United Republic of Tanzania
Parliament of Tanzania
SPIKA wa Bunge Mhe. Job Ndugai amewataka Watanzania kujitokeza kusajili laini zao mapema kwa kutumia mfumo wa kielektrioniki ili kuepuka usumbufu unaoweza kujitokeza baada ya muda kuisha.
Mhe. Spika alitoa wito huo Jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari baada ya kutembelea mabanda ya kampuni mbalimbali za simu ambazo zilisogeza huduma hizo bungeni ili kuwezesha wabunge na watendaji mbalimbali kusajili laini zao za simu bila usumbufu
Alisema Watanzania wanapaswa kuhakikisha wanajiandikisha Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) ili wapate vitambulisho au namba zitakazowawezesha kusajili laini zao za simu kwa kutumia mfumo wa kielektrioniki.
“Mimi nimeshatoka kujiandikisha kwa kutumia kitambulisho cha NIDA hivyo watanzia wajiandikishe mapema badala ya kusubiri hadi muda uishe ifikapo Desemba 31. Hii itapunguza uhalifu kwa njia ya mtandao kwa kiasi kikubwa,”alisema.
Aidha, alisema hakuna Mbunge yoyote ambaye atashindwa kusajili laini yake ya simu kwa kutumia alama za vidole kwa kampuni anayoitaka.