Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Grace Victor Tendega (47 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kupata fursa ya kuchangia kwa maandishi kuhusu Wizara hii. Kwa masikitiko makubwa nalaani kitendo cha kutokuwa na uhuru wa tasnia ya habari kama inavyotekelezwa na Bunge lako Tukufu. Kwa sisi akinamama na vijana katika nchi hii tumekuwa tukipambana na maisha na mara nyingi tulikuwa tunasahaulika. Uhuru wa vyombo vya habari ulifanya wanawake wengi waingie kwenye tasnia ya siasa kwa kuwa wamekuwa wakiwaona wenzao waliotangulia wakifanya uwakilishi wao Bungeni vizuri na hii ilihamasisha wanawake wengi kuona kuwa wanaweza.
Mheshimiwa Spika, akina Getrude Mongela, Asha Rose Migiro, Spika aliyestaafu Mheshimiwa Anne Semamba Makinda, Mheshimiwa Halima Mdee, Mheshimiwa Pauline Gekul na wengine walionesha mfano kuwa wanawake tunaweza. Kwa namna hii inaonesha kuwa, Bunge hili linataka kudidimiza kufikisha 50 kwa 50 kwani wengi wanawake waliogombea wameweza kushinda Ubunge wa Majimbo na waliaminiwa na wananchi wao kwa kuwa walionekana wakitetea maslahi ya Watanzania.
Mheshimiwa Spika, nashauri Bunge hili lirushwe live ili wanawake tupate fursa ya kuonekana ili kuondokana na kuwa Wabunge wa Viti Maalum.
Mheshimiwa Spika, suala la Zanzibar. Nchi yenye utawala bora haina woga wowote, lakini nchi yetu imeonesha ufinyu wa demokrasia kwa suala la uchaguzi wa Zanzibar. Serikali inapaswa kutumia busara zaidi na si ushabiki kuhakikisha Zanzibar inakuwa tulivu.
Mheshimiwa Spika, kuhusu Watumishi hewa; naunga mkono hotuba ya (KRUB) iliyofafanua jinsi udhibiti wa wafanyakazi utakavyokuwa kwa kuunganisha mfumo, mfano, mfumo wa Utumishi wa Umma uunganishwe na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kama vile NSSF, PSPF, LAPF, GEPF na kadhalika. Kwa wale wahusika wote pia wachukuliwe hatua za kisheria.
Mheshimiwa Spika, nimeshukuru na naunga mkono hoja ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni (KRUB).
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata fursa hii ya kuchangia kwa maandishi na nitajikita katika kilimo. Nashauri Serikali ijikite katika kutoa elimu juu ya uzalishaji wa mazao bora ya kilimo. Kwa mfano, Mkoa wangu wa Iringa una Kiwanda cha Nyanya chini ya mwekezaji kiitwacho DARSH kwa ajili ya kusindika nyanya. Iringa huzalisha karibu zaidi ya 50% ya nyanya inayozalishwa Tanzania lakini kumekuwa na changamoto ya upatikanaji wa uhakika wa nyanya. Wakulima wamekuwa wakilima nyanya zisizokidhi ubora unaotakiwa kiwandani kwa kukosa elimu ya kilimo bora cha nyanya.
Pia wakulima hawa hawajaandaliwa kwa kilimo hicho kwani wengi wao hulima kienyeji. Mahitaji ya kiwanda ni zaidi ya tani 200 kwa siku ambapo mara nyingi hazipatikani na wengine husafirisha kwenda Mkoa wa Dar es Salaam. Hivyo, uzalishaji wa kiwanda hicho hauna tija kwa kuwa wakulima hawajaandaliwa. Nashauri Serikali iwaandae wakulima kuzalisha kwa ubora na uhakika.
Mheshimiwa Naibu Spika, sababu au changamoto nyingine ni gharama ya mbegu. Mfano, hybrid seed (Eden na Asila) gramu 30 kwa ekari moja ni Sh. 210,000. Ni gharama kwa wakulima wetu walio wengi, nazungumzia (hot culture). Vile vile hakuna Maafisa Ugani wa kutosha kupita kwa wakulima vijijini hasa katika Wilaya ya Iringa, Jimbo la Kalenga, Kilolo na Isimani. Nashauri Waziri anapojibu hoja hizi atueleze ni lini wananchi wa Wilaya ya Iringa watapatiwa Maafisa Ugani wa kutosha?
Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri mkulima awezeshwe bajeti ya mbegu, mbolea na viatilifu (pesticides). Wakulima ambao wanatumia madawa hayo kwenye mazao mara nyingi magonjwa hayaishi mfano ugonjwa wa kantangaze kwa sababu madawa haya wakati mwingine ni feki. Makampuni mengi yanauza madawa yasiyofaa, Waziri afuatilie na kuzingatia hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mbolea zinazotumika ni za gharama kubwa mfano yara. Mbolea hii mfuko mmoja ni Sh. 90,000 wananchi wa kawaida hawawezi kumudu kutumia na hivyo kusababisha kuzalisha mazao yasiyo na ubora.
Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo cha umwagiliaji ni suluhu kwa uzalishaji mazao mbalimbali. Wizara ihamasishe kilimo cha matone lakini wakulima wawezeshwe kwani hawataweza kumudu drip lines. Serikali itoe mitaji kwa wakulima na pia iwe na Benki ya Wakulima.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Kiwanda cha Chai kilichopo Wilaya ya Kilolo, mpaka leo hii kimefungwa na kinakatisha tamaa wakulima wa chai wa wilaya hiyo. Naomba Serikali itoe majibu ni lini kiwanda hiki kitaanza kuzalisha ili wakulima wa chai waweze kujikwamua kiuchumi?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia REA inafanya kazi ya kusambaza umeme vijijini, pamoja na kufanya kazi hiyo katika Mkoa wa Iringa, Wilaya ya Iringa Vijijini kuna substation iliyopo katika Kijiji cha Tagamenda ambapo umeme umeanza kusambazwa kwenda mikoa mbalimbali ikiwemo Shinyanga na mingine
Mheshimiwa Naibu Spika, kitu cha kushangaza, wanakijiji wanaofanya kazi ya kulinda umeme huo, hawajapata umeme hata huo wa REA. Swali kwa Wizara, hivi hawaoni kuwa hawawatendei haki wananchi wa Vijiji vya Tagamenda, Wangama, Ikuvilo na vingine ambao huishi karibu na kituo hicho substation kuunganisha umeme huo au hata wakapata umeme wa REA na wasiwe walinzi tu wa kituo na nyaya hizo?
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, anapohitimisha naomba kupata majibu ili tuweze kuondokana na adha hii kwa wananchi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika bajeti hii ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Nianze kwa msemo usemao; if education is expensive try ignorance.” Kwa tafrisi ya kawaida tu inasema kwamba, kama elimu ni gharama jaribu ujinga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nazungumza hivi kwa sababu, tunaangalia jinsi ambavyo elimu ya nchi hii inavyokwenda. Nashukuru sana Kamati ilivyotoa maoni yake kwa ajili ya kujenga na kuboresha Wizara hii ya elimu. Naafiki kabisa maoni na mawazo ya kamati ambayo yametolewa, yatasaidia sana kuboresha katika Wizara hii ya Elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, najikita katika sehemu kubwa kuhusu udhibiti ubora, kwa maana ya kwamba, zamani tulikuwa tunasema ni ukaguzi. Tunazungumza, watu wengi wanazungumza kwamba, ooh, tubadilishe mitaala, tufanye hiki, tufanye vile, ili tuendane na hali halisi ya maisha yanavyokwenda. Ni kweli ni vizuri tukafanya hivyo, lakini kitendo cha kubadilisha, yaani total over hauling ya curriculum inachukua miaka mingi sana. Kwa hiyo, huwa tunakwenda tunabadilisha, labda tunaboresha wakati tuna-plan kubadilisha hiyo mitaala kulingana na haja kamili tunayoitaka ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi mbalimbali zinakuwa na targets kwamba, sisi tunataka nchi yetu iwe ya namna gani? Tunataka wananchi wa Tanzania wajikite kwenye mambo gani? Kilimo, muziki ama ni watu wa viwanda sana au kitu kama hicho? Kwa hiyo, lazima kuwe na tafiti ya muda mrefu na wananchi wakubaliane na wadau kujua kwamba, tunataka nchi yetu iendeje na uchumi wetu uweje?

Mheshimiwa Spika, sasa kwa sababu bado hatujaanza huo mchakato, nashauri katika usimamizi ubora wa elimu, udhibiti ubora. Sasa nikianza na hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Elimu aliyoitoa hapa, ukurasa wa tisa na ukurasa wa 15 nimeona kuna contradiction kidogo ya taarifa zake katika namba. Waziri amezungumzia kwamba, katika mwaka huu uliopita walikuwa wameweza, plan yao ilikuwa ni kukagua shule 4,700 za msingi, lakini walikagua shule 2,755, kati ya shule 2,726 ambayo ni asilimia 101.

Mheshimiwa Spika, ujue tuna shule 18,152. Sasa tukiwa tunajipima hivyo kwamba, hapa tumekagua asilimia 100, lakini hali halisi tunaiona, shule zetu hazikaguliwi na usipokagua watu hawafanyi kazi kwa ufanisi, walio wengi. Sasa kwa sababu, hawafanyi kazi kwa ufanisi mtaona kama ile mitaala haifanikiwi, lakini kumbe ufanisi, ukimkagua mtu anaongeza juhudi, anaongeza speed ya kufanya kazi. Sasa kutokuweka idadi kubwa na targets zao za kukagua sana shule zetu wataona changamoto zilizopo kati ya shule za Serikali na shule za private. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, shule za private zinakaguliwa na zinakaguliwa kwa sababu shule zile zinatoa pesa wakaguzi wanakwenda kukagua zile shule. Kwa hiyo, utakuta kwamba, mara nyingi wale wanafanya kazi kwa juhudi kwa sababu, kuna ukaguzi uko pale, lakini shule zetu zinakwenda tofauti na hivyo.

Mheshimiwa Spika, sasa nitajikita katika udhibiti ubora katika shule zenye mahitaji maalum. Katika Ripoti ya CAG amezungumza kwamba, kuna changamoto ya usimamizi wa ubora wa elimu katika hizi shule, unakuta kuna miaka inapita hazikaguliwi kabisa. Na kama hazikaguliwi, lakini tuna uhaba wa Walimu wa kwenda kukagua hizo shule, ni wachache. Katika, anasema ni asilimia nane tu ndio waliopo ambapo tuna mahitaji ya Walimu 1,306, sisi tuna asilimia nane tu.

Mheshimiwa Spika, hawa ni wenzetu, watu wenye ulemavu ni wenzetu. Shule zipo, lakini tuna chuo kimoja tu kinachotoa Walimu wa watu wenye ulemavu ambacho kiko Patandi. Walimu wakisomea pale wanapelekwa katika shule ambazo hazina watu wenye mahitaji maalum. Kwa hiyo, unakuta kwamba, Wizara inaweza ikawa inapeleka watu kusomea hicho kitu, lakini hawapangiwi kule, matokeo yake inakuwa ni changamoto ileile inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama hiyo haitoshi, imeonesha kwamba, hakuna vifaa vya kufundishia asilimia 68 katika shule 17 kati ya 18 walizotembelea, lakini hakuna utaratibu endelevu wa kugharamia ukaguzi katika hizo shule. Mwaka jana walitenga shilingi milioni 272 katika Wizara ya Elimu kwenda kukagua hizo shule.

Mheshimiwa Spika, kwa kitendo ambacho kinaumiza kabisa badala ya kwenda kukagua, Wizara ilipeleka hizo fedha kwa ajili ya mitihani ya darasa la nne na pia ilipeleka kwenye mashindano ya lugha ya Kiingereza Afrika Mashariki. Sasa utaona jinsi ambavyo zile pesa zilitengwa, lakini hazikwenda kwenye ukaguzi wa hizo shule. Matokeo yake ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utaona kwamba, tunapata changamoto kubwa ya kuziendesha hizi shule kwa sababu, hakuna wakaguzi, hatuna Walimu, hakuna uendelevu wowote wa utengaji wa fedha katika hili. Nimwombe Mheshimiwa Waziri aweze ku-consider na hii sekta kwa watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, niende sasa katika mafunzo kwa Walimu kazini. Tulikuwa na kawaida miaka iliyopita Walimu kazini walikuwa wanapata mafunzo wanapelekwa kwenye vyuo; Chuo cha Songea, Butimba, Morogoro na vyuo vingine kwa miezi mitatu, mitatu angalau kunolewa kuona ni nini ambacho watakwenda kufundisha. Mkiboresha mitaala kuwa ya competence-based curriculum hiyo, unachukua Walimu wale wakapate ile knowledge ya kufundisha hivyo, kwa sababu, kila mara kuna mabadiliko yanatokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hiki kitendo kimekuwa ni cha, kama wanatoa ni kidogo sana, lakini Walimu wanahitaji kupata haya mafunzo ili waweze kunolewa kwenda na wakati. Kama tunavyosema kwamba, tunataka mitaala iende na wakati, lakini tunataka na Walimu waende na wakati, ili waweze kufundisha vizuri wanafunzi wetu tusilalamike kwenye matokeo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia Taarifa ya CAG inaonesha kwamba, hakukuwa na mpango wowote wa kutoa mafunzo kwa Walimu wa sekondari. Walimu wa sekondari hawakupata kabisa mafunzo hayo kazini ambapo ndipo wanaponoa wanafunzi wetu waweze kufanya vizuri katika masomo yao.

Mheshimiwa Spika, pia nakubaliana na Kamati wanavyosema kwamba, tuweze kuwawezesha kutoa mikopo kwa wanafunzi wanaochaguliwa kwenda kwenye vyuo ambavyo vinasimamiwa na NACTE kwa sababu pale ndio tutapata wanafunzi ambao wakitoka ndio watakuja kuwa watenda kazi katika viwanda ambavyo tunavitarajia kuvijenga. Kwamba, tutakuwa na viwanda, watenda kazi watakuwa ni wale wanafunzi watakaokuwa kule, lakini kama hawatakuwa wanapewa mikopo ni changamoto bado inabaki kuwa kubwa kupata hii kada ya chini ambayo ndio ya watenda kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kweli, kwa kutoa ile asilimia ambayo ilikuwa kwenye Bodi ya Mikopo, asilimia sita na pia Mheshimiwa Waziri amezungumza hapa pia, wametoa hata ile asilimia nyingine 10. Nipongeze kwa hilo kwa sababu, hiki kilikuwa ni kitu ambacho kinawaumiza sana vijana wengi na wengi ambao wanasoma elimu ya juu kuona kwamba, wanaweza kulipa namna gani, mishahara ilikuwa inakatwa, walikuwa wanashindwa kufikia malengo. Napongeza kitendo hicho kinasaidia sana, kitasaidia watu kufanya kazi kwa juhudi na kujua kwamba, Serikali yao inawajali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende sasa kwenye jambo ambalo sio la mwisho kwa umuhimu, tuna wanafunzi wa kike wanaopata ujauzito kwa bahati mbaya. Sihalalishi kwamba, wale wanaofanya hivyo kwamba, ni halali, hapana, lakini kuna wanafunzi kwa mazingira yaliyopo kule vijijini na maeneo mengine wana mazingira magumu ambayo inafikia wanakutwa na hali hiyo. Nakumbuka mwaka 2015 kulikuwa na swali lilitolewa hapa na Mheshimiwa Magreth Sita na Naibu Waziri akaahidi kwamba watatengeneza mwongozo wa namna ya kuwahakikisha hawa vijana wanarudi shule. Kwa hiyo naomba mheshimiwa Waziri anapohitimisha basi tujue wanafunzi wetu watafikia wapi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakumbuka mwaka 2015 kulikuwa na swali lilitolewa hapa na Mheshimiwa Margaret Sitta na Naibu Waziri akaahidi kwamba watatengeneza mwongozo wa namna ya kuwahakikisha hawa vijana wanapata kitu.

SPIKA: Ahsante.

