshimiwa Rais kipindi kile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, TAKUKURU walichunguza mpaka leo hatujajua nini kinaendelea, hatujapata feedback kujua nini kilionekana huko kwamba walikutwa na hatia au hawakukutwa na hatia. Naomba Waziri atakapokuja kuhitimisha aeleze nini kilitokana na uchunguzi uliofanywa na TAKUKURU kwa TFF ili kujua matumizi ya zile fedha, kwa sababu mpaka sasa hivi Hoteli ya Holiday Inn ambayo wachezaji walikwenda kufikia pale baadhi waliotoka nje inadai shilingi milioni 80. Kwa hiyo, nitapenda Waziri atuletee feedback nini kiliendelea ili Watanzania wajue, kwa sababu TFF kiukweli inalalamikiwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini mwezi Julai, TFF inakwenda kwenye uchaguzi; sasa hivi wamebadilisha Katiba yao, kinyume na Katiba ya nchi, kinyume cha FIFA, kinyume na CAF wameweka kigezo cha elimu cha juu kuliko inavyotakiwa. (Makofi)

Sasa tunapata dukuduku kidogo kuona kwamba kwa nini wanakaribia uchaguzi halafu wanabadilisha badilisha katiba bila ya kufuata utaratibu. Na Wizara hatujaisikia ikisema chochote kwenye hilo yaani TFF imekuwa kama ni dude kubwa hivi ambalo ni ligumu kulifikia, ni kama wanalindwa fulani nisiende huko sana, lakini tunataka tusikie Wizara inazungumza nini kuhusiana na TFF kubadilisha Katiba yake kwenye suala la elimu, wameweka kiwangu tofauti kabisa hata na utaratibu wa nchi.

Mheshimiwa Spika, lakini TFF imeonekana ikiwaonea baadhi ya viongozi wa michezo kwenye nchi. Nitatoa mfano wa Mwakalebela aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa Yanga. Ukionekana unakosoa TFF unakuwa labeled kama mtu ambaye uko against TFF na wanakushughulikia vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa TFF nitapenda Wizara wakati inafanya hitimisho itoe majibu kwenye hayo kwa kweli ni sehemu ambayo inaleta mtanziko mkubwa kwa watu ambao ni wapenda michezo.

Mheshimiwa Spika, lakini pia nitazungumza kuhusiana na kukuza vipaji vya wanamichezo wetu kwenye nchi. Tumezungumzwa kuhusiana na sports academy. Mimi nina fikra tofauti kidogo kwa sababu mimi ni muumini wa Tanzania, ninapenda michezo lakini pia ni muumini wa timu ya Taifa ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, ukweli ni kwamba timu ya Taifa inakuwa constituted na vilabu yaani na vilabu, kwa sababu ni miaka mingi tumezungumza tumesema kwamba tutengeneze sports academy kwenye nchi, lakini haifanikiwi, ninachojaribu ni kutoa solution ya tunaweza kufanya nini kutokana na experience ya nchi nyigine. Nigeria inaonekana inafanya vizuri sana kwenye michezo, lakini Nigeria hata zile private sector wana football academy nyingi na zinafanya vizuri na ndio Serikali inategemea huko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nafikiri badala ya kuimba kila siku tutaweka football academy ya Taifa Stars na haifanikiwi, nafikiri kuna haja ya kuwezesha hizi sports academy za club kama Namungo, Ruvu JKT huko kwa sababu tunategemea wanamichezo wetu watoke kwenye hizo klabu. Ni kweli kwamba tunategemea pia nchi zingine kutuletea wanamichezo kwetu, lakini pia mimi nafikiri tutengeneze ndani zaidi kwa sababu ndio tunaowategemea na tuna-feel proud kama tutapata kina Samatta wengi zaidi maana yake ni faida pia kwa Taifa, kwanza anatangaza Taifa, lakini pia inaleta hamasa kwa vijana wengine ambao wanafanya michezo Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nafikiri sasa Serikali kuna sports academy Tanzania nitazitaja na najua Waziri either anazifahamu au kama hazifahamu aangalie namna ambavyo unaweza kuzisaidia. Kwa upande wa shule, shule ya Fountain Gate Academy, sports academy wanafanya vizuri sasa hivi wameingiza timu ya wasichana under 17. Wanafanya vizuri sana na mnajua kuna football academy Morogoro na hapa ya Fountain Gate, they doing very great na hapa kwa kweli kwenye hili nawapongeza pia Simba Queens chini ya uongozi wa Fatma Dewji kwa kweli wanafanya vizuri pamoja na kwamba mimi mwenyewe Simba tunawapongeza Simba wale. Lakini Simba Queens kwa sababu wanafanya vizuri sana this time tunawapongeza pia na nafikiri wanahitaji kupewa support kwa namna moja ama nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kuna sports academy kama Roho Sports Academy, Gymnastic Sports Academy, Dar es Salaam International Academy, A Future Stars Academy, Football Academy Arusha, Street Children Sports Academy, Faome Highway and…

T A A R I F A

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa Mheshimiwa Nusrat.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nilitaka nimpe taarifa Mbunge anayeongea sasa kwa kuwa amesema kwamba timu ya Simba Queens Sports Club inafanya vizuri sana na kwa misingi hiyo mimi nilikuwa nataka niseme kwamba angeendelea kuongelea kwamba hii timu walau sisi Wabunge tungewachangia ili kuwatia motisha waendelee kufanya vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kwa msingi huo nimuombe Mheshimiwa Nusrat atoe hoja ili sisi tuiunge mkono na hawa vijana wetu, mabinti zetu waweze kupata motisha ili waweze kufanya vizuri zaidi. Ahsante. (Makofi)

SPIKA: Unapokea hiyo hoja Mheshimiwa Nusrat. (Kicheko)

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, naipokea na kimsingi hili ni suala tunaweza pia kusema ni la Kibunge zima, kwa hiyo, Yanga pia watulie ikifika na wao hatua yao, kwa kweli hili kama itabidi tuweke utaratibu mzuri ili watu waichangie Simba Queens, kwa hiyo naipokea. Nafikiri niendelee kuchangia.

WABUNGE FULANI: Endelea.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, kwenye sehemu ya kukuza vipaji kwenye Taifa kwa masikitiko makubwa sana…

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi naomba nimpe taarifa Mbunge anayechangia kwamba anapoipongeza Simba kufanya vizuri ajue kwamba kuna mwanamke lazima ampongeze pia Barbara kwamba wanawake sasa hivi hata Yanga wakimuweka mwanamke wanaweza wakafanya vizuri zaidi. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Nusrat unapokea taarifa hiyo kwamba wanawake mnaweza?

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, naipokea na nilimtaja Fatma Dewji kwa sababu ndio anasimamia Simba Queens, lakini Barbara ndio top in charge mwenyewe kwa hiyo tunampongeza. Yanga tulieni! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, upande huo huo wa kukuza vipaji, nasikitika sana kuna dada anaitwa Hadhara Charles Mjeje alishinda mashindano ya football free style ya danadana mnamfahamu, alishinda na anatoka Tanzania mpaka Rais Donald Trump alim-post, alifanya video call na Messi, walimpongeza sana na kuna baadhi ya makampuni walijitolea kuingia naye kwenye contract kwa ajili ya kutangaza bidhaa zao za michezo kwa sababu she is really good.

Mheshimiwa Spika, lakini nasikitika sana alikuwa amepata deal ya ten years akafanye na kampuni moja ya kutangaza bidhaa za michezo South Africa, lakini inaonekana Serikali iliomba ile kampuni ibadilishe muda isimuwekee ten years mpaka tunapozungumza yupo mtaani na juzi alikuwa anahojiwa, ana maisha magumu mno.

Mheshimiwa Spika, ina-demoralised, inashusha morali na ari ya vijana na wote watu wa Tanzania ambao wanajituma sana na wanavipaji ambavyo wamebarikiwa. (Makofi)

Sasa kuna siku moja ulizungumza kuhusu less government kwenye intervention, Serikali ni sehemu moja wapo ya kuweka link kati ya wananchi na yenyewe Serikali kwa maana ya utaratibu, lakini isiwe kikwazo cha kusaidia vijana wetu na wana michezo wetu kufanya vizuri kwenye Taifa. Kwa hiyo, nafikiri huyu sasa kwa sababu pia umri pengine umekwenda na nini, lakini ikitokea vijana wengine wana uwezo wa kufanya vizuri, tunahitaji sana kuwasaidia. Tunategemea Wizara iwe sehemu ya kuwa-link na kuwasidia kwa sababu wanatangaza nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi uki-google unaandika Mtanzania aliyepostiwa na Donald Trump, unaweza kusema ni kitu kidogo, lakini Tanzania imeshaingia kwenye hiyo statement Tanzania imeshaingia, lakini pia is our very own, ni wa kwetu, kwa hiyo vitu vya kwetu lazima viwe protected sasa in the same spirit tunaomba Diamond Platinum asaidiwe kuhakikisha kwamba anashinda tuzo anayogombea kwa sababu in the name of the country, ukiachana na hivi vitu vyote, kwanza ukweli usiopingika anafanya vizuri, huo ndio ukweli anafanya vizuri, very good. Kwa hiyo tuna sababu pia kila sababu ya kumsaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nimalizie kwenye upande wa wasanii wetu, namna gani tunaweza tukalinda kazi za wasanii wetu na kwa kweli pamoja na mambo yote Serikali imekuwa ina mkono mzito sana kwenye kuwabana wakifanya vibaya. Lakini kwenye kuwasaidia imekuwa ni changamoto kubwa sana. Nashauri kuundwe chombo maalum ambacho kitakuwa kina waratibu wasanii wao, najua kuna vyombo vingi huko, lakini kuna mgawanyiko na ninyi mnajua kuna madudu mengi sana yanaendelea huko, wana mambo yao wenyewe ndani wanajua kina Mwana FA.

Mheshimiwa Spika, lakini nafikiri pia kuna namna ambavyo hata kupiga kazi zao. Nashauri Serikali itoe mwongozo asilimia 80, yaani asilimia 100 ya kupiga nyimbo za wanamuziki duniani basi asilimia 80 zipigwe za Watanzania, zipigwe za kwetu. Hilo suala mnaliweza, ni suala tu la kutoa mwongozo.

Mheshimiwa Spika, tunahitaji vijana wetu wanaofanya muziki wapate coverage kubwa na wajisikie fahari kufanya sanaa Tanzania. Ukweli ni kwamba Afrika Mashariki nchi ambayo inafanya sanaa nzuri ya uimbaji ni Tanzania. Wakenya wapo wanapiga tu kazi zetu kwenye club zao, redio zao na television zao kwa sababu tunafanya muziki mzuri. Kwa hiyo, ikawe pia ilete tija. Kamati imeshauri kuhusu aggregation na mimi nashauri na naongezea hapo hapo kwamba ili wapate kipato, wekeni utaratibu mzuri kuwasiliana na Wizara ya TEHAMA kuona namna gani wasanii wetu wanaweza wakapata faida kutokana na kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawashukuru sana kwa kunipa nafasi. Nategemea majibu ya maswali niliyowauliza Wizara kwenye masuala ya TFF, kwa kweli ni very important, tunahitaji kusikia mnazungumzaje kuhusu TFF. Ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi ili na mimi nichangie kwenye Bajeti Kuu ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi bajeti hii ni bajeti ya kwanza katika Awamu ya Tatu ya Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano, na ni bajeti ya kwanza kwenye Serikali ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan. Kwa utaratibu huo maana yake tukiangalia, Mheshimiwa rafiki yangu, kaka yangu, ndugu yangu Mwigulu, Mheshimiwa Waziri mwenyewe ameiita bajeti ya kimkakati. Hata hivyo naomba nimbadilishie kidogo, hii bajeti pamoja na kwamba unasema ni ya kimkakati lakini ni bajeti ambayo mimi naiita bajeti ya tamu-chungu; yaani tunang’atwa halafu tunapulizwa, yaani tunatekenywa huku tunafinywa. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, yes, bajeti hii kimsingi kuna mambo makubwa ambayo hayajawahi kuzungumzwa katika bajeti za miaka kadhaa mitano tukirudi nyuma. Kuna vitu ambavyo vimekuwa vikilalamikiwa mara kwa mara na Waheshimiwa Wabunge mpaka na wananchi wetu huko, ambavyo vilikuwa havijaingizwa lakini kipindi hiki tunaviona. Pia, at the same time kuna vitu ambavyo kimsingi, vimewekwa kwenye lugha za kiuchumi sana, unaweza kuona havikuumizi, lakini kimsingi vinaumiza Watanzania kwa kiasi Fulani, nitaelezea.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiwa tunazungumzia Bajeti Kuu ya Serikali mwaka 2021/2022 ni muendelezo wa mipango ile ya miaka mitano mitano ambayo imeshapita, na sasa hivi tuko watatu, maana yake tumetoka wa pili. Hatuwezi tukazungumza leo bila kuangalia tulipotoka, tulipo na tunapotaka kwenda. Kwa hiyo ni lazima tujifanyie evaluation kama nchi, kwamba tumetoka wapi, tupo wapi na tunataka kwenda wapi. Kwa sababu ni muendelezo, ndiyo maana tukasema ni awamu kwa awamu, awamu ya kwanza, ya pili na ya tatu. Hivyo tumekuwa tuna tatizo kubwa sugu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunapanga mipango ya maendeleo ya miaka mitano mitano, tunatengeneza bajeti/tuna-formulate bajeti za kutusaidia ku- implement mipango; lakini kumekuwa kuna tatizo sugu la kutopeleka fedha za miradi ya maendeleo kama zinavyopitishwa na Bunge hili. Hili nalisema kwa nia njema ya taifa langu na ninalipenda sana taifa langu. Kimsingi Watanzania ukiangalia comments zao baada ya bajeti kusomwa kuna vitu wanavifurahia. Ninachosikitika mimi ni kwasababu, ninajua kuna mahala itafika tutakwama na tutarudi mwakani kusoma bajeti ya mwaka 2022/2023 tukiwa kuna sehemu hatujatekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninasema hivyo kwa sababu, mathalani, zipo Wizara ambazo zinachangia Pato la Taifa kwa kiasi kikubwa na zinagusa maisha ya Watanzania kwa kiasi kikubwa sana, ambazo utekelezaji wake wa bajeti ni chini ya asilimia 30 kwa miaka mitano consecutively, tangu mwaka 2016, mpaka mwaka huu tunaozungumza sasa hivi, 2020/2021. Kwa hiyo, unaona ni namna gani tunavyozungumza kwamba kuna shida sehemu. Tunapanga bajeti, tunapitisha vizuri, tunashangilia, tunafurahi lakini tukitoka hapo utekelezaji wake ni chini ya asilimia 30.

Mheshimiwa Naibu Spika, mathalani bajeti ya Wizara ya Kilimo kwa miaka mitano mfululizo, consecutively, tangu 2016 average ya bajeti yake ya miradi ya maendeleo imepelekwa asilimia 19.3 tu. Sasa tunategemea Watanzania wengi wameajiriwa na sekta hii, pia tunategemea ndiyo sekta inayolisha Watanzania asilimia 100, na vilevile Wizara hii inachangia Pato la Taifa asilimia 27.7 na sasa tunapeleka fedha katika kiwango hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na tumekuwa tukilalamika kwamba bajeti iongezwe, lakini hata ile ndogo inayotengwa haipelekwi pia kwa wakati nabadala yakeinapelekwa mwishoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ina-good faith kwa ajili ya taifa letu ni lazima tuone kwamba ni namna gani hizi Wizara ambazo tunasema zinaajiri asilimia kubwa ya Watanzania na kwamba zinachangia Pato la Taifa kiasi kikubwa, tunapeleka fedha kiasi gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya pili ambayo ina tatizo kwenye kupelekewa fedha ni Wizara ambayo kimsingi imebeba dhima kuu ya kauli mbiu ya Chama cha Mapinduzi, na hapa nipo na Ilani ya Chama cha Mapinduzi, Tanzania ya Viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu viwanda na biashara, kutoka ukurasa wa 56 - 60 kwenye hii Ilani ya Chama Cha Mapinduzi wamezungumza kwa undani na kufafanua masuala ya viwanda na ya biashara; lakini utekelezaji huu wa bajeti ya Wizara ya Viwanda na Biashara consecutively in years ni asilimia 20. Kwa hiyo maana yake Serikali ya Viwanda, Tanzania ya Viwanda asilimia 80 ya bajeti haijatekelezwa kwenye miradi ya maendeleo na tunazungumzia kauli mbiu ambayo tunaenda nayo; kwa hiyo kuna changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ya tatu ni kuhusu mifugo na uvuvi ambayo inachangia asilimia tisa ya Pato la Taifa; bjeti yake yaani imetekelezwa kwa asilimia 21 consecutively kwa miaka mitano ambao ndio Mpango wa Pili wa Maendeleo; sasa ni changamoto kwa kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia Wizara ya Afya ambayo ndiyo inayotoa nguvu kazi ya taifa bajeti yake imetekelezwa kwa asilimia 18.1 tu. Watanzania wakiwa wagonjwa hatutaweza kuzalisha. Bajeti ya mwaka 2020/2021 ya afya Wizara iliomba shilingi bilioni 360 lakini mpaka Machi mwaka huu 2021 walipelekewa shilingi bilioni 83 tu za kutibu Watanzania ili Watanzania wawe wazima wazalishe; ni changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi ninajua kabisa, nikiwaangalia Mawaziri ninaona nia yao ni njema, changamoto ni tuna kasungura kadogo tunagawana hako hako, ndiyo shida. Kwa sababu ili tupate fedha za bajeti tupeleke kwenye miradi ya maendeleo ni lazima tukusanye kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na Mwalimu Nyerere alishawahi kusema, kwamba, Serikali ambayo haikusanyi kodi kimsingi haiwezi kwenda kokote. Mimi ninajua kuna changamoto, na najua nia ni njema; tunatenga fedha zinatakiwa zije ziende zote, lakini tunashindwa kupeleka kwa sababu hatuna fedha. Sasa Mamlaka ya Mapato Tanzania kimsingi inatufelisha kwa kiasi kikubwa. Mpaka leo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) wana matatizo yao mengi kule ndani, na inawezekana kuna mianya ya rushwa pengine ndiyo maana tunashindwa hata kufanya evaluation ya kodi. Kwa sababu wanaolipa kodi, wewe unafahamu, ni asilimia tano tu ya Watanzania milioni 60, haiwezekani.