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba mheshimiwa Waziri unapohitimisha basi tujue wanafunzi wetu watafikia wapi ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. GRACE V. TENDEGA: Me Spika, hoja yangu ni kuhakikisha tunajumuisha umeme wa jua ili kuongeza nguvu kwa TANESCO. Kule Iringa kuna mwekezaji ameshaainisha eneo Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Jimbo la Kalenga, Kijiji cha Kilambo. Naishauri Serikali iweze kuharakisha katika kuidhinisha mradi huu uanze, kwani utasaidia siyo tu kutoa ajira, bali kuharakisha maendeleo. Ahsante.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ilii na mimi nichangie katika hotuba hii ya bajeti iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilikuwa inanipa ugumu sana kupongeza sana, lakini kwa mara ya kwanza ninapenda kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuleta bajeti ambayo kiasi fulani imeakisi zile kelele ambazo tulikuwa tukizipiga. Ninasema hivi kwa sababu Mheshimiwa Rais alituita pia wanawake wote bila kujali itikadi. Tulikwenda, tulimsikiliza na tukaona kwamba vitu anavyovizungumza ni vitu ambavyo vikitekelezwa ipasavyo vitamkomboa Mtanzania na kuhakikisha kwamba nchi yetu inasonga mbele. (Makofi/ vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya hivyo katika bajeti hii nitanukuu vitu vichache ambavyo tumeona angalau vinaweza vikasaidia Halmashauri zetu Mikoa yetu, Wilaya zetu, wananchi wetu wakasonga mbele kama tutatekeleza vile anavyotaka. Mheshimiwa Waziri amesema katika hotuba yake kwamba watahakikisha kwamba fedha ambazo zilikuwa zikitumwa katika Halmashauri mwishoni mwishoni, yaani kwa mfano mwezi Juni au Mwezi Mei wataniacha na wataziacha zitekelezwe lakini tunaomba Mheshimiwa Waziri mtuletee kanuni ili zikienda kule zisiende zikakae muda mrefu pia ili ziweze kutumika. Tunapongeza kwa hilo kwa sababu zilikuwa zikifika Juni na zinaondoka, kwa hiyo ilikuwa inaleta shida sana katika utekelezaji wa majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia watu wamezungumza kuondoa ushuru wa nyasi bandia. Nasisitiza hili ni jambo jema kwa sababu tunakuza nyanja zote, ukikuza hata katika michezo hii itasaidia, lakini wasiishie mijini tunaomba Mheshimiwa Waziri waende mpaka vijijini, zile halmashauri ambazo zitaweza kuwa na viwanja wakanunua hizo nyasi basi wafanye hivyo, waliangalie wakati anakuja kuhitimisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi kupungua asilimia tano za mabango ya categories zote, hii ilileta shida sana, tukakuta kuna watu walianza sasa kuwa wanaweka kaa alama tu kadogo pale wakawa wanakosa kodi. Sasa kupunguza watu watalipa kodi na watapata mapato na kodi ikitolewa ndipo tutaweza kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nina mambo mawili pia ya kusisitiza katika hili. Kodi ya majengo wamesema itakuwa kupitia LUKU. Wamezungumza wengi hapa kwamba nyumba ikiwa na wapangaji wengi itakuwaje wataiwekaje sawa. Nataka wanapokuja kuhitimisha waniambie, kuna nyumba ambazo zinatumia solar, kuna nyumba ambazo zinatumia biogas, sasa hazina LUKU watapataje sasa kodi zake hapo? Mheshimiwa Waziri aje atuainishie namna ambavyo watapata kodi kupitia hii, kwa sababu siyo wote wana umeme na kuna maeneo mengine hakuna umeme. Kwa hiyo, waje na mkakati maalum wa kujua kwamba kama watachukua kwa kupitia LUKU watafanyaje, lakini waliweke sawa pia kwa sababu mwenye nyumba yupo, wakiwa wapangaji watupu pesa zile atakwenda kuchukua kwa wapangaji. Sasa hili watuwekee sawa hapa Waziri anapohitimisha ili tujue tunafanyaje katika hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kodi ya mapato Pay As You Earn wamesema kiwango cha mwanzo hawatozi kodi, lakini kiwango kinachofuata kinatozwa kodi. Ukiangalia hii napongeza kweli wametoa asilimia moja safi kabisa, lakini haitoshi. Ukipiga mahesabu unakuta karibu tu ni Sh. 2,700. Sasa Sh.2,700 bado ni kidogo, ni ndogo sana. Kwa hiyo tuombe waiangalie vizuri kukata mzizi wa hili lote, tuwapandishie mishahara watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwapandishia mishahara watumishi, wataweza kulipa kodi, lakini pia ni motisha kwao kwa kufanya kazi kwa juhudi na vile vile wanaweza wakatoa kodi. Kwa hiyo Serikali itapata benefits humo kwa kufanya hivyo kwa sababu itawafanya wawe na moral kubwa kabisa ya kujenga uchumi wa nchi na vile vile kiinua mgongo kitapanda. Tunajua kabisa watu wanastaafu, viinua mgongo vinakuwa chini, wameona kwa miaka mitano watumishi hawakupandishiwa mishahara, kwa hiyo wakifanya hivyo wataondoa kero ambazo zinawaumiza sana Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mama amezindua kule Mwanza SGR kwa Mwanza. Sasa waharakishe basi ikamilike, kwa sababu kwa SGR tutaondoa mrundikano unaokuwepo pale Dar es Salaam. Kwa hiyo mizigo itakuwa inakwenda kwa haraka na uchumi utapanda. Hivyo, wakiweka mikakati mizuri wataweza kufika mbali na kuondoka kero za wananchi ambazo zipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende katika suala la kodi. Naomba Mheshimiwa Waziri anisikilize, mkoloni alikuja, alivyokuja hakuja na hela, alipokuja alikuja na wazo, alikuja na idea kwamba atafanya nini, kaikuta nchi ya Tanzania, akakuta kuna ardhi, alivyokuta kuna ardhi akaona hii ardhi itanufaisha watu kwa kilimo, kukawa na kilimo cha mkonge, katani na vitu kama vile. Akasema anatunga Sheria ya Kodi, kwa hiyo alivyotunga Sheria ya Kodi wananchi wao wenyewe waliinuka kwenda kufanya kazi pale ili waweze kupata pesa, watoe kodi na ndiyo hayo unayoyaona, tukachenjua barabara hizo mnazoziona, kodi ilitumika kujenga nchi, tukaweza kufanya mambo mengi sana ambayo yalifanyika kipindi hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hapa katikati tulilegalega, kodi inatolewa lakini mambo hayaendi, watu wakawa hawajui kodi inaenda kufanya nini. Sasa nimwombe Mheshimiwa Waziri, hawa watu wa Wizara wawe na mikakati maalum ya ukusanyaji wa kodi. Huu ukusanyaji usiwe wa kinguvu, iende ifike mahali wananchi wenyewe waone kwamba kutoa kodi inamlazimu, yaani akinunua kitu asitoe kodi yeye mwenyewe kwa maumivu. Hivi kweli unaletewa barabara nzuri, kuna maji safi na salama, una afya unapata madawa na nini hospitalini, nani atakataa kutoa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kila kitu kikionekana kinafanyika vipi, wananchi watakuwa tayari kutoa kodi. Kwa hiyo waende wakafanyie kazi. Naomba niwape mfano tu wa Rwanda; Nchi ya Rwanda walikuja na sera ya kuondoa majani kwenye nyumba zao, lakini lengo lao lilikuwa siyo kuweka bati pekee, ilikuwa pia ni kukusanya maji. Kwa hiyo, walisema tunaondoa nyasi watu waezeke kwa mabati, japokuwa hapa kwenye mabati Wizara wameongeza tozo, ili katika mabati yale wakusanye maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa baada ya kupata maji, yale maji yakawa yanatiririka kwenye udongo, yanaharibu ardhi unakuwa mmomonyoko wa udongo, wakatunga tena sheria kwamba hakuna kutiririsha maji, kila mtu lazima hata awe na matuta mawili, matatu ya mboga kwenye nyumba zao. Kwa hiyo hii siyo tu kwamba mna-save vitu vingi, watu watapata vitamins kwenye mbogamboga, watu watapata maji, vile vile watu watapata pesa. Wale wanaouza gator zile watapata biashara, mafundi watapata kazi, kunakuwa na chain pale ya watu kupata ajira na fedha inapatikana. Kwa hiyo sheria ndiyo mzizi wa kila kitu wa kupata pesa na kupata kodi. Kwa hiyo, naomba waangalie, watuletee tuone ni zipi ambazo zitafuatwa ili Watanzania waweze kuona namna gani wataweza kujenga nchi yao kwa mapenzi, siyo kwa shuruti, ili tuweze kupata fedha za kuendeshea nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi, kuna kitu kimoja naomba nishauri, kuna mapendekezo ya kodi kwenye laini za simu kutoka Sh.10 mpaka Sh.200 kwa siku. Maana yake ni kwamba mtu atalipa Sh.6,000 kwa mwezi na kwa mwaka Sh.72,000, lakini tumesema tunataka tuingie kwenye teknolojia. Naomba isubiriwe kwanza, siyo Watanzania wengi wanaomiliki hiki kitu na Mheshimiwa Rais ametoka kuzungumza siku mbili, tatu hizi, kwamba tuangalie tujifunze kwa wenzetu masuala haya ya teknolojia yakoje na sisi twende nayo. Kwa hiyo tukianza kutoza huku tutakimbiza Watanzania wanaoweza kumiliki simu, Watanzania ambao wanaweza wakafanya biashara na uchumi ukakua kwa kutumia simu. Kwa hiyo waliangalie suala hili linaweza likawa zuri, lakini linaweza likaathiri kwa upande mwingine wa ukuaji wa teknolojia ili tuhakikishe kwamba Watanzania na sisi tunakwenda kama nchi zingine zinavyokwenda. Kwa hiyo twende na sisi tukazidi kusonga mbele na kuleta maendeleo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Grace.

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa na mimi nichangie katika Bajeti ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kurudisha Tume ya Mipango ambayo kwa kweli tumekuwa tukiipigania kwamba irudi na iweze kufanya kazi yake sawasawa. Ukiangalia katika mpango wa maendeleo wa tatu wa 2022/2023 ulitengewa trilioni 15.0 ambayo ni sawasawa na asilimia 36 ya Bajeti Kuu, hadi tunafika mwezi Aprili 2023 Serikali ilikuwa imeshatumia trilioni 11.5 ambayo ni asilimia 76.5 ambayo kwa kweli ni asilimia nzuri, ninaipongeza na ndiyo maana nimesema napongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nashukuru kwa kuondoa zile ada za vyuo vya ufundi ambavyo ni DIT, MUST pamoja na ATC. Wananchi wengi walikuwa watoto wetu wanapata shida kule lakini kwa kuondoa hiyo wanafunzi wengi watasoma na tunaendeleza elimu ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Waziri kwa usikivu ameleta katika misingi yake sita, kuna msingi mmoja wapo wa ongezeko la ushiriki wa sekta binafsi kwenye shughuli za uwekezaji. Hiki ndiyo kitu cha msingi ambacho tulikuwa tukikipigania kwamba Serikali peke yake haiwezi kufanya kazi bila kuwa na PPP, hii itasaidia kwenye masuala mengi kuondoa umaskini lakini pia kuleta ajira, kwa kufanya hivyo unakuta kwamba ni nchi nyingi, Serikali siyo Mwajiri Mkuu, Mwajiri Mkuu ni hizi private sector.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta kuna kitu ambacho concept hii haieleweki vizuri, tuna shida kubwa sana ya kutokuielewa kwa nini? Wakati tunakusanya labda kodi tunaagalia vyanzo vya kodi kwa mfano tuna vyanzo 50 vya kodi, tunataka bilioni moja mwaka huu, lakini mwakani tena tuna vyanzo hivyohivyo 50 tunataka bilioni tatu, badala ya kuongeza vyanzo viwe vikubwa ili tuweze kupata kodi nyingi. Kodi nyingi tutaipata tukiwa tumeweza kuweka mazingira wezeshi kwa vijana na watu wengine kuweza kupata mikopo kwa bei rahisi ambayo itawawezesha kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii itasaidi sana. Nazungumzia hivi kwa sababu kodi imekuwa kubwa. Kodi ikiwa kubwa, wananchi wengi wanashindwa kujiajiri, wanashinda kuajiri wenzao. Nitatolea mfano. Kwa mfano, mtu ana biashara yake, ameagiza kontena, labda la shilingi milioni 300 limefika pale bandarini, Afisa wa kutoza ushuru anakuja anamwambia kabisa, badala ya shilingi milioni 300, lipa shilingi milioni 70 nami unipe shilingi milioni 20. Watanzania walio wengi wanajikuta wakiingia huko. Mnaweka mazingira ya watu kutoa rushwa, lakini ukitoza bei ambayo ni reasonable, watu watakwenda kulipa na Serikali itapata fedha nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tujitahidi kuongeza ukubwa wa vyanzo vya mapato ili wananchi wengi waweze kufanya kazi yao na Serikali ipate kodi nzuri. Kwa mfano, unaangalia changamoto iliyotokea Kariakoo, wananchi wengi kupiga kelele, lakini yote hii ni kwa sababu ya kodi kubwa. Mmeona jinsi ambavyo mkitekeleza hivyo wananchi wengi watapata ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tozo zimekuwa kubwa. Mnatoza magari tozo kubwa. Kwa mfano, gari jipya ili lifike hapa, tozo yake ni kubwa sana. Kodi yake ni kubwa sana. Hata lori mnatoza. Kwa nini mnafanya hivyo? Kwa sababu wananchi wanashindwa ku-afford kununua magari mapya, ndiyo maana wanaingiza magari chakavu. Tumeona kabisa magari chakavu yanaingia, na yakiangia yanaharibu mazingira na Serikali vilevile inakosa kodi, kwa sababu magari yale yanakuwa chakavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini wasi-enjoy kuendesha magari mapya? Punguzeni kodi ili wananchi wanunue magari mapya. Kwa mfano, lori. Lori ni uchumi, linaweza likaajiri watu wengi sana; dereva, fundi, utingo na watu wengine ambao wanabeba mizigo. Sasa ukiweka ushuru ukawa mdogo, malori mengi yataingia, wananchi watakuwa wanawaletea kodi kila mwaka na mtapata magari mengi ambayo yatakuwa yanahudumia watu na wananchi wengi watapata ajira. Mkianza kuweka kodi kubwa, tunashindwa kupata hivyo. Kwa hiyo, naomba mpunguze kodi katika vitu hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine, nitazungumzia ongezeko la bei ya mafuta. Bei ya mafuta itakapoongezeka, automatically vitu vyote vinapanda bei, na hii ni shida. Kwa nini inafika hapo? Kwa nini tusiwe na utaratibu mzuri wa kuweza kuangalia vyanzo gani vitatupa fedha? Napendekeza kwa mfano, matumizi badala ya mafuta, tuangalie namna tutavyotumia gesi. Tunayo gesi na tumekuwa na upungufu wa dola hapa ndani. Kwa sababu tuna upungufu wa dola, tuanze kutumia gesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Dangote anatumia gesi. Amekuja kuwekeza kwenye viwanda, lakini magari yake yanatumia gesi. Kwa nini Serikali tusianze na magari ya Serikali, mwendokasi tutumie gesi yetu? Kwanza tuta-save dola, tutatunza mazingira na vilevile ajira zitakuwa nyingi. Tukianzia hapo, na wananchi wataanza kutumia gesi katika magari yao, halafu tutakuwa tume-minimize kutumia dola yetu kwenda nje na tutabaki nayo hapa ndani. Kwa hiyo, badala ya ku-import mafuta kwa kutumia hiyo, tutakuwa tunatumia gesi yetu. Kwa hiyo, namshauri Mheshimiwa Waziri tuangalie suala hili kwa umakini kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hivyo, naomba nichangie pia kuhusu kutengeneza mabilionea. Yaani tutengeneze hata mabilionea kumi ambao ndio watakuja kutuletea mambo mengi katika nchi hii. Hayati Dkt. Magufuli aliweza kuwezesha Kiwanda cha Sukari cha Bakhresa, akatoa eneo, akaiamuru Benki ya Kilimo iweze kum-support, I think ilikuwa shilingi bilioni 100 kama sikosei. Sasa hivi tunaanza kuona sukari siyo shida kubwa vile. Kwa nini tusiende tukatengeneza watu kama hao hata kumi ili waweze kufanya vitu vikubwa kama hivyo vikaweza kusaidia nchi yetu kusonga mbele. Kwa hiyo, nashauri tufanye hivyo. Hii itatusaidia sana kuondoa tatizo la ajira, kuondoa umaskini na vilevile uchumi utakua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la ongezeko la fedha kwenye utoaji wa simu. Tunajua nia siyo mbaya, lakini mnawaonea wananchi wa chini. Kwa sababu unapoweka hiyo ina-cut across kwa mwananchi wa kipato cha chini na kipato cha juu. Sasa wote wanatoa, unapofanya hivyo, wale wananchi kule kijijini unakuta mtu anatumiwa shilingi 5,000; shilingi 10,000, au shilingi 6,000, unapokata, ujue wale wote inawakuta. Kwa nini tusiangalie kitu kingine kitakachowasaidia? Kwa sababu wananchi wetu wanapata shida. Unapoweka shilingi 10,000, unamkata tena, anakuwa hapati fedha inayotakiwa. Kwa hiyo, ina-cut across kwa wote. Nia ni nzuri, lakini tuangalie namna ambavyo inaweza ikafanya kazi vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tozo ya pikipiki, sikatai, pia ni tozo nzuri, lakini mimi nilikuwa nadhani, utaratibu wa kupata kodi lazima uangalie economy, yaani usitumie hela nyingi kuchukua pesa kidogo. Nataka kujua kwa Mheshimiwa Waziri, anapokuja hapa atuambie, tuna pikipiki ngapi ambazo anatarajia kukusanya hizo kodi zake na ana staff wangapi wa kukusanya hizo pesa kutoka kwenye hizo pikipiki? Kwa sababu ni ngumu sana ukiangalia, lakini atakuja atatueleza, ni namna gani atafanya ili aweze kupata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi walio wengi kwa kweli unakuta wana kipato cha chini, wale vijana ndio wanaanza kutafuta maisha. Kwa hiyo, tuangalie namna ambavyo tunapona. Tuna vyanzo vingi vikubwa. Ukiangalia vyanzo ni vingi vikubwa ambavyo tunaweza tukapata fedha nyingi na kuweza kuendesha nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hili suala la kilimo. Nitajikita kwenye kilimo cha parachichi. Kule Iringa tunalima parachichi, Njombe na kwingineko wanalima parachichi. Tunapenda tuimarishe vituo vya tafiti. Kwa mfano, kuna kile kikonyo kinaitwa sayo. Kile kikonyo ni cha muda mrefu, tuangalie namna ya kuhuisha ili mbegu ile iendelee kuwa na ubora. Ikiendelea kuwa na ubora, wananchi wataweza kuzalisha parachichi nyingi zaidi. Kwa hiyo, hiyo imekuwa ni changamoto na tumeona kule kwetu, kile kikonyo kikiendelea kwa ile ile privet ya mwanzo inaleta shida katika uletaji wa mazao. Kwa hiyo, parachichi inapungua jinsi unavyoendelea kama kile kikonyo hakijawa kizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali iweke msamaha wa kodi ya magari ya baridi (cold trucks), zile cold containers. Mkiweka msamaha wa kodi, wananchi wanaweza wakafanikiwa sana, kwa sababu imekuwa ni gharama kubwa, wananchi wanashindwa kuhimili kumudu hayo magari na kusafirisha nje, na soko linataka uhifadhi katika chombo kama kile. Kwa hiyo, mkikitolea msamaha hapo, mtawezesha wananchi wangu wa Mkoa wa Iringa, wale wakulima wa parachichi na wengine katika mikoa mingine waweze kufanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza napenda kukushukuru kwa kupata nafasi hii na pia napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kupata fursa hii ya kuchangia katika Wizara hii ya Elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja ya Kambi ya Upinzani kwa asilimia 100. Ninavyounga mkono, naomba ninukuu maneno ya Hayati Baba wa Taifa katika kitabu chake cha Binadamu na Maendeleo alipokuwa akizungumzia faida ya elimu katika nchi. Naomba ninukuu baadhi ya mistari, anasema:- “Tunatumia fedha nyingi sana zisizolingana na uwezo wetu kuwasomesha watu wachache ili baadaye na wao walete faida kubwa kiasi hicho hicho katika nchi. Tunatumia fedha nyingi kutafuta faida katika akili ya mwanadamu kama vilevile tunavyotumia fedha kununua trekta na kama vilevile ambavyo tukinunua trekta tunatarajia kufanya kazi kubwa zaidi kuliko kazi ya mtu na jembe la mkono”. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunaona elimu ni gharama tujaribu ujinga, walikwishazungumza watu wengi. Elimu ya nchi hii imewekwa rehani. Watanzania walio wengi hawaoni umuhimu wa kupeleka watoto wao katika shule zetu za Serikali kwa sababu ya matokeo ambayo tunayaona sasa hivi. Watoto wengi wamekuwa wakimaliza shule bila hata kujua kusoma na kuandika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Waziri wa Elimu aweze kunisikiliza kwa makini. Hakuna elimu bora bila kujali Walimu. Walimu ndiyo wanaofanya elimu hii ikawa bora zaidi hata kama shule ikiwa haina madawati mengi, haina miundombinu mizuri zaidi lakini Walimu wakawa wameboreshwa vizuri wanaweza wakafanya elimu hii ikawa bora hivyo vingine vinasaidia kuwa bora zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi hii imewatelekeza Walimu. Tumesema tunahitaji Walimu wa Sayansi katika nchi hii lakini tuna vyuo vya ualimu visivyo na maabara. Nitavitaja baadhi muone kama vyuo vya ualimu ambavyo vinafundisha Walimu wa Sayansi havina maabara unategemea nini huko? Kuna Chuo cha Ualimu Vikindu, Chuo cha Ualimu Singa Chini, Chuo cha Ualimu Mpuguso, Chuo cha Ualimu Kitangali na vinginevyo hivi navitaja ni baadhi havina maabara na hakuna vifaa vya maabara. Sasa tunatarajia nini na tunajenga maabara nchi nzima tukitarajia kwamba tutapata Walimu bora ambao watakuja kufundisha watoto wetu lakini kule tunakoandaa Walimu wetu hakuna maabara. Serikali hii inafanya masihara na elimu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Walimu hao hao wa Sayansi waliahidiwa kupewa mikopo, hapa ninavyozungumza Walimu hao wa Sayansi hawajapata fedha za mikopo mpaka dakika hii. Nina ushahidi nitakuletea orodha ya Walimu Mheshimiwa Waziri kama utahitaji, wengi hawajapata mikopo katika sekta hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende kuzungumzia katika suala la mitaala. Naomba ni declare interest mimi ni Mwalimu na pia nilikuwa mkuzaji wa mitaala kabla sijaacha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kabisa tunapozungumzia elimu bora tunahitaji mitaala iliyo bora na mitaala ili iwe bora ina process zake za uandaaji. Zile hatua zikipindishwa ndiyo tunapata matokeo haya sasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunatakiwa tufanye research ili kujua Serikali yetu au nchi yetu inataka Watanzania wawe na elimu ya namna gani ili kuwanufaisha hao Watanzania, ile sera kwanza haipo vizuri. Tulikuwa tuna falsafa ya elimu ya kujitegemea huko nyuma lakini sasa hivi haieleweki na haitafsiriki vizuri kwenye mitaala kwamba tunakwenda na falsafa ipi sasa hivi. Je, bado ni elimu ya kujitegemea mpaka sasa hivi ama tuna nini ambacho kipo?
Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya process nyingine zinarukwa, tunatakiwa tuite wadau ili tukubaliane nao ni yapi ambayo tunatakiwa kuyaweka kwenye mitaala. Mheshimiwa Waziri alikuwa ni Mjumbe wa Bodi katika Taasisi ya Elimu Tanzania anaelewa matatizo yaliyopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingi tulikuwa tukiomba fedha Wizara ya Elimu lakini fedha za kufanyia mambo hayo mengi zinakuwa hakuna, unatarajia upate nini? Unatakiwa ufanye utafiti, uitishe wadau lakini kwa kiasi kikubwa wadau wa nchi nzima unaweza ukaita wadau 60 au 100, hao watasaidia kuweza kujua kwamba nchi hii inahitaji twende katika mrengo upi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika suala hilohilo kuna masuala ya vitabu. Mheshimiwa Waziri amezungumza katika hotuba yake, amezungumzia masuala mengi yanayohusu masuala ya vitabu. Kulikuwa na bodi iliyokuwa inaitwa EMAC ambayo walikuwa wanashughulikia vitabu vyetu, ilivunjwa wakarudisha Taasisi ya Elimu Tanzania iweze kufanya kazi hiyo. Hivi ninavyozungumza hapa shule zetu kule hazina vitabu, Wizara imeandaa masuala ya KKK lakini sijui huo usambazaji TAMISEMI unakwenda vipi. Walimu wanakwenda wanafundisha bila vitabu na vitabu vyenyewe vilivyokuwa vimetolewa kwa masomo mengine vinatofautiana, hii ni changamoto kubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, miaka ya 80 kulikuwa na ushindani baina ya shule za Serikali na shule za watu binafsi. Leo hii mnaleta bei elekezi, hivi hawa wenye shule binafsi wangekuwa hawakuweza kuwekeza hivyo wale watoto wetu waliokuwa wanaachwa wangekwenda wapi?
Mheshimiwa Naibu Spika, badala ya kukaa tukaboresha elimu yetu katika shule zetu za Serikali ndipo sasa tuanze kuona kwamba tunaweka bei elekezi baadaye, kwa nini tunaanza kubana watoto wetu wasiweze kusoma katika hizo shule kwa sababu huku waliachwa katika nafasi ya shule za Serikali?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu shule za Serikali zinawachukua wale ambao ni bora na hawa shule binafsi zinawachukua wale ambao siyo bora ilivyokuwa zamani. Sasa hivi hata wazazi hawaoni umuhimu huo kwa sababu kule shuleni tunakuta hakuna Walimu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe mfano katika Mkoa wangu wa Iringa kuna baadhi ya shule ina Mwalimu mmoja shule nyingine zina Walimu wawili, shule ya sekondari wanatakiwa wafundishwe masomo yote.
Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kimoja Mheshimiwa Waziri lazima mtambue utahini wa mitihani. Shule X ambayo ina Walimu wa masomo yote na shule Y ambayo kwa mfano ina Mwalimu mmoja au wawili lakini mwishoni mwa utahini mnatahini mitihani sawa. Hii siyo sawa hata kidogo!
Mheshimiwa Naibu Spika, tuwaangalie wale ambao wamefundishwa na Mwalimu mmoja somo moja tutahini kwa kile walichofundishwa! Kwa nini mnawafelisha watoto wetu wakati mwingine wakati siyo makosa yao kwa sababu…
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyikiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia katika Bunge hili. Kwa sababu ni mara ya kwanza na mimi kuchangia katika bajeti napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kuweza kuja humu kuwakilisha akina mama wa Mkoa wa Iringa. Napenda pia kushukuru chama changu ambacho pia kimeniwezesha kuwa Mbunge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nichangie kwa kuanza na kitabu cha Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 89, ukatili wa kijinsia. Kumekuwa na matatizo mengi, kumekuwa na ukatili wa kijinsia ambao unafanyika katika nchi yetu na hasa waathirika wa tatizo hilo ni wanawake na watoto. Tumeona wanawake wengi wanafanyiwa ukatili wa kinyama, tumeona watoto wetu wanafanyiwa ukatili wa kinyama, tumeona watoto wanachomwa moto, tumeona watoto wanamwagiwa maji ya moto, tumeona madhara mengi kwa watoto wetu wa nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri ameeleza katika hotuba yake kwamba wataendelea kusimamia sheria, sheria zipo Mheshimiwa. Kama zipo na matukio yanaendelea kuna tatizo kubwa katika nchi hii la usimamizi wa sheria. Nikuombe Waziri unapokuja kuhitimisha hoja zako uweze kutueleza usimamizi huo utakuwaje tofauti na mazoea ya siku za nyuma ambayo yalikuwa yakiendelea ambapo akina mama wengi wananyanyasika, watoto wengi wananyanyasika, watoto wamekosa kabisa wa kuwasemea, tumeona watoto wanafichwa kabisa ndani kwa miaka kadhaa. Inatia uchungu kwa sisi wazazi ukiona matukio yale yanaendelea katika nchi hii ambayo tunasema ina amani na utulivu. Mheshimiwa Waziri tunaomba uweze kulisimamia na kwa sababu ni mwanamke mwenzetu basi uchungu huu najua unao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende katika masuala ya afya kwa ujumla. Tukiangalia bajeti ambayo imetengwa kwa Wizara hii, asilimia ambazo waliomba 100 wao wamepewa asilimia 11, hivi tutatekeleza kweli haya yote? Ndiyo maana wenzangu waliotangulia wanasema wanamuonea huruma Waziri kwa sababu matatizo ni mengi, mahitaji ya afya ni mengi huko kwenye Wilaya na majimbo yetu kuna matatizo lukuki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nikizungumzia katika Wilaya ya Iringa, Jimbo la Kalenga, tumekuwa na shida kubwa ya huduma za afya. Zahanati wananchi wamejenga, ukienda Wasa wamejenga zahanati lakini hakuna madaktari na manesi wananchi wanatoka kule kuja hospitali huku Ipamba ambapo ni mbali. Watu wanatoka Kata ya Magulilwa na kata mbalimbali kwa sababu hakuna hospitali za kuwahudumia na wakifika pale wanapata shida kwa sababu dawa lazima wanunue na dawa ni gharama na wakati mwingine hazipo. Kwa hiyo, kumekuwa na changamoto kubwa sana katika hospitali zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Mheshimiwa Waziri aweze kutupa majibu hizi changamoto zitatatuliwa lini, huu upungufu wa madaktari na wataalam katika maeneo yetu utakwisha lini? Hawa wananchi wameweza kujitolea kujenga majengo lakini mengine yamekaa kama magofu hakuna madaktari wala dawa. Serikali hii mnasema ni sikivu lakini watu wanapotea na tunasema afya ndiyo mtaji wa kwanza kwa jamii yetu. Sasa kama Serikali hii ambayo mnasema ni ya viwanda kwa sasa hivi, je, hivyo viwanda vitaendeshwa na watu wasio na afya bora. Tunahitaji kuwekeza kwenye afya ili tupate Watanzania wenye fikra bunifu za kuweza kuwekeza huko kwenye viwanda. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri uweze kuja na majibu ya masuala hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwa upande wa wazee, huko ndiyo kabisa. Tunashuhudia wazee wetu wakipata shida hospitalini. Hii Sera ya Wazee kupata huduma ya afya bure haitekelezeki, hawapati dawa. Wazee wanakwenda hospitalini wale wahudumu wetu madaktari na manesi wanatoa maneno ya kashfa kwa wazee wetu, inatia uchungu. Wazee hawa wameifanyia kazi kubwa nchi hii, wameweza kufanya mambo mengi kwa nchi hii lakini sisi hatuwalipi hata fadhila ya kupata dawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta ni rahisi kwa nchi yetu na Serikali hii ya CCM kuitisha mkutano wa wazee Dar es Salaam, lakini mara nyingi haiwezi ikawatimizia ahadi zao. Ni rahisi sana wakawa wamewekwa sehemu wazee wasikilize lakini kutimiza ahadi zao inakuwa ni ngumu. Tukuombe Mheshimiwa Waziri uweze kutuambia hawa wazee matibabu bure yatapatikana lini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwa huduma za afya kwa watu wenye ulemavu. Mara nyingi tupo nao, tukiwa kwenye foleni hospitalini mnawaona hawa watu hawapewi kipaumbele kama inavyotakiwa. Hawa watu wanahitaji kuhudumiwa kwa ukaribu. Mimi nikuombe tu Mheshimiwa Waziri kwenye hitimisho lako hawa watu ikiwezekana wapewe bima ya afya ili waweze kutibiwa kwa bima ya afya. Kwa sababu wanapata shida sana, wengine hata hawajiwezi, hawajui wapate wapi pesa ya matibabu, hawajui wataendaje hospitalini lakini hawahudumiwi! Tunaomba wapate bima ya afya kwani itawaokoa wao kuweza kutibiwa na kuweza kuwa kama watu wengine kwa sababu na sisi ni walemavu wa kesho, hakuna ambaye sio mlemavu, ikitokea itakuwa ni bahati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende sasa katika Mfuko wa Bima ya Afya. Mfuko wa Bima ya Afya huko ndio kabisa, ukimgusa mwananchi huko kijijini ukamuelimisha anakuelewa lakini anakuja na swali tukienda hospitalini watu wenye kadi za bima ya afya wanatengwa, hawapati huduma haraka, wananyanyapaliwa sana, hii adha itaisha lini? Unakuta mtu ana bima ya afya lakini akienda pale wanasema tunahudumia kwanza wanaolipa cash wengine mtasubiri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie na WAVIU wale Watu Wanaoishi na Virusi vya UKIMWI …
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante sana.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niweze kumshukuru Mwenyenzi Mungu aliyenijalia afya na pia niwashukuru sana wote waliochangia kuhusu Wizara hii ya Afya kwa sababu bila afya hatuna hiyo Tanzania ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninazungumza kwa huzuni sana kwa sababu bajeti ya Wizara hii kwa kipindi hiki ambacho tumebakiza muda mfupi sana haijatekelezeka kwa asilimia 60; japokuwa tuna Mawaziri ambao kwa kweli wanajitajidi kufanya kazi, lakini hawapati fedha za kutosheleza bajeti yao, na tunaona afya za Watanzania zinazidi kudorora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinga ni bora kuliko tiba, nilikuwa natengemea Mheshimiwa Waziri pia aje na jinsi ambavyo tutazungumzia jinsi ya kuwakinga Watanzania kutokupata maradhi mbalimbali, ukija ukaangalia katika maendeleo ya jamii ambako ndiko wako vijana wetu wafanyakazi ambao wanaweza wakaenda na wakawasaida Watanzania, bajeti yao ni ndogo na huko tunakotoka kwenye Halmashauri hawajaliwi, wako kama wanyonge ukiwakuta kule utawaonea huruma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri vijana wetu kule wananyanyasika hawako vizuri kabisa katika hii sector, ninaona kwa mfano, kuna masuala ya afya ya mazingira ambayo unaweza ukashirikiana na Wizara ya Mazingira, mkaanza kuona ni jinsi gani mnaweza kupunguza masuala ya maabukizi mbalimbali. Kwa mfano, Dar es Salaam asilimia 90 ni vyoo vya shimo, asilimia tisa tu ndiyo ina vyoo vya kuvuta, hizi ni takwimu ambazo zimetolewa na mashirika mbalilmbali waliopita na kufanya tafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa utaona kipindi cha masika jinsi ambavyo mtiririko wa maji taka unavyosambaa katika Jiji lile. Hii inakwenda kuleta maambukizo mbalimbali. Tunaambiwa kwamba Watanzania asilimia kubwa tuna kawaida ya kutonawa baada ya kwenda sehemu za kujisaidia na sehemu mbalimbali na hizi zinasababisha maradhi mbalimbali ambayo tunayapata na magonjwa mbalimbali. Kwa mfano, UTI ambao inafikia mahali sasa umekuwa ni ugonjwa wa kawaida lakini pia unaua. Mheshimiwa Waziri uweze kulitizama hilo na kulifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika makubaliano ya Abuja (Abuja Declaration) makubaliano yalikuwa asilimia 15 ya bajeti mzima inaweza kutatua changamoto za afya, lakini asilimia hii imekuwa haitolewi kwa muda wote wa bajeti. Ukianzia mwaka 2015/2016 zilitengwa shilingi trilioni nne zikaidhinishwa shilingi trilioni 1.5 tu. Ambayo ilikuwa ni asilimia saba hatukuweza kufikia hata hapo. Kwa hiyo, hii inaonesha jinsi ambavyo hatuwezi kutekeleza baadhi ya mipango ambayo tumeipanga ili iweze kutekelezeka kwa Watanzania wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nizungumzie suala hili la kutokupeleka fedha vizuri ambalo linaanzia ngazi ya sera tunavyotunga sera katika Wizara ya Afya tunakwenda katika mikoa, halmashauri mpaka vijijini, jinsi ambavyo mtiririko mzima unavyochanganya. Huu mchanganyiko wa kiutendaji katika Wizara hii unatuletea shida katika utekelezaji na ufuatiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kamati tumependekeza mara zote kwamba ingewezekana Wizara ya Afya kama ilivyo Wizara ya Elimu, kuwe na mtiririko kutoka sera mpaka utendaji wake. Unakuta katika Halmashauri baadhi ya masuala hayatekelezeki tunaambiwa hii iko TAMISEMI, hii iko Wizara ya Afya, basi unakuta ni mchanganyiko na fedha zinakuwa hazifuatiliwi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Waziri aweze kumshauri Rais jinsi juu ya Wizara hii nyeti ambayo itatengeneza Watanzania ambao wenye akili timamu na nzuri, wenye afya bora wa kuweza kuendeleza na kuleta maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Menyekiti, nizungumzie kule kwangu japokuwa kuna baadhi ya mambo ambayo yalitakiwa yazungumzwe kwa TAMISEMI, kwa sababu sikupata nafasi lakini pia kwa sera yakwenda. Kwa mfano, katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa waliomba shilingi milioni 150 waliidhinishiwa shilingi milioni 35 na hawakupata hata shilingi moja, unategemea hawa watafanyaje kazi zao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia OC ilikuwa ni shilingi milioni 25 badala yake wamepelekewa shilingi milioni sita tu. Ukija katika Halmashauri ya Kilolo kwanza Halmashauri ile ina upungufu wa watumishi asilimia 51, waliopo ni asilimia 49 na hao tumepata wenye vyeti fake 13 bado kuna upungufu wa watumishi katika Halmashauri hiyo ya Kilolo.
Kwa hiyo, katika mgawanyo wenu wa watumishi wa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja ya Kambi ya Upinzani.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, napenda kuchangia katika Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, maadili na utamaduni wa Mtanzania; maadili na utamaduni wa Mtanzania yameendelea kuporomoka siku hadi siku kutokana na mambo mengi ikiwemo ukuaji wa teknolojia. Watu walio wengi, hasa vijana, wamekuwa wakikosa maadili mema kwa kuangalia au kuiga mila na tamaduni za nje ya nchi. Baadhi ya watoto wamekosa heshima kwa wakubwa.

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali kutunza mila nzuri na tamaduni zetu kwa kuchukua hatua pale panapotokea ukiukwaji wa mila na desturi, wazazi pia wanapaswa kuangalia maadili ya watoto wao. Elimu kuhusu utunzaji wa mila na desturi itolewe katika jamii. Tunahitaji Tanzania yenye Watanzania walio na maadili mema.

Mheshimiwa Spika, uboreshaji wa viwanja vya michezo; viwanja vingi katika mikoa mbalimbali havikidhi vigezo vya kuwa viwanja vya michezo, hasa vile vinavyomilikiwa na CCM. Katika Mkoa wa Iringa, Uwanja wa Samora Machel umejengwa maghala ndani yake na kusababisha uharibifu pamoja na kuharibu lengo la kuwa na uwanja huo. Napendekeza kuwa Serikali, kupitia Wizara, iwashirikishe Sekta Binafsi ili kuendeleza viwanja hivyo hasa Uwanja wa Samora Machel Mjini Iringa ili kuweza kuinua kiwango cha michezo. Serikali pia ijenge viwanja vipya vya michezo.

Mheshimiwa Spika, Chuo cha Sanaa Bagamoyo; wananchi walio wengi, hasa vijana, wamekuwa wakijishughulisha na sanaa. TASUBA ni chuo kinachotoa mafunzo ya sanaa lakini miundombinu yake haikidhi mahitaji. Katika fedha waliyotengewa Bajeti 2016/2017, milioni 300, wamepata milioni 100 tu, sawa na 5.6%. Nashauri Serikali iweze kuwamalizia kiasi cha fedha kilichobakia kwani chuo hiki ni tegemeo la vijana wengi kupata ujuzi ili wajitegemee kimaisha.