Mheshimiwa Naibu Spika, halafu wale ambao wanalipa kodi ambao ndio mnajua system zao, ni walimu, ni wafanyakazi wa Serikali, mnajua system zao za mishahara, ndio wanakatwa. Kwa hiyo ni Watanzania wachache wanaoendelea kunyonywa kwa kulipa kodi, kuna wengine wengi ambao hawalipi kodi kwa sababu hamna utaratibu mzuri wa kuwafuatilia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mamlaka ya Mapato Tanzania imeshindwa kufanya ukaguzi wa walipa kodi. Mimi leo ninaweza nikatoa taarifa za uongo za biashara yangu, nikalipa mara ya kwanza na nikaendelea kufanya biashara miaka mitano, bado nitaendelea kulipa kiwango kile kile, niwe nimekua, niwe sijakua hakuna nia njema. Tulisikiliza wote hotuba ya Mheshimiwa Rais, nia yake, na kwa sababu alizungumza. Kwamba wigo wa ulipaji kodi ni mdogo sana, tunahitaji kupanua wigo, kwa sababu lengo ni kupata fedha tukapeleka kwenye miradi ya maendeleo, kwa hiyo ni changamoto kimsingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi naomba nimshauri Mheshimiwa Waziri, kwamba, kuna wale wawekezaji ambao tunategemea kuwa ni sehemu ya sisi kupata kupata mapato ili tuweke kwenye miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna watu wana kesi na kuna kesi ziko mahakamani. Mpaka sasa tuna mashauri ya rufaa mahakamani, yanayosubiri kuamuliwa ya muda mrefu, tunadai takriban trilioni 360 na dola za kimarekani milioni 181. Hizi fedha ni za muda mrefu sana, na tumekuwa tukiimba kwamba zikipatikana zote zitasaidia kuendesha nchi miaka 10, na nini story zinanoga. Lakini kimsingi inawezekana mkatafuta mazingira ya kuongea na hao watu, either wasamehewe hizi kodi, waendelee kufanya biashara katika mazingira mazuri, au mtafute namna bora ya kuangalia. Lakini kwa sababu ya muda nashukuru, sitaunga mkono.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ili niweze kuchangia. Kwenye bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu na nitachangia Fungu 65 - Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitachangia specific kwenye eneo moja sana kwenye maendeleo ya vijana kwa sababu pamoja na kwamba tunafanya sensa mwaka huu lakini sensa ya mwisho kufanyika bado imeonesha kwamba nguvu kazi ya Taifa sehemu kubwa sana ni vijana na hatuwezi kuzungumza maendeleo ya vijana bila kuangalia mambo ambayo yanawakabili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasikitika kwamba baadhi ya Mawaziri na Mawaziri wengi sana hawapo hapa na kuna vitu ambavyo tunaongea vingine vinaingia kwao moja kwa moja. Kwa hiyo niseme hivyo, lakini kwenye kitengo na segment kuu ya maendeleo ya vijana kwenye Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwenye upande wa Sera ya Maendeleo ya Vijana. Mwaka 2019 vijana wa nchi waliitwa kutoka maeneo mbalimbali wakakaa wakajadili na wakapitisha kwa kutoa mapendekezo yao kuhusu namna ambavyo tunaweza tukawa na Sera ya Maendeleo ya Vijana yenye tija. Mpaka sasa ni miaka minne Sera ya Maendeleo ya Vijana ambayo kimsingi ndiyo inayotoa dira ya shughuli za vijana kwenye nchi, sera inatoa dira kwenye masuala ya Maendeleo ya Vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunafahamu wote kwamba life span yaani umri wa kuishi sera ni miaka 10. Kwa hiyo mpaka sasa hivi katika miaka 10 ya sera ya vijana tumeshakula miaka minne mpaka sasa hivi hatujui nini kitakachofuata, lakini kimsingi watu wanatakiwa wajue. Kwa hiyo wakati sera inakuja tayari imeshakula miaka minne bila kutekelezwa na kimsingi nina sera hapa ambayo kuna baadhi ya vitu tayari vimeshakuwa outdated, vimeshapitwa na wakati ambapo pia inatakiwa irudishwe ikapitiwe upya ndiyo iende tena kutekelezwa, four years. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuwezi kuzungumzia Maendeleo ya Vijana bila kuzungumza uwezeshaji wa vijana kiuchumi. Kamati imetoa mapendekezo yao na nimekuwa nikisoma taarifa za Kamati miaka kadhaa ya nyuma siyo mwaka tu wa leo na leo pia wamezungumza kuhusu Mfuko wa Maendeleo ya Vijana. Mfuko huu umekuwa ni kichomi na kimsingi nilikuwa nasoma pia Ilani ya Chama cha Mapinduzi hapa kuanzia ukurasa wa 26 mpaka ukurasa wa 30 wanazungumzia masuala ya vijana, lakini mwelekeo wao umejiwekeza katika kutoa semina, kufanya warsha, kufanya makongamano na kujengea uwezo vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, imetosha kujengea uwezo vijana, tunataka Mfuko usaidie vijana kujiendesha kiuchumi. Serikali haiwezi kuajiri vijana wote, soko la ajira linatoa watu wengi sana, haiwezekani, kwa hiyo lazima Mfuko huu usaidie vijana kujitegemea kujiajiri na kulipa kodi kuchangia maendeleo ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeangalia pia taarifa hata Kitengo cha Ofisi ya Waziri Mkuu pia na wao wanazungumza ni semina, makongamano, warsha na kujengea uwezo, inavunja moyo kwa sababu sasa hivi kuna kitu kinaitwa startups mmekuwa mkisikia, inawezekana watu hawaelewi nitafafanua startups business ni biashara ambazo ni za Watanzania zimebuniwa humu, yaani vijana wetu wa Kitanzania wanabangua bongo zao wanaandaa biashara kwa kutumia sayansi, teknolojia na ubunifu kuitikia mabadiliko ya sayansi na teknolojia duniani, lakini kuitikia maendeleo ya viwanda yaani mapinduzi ya nne ya viwanda. Sasa vijana hawa kuna vitu wanahitaji kufanyiwa hawahitaji warsha na makongamano, walishatoka huko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, startups za Tanzania kuna kitu kinaitwa Tanzania Startups Association ambayo ndiyo imeunganisha startups za Tanzania ambazo zipo 587. Waheshimiwa wana vishikwambi, wachukue tabulates zao, wa-google Tanzania Startups Association wataona jinsi ambavyo vijana wetu wanabuni vitu vikubwa ambavyo wengine wanashinda mpaka tuzo Afrika. Kuna startup inaitwa Agree Info wameshinda katika nchi 19 Afrika, lakini sisi tunajadili warsha na makongamano yaani irrelevant kabisa, yaani tunakuwa hatulingani na jinsi vijana wanataka twende. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vijana hawa wanabuni vitu ambavyo ni vya kielektroniki, wengine wanahitaji vitu vidogo vidogo kwa mfano, badala ya kujadili warsha na makongamano, tujadili ni namna gani tunatunga sheria kwa ajili ya kuzilinda startup business. Tutunge sheria, sasa hivi ninavyozungumza nilikuwa napitia Kenya, Kenya mwaka 2020 mwezi wa Tisa wamepeleka Bungeni Muswada wa startups Kenya kwa ajili ya kuzilinda biashara za kiteknolojia ndogo ambazo zinaanzishwa na vijana wa Kenya. Sasa si kitu kibaya kuiga kwa wenzetu kama kuna kitu kizuri kinafanyika, si mpaka tuchelewe sana, tuje mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kitu kingine mfano mzuri wa startup ya Tanzania ni ile gari ya juzi ya Masoud Kipanya ile ni ya ndani, Masoud ameanzisha kile kitu from the scratch ameagiza mitambo kutoka nje. Sasa kama vijana wetu wapo wengine ambao wanaagiza mitambo kutoka nchi mbalimbali kwa maana ya kuja kuhakikisha wanakuja kutengeneza vifaa vyao vya kielektroniki basi tuwaondolee VAT kwa ajili ya kuwa-support na kuhakikisha kwamba tunakuza ubunifu katika nchi yetu. Sasa haiwezekani Wizara ambayo ita-deal na masuala ya Vijana inajadili warsha na makongamano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu nyingine ambayo ninawe nikazungumza, sasa hivi ni miaka saba tangu Bunge hili litunge Sheria ya Baraza la Vijana la Taifa, na ni miezi saba tangu Mheshimiwa Rais aongee na Vijana wa Tanzania kupitia Jukwaa la Vijana wa Tanzania kupitia jukwaa la Vijana wa Mkoa wa Mwanza kutoa maelekezo tuunde Baraza la Vijana wa Taifa. Sasa sitazungumza faida yake lakini nataka tu muone double standard, Zanzibar kuna Baraza la Vijana la Taifa, hawawezi kupata kitu chochote kwenye kuiwakilisha nchi kwa sababu Zanzibar siyo nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapozungumza kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki wameanza mchakato wa kuanzisha Baraza la Vijana la Jumuiya ya Afrika Mashariki lakini Vijana wa Tanzania hawatashiriki kwa sababu sisi tunaendekeza siasa mpaka kwenye mambo ya msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna fursa mbalimbali ambazo Vijana wa Tanzania wanaweza kuzipata, sasa labda tuulize Serikali hivi ni kweli mnataka kuwanyima vijana wa Tanzania fursa za kushirika katika Jumuiya ya Afrika Mashariki na Vijana wenzao?

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa!

T A A R I F A

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpe taarifa ndugu yangu Nusrat Hanje, kwa kusema kwamba Zanzibar siyo nchi. Kwa hiyo naomba atufafanulie hapa. Ahsante sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Hebu zungumza tena hoja yako.

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Hoja yangu nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Nusrat Hanje kwamba Zanzibar ni nchi, kwa hiyo naomba aipokee hiyo taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Nusrat.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika nashukuru na ninaelewa concern ya ndugu yangu hapa, lakini katika representation katika uwakilishi wa nchi kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki haiwi-considered kama nchi, sitazungumza hapo zaidi lakini ninajua concern yake na ninafahamu na ninaheshimu masuala yote ya Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hatuna Baraza ambalo lingeweza kuwa chombo kiunganishi, kimsingi hata Mheshimiwa Rais anajua hilo Ndiyo maana hata yeye ndiye aliyezindua Baraza la Vijana la Zanzibar akiwa Makamu wa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya Nne ambayo ndiyo ya mwisho nitazungumza leo ni katika maendeleo ya vijana kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu kuna kitu kinaitwa Mbio za Mwenge wa Kitaifa.

Ninafahamu, ninaheshimu na ninatambua umuhimu wa mbio za Mwenge za Kitaifa kwa maana ya Mwenge wa Uhuru. Ni kitu ambacho tumeki-respect na tunakiheshimu sana, ni kitu ambacho kimefanya vitu vikubwa kwenye hii nchi. Lakini kama Mfuko wa Vijana kwa mwaka unatengewa bilioni moja haipelekwi kwa sababu hakuna pesa na tunakimbiza Mwenge nchi nzima kwa ajili ya kumulikia umoja, amani, upendo na mshikamano, tunaviheshimu sana na tunavihitaji sana kwenye nchi, lakini mimi nafikiri tufikiri kuna haja ya kuendelea kutumia gharama kubwa ambayo kimsingi hatuzijui, kwa sababu labda mimi ni mgeni, lakini sijawahi kuona Bungeni inajadiliwa Bajeti ya mbio za Mwenge za Kitaifa, hatujui wala sijawahi kusoma ripoti ya CAG imejadili kuhusiana na gharama za Mwenge na tunaheshimu na naomba ieleweke hivyo. Lakini hivi hatuwezi kutumia ubunifu mwingine kwa ajili ya kuenzi na kuheshimu Mwenge huu ambao kimsingi Luteni Kanali Alexander Nyerenda alianza yeye kwa kwenda kuweka pale juu na tunaheshimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunaweza kukosa Bima za Afya kwa wote kwenye nchi lakini tusikose pesa ya kukimbiza Mwenge tunakuwa hatutendei haki Vijana wa Taifa hili. Ninasema hivi ili Vijana waelewe mbio za Mwenge kwenye Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu zipo upande wa maendeleo ya Vijana. Kwa hiyo, vijana wajue kwamba kama kuna mambo yanashindikana maana yake ni kwa sababu tunakimbiza Mwenge! Yaani haijawahi kukosekana pesa ya kukimbiza Mwenge kwenye nchi hii. (Makofi)

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa!

T A A R I F A

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa Mheshimiwa Mbunge kwamba katika hoja yake ameeleza kwamba ameshangaa kuona Mfuko wa Vijana haujatengewa fedha. Mfuko wa vijana ulitengewa Bilioni Moja na fedha zote Bilioni Moja zilipatikana kwenye Mfuko wa Vijana, isipokuwa Vijana wengine hawakukidhi vigezo, Milioni Mia Mbili na Tano zilishatolewa kwa ajili ya Vijana hao na fedha zilizobaki zinawasubiri Vijana kuziomba kwa kuzingatia vigezo.(Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante, Mheshimiwa Nusrat.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru na ni ufafanuzi mzuri lakini kwa vijana kule hazifiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda hoja yangu hajanielewa, yaani hivi hakuna namna ambazo sisi kama nchi na machinery zote ambazo tunazo, Ma-Professor, Waatalam, hivi hatuwezi kufikiri namna bora tunaweza tukauenzi na kuuheshimu huu Mwenge zaidi ya kuuzungusha kutumia gharama ambazo hatuzijui? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe Mbuge hili, labda ifike muda tuletewe bajeti ili tuone value for money. Mwenge unaweza ukakimbizwa kwa Shilingi Bilioni Mia Tisa ukaenda kukagua miradi ya Shilingi Milioni Mia Nne au Shilingi Bilioni Moja, yaani value for money katika kujenga.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu sisi hii ni awamu ya kwanza kuna watu wana awamu nyingi humu, labda tusaidiane na ni katika kujenga tusaidine hivi hamna namna nyingine tunaweza tukafanya. Kwa sababu kama Vijana wanakosa pesa, Vijana wenyewe kazi yao ni kwenda kufunga majukwaa, tunahitaji pesa tuende tukafanye miradi ya maendeleo, tunahitaji pesa kwa ajili ya kwenda kujenge barabara. Waheshimiwa Wabunge jana walikuwa wanadai vituo vya Polisi hapa.

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa!

T A A R I F A

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba Mwenge wa Uhuru ni nembo ya nchi, tunapokuwa tunapozungumzia nembo tunazungumzia culture kwa maana ya utamaduni wa Taifa huwa hatuwezi kuangalia value for money kwenye mambo yanayohusu utamaduni na alama ya nchi. Utamaduni huu wa National Torch siyo kwa Tanzania peke yake, Mataifa mengi yana tamaduni zao na wanatumia mbio za Mwenge kwa ajili ya kuhamasisha, kutia ari na kuweka nguvu katika kuhamasisha shughuli za maendeleo ya nchi husika. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Nusrat.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2015 tuliahirisha sherehe za Uhuru, Mwenge ulikuja baada ya kupata Uhuru kwa hiyo sidhani kama kuna kitu ni muhimu kuliko uhuru wa nchi. Kama tuliweza kuahirisha sherehe za uhuru tukapeleka pesa na Mheshimiwa Rais wa kipindi hiko alitoa maelekezo zifanyiwe nini. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Miaka Mitano, mpango wa mwaka mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu hali ya uchumi, ukuaji wa uchumi, mfumuko wa bei, maendeleo ya watu na vitu vingine. Hakuna Serikali ambayo inataka kuona watu wake wanateseka, haipo, kwa jinsi ninavyofahamu. Hakuna Serikali ambayo imejidhatiti kusimamia wananchi wake na kuhakikisha kwamba wanaishi katika mazingira mazuri na wanajikwamua kwenye umaskini ambayo inafurahia wananchi wake kupitia katika mfumuko wa bei uliokithiri, uchumi unaokua kwa kasi ya kinyonga na maendeleo ya watu yasiyo maendeleo ya watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi umekua kwa asilimia 0.4 kwa mujibu wa mpango huu na hotuba ya Mheshimiwa Waziri, lakini mfumuko wa bei bado umeendelea kuishi nje ya malengo ya Serikali ambayo ni kwamba mfumuko wa bei ulikuwa ubaki stable kwenye asilimia 3.0 mpaka 5.0. Tumeshuhudia malengo ya Serikali yakiwa mbali kabisa na hali ilivyo kwa sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukizungumzia maendeleo ya watu maana yake tunategemea kuona watu wakijikwamua kwenye lindi la umaskini. Nimesema mwanzo kwamba haipo Serikali ambayo inatamani watu wake wateseke, kwa hiyo mimi naamini, pamoja na jitihada zote zinazofanywa na Serikali, lengo lao ni kuhakikisha kwamba wanawatengenezea Watanzania mazingira mazuri ya kuishi ili uchumi wa Mtanzania mmoja mmoja ukiwa mzuri Serikali kazi yake ni kukusanya kodi. Kwa hiyo ninaamini nia njema ipo kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunajikwamua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini zipo sababu nyingi sana zimetajwa kwamba kwa nini tuna changamoto hizi, kwa nini bado mfumuko wa bei hauko stable kwa sababu kuna athari za vitu vingine ambavyo vimetajwa, masuala ya kupanda kwa bei ya mafuta, mbolea na nini. Kuna sababu nyingi ambazo sidhani kama tuna haja ya kujielekeza huko kwa sasa kwa sababu Mheshimiwa Waziri ameeleza vizuri na Kamati wamefafanua vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Deni la Taifa; kwa hali isiyo ya kawaida Deni la Taifa kutoka mwezi Aprili mwaka huu mpaka mwezi Juni mwaka huu, 2022, limeongezeka kwa kiasi cha shilingi trilioni 2.119 kutoka shilingi trilioni 69.44 Aprili mpaka shilingi trilioni 71.559.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunajua kwamba kuhakikisha kwamba tuna-fund miradi ya maendeleo ili tu-move, it’s well and good. Na kwamba Deni la Taifa linahimilika, kwa sababu siku zote tumekuwa tunasema kwamba Deni la Taifa bado linahimilika, Deni la Serikali bado ni himilivu na nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani kwa hapa tulipofika na tunapokwenda, kwenye shilingi trilioni 71.559 ninaomba Bunge hili liweke ukomo wa uhimilivu wa Deni la Taifa. Kwa sababu ni kweli tunakopa kwa ajili ya ku- fund kwa sababu hakuna mtu anakopa akafanye starehe, ndiyo maana nilisema kwamba hakuna Serikali inayotaka wananchi wake wateseke.

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa binti yangu, Mheshimiwa Nusrat, kwamba Serikali inakopa kwa factors za kiuchumi, siyo factors za kuwekewa limit. Factors za kiuchumi za nchi ndizo zinazotoa direction ya Serikali kuwa na uwezo wa kukopa ama la. Tukisema Bunge liweke ceiling ya Serikali kukopa tutakuwa tunakwenda kinyume na principles za kiuchumi katika masuala mazima yanayowezesha mambo ya ukopaji katika masuala ya kuendesha Serikali duniani.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nusrat.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwenendo wa biashara ya bidhaa na huduma kwenye Taifa letu; tumesema nia yetu ni njema, hatutaki wananchi wetu wateseke na tunataka pato la ndani wananchi walifaidi wenyewe. Lakini kwa sasa hivi hali ilivyo tunaendelea kulipa madeni, it’s well and good kwa sababu tunaona flagship projects na nini, lakini aim si ni kujenga?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sikilizeni tushauri; kwanza kuhusu mwenendo wa biashara na huduma ndani na nje. Taarifa ya Mheshimiwa Waziri na Mpango inatueleza kwamba tumekuwa tuna-import zaidi kuliko ku- export. It’s well and good kwa sababu kwenye taarifa kunaonekana kuna ongezeko la kutoa bidhaa nje (ku- export) kwa asilimia 25, na kwamba tumetoka dola za Kimarekani milioni 8,811 mwezi Juni mwaka jana mpaka dola za Kimarekani milioni 11,116.7.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna progress, lakini ukweli ni kwamba sekta ya utalii – na niwapongeze sana kwa jitihaa zilizofanyika – sekta ya utalii ndiyo imekuza hii; lakini ongezeko la ku-import ni kubwa kwa asilimia 39, limeongezeka kwa asilimia 39 zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana mwezi Juni kwenye ku-import tulikuwa tume-import kwa takribani dola za Kimarekani milioni 9,841 mpaka dola za Kimarekani milioni 13,715, sawasawa na ongezeko la asilimia 39. Tuki-export kidogo tuka-import zaidi tunajikosesha fedha za kigeni, maana na sisi Tanzania mazingira yetu pia ya biashara yanakuwa siyo mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe kwenye mpango huu Serikali ijielekeze zaidi katika kutengeneza mazingira yetu ya bidhaa za ndani ili tupunguze ku- import. Lakini pia kutengeneza mazingira ya kwetu ili tu- export zaidi; na hii ni principle ya kawaida tu ya biashara, wala haihitaji Ph.D, ni suala tu la kawaida, uki-export zaidi unapata mapato ndani zaidi, uki-import zaidi unatumia mapato yako ya ndani zaidi kupeleka kwa watu wengine, kwa hiyo ni biashara tu ya kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe, kwa sababu tunatafuta ubunifu na mbinu zaidi kwa ajili ya kupata mapato kwenye nchi kwa sababu lengo si ni kuhakikisha kwamba Watanzania hawateseki? Sijaona. Nimeangalia mpango mzima, na nimeangalia kwenye hotuba nzima ya Mheshimiwa Waziri, sijaona kitu kinaitwa carbon marketing.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kutokana na mabadiliko makubwa ya tabianchi, nchi zenye misitu ikiwemo Tanzania sasa hivi zinafanya biashara ya carbon. Kwa hiyo nilitegemea kiwe ni chanzo kipya cha ubunifu cha kibiashara kwa ajili ya kuongeza pato kwenye nchi. Kwa hiyo niombe Mheshimiwa Waziri atusaidie kuelewa mpango wa Serikali kwenye masuala ya kufanya biashara ya carbon. Najua anajua carbon marketing.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende sehemu ya tatu na ya mwisho; sekta ya madini. Taarifa za Taasisi ya Jiolojia na Utafiti Tanzania (GST) inatuambia kwamba Tanzania tuna takribani critical minerals 24, kwenye utafiti ambao umefanywa na Taasisi ya Jiolojia na Madini Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Profesa amezungumza, lakini nafikiri tusaidiane kuelewa; ukisoma hotuba nzima ya Mheshimiwa Waziri, ukurasa wa 14 ambao amezungumza yeye kwenye hotuba masuala ya madini, ukurasa wa 68 ambao amezungumza masuala ya madini kwenye mpango, ukurasa wa 24 amezungumza masuala ya madini kwenye mpango, hakuna kitu kinaitwa critical minerals.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tofauti kati ya critical minerals na strategic minerals. Critical minerals ni madini muhimu, strategic minerals ni madini ya kimkakati. Madini ya kimkakati maana yake ni madini ya kusaidia kukuza uchumi. Madini ya kimkakati ndiyo tumeyazoea tangu mimi nasoma; kuna gold, tanzanite, aluminum na madini mengine ya kawaida ambayo yanatusaidia kukuza uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dunia inazungumza mabadiliko ya tabianchi. Wakati tunatoka kwenye mhamo wa nishati (energy transition) kutoka kwenye nishati ambazo ni chafu kwenda kwenye nishati safi tunategemea kuna soko kubwa la madini muhimu. Madini muhimu ni pamoja na graphite, lithium, helium, nickel, cobalt na mengine, yako 24. Waheshimiwa Wabunge waende kwenye websites za masuala ya energy, kuna International Energy Agency, wana website yao, ukiangalia tu kwenye tablet yako unapata information nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa masikitiko makubwa sana, kwanza Sheria ya Madini ya mwaka 2009 haizungumzi chochote kuhusiana na mhamo wa nishati (energy transition) kuelekea kwenye critical minerals. Na ni well and good kwa sababu tunataka tupate pato la nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Geological Survey of Tanzania, Tanzania ni ya tano kwa kuzalisha graphite lakini ina reserve ya tani milioni 18 ya graphite kweye ardhi. Na naomba niwaambie kwamba GST haina teknolojia ambayo ingetusaidia kujua zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nina uhakika kabisa kuna uwezekano mkubwa sana hiki tunachokisema inawezekana Tanzania ni ya kwanza duniani kwa sababu hatuna teknolojia. Kwa hii teknolojia yetu ya kawaida tu imesababisha tujue kwamba kuna tani milioni 18 kwenye ardhi. Sasa hapo hatujazungumza nickel, hatujazungumza rare earth minerals, kwa sababu hizi iPhones, Waheshimiwa wana iPhones hapa, iPhones zinatengenezwa na aina ya madini ambayo ni critical, yanaitwa rare earth elements.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia mhamo (transition) wa nishati unatusababisha twende kwenye nishati ya jua, twende kwenye nishati ya upepo. Hizo critical minerals 24 nilizosema Tanzania zipo kwa mujibu wa GST, zinatusaidia kutengeneza solar panels, wind turbines – Kiingereza hapo kidogo, lakini sasa hatuna Kiswahili chake – mitambo ya kuzalisha umeme wa jua, mitambo ya kuzalisha umeme wa upepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dunia inazungumza electric cars, kuna madini ambayo yanatengeneza electric car batteries. Kwa hiyo tuache kuzungumza kuhusu gold…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na nitachangia fungu 65, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majukumu ya msingi ya kuanzisha Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu. Miongoni mwa majukumu ya msingi ilikuwa ni kuandaa, kuratibu na kusimamia sera kanuni sheria na miongozo mbalimbali ya kitaifa na kimataifa yanayohusiana na masuala ya maendeleo ya vijana, kazi ajira, watu wenye ulemavu na hifadhi ya jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu randama na document zote zinazohusiana na Ofisi hii upande wa maendeleo ya vijana wamezungumzia shughuli ambazo zinaitwa shughuli za maendeleo ya vijana ni pamoja na wiki ya vijana kitaifa, pamoja na kumbukumbu ya Baba wa Taifa lakini na Mbio za Mwenge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haitoshi kwa sababu ukiangalia Integrated Labour Force Survey Review ya mwaka 2021 utaona vijana ni asilimia 57 ya labour force ya nchi yetu. Haitoshi kuzungumza vijana kwa nusu paragraph kwa kutaja hizi ndio shughuli zao ambazo zinaitwa shughuli za maendeleo ya vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo changamoto nyingi hatuwezi kuacha kuzungumza tatizo la ajira lakini siyo kwa ujumla wake ni tatizo la ajira kwa vijana kwa sababu ndio labour force, lakini pia tatizo la ajira kwa vijana wasomi hatuwezi kuacha kuzungumza hilo. Ukiangalia rate za graduate unemployment zinakua kila mwaka na tunatengeneza bomu bila kulielezea tunalitatua vipi, hatuwezi kuzungumza jumla jumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninasikitika sana kwa sababu hawa wanaozungumza hapa ambao ndio wanaoshiriki kwenye wiki ya vijana kitaifa, wanaoshiriki katika mbio za mwenge, na wanaoshiriki katika maonesho na kujitolea na midahalo ndio Ofisi ya Waziri Mkuu inazungumza kwamba ndio shughuli za vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya sana hata hicho kimfuko cha vijana kidogo ambacho kimetengewa bilioni moja. Ilitengwa bilioni moja mwaka 2022/2023 na haijapelekwa mpaka sasa hivi imepelekwa ziro haijapelekwa hata senti moja lakini hata mwaka wa fedha uliopita ambao ndio tuna malizia sasa hivi hata the previous year bado walipelekewa milioni 200 na wakaambiwa hawana vigezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Ofisi ya Waziri Mkuu ina programu za kuwajengea uwezo vijana, uanagenzi na vitalu nyumba vinaus na wana - graduate kwa qualifications za Ofisi za Waziri. Hata hawa ambao mmewa-train wenyewe hawana vigezo kiasi kwamba hamuwapi hizo pesa. Vijana hawatuelewi kwa sababu hawatuelewi tukisema wamekosa vigezo kwa sababu wana qualify kwa qualifications ambazo tumeziweka sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hizi ambazo mmezungumza lakini kuna changamoto nyingine. Kwa mfano vijana hawana jukwaa la kukutana ambako wanazungumza mambo yao, lakini pia vijana hawana sera ambayo inaendana na mabadiliko ya sasa hivi. Mabadiliko ya sayansi na teknolojia, masuala mbalimbali ambayo yanaendelea kwa sababu sera yetu ya vijana ni ya mwaka 2007 ambayo ina miaka 16 na iko outdated.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiingiza hii taarifa kwenye tablet yako, ukiingiza taarifa zote zinazosomwa ukaandika sera ya maendeleo ya vijana uka-enter hautapata information yoyote. Huwezi kuzungumza maendeleo ya vijana usizungumze sera yao ambayo ni outdated, haiwezekani. Kwa sababu sera ndiyo inatoa muongozo na inatoa utaratibu wa namna ambavyo masuala ya vijana updated kutokana na sayansi na teknolojia na mambo yanavyoendelea, kwa sababu inawezekana nyie mnazungumza lugha nyingine na vijana wanazungumza lugha nyingine, kwa sababu hamzungumzi lugha moja sera haipo updated. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa uchache sana naomba nizungumze kuhusiana na jukwaa la vijana kukutania. Mwaka 2015 Bunge hili lilitunga Sheria namba 12 ilioitwa Sheria ya Baraza la Vijana la Taifa ambayo mpaka leo ni miaka nane tangu tumetunga sheria. Tumetumia rasilimali za Serikali kutunga sheria ambayo haijawahi kutekelezwa tuna kigugumizi, lakini mpaka leo imepitia mwaka moja na miezi tisa tangu Mheshimiwa Rais atoe maelezo ya mwisho alivyokutana na vijana Mkoa wa Mwanza, Mwezi wa Sita 2021. Akaiambia Wizara inayohusika na masuala ya vijana waangalie nini kinaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama hiyo haitoshi, naomba nisome Sera ya Vijana ya Mwaka 1996, kwa kunukuu naomba ninukuu. Sera inaelezea sura ya 4, Ibara ndogo 4 (1)
(8) inaelezea kwamba kuwe na mtandao wa kupeana na kubadilishana habari kuhusu shughuli za maendeleo ya vijana, hiyo ni Sera ya Vijana ya Mwaka 1996. Sera ya Maendeleo ya Vijana Mwaka 2007 inatamka katika tamko la sera inasema Serikali itasimamia zoezi la kuundwa kwa baraza la vijana la Taifa na kutengeneza kanuni za usimamizi wa shughuli za baraza. Hiyo ni sera ya vijana, lakini African Youth Charter 2007 Ibara ya 11 inasema nchi wanachama watapaswa kuhakikisha ushiriki wa vijana katika Bunge na vyombo vingine vya maamuzi ipasavyo kama sheria inavyoelekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuratibu uanzishwaji au uimarishwaji wa majukwaa kwa ajili ya vijana kushiriki kufanya maamuzi ngazi ya chini kitaifa, kikanda na katika ngazi mbalimbali za kimataifa za kiutawala, lakini Katiba inayopendekezwa hii sio muhimu kwa sababu haijapitishwa; lakini pia Katiba inayopendekezwa well enough vijana walitoa mapendekezo kwamba jambo la vijana au baraza la vijana liingie kwenye katiba ya mapendekezo na yenyewe ilisema Serikali itaanzisha Baraza la Vijana la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tamko la Mheshimiwa Waziri Mkuu mwaka 2016 wakati anasoma Bajeti ya Serikali mwaka 2016/2017 alisema katika hotuba yake “ili kuimarisha dhana ya ushiriki na ushirikishwaji wa vijana katika shughuli za maendeleo, Bunge la Kumi lilitunga sheria namba 12 ya Baraza la Vijana la Taifa ya Mwaka 2015, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba sasa kanuni za utekelezaji wa sheria hiyo zimekamilika. Hivyo katika mwaka 2016/2017 Serikali itaendelea kuratibu uanzishwaji wa Baraza la Vijana la Taifa na kuhimiza ushiriki na ni uanzishaji na uimarishaji wa SACCOS za vijana katika halmashauri zote ili vijana waweze kushiri katika shughuli za maendeleo”. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo yote kuna kigugumizi gani kwenye Serikali kuhusiana na baraza, tunaenda kwenye mikutano ya nje ya nchi, nchi za wenzetu vijana wanaowakilisha vyombo vya vijana kwenye nchi zao wanakaa. Sisi kila mwaka tunasema tupo kwenye mchakato, tupo kwenye mchakato mpaka leo tupo kwenye mchakato, walikuwa vijana kipindi hiko wameshazeeka bado hatupati. Ninajua kuna vitu ambavyo vinasabaisha kwa nini hatuleti baraza, lakini ukisoma Sheria ya Vijana ina solution kwamba chombo kitakuwa cha kisiasa? Kuna utaratibu wa kinidhamu kwamba chombo kitakuwa hakina pesa? Sheria inasema vijana wataweza kupata ruzuku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiufupi ninatamani kujua nini kinaendelea kuhusiana na Sera ya Vijana ya Taifa, Sera ya Maendeleo ya Vijana lakini pia Baraza la Vijana la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nimalizie, Mwenge wa Uhuru; kwanza ni miongoni mwa champions wa hicho kwa uzalendo na kwa ukubwa wa Mwenge wa Uhuru. Nilikuwa miongoni mwa watu waliotoa maoni kwamba mwenge uingie katika urithi wa utamaduni wa dunia usioshikika; na tunaendelea ku-champion mwenye uingie pale na tunaheshimu mno, lakini Mwenge wa Uhuru was a political instrument design to propagates brotherhood and self-reliance brotherhood philosophy. Ulikuwa ni nyezo ya kisiasa kupropagandisha falsafa ya ujamaa na kujitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunazungumzia Diplomasia ya Uchumi na tumesema nchi imefunguka bado tunakimbiza mwenge tena very unfortunately. Nakuomba nisome barua ambayo inatoka kwa Mkurugenzi wa Mji wa Ifakara. “Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Halmashauri ya Mji wa Ifakara, Mchango katika kufanikisha Shughuli za Mwenge wa Uhuru Mwaka 2023”. Nitasoma para ya pili, “kwa barua hii napenda kukujulisha kuwa unapaswa kuhamisha walimu katika shule yako kufahamu falsafa ya Mwenge wa Uhuru ili kushiriki na kuchangia fedha za kufanikisha shughuli ya Mwenge wa Uhuru 2023 kwa mchanganuo wa shilingi 50,000 kwa wakuu wa shule na 5,000 kwa waalimu wa kawaida”, sasa mwenge? Look at this! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaenda vizuri, nchi imefunguka Mama anafanya mambo makubwa wasaidizi wake wapo ambao wanamsaidia, what is this? Hii inawashushia credit, mbona sisi hatujawahi kuchangishwa hapa Bungeni hata 100 kuchangia mwenge, sijawahi kuona barua kwa sababu na sisi tuletewe Mwenge wa Uhuru, Waheshimiwa Wabunge kupitia Bunge lako changieni milioni kumi kumi tukakimbize mwenge. Mimi nafikiri sasa kama ni msingi…

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, … ni kitu cha msingi the you don’t have to do this, why are you doing this?

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nusrat kuna taarifa. Mheshimiwa Naibu Waziri.

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa nafasi hii. Pamoja na mchango mzuri wa Mheshimiwa Mbunge, naomba kumpa taarifa kwamba katika suala la Mwenge wa Uhuru, kwanza ni tunu ya Kitaifa ambayo mwenge ukizungumzia suala la mwenge ni falsafa. Usione kama kile chombo, falsafa inayobeba ni kuhusiana na Utanzania wetu, Utaifa wetu, uzalendo wetu, mafunzo kwa ajili ya vijana lakini zaidi ya hapo ni chombo ambacho kinapita nchi nzima kuangazia na kumulika kwa sasa kuangalia value for money katika miradi ya maendeleo ambayo fedha nyingi zinaenda kwa ajili ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini zaidi ya hapo masuala ya uadilifu yanaangaziwa na mwenge. Sasa ukisema kuhusiana na suala la michango, michango ni hiari ni uzalendo wa watu hakuna utaratibu wala kanuni zinazoelekeza watu wachangishwe fedha kupitia mwenge wa uhuru. Kwa hiyo, kama aliandika huyo Mkurugenzi ni kwa utashi wake lakini sio kwa utaratibu ambao upo kwa mujibu wa sheria na utaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini zaidi ya hapo nipende pia kutoa taarifa kuna eneo amelieleza mchango ni mzuri, lakini si vyema sana ikienda tofauti huko nje, kwamba katika fedha alizosema za vijana ile bilioni moja katika mwaka huo wa fedha tulitoa bilioni 1.8 ambayo imekwenda na sasa tayari Wizara ya Fedha imeji-commit kwamba tutapata fedha hizo awamu ya pili ya mwaka ule wa fedha kutoa ile bilioni 1 kwa ajili ya vijana hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kuhusu masuala ya vijana kwa ujumla, hata bilioni tisa nyingine zilitolewa kwa ajili ya kutoa mafunzo ya ukuzaji ujuzi kwa ajili ya vijana. Kwa hiyo, Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan, yupo makini na vijana wake, anajua wakati gani anawapa fedha na wakati gani anatengeneza utaratibu wa kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana sisi ni kipaumbele katika Taifa hili na Mama amesema ukichezea vijana wake basi utaweza kumuona kwenye sura zote. Mheshimiwa Rais anawaangalia vijana, nikuhakikishie Mheshimiwa Hanje hata wewe ni mmoja wa vijana ambao Mheshimiwa Rais anakuangalia kwa jicho kama kiongozi mzuri wa baadaye. Tuendeleze uzalendo wetu, tutunze Tunu zetu za Taifa na tujisimamie katika kuhakikisha kwamba Tanzania yetu tunabaki kuwa salama, ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Nusrat unaikubali taarifa.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, barua imeandikwa unapaswa kuchangia na kama ni uzalendo tunatakiwa tuanze sisi kwa sababu mimi mwenyewe ni mzalendo. Tuanze humu tuchange milioni 20, milioni Hamsini Hamsini. Mwenge unaenda kumwaga gongo. Kuna Kamati ya Bunge inaenda kukagua miradi, tuna CAG anakagua miradi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Mpango wa Maendeleo wa Mwaka Mmoja. Nitachangia katika maeneo mawili; eneo la kwanza nitachangia kwenye elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekaa kwenye kikao hiki kwa ajili ya kupanga mpango wa maendeleo, lakini maendeleo ni elimu. Yaani elimu yetu kama Taifa ndiyo inachora ramani ya maendeleo. Tunazungumza, tunajadili, lakini kama hatutazungumza elimu, tutakuwa hatujatendea haki Taifa hili. Muda sasa tumekuwa tukijadili kuhusiana na kurekebisha Sera ya Elimu nchini ambayo ni ya mwaka 2014 na kurekebisha mtaala wa elimu ambao ni competence- based lakini 2005 mara ya mwisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili sisi kama Wabunge ambao tunapewa hizi nyaraka na tunasoma, tuone kama uhalali wetu wa kujadili haya upo, tunatakiwa tuyaone katika Mpango. Siyo kwenye bajeti wala siyo kwenye Mpango huu wa mwaka mmoja Wizara imetenga hata senti moja kwa ajili ya kufanya mchakato wa mapitio ya sera na mapitio ya mtaala wa elimu. kwa kifupi mpaka sasa Serikali haijatenga hata shilingi moja kwa ajili ya ku-facilitate wanaofanya mchakato wa mapitio ya sera na mapitio ya mtaala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia ratiba yako, wewe unafahamu zaidi na namna ambavyo tunapanga mambo yetu, unajua kwamba possibility ya kufanikisha tunachokizungumza kila siku ni ama 2023 au 2024 kwa sababu watu hawawezi kwenda kufanya kazi ngumu ya kukusanya maoni na kufanya mapitio, kuita wadau ambao ni professionals, ambao ni Watanzania ambao wanaitakia mema nchi hii, bila kutumia gharama. Haiwezekani! Kwa hiyo hapo nimesema kwa kweli kwa kutoa masikitiko yangu sana kwa sababu nilitegemea mpango uwe na at least hata pesa kidogo kwa ajili ya kuanza mchakato wa mapitio ya mtaala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nitakuwa nimekwenda mbali sana Wizara ilishakutana na Wajumbe wa Kamati inayohusiana na masuala ya elimu, Kamati ya Huduma na kwa taarifa zilizopo ni kwamba tarehe 11 Novemba wanakutana na Wabunge wote kwa ajili ya kupokea maoni. Sasa naomba niombe sasa badala ya kujadili kuhusiana na mtaala, wajadili kuhusiana na sera, kwa sababu kwa taarifa Wizara inajaribu kurekebisha mtaala na sera at the same time, kitu ambacho hakiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtaala ni zao la sera. Bunge lako litusaidie kuifanya Serikali ituletee mjadala wa kujadili Sera ya Elimu tarehe 11, siyo mtaala wa elimu. Nasema hivi kwa sababu hatuwezi kujadili sera hatujapanga tutafanya nini kutoka mwaka 2014 kwenye sera. Wabunge sehemu pekee ambayo tunaweza kuchangia sisi, ni tunaiona wapi nchi yetu after few years to come, ndiyo tutaeleza malengo. Tafsiri ya tunapotaka nchi yetu ifike ndiyo itatuambia tuandike nini kwenye sera ili sera ikatusaidie watu wanaoandika mtaala wakatoe tafsiri ya tunataka nini kwenye elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanzo nilisema maendeleo ni elimu. Kwa hiyo kama tunapanga mpango wa maendeleo na hatujadili kuhusu nchi yetu tunataka kwenda wapi. Nitatoa mfano, Kenya wametoka kwenye competence-based, CBC – Competence-Based Curriculum na sasa wanajadili talent and professions, talanta na taaluma. Walishafanikiwa kwenye competence-based.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2005 wakati tumefanya marekebisho ya mtaala ndiyo tuliweka Competence-Based Curriculum ambayo tunayo mpaka sasa hivi. Tukiletewa Waheshimiwa Wabunge wataona kwamba hatuna shida kwenye documentation kama nchi, yaani utashangaa kwani huwa tunajadili nini kuhusiana na kurekebisha mtaala. Kwa hiyo kuna shida kutoka kwenye mtaala kwenda kwa anayepelekewa, yaani kuna shida kutoka kwenye kilichoandikwa na kinachomfikia, katikati hapo ndiyo kuna shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo nitapongeza jitihada ambazo zimefanyika kwa sababu kwenye mpango wametuambia kuhusiana na, kwa kweli tunahitaji maeneo ya kujifunzia; madarasa, Walimu na vitendea kazi. Kwa hiyo tunahitaji na tumeona kwenye Mpango wameweka. Kama mdau wa elimu siwezi ku-ignore jitihada ambazo zimefanyika. Kwa hiyo tuna-encourage sana jitihada, lakini tukumbuke kwamba dunia haitusubiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dunia inazungumza Mapinduzi ya Nne ya Viwanda (Fourth Industrial Revolution) ambayo inazungumza artificial intelligence, inazungumza algorithm, vitu ambavyo vina-replace human labour. Sisi tunazungumza competence based education ambayo inafundishwa kwa knowledge based education. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtaala wa 2005 unatuambia competence based lakini kinachokuwa delivered darasani ni knowledge based. Knowledge based maana yake mwanafunzi anasoma, anakariri na kukariri ili akafanye mtihani knowledge-based, unajaziwa madude kibao. Kwa hiyo sasa kwa sababu hatutakwenda huko leo, naomba sana kwa sababu tunatumia rasilimali zetu vizuri, dunia inazungumza hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi wakati tunasema dunia inazungumza artificial intelligence, nimpongeze sana Rais, Dkt. Mwinyi na kwa sababu kwenye umri wa vijana tunam-consider kama bado kijana mwenzetu, amejitahidi, kwa sababu amezungumza kuhusu digital currency na imechukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais pia kwa sababu anajaribu kuona opportunities. Kwenye hili nitasubiri mjadala ambao tutajadili Sera ya Elimu ambayo tunasubiri muda mrefu kwa sababu ya resources, twende kwenye sera kwanza, tuone mwelekeo wa nchi kwenye elimu tunataka nini, halafu ndiyo tuje tujadili mtaala, kwa sababu najua pia resource scarcity.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ni-move kwenye jambo la pili ambalo ni la jumla. Mimi ni Mbunge kijana, thinking yetu sisi millennials na hili nitalisema na watu wanaojua generation differences watakuwa wanaelewa. Asilimia kubwa ya Watanzania na asilimia kubwa ya Waafrika wanaitwa millennials, watu waliozaliwa mwaka 1980 mpaka mwaka 1996; thinking, smartness, activeness, watu tunataka matokeo, tupo wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani tukawa tunaendelea kuendesha nchi kwenye mfumo wa tunapanga, kesho tunapanga tena na tena, the same way. Tunaomba tu-move. Tupo wengi tunaomba tu-move, yaani inawezekana kabisa. Watanzania wanataka majibu ya shida zao. Kwa maana tuwe tuna flagship projects, watu wanataka pesa mfukoni, watu wanataka bima za afya, wanataka price fluctuation (mfumuko wa bei) usiwepo, wanataka kula, wanataka wafanye kazi, projects zote tunazoziweka tunazitambua na ni vitu vizuri; progress, miradi mikubwa. Hata hivyo, tunakuwa irrelevant kama nchi kwa sababu Watanzania hawaoni kama hayo mambo yanawagusa directly. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ninachojaribu kusema ni kwamba, Watanzania wanataka majibu ya shida zao na shida zao tunazijua kwa sababu ndiyo wapigakura wetu. Kwa hiyo nchi ambayo inashindwa kutoa majibu ya watu wake definitely at the end of the day inakuwa irrelevant, inakuwa haiishi wanachokitaka wapigakura.