Mheshimiwa Spika, uhuru wa kupata habari; kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasisitiza kuwa wananchi wanao uhuru wa kupata habari, Serikali imezuia wananchi kupata habari za Bunge Live. Naishauri Serikali isiwe na woga wa kukosolewa kwani ni afya kwa Taifa na watajipanga kuweza kutekeleza majukumu yao. Niiombe Serikali iruhusu uhuru wa vyombo vya habari ili wananchi wapate haki yao.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi nichangie katika hotuba hii. Naomba niungane na wenzangu kwa kuwapa pole wafiwa wote wa watoto waliopata ajali Mkoani Arusha, Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema peponi Amina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na maneno ya wanazuoni ambayo yanasema ukitaka Taifa bora, boresha elimu; ukitaka kuboresha elimu boresha walimu na ukitaka Taifa la watu wanaojiheshimu, heshimu walimu. Ninazungumza hivi kwa sababu walimu wetu kwa kweli wamekuwa na kinyongo cha kufanya kazi yao, wengi wamekuwa na malalamiko mengi na wamekuwa hawapati haki zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, walimu zamani walikuwa wakipata posho ya mazingira magumu ya kazi na hasa wale wa vijijini ili yawavutie, lakini sasa hivi hakuna posho hizo. Napenda kusema kwamba mimi pia ni mwalimu, wakati huo tukifundisha kulikuwa na posho, wale walimu wa sayansi walikuwa wana posho ya ziada ya walimu wengine wa masomo ya arts na biashara, maslahi hayo yalikuwa yanatia moyo na mwalimu anafundisha kwa nguvu kubwa sana na wanafunzi walikuwa wakifaulu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile unaona kwamba kada hii ni kada inayofanyakazi kwa saa 24. Mwalimu anaandaa somo, mitihani na anasahihisha, mwalimu anapanga matokeo, muda wote wa siku mwalimu anafanya kazi hizi, lakini Serikali hii imekuwa haiwalipi posho ya kufundishia walimu ambayo ilikuwa ni kilio chao cha siku nyingi na walimu wamekuwa hawapati hizo posho. Tunaomba Serikali iangalie suala hili ili walimu wetu waweze kupata posho ya kujikimu na waweze kufanya kazi vizuri, hasa walimu wanaokaa kwenye mazingira magumu. Tumeona wengine wakifuata mishahara yao wanafunga shule kabisa. Mimi nina shule yenye walimu wawili kutoka mkoani kwangu, wakati wa kufuata mishahara mmoja anabaki, mwenzake anakaa na darasa la kwanza mpaka la saba. Kwa kweli, hii ni kazi kubwa kwa walimu, tuwatizame kwa jicho lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna uhaba wa walimu wa masomo ya sayansi hawapo, tunaomba Waziri alitizame suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie sasa suala la vitabu. Vitabu ndiyo moyo wa mwalimu katika kufundisha, tuna mitaala, vitabu na vilevile tuna masuala mengine ambayo yapo katika ufundishaji. Mwalimu akikosa kitabu, akipata kitabu ambacho kinamwongoza mwanafunzi vibaya Taifa zima litakwenda kwenye fikra hizo na tutatengeneza Watanzania wenye fikra ambazo zimepotoshwa. Vitabu hivi kama tulivyokwisha kuviona na wenzetu wamevionesha hapa asubuhi vimekuwa na mapungufu mengi, hivi Serikali inataka tuende wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anafahamu, alikuwa kwenye Bodi ya Taasisi ya Elimu na amefanya kazi anajua jinsi ya kuandaa vitabu anafahamu kabisa. Baada ya kumaliza kazi hii inatakiwa watu wa kuhakiki, kuna panels za masomo ambazo zinatakiwa zipitie. Kweli kama panel zile zilipitia na makosa haya yakatokea basi hawa waliofanya kazi hiyo wachukuliwe hatua, kwa sababu hii ni hasara kubwa kwa Taifa letu, Watanzania na watoto wetu wanakwenda kufundishwa vitu ambavyo vitawapoteza na vitawapotosha. Kwa sababu wanasema unapopata elimu ya msingi bora ndiyo itakayokuongoza mpaka kwenye maendeleo ya baadae. Hivyo, ukimkosea mtoto hapa toka kwenye msingi kwa kweli utamfikisha mahali ambapo siyo panakotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala sasa la ufundishaji hasa kwa watoto wa kike na masuala ya mazingira ya watoto wa kike katika elimu. Tumeona kwamba kuna changamoto nyingi…

(Hapa kengele ililia kuashiria muda wa mzungumzaji kuisha)

MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja hotuba ya Kambi ya Upinzani na ile ya Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shule zetu huko vijijini zina matatizo mengi. Hakuna mabweni kwa ajili ya wanafunzi wala walimu wa kutosha. Watoto wa kike wanapangiwa vyumba vya kulala kwa kukosa mabweni, huko wanarubuniwa na kushawishiwa kwa kuwa hukosa pia fedha za kujikimu kwani wazazi wakati mwingine hawawapi kutokana na umaskini walio nao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto wa kike huweza kubakwa na kupata mimba, hivyo ninashauri Serikali ione namna ambavyo mtoto huyu anayepata mimba atakavyoweza kupata elimu baada ya kujifungua. Imekuwa kama adhabu kwa sababu tu ya kuwa ni wa jinsi ya kike kwani kama kijana aliyempa ujauzito huendelea na masomo hata kama sheria ipo hatujaona utekelezaji wake. Tunaomba Wizara ione hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la VETA tunaomba lipewe kipaumbele pamoja na FDCs ili wale watakaopewa kipaumbele kwa sehemu hizo wapate mafunzo na kuweza kujiajiri pindi watakapomaliza na hasa kupunguza wimbi la ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirejee katika Mkoa wa Iringa. Wazazi wameweza kujenga ama kuhamasisha ujenzi wa mabweni kwa ajili ya wasichana hasa shule ya sekondari Lyandembela Ifunda Mkoa wa Iringa na sekondari ya Mseke. Tunaomba Wizara iweze kushirikiana na TAMISEMI kuweza kusaidia katika umaliziaji wa majengo haya pamoja na kugaiwa walimu wa masomo ya sayansi, walimu watakaokuwa walezi wa wanafunzi kwa ajili ya kufundisha unasihi. Mheshimiwa Waziri utakapohitimisha uweze kutueleza mkakati wa kuwa na walimu wa ushauri nasihi mashuleni hasa shule za sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kutoa mchango wangu katika Wizara hii kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, maji ni uhai, bila maji maisha hayawezi kwenda mbele. Naishauri Serikali iongeze tozo ambapo asilimia 70 ielekezwe vijijini na asilimia 30 iwe mijini, kwa kuwa kuna vijijini ndiyo kuna shida sana ya maji. Wanawake wa vijijini wamekuwa wakipata adha kubwa kwa ukosefu wa maji safi na salama. Wanashindwa hata kufanya shughuli za kiuchumi na maisha kuwa duni.

Mheshimiwa Naibu Spika, mamlaka nyingi za maji zinadaiwa bili za umeme kwa kushindwa kulipa na wao pia wanazidai taasisi nyingi za Serikali, hivyo kufanya wananchi wanaolipa bili za maji kukosa maji. Naishauri Serikali iweze kulipa madeni ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Iringa yenye Majimbo mawili ya Kalenga na Isimani imekuwa na shida kubwa sana ya maji safi na salama wakati kuna vyanzo mbalimbali vya maji kama vile Mto Mtitu, Ruaha pamoja na chanzo kinachoitwa Ibofwe. Maombi mbalimbali ya fedha yametolewa, lakini utekelezaji wake haupo na inakatisha tamaa sana kwa wananchi ambao ni wapiga kura.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri Serikali iweze kutoa fedha ili maji yapatikane katika majimbo haya. Kuna maji ardhini ambapo pia, Serikali inaweza kuwekeza kwa kuchimba visima na maji yapatikane. Kwa hiyo, fedha ziwe zinatolewa kwenda kwenye Wizara hii ili waweze kufanya kazi ya kufumbua tatizo la maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri Serikali pia, ihimize uvunaji wa maji kwa kushauri kila anayejenga nyumba yenye bati kibali kitolewe tu kama ataweka na mfumo wa uvunaji maji, uchimbaji wa mabwawa na malambo hasa wakati wa masika ili kuvuna maji yatakayowasaidia wananchi; ni jambo la kutiliwa mkazo kwa Wizara hii. Naitaka Serikali/Mheshimiwa Waziri atakapohitimisha aniambie utekelezaji wa haya niliyoeleza ukoje?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa Sheria ya Fedha za Umma ya mwaka 2001 (The Public Finance Act, 2001 No.4) inaitaka Serikali kuleta Bungeni bajeti ya nyongeza kwa ajili ya kupata idhini ya Bunge ikiwa fedha za awali hazikutosha. Kwa sasa kuna baadhi ya miradi ya maendeleo inatekelezwa nje ya bajeti na hatujaona Serikali ikiomba bajeti ya nyongeza, mfano, ujenzi wa mabweni ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ujenzi wa barabara za juu Dar es Salaam, ni baadhi tu. Kitendo cha Serikali kuamua kufanya matumizi bila kupata idhini ya Bunge ni uvunjaji wa Katiba na sheria na kitendo hicho kinaweza kuruhusu mianya ya rushwa na ubadhirifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mikopo ya elimu ya juu, katika mwaka wa fedha 2016/2017 wanafunzi waliopata mikopo walikuwa 20,183 na wanafunzi takribani 27,053 walikosa mikopo. Mheshimiwa Rais katika kampeni za mwaka 2015 alisema yeye atakuwa muarobaini wa mikopo ya elimu ya juu. Utolewaji wa mikopo umekuwa na ubaguzi na usumbufu mkubwa, ni vyema Serikali katika Mpango wake iweke commitment ya kuandaa mfumo bora wa utoaji mikopo ili kuondokana na tatizo hili. Vilevile kumekuwa na tatizo au hakuna mfumo mzuri wa urejeshaji mikopo kwani sheria iliyopo inawaumiza sana waliopo katika ajira kukatwa asilimia kubwa kulingana na kipato wanachopata na kushindwa kuhimili maisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haionyeshi uwezo katika kuziwezesha sekta binafsi kukua ili ziweze kuipunguzia Serikali mzigo wa walio wengi kukosa ajira. Wafanyabiashara walio wengi wamefunga biashara zao au kupunguza wafanyakazi kutokana na kushindwa kumudu gharama za uendeshaji, kushuka kwa mapato kwa baadhi ya makampuni, mfano, viwanda vya vinywaji, makampuni ya kitalii, nyumba za starehe zikiwemo baa na hoteli. Mfumo huu unaangamiza kabisa sekta binafsi. Sekta binafsi ndiyo inayochangia mapato ya Serikali kupitia kodi inayokusanywa kwa bidhaa na waajiriwa. Vilevile kumekuwa na tabia ya kuwatishia wafanyabiashara kufunga makampuni kiholela, hii inaongeza umaskini kwa Watanzania walio wengi. Hivyo, nashauri Mpango huu uzingatie na uweke kipaumbele katika kuwezesha sekta binafsi kufanya kazi bila bughudha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wa viwanda, kama Tanzania ya viwanda ni uhalisia na siyo ndoto basi suala hili lisingekuwa ni la matamko kwani hivi karibuni Waziri wa TAMISEMI amenukuliwa na vyombo vya habari akieleza kuwa kila mkoa kujenga viwanda 100 ambapo hadi Desemba, 2018 katika Mikoa yote Tanzania Bara inatakiwa kuwa na viwanda 2,600. Kama miaka yote iliyopita imeshindikana kufufua tu viwanda vilivyokuwepo hii leo ya mwaka mmoja itawezekana? Kwa Mkoa wangu wa Iringa tu kulikuwa na viwanda vifuatavyo:-

1. Kiwanda cha Vifaa vya Nyumbani kama masufuria kiliitwa IMAC;

2. Kiwanda cha Nyuzi na Nguo (COTEX);

3. TANCUT Almasi;

4. Kiwanda cha Magurudumu ya Magari (VACULUG);

5. Kiwanda cha Tumbaku;

6. Kiwanda cha Coca cola; na

7. SIDO

Mheshimiwa Mwenyekiti, vyote hivyo havipo tena. Maelekezo hayo ya viwanda 100 yanashangaza kwa sababu kama mikopo kwa sekta binafsi imepungua na kama Serikali haifanyi biashara hivyo viwanda vitajengwa na nani? Serikali inabidi ijipambanue ili kujua mfumo upi inaufuata kama ni uchumi wa kijamaa au uchumi wa kibepari au soko huria ili ijikite madhubuti katika mfumo itakaoamua kuufuata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo ndicho kinachotoa ajira kwa Watanzania zaidi ya asilimia 70. Katika Mpango huu bado sekta hii inaendelea kupuuzwa na matokeo yake ni kudorora kwa uchumi na hiyo Tanzania ya viwanda inaendelea kuwa ndoto. Kuna changamoto kwenye kilimo kwani wakulima hawapati pembejeo kwa wakati, kilimo cha umwagiliaji hakitiliwi mkazo, Maafisa Ugani hawako wa kutosha, baadhi ya mabenki kutokopesha wakulima kwa madai kwamba mikopo katika sekta ya kilimo huwa haina uhakika wa kurudi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mpango huu Serikali inatakiwa kubuni utaratibu maalum wa kuziwezesha benki za biashara kuweza kutoa mikopo hiyo. Wanawake na vijana wakiwezeshwa hasa katika mikopo ya kilimo na ufugaji ukosefu wa ajira utapungua.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima walipata ari ya kujihusisha katika kilimo hususan kilimo cha mahindi na alizeti katika Mkoa wa Iringa japo gharama za pembejeo ni ghali na wakafanikiwa kupata mazao hayo kwa wingi. Kitu cha kushangaza ni kutolewa kwa maagizo toka Serikalini ya zuio au uuzaji mazao yao hasa mahindi nje ya nchi na kuathiri wakulima hao kujipatia kipato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali iweze kuruhusu wakulima hao kufanya biashara hiyo ya kutafuta namna ya kuwafanya wakulima hawa waweze kuendelea na kilimo kwani zuio hilo limeshusha bei ya mahindi hadi kufikia sh.6000 kwa debe moja gharama ambayo haitoshelezi hata ununuzi wa mfuko mmoja wa mbolea kwa gunia moja la mahindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Iringa wanashughulika pia na kilimo cha nyanya na mbogamboga. Changamoto kubwa katika kilimo hiki ni ukosefu wa elimu hasa kwa wakulima kuhusu kilimo cha kisasa. Hii husababisha uzalishaji mdogo usio bora kwa zao hilo. Aidha, changamoto ya pembejeo na magonjwa ya nyanya, Serikali itoe elimu ya kilimo cha mazao haya na iyape kipaumbele. Itengwe bajeti ya kutosha kuwezesha shughuli za tafiti kwa ajili ya namna ya kutibu magonjwa ya nyanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Benki ya Maendeleo ya Kilimo. Wakulima walio wengi wanashindwa kukuza kilimo kwa kukosa mitaji. Benki ya Kilimo, (TADB) iliomba shilingi bilioni 800 lakini hadi Desemba, 2017 walikuwa na mtaji wa bilioni 66.7 tu. Hivi ukijiuliza watawafikia wananchi wangapi kwa fedha hiyo tu? Naishauri Serikali iweke msisitizo katika upelekaji wa fedha katika benki hiyo kwani itawafikia wakulima walio wengi na kusaidia kupunguza umaskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo cha umwagiliaji. Serikali iweze kutoa kipaumbele katika kilimo cha umwagiliaji kwani ndio utatuzi hasa pale ambapo kunakuwa na uhaba wa mvua. Ni asilimia ndogo sana inatumika kwa kilimo hiki, Serikali ikiweza kujenga mabwawa ya kutosha kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ya Kamati.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachangia katika suala la kazi na wafanyakazi hasa Watendaji wa Vijiji ambao wameondolewa kazini kwa sababu ya kiwango chao cha elimu, yaani darasa la saba. Wafanyakazi hawa wamelitumikia Taifa letu wakati likiwa kwenye uhaba mkubwa wa watumishi na wengine walishindwa kujiendeleza kwa sababu ya mazingira halisi ya maslahi yao. Kuwaondoa bila hata kupata marupurupu siyo haki kwao. Nashauri Serikali itazame upya suala hili, kwani linaleta chuki kwa Serikali yao, kama hawatarudishwa kazini, basi wapewe stahiki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la viwanda. Viwanda 3,000 ambavyo inasemekana vipo, ni vema vikaainishwa ili Watanzania waweze kutambua vipi ni viwanda vikubwa, vya kati na viwanda vidogo. Vilevile tujulishwe viko wapi kwa ajili ya utambuzi. Nashauri pia Serikali iweke mazingira tulivu ya uwekezaji ili kupata wawekezaji wengi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niongelee kuhusu suala la walemavu. Pamoja na kwamba hatua mbalimbali zimekuwa zikifanywa kuwawekea mazingira mazuri watu wenye ulemavu, bado kuna tatizo la tengeo la fedha hasa kwa ajili ya vifaa tiba vya albino (mafuta) pamoja na huduma za afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali ifanye utafiti wa kina ili kubaini watu wenye ulemavu wasio na uwezo wa kujitibu wapatiwe matibabu bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa ushauri kwa Serikali kwamba suala la kuhamisha Walimu wa Shule za Sekondari kwenda Shule za Msingi liangaliwe kwa jicho la kipekee, kwani kuna changamoto katika utekelezaji wake. Walimu hao wapewe fedha za uhamisho, wapatiwe mafunzo ya kufundisha elimu ya msingi (child psychology), saikolojia ya mtoto ili wakafundishe kwa ufanisi. Vinginevyo, badala ya kujenga, tutabomoa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia katika masuala yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sekta ya Michezo, imekuwa ikikumbwa na changamoto ya gharama kubwa ya vifaa vya michezo inayotokana na kodi inayotozwa hasa vifaa vinavyotolewa kama msaada kwa mfano kulikuwa na nyasi bandia ambazo hadi sasa sijui suala hilo limefikia wapi kwani zilizuiliwa bandarini. Waziri atupe majibu ya suala hilo. Kuna uvamizi na kubadilishwa kwa matumizi ya viwanja vya michezo. Serikali itupe majibu na pia kuna uvamizi wa maeneo yaliyotengwa kwa burudani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, michezo ni biashara, hivyo ni lazima tufanye uwekezaji kama biashara yoyote inavyotakiwa ifanyike. Uwekezaji lazima uanzie katika ngazi ya chini kwa kutayarisha watoto wetu kuwa wachezaji wazuri kwa michezo mbalimbali au sanaa na utamaduni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shughuli za michezo na utamaduni katika halmashauri zinakuwa chini ya Idara ya Elimu msingi ambayo ina majukumu mengi ya kushughulikia elimu na sehemu kubwa ya bajeti yake matumizi ya kawaida inatoka Serikali Kuu. Kitengo cha michezo kinamezwa na shughuli za elimu, hivyo kushindwa kutimiza wajibu na majukumu yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri zile asilimia 10 za wanawake na vijana ziwekezwe kwa kuwapa mafunzo vijana na wanawake katika vyuo mfano, TASUBA ili wapate ujuzi na wawekeze katika sanaa. Halmashauri zinaweza kusomesha hata vijana wawili kila mwaka. Hii ni sawa na
kuwapa ndoano badala ya kuwapa samaki. Tusiwape fedha tu, mafunzo ni muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la Kilimanjaro Marathon. Michezo hii ilianza kufanyika Mkoa wa Kilimanjaro lakini pia Mkoa wa Mwanza wameanzisha marathon. Mapendekezo au ushauri wangu ni kuwa; Serikali iangalie namna watakavyogawa mikoa na shughuli mbalimbali na tofauti ili iweze kuwa tulivu. Mfano, Mikoa ya Kusini wanaweza kuwa na mashindano ya vifaa vya majini kama vile mashua na boti na mikoa mingine itafutiwe michezo kulingana na mazingira yake kama vile mashindano ya magari na kadhalika hii itasaidia wananchi kujua na kutilia maanani sehemu ambayo mchezo anaoutamani na mahali atakapokwenda kufanyia ushindani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia bajeti hii ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii ya uhai kuweza kuwa mahali hapa kufanya kazi hii ambayo ni kwa ajili ya wananchi. Nitajielekeza moja kwa moja katika kuchangia bajeti hii. Namheshimu sana Mheshimiwa Waziri wa Afya pamoja na Naibu wake lakini katika majibu ya mwezi Mei mwaka 2017 kuna hoja ambazo tulikuwa tukiuliza kuhusu afya ya mama na mtoto na jinsi ambavyo wanaweza wakakinga akinamama kutopata vifo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika majibu haya tuliambiwa kwamba, Wizara na Serikali kwa ujumla imejipanga kuhakikisha kwamba wanapunguza katika vizazi hai 100,000 watafikia wanawake 292 angalau watakaokuwa katika hilo. Hata hivyo, sasa hivi mmeona wanawake katika vizazi hai 100,000 wanaopatwa na vifo ni 556, imepanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hiyo naomba majibu Mheshimiwa Waziri atuambie ni mkakati gani ambao wanaenda kufanya akinamama hawa wasiweze kupoteza maisha yao wakati wa uzazi. Tunaomba mkakati madhubuti wa Serikali ambao utakwenda kupunguza ama kumaliza tatizo hili la akinamama pamoja na kazi kubwa ambayo inafanyika ya kupeleka vifaa na kadhalika nini kilichopo hapo kinachopelekea ongezeko hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ni bajeti kutotoka kwa wakati. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, kama alivyokwishasema mwenzangu tunatenga bajeti, lakini utekelezaji wake unakuwa ni mdogo sana. Waziri atuambie nini kinafanya hivyo, tumekwenda katika ziara katika Mkoa wa Iringa, tumekwenda Mkoa wa Mbeya, tumeona wenyewe, inafika mahali mnaona aibu kama Wabunge, mnakwenda kukagua miradi ambayo pesa hatukupeleka. Tunawaweka katika mazingira gani hawa Watendaji ambao tunasema tunakuja kukagua pesa ambazo zilitumwa, tuliidhinisha mwaka wa fedha huu wa 2017/2018 halafu mnakwenda pale hakuna hata shilingi moja iliyokwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekwenda Chuo cha Rungemba cha Maendeleo ya Jamii, hakuna fedha iliyokwenda. Tumekwenda Chuo cha Uyole Maendeleo ya Jamii, hakuna fedha iliyokwenda. Tumekwenda katika Hospitali ya Rufaa ya Mbeya ambayo inahudumia mikoa saba lakini hakuna fedha iliyotengwa iliyokwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli wale Wakurugenzi wanafanya kazi kubwa sana. Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mbeya ameweza hata kuajiri wafanyakazi kwa kutumia own source, kazi ambayo ilikuwa ifanywe na Serikali hii lakini amekwenda kufanya hiyo kazi. Tunampongeza kwa sababu wananchi waliweza kupata huduma. Tunaitaka Serikali ipeleke pesa wananchi waweze kupata huduma kama tunavyopitisha bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya mwaka 2017/2018 iliongezeka kwa asilimia 35 kutoka bajeti ya 2016/2017, lakini bajeti hii ambayo tunaijadili sasa imepungua kwa asilimia
20. Hii maana yake nini? Ni kwamba tunakwenda kuwahangaisha wananchi tena kule, hawatapata madawa, hawatapata huduma bora inayotakiwa, vifaa tiba na kadhalika, hii inakwenda hadi kwenye Mkoa wangu wa Iringa, ukiangalia Mkoa wa Iringa Wilaya ya Kilolo ambako…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninatoa masikitiko makubwa sana kwa ukosefu wa maji katika majimbo ya pembezoni ya Mkoa wa Iringa. Wananchi wanapata adha kubwa sana. Katika kitabu cha Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 271 namba 63, 65 na 66 jinsi ambavyo Wizara na watendaji wake wamefanya kazi ya ku–copy and paste kwani wameonesha visima hivyo vipo katika Mkoa wa Iringa wakati visima hivyo vipo Mkoa wa Njombe na si Iringa.

Mheshimiwa Naibu Spika, haya makosa yanasababisha adha kubwa kwa wananchi wa Mkoa wa Iringa hasa Wilaya ya Iringa, Jimbo la Kalenga na Isimani ambapo kuna changamoto kubwa sana ya maji. Kuna shida kubwa ya fedha kwa ajili ya ujenzi wa mabwawa ya umwagliaji ya vijiji vya Ibumila na Mgama ambavyo vipo kata ya Mgama.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kalenga kumekuwa na uchakavu wa miundombinu ya maji yote, hivyo tunaiomba Serikali itoe pesa wananchi wapate maji. Vivyo hivyo kata za Kihorogota na Kisinga vilivyopo Jimbo la Ismani vipatiwe maji.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata fursa ya kuchangia katika Wizara hii ya Kilimo ambayo ni muhimu kwa zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja, kwanza kabisa ni bahati mbaya sana sekta hii ya kilimo imekuwa haipewi kipaumbele. Asilimia zaidi ya 80 ya Watanzania ni wakulima na napenda niseme katika taarifa ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha wakati akiwasilisha ukomo wa bajeti alisema kwamba katika bajeti ya mwaka 2018/2019 bajeti hii imetoa kipaumbele katika mambo yafuatayo, nitayasema machache. Alisema kwanza kulipa deni la Serikali; pili, kugharamia ujenzi wa miundombinu pamoja na reli na viwanja vya ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeweka kipaumbele katika vitu na si watu na ndiyo maana watu wanajiuliza, hivi mnavyosema uchumi umekua, umekua wapi? Mifukoni mwa watu hawana pesa, wakulima wanalima hawapati masoko ya mazao yao. Hawa wakulima sijui itakuwaje, mtawajibu nini mwaka 2020 kwa sababu mmewatelekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi katika Mkoa wangu wa Iringa wananchi wanalima mahindiambayo ndiyo zao lao la chakula na ndiyo zao lao kuu la biashara pamoja na mazao mengine yakiwemo alizeti, ngano, karanga, viazi na vitu vingine. Haya mahindi yalikuwa yanauzwa mpaka shilingi 80,000 kwa gunia mpaka shilingi 100,000 mwaka jana. Sasa hivi gunia la mahindi ni shilingi 25,000, debe moja ni shilingi 5,000 mpaka shilingi 4,000. Huyu mkulima amenunua mbolea kwa gharama kubwa sana mwishoni anakuja kuuza gunia la mahindi kwa bei ambayo hata nusu ya mfuko wa mbolea haifikii, hii haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukijigamba hapa tunakwenda kununua ndege ili wananchi wapande, wananchi wangapi wanaopanda ndege? Katika Mkoa wangu wa Iringa ukitaka kuhesabu wanaopanda ndege asilimia zaidi ya 90 hawapandi ndege. Tunaomba mkae mliangalie suala hili ili wananchi hawa waweze kupata fedha kwa kuwapatia masoko ambayo yatakuwa yanawasaidia wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende katika suala la mbolea. Mbolea zimekuwa haziji kwa wakati, sisi kule kilimo chetu msimu wetu unaanza Novemba amabo ndiyo mvua za kupandia zinaanza lakini inapofika Februari au Machi ndiyo mbolea zinakuja, hii mbolea itamsaidia nani? Tumewatupa watu wetu na hatuwapi mambo yanayostahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijawa Mbunge nilikuwa nasikia masuala haya ya kulalamikia bajeti ya Wizara ya Kilimo, ya kulalamikia jinsi ambavyo mawakala wanapata shida. Nimekuja nipo Bungeni mwaka 2015 hivyo hivyo, mwaka 2016/2017 hivyohivyo, naingia hii mwaka 2017/2018 bado suala la kulalamikia bajeti ndogo ya Wizara ya Kilimo iko vilevile. Tunaenda wapi na nchi hii? Tunakwenda wapi na Watanzania wanakwenda wapi? Mmesema tunataka tuwe na nchi ya viwanda, viwanda hivi vitapata malighafi kutoka wapi? Wakulima wamekata tamaa kabisa, hawana matumaini na Serikali yao... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kupata nafasi hii ya kuchangia katika Wizara hii. Kwanza kabisa niweze kutoa pole kwa Mheshimiwa Heche kupotelewa na ndugu yake, Mungu ailaze roho ya Marehemu mahala pema peponi, Amina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naenda moja kwa moja katika kuchangia na naomba nianze na maneno yafuatayo ya aliyekuwa Rais wa Marekani Abraham Lincoln ambaye alishawahi kusema naomba ninukuu; “The philosophy of the school room in one generation will be the philosophy of the government in the next.” Ana maana kwamba falsafa ya elimu inayotolewa darasani kwenye kizazi cha leo ndiyo itakayokuwa hatma ya Serikali ya kesho. Tunaona jinsi ambavyo elimu yetu inakwenda ICU. Elimu yetu haiko katika muafaka kabisa, watoto wengi wanamaliza wakiwa hawana ujuzi, maarifa na ubunifu mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona katika ripoti ya Kamati jinsi ambavyo shule binafsi zinaongoza kuanzia mwaka 2016. Mwaka 2016/2017 shule 10 bora zote za kitaifa zilikuwa za private na watoto bora wote wa kitaifa walikuwa wanatoka shule za private na ukiangalia kidato cha pili hivyo hivyo. Hii maana yake nini, maana yake kwamba kama kungekuwa hakuna shule zisizo za kiserikali division one, two na three zingekuwa hazipo kabisa. Sasa tufanye nini? Mimi naumia sana ninavyosikia kwamba mnazuia kukaririsha katika shule za private. Shule za private wanakaririsha kwa sababu wanataka wapate vijana wenye ujuzi, wenye maarifa, wasiende kama taburarasa, waende wakiwa wanaelewa nini wanachokifanya kwa kila kidato, kuanzia darasa la nne, saba, form one, two mpaka form four, sisi tunataka walingane, ama mnataka kutekeleza ule usemi wa Mheshimiwa Rais aliyosema kwamba matajiri wanataka waishi kama maskini. Kwa sababu wanapeleka watoto kule ili waweze kujikwamua katika elimu ninyi mnataka walingane wote tupate ma-zero, hili halikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende katika suala la Bodi ya Walimu ambayo itakuwa ni independent board. Naomba hili lifanyike, Mheshimiwa Waziri unapokuja utuambie ni lini Bodi hii itaanza, kwa sababu itawianisha na kupima shule za private zinakaguliwa na kupewa masharti lukuki, lakini shule za Serikali hakuna masharti yoyote yanayotolewa. Iwe haina choo, iwe ina choo ni kuendelea, hii haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakwenda sasa katika suala la walimu. Walimu wamekata tamaa, asilimia 37.8 ya walimu ndio wenye hamasa ya kufundisha, lakini asilimia 60 ndio hawana hamasa kabisa ya kufundisha. Ina maana hawa walimu kama mlivyosema kauli zile zinazotolewa mara kwa mara kwamba asiyetaka kazi aache.

Sasa walimu wameacha kazi wamebaki na utumishi. Mheshimiwa Waziri walimu wameacha kazi, wako na utumishi. Wamekata tamaa kwa sababu hawana motisha kama ambavyo wanapewa shule za private, walimu hawa unakuta anafanya bora liende, shule hakuna discipline, mwalimu anaenda anasoma anaweza akawa anafundisha au asifundishe, haya yanatokea Mheshimiwa Waziri. Kwa hiyo, tukuombe Mheshimiwa uliangalie kwa jicho la ndani kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la lugha ya kufundishia; kiingereza na kiswahili. Wamezungumza wenzangu hapa lugha za kufundishia ni jambo muhimu sana katika elimu. Usipokuwa na lugha ambayo umeamua ifundishiwe tunakuwa na mchanganyiko. Tumeona katika shule za private wanafundisha kwa Kingereza. Wanaaanzia darasa la tatu kiingereza wanakwenda nacho na shule za government ni Kiswahili lakini darasa la nne wanakutana na mtihani wa pamoja, sijui kusudi na maudhui yake mnataka wapate nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakienda kufika darasa la saba wanamaliza, wakienda sekondari hawa waliotoka shule za government wamesoma Kiswahili, wanaenda kukutana na lugha ya Kiingereza wanapata taabu, matokeo yake unakuta wanaanza kuibia. Kwa hiyo, kunakuwa na kazi kubwa sana watoto wanaibia wanasema wanapiga chabo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa toka form one mpaka form four, anakwenda form five mpaka form six anapiga chabo; unatarajia huyu mwanafunzi akija kupata kazi atapiga chabo wapi sasa wakati anafanya kazi? Kwa hiyo, hii ni changamoto Mheshimiwa Waziri uangalie kama

hakuna lugha maalum ya kufundishia muone jinsi mtakavyofanya. Mimi ni mwalimu by profession, lugha ya kiingereza unakuta zile phonetics watoto wadogo wanasoma kwa sauti, unajua sauti ndiyo inaingia na inakaa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia suala la uhifadhi na uendelevu wa mazingira. Dhana hii ni pana na inajumuisha vitu vyote vinavyotuzunguka katika sekta mbalimbali kama vile maji, kilimo, nishati na kadhalika. Bado sekta hii ya utuzaji wa mazingira na uhifadhi haijapewa umuhimu na uzito unaostahili, kwani utekelezaji wake unakumbana na changamoto kadha wa kadha hasa upatikanaji wa rasilimali fedha zinazoendana na Ofisi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Iringa hasa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa kwa sehemu kubwa ni kame kwa sababu ya matumizi mabaya ya mbolea ya chumvichumvi bila kufuata ushauri wa wataalam pamoja na kukata miti hovyo. Nashauri Wizara itenge fedha kwa ajili ya kutoa elimu kwa umma kupitia luninga, redio vipeperushi na wadau hususan Serikali za Vijiji na Vitongoji pamoja na sekta binafsi kueleza madhara ya uharibifu huo wa mazingira, ikiwemo Operesheni Kata Mti Panda Mti itengewe fedha pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mifuko ya plastiki. Waziri Mkuu alivyokuwa akihitimisha hoja ya Wizara yake, alipiga marufuku matumizi ya mifuko ya plastiki kuanzia miezi miwili ijayo. Hata hivyo, nitaomba Mheshimiwa Waziri wa Mazingira anavyohitimisha hoja yake aje na mbinu mbadala kuhusu vifungashio vitakavyotumika katika nchi yetu na namna watakavyoweza kuzibiti mifuko itokayo nje ya nchi yetu. Vilevile ashirikiane na wahusika wa viwanda vilivyokuwa vikitengeza mifuko hiyo ili kuona namna watakavyoshirikiana nao kufanya kazi mbadala kwa sababu ughafla wa taarifa hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kampeni ya upandaji miti. Katika Mkoa wa Iringa kuna ustawi wa miti, matunda na mboga mboga. Nashauri Serikali iweze kutenga fedha ili kusaidia kampeni ya upandaji miti ya matunda ambayo pamoja na kuhifadhi mazingira itasaidia wananchi kupata kipato na kuboresha afya zao. Kwa mfano, wananchi wakipatiwa miti ya miparachichi na apple (matufaa) itakuza sana pato kwa wananchi na kuhifadhi mazingira.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa pongezi kwa Mheshimiwa Waziri wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI pamoja na watendaji wenzake kwa kazi kubwa wanayofanya katika Wizara hii. Hata hivyo, napenda kushauri yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ugatuaji wa madaraka D by D halitekelezwi inavyopaswa kati ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Wizara hii, ningependa kufahamu ni wapi wanapokutana kuweka masuala ya elimu sawa? Hizo hati idhini walizonazo zinawakutanisha kwenye masuala gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano suala la Walimu wa Shule za Sekondari kuhamishiwa katika Shule za Msingi ni mambo gani wamejadiliana na Wizara ya Elimu, hususan, suala la mafunzo (Induction Course) kwa Walimu hawa? Nani atatoa mafunzo ya Child Centered Psychology ambayo ni kipaumbele kwa Walimu hawa kwa kuwa, tunafahamu kwamba, Wizara ya Elimu ndio mtoaji wa mafunzo? Je, Wizara imeshawaandalia fedha zao za uhamisho au posho ya usumbufu? Mheshimiwa Waziri anapohitimisha atuambie ni nini watakachokitekeleza kwa Walimu hawa hasa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la upungufu wa Walimu shule za msingi na Walimu wa sayansi kwa shule za sekondari. Tatizo hili ni kubwa, katika Mkoa wa Iringa hadi 2017 kulikuwa na upungufu wa Walimu shule za msingi 785, kwa Walimu wa sekondari sayansi mahitaji yalikuwa 1,290, waliopo 619, upungufu Walimu 671. Tatizo hili ni kubwa, hivyo nashauri Wizara iajiri Walimu wa kutosha na wapelekwe hasa shule zilizopo vijijini na wapewe motisha ya mazingira magumu ya ufundishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya afya; kuna tatizo ama upungufu wa watumishi katika sekta hii, hasa kwa Mkoa wa Iringa katika zahanati na vituo vya afya, Wilaya ya Kilolo na Iringa Vijijini hasa. Naiomba Serikali iajiri watumishi hawa na kupelekwa huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wakala wa Barabara, TARURA. Hiki ni chombo muhimu sana, lakini kina changamoto ya uhaba wa fedha. 30% wanayopata ya fedha ni kidogo sana kukamilisha miradi. Naungana na maoni ya Kamati kuongeza hadi angalau 50% ya fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba barabara inayounganisha Wilaya toka Iringa Manispaa kupitia Jimbo la Kalenga, Kata ya Luhota na Magulilwa kwenda Wilaya ya Kilolo ambazo ni kilometa chache tu zitengewe bajeti na kujengwa kwa kiwango cha lami kwani kuna wafanyabisahara na wakulima wa mazao mbalimbali kama vile matunda, mahindi, njegere. Miti ambayo inazalisha mbao hupata tabu kupita katika barabara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na maoni ya Kamati kuhusu suala la kuwasilisha Bungeni Muswada wa kusudio la kutunga sheria itakayosaidia kusimamiwa utengaji, utoaji na urejeshaji wa fedha zinazotokana na 10% ya mapato ili kuwezesha wanawake na vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile suala la kuondoa kodi au kupunguza kodi kwa taulo za kike ili kuwezesha watoto wa kike hasa kutoka katika familia maskini kumudu gharama hizo na kuweza kuhudhuria masomo kikamilifu na ikiwezekana wapewe bure kama ilivyo katika nchi za Kenya, Shelisheli na nyinginezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la utawala bora. Kumekuwa na kawaida katika Awamu hii kutoongeza mishahara kwa wafanyakazi wakati maisha kila siku yanapanda kwa gharama za bidhaa. Wafanyakazi wengi hawana raha kwa kutokuweza kukidhi mahitaji na kushindwa kufanya kazi kwa ufanisi. Serikali iweze kupandisha au kuongeza mishahara kwa wafanyakazi wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ukiukwaji wa sheria na taratibu. Mfano Mkurugenzi kutotii mamlaka ya Waziri mwenye dhamana mfano Mkurugenzi wa Tunduma Mkoa wa Songwe, Mkuu wa Wilaya na wengineo wateule wa Rais kutofuata taratibu. Hii ni kinyume kabisa na utawala bora tunaotarajia, Serikali ilifanyie kazi suala hili ili wananchi wapate haki yao ya kupata maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia hoja hii kwa kuanza na Mahakama. Mahakama nyingi zimechoka hapa nchini hasa Mahakama zilizoko vijijini, hazina vyoo, vitendea kazi, samani na vinginevyo. Hata Mahakimu wakitoa hukumu, upatikanaji wa hati unakuwa mgumu kwa kuwa ni vigumu kupata hati au hukumu ya kesi iliyochapishwa kwa kukosa vifaa. Nashauri Serikali izingatie hilo hasa katika mkoa wangu wa Iringa kwa zile Mahakama za ngazi ya chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyumba za Mahakimu ni chache, hii inahatarisha usalama wao, kwani wengi wao wanaishi uraiani, mitaani na wamepata usumbufu. Serikali ihakikishe inajenga nyumba za Mahakimu. Mahakama nyingi hazina mahabusu na kunapotokea wahusika kupelekwa Mahakamani inakuwa ni gharama pia kwa kuwa hawana sehemu ya kuhifadhi mahabusu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mishahara ya Mahakimu na posho kama vile posho ya nyumba lakini waendesha mashtaka wanapewa posho, hivyo na Mahakimu wapewe pia posho. Mfumo wa mashtaka ni mbovu, wananchi wengi wanaonewa sana, haki haitendeki. Nashauri mfumo huu ufumuliwe na uundwe upya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia uchunguzi unachukua muda mrefu sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kupata nafasi ya kuchangia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kumpongeza Mwenyekiti wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Mheshimiwa Freeman Aikaeli Mbowe kwa kazi kubwa yenye changamoto anayoifanya na sisi tuko nyuma yake tutaendelea kufanya kazi naye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanzia katika sehemu ya lishe, nazungumzia suala la udumavu. Tanzania ni nchi ya tatu Afrika inayoongoza kwa udumavu na ni nchi ya kumi duniani inayoongoza kwa udumavu wa kiakili na kimwili na vilevile zaidi ya asilimia 42 ya watoto wenye umri chini ya miaka mitano wana udumavu wa kiakili na kimwili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini ninazungumzia hili? Ninazungumzia hili kwa sababu tunataka tujenge Taifa lenye watu ambao hawana udumavu, tunataka tujenge Taifa ambalo watu wake watakuwa na maamuzi sahihi, tunataka tujenge Taifa ambalo tutaendeleza kizazi na kizazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahatma Gandhi alisema; “Ishi kama utakufa kesho na fikiri kama utaishi milele.” Hii ina maana gani? Tunayoyatenga hapa katika bajeti yetu, tunayoyapitisha katika bajeti yetu, basi yaende yakafanye kazi kubwa ya kuweza kuendeleza vizazi na vizazi na siyo ya kuangalia miaka mitano mitano, tuangalie nini mwisho wa kizazi cha Tanzania hii? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, udumavu huu ninaozungumza unaendana na changamoto nyingi za kukosa elimu hasa kwa hawa watu walioko vijijini na hata wa mijini. Utaona hata sisi wenyewe Waheshimiwa Wabunge tupo tunavyoenda kula pale canteen tunakosa kujua ni vipi tule vitakavyokuwa na uimara katika miili yetu na katika afya zetu. Sasa je, wale walioko vijijini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia bajeti inayotengwa, kwa mfano, Sekta ya Maendeleo ya Jamii ambao ndio wanaotakiwa kuelimisha watu katika maeneo ya vijijini, hawaajiriwi. Wanatakiwa waajiriwe Maafisa Maendeleo ya Jamii 4,000 sasa hivi wako 1,700, tuna upungufu wa takribani Maafisa Maendeleo ya Jamii asilimia 57.5. Sasa hii kuonesha kwamba tutaendelea kuwa na kizazi chenye matatizo ya udumavu. Mikoa mingi ambayo ina udumavu wa kimwili na kiakili ni watu ambao pia wana vyakula, ni mikoa ambayo inazalisha chakula, lakini wanakosa upangaji mzuri wa vyakula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maziwa yamekuwa ni anasa katika familia zetu, mayai ni anasa katika familia zetu, mtu anaweza akawa na maziwa hanywi maziwa. Wenzetu nchi ya Kenya wanapanga kabisa mtu yeyote lazima anywe lita kadhaa kwa wiki. Sisi Serikali yetu mmejipangaje kuhakikisha hawa wananchi wanapata hiyo elimu? (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli itakuwa ni vigumu sana kwa Serikali yetu hii kufikia malengo tunayohitaji ya milenia yale tunayosema kama hatuwekezi mkakati mzuri wa kutokomeza hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakwenda katika suala lingine, kuna ahadi ya Waziri wa TAMISEMI ambayo aliitoa mwezi Juni, 2018 wakati wa matokeo ya Kidato cha Tano yalivyokuwa yanatoka. Alisema atapeleka shilingi bilioni 29 kujenga madarasa 478 na mabweni 269 kwa watoto waliofaulu kwa Kidato cha Tano. Napenda kujua, wamefikia wapi katika utekelezaji? Tuambiwe tujue wamefikia wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya mabweni mnaiona, watoto wa kike, walemavu na wengine wote, mnawaona. Nimekwenda kwenye shule moja unakuta walemavu wanapata changamoto, hakuna uzio kwenye hizo shule, kwa sababu kuna elimu jumuishi. Wale watoto kuna wengine ni Albino, wanataka kuibiwa, Serikali mnajipangaje kuhakikisha hiyo elimu jumuishi, hawa watoto wanasoma na wenzao, hawawezi kuibiwa? Hilo ninaomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kufanya majumuisho ni vizuri wakatuambia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ni taulo za kike. Mwaka 2018 Mheshimiwa Waziri wa Fedha hapa alitutamkia na tukafurahi kwamba wanafunzi wa kike taulo zitaondolewa VAT. Imekuwa ni changamoto, hatujauona mkakati mzuri unawekwa watu wakajua ni zipi ambazo mmeamua zipi salama, zipi siyo salama na wapi na kiasi gani? Hakuna utaratibu unaojilikana. Kama inashindikana, basi tupelekwe kwenye capitation grants ili tujue kwamba kule watapata shuleni, maana hilo ndiyo lilikuwa lengo kubwa la TWPG na wote ambao tulikuwa tunashiriki katika hilo. Tunaomba ufafanuzi wa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni hili la vitambulisho vya ujasiriamali. Napenda kuuliza, hivi mlifanya utafiti kwamba hawa wajasiriamali shida yao kubwa ni vitambulisho? Mlifanya utafiti kweli! Kwa sababu akina mama na vijana wanaofanya biashara ndogo ndogo, amebeba ungo ameweka maembe, ameweka mchicha na kila kitu, anatakiwa atozwe hicho kitambulisho atoe shilingi 20,000/=. Sasa mnasema hivi, mliahidi shilingi milioni 50 kila kijiji. Hizo shilingi milioni 50 ziko wapi? Hamjapeleka, leo mnakuja na vitambulisho. Huyu mama anaishia kukimbia. Anavyofanya vile, anataka ajikimu kimaisha, akauze mchicha ili akalishe watoto, akauze mchicha ili aweze kusomesha watoto. Ninyi mnakwenda kuwadai hao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kupata kauli ya Serikali, mlifanya utafiti? Utafiti ulisema wapate vitambulisho? Kama siyo, utekelezaji huo, ni kweli? Kama ni kweli unafanyika hivyo, ndivyo mlivyodhamiria kuwakomboa hao wananchi wanyonge kama mnavyojinasibu? Hao wananchi wanyonge kweli watakomboka hapo? Maana tunakwenda tunaona wanazidi kudidimia kwa umasikini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana nasema udumavu ni tatizo, tukiwa watatu Afrika ni shida, tunapaswa tufikiri zaidi, tuone kwamba ni biashara gani, ni mambo gani ya muhimu ambayo tunatakiwa tuyafanye kuleta maslahi mapana ya Serikali, lakini siyo kwenda kukamata hawa wajasiriamali wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uwekezaji. Mnazungumzia uwekezaji lakini changamoto kubwa ya uwekezaji katika nchi hii, mazingira ni magumu mno na ni mabovu mno na yanasababisha watu kushindwa kufanya biashara na kuwekeza katika nchi. Kumekuwa na kauli za viongozi za kukatisha tama. Wawekezaji wengine wanaonekana ni kama wanakuja kuchukua mali na kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri lazima aangalie hili. Wawekezaji ndio watakaosaidia Sekta ya Ajira ipatikane. Kama mtawawekea mlolongo mkubwa wa kodi, mtawawekea mazingira magumu ya kuweza kufanya kazi zao… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, napenda kuchangia hoja hii katika vipengele vifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, sanaa, michezo na utamaduni kama kichocheo cha fursa za kiuchumi na umoja na upendo kwa Taifa letu. Takwimu za ukuaji wa kiuchumi katika nchi yetu zinaonesha kwamba sekta hii inachangia zaidi ya asilimia kumi na moja ya pato la Taifa. Hii inaashiria kuwa tukiwekeza zaidi tunaweza kukuza na kuongeza zaidi pato la Taifa letu. Hivyo nashauri Wizara ya Fedha iongeze ukomo wa bajeti kwa Wizara hii ili iwekeze zaidi kwa sekta za sanaa, utamaduni na michezo, kwani bajeti katika Wizara hii ni ndogo sana. Tuwekeze kwenye vyuo vya michezo pia TASUBA na masuala ya utamaduni.