Kwa hiyo hatutachoka kuongea, hatutachoka kushauri kwa sababu haiwezekani sekta ambayo kila Mbunge akiongea anazungumza; kilimo, tunapata chakula, inachangia pato la Taifa, lakini kila mwaka tunapanga the same. Kwa nini hatuweki pesa kwenye kilimo? Inachosha na inavunja moyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naongea kwa sababu hii nchi, mimi Muislam, kuna kitu kinatwa masuulia, yaani ukiwa una nafasi kwenye Taifa unatakiwa ufanye maamuzi, ukishindwa kufanya maamuzi, kesho Mwenyezi Mungu atakuhoji kwa kushindwa kufanya wajibu wako.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hanje kengele ya pili hiyo.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania wanataka majibu ya shida zao, naomba tuwasaidie kuwapatia. (Makofi)
Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuanzia Januari, 2021 hadi Februari, 2022 pamoja na Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kwa Kipindi cha Januari 2021 hadi Januari 2022
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia kuhusiana na hotuba ya Kamati ya Viwanda na Bishara lakini pia Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kuna vitu tunavikosea sana, mathalani…

(Hapa Mhudumu wa Bunge alimkabidhi nyaraka zake)

MBUNGE FULANI: Hajajipanga huyo.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, na samahani kwa hicho kilichotokea, maana ni kama nimekuwa ambushed, na pia sijawahi kuchangia kutoea upande huu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza leo tarehe 11 Februari ninachangia, itakumbukwa kwamba leo ni Siku ya Kimataifa ya Wanawake na Wasichana katika Sayansi. Na jana imesomwa taarifa ya Kamati ya Sayansi na Teknolojia, lakini ninyi nyote ni mashahidi kwamba sayansi, teknolojia na ubunifu, suala la ubunifu ni suala ambalo kama halitambuliwi vizuri na Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hivi tunavyozungumza Taifa hili linatambua sayansi na teknolojia ambayo kuna Sera ya Sayansi na Teknolojia ya mwaka 1996, lakini pia kuna Wizara ya Teknolojia na Mawasiliano ambayo ina teknolojia, halafu kuna Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, zote hazina neno ubunifu, kwa maana ya innovation.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ninyi nyote ni mashahidi, nchi zote ambazo tunazitolea mfano kwenye Taifa hili, kwamba ni nchi ambazo zimefanya vizuri kwenye masuala ya viwanda na biashara, kama nchi ambazo zimefanya vizuri kwenye biashara na kwenye maendeleo, kwa maana ya nchi ambazo zimeendelea wote wamefanya vizuri katika masuala ya sayansi na teknolojia, lakini pia na ubunifu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo sisi kama Taifa tuna Wizara nyingi, yaani kama kuna Wizara ambazo hazihusiani na masuala ya sayansi, teknolojia na ubunifu (STI) hazizidi tano, hazipo. Wizara yenyewe ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji inahitaji innovation science and technology. Pia Wizara ya Afya inahitaji science innovation and technology, Wizara ya Elimu, Wizara ya Kilimo yenyewe pia, zote zinahitaji science, technology na ubunifu kwa maana ya innovation.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hatutapiga hatua kama taifa kama hatutakuja kuharakisha na kufanikisha mchakato wa sera itakayoitwa Sera ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu. Kwa sababu mpaka sasa hivi tunavyozungumza sera hiyo ina miaka 28. Tumeanza kuipigia kelele tangu tuko nje, hatujaingia kwenye Bunge hili mpaka sasa hivi. Itakapokuja kufika hatua kwamba sera inaletwa itakuwa outdated kwa sababu tunakusanya maoni leo. Tutakaa miaka 10 ijayo ndipo tuje tulete sera ambapo maoni yamekuswanywa leo, maana yake hatutakuwa tumefanikiwa. Kwa hiyo, ili tufanikiwe tunahitaji kuwa Sera ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kwenye viwanda na biashara Sera ya Maendeleo ya Viwanda Vidogo na Biashara Ndogo ina miaka 19, ni ya mwaka 2003. Lakini pia Sera ya Taifa ya Biashara ina miaka 19; ni ya mwaka 2003, iko outdated. Waheshimiwa Wabunge mkumbuke kwamba life span ya sera ni miaka kumi. Kwa hiyo, tuna sera ambayo tunategemea ituletee maendeleo kama Tanzania ya Viwanda, sera ambayo ina miaka 19 hatuwezi kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Taifa mpaka sasa hatuna Sera ya Taifa ya Ubora, hatuwezi kufanikiwa. Watanzania wenye biashara ndogo ndogo na biashara ndogo sana hawajui kuhusiana na blue print, sisi tunajua blueprint. Hatuwezi kufanikiwa kama Taifa, na ni lazima tuvuke hatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuwezi kufanikiwa hata kama tuna Tume ya Ushindani (Fair and Competition Commission) kwa sababu hatuna innovation. Vitu vyote vinahitaji watu wafikiri, sasa sisi kama nchi hatujajipanga kuhakikisha kwamba tunasaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nitoe ushauri kwa Serikali, umefika muda sasa iundwe wizara maalum iitwe Wizara ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu. Kenya, Rwanda, Burundi, Uganda, Malaysia pamoja South Africa wamefanya hivyo na wamefanikiwa, ukiachana na China na nchi nyingine ambazo zinaonekana ni first world…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye taarifa ya Kamati ya UKIMWI lakini taarifa ya Kamati ya Nishati na Madini. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Nishati na Madini, lakini nitachangia maeneo mawili kwenye Kamati ya Nishati na Madini, upande wa nishati na upande wa madini na muda ukibaki nitachangia jambo la tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza upatikanaji wa umeme katika Grid ya Taifa nchini, kwa ujumla ukweli uhitaji wa umeme kwenye nchi yetu ni mkubwa sana ukilinganisha na umeme ambao tunao. Labda nitaje vyanzo vya umeme ambavyo vina-feed kwenye Gridi ya Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, chanzo kikubwa kinacho-feed Gridi ya Taifa kinachoongoza ni gesi asilia ambayo ni asilimia 62 ambayo ni megawati 1,103 lakini kuna umeme wa maji megawati 574 sawa sawa na asilimia 32 lakini kuna chanzo cha mafuta ambayo ni megawatit 88.13 sawasawa na asilimia 4.96 lakini umeme kutokana na tungamo taka ambayo ni megawati 10.50 sawasawa na asilimia 0.57 ambayo inatengeneza jumla ya megawati 1,777 ambayo ni asilimia 100 ya umeme wetu nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, jitihada za Serikali tumeziona kwa sababu mradi wa umeme wa Mwalimu Nyerere unaweza kwenda kutengeneza megawati 2,115 ambayo itaongeza nguvu kwenye Gridi ya Taifa kufikia megawati 3,892.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimetaja takwimu hizi ili tuone namna ambavyo bado tunauhitaji mkubwa wa umeme kwenye Taifa, na ni lazima watu wafahamu kwamba pamoja na miradi, huu ni mradi mkubwa kabisa ambao nimeutaja kwa sababu ni mradi ambao ni flagship ni mradi ambao ni wa kimkakati na ni mradi ambao wote tumetolea macho huko, lakini bado hata tiukipata megawati hizi bado uhitaji wa umeme ni mkubwa sana kwa sababu tunategemea umeme nchi nzima, kuna biashara, kuna maisha ya kawaida ya Watanzania kwa hiyo uhitaji bado ni mkubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni miongoni mwa watu wanaoamini katika nishati jadidifu ikiwemo mradi wa Mwalimu Nyerere ndiyo maana tunaushikia bango kwamba mradi wa Mwalimu Nyerere ni lazima ukamilike, kwa sababu ukikamilika tunaongeza base- load kwenye Gridi ya Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda niseme kitaalamu ili uzalishe umeme wa nishati jadidifu nyingine kama nishati ya upepo na nishati ya jua ni lazima base-load iwe na umeme ambao ni sufficient umeme ambao ni wa uhakika na ni umeme wa maji pekee ambao ndiyo umeme pekee wa uhakika dunia nzima. Kwa hiyo, kukamilisha umeme wa Mwalimu Nyerere ni kuongeza base-load ili tuweze ku-feed kwenye Gridi ya Taifa kwenye umeme mwingine, kwenye nishati jadidifu kwa sbababu kuna madhara mengi sitayazungumza hapa kuhusiana na sasa hivi chanzo cha umeme ambacho kinaongoza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama sasa hivi tungekuwa tumekamilisha mradi wa Mwalimu Nyerere kama ambavyo ilitakiwa mwanzo, tungekuwa bado hatuwezi kuutoa umeme pale kwenye mtambo Selous Bwawani kuupeleka kwenye kituo, kwa sababu transmission line imefika asilimia 83.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu umeme pale tunaweza tukaona mitambo inafanya kazi lakini kuutoa pale kuupeleka kwenye kituo cha kupoozea umeme kuna line inatakiwa ijengwe iko asilimia 83 haijakamilika. Kwa hiyo, kama ile kudra za Mwenyezi Mungu paap maji yamejaa Mwalimu Nyerere hatuwezi kuutoa ule umeme tutabaki tunauangalia pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kituo cha kupooza umeme Chalinze ambapo ndiyo umeme ule unaenda kupoozwa pale, kiko asilimia 47. Kwa hiyo, niseme naomba nipendekeze kwenye maazimio, Bunge hili liitake Serikali kuharakisha ujenzi wa transmission line kupeleka kwenye kituo lakini pia kujenga kituo cha kupooza umeme cha Chalinze, kwa sababu maji mvua zinaendelea kunyeesha tumeshafanya marekebisho huko kwenye vyanzo vya maji ambavyo vina-feed Bwawa la Mwalimu Nyerere, hamadi! bwawa limejaa hatuna sehehmu ya kupeleka umeme, hatuna njia, hatuna mtambo, maji yanaendela kujaa. Kwa hiyo, tuweke pia azimio la kuhakikisha kwamba transmission line na kituo kinajengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni Mwanza Refinery, mwaka 2021 Juni, Mheshimiwa Rais Samia alizindua kituo cha kusafisha dhahabu cha Mwanza kwa masikitiko makubwa sana mpaka leo bado kituo hakijapata ithibati na sababu ya ile refinery ya Mwanza kukosa ithibati ni kwa sababu hatuna rasilimali ya kutosha ku-feed ile refinery tuliyoijenga pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge hili mwaka 2017 lilitunga sheria inaitwa Sheria ya Madini ya mwaka 2017 ambayo sheria hiyo Sura ya 123 kifungu cha tisa, lengo lake ilikuwa ni kwamba dhahabu inayozalishwa Tanzania kabla haijapelekwa nje isafishwe hapa ili kuiongezea thamani, na lengo lilikuwa zuri. Mikakati ya Serikali kwa sababu mtu hawezi kuelewa, kwa siku kile kiwanda kinahitaji kilo 59 sawasawa na kilo 1,770 kwa mwezi kile kiwanda kinahitaji ili kifanyekazi, kinakosa ithibati kwa sababu hatuna rasilimali ya kutosha ku-feed kile kiwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchakato ya Serikali wanataka wakanunue dhahabu Congo it is well and good, lakini mimi nazungumza kwa ajili ya Watanzania, vijana ambao tunataka tufaidike na value chain, mnyororo wa thamani, ardhi yetu Tanzania ina dhahabu. Kwa sababu hilo soko la Congo, East Africa yote inaangalia soko la Congo, Rwanda wanaangalia soko la Congo na nchi nyingine, kwa sababu sidhani kama Wakenya nao hawaangalii, soko la Congo ni probability. Hebu tuangalie hapa Tanzania dhahabu yetu kweli haitoshi ku-feed kile kiwanda mpaka tuende Congo? Ni kweli ni initiative nzuri kwa sababu tunataka wauze hapa na maendeleo yataendelea vuzuri nami niwapongeze, lakini GST imekosa uwezo wa kusaidia vijana wetu kiteknolojia, kuwafanya vijana wetu wapate uhakika na sampuli za madini wanazozipeleka pale, kwa sababu eti hatuna certified reference materials, kutoa ithibati, kuthibitisha uhakika wa madini yanayopatikana ardhini matokeo yake tunategemea nchi nyingine zituuzie dhahabu wakati vijana wetu nasi tunataka waendelee!

Mheshimiwa Naibu Spika, tumechoka kuona migodi kule Mwanza yamebaki mashimo vijana wetu wamebaki na umaskini, tunatamani tushiriki kwenye mnyororo wa thamani ili nasi tuendelee na tunufaike. Kwa hiyo niwaombe sana liongezeke azimio la kuitaka STAMICO na GST ishirikiane kwa ukaribu kutafuta mbadala, kutafuta suluhisho la dharura ili GST iwe na uwezo wa kiteknolojia na hizo sampuli zinazopelekwa pale kwenye maabara za GST zituletee majibu ambayo yana uhakika ili vijana wetu wakachukue mikopo benki na hayo majibu ya GST, waende wakachimbe dhahabu, dhahabu iende ika- feed Mwanza refinery kwa sababu mwaka mzima tumeshindwa, ni kitu ambacho hakiwezekani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kile kiwanda kinauwezo mkubwa kwa sababu kwa viwango vya kimataifa kile kiwanda kinauwezo wa kusafisha dhahabu 99.9 purity ambao tunaweza tukawa ni kiwanda kikubwa Tanzania na Afrika ikiwezekana hata Afrika Mashariki, kwa hiyo ni kitu kikubwa, haiwezekani tukawa tumepoteza rasilimali mwaka mzima kama hivyo halafu ikabaki hatusemi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda kuna jambo moja ambalo limefanyika for the first time in our country, Mfuko wa Nishati safi ya Kupikia (Cook Fund). Ninaipongeza sana Wizara ya Nishati pia ninaipongeza Serikali kwa ujumla, kwa sababu ni miaka mingi lakini for the first time tumefanya mjadala wa Kitaifa kuhusiana na nishati safi ya kupikia, na kwa sababu mimi ni mama pia napika lakini pia natoka kijijini kabisa ambako tunajua kwamba…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa sababu ya muda na umenipa mchache sana naomba niongee kwa kifupi sana.

Kwanza nashukuru kwa kupata nafasi na mimi niweze kuchangia huku na nitachangia upande wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia 57 ya nguvu kazi ya Taifa kwa mujibu wa Integrated Labour Force Survey ya mwaka 2021 ni vijana, lakini asilimia kumi tu kati ya vijana laki nane plus wanaoingia kwenye soko la ajira ndio wanaopata ajira rasmi. Lakini pia sekta binafsi inaajiri asilimia 64.9 ya vijana wote wanaoingia kwenye soko la ajira ambao ndio nguvu kazi ya Taifa, lakini pia findings za Inter-Universal Council of East Africa inasema asilimia 61 ya vijana wanaoingia kwenye soko la ajira, they are not fit for the job, yaani they are not cooked well natumia lugha hiyo, lakini wao wanasema asilimia 61 ya vijana wa Tanzania walifanya kwa East Africa yote inaonekana hawana uwezo wa kuajirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetaja hizi takwimu kwa haraka haraka na nimezijumuisha, nataka tu tuone namna ambavyo vijana ndio msingi tunapozungumza suala la ajira. Vijana ndio centre yaani ndio msingi na ndio mhimili mkuu kwenye sekta ya ajira kwa sababu ndi nguvu kazi ya Taifa. Lakini kwa takwimu hizi tunaona kwamba sekta binafsi ndio inaajiri kwa kiwango kikubwa sana kuliko public sector. Kwa hiyo, maana yake michakato na miundombinu yote tunayoitengeneza kwa ajili ya kuhakikisha tunaijengea uwezo sekta binafsi ili iendelee kuajiri, iendelee kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ya Kamati inasema kwamba kuna fedha asilimia 79 ambazo ziko kwenye Mfuko wa Maendeleo ya Vijana zimebakishwa huko kwa sababu vijana hawana vigezo na hiyo ndio tunategemea wachukue fedha hizo waende sekta binafsi wakajiajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wakitusikia kwenye taarifa tunasema kuna fedha asilimia 79 zimebaki na ni milioni 200 tu ndio zimepelekwa kati ya bilioni moja ambayo ilitengwa hawatuelewi kwa sababu kuna MAKISATU, vijana wanafanya ubunifu mkubwa wanatakiwa wawezeshwe halafu tunasema kuna pesa zimebaki kwa sababu hawana vigezo, hawatuelewi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitaje kwa kifupi sana na kwa sababu ya muda vigezo ambavyo tunavipeleka kwenye soko la ajira. Kigezo cha kwanza ambacho kipo kwenye soko la ajira ili kijana aajirike Tanzania anahitaji kuwa na uzoefu miaka miwili hadi 15; kigezo cha pili anatakiwa awe na elimu degree, PhD, Masters, certificate na diploma kwa uchache sana; lakini cha tatu anatakiwa awe na soft skills, lakini taarifa ya Kamati inatuambia kwamba Serikali imeweka mkakati wa kuwajengea uwezo wa hivi vigezo hawa wahitimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi shida yangu iko kwa nini Serikali itengeneze mkakati wa kuwajengea uwezo wakati tuna mfumo wa elimu ambao kila kijana ni lazima apite kwenye nchi hii? Ni kwa nini hizi soft skills, hizi soft skills ninajua ndio uwezo wa kutatua migogoro, uwezo wa kuchangamana kazini, uwezo wa ubunifu, uwezo wa kuhimili mikiki mikiki, hizo ndio soft skills, confidence, self esteem ndio hizo life skills, kwa nini zisiwe integrated kwenye mfumo wa elimu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio maana niliwahi kuzungumza kwa nini tusilifanye life skills liwe somo ili wasome mwanzo mwisho? Hivi takwimu zinazotuambia kwamba asilimia 61 ya wahitimu wa vyuo vikuu hawana uwezo kwa ajili ya kazi mpaka wakapate skills nyingine, kwa sababu unafikiri watafanya nini wanaposema tunakwenda kuwajengea uwezo ili waajirike? Ni kwenda kuwaambia hivi vitu, sasa hatuwezi kuwa tunazungumza vitu hivi kila siku. Kwa sababu hii taarifa ni kama wamei-copy na kui-paste, Sera ya Vijana hatuna mpaka leo tunazungumza sera za 1996 na sera ya mwaka 2007 leo miaka 16.