Mheshimiwa Spika, uhuru na haki ya kupata habari nchini; Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizoridhia na kusaini azimio la kimataifa la uwazi katika uendeshaji wa Serikali. Kupata habari wananchi ndio utawala bora. Imekuwa ni kawaida sasa wananchi hawaoni Bunge live kwa kuwa wanataka kuona wawakilishi wao wanapeleka hoja zao kwa Serikali. Hivi ni kinyume kabisa na haki ya kupata habari na masharti yaliyoridhiwa.

Mheshimiwa Spika, upungufu wa bajeti ya maendeleo; bajeti ya maendeleo haitoki kama inavyoombwa na kumekuwa na changamoto nyingi katika W izara hii na miradi ya sekta hii katika uwanja wa Taifa, wadhamini mbalimbali wamekuwa wakihudumia uwanjahuo wakiwemo Wachina ambao mkataba wao unaishia mwezi Agosti, 2018 na sportpesa mkataba wao mwisho mwezi Mei, 2018. Hata hivyo, hakuna mkakati wowote unaoonesha viwanja hivi vitashughulikiwa kwa kuwa hata bajeti haijajionesha wazi. Waziri anapohitimisha atueleze mkakati ukoje wa kuhakikisha uwanja huu umetunzwa ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, nazidi kusisitiza kuwa na maandalizi mazuri ya michezo kuanzia under 17 kwa jinsia zote, kuwe na mkakati wa mafunzo maalum na maandalizi kwa timu zetu. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, napenda kuchangia hoja hii katika suala la uvunjwaji wa Sheria ya Vyama vya Siasa katika utundikaji au upeperushaji wa bendera za vyama kwenye Ofisi na mabango mbalimbali. Hivi karibuni katika Mkoa wa Iringa umetokea mtindo anakuja kiongozi wa nchi bendera za CHADEMA zinaondolewa zote na kutundikwa bendera za CCM. Hii haikubaliki tuko katika mfumo wa vyama vingi ni vyema Jeshi la Polisi likalinda mali za jamii na watu wake. Bendera ziliondolewa Mafinga na Iringa Mjini.

Mheshimiwa Spika, askari wanahitaji kuongezewa mishahara na pia kupata posho za mazingira magumu ya kazi yao. Mara nyingi wanakosa karatasi, printer na mafuta ya kuendesha programu mbalimbali. Nashauri waongezewe fungu ili wafanye kazi kwa ufanisi.

Mheshimiwa Spika, Jeshi la Magereza wamekuwa hawana mavazi/sare kwa kugharamiwa na Serikali, wananunua kwa fedha zao wenyewe kinyume na taratibu. Serikali ifanyie kazi suala hili ili wapewe sare za kazi.

Mheshimiwa Spika, suala la maadamano na mikutano ya hadahara limekuwa ni changamoto kufanyika hasa kwa vyama vya upinzani. Nashauri Jeshi la Polisi lifuate sheria na Katiba inayotaka kuwapo kwa maandamo pamoja na mikutano ya hadhara na mikutano/vikao vya ndani. Jukumu la Jeshi la Polisi ni kulinda amani katika mikutano/vikao na maandamano.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na mlundikano wa mahabusu. Nashuri kuanzishwe Kitengo Maalum cha Usuluhishi Polisi ambacho kitasuluhisha migongano ya waliofika kituoni ili kuwajengea umoja wananchi na kuwaweka karibu na Polisi kama sehemu ya kimbilio.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, napenda kuchangia hoja hii katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, mgawo wa bajeti ya maendeleo kwa Wizara ya Ujenzi mwaka 2016/2017 ulikuwa shilingi trilioni 4.8, mwaka 2017/2018 shilingi trilioni 4.9, mwaka 2018/2019 shilingi trilioni 4.1 ambayo ni 34.5% ya bajeti yote ya maendeleo. Mpaka mwaka huu wa fedha unaisha Bunge litakuwa limeidhinisha jumla ya shilingi trilioni 13.8 kwa miaka mitatu.

Mheshimiwa Spika, napenda kujua ni sekta zipi nyingine za uchumi zimechochewa kutokana na uwekezaji huu kama viwanda, ni vingapi vimeanzishwa? Watanzania wangapi wameondokana na umasikini? Pato la Taifa limeongezeka kwa kiasi gani kutokana na uwekezaji huu?

Mheshimiwa Spika, sekta ya ujenzi. Kumekuwa na changamoto kwa wakandarasi Watanzania kutopata kazi za kufanya ndani hata nje ya nchi. Serikali ina mkakati gani wa kufanya wakandarasi hawa waweze kupata angalau asilimia 50 ya kazi za ndani ya nchi na hata za nje ya nchi?

Mheshimiwa Spika, TBA wanapewa kandarasi za Serikali na mara nyingi hawashindanishwi. Hii imefanya kazi zao kuwa chini ya kiwango na malalamiko yamekuwa mengi, Serikali ifanyie kazi suala hili.

Mheshimiwa Spika, barabara nyingi zimekuwa hazikamiliki kwa sababu fedha nyingi zinaenda kwenye upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ambao unachukua muda mrefu sana. Wananchi wanaathirika kwa kutosafirisha mazao yao kwa wakati na uchumi kusuasua.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, kuna ahadi za Mheshimiwa Rais kutekeleza ujenzi wa barabara za Mkoa wa Iringa, nikitaja chache barabara ya Rujewa – Madibira, Iringa Mjini – Hifadhi ya Taifa ya Ruaha (kilometa 14) na Ipogolo - Kilolo (kilometa 133). Barabara zote hizi fedha za ujenzi bado hazijafika, kinachofanyika ni usanifu tu. Pamoja na utengaji huu wa fedha mnaouainisha, naitaka Serikali hii itekeleze ahadi hizi mapema ili wananchi wasipate adha.

Mheshimiwa Spika, bado nasisitiza uendeshaji wa Shirika la Ndege la ATCL ni wa hasara. Serikali iangalie suala hili kwa makini kwani kodi za wananchi zinazidi kuteketea.

Mheshimiwa Spika, mradi wa SGR vifaa vinavyotumika vinatoka nje ya nchi. Nashauri Serikali itumie malighafi kutoka hapa nchini. Kwa mfano, makaa ya mawe ambayo yapo Mchuchuma yangetumika katika mradi huu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Ahsante sana, kwa kunipa nafasi na niweze kuchangia katika hoja iliyoko mbele yetu ya Wizara ya Elimu. Kwanza kabisa namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii leo pia naunga mkono asilimia mia hotuba ya Kambi ya Upinzani yote ambayo yamo mule, ninaunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie katika masuala matatu nikianzia na suala la kwanza, la kupungua kwa bajeti ya Wizara hii ya Elimu. Awamu ya Nne ya Serikali yetu ilikuwa ikienda kila mwaka ikipandisha bajeti ya Elimu, lakini toka tumeingia Awamu hii ya Tano, tunaona kuna mserereko wa kupungua kwa bajeti ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukianzia mwaka 2016/2017 na chanzo cha takwimu hizi ni haki elimu, wanasema toka mwaka 2016/2017 imepungua bajeti kutoka trilioni 4.770 hadi kufikia trilioni 4.706 kwa mwaka 2017/2018. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona pia kwa mwaka 2018/2019 pia imepungua mpaka kufikia trilioni 4.628. Pamoja na hayo, tukiangalia uwiano mkubwa wa bajeti ya Serikali pia, tunaona kwamba imepungua kutoka asilimia 16.1 mwaka 2016/2017 mpaka 2018/2019 asilimia 14. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inapingana kabisa na azimio ambalo tumeridhia sisi la nchi za kusini mwa jangwa la sahara kwamba tufikie asilimia 20. Sasa tunavyopunguza bajeti ya Wizara ya Elimu, athari zake ni kubwa mno, mnaona Waheshimiwa Wabunge karibu wengi wanazungumza hapa wakilalamika jinsi ambavyo Wizara hii imekuwa haipati fedha kwa ajili ya kutatua changamoto zilizoko huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miundombinu iliyoko katika shule zetu, vyuo vyetu, ina mashaka makubwa mwaka huu kumekuwa na ongezeko la asilimia 17 ya wanafunzi wanaoingia shule za msingi, tofauti na miundombinu ambayo tunakwenda kwa asilimia moja. Sasa ukiona, miundombinu vis-a-vis hao wanaoingia mashuleni unakuta kwamba kuna wanafunzi wameingia kidato cha kwanza mwezi wa tatu, kuna wengine wameingia mwezi wa nne. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalalamika nini hapa kwamba hawa watoto wanatoka hawajui kusoma na kuandika wakati wameingia mwezi wa tatu mwezi wa nne na mtaala unataka waanze mwezi Januari.

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti,

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Nimekataa taarifa kwa sababu hazinisaidii sana, kwa muda wangu.

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Yah (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kumpa taarifa kwamba.

MWENYEKITI: Hapana nimekataa. (Kicheko)

Endelea!

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hii tunavyozungumzia ni changamoto kubwa ambayo ipo katika jamii yetu, kwa Wizara hii kupunguza hiyo bajeti ya Wizara ya Elimu. Kuna upungufu wa vifaa maabara nyingi ambazo wananchi wamejenga, na Serikali haijamalizia kuna upungufu wa kemikali zinazotakiwa kwenye maabara zetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tunapunguza bajeti ya Wizara ya Elimu, tuna uhaba pia wa vifaa vya ufundishaji, na kufundishia, unakuta kwamba kuna walimu wengi wanalalamika kuna somo linaitwa stadi za kazi, mwalimu amepewa kitabu chake cha kiongozi, anaambiwa chukua msumeno na ubao onyesha wanafunzi waanze kukata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu mwalimu ambaye mshahara hamumuongezi? Huyu mwalimu ambaye madaraja yake hayapandi, hana pesa, lakini anatakiwa awe na vifaa darasani, wanafunzi wamezuiwa wasichukue vifaa majumbani wanasema tumesema elimu bure. Sasa mwalimu anafundishaje huyu? Hivi vifaa vinatakiwa kwa ajili ya mwanafunzi kupata ujuzi wa vitendo katika kazi zake. Zamani sisi tunavyosoma tulikuwa tunaambiwa katika masomo ya sayansi kimu mwingine aje na mafuta, mwingine aje na mchele, mwingine aje na sijui na chumvi, mwingine aje na kile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanafunzi mnakaa darasani mwalimu anawafundisha kupika, mnapika, sasa hivi walimu wanashindwa kufanya hivyo? Capitation grands ambazo tulitaka zienda mashuleni zile 10,000 kwa shule za msingi na 25,000 kwa shule za sekondari kwanza haziendi, pili ziko chini hazitoshelezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwanza napendekeza Mheshimiwa Waziri, hizo capitation grands ziende mashuleni kama zinavyohitajika kuna shule nyingi sana, ambazo hawapati, na hawapati wengine kwa wakati, lakini pia ni ndogo kama tulivyosema kwa dola, sasa dola inapanda, na sisi tumebakia na kiasi kile kile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba ipandishwe kwa primary school iwe angalau shilingi 20,000/= na kwa shule za sekondari iwe shilingi 50,000/=. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende katika suala la utekelezaji wenye mashaka sana wa bajeti katika fedha zetu za maendeleo kwa Wizara hii ya Elimu. Unakuta katika bajeti ya elimu, fedha za maendeleo zilizotengwa karibia nusu, shilingi bilioni 857 zilizotengwa katika maendeleo, shilingi bilioni 427 ndizo zinakwenda katika Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu. Hizi fedha ni nyingi, zinakwenda kule lakini tunakuta Wizara hii inabakia na pesa kidogo ambayo ndiyo tunasema Wizara imepata pesa nyingi. Hii Wizara haipati pesa nyingi kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Waziri wa Fedha awaongezee fedha Wizara ya Elimu kwa sababu kile kiasi kinachobaki ni kidogo. Miradi ya maendeleo karibu 40 haijapata fedha. Nikianzia huu mradi huu wa Kitengo cha Kudhibiti Ubora. Mwaka 2017/2018 walitengewa shilingi bilioni moja mwaka 2018/2019 walitegewa shilingi bilioni 1.5 lakini miaka yote hii hawakupata fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge mnajua, hiki ni kitengo muhimu sana ambacho kinakagua jinsi ambavyo wanafunzi wetu au vijana wetu na walimu wetu wanatakiwa wafanye kazi, lakini hawatengewi fedha za kutosha; na tunajinasibu kwamba tunakusanya fedha nyingi, lakini fedha hazijaenda, hawa hawafanyi kazi ya ukaguzi, hawa watu wetu wa udhibiti ubora hawakagui shule zetu, lakini shule binafsi wanatoa pesa wenyewe kwa hawa Wadhibiti Ubora ndiyo maana wanaenda kukaguliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona katika shule kumi bora huwa zinaongoza shule binafsi na shule za Serikali hazipo. Sasa mimi nasema hivi, if you fail to plan, you plan to fail. Wekezeni vya kutosha katika elimu. Namwomba Mheshimiwa Waziri, tuwekeze vya kutosha katika elimu, tuweke foundation ya kutosha katika msingi, twende sekondari ndio tutapata watu wazuri katika vyuo vikuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko vyuo vikuu tunakuta Wahadhiri wanalalamika kwa sababu hatujawekeza vizuri katika sekta hizi chini. Utaona tunazungumzia hapa, lakini tukisema elimu imeshuka Waziri haangalii Waziri wa TAMISEMI, unaangaliwa Waziri wa Elimu. Kwa hiyo, nawaomba mkae pamoja muone jinsi ambavyo mnaweza mkaboresha msingi ili huku juu tuwe na ubora unaotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja klatika suala la Taasisi ya Elimu Tanzania. Tunalalamika kuhusu vitabu hapa, lakini Taasisi ya Elimu Tanzania ilitengewa shilingi bilioni 40. Katika shilingi bilioni 40 miaka miwili mfululizo hawakupata fedha, wamepata mwaka huu shilingi bilioni nne ambayo ni asilimia 10. Sasa asilimia 10 tunalalamika lakini asilimia 10 Mheshimiwa Waziri mnaowapelekea inatosha kufanya kazi zote hizo za kuandaa vitabu, kiongozi cha mwalimu na kufanya kazi zote ambazo zinatakiwa pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara iangalie Taasisi ya Elimu, kama wana shida ya kufanya elimu hii iwe bora. Taasisi ya Elimu iboreshwe lakini naomba mshirikiane na sekta binafsi PPP ili…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia hoja hii katika suala la mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa kwa vijana kwa mwaka 2018/2019 jumla ya vijana 19,895 wa mujibu wa sheria walipatiwa mafunzo kwenye kambi mbalimbali. Aidha vijana 21,966 wamepata mafunzo kwa kujitolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana hawa wakimaliza mafunzo hawapati ajira na huku wamepata mafunzo hata ya kivita. Ningeomba Serikali iweze kuona athari za vijana hawa waliofundishwa kutumia silaha kubaki mitaani bila kazi ya kufanya. Ninashauri Serikali hata kama haiajiri waweke utaratibu au kuanzishwe programu wakishirikiana na VETA ili wawatumie vijana hawa kupata kozi anuai ambazo zitawasaidia kujiajiri na kuweza kukuza uchumi binafsi na wa Taifa, kwa mfano yanaweza kuwepa mashamba na wakapewa mitaji ya kuzalisha malighafi zinazoweza kutumiwa katika viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu nyongeza ya mishahara kwa wanajeshi, ninaiomba Serikali iwape nyongeza za mishahara wanajeshi kama kada nyingine zinavyotakiwa kwani hawajapata nyongeza zao tangu Serikali hii ya Awamu ya Tano imeingia madarakani. Tuwape kipaumbele kwa maslahi yao kwa kuwa kada hii imejitoa kwa gharama ya uhai wao katika kulinda mipaka ya nchi yetu ili iwe salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, napenda kuchangia hoja hii hasa katika suala la miradi ya umeme vijijini REA III hasa kwa Mkoa wa Iringa. Hadi sasa jumla ya wateja 3,541tu kati ya wateja 13,556 ndio wameshaunganishiwa umeme katika vijiji 67 kati ya vijiji 179. Hii spidi ni ndogo na vijiji vingi havijapata umeme huu hasa Jimbo la Kalenga, Kata ya Luhota, Vijiji vya Tagamenda, Wangama, Kitayawa na Kata ya Mgama na Mseke kuna baadhi ya vijiji havina umeme.

Mheshimiwa Spika, nashauri hata vijiji vilivyowekewa umeme ni nyumba chache sana zenye umeme na hata maeneo ya shule, zahanati nazo bado hazijapata umeme. Hivyo Serikali iweze kuweka umeme katika Jimbo na Kata zake zote pamoja na vijiji vilivyopo katika jimbo hilo. Niliuliza swali la msingi na majibu yalikuwa kwamba hii REA III itamaliza matatizo katika jimbo hilo na mkoa kwa ujumla, naomba bajeti hii iziangatie hilo.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. GRACE V. TENDEGA – MWENYEKITI WA KAMATI YA HESABU ZA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote, nakushukuru sana wewe na wote waliochangia hoja hii na Mawaziri wote ambao wamechangia kwa namna moja au nyingine katika kujibu hoja hizi. Nawashukuru sana kwa sababu wameunga mkono hoja zote za Kamati ambazo tumezitoa na ndiyo maana tulizitoa katika maoni yetu na pia nimepokea pongezi zenu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wengi wamejikita kujengea tu hoja zile namna ya kutoa maelekezo, basi nitambue michango ya waliochangia katika Kamati yetu ya LAAC. Kwanza Mheshimiwa Selemani Zedi, Mheshimiwa Twaha Mpembenwe, Mheshimiwa Ali Kasinge, Mheshimiwa Conchesta Rwamlaza, Mheshimiwa Tauhida Gallos Nyimbo, Mheshimiwa Abubakari Asenga, Mheshimiwa Francis Mtinga,

Mheshimiwa Japhet Hasunga, Mheshimiwa Anastazia Wambura; na Mawaziri, Mheshimiwa Dkt. Festo Dugange na Mheshimiwa George Simbachawene, tunawashukuru kwa michango yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yale yote ambayo wameyasema, basi tunaomba yakawe katika utekelezaji kwa sababu tunafanya kazi kwa mujibu wa taarifa ya CAG. Kwa hiyo, tunashukuru sana kwa yale ambayo wameji-commit lakini katika mifumo, lakini kama alivyoeleza Mheshimiwa Naibu Waziri Dkt. Festo Dungage tuwaombe basi Ofisi ya Rais, TAMISEMI mharakishe kuleta mifumo kama huo mfumo wa tausi ili kuweza kudhibiti hizo fedha ambazo zinatumika fedha mbichi. Hii itasaidia Serikali iweze kupata mapato ya kasaidia wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia hii ya kufuata miamala, mmesema mtaangalia ile bureaucracy the way ilivyo kuhakikisha Maafisa Masuhuli wanakuwa responsible, itasaidia sana kwa sababu yeye ndio accounting officer atatusaidia kuweza kuona kwamba fedha zile zinakuwa katika mikono salama.

Mheshimiwa Spika, upungufu wa watumishi na watu wengine kama walivyosema Waheshimiwa wa Bunge katika kuchangia kwao, Serikali iweze kutoa mafunzo kama tulivyosema katika taarifa yetu, itasaidia sana watendaji kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa na kuongeza mapato.

Mheshimiwa Spika, kuhusu 10%, hilo tunaomba Serikali iweze kufanyia kazi kwa umadhubuti kabisa kwa sababu fedha zile zikirudi kuna baadhi ya Halmashauri zitakuwa zimefikia ukomo wa kutenga tena; na zile fedha zitatosha kuwakopesha wananchi wetu wengi zaidi wakaweza kunufaika.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kukushukuru na nishukuru watendaji wote wa meza yako.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika hoja iliyopo mbele yetu ya Taarifa za Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii pamoja na Taarifa ya Ukimwi. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii. Maoni ambayo ametoa Mwenyekiti wetu ndiyo tumeyafanyiakazi na nina hoja zifuatazo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitazungumzia katika sekta ya afya pamoja na elimu. Katika sekta ya afya, ninapozunguma sasa, kwa takwimu za UNICEF tuna watoto chini ya miaka mitano ambao wanafariki kila siku kwa idadi ya watoto 312 kwa siku. Ninapozungumza hapa, watoto 312 kila siku wanafariki. Hii ina maana gani? Tukiona kuna ajali inatokea ya basi kwa mfano lenye abiria 65 na tunasikitika watu hawa wamefariki basi moja, kwa watoto 312 ambayo yanaangusha abiria kila siku. Kwa hiyo watoto hawa wanapoteza uhai, na hii ni kwa sababu ya changamoto kubwa tunazozipata katika utoaji wa huduma na ukosefu wa huduma za afya zikiwemo huduma za dharura za upasuaji kwa wakina mama na mtoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa haya ni masuala ambayo tunapaswa tuyaone na tuyaangalie kwa mapana kwa sababu tunapoteza watoto wengi wakati huo huo sisi tunasema kwamba tuna makusanyo makubwa ya fedha; haya makusanyo makubwa yanakwenda wapi? Hatuna watumishi wa kutosha takribani asilimia zaidi ya 50, hawapo. Sasa kama Serikali hatuna watumishi zaidi ya asilimia 50 kwa Sekta ya afya tunatarajia nini? Hawa Watanzania wengi tunaowapoteza matarajio ni yapi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali lazima ijipime, ijiangalie, wapi ambako wanatakiwa waweke mkazo tumesema tunakusanya fedha nyingi za mafisadi sawa japokuwa mimi sijaona hao mafisadi wameweza kuhukumiwa wapi tukapata hizo pesa, lakini hatujaajiri wafanyakazi ni miaka mwaka wa nne unakwenda wa sekta ya afya hawapo, hii inaleta adha hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakwenda katika sekta hiyo ya afya watumishi wa Sekta ya Maendeleo ya Jamii. Sekta hii ni muhimu, ndiyo kinga. Tunapata semina mbalimbali hapa Wabunge viribatumbo, sijui kuna hiki, kuna kile; yote haya ni kwa sababu sekta hii hajaajiri, tuna upungufu takribani asilimia 95 ya watumishi wa maendeleo ya jamii katika sehemu zetu kwenye kata na vijiji ambao walikuwa wakipita zamani wakielimisha jamii, kuleni kuku, mayai, mboga, samaki, maziwa havipo tena sasa hivi ambao walikuwa wanaelimisha, wanawaelekeza wakina mama na wananchi kwa ujumla wapate hiyo elimu, haipo. Sasa kama hatuwezi kuwekeza kwa watumishi hawa ambao ndio kinga matarajio yetu ndio hii kuongeza bajeti ya dawa ambayo inatu-cost kama Serikali. Kwa hiyo Serikali lazima iangalie, kinga ni bora kuliko tiba; tuwekeze kwenye sekta hii na tupeleke wafanyakazi ili waweze kuhudumia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi za wenzetu unakuta watu wana-volunteer, wanajitolea. Serikali haiamasishi hicho, hamasisheni wananchi wajitolee wakiwa shuleni, wanapotoka shuleni waende wajitolee. Tunaona volunteers wengi wanatoka nje wanakuja hapa sisi wa kwetu tunapelekea wapi? Hatuna huo mkakati, Serikali iweke mkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija katika sekta ya elimu, ninapozungumza ratio ya mwalimu wa elimu ya awali ni mwalimu mmoja kwa wanafunzi 146; inayotakiwa ni mwalimu mmoja kwa wanafunzi 25, na pale ndipo tunapojenga msingi wa elimu, tunapowakuza watoto wetu wakuzwe vipi, wawe na study zipi , wafanye nini, baadae waweje hapa ndio tunapokuza. Lakini sasa tuna uhaba wa walimu 44,273, ni zaidi ya mara nne ya walimu tulionao, miaka 50; miaka 50. Ina maana tutatumia zaidi ya miaka 200 kupata walimu ambao watatosheleza katika nchi yetu, halafu mnasema mtaendelea kuchaguliwa katika awamu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende sasa kwenye suala la wasichana kurudi shuleni wapatapo ujauzito; hiyo ni haki yao ya kielimu. Katika Ilani yenu ya Chama Cha Mapinduzi Kifungu 52 ukurasa 99 kipengele cha elimu (i) roman(ii), naomba ninukuuu, kinasema;

“Wasichana wote wa elimu ya msingi wanaoacha shule kwa sababu ya kupata ujauzito wataendelea na masomo”

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo imenukuliwa, na hii mliipeleka kwenye mpango na ikawa mpango mzima wa utekelezaji; hata tunavyotafuta fedha kwa wafadhili tunatumia kifungu hicho. Niwaulize imetekelezwa wapi? Hawa wanafunzi wengi; mimi siwezi kutetea kwamba mwanafunzi apate ujauzito lakini wale kwa bahati mbaya ambao wanapata ujauzito hakuna mkakati mzima wa kutengenezea utaratibu wa kwenda kwenye masomo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzetu Zambia wameweka utaratibu, huyu mtoto anatokaje shule, atafanyaje, ataendelezwaje mpaka atarudije shule kuwa-formal education; sisi tunataka tumpeleke kwa upeo mwingine aende akatengeneze sijui vitambaa, kufanya hivi. Huyu alikuwa na ndoto zake pengine awe Pilot, awe engineer, awe mtu ambaye ana mtazamo wake alikuwa anautaka sisi….(Makofi)

MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Grace Tendega kuna taarifa Mheshimiwa Ally Keissy.

MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, nampa taarifa mzungumzaji kama alikuwa na ndoto zake kwa nini alipata mimba ungemzuia asipate mimba.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Grace Tendega endelea na mchango wako.

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, siipokei ninasema hivi kama tendo hilo hilo ambalo linafanya watoto wapate ujauzito na tendo hilo hilo linafanya watu wapate UKIMWI mbona kwenye UKIMWI hatusemi chochote na tunapeleka fedha wanahudumiwa? Kwa nini kwa upande huu tunasema haipo? Ama kwa sababu kwenye UKIMWI na wanaume wanakuwemo? Lazima tuliangalie hili na tupigie kelele hawa watoto wa kike wapate elimu, wapate ndoto zao ambazo wanazitarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi za Afrika Mashariki wameweza kuingiza hilo ukiangalia Kenya, ukiangalia Uganda na soko la ajira ni moja. Sisi tunapokuja kuwa hatuna soko la pamoja tunasema tuko nyuma ni kwa sababu hatuweki mkakati madhubuti watoto wa kike kwenda shule na kuendelea na shule zao. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa muda wako umekwisha ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kupata nafasi hii ya kuweza kuchangia mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano ambao ni wa kuanzia mwaka 2021/2022 na 2025/2026. Nianze tu kwa kusema kupanga ni kuchagua, unavyopanga mpango matarajio ni kwamba, mpango ule angalau utatekelezeka kwa asilimia kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepanga katika maelezo ya Mheshimiwa Waziri, wanasema wametenga karibu trilioni 118 za miradi, lakini nikisema niseme jinsi fedha zinavyotolewa katika mipango ambayo imekuwepo toka Mpango wa Kwanza, Mpango wa Pili na sasa tunakwenda Mpango wa Tatu; nichukulie tu mfano sekta ya viwanda, kwa fedha za maendeleo ambazo zilitolewa kwa mwaka 2016/2017 ilikuwa ni asilimia 44; mwaka 2017/2018 ilikuwa asilimia 9.5; na mwaka 2018/2019 ilikuwa asilimia 6.5 tu. Sasa hivi ukijumlisha kwa miaka hiyo unakuta kwamba, utekelezaji wake ulikuwa ni asilimia 20 tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunavyokuwa tunapanga hii mipango wananchi wanakuwa na mategemeo makubwa sana ya kuhakikisha kwamba, mipango tuliyopanga itatupeleka katika uchumi ambao tumesema tunataka kufikia, uchumi wa kati, lakini nashukuru Mheshimiwa Muhongo ameielezea vizuri jinsi ambavyo tunaweza tukafikia katika uchumi huo wa kati kama tukifuata mikakati na jinsi ambavyo tutaishauri Serikali iweze kufikia katika huo uchumi wa kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya viwanda ambayo kwa miaka minne, Awamu ya Nne mwaka 2015 tulifikia kiasi cha dola 1.3 bilioni, lakini kwa Awamu ya Tano tulishuka, mwaka 2018/2019 ilikuwa ni dola milioni 894, mwaka 2019/ 2020 dola 805.2 milioni. Sasa unaangalia thamani ya mauzo ya nje ya viwanda, hii value of exports tumeshuka, sasa kama tumeshuka, je, nini ambacho kinakwamisha tusifike kule? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachotukwamisha ukiangalia masuala mengi hatuna mazingira muafaka ya uwekezaji. Mazingira ya uwekezaji yamekuwa ni ya kusumbua wawekezaji, watu wanafilisiwa, watu wamehamisha biashara Mheshimiwa Musukuma amezungumza, utitiri wa kodi, sasa hivi vyote vinaikosesha Serikali mapato. Kwa hiyo, Serikali lazima iangalie namna ambavyo inaweza ikarekebisha tozo mbalimbali zikawasaidie wawekezaji na uchumi uweze kupanda na tuweze kunyanyua kipato hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hakuna mkakati mahususi kwa vijana wetu. Nasema kwa vijana kwa sababu, unapowekeza kuanzia kwa vijana mpaka watafika mbele watatengeneza uwanda mpana sana wa maendeleo. Sasa private sector haijapewa mkakati mkubwa, tumeiweka pembeni hatuitilii mkazo, vijana hawaandaliwi kuja kuwa wawekezaji. Kwa hiyo, lazima Serikali iwe na mkakati wa kuhakikisha vijana wanaandaliwa kuja kuwa wawekezaji katika nchi hii. Tunasema vijana ni Taifa la leo, wawekewe mikakati mahususi ya kuhakikisha kwamba, watakuwa wawekezaji wazuri katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine lazima tuwezeshe uchumi wa wananchi kuwa na mtaji. Waziri wa Viwanda aliyetangulia, Mheshimiwa Mwijage, alikuwa anatuambia hata ukiwa na vyerehani vitatu au vinne ni kiwanda, hata ukiwa na blender ni kiwanda, lakini lazima tutengeneze uwezo wa kuwawezesha watu kuwa na mitaji. Hii itafanya watu kuwa wanawekeza kwenye viwanda, Watanzania hata watu wa nje wanaweza wakawa na mitaji ya kuweza kuwekeza katika nchi yetu. Sasa Serikali iangalie hawa Mawaziri ambao wanakuja wakitamka maneno ya namna hiyo na kuwafanya Watanzania washangae.

Mheshimiwa Mwenyekiti, enzi za Mwalimu ilikuwa ukitamka kiwanda unajua kuna kiwanda cha TANCUT Almasi, kuna MWATEX, kuna Kiwanda cha Magurudumu, vilikuwa vinaeleweka, lakini leo tunatajiwa kwamba, kuna viwanda elfu nane na kitu ambacho Mheshimiwa Waziri ametamka hapa, lakini ukiangalia vingi viko kwenye makaratasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kKivitendo kwenda ukaviona hivyo viwanda ni changamoto. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri anaporudi kujibu hapa atueleze kinagaubaga uwekezaji huo umewekezwa wapi? Pamoja na kwamba, wametaja baadhi ya viwanda vinne, vitano, ambavyo viko pale kwamba 201 hivyo ni viwanda vikubwa, lakini sijui kuna viwanda elfu nane na kitu ambavyo hivyo havieleweki viko wapi? Naomba ufafanuzi uwepo wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tuangalie jinsi ambavyo tutaoanisha kilimo na viwanda. Kilimo tumekitupa kabisa katika, hatujawekeza. Mwaka, kama sikosei 2018/2019, ni asilimia mbili tu ya fedha za maendeleo ndio ilitolewa kwenye kilimo. Kwa hiyo, nashauri tuwekeze katika kilimo kwa sababu, kilimo ni ajira na vijana wengi na asilimia zaidi ya 67 wanaweza wakapata ajira kupitia kilimo, akinababa, wanawake, vijana, wanaweza wakapata ajira kupitia kilimo. Kwa hiyo, Serikali lazima iangalie katika utoaji wa fedha katika bajeti ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tunafanya mipango, tunaisoma kwenye maandishi, utekelezaji Wizara ya Fedha toeni fedha katika utekelezaji katika sekta hii kwa sababu, fedha hazitoki. Tutaona, tutakwenda tutaangalia katika bajeti, fedha ambayo ilitengwa 2020/2021 utakuja kukuta kwamba, asilimia kubwa kabisa haijatolewa. Kwa hiyo, tuombe Serikali itoe fedha kwenye sekta ya kilimo ili hawa watu waweze kufanya kilimo chenye tija na waweze kutumikia nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi katika miundombinu ya kilimo cha umwagiliaji. Kilimo cha umwagiliaji kitasaidia sana katika kuongeza pato na mpango ukaweza kufanikiwa, lakini sisi hatuna miundombinu inayoridhisha katika kilimo cha umwagiliaji, sisi tunategemea mvua ambayo Mwenyezi Mungu anatupa. Kwa hiyo, tuwekeze katika kilimo cha umwagiliaji kwa nafasi kubwa, ili tuweze kukidhi hayo yanayotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende katika suala la ukuaji wa pato la Taifa. Pato la Taifa wanasema linakua, lakini hali- reflect hali halisi. Wanasema pato limekuwa, lakini hali halisi tunaiona, wamezungumza Waheshimiwa Wabunge wenzangu hapa, ukiangalia Maisha ya Mtanzania, hali ni ngumu, watu wanaweza wakasema kwamba, ooh, sijui kuna kubana matumizi, kuna hiki, kuna kile, lakini hili pato la Taifa ambalo tunasema limekua kiuchumi, tunaomba wachumi wenzetu watueleweshe vizuri, wale wakulima wa kule kijijini wanavyosikia pato limekua hawaelewi kwamba, limekuaje? Maisha yanazidi kuwa magumu, vitu bei zinapanda na masuala mengine kama hayo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo…

MWENYEKITI: Sentensi ya mwisho, malizia.

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hotuba ya Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Nitajikita hasa katika sehemu mbili na kama kuna muda nitaongeza, lakini najikita katika ajira pamoja na elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapozungumzia ajira, ni kwa ajira kwa watu ambao wana ujuzi wa kutosha kufanya majukumu katika ajira hizo. Namaanisha Skilled Labor. Tunapozungumzia uchumi wa kati ambao tumeshaingia; katika hotuba hii nimeangalia sijaona vizuri namna ambavyo tumedadavua vizuri kupata ajira vizuri kwa vijana na wengine, lakini pia ajira yenye ujuzi. Nina maanisha nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapozungumzia ajira, nazungumzia ajira na watu ambao wana ujuzi wa kutosha kufanya majukumu katika ajira hizo, namaanisha skilled labour. Sasa tunapozungumzia uchumi wa kati ambao tumeshaingia uchumi wa kati, katika hotuba hii nimeangalia sijaona vizuri namna ambavyo tumedadavua vizuri kupata ajira vizuri kwa vijana na wengine, lakini pia ajira yenye ujuzi inamaanisha nini? Tumejikita kutoa elimu mpaka kufikia Vyuo Vikuu, kupata degree na na tunavyoandaa hawa watu wakiondoka pale, hawa wanakuwa katika level ya managerial, yaani wanakuwa ni supervisors, lakini katika level ile ambayo ni watendaji kazi ambao wapo hasa katika VETA, hatujajikita sana. Hapa ndipo tutaandaa wale watenda kazi, ambao watasaidia kuinua uchumi wa nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiangalia vyuo vya VETA vilivyopo, siyo mikoa yote ina VETA, lakini kama mikoa yote haina VETA, bado Walimu wanaokwenda kufundisha wanafunzi wetu ni wachache na vyuo vinavyotoa ni vichache. Kwa hiyo hapa sasa ndio Serikali ijikite katika kui- invest huko, kuhakikisha tunapata Walimu wazuri ambao watakwenda kufundisha, yaani hao technicians watakaokwenda kufundisha VETA ili tuweze kupata watu ambao ni skilled. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya nusu ya Wabunge tuko hapa kila mmoja utakuta mtu anakuuliza kuna ajira wapi, vijana wanatuuliza, wanasema nataka ajira, lakini tumeweka ajira kama kitu ambacho watu wamefika university, lakini kumbe mtu akifunzwa vizuri kuhusu nyanja yake kwa mfano tukisema wafanyakazi wa majumbani qualified, wafanyakazi wa saloon qualified, gardeners qualified, tuwapate wapi watu ambao ni qualified katika nyanja tofauti hawa ndio watapata kipato na pia wataweza kuajiriwa kwa sababu wana ujuzi na wanaweza kuongeza pato la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji kutengeneza middle class wengi ili tuweze kupata kodi na Serikali iweze kujiendesha. Sasa Serikali, haijajikita hapo. Tukiangalia katika bajeti ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kitengo Vote 65 ambapo walitengewa bilioni moja mpaka nazungumza hapa haijatoka. Hii inaonesha kwamba bado Serikali haiko serious kuangalia ajira kwa vijana. Kwa hiyo naomba Serikali iweze kuangalia hivyo na Serikali ihamasishe, kuna short courses za mambo hayo. Serikalini hawazungumzi kwamba kuna short courses ya hiki, hiki, hiki. Watu wakifikiri ajira anajua aende akasome, amalize form six, aende mpaka chuo kikuu, lakini hao wanaomaliza darasa la saba kwenda mpaka kidato cha nne tunawapeleke wapi? Tuandae katika bajeti yetu, waende wakafanye kazi waweze kuleta uchumi wa nchi hii, wafanye kazi inayotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wezetu China mwaka 2017 walikuwa na technicians milioni hamsini. Sasa na sisi tukijiwekea malengo angalau wanafunzi hao wanaomaliza darasa la saba mpaka form four tuwa-train katika hizo kada, wote wanaofanya decoration na whatever hivyo tutafika mbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hiyo haitoshi, napenda nikazie pia hawa Walimu ambao wanapata diploma kwenye DTE hao Walimu ni muhimu, wako wachache, unakuta nyumba wamekutengenezea mlango, mlango haupendezi, lakini finishing kama hii wanafundisha pale na ndizo ajira, tunahitaji tupate vitu hivyo vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kimoja nataka tuzungumzie kwa watu wenye ulemavu, watu hawa wamekuwa wakitozwa kodi, niombe Serikali itoe kodi kwenye vifaa ambavyo ni vya watu wenye ulemavu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana.

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kupata fursa ya kuchangia hotuba hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, sekta ya kilimo; hivi mkulima ni nani? Ni vigezo vipi vinafanya umuite mkulima? Je, ile asilimia 76 au 65 ya ajira za wakulima huwa mnaitoa wapi? Je, mnayo orodha ya wakulima wa nchi hii kwa asilimia? Mmewaainisha kila daraja? Tunalenga kuwa na wakulima wangapi?

Mheshimiwa Spika, Serikali ije na majibu hayo, tumeona Mheshimiwa Rais ametoa vifaa kwa Maafisa Ugani, ni jambo jema. Tunaitaka Serikali kupitia maafisa hao watuletee sasa majibu hayo.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu; Serikali ihakikishe wakulima wanapata mafunzo juu ya kilimo bora. Tuwekeze TARI kwenye tafiti ili kupata mbegu mpya na bora, vinginevyo hatutaweza kushindana na wenzetu nchi nyingine. Tuwekeze katika mazao ya kimkakati.

Mheshimiwa Spika, katika hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu ukurasa 26 imeeleza hali ya upatikanaji wa pembejeo za kilimo. Takwimu za Wizara zinaonesha mahitaji ya uzalishaji na usambazaji wa mbolea nchini hadi tarehe 28 Februari, 2022. ni kama ifuatavyo; makadirio ni tani 698,280, jumla ya upatikanaji ni tani 480,848, kilichouzwa ni tani 283,411. Hii inaonesha kuwa pamoja na upatikanaji huo wa mbolea bado wakulima wanashindwa kununua sababu ya gharama hiyo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kupanda bei ya mbolea, Urea mfuko kilo 50 imeongezeka kwa wastani wa shilingi 55,000 hadi 130,000 sawa na ongezeko la asilimia 120; CAN mfuko mmoja shilingi 34,000 hadi 125000 sawa na ongezeko la asilimia 150; DAP sh 60000 had 120000 ongezeko la asilimia 100. Mfumuko huu utasababisha kuingia kwa baa la njaa siku za usoni na uzalishaji utapungua. Nini kifanyike?

Mheshimiwa Spika, Serikali ichukue hatua za haraka ili kunusuru mfumuko huu wa bei, pia Serikali itoe motisha maalum kwa wawekezaji wa viwanda vya mbolea nchini. Aidha, Serikali ipunguze kiwango cha tozo za mrahaba kwenye malighafi za mbolea zinazochimbwa nchini. Serikali itoe ruzuku kwenye mbolea ili kushusha gharama na bei iwe nafuu kwa wakulima na Serikali iweke bei elekezi ya usambazaji hadi mwisho.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara hii ya Maji. Kwanza nianze kwa kusema, bila maji kunakuwa hakuna uhai tena. Nitachangia kwa kuanzia na gharama ya kuunganisha maji. Tunasema tunakwenda kumtua mama ndoo kichwani, lakini gharama za kuunganisha maji zimekuwa ni kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimewasikia Waheshimiwa Wabunge wengine wakizungumza hapa, hii inamfanya mtu anataka kuunganisha maji, anatamani apate maji safi na salama, lakini anashindwa kuunganisha maji yafike nyumbani kwake kwa sababu ya kutotimiza takwa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri aweze kuangalia katika Wizara yake namna ambavyo wanaweza kupunguza gharama kwa kuwafanya hawa wanaotaka huduma ya maji angalau waunganishiwe kwanza iangaliwe jinsi wanavyofidia bili zao ili waweze kupata maji. Kwa maana wengi wanataka maji lakini wanashindwa kwa sababu ya gharama ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, vifaa vya kuunganisha maji ni gharama kubwa sana. Kwa hiyo, mwone mtakavyoona vifaa hivi viweze kuwa na gharama ndogo ili watu wengi waunganishe maji na tupunguze hii adha ya akina mama wengi kukosa maji kwa sababu ya gharama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ni kwamba kumekuwa na mabambikizo ya bili za maji. Wakati mwingine maji yanakuwa hayatoki, lakini unakuta bili inakuja kubwa sasa kuna maeneo mengine ambayo tunaishi unakuta angalau wanatoa taarifa hata message kwamba msoma mita amekuja, amesoma unaweza uka-compare na mita ukaona. Basi hii ienee maeneo mengi ili wananchi wengi waache kulalamika kwa sababu kumekuwa na mabambikizo makubwa ya bili za maji wakati mwingine sivyo zinavyokwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tufanye kama wanavyofanya TANESCO, pia tuwe na prepaid meters. Zile meter zinasaidia. Katika Mkoa wa Iringa zipo kwa baadhi, mijini, lakini tunapenda angalau ziwepo, maana mtu atatumia maji kulingana na anavyohitaji maji na hatakuwa na malalamiko hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, upotevu wa maji. Wamezungumza wenzangu hapa, wakati tunakua sisi wengine umri umekwenda kidogo. Wakati tunakua kulikuwa na watu ambao wanatazama haya maji yanavyotoka na kuangalia bomba linafunguliwaje, wanafunga na kama bomba limetoboka wana-repair, lakini sasa hivi hakuna hicho kitu. Unaweza ukapita mara tano mpaka mara sita wiki nzima maji yanamwangika tu, hakuna anayetoa taarifa, hakuna anayepita kuangalia haya maji. Inaumiza kwa sababu maji yanapotea na tunapoteza fedha nyingi. Kwa hiyo, mwangalie jinsi ambavyo mnaweza mkaweka utaratibu wa maji haya yasipote ovyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hiyo haitoshi, naomba nimshukuru Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, alisema atabeba ajenda ya maji kuhakikisha wanawake na Watanzania tunapata maji safi na salama. Namshukuru pia Mheshimiwa Waziri, kwani katika Mkoa wa Iringa nimeona kuna miradi 34. Nashukuru sana kwa sababu kwa miaka mitano tulikuwa tunapiga kelele maji yamekwenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi natokea Kalenga. Nimekuta kuna miradi ambayo itabeba Kata ambazo tulikuwa tunazipigia kelele. Kuna hii Nyamlenge Construction nimeiona, Isupilo, Tanangozi na nyingine za Isimani na Iringa nzima, tunashukuru hiyo miradi. Tunaomba pesa zinazotengwa, basi na zitoke ziende zikafanye kazi hiyo, maji yapatikane. Tutarudi mwakani tutaulizana hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri akasimamie ili pesa hizi zitoke na maji yakapatikane. Wamezungumza wengine pia, lakini pesa pia zikitoka tuhakikishe wale wanaosimamia maji vijijini, hawana mafunzo yoyote wanayoyapata. Hakuna mafunzo wanayoyapata wale wasimamizi wa maji ndiyo maana unakuta miradi mingi inaanzishwa na inakufa. Kwa mfano, Maafisa Elimu huwa wanakwenda mpaka vijijini, tuache mijini. Mganga wa Wilaya anakwenda kuzungukia wilaya yake. Kwa nini tusiwe na watu wa maji wazungukie hivyo hivyo ili wahakikishe maji yanapatikana kila sehemu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, uangalie utaratibu utakaofaa kuhakikisha hawa wanaoendesha maji huku, vikundi vile vipate kwanza mafunzo ya kuona jinsi ambavyo maji yatatoka vizuri na pia wale wasimamazi waende kule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa ya CAG imezungumzia jinsi ambavyo Wizara hii imepata changamoto kubwa na nivitu gani ambavyo vimesababisha hiyo? Wamesema miradi mingi haikukamilika kwa wakati kwa sababu hiyo, imeongeza gharama ya miradi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Waziri ahakikishe jeshi lake au kundi lake linakamilisha miradi kwa wakati ili tusiingize pesa nyingine zaidi katika miradi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halafu hakuna ubora. Unakuta kuna maeneo wamechimba visima, lakini havitoi maji kwa sababu hakuna chanzo cha kudumu cha maji. Sasa tunajiuliza, hawa ni ma-engineer gani wanaokwenda pale kuchimba kisima tupoteze pesa baada ya mwezi mmoja hakuna maji? Hii haikubaliki, lazima usimamizi madhubuti uwepo kwa Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile, kumekuwa na ucheleweshaji wa fedha kwa wakandarasi. Wanafanya kazi, lakini pesa haitolewe kwa wakati. Ofisi ya Rais, TAMISEMI ikiwa na Wizara ya Maji, mhakikishe mnatoa pesa kwa wakati ili wale wakandarasi waweze kuendeleza shughuli za utoaji na kukarabati miundombinu yote ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, najua muda umekwenda lakini mengine nitaleta kwa mahandishi ili niweze kutoa ushauri. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuweza kuchangia hoja iliyopo mbele yetu ambayo ni ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kusema naomba ninukuu dira na dhima ya Wizara ya Afya. Dira yao inasema hivi; ni kuwa jamii yenye afya bora na ustawi inayochangia kikamilifu katika maendeleo ya mtu mmojammoja, jamii na Taifa. Dhima ya Wizara ya Afya inasema hivi; kutoa huduma endelevu za afya zenye viwango vinavyokubalika kwa wananchi wote bila kikwazo cha fedha kwa kuzingatia uwiano wa kijiografia na usawa wa jinsia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nimesema nitangulize dira na dhima ya Wizara ya Afya? Ni kwa sababu ya mambo ambayo yanaendelea kutendeka katika utoaji wa huduma wa Wizara hii. Nakwenda kwa CHF iliyoboreshwa ambayo ndiyo inayopatikana katika mazingira tunayotoka na wananchi wetu ndio wanayoipata. Sasa CHF iliyoboreshwa iko hivi; wananchi wanatoa ile 30,000, wanaambiwa watakwenda kutibiwa kwenye zahanati, lakini kinachotokea, wakifika pale kwenye zahanati wanaandikiwa tu na Daktari waambiwa dawa nenda katika dirisha lile pale uende ukafuate.

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo imetokea kwenye mazingira yetu, mimi natoka Kalenga mazingira yako hivyo; Isimani hivyo hivyo na maeneo mengine iko hivyo hivyo. Kwa hiyo kunakuwa na uhaba wa dawa, hawapati dawa kwa CHF hiyo iliyoboreshwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hii inasababisha nini; unakuta kwamba mtu anakwenda pale labda ana 10,000 ambaye siyo mtu anayepata ile huduma ya CHF, anahudumiwa na Daktari pia pale, tena hao wanashughulikiwa harakaharaka na akienda pale ananunua dawa kama yule. Sasa watu wameona kwamba hivi huduma ya afya ni bure ama ni ya kulipia hata kama una CHF au NHIF.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kuna hata hii bima ya NHIF ambayo watumishi wapo katika kada hizo, Walimu na watumishi wengine walipo katika sekta hizo vijijini wanalalamika kukosa dawa katika zahanati. Ukikosa unaambiwa uende mjini ukadai, kuna fomu ukajaze ukijaza hiyo fomu ndiyo utakwenda kuchukua dawa. Sasa imagine unatokea Pawaga ama unatoka Magulirwa, umekwenda Kalenga ambayo unafika kwanza mjini halafu unakwenda Kalenga hizo kilometers. Sasa unakwenda kule kwenye zahanati unatibiwa unarudi tena mjini uandikiwe na hao Maafisa Afya ambao wako Gangilonga pale Iringa Mjini; natolea mfano wa Iringa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii inaleta gharama kubwa sana kwa wananchi. Matokeo yake wameona kwamba hii CHF ni kama siyo msaada kabisa, hata NHIF. Kwa hiyo niishauri Wizara kutokuwepo kwa dawa ni changamoto kubwa sana na hii inafanya wananchi wasiiamini Serikali au NHIF kwa sababu hakuna dawa, watu hawatajiandikisha wengi kwenda huko. Ukiangalia unakuta kwamba kuanzia mtoto wa mwaka mmoja, mtoto anayezaliwa mpaka miaka mitano kupata kile kitambulisho cha NHIF ni siku 90. Kwa hiyo unakuta wanaona kwamba kuna changamoto; naomba wabadilishe na waboreshe hicho kwa sababu ni changamoto kubwa ambayo wanaipata wananchi wanaona kwamba hakuna haja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tunataka twende kwenye Bima ya Afya kwa Wote na Waziri amezungumza hapa, tunataka Bima ya Afya kwa Wote. Bahati nzuri sisi wakati huo Bunge lililopita, mimi nilikuwa katika Kamati ya Huduma, tulikwenda Rwanda, wengine walikwenda Ghana na wengine walikwenda mahali pengine, lakini tulikuta wenzetu wamefanikiwa kuwa na bima ya afya kwa wote, waliweka mkakati maalum kwa nchi yao kuhakikisha wananchi wanapata bima ya afya kwa wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona kuna fedha imetengwa pale kwa mchakato, lakini tuliambiwa kwamba ni Bunge lile utakamilika lakini tumekuja hapa naona Waziri tena ameweka mchakato. Watueleze lini wanakamilisha ili tuwe na Bima ya Afya kwa Wote na wananchi wetu waweze kupata huduma ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja katika kipengele cha watumishi wa afya; tuna changamoto kubwa ya watumishi wa afya; sekta ya afya vijijini na mijini nadhani, kuna changamoto kubwa. Unakuta kuna mganga mmoja ndio anayehudumia wananchi wote walioko pale. Uzuri Kamati imetoa takwimu kwamba ni asilimia 53 ya uhaba wa watumishi wa sekta ya afya. Mheshimiwa Waziri atueleze wanaajiri lini ili waweze kukimu hii asilimia 53 ya watumishi wa afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na yote hayo, hawa watumishi wa afya wamekuwa wakipata adha nyingi; wamekuwa hawapandishwi