MWENYEKITI: Haya ahsante sana Mheshimiwa Nusrat, ahsante sana.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Bajeti ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, na nitachangia upande wa Fungu 31, Idara ya Mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mazingira kwa umuhimu wake ni jambo ambalo mpaka sasa naona hatujalipa umuhimu wa kutosha kama ambavyo linastahili. Labda nitaje sekta ambazo zinaathirika kwa namna moja au nyingine na suala la mazingira, kwa namna zozote zile; sekta za maji, kilimo, afya, miundobinu na uchukuzi, nishati, madini, mifugo na uvuvi, maliasili na utalii, viwanda na biashara, teknolojia, elimu and the list goes on.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka hapa tulipo sisi kila Mbunge anawakilisha jimbo analotoka, kwa namna moja au nyingine hawezi kukwepa kuzungumza suala la mazingira na sasa hali ilivyo, mabadiliko ya tabianchi. Lakini inasikitisha kwamba upangaji wetu na mgawanyo wa fedha katika bajeti zetu za miaka ya fedha kwenye sekta ya upande wa maendeleo kwenye upande wa mazingira hatujatendea haki sekta na idara ya mazingira kama ambavyo inastahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, labda nitaje kwa mfululizo miaka ya fedha mitatu mfululizo; fedha za miradi ya maendeleo zimetengwa kwa kutegemea sana fedha za nje katika kiwango kilichokithiri. Mwaka 2021/2022, Bunge liliidhinisha shilingi bilioni 2.979, lakini asilimia 86.54 ya fedha hizi zilikuwa za nje, sawa na shilingi bilioni 2.570. Fedha za ndani zilikuwa milioni 400 tu ambayo ni sawa na asilimia 13.54, ndiyo hizo pesa zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2022/2023 Bunge liliidhinisha jumla ya shilingi bilioni 18.642, lakini fedha za nje zilikuwa asilimia 98.5, sawa na shilingi bilioni 18.360. Fedha za ndani ambazo ni za kwetu zilikuwa asilimia 1.5, sawa na shilingi milioni 282 hivi; hiyo ndiyo pesa yetu sisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka huu wa fedha, Serikali imeomba shilingi bilioni 16.656, lakini tunategemea shilingi bilioni 15.056 fedha za nje, sawa na asilimia 90.4. Lakini fedha za ndani, za kwetu sisi sasa, ni shilingi bilioni 1.6 pekee.

Mheshimiwa Naibu Spika, atahari ya kutenga fedha kwa kutegemea fedha za jirani, fedha za wahisani, fedha za nje, ili upange mipango yako, ni sawasawa na sikukuu imefika unataka upike pilau lakini wewe una sufuria na mwiko, unategemea kila kitu pamoja na nyama na kuku na kila kitu kutoka kwa jirani. Jirani akiuguliwa, akifiwa, akiwa anapigana vita, wewe huwezi kula athari yake ni kubwa. Labda nikiongea hivi inawezekana ikawa lugha nyepesi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe mfano. Mwaka 2017, Mfuko wa Green Climate Fund (GCF) ulitenga fedha kwa ajili ya Mradi wa Climate Change wa Mkoa wa Simiyu Dola milioni 187.7, lakini fedha hizo hazikuletwa zikaweza kuletwa mwaka 2020. Kutoka mwaka 2017 athari zimetokea, mradi umefanikiwa kupita kwenye vigezo vyote vya kupewa fedha lakini fedha imeletwa mwaka 2020. Kwa sababu anayetoa fedha ndio anayechagua wimbo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, athari zilizosababisha watu wa Mkoa wa Simiyu wapewe hizi fedha bado zinaendelea. Lakini kwa sababu tumeomba fedha kwa wahisani – na ni kitu kizuri, sisemi kwamba ninabeza kwamba haifai kupewa fedha za wahisani – lakini kuitegemea fedha za nje kwa kiasi hiki, zaidi ya asilimia 90, maana yake unashindwa kutekeleza miradi yako kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sekta nyingine zote nilizozitaja hapa zimetengewa fedha za ndani. Utekelezaji wake unategemea hizi fedha.

TAARIFA

NAIBU SPIKA: Taarifa.

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba hata hizo fedha ambazo mradi unatekelezwa kule Simiyu ziliombwa kupitia Save the Children Fund, Tawi la Canada. Kwa hiyo, hoja yake ni ya msingi sana kutenga fedha za kutosha hata hapa ndani. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Nusrat, taarifa hiyo.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, napoikea taarifa hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu chako ukikiuona ni cha muhimu utakipa first priority na utakitengea fedha. Bahati mbaya sana Serikali inapeleka fedha kutoka kwenye vyanzo mbalimbali kwenye sekta nyingine ambazo nilizitaja hapa ambazo zinaathirika kwa namna moja au nyingine na mazigira. Lakini fedha hizi utekelezaji wake pia unategemea stability ya mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunashindwa kutekeleza miradi ambayo Serikali imeitengea fedha nyingi kwa sababu ya athari za mabadiliko ya tabianchi na athari za kimazingira. Kwa hiyo, tunasababisha kupoteza wakati mwingine rasilimali za nchi kwa sababu hatuja-prioritize kutoka kwenye vyanzo vyetu vya uhakika ambavyo ni vya ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda nitoe mfano. Mwaka huu ili tuone umuhimu wa kutenga fedha kutoka kwenye vyanzo vya ndani – mwaka huu wa fedha hizi shilingi bilioni 1.6 ambazo ndiyo chanzo cha ndani, asilimia 9.6 ya fedha za ndani kwenye mwaka huu wa fedha, hizi zinakwenda kujenga vitu vya msingi sana, wameongea watu wa kutoka upande wa pili wa Muungano, tunakwenda kujenga kingo ya Mikindani, Mtwara na Sipwese, Pemba kule, kwa hiyo unaona umuhimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tutakuwa na projects za namna hii ambazo zinaangalia palipoathirika zaidi na kwenda kutafuta namna ya ku-solve pale kutoka kwenye vyanzo vyetu vya ndani, sisi ndiyo tutakuwa tumetoa fedha na wimbo tumechagua sisi maana yake tunakwenda kutibu athari za mabadiliko ya tabianchi ambazo wananchi wanaziona moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, labda nizungumze jambo la pili kwenye climate funding. Green Climate Fund ndiyo mfuko mkubwa ambao Shirika la Umoja wa Mataifa la kukabiliana na Athari za Mabadiliko ya Tabia Nchi (UNFCCC) wanautumia kwa ajili ya ku-fund projects za masuala ya climate. Lakini sisi nchi yetu, taasisi za Serikali hakuna hata taasisi moja ambayo iko accredited, haipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi katika Jumuiya ya Afrika Mashariki ndiyo nchi ambayo ina miradi mitano tu kupitia Green Climate Fund, lakini Kenya wana miradi 16, Uganda wana miradi 10, Rwanda wana miradi tisa. Sisi tumeshindwa kuzisaidia taasisi zetu ambazo ziko chini ya Serikali kupata accreditation ili tupate hizi fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, CRDB peke yake ndiyo imepata accreditation lakini mnakumbuka CRDB wanafanya kwa njia ya mikopo, siyo grants. Sisi taasisi zetu zinatakiwa zipate fedha…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mimi kama Mwenyekiti wangu wa Kamati na Wajumbe wenzangu wa Kamati na watu wote ambao wamepongeza jitihada ambazo zimefanywa na Kamati ya Mapitio ya Sera na Mitaala. Pia nimpongeze sana Mheshimiwa Profesa Joyce Ndalichako ambaye alianza mchakato, lakini pia Mheshimiwa Profesa Adolf Mkenda, ambaye na yeye alipokea mchakato wa mapitio ya sera na mtaala, lakini kwa upekee sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa sababu, yeye alionesha political will kama kiongozi wa nchi kwamba, kuna umuhimu mkubwa wa kufanya mapitio ya mfumo wetu wa elimu kwa ajili ya kuendana na mazingira ya sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee sana nimpongeze Profesa Makenya Maboko kwa sababu, amefanya kazi iliyotukuka na viongozi wote, Mheshimiwa Katibu Mkuu wa Wizara, mama yangu Profesa Carolyne Nombo, anatuheshimisha sana kama wanawake na tunaona kwamba, tukipewa nafasi tunaweza kufanya makubwa zaidi. Kwa hiyo, majina yao yataandikwa kwa wino wa dhahabu kwa sababu, hii document ambayo wameitengeneza ukweli ni kwamba, ni one of the outstanding documents kwenye East Africa, inawezekana hata Nchi za Kusini mwa Afrika na inawezekana Afrika kwa hii document iliyotengenezwa, ni one of the best, kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wamepitia na wataalam wamepitia. Nipongeze kwa sababu walijipa muda wa kukusanya maoni na hawakuchukua speed kubwa sana, kwenda harakaharaka, wali-take time waka-exhaust na wamefanya kazi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda kabla sijaanza kuchangia nizungumze jambo moja kwa sababu, mapitio ya mtaala ya sasa hivi na sera tunasema falsafa ya sasa hivi ni self-reliance, elimu ya kujitegemea. Sasa labda kwa sababu Mheshimiwa Dkt. Chaya ni Mwalimu wangu chuo kikuu niseme tu kidogo kwamba, alichokizungumza kwamba, tuache VETA tusubiri walio-drop wameshindwa waende VETA, maana yake tunakuwa hatutekelezi lile lengo la kusema kwamba, tunatengeneza mfumo wa elimu ya kujitegemea. Tunataka wazazi na Watanzania wote waone kwamba, aliyepo VETA ni ameamua tu alternative pathway, amechagua kwenda huko, sio kwamba, hana uwezo na ninajua ndio dhamira ya kufanya marekebisho na mapitio kwa sababu, tunajenga ujuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee sana nipongeze mchakato uliofanyika kwa ku-integrate skills za karne ya 21. Study za karne ya 21 ambazo wamezi-integrate, japo nina mambo kadhaa ya kuzungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nipongeze kwa sababu, wame-integrate communication, tulikuwa tuna tatizo hilo, lakini pia wame-integrate collaboration, wame- integrate creativity na innovation, lakini critical thinking, tafakuri tunduizi na nimekuwa nikizungumza, lakini problem solving, utatuzi wa matatizo, digital literacy, ethics and patriotism. Wameamua kuzichukua kwa sababu ndio karne ya 21, labda niwaambie Waheshimiwa Wabunge dunia tunayoishi sasa hivi ni dunia soft, inahitaji watu ambao wanafikiri sana na wanatatua matatizo yanayowazunguka kwa sababu, matatizo yanakuja kila siku na yanahitaji akili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kweli kuna maendeleo makubwa ya sayansi na teknolojia, lakini the only thing ambayo haiwezi kuwa replaced na mabadiliko ya sayansi na teknolojia ni kufikiri. Kwa hiyo, ni lazima mfumo wetu wa elimu uendane na namna gani ambavyo tuna-feed hilo gap la fikira kwa sababu, mwanadamu pekee ndio Mungu amempa uwezo wa kufikiri. Sasa kama una mfumo wa elimu ambao mtoto anatumia muda mwingi darasani na mfumo huo haumwelekezi huyu mtoto kufikiri, kuanza kung’amua matatizo yanayoweza kujitokeza baadaye, maana yake mfumo wako wa elimu unakuwa redundant. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nipongeze kwa hilo, ila nina changamoto moja; wameeleza, ukiangalia kwenye tamko la sera ambalo linaenda kusababisha mitaala kutengenezwa, tamko 3.3.6. Wanasema kuwa Serikali kwa kushirikiana na wadau itahakikisha mtaala unalenga kukuza stadi za karne ya 21 ambazo amezitaja hapo kwa mfumo wa kuchopeka, ku-integrate. Wasiwasi wangu ni hapo kwenye ku-integrate kwa sababu, unawezaje kupima kitu ambacho Umeki-integrate kwenye process? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu, hakuna utaratibu waliouweka kwenye kupima. Labda niseme hivi, wameeleza kwamba, anayeenda kutekeleza mtaala, tunajua anayeenda kutekeleza mtaala ni Mwalimu na anaenda kujenga umahiri kwa wanafunzi na anaenda kujenga hizi stadi za karne ya 21, lakini hata kwenye marekebisho ya elimu ya ualimu, Mwalimu hajawekewa somo la kujenga umahiri wa hizi stadi. Mtu ambaye unamtegemea akazijenge stadi hujamwekea somo la kuzijua na nina mashaka sana kwa sababu tunawajua Walimu wetu ambao tunao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hizi stadi, kwani leo tunakosa nini? Kwa sababu, hizi stadi tukienda, tukirudi kwenye Sera ya mwaka 2014, tukirudi kwenye competence based hiki ambacho tunakirekebisha leo, hizi zilikuwepo na zilikuwa kwenye mfumo huu huu. Hazikuwa zimeandikwa kama hivi, lakini zilikuwa kwenye mfumo huu wa kuchopeka, sasa badala ya kuchopeka kwa sababu, tukichopeka tutakuwa hatuna namna ya kuzipima. Kwanza anayeenda kutekeleza hajajengewa umahiri wa hicho kitu, lakini kuzipima hatutaweza kuzipima kwa watoto wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini sasa tusitafute namna ya kuzifanya ziwe kwenye namna kama mada au somo kwa sababu, tumeweka ile elimu ya historia ya Tanzania na maadili? Kwa nini isiwe huko ili sasa tufuatilie hatua kwa hatua ili tuweze kujua ni namna gani ambavyo tunaweza tukampima mtoto mwisho wa siku kwamba, tumefanikiwa kumfanya awe ni mtatuzi wa matatizo kwenye jamii kwa kiasi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika pia kwamba, kwenye hizi skills, skill ambayo ni muhimu sana ya self- awareness, kujitambua, haipo katika hizi skills, haijawekwa. Niwaambie tu Waheshimiwa Wabunge kujitambua ni pamoja na wewe binafsi, intra personal na inter personal skills ambazo zinamfanya mtu ajitambue kihisia yeye ni mtu gani na zitatusaidia pia ku-solve matatizo ya kimaadili kwenye jamii kwa sababu, inawezekana watoto wanaangalia vitu vingine ambavyo vinawafanya wasijitambue wao ni akina nani na ndio wanakua katika utaratibu huo. Kwa hiyo, skills kama self- awareness ni muhimu mno iwepo katika mfumo wetu wa hizi skills za karne ya 21.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, upimaji na tathmini. Niseme tu katika Rasimu ya Mtaala, Sura ya Nane, Kipengele cha 10, Wizara imezungumza na wameeleza gaps zilizokuwepo kwenye upimaji. Naunganisha na masuala ya hizi stadi za karne ya 21 kwa sababu hata upimaji wake haueleweki. Kwenye mfumo wa kawaida wa shule continuous assessment, upimaji endelevu, umepewa asilimia 30, halafu upimaji wa mwisho umepewa asilimia 70 kwenye mfumo wa kishule, lakini kwenye mfumo wa elimu ya ualimu ni fifty-fifty angalau, hamsini-hamsini, lakini kwenye inactivate, amali, wao wameenda mbali zaidi wana zaidi ya asilimia 70 na kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ni kweli kabisa mtihani wa mwisho unaweza kumtambua mtoto kwamba ana akili au hana? Kwa sababu, hiki kilichoandikwa sasa hivi sio kwamba, hakikuwepo. Tumefanya review sasa hivi tume-highlight na vizuri kabisa Serikali imeonesha kuna gaps, lakini ni kwamba tume-highlight tu. Ukweli ni kwamba, continuous assessment, upimaji endelevu wa ndani ya shule, Mwalimu na mwanafunzi ulikuwa haufanyiki. Yale matokeo mnaona tunafanya ranking leo tunalalamika tumeondoa ranking, lakini yale ni matokeo ya mwisho. Kuna factors nyingi zinaweza kusababisha mtoto afeli mtihani wa mwisho, lakini sio kwamba, hana uwezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kuniambia kwamba, mtoto aliyefaulu standard seven, akafaulu kidato cha pili anakuja kufeli form four tena kwa zero, haiwezekani, kuna namna ambavyo huyu mtoto katika kujifunza kwake kuna vitu anajua. Kama lengo letu la elimu kama ninavyolielewa mimi ni kumjenga Mtanzania mwenye umahiri, anayeelewa, ambaye anaweza kuwa mwananchi ambaye atakuwa na mchango kwenye nchi, tunahitaji kuongeza asilimia za continuous assessment. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sio tu kuziongeza, tuzipime kiuhalisia kwa sababu, Mheshimiwa Waziri anajua kwa sababu yeye pia ni Mwalimu na wapo Walimu wanafahamu. Ukweli ni kwamba, hakuna namna ambavyo wanafuatilia, tunaambiwa tu huu ni mkusanyiko wa mitihani yako ambayo umefanya. Lengo la continuous assessment ninayozungumza mimi sio majaribio na mitihani, kama tunapima problem solving ni lazima tuwe tuna utaratibu wa kuwapima watoto kwenye matatizo yanayowazunguka katika mazingira yao pale pale shule. Kwa hiyo, ni ushirikiano wa Mwalimu na mwanafunzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama NECTA ni machinery ambayo ina full autonomy ya kwake, utaratibu wake wa jinsi ya ku-operate, itafutwe namna tunaweza tukai-integrate. Kwanza tuongeze asilimia ili tufike angalau 50 mpaka 60 au angalao fifty-fifty, lakini nzuri ikiwa 60 kwa sababu ya kitu ambacho tunategemea tukipate hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu muda umebaki kidogo nimalizie kuhusiana na lugha ya kufundishia. Kwanza niwapongeze Serikali wame-play neutral role, wame-play neutral ground kwa sababu wamesema kwamba, anayetaka kufundisha Kiswahili ataomba kibali na anayetaka kufundisha Kiingereza ataomba kibali, kwa hiyo, wamejaribu ku-play politics hapo, lakini tunajua, sitazungumza kwenye lugha ya Kiswahili sana, najua siku zote huwa nazungumza kwamba, ni muhimu sana tujifunze kwa lugha tunayoielewa, lakini hata hicho Kiingereza, mimi nimesoma HKL Form Six, tumesoma syntax, phonology, semantics, vitu ambavyo tunajua leo hapa hatuzungumzi syntax, hatuzungumzi phonology.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunafundishwa Kiingereza tufundishwe kama communication language, lugha ya kuwasiliana, kwa sababu, tunataka hawa watoto wakitoka wamejua wamegundua vitu vyao, wawe wana uvumbuzi, waweze ku-communicate, waende wafanye biashara bila kutafuta mkalimani, aendee nchi yoyote duniani. Kwa hiyo, kama tunakubaliana ni Kiswahili basi kiwe Kiswahili na kama tunakubaliana ni Kiingereza basi kiwe Kiingereza, watoto wasikutane na Kiingereza barabarani. Nazungumzia watoto wa Kantalamba huko, wasikutane na Kiingereza barabarani, waanze kutoka darasa la kwanza, kutoka awali, la kwanza, waende na Kiingereza. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ni jukumu lake kujenga umahiri kwa Walimu ili wawe the best. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vitu vingi hapa tunaweza tukavizungumza, vingine najua tutaviandika huko, lakini cha mwisho kabisa, bajeti ya Wizara ya Elimu. Asilimia zaidi ya 64 ya bajeti ya Wizara ya Elimu yote inaenda kwenye mikopo. Tutafute solution ya kudumu ya ku-fund mikopo ya elimu ya juu kwa sababu, tunakosa pesa za kufanya vitu vingine kwenye Wizara, kwa mfano, kitu muhimu kama utafiti hatuna pesa za utafiti. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
The Written Laws (Miscellaneous Amendments) Act, 2023
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye marekebisho ya Sheria mbalimbali. Nitajikita kwenye Sheria ya Huduma za Habari ya mwaka 2016 Sura ya 229 ambayo ndio Serikali inafanyia marekebisho. Kwanza niipongeze sana Serikali kwa kuona umuhimu wa kusikiliza maoni ya wanahabari na wadau wa tasnia ya habari lakini pia na watanzania wote ambao walipiga kelele baadhi ya vifungu kwenye Sheria ya Huduma za Habari ya mwaka 2016.

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi nakubaliana na maoni ya kamati kuhusiana na marekebisho yaliyofanywa lakini pia naunga mkono taarifa ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuhusiana na sehemu ambazo wamesema wamezifanyia marekebisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda tu kwa kukazia, Serikali kwa kuona umuhimu wa maoni ya watu wamefanya marekebisho kwenye vifungu tisa ambavyo vilikuwa na utata lakini kwenye vifungu hivi tisa vifungu vitatu ndio vifungu ambavyo tumeviona kwamba ni tangible na nitavielezea baadae lakini vifungu sita vilivyobakia ni vifungu ambavyo vimezungumzia adhabu. Ni jambo zuri kwa Serikali kuona kwamba kulikuwa kuna nia ya kupunguza adhabu ya makosa kwenye masuala ya tasnia ya habari kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, vifungu sita vyote vinahusiana na masuala ya kupunguza adhabu ni jambo zuri na tunawapongeza. Lakini vifungu vitatu pia na vyenyewe ni tangible na nitavielezea kwa sababu ya umuhimu wake kwa sababu vilipigiwa makelele na Serikali imesikia. Kuna kifungu cha tano ambacho kimemwondolea mamlaka Mkurugenzi wa Idara ya Huduma za Habari ambaye kimsingi alikuwa anapewa mamlaka makubwa sana. Kumwondolea Mkurugenzi wa Idara ya Huduma za Habari jukumu la kuratibu matangazo yote ya Serikali, kuiwezesha Serikali kuwa na uhuru wa kuchagua chombo cha Habari ambacho kitashirikiana nacho kuzingatia na ushindani wa vyombo vya habari. Kwa hiyo, hili ni jambo ambalo tulilipigia kelele kwa sababu lilikuwa linampa mamlaka makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kifungu cha 64 pia kimefanyiwa marekebisho ambacho kimeondoa adhabu kwa wamiliki wa mitambo ya kuchapisha kwa sababu kwa kweli hawana mamlaka, uwezo wa moja kwa moja kuchagua nini kinachapishwa kwenye mitambo yao, kwa hiyo, ni jambo zuri na nifikiri hata watu ambao wanamiliki mitambo ya kuchapisha wamefurahi kwa hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kifungu kingine ambacho kimefanyiwa marekebisho na Serikali ni kifungu cha 38(3) ambacho kinalenga kuongeza wigo wa watanzania wote wakiwemo wanahabari kutoa maoni. Kwa sababu kuna makosa ambayo yalikuwa yanaonekana kama ni makosa, kwa hiyo, imefuta adhabu kwa mtu ambaye atachapisha taarifa ambayo ilikuwa inaonekana kwamba inaingilia uhuru usiozuilika wa watu, kwa hiyo, ni kitu kizuri tunapongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nielezee mambo ambayo naona yameachwa ambayo pengine yalitakiwa yawepo katika marekebisho haya. Jambo la kwanza ambalo limeachwa kwa kweli ambalo ni la msingi kwa ajili ya kurekebisha na kuweka mazingira mazuri kwa watu wetu wa tasnia ya habari kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo moja ambalo halijaguswa kabisa ni kuhusiana na leseni. Sheria mpaka sasa hivi ambavyo ilivyo inataka kila mwaka wamiliki wa magazeti wasajili leseni kila mwaka, annually licensing ya magazeti, kitu ambacho kinazuia hawa ambao ni waandishi wa habari kufanya kazi zao wakiwa wana-confidence ni kama kinawondolea confidence. Kwa hiyo kifungu cha 5(e), 8 na 9 vyote vinalazimisha wamiliki wa magazeti kusajili kila mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa maoni yangu, kwanza tuondoe neno license badala yake tulibadilishe na registration. Kwa hiyo, tuwe na usajili ambao tunaweza tukakubaliana hata kama ni five years, au hata kama ni ten years lakini watu watajiwe gharama ya kusajili magazeti ili wapate uhuru wa kufanya kazi zao za uhandishi kwenye magazeti kwa muda ambao wanajua wameshafanya usajili na Serikali inajua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kila mwaka mmiliki wa magazeti anatakiwa akasajili. Kwanza hapo kuna gharama, kuna implication ya cost ambapo kila mwaka anavyosajili analipa lakini pia hii ni sehemu moja wapo ambayo sisi tunaamini kwamba inaweza ikasababisha watu wengine ambao kwa namna moja au nyingine wataonekana wana ukali fulani wakaondolewa wakawa fenced out. Kwa hiyo ni kama technique fulani ambayo kiukweli tunashauri muone namna gani, kwa sababu kwa kweli magazeti yatapungua. Kwa sababu wangapi wata-comply nayo na mnajua kwamba ni vijana wengi sana wamejiajiri kwenye vyombo hivi ikiwemo magazeti. Watu wana kalamu zao wanaandika watu wanamiliki ni biashara na kimsingi tunahitaji watanzania waweze kumiliki uchumi, hii ni sehemu moja wapo ya income za watu na nafikiri kuna haja ya kuangalia kwa sababu hatuviziani.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo limeachwa ni mamlaka ya Waziri kuzuia machapisho kutoka nje. Nchi yetu ni nchi huru kama tulivyokubaliana kwa hiyo, sioni kama ni busara kuzuia machapisho mengine yenye lengo la kujifunza kwa sababu ya ministerial capacity ambayo Waziri amepewa kuzuia machapisho kutoka nje. Kwa hiyo, sioni kama ni busara sana, lakini pia kitu kingine ambacho nishauri sana wakiangalie ni pamoja na hiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumesema waondoe ukomo wa adhabu kwa sababu, sasa hivi ilivyo ni kwamba vile vipengele sita vilivyofanyiwa marekebisho, vyote vimetaja adhabu juu na chini lakini ni bora sana. Kuna kifungu kimoja kimeandikwa vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri kwa sababu mwenendo wa kesi ni tofauti na sisi tunavyozungumza, ukimwekea mtoa hukumu kwenye Sheria kwamba anatakiwa atoe hukumu kwa kosa hilo kwa kutaja faini lakini pia ukamwekea kifungo kisichopungua miaka mitatu na kisichozidi miaka mitano, wakati mwingine mwenendo wa kesi unaweza kufanya ukaona kwamba hili kosa sio la miaka mitatu lakini Sheria inamlazimisha mtoa hukumu ahukumu minimum three years. Kwa hiyo. nashauri baada ya kusema minimum three years na maximum ni bora ikatajwa maximum au ikatajwa kama ilivyotajwa kwenye kifungu hiki hapa nakisoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kifungu cha 63(1) nina kinukuu kwa kingereza kama kilivyoandikwa na ninashauri kwa sababu kipo kwenye Sheria hii hii na Serikali ndio imekiandika, nashauri vifungu vyote vinavyohusu adhabu viandikwe hivi, “commits an offence and upon conviction shall be liable to fine of three million shillings or five million shillings and imprisonment of five years or two years or both” hakuna minimum hakuna maximum. Nashauri vifungu vingine vyote vinavyofanana na hivi kwenye adhabu viandikwe hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii inatoa uhuru kwa anayetoa hukumu kwa sababu sio lazima kwa kuwa Sheria nyingine zimeandikwa hivi na hii iandikwe hivi, kwa sababu tunaweza kuchagua namna bora ya kuandika Sheria nyingine ambazo zikawa nzuri, sio lazima tufate vya zamani na kwa sababu hiki kifungu ni cha kwenye Sheria hii. Sasa kwanini vifungu vingine vyote vilivyotaja adhabu ambavyo niliviorodhesha hapa vingeandikwa hivi ingekuwa na picha nzuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kitu kingine ambacho kimeandikwa bado kipo humu na hakijajadiliwa sio katika amendment ni defamation kwenye Sheria hii, kashfa bado ni kosa la jinai. Kitu ambacho ni kinyume kabisa na viwango vya kimataifa vya Sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, kifungu cha 35 na 36 kwenye Sheria hii ya Huduma za Habari inaeleza kashfa kama kosa la jinai na ninashauri kiangaliwe upya. Kipitiwe kwa sababu kwanza au kiondolewe kwa sababu internationally kashfa ama defamation sio kosa la jinai ni madai kama madai mengine ambayo tutaenda tu-battle mahakamani huko lakini sio kosa la jinai na kwa sababu ya tasnia hii ya habari hili jambo ni pana sana kwa upana wake tunaweza tusilizungumze hapa kwa sababu wakati mwingine kitu ambacho ni ukweli kinaweza kuchukuliwa kama ni kashfa kwa sababu mwandishi wa habari ameandika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo vingine tutaendelea kushauri…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. NUSRAT S. HANJE: …lakini kimsingi niwapongeze sana Serikali kwa kuona umuhimu wa kufanya amendment japo kuna vitu wameviacha. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia bajeti ya Wizara ya Madini kwa mwaka wa fedha 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2017 Bunge hili lilitunga Sheria inayoitwa Natural Wealth and Resources Permanent Sovereignty Act, 2017, ambayo ni Sheria inayoeleza umiliki wa milele wa rasilimali na maliasili za nchi yetu. Na lengo la Sheria hii ilikuwa ni kuhakikisha kwamba Watanzania wote wanatamkwa kwenye Sheria kwamba ndio wamiliki wa rasilimali za Taifa hili na maliasili zote. Niwapongeze sana Wabunge waliokuwepo wakati huo kwa wakishiriki kutunga Sheria hii. Kwa sababu ukweli ni kwamba Watanzania na wanachi wote, sisi ni miongoni mwao ndio, wamiliki wa milele wa rasilimali zetu. Lakini haitoshi kusema kwenye Sheria kwamba Watanzania ndio wamiliki wa milele wa rasilimali na maliasili ya nchi yetu tukaishia hapo bila kuonesha kwa vitendo athari ya kimaendeleo inayotokana na umiliki wao wa milele wa rasilimali za nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeanza na utangulizi wa Sheria hiyo ambayo imetungwa na chombo hiki kitukufu ambacho hata leo hii mimi nimesimama hapa naongea kwacho kwa sababu tukumbuke na tuone umuhimu wa chombo hiki kwenye Taifa hili. Kwa sababu kwenye chombo hiki kuna wawakilishi wa nchi nzima, Wabunge, Wawakilishi wa Majimbo yote Tanzania nzima wako kwenye chombo hiki. Maana yake uwakilishi wa Tanzania nzima wa hao wamiliki wa rasilimali za nchi yetu upo katika chombo hiki. Kwa hiyo, tunategemea pia kuona kwa namna kubwa wanaotajwa kama wamiliki wa milele wananufaika pia na rasilimali zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kuzungumza kuhusiana na Sekta ya Uziduaji (Extractive Industry) na namna ambavyo sisi wa kizazi cha leo tunatamani wasifanye makosa waliyofanya watangulizi wetu kwa kuacha mashimo ya dhahabu na almasi, wakati ukitoka tu kwenye mgodi nje kuna watoto wana shule wanakaa chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa natambua jitihada ambazo zimefanyika mpaka leo kuna CSR, kuna miradi ambayo imetokana na uwekezaji ambao umefanywa kwenye Sekta ya Uziduaji. Hata hivyo bado, kama vijana na Watanzania ambao tunasema ndio wamiliki wa milele wa rasilimali zetu, tunatamani tushiriki katika value chain ya migodi, value chain ya madini yetu ambayo tunayo kwa sababu haitoshi kuitwa wamiliki wa milele, ni lazima tuoneshe na tuonekane kwa vitendo tumetajirika sisi binafsi kutokana na rasilimali tulizonazo kwenye ardhi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2015, Bunge hili lilitunga Sheria ya Uziduaji ambayo iliitwa Extractive Industry Transparent and Accountability na leo nitajikita hapo tu, uwazi na uwajibikaji kwenye mikataba ya Sekta ya Madini. Kwa wivu mkubwa sana, mimi kama mwakilishi wa chombo hiki kitukufu, nasikia wivu sana kama nitakuwa sijui nini kinaendelea katika makubaliano kati ya nchi yetu na mataifa mengine na kampuni nyingine za uziduaji kama haitajadiliwa kwenye Bunge hili kwa sababu tutajua vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua wanaoshiriki kuingia mikataba hii ni binadamu, ndio maana tunahitaji vichwa hivi kutoka Tanzania nzima vishiriki katika kujua mikataba hii line to line ili tushauri kwa sababu hakuna mtu ana bifu na hii nchi, tunaipenda na tunataka rasilimali zetu ziwanufaishe Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi Aprili nchi yetu imeingia makubaliano, wasiwasi wangu mkubwa sana athari ya Mikataba ya kutoletwa Bungeni imeanza kuonekana juzi. Waheshimiwa Wabunge wakiingia kwenye tablet zao website ya Kampuni inayoitwa peak layer earth limited utaona mkataba wa Nguala - Songwe umesainiwa juzi hata mwezi haujapita. Kwenye Mkataba wale wa kampuni wanasema project ina-expect kutumia Shilingi Dola Milioni 320, lakini kwenye website ya Wizara inasema project inategemea kutumia shilingi Dola Milioni 439 difference ni Dola Milioni 119.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niamini ni errors, ni kukosea kwenye kuandika, lakini siamini kama nikukosea kwenye kuandika kwa tofauti kubwa kabisa ya fedha hizi ambazo ni sawa na zaidi Shilingi za Kitanzania Bilioni 276.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nisingezungumza hapa kama mkataba na mikataba ya design hii ikaletwa Bungeni tukajadili. Hakuna mtu ana bifu na mtu yeyote, hakuna mtu ana wasiwasi na chochote katika nchi hii, bali tunataka tujue kwa sababu ya sheria ambazo zimetungwa na Bunge hili kwamba kila Mtanzania ni mmiliki wa milele wa rasilimali za nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumza haya kwa sababu tuna mashimo ya gold, tanzanite na madini mengine tumeyaacha kule. Sasa hivi tunazungumza critical Minerals, layer earth element ni miongoni mwa critical minerals, ni kitu ambacho ni kipya na na tunakichukulia kama kipya, tunafikiri tunaweza kufanya kama tulivyofanya zamani. Sioni kama ni busara, kama ni sahihi kufanya kama tulivyofanya zamani. Natamani tuwe na jicho jipya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi hata Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabau za Serikali hana mikono kwenye kukagua mikataba ya madini inayoingiwa katika nchi yetu. CAG aliondolewa mamlaka kisheria ya kupitia hii mikataba na kuikagua. The only provision ambayo CAG anapewa ni ambayo ataombwa na TEITI kwenda kukagua mikataba hii tena ikitokea kuna hitilafu kwenye hesabu, si chini ya one percent kwenye hesabu ndogo ndogo ambayo ataomba na TEITI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe, kwanza, Ripoti za TEITI zote, kwa sababu CAG hana mamlaka kwenye ukaguzi wa mikataba, basi kwa sababu tumempa TEITI, basi wakati tunajadili ripoti za CAG, tujadili na ripoti za TEITI kwenye Bunge hili, ili sasa tupitie huko kwenda kuuliza nini kinaendelea kwenye mikataba yetu, kujua in details what is going on kwenye Sekta ya Uziduaji kwenye Taifa letu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia sheria ilitungwa na Bunge hili na sisi ni wajibu wetu kuitekeleza sheria. kwa hiyo, naomba sasa Sheria ya Extractive Industry Transparent and Accountability itekelezwe. Tuletewe mikataba iliyoingiwa na Serikali ili Bunge hili kwa heshima yake lijadili kinaga ubaga na lijue mikataba ambayo Serikali yetu imeingia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nne, CAG aruhusiwe kwenda kukagua mikataba kwa sababu sisi kama Bunge, CAG ndiyo jicho letu na ndiye tunamtegemea .

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, kwa sababu sisi tumesema tunataka tutekeleze Sheria ya Watanzania ku-enjoy rasilimali zao, basi waziduaji na wachimbaji wadogo wa madini ni sehemu ya Watanzania ambao tunatamani washiriki na wao kiasi kusherehekea rasilimali ambazo tunazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka hivi sasa ninavyozungumza kuna mambo mawili. Kwanza, Serikali ilionesha nia ya kutaka kuwasaidia wachimbaji wadogo na kuna vitu wamewafanyia, lakini kuna VAT kubwa sana katika suala la umeme. Hii ni kwa sababu Mheshimiwa Waziri wa Madini watu wake wa migodi uunganishaji wao utasababisha watu wa madini waongeze kuchangia pato la Taifa, kwa sababu wanalipa kodi. Hata hivyo, kwa sababu wanarundikiwa madeni makubwa, wameunganishwa na umeme lakini wanatozwa VAT kiasi kubwa, kuna malimbikizo makubwa, wanashindwa kuendesha migodi, matokeo yake Serikali haipati pato na wachimbaji wadogo wanashindwa kupata pato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe sasa Mheshimiwa Waziri atafute namna bora ya kuona namna gani anaweza kuwasaidia wachimbaji wadogo. Vile vile, hao hao wachimbaji wadogo kwenye upande mwingine kuna tax exemption walipewa kwenye vifaa vya kuwasaidia kuchimba madini, lakini wanaopewa tax exemption wanarudi wanakatwa tena na Serikali wakati wa kutoa vile vifaa bandarini. Kwa hiyo, sidhani ile nia bora ya kuwasaidia wachimbaji wadogo, kama tutakuwa tunaitekeleza kwa vitendo kama tunawapa kwa mkono huu na tunachukua na mkono huu. Nchi hii ni ya kwetu wote na lengo letu wote tu-enjoy rasilimali za Taifa kwa pamoja na tuweze kunufaisha nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia bajeti ya Wizara ya Fedha na Mipango.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma hotuba ya Mheshimiwa Waziri pia nimesoma maoni na mapendekezo ya Kamati, ninakubaliana na maoni na mapendekezo ya Kamati kwa vitu walivyoshauri namna bora ambavyo tunaweza tukaboresha mfumo wetu especially wa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitachangia eneo moja tu na ni kwa wema sana, kwa sababu mimi naamini namna bora ambazo tunaweza tukafanya kusaidia nchi yetu ni pamoja na kujengea uwezo Wizara hii, kwa sababu Wizara hii kila Wizara nyingine zote tukilia hakuna barabara, tukilia hakuna maji, tukilia kuna shida hatuna madawati, hatuna madarasa, bado tutanyooshea mikono, tutawanyooshea vidole Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami siamini kama kweli Serikali haina mapenzi na wananchi wake, siamini kabisa. Kwa hiyo, ninaamini sana Wizara hii pamoja na Serikali lengo lake ni kuhakikisha kwamba wanajenga uwezo wa Watanzania kukusanya kodi wenyewe, ili baadaye wakitaka kuzitumia wazitumie kwa kuona maendeleo ambayo walikusanya kodi leo barabara inapitika, mimi naamini hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na makandokando yote lakini kama Wizara ya Fedha kwenye kitengo cha kukusanya kodi, itakusanya kodi kama inavyostahili sidhani kama kaka yangu Mwigulu kama ambavyo muda wote amekuwa akisimama humu akiambiwa sasa peleka pesa, peleka pesa sidhani kama wanazo fedha halafu hawataki kupeleka, siamini kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nitazungumzia mwenendo wa ukusanyaji wa kodi na upotevu wa mapato kwenye Taifa letu. Kwanza hazijabadilika sana, takwimu hazijabadilika sana za wanaolipa kodi mpaka sasa hivi tunavyozungumza hazijabadilika sana, bado range haijafika milioni tano, yaani hapo haizidi hapo kama imezidi haizidi hapo. Kwa hiyo bado tuna tax base ndogo mno ambayo tunalazimika kuwaminya wachache ambao ndiyo tunaowahesabu kama ndiyo walipa kodi. Kwa hiyo, bado hoja yangu ya kuongeza tax payers, kuongeza tax base idadi ya walipa kodi kwenye nchini kwetu ni hoja ambayo nitaendelea kuizungumza, kwa sababu naamini tukilipa kodi wengi tutakuwa tunaminyana kidogo kwa sababu tuko wengi tunachangia, tofauti na mkiwa na walipakodi wachache. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kuna nchi nyingine jirani na tukisema tunataja majirani siyo kwa sababu kwetu hatuthamini, tunajaribu kwa sababu kama tuko kwenye uwanda mmoja, kama tuko African Community pamoja, ninaamini tunajifunza humu kwa sababu kuna agreements nyingi tunaingia vikao pamoja mpaka miaka ya fedha tumeirudisha nyuma, wote wameirudisha nyuma nchi zao, tumekuwa pamoja tunamaliza Juni 30, Mwaka wa Fedha unaanza tarehe 01 Julai, East Africa yote, ndiyo maana tunasema kama ni mifano ambayo haihusiani na Malaysia huko na wapi, basi ya humu pia tuisikie kwa sababu ni East African community.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nchi kama Kenya ambayo tax base yao ni angalau ni watu milioni saba wanalipa kodi plus, Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti, amezungumza pia hata namna ambavyo GDP Kenya, Rwanda mchango wa mapato ya kodi kwenye GDP sisi ni asilimia 11, natamani sasa tuone namna gani tunaweza tukaboresha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma taarifa ya Wizara ukurasa wa tano ambayo ameeleza mwenyewe Mheshimiwa Waziri, miongoni mwa vipaumbele vyake, Mwaka wa Fedha uliopita na Mwaka wa Fedha huu ni kukusanya, kudhibiti upotevu wa kodi na kuhakikisha kwamba wanadhibiti matumizi bora ya fedha za umma, which is nzuri sana, lakini ukienda kwenye mikakati yake kwenye kudhibiti upotevu wa mapato ya Serikali anasema kufanya doria kwenye mipaka, lakini pia kidhibiti mifumo ya TEHAMA.

Mheshimiwa Naibu Spika, Shida yangu iko hapo kwenye Mifumo ya Tehama, kwa sababu kama tunazungumza digital economy na hatuzungumzi namna bora ya kudhibiti upotevu wa fedha; kwa sababu takwimu zilizotajwa na Viongozi wa Serikali ni kwamba tunapoteza shilingi milioni 500 mpaka shilingi bilioni moja kwa siku kwenye mifumo ya Tehama. Nataka niwaambie hizo ni takwimu zilizotajwa na Serikali. Nawapa benefit of doubt, lakini tukienda into details, ni zaidi ya hizo fedha tunazopoteza kwenye mifumo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuko tayari kuwasaidia Serikali. Kama kweli hatuna resources, tuna vyuo, tume-train vijana wetu, wana uwezo, wana elimu kubwa ya cyber security, tumeshindwa kutumia investments zetu za shule, tumeshindwa kusomesha vijana kwenye vyuo ambavyo tunaweza kusema tunaviamini ili wazuie upotevu wa fedha, tuko tayari. Mimi nipo tayari kusaidiana na Waziri tukutafutie wataalam the best, na ni Watanzania. Wengine wamechukuliwa na nchi nyingine kwenda kusaidia kudhibiti upotevu wa fedha. Sisi tunao watu wetu ambao ukiongea nao wanakwambia wewe Mchaga gani hupendi hela? Watu wana mipango yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, inawezekana, probably kuna possibility kubwa sana ya kwamba wanaopiga hizo pesa ni watu wa kwenye mifumo huko huko. Ndiyo maana hawatafuti suluhisho la kudumu la kuzuia upotevu wa fedha. Watanzania sio wapuuzi kwenda kuweka fedha zao kwenye mifuko ya rambo nyumbani kwao. Siyo kwamba hawapendi nchi yao, hawataki kulipa kodi ndiyo maana wanapeleka huko, usalama wa fedha zao ni changamoto. Tunaweza tukatumia fedha ndogo sana kutengeneza mfumo ambao utatusaidia kuwa na strong cyber security ili kuwe na uhakika wa fedha za watu wetu, ziwe na usalama wa kueleweka.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri na Wizara nzima waangalie how best tunaweza tukatumia teknolojia, tukatumia investment zetu zote na resources zetu zote kuweka mfumo wa udhibiti wa upotevu wa mapato ya kidigitali. Sasa hivi dunia haizungumzi mapato, magendo eti mpakani yaani mpaka naona vibaya kwamba kwa nini nipo kwenye…, kwa sababu naona kama tunazungumza miaka ya 1980 huko. Kwa nini hivi vitu bado vipo? Siyo sawa. Naona kama tunafikiri kurudi nyuma, badala ya kufikiri kwenda mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine, tangu Bunge la Kumi, Bunge la Kumi na Moja, Bunge la Kumi na Mbili tunazungumza hivi hivi kwamba mifumo haioani, yaani mifumo haisomani, na tuna kitengo cha teknolojia. Eti hatuna kompyuta, hatuna laptop. Yaani bado tunazungumza hivi vitu hii nchi! Mimi nafikiri siyo sawa. Ifike hatua sasa habari ya mifumo haioani iishe. Kwa sababu mimi naamini kwamba hivi vitu ni vidogo vidogo ambavyo mnaweza mka-deal navyo kwenye Wizara huko huko. Kwa sababu kama una Wizara nzima ina-deal na masuala ya teknolojia, kwa nini bado unahangaika eti mifumo haioani? Sioni kama ni sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, migogoro mingine kama ya Kariakoo ambayo inajitokeza pale, ni vitu ambavyo mimi naamini, kaka yangu wewe Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, Waziri wa Fedha, hivi vitu unaweza kuvi-clear kabisa. Watu wataona hawaumii sana kama wanalipa kodi wengi. Ningekushauri, natamani kuiona Tanzania ambayo hatutumii fedha tena, yaani tumeenda cashless kabisa, kwa sababu ndiyo dunia inapoenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, naweza nikakushauri kwamba ukitangaza leo unabadilisha fedha, utaona fedha zitakakotoka kuja BOT. Kwa sababu unahitaji kuwekeza kwenye kuwapa watu elimu waone hawapigwi, yaani hawapigwi. Ndiyo dunia inavyotaka twende. Halafu jipe time, wekeza kwenye kuelimisha watu. Kwa sababu Watanzania wanatamani tuongee hivi taratibu, yaani kwa sauti ndogo tu kwamba ni wajibu wa kila Mtanzania kulipa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hawaelewi, tutumeni sisi wengine. Mimi nitajitolea hata kwenda kuwa Balozi. Jamani, usipolipa kodi barabara haipitiki, hatutapita. Tukisema hakuna madarasa, maana yake tunategemea tulipe kodi sisi. Bila hivyo, tutaendelea kwenda kuomba huko misaada huko nje na kila siku tunalalamika deni la Taifa linakua, lakini tukilipa kodi wenyewe, tunachagua wenyewe cha kufanya.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Nusrat.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye bajeti ya Wizara ya Kilimo. Kabla sijaanza, hii ni bajeti ya washikaji zangu, naomba niseme hivyo. Yaani hii Wizara ni ya wazazi, yaani kuna mzazi one, na mzazi two, wanajuana wenyewe Wizarani huko wanavyofanya. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi, kwa niaba ya vijana, kwa sababu ni miongoni mwa Mawaziri ambao sisi vijana tunajivunia, kwa hiyo, wanafanya vizuri, yaani mnafanya poa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, ni kwa nini nasema hivyo kwamba wanafanya poa? Ni kwa sababu mwaka 2021 mimi nilichangia wakati tunajadili hii bajeti ya Wizara ya Kilimo na kuna vitu ambavyo nilivishauri hapa na vimefanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yaani tunaposema wamefanya poa, ni kwa sababu wako hatua moja mbele, wanafikiri tunavyofikiri. Yaani wanafikiri namna ambavyo Watanzania wanaamini kwamba sekta ya kilimo inastahili kupewa heshima inayopewa. Wanafanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nawapongeza kwa sababu kuna mambo wameyafanyia kazi. Jambo la kwanza, nilizungumza mwaka 2021 kwamba muda ambao vijana wetu wanakaa field ni mfupi sana, yaani kijana ili awe ame-master vizuri kabisa sekta ya kilimo akitoka Chuo, Waziri amezungumza kwamba wanafanya mikakati. Tunaamini, kwa sababu tutawauliza tena; wameongeza muda wa vijana kukaa field mpaka mwaka mmoja. Ni kitu kizuri, kwa sababu ninaamini wanajifunza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine tulizungumza kuhusu ku-miliaturize sekta ya kilimo. Nilisema kwamba tunatamani, yaani kipenga kikipigwa Wizarani, Maafisa Ugani (extension officers) wanaitikia, mambo yanaenda. Wamefanya vizuri. Wasiwasi wangu, hawa Maafisa Ugani (extension officers) wako chini ya TAMISEMI. Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI sekta zao ni tofauti, lakini hawa ambao Wizara ya Kilimo inatenga fedha nyingi na kuwapa vitendea kazi; na tulishuhudia pale, wamepewa vifaa vya kupimia udongo, wamepewa usafiri, wamepewa vitu vingi na ni kitu kizuri, na walikuja tukawaona lakini wako sehemu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge, tumsaidie Mheshimiwa Waziri kuhamisha extension officers (Maafisa Ugani) warudi kwenye mikono ya Wizara ya Kilimo. Kwa sababu pale, mwenye uchungu na hizi fedha, kwa sababu tunasifia wote kwamba fedha ya kwenye Wizara ya Kilimo imeongezeka, lakini hatutaona tija, kama watu ambao tunaamini ndio askari wetu hatuna mandate nao, yaani Wizara ya Kilimo haina mandate na Afisa Ugani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge, niwakumbushe, pamoja na kwamba tunasema bajeti ya Wizara imeongezeka na tunajua imeenda kwenye umwagiliaji na sehemu nyingine, lakini ikumbukwe kwamba mpaka sasa hivi kwenye upande wa fedha za maendeleo, imetekelezwa kwa asilimia 35.86 tu upande wa miradi ya maendeleo. Kwa hiyo, bado tunasisitiza kupelekwa kwa fedha tunavyopitisha kwenye Bunge hili, kwa sababu mikakati iko vizuri, tunaongea hapa sana lakini fedha hazipelekwi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Nichangie upande wa pili ushiriki wa vijana wa Taifa hili kwenye kilimo. Bado vijana wanajitahidi kwa kiasi kikubwa sana kupambana na kushiriki katika mnyororo wa thamani kwenye sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wanalima, wanachakata, wanafanya kazi za consultation, wako vijana ambao wamejifunza masuala ya kilimo, wanashauri vijana wenzao. Kwa hiyo, tunashiriki kwa kiasi kikubwa, tunajitahidi kushiriki. Hata hivyo, bado tuna changamoto, kuna vijana wako field wana mashamba makubwa, wana greenhouse, wamejiandaa, wako tayari kushiriki kwenye mnyororo wa thamani katika sekta nzima ya kilimo lakini hawapati mikopo kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ameongea Mheshimiwa Mariam Ditopile hapa, kuna watu kabisa wana kitu, yaani siyo kama labda anachukua mkopo ili akaanzishe, kuna wengine tayari walishaanza, wanatakiwa kuwa boosted tu, lakini ni hizo bureaucracy (urasimu) kupewa mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ili vijana washiriki kwenye kilimo, tulisema tunataka tufanye kilimo kiwe romantic. Nafikiri tunaelewana. Tukifanye kilimo kiwe rafiki, kwa sababu najua vijana ndio hao wa millennials, hutegemei aende akashike jembe la mkono alime. Sasa huwezi kuzungumza ku-romanticize kilimo halafu usizungumze kuhusiana na teknolojia na ubunifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kwenye Taifa letu tuna kituo cha kukuza ubunifu na zana za kilimo cha Arusha CAMARTEC. Hiki Kituo wametengeneza matrekta, mashine za kulimia, mashine za kupanda, wanajitahidi wametengeneza ziko pale, lakini kile Kituo hakina fedha. Hakijapewa fedha kwa ajili ya kuhamisha maarifa yao kupeleka kwa wakulima. Kwa hiyo, wametengeneza vitu vikubwa wamebaki navyo pale kituoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri ahakikishe kwamba anatenga fedha kwa ajili ya kuwapelekea kituo hiki waweze kuhamisha ujuzi kutoka kituoni kupeleka kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa kumalizia… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Malizia sentensi ya mwisho kabisa hiyo.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna fedha za Benki ya Kilimo zimechukuliwa Shilingi bilioni saba. Mheshimiwa Waziri kuna watu walizungumza, nami naomba nisisitize; tunaomba majibu ya hizo Shilingi bilioni saba kwa sababu zilikuwa za mikopo, vijana wangepata mikopo. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia bajeti ya Wizara ya Nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitanukuu maneno ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere mwaka 1962 alipata kusema; “hatuwezi kutatua matatizo yetu kwa kujidanganya kwamba hayapo.” Wizara hii ni Wizara ambayo mimi naweza nikaichukulia kama Wizara ya mfukoni kwenye pochi la mama, kwa sababu mama ameweza kutoa shilingi bilioni 100 kwa ajili ya kusaidia kushusha bei ya mafuta ambayo imeonekana inaathiri wananchi wengi sana wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa masikitiko makubwa sana leo mpaka tunafunga Bunge saa 7.00 mchana bado Wabunge walikuwa hawajapata taarifa ya Kamati kuona mapendekezo ya Kamati kwa sababu ya unyeti wa information ambazo Wabunge wangeweza kusaidia/kumsaidia mama ili fedha aliyoitoa asione kama imepotea kupeleka kwenye sehemu ya mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo niwapongeze sana Wabunge wenzangu kwa sababu wamejitahidi kutafuta taarifa nyingine sehemu nyingine na wameendelea kusaidia kuchangia kwenye kuona namna gani tunaweza tukasaidia Taifa letu na isionekane kama Serikali imepoteza fedha, kwa sababu tunahitaji fedha mno kuna miradi ya barabara, kuna miradi ya hospitali, kuna miradi ya shule, lakini mama ameona apeleke upande wa mafuta kwa ajili ya kupunguzia Watanzania gharama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tarehe 25 Mei Mkoa wa Singida mzima ulikatika umeme na kwenye mitandao ukaonekana kibonzo kinasambaa kwamba mtu anasema Singida nzima umeme umezima halafu mwenzie anamjibu kwamba unaishi Singida kwani wewe ni alizeti? (Kicheko)

Mimi kama Mbunge wa kutoka Mkoa wa Singida kwa mpango huu ambao nimeona na namna ambavyo Mkoa wangu umetajwa kwenye bajeti ya Nishati, ninasikitika kwamba inawezekana Serikali inafikiri wanaoishi Singida wote ni alizeti. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka mingi tumekuwa tunajadili kuhusiana na umeme wa upepo Mkoa wa Singida na kila Mbunge wa Mkoa wa Singida anayesimama anaongea kwa sababu kuna uwezekano mkubwa sana wa umeme wa upepo Mkoa wa Singida ukasaidia wananchi wa Mkoa wa Singida, lakini pia ukasaidia watanzania wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka tunapozungumza Singida ni miongoni mwa Mikoa ya Tanzania ambayo miundombinu yake na upatikanaji wake wa umeme bado unasuasua. Ukisoma bajeti ya Wizara ya Nishati inaonesha kwamba wana-respond (wanaitikia) ile mipango ya maendeleo endelevu SDGs namba saba ambayo inalenga kutoa upatikanaji wa nishati safi ya uhakika na gharama nafuu. Lakini nasikitika sana mimi nimezaliwa kijijini kwenye giza, kwa taarifa za waliokuwepo wakati nazaliwa wanasema nilizaliwa kijijini kabisa kwenye giza, kwa hiyo, ninasikitika sana kwamba mimi nakaribia kuzeeka bado Watanzania wamama wa Singida wanajifungulia kwenye vibatari na giza kwa sababu bado Singida hospitali hazijaunganishwa kwenye umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha sana na jambo hili sio geni, Wabunge wengi sana wanaotoka vijijini wanajua kama Watanzania bado wanajifungua kwenye vibatari, bahati mbaya hata bei za mafuta zinazotegemewa kushuka bei ya mafuta ya taa bado haijaguswa kabisa. Mimi natoka mkoa ambao sehemu kubwa ni vijijini, kwa hiyo, watumiaji wa vibatari na taa za chemli bado wapo ni masikitiko yangu makubwa sana. Kwa sababu mimi ni mama wa Mkoa wa Singida, naomba nitaje katika Wilaya ya Ikungi zipo zahanati ambazo hazijaunganishwa na umeme. Bahati mbaya sana katika Wilaya ya Ikungi zahanati 33 hazijaunganishwa na umeme lakini pia bahati mbaya zaidi Jimbo la Singida Magharibi zahanati 20 hazijaunganishwa na umeme mpaka tunapozungumza na umeme umepita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo wananchi wanakwenda hospitali, wanatumia tochi, mama anajifungua kwa kutumia tochi anatoka nje anaangalia umeme umepita juu. Zahanati ya Kintandaa, zahanati ya Mtunduru, zahanati ya Ihombwe, zahanati ya Msosa, zahanati ya Mgungira, zahanati ya Yumbu, zahanati ya Mwaru, Ntuntu, Minyuhe, Iglansoni, Muhintiri, Nduru, Mpugizi, Mnang’ana, Kipunda, Songandogo and the list goes on. Inasikitisha mno Ubunge wangu mimi mwanamke kutoka Singida hautakuwa na maana kama tutaendelea kuacha akina mama wajifungue kwa kutumia tochi za simu, haiwezekani. Bajeti ya Wizara ya Nishati imeongezeka asilimia 13; kuongezeka kwa bajeti hii kukatoe tafsiri kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania hawajui miradi mikubwa na tunaipongeza, lakini niseme tu matumaini ambayo ninayo kama mimi kwa sababu mimi pia Mjumbe wa Kamati miongoni mwa miradi ambayo imepewa fedha kubwa sana katika ongezeko la bajeti ambayo imeongezeka ni pamoja na umeme wa REA Vijijini.

Kwa hiyo, Watanzania waelewe na tunategemea huwa nashangaa kwa nini Serikali wakati inaweka mikakati haiangalii maeneo muhimu? Hatuwezi kujadili kupeleka umeme shule, kupeleka umeme kwenye mahakama bila kujadili hospitali? Mimi naweza nikalala nyumbani kwangu na kibatari, lakini nakwenda kujifungua hospitali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma za afya zinategemea umeme, kuna vipimo vingine lazima utumie umeme. Kwa hiyo, wakati unapanga na tunategemea REA kwa ongezeko hili na wao ni sehemu ya kipaumbele watumie ubunifu wao wote kuhakikisha kwamba kipaumbele cha kwanza kinakuwa kuunganisha vituo vya afya na zahanati zetu ili akina mama ule mzigo ambao Mheshimiwa Rais alisema kwamba mzigo wa usawa wa kijinsia kwenye mabega yake ni mzito zaidi, kwa sababu ni aibu tuna Rais mwanamke, halafu kuna watu ambao wanatakiwa wamsaidie ili wanawake wenzake wasijifungulie kwenye giza, lakini wasaidizi wake inaonekana wanashindwa kumsaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana kwa niaba ya akina mama wa Tanzania tunaomba muwasaidie wanawake kuunganisha hospitali umeme ili waweze kupata huduma za afya kwa mazingira ambayo ni rafiki ili waweze kufanya kazi ambazo zitasaidia wao kuchangia Pato la Taifa, tumsaidie Mheshimiwa Rais kufanya kazi, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Na.3 wa Mwaka 2021 (Toleo la Kiingereza)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi na mimi nichangie katika Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 3) wa Mwaka 2021 [The Written Laws (Miscellaneous Amendments) (No. 3) Bill, 2021].

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, after 100 days tangu Mheshimiwa Rais aingie madarakani, these was one of the strategic projects (hizi zilikuwa miongoni mwa miradi ya kimkakati) ambayo ilikuwepo na ameonyesha nia ya kuendelea kwenye yale ambayo yana faida kwenye nchi. Kwa kweli kwenye hili nampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia katika ile hali ya kupenda nchi yetu kwenye jambo kama hili ambalo lina maslahi mapana ya Taifa kwa sababu, marekebisho ya sheria hizi yanatusaidia kwenda ku-facilitate (kuwezesha) uwepo wa mradi huu ambao ni mradi actually Wakenya wenzetu waliukosa kwa sababu kadhaa lakini sisi tumeupata. Kwa hiyo, ni kitu ambacho kwa kweli ni kikubwa kwa maana ya faida kwenye nchi kwa sababu tunaenda kuongeza pato la Taifa lakini pia, faida kwa vijana wa Tanzania ambapo kimsingi kuna ajira ambazo zinatarajiwa si chini ya 10,000 kwa Watanzania. Kwa kweli hili ni jambo kubwa sana. Pia, katika masuala ya diplomasia na ushirikiano wa Afrika Mashariki pamoja na wenzetu Waganda, hili ni suala ambalo linaendelea kuimarisha ushirikiano wetu na wenzetu Waganda na Afrika Mashariki kwa ujumla pamoja na kwamba tumewawahi Wakenya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu tunajua kuna faida kubwa kwenye mradi huu na tunaipenda nchi hii na tunatamani tufanikiwe, kuna mambo ambayo kimsingi ni lazima tuyashauri Serikalini. Marekebisho ya sheria 14 kwa ajili ya ku-accommodate Bomba la Mafuta, kuna tatizo moja ambalo naliona. Kwanza niseme kwamba mimi pia ni miongoni mwa walioteuliwa kwa ajili ya kuungana na timu ya Katiba na Sheria kwa ajili ya kushughulikia marekebisho haya na wenzangu wameshazungumza baadhi ya vitu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la uwajibikaji kisheria naliona linawekewa utaratibu kidogo ambao utatupa shida kwa sababu tunajua pia kuna masuala ya utawala bora lakini pia na uwajibikaji Kitaifa. Katika vifungu vilivyofanyiwa marekebisho kuna maneno yamerudiwa kutajwa mara kadhaa na ambayo yanalipa sifa Baraza la Mawaziri na kuondoa mandate ya Bunge hili kuwa kwenye utaratibu mzuri. Tunafanya marekebisho ya sheria lakini bado kuna kifungu ambacho Bunge hili leo tukipitisha kama kilivyo, kinaenda kutoa madaraka makubwa kwa Baraza la Mawaziri na nina wasiwasi nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kipengele ambacho kina-support kinasema: “Where there is an agreement that provides for special arrangement relating to implementation of this provision, and the said agreement has been approved by the Cabinet, the application of the provision of this section, shall not prejudice the implementation of such agreement”. Kwa maana kwamba kama kuna makubaliano yatahitaji utaratibu maalum kuhusiana na utekelezaji wa masharti ya sheria husika na kama utaratibu huo umepata kibali cha Baraza la Mawaziri basi masharti ya sheria husika hayatazuia au kuathiri utekelezaji wa makubaliano hayo. Kifungu hiki kinakwenda kutoa mwanya kwa Baraza la Mawaziri wakati mwingine kufanya vitu, kwa sababu hawa ni watu na tukitoa mandate kubwa kwenye jambo kama hili, inawezekana wakaingia makubaliano yasiyo na tija kwa wawekezaji ambao watakwenda kufanya uwekezaji kwenye ujenzi na ile restructuring ya Bomba zima la Mafuta. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Hicho ulichosoma ni kufungu namba ngapi?

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, katika kurekebisha zile sheria 14 wametumia mara kadhaa maneno hayo, nimeya-quote. Ukisoma kwenye marekebisho utaona wameyatumia mara kadhaa na Mheshimiwa Ramadhan ambaye tupo kwenye Kamati moja pia ameyazungumzia. Aim ni kujenga wala hatuna nia mbaya kwa sababu hili ni jambo jema kwa kweli na mimi niseme naliunga mkono na naamini Wabunge wengi wanaunga mkono kwa sababu tunajua faida yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema athari yake ni kwamba inawezekana Baraza la Mawaziri wakati wanatekeleza jambo hili wakaingia makubaliano na wawekezaji kwenye mradi huu ambayo yanaweza hayana tija kwenye nchi. Kwa ajili ya kuwasaidia nashauri badala ya kuweka kama ilivyo kwenye kutoa authority na mandate kwenye Bazara la Mawaziri, isomeke kwamba: “Makubalino yoyote yenye kuhitaji utaratibu maalum wa utekelezaji na ambayo yana kibali cha Bazara la Mawaziri hayatakuwa na sifa ya kuandaliwa utaratibu maalum wa utekelezaji, isipokuwa yatapitishwa na Bunge kupitia Kamati ya Bunge ya sekta husika kuwa yanahitaji kuandaliwa utaratibu maalum wa utekeelzaji”. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nime-propose hivi kwa sababu Kamati za Bunge hili ni Kamati zinazoheshimiwa sana na Bunge hili na sisi tuna imani na Kamati hizo ndio maana wanakuja kusoma taarifa za Kamati. Kwa kweli mimi mwenyewe nilikuwepo kwenye Kamati na pia nakubalina na mapendekezo ya Kamati. Tukiweka hivi itatusaidia pia Bunge ku-oversight na ku-oversee kwenye masuala mbalimbali, pamoja na kwamba yatapitiwa kwenye Baraza la Mawaziri na Baraza la Mawaziri lita-authorize, lakini Kamati mahsusi za kisekta zitakuwa na mkono wake kwenye jambo hili. Wakati mtoa hoja anakuja kuhitimisha nashauri sana aangalie jambo hili upya na kwa ubora na kwa umakini zaidi. Tuone namna gani tunaweza kusaidia nchi yetu kwa sababu tumezungumza kwamba baadaye inaweza kutokea changamoto lakini kwa sasa hivi nashauri iwe hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati imeshauri na mimi naendelea kushauri, wenzetu Waganda tayari wameshaanza maandalizi ya kutunga sheria mahsusi kwa ajili ya ku-facilitate Bomba hili. Sisi tunafanya marekebisho kwenye zile sheria 14 ambazo zinahusiana na Bomba hili lakini in the future tukiwa na sheria mahsusi ambapo Bunge tutajadili kwa upana wake kama ambavyo Waganda wenzetu wanatunga sheria mpya kwa ajili ya kuwezesha utekelezaji wa Bomba hili itakuwa vizuri sana. Nashauri pia Bunge letu Tukufu tutunge sheria hii mahususi, kwa ajili ya Bomba hili ambayo itatusaidia kuweka mambo mengi kwa upana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. (Makofi)
The Water Resources Management (Amendment) Act, 2022
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Muswada wa Sheria ya Usimamizi wa Rasilimali za Maji kama ambavyo wenzangu wameshaanza kuchangia. Kwanza nipongeze flexibility ya Serikali, sasa neno flexibility hapo utasema tuongee Kiswahili moja kwa moja tutasaidiana. Nipongeze utayari na hiyo flexibility ya Serikali namna ambavyo wameweza kuingiza mawazo ya Wajumbe wa Kamati lakini pia na wadau mbalimbali ambao wametoa maoni yao kwa maana ya watumiaji wa maji, lakini pia taasisi ambazo zinashughulika na usimamizi wa masuala ya maji. Kimsingi ndiyo jukumu la Serikali la msingi kusikiliza na pamoja na kufanyia kazi ushauri wa wataalam, lakini pia na watu ambao wako kwenye hiyo sekta ya matumizi ya maji tukiwemo sisi Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii sasa ndiyo kazi ya Bunge tunayoizungumza, kwamba hapa sasa ndiyo tunatunga sheria na naona jukumu langu la msingi kuhakikisha kwamba tunashauri Serikali kwenye namna bora tunaweza tukatumikia watu waliotupa majukumu ya kuja humu ndani kwa ajili ya kuwawakilisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nisaidiane na Mheshimiwa Waziri kama na yeye huu Muswada ambao tunaufanyia marekebisho unasomeka kwamba ile sheria mmei-quote kwenye Muswada kwamba ni Water Resources Management Act. Kwenye bill imeandikwa 2019 na sijui kama kwa Waziri pia iko hivyo, nafikiri ni tatizo la uandishi kwa sababu katika Sheria zote za Maji, Sheria ya mwaka 2019 ni Water Supply and Sanitation Act ndiyo ya mwaka 2019, kwa hiyo naomba hapo irekebishwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo mengi ambayo Wizara imejaribu kuyagusa katika kufanya marekebisho ya hii sheria, kuna sehemu moja ambayo wameitaja na nawapongeza sana kwa sababu wanajaribu kuingiza dunia inapokwenda mabadiliko ya tabia ya nchi na athari za kimazingira. Kifungu cha 37 kwenye sheria mama ambacho kinaeleza maeneo tengefu ya maji wameingiza na kwa kweli ni jambo zuri ambalo kwenye bill ni namba nane, ni jambo zuri kwa kweli nalipongeza. Kwenye Muswada ni namba nane lakini kwenye sheria mama ni namba 37.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jambo zuri na kwa kweli sisi linatuonyesha utayari wa Serikali kwenye kulinda vyanzo vya maji, kwa sababu watu wote katika sisi wananchi wote duniani humu kinachotutambulisha ambacho kinatuunganisha, kwa sababu maji yako dunia nzima, kwa hiyo jitihada za Serikali kuhakikisha kwamba wanalinda vyanzo vya maji na maeneo tengefu ni jambo la kupigia mfano na tuwapongeze pia Kamati kwa kuishauri Serikali na Serikali kupokea na wamefanyia kazi, kwa hiyo yapo mazuri mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa lengo tunataka tujenge, kuna mambo mengine wameyaweka ambayo nafikiri katika uandishi bora wa sheria kwa kipindi ambacho tunacho kuna kifungu cha 24 cha sheria mama ambacho kwenye Muswada ni kifungu cha 7 ambako wameweka sifa za Mkurugenzi wa Bonde la Maji kwa kuandika kabisa sifa:

(a) Atatakiwa awe na Shahada ya kwanza katika masuala ya maji;

(b) Anatakiwa awe na uzoefu wa miaka mitano katika nafasi za uongozi na utawala;

(c) Awe ana uelewa na uzoefu kwenye sekta ya maji; na

(d) Ama sifa nyingine zinazofanana na hizo

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiki ni kitu kizuri kwa sababu hatuna uhaba wa wataalam, tuna Chuo cha Maji na wanatoa wataalam ambao ni the best na masuala ya uzoefu kwa sababu pia tunahitaji watu ambao at least wameshafanya hivyo vitu, wanajua, kwa sababu nchi hii bado inaendelea kwenda mbele na kwa sababu tunao hao watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri badala ya kuweka kwenye sheria kama ilivyo sasa hivi kwa sababu tuna kanuni, kuna regulations, bila kutoa chochote inaweza ikawekwa kwenye regulation badala ya kuwekwa kwenye sheria kama ilivyo. The best way ya kutunga sheria kwa sababu hata kama zipo sheria kwenye nchi yetu nyingine ambazo wameweka sifa za wataalam kwenye sheria, lakini kwa sababu hili Bunge ndiyo kazi yetu kutunga sheria, nashauri tuweke kwenye kanuni badala ya kuweka kwenye sheria, vingine vilivyobaki sina shida navyo kwenye kipengele hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu cha 44 kwenye Principal Act ambapo kwenye bill ni kifungu cha 11 kinafutwa na kuandikwa upya na lengo lake lilikuwa ni kuweka masharti ya adhabu na kuyatambulisha makosa ya masuala ya matumizi ya maji. Najua hapa lengo lilikuwa zuri, lakini kuna maneno nitayanukuu: -

“Kwamba mtu yeyote anayetumia maji zaidi ya kiwango kilichoidhinishwa kwenye kibali chake cha matumizi ya maji au anatumia maji kwa dhumuni tofauti na lile lililoidhinishwa katika kibali chake cha matumizi ya maji anatenda kosa na akipatikana na hatia, faini ni kuanzia laki tatu mpaka milioni tano au kifungo cha miezi mitatu ama miezi sita.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni sawa, najua wanajaribu kubana kwa sababu hata mimi ningekuwa Waziri, huwezi kuwa wewe kazi yako kwenda kukagua tu, kwenda kuzindua mabomba ya maji sijui na nini na kuna watu wanaharibu vyanzo vya maji. Kwa hiyo najua lengo ilikuwa ni kuhakikisha kwamba tunatengeneza mazingira ya watu kuheshimu vyanzo vya maji, lakini kuhakikisha kwamba Serikali inatimiza jukumu lake la kuhakikisha kwamba watu wanapata maji safi na salama which is very good.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwamba mtu amezidisha matumizi ya maji tofauti na kibali alichoomba, tunajua watu wanaoshughulika na masuala ya maji huwezi kufanya approximation mtu akatumia maji 100 percent kama walivyofanya makadirio. Kwa hiyo, nilifikiri ni busara mtu ambaye ameomba kibali cha matumizi ya maji asihesabike kama amefanya kosa endapo atazidisha ila alipe kutokana na kiwango kilichozidi katika matumizi yake, kwa sababu tunaishi kwenye nchi ambayo uchumi wetu pia maji ni sehemu ya mikakati au vyanzo vya uchumi kwenye nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wanafuga, watu wanalima sasa wakati mwingine huwezi kukadiria asilimia 100 ndiyo maana tunasema mtu asionekane kama ametenda kosa badala yake alipie kwa sababu tuna chagiza na tunasisimua uchumi tunaita baadae of course nimeleta schedule of amendment tunaweza tukaona namna gani ambavyo tunaweza tukashauri kiandikwe katika namna bora sana ambayo bado utaendelea kuweka mikakati, kwamba unaendelea kulinda vyanzo vya maji na matumizi ya maji lakini unatoa pia nafasi kwa Watanzania kufanya shughuli zao za kiuchumi kwa sababu hata Serikali inategemea kupata mapato kutokana na shughuli za kiuchumi kwenye nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye Kifungu hicho kuna kipengele kingine ambacho kinazungumzia kutumia maji tofauti na kibali mtu alichoomba, hapa imeonekana kwamba ni kosa kama mtu ataomba kibali hiki baadaye mtu ukabadilisha matumizi. Nafikiri ilikuwa ni bora sana kama tutatafuta namna bora tusifanye kama kosa la jinai hichi kitu kwamba analazimika mtu a-notify Bodi ya Maji, a-notify kwamba amebadilisha matumizi, nafikiri Serikali ijikite kwenye umetumia kwenye kiwango ambacho uliomba utatumia na ikizidi ulipie palipozidi kuliko kwamba leo niliomba kibali cha kufanya umwagiliaji lakini nimepata fedha sehemu nataka niongeze na ufugaji nionekane kwamba nimebadilisha matumizi ya maji, nafikiri siyo sahihi ni kwenye namna tu ya uandishi mtaangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema ninakubaliana na kwamba tunajaribu kutafuta namna ambapo Serikali inaweza ikafanya jukumu lake la kulinda vyanzo vya maji na matumizi sahihi ya maji. Otherwise niwapongeze sana Serikali na niseme tu kwamba tupo pamoja kwenye hili na nikutakie kila la kheri katika usimamiaji kwa sababu tunakufahamu ndugu yetu umekuwa ukifanya majukumu makubwa na watu wa Kamati pia tunawapongeza sana kwa sababu wameendelea kila siku bila kuchoka kutoa michango yao kwenye Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.2) wa Mwaka 2023
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali, (Na. 2) ya Mwaka 2023. Kusema ukweli kabisa nilikuwa nimejiandaa kuchangia Sehemu ya Nne na ya Tano ya Muswada.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, ninafahamu sana majukumu na kazi ya Bunge hili na kwa kweli imekuwa ni desturi kwamba, tunatunga sheria na tunajipa muda kwa sababu ni ukweli kwamba ukishatunga sheria unahitaji muda ili u-practice uone kama kuna shida ili sasa Bunge hili lirudie kazi yake ya aidha kurekebisha, kuandika upya ama kutunga sheria nyingine ambayo itakuwa kwa maslahi mapana ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama ambavyo ninajua kwamba, ni desturi hiyo siku zote kwenye Bunge hili tunafanya, nilitegemea pia tujadili sana kuhusiana na hili, lakini niipongeze sana Serikali kwa kuona hayo ambayo yalionekana na wengine na Kamati pia imeshauri. Kwa hiyo, nikubaliane na Kamati walivyoona kwamba, na wao wameipongeza Serikali kwa kuondoa vifungu hivi kwa sababu za sasa hivi, lakini pia niwaombe Serikali wala siyo jambo la kuwa na wasiwasi nalo, kwa sababu lengo ni kuhakikisha kwamba tunavuna rasilimali zetu kwa faida ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama kuna sheria nyingine yoyote ambayo mnafikiri kwamba, Bunge hili linahitaji liletewe ili tuireirekebishe kwa ajili ya kuvuna rasilimali za Taifa hili kwa urahisi ili Watanzania wenye rasilimali hizo wanufaike basi tusiogope kuleta. Mimi nitakuwa tayari na ninajua Waheshimiwa wenzangu pia watakuwa tayari kwa ajili ya kujadili muda wowote ambao tutaona ni wakati sahihi wa kujadili pamoja na hiki Kifungu cha Nne na cha Tano kwa sababu, tunajua kabisa kuna maslahi mapana kwenye jambo hili.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa sababu hilo sasa hivi limeshaondolewa na tutalisubiri tunajua wakati mwingine linaweza kuja, kwa sasa hivi kwenye hizi zilizobakia ninaomba nichangie Sehemu ya Tatu ya Muswada ambayo inahusiana na Dar es Salaam Maritime Institute Act, Cap. 253, kwa sababu, na mimi pia ni Mjumbe wa Kamati, siyo Kamati hii ni Mjumbe wa Kamati ya Elimu na hili jambo linahusiana na taasisi mojawapo ambayo inatoa elimu hiyo specific. Kwa hiyo, niwapongeze. Kwenye huu Muswada mzima utaona ni ukurasa wa 16 mpaka 34 umezungumza na kwa Ibara zote ambazo wameona.

Mheshimiwa Spika, nikianzia Ibara ya 17 ambayo inaainisha cheo sahihi cha Mkuu wa Chuo kuendana na NACTE (NACTVATE), lakini pia Ibara ya 18 ambayo imeondoa mamlaka ya Waziri kutoa ithibati kwa wanafunzi kuanzisha taasisi ya wanafunzi, tunazijua zile za DARUSO, UDOSO na nyingine kama hizo, lakini ya pale na kuipa Bodi. Niwapongeze sana kwa hili kwa sababu najua kwamba, Bodi wanaweza kufanya vizuri kwa practice ambayo tumeiona.

Mheshimiwa Spika, lakini hiyo ni (A) na (B) yake ambayo imeongeza tafsiri ya Academic Council ambayo ni sehemu ya marekebisho katika hizi ambazo wanazifanya kwenye hii Sheria ya Bandari. Hilo pia nilipongeze ni jambo zuri katika practice. Ibara ya 22 ambayo imeanzisha Baraza la Taaluma la Chuo, ninakubaliana pia na maoni ya Kamati ambayo wametoa na kwa kweli, tungekuwa na muda hata usingetosha kujadili lile jambo la mwanzo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi nipongeze na kwa kweli, sisi tuko tayari kwa ajili ya kutunga hiyo sheria ili Mheshimiwa Rais akaipitishe ili mambo yaende. Na sheria hiyo nyingine ya masuala ya atomic, wamezungumza Waheshimiwa wenzangu na ninakubaliana na maoni yao na kwa kweli, niseme naunga mkono hoja hiyo ya kufanya marekebisho ya sheria hizi ili tuendelee ku-practice kazi ya Bunge hili ambayo ni kutunga sheria na kurekebisha sheria ambazo tunaona katika practice zinawezekana zina shida. Ahsante. (Makofi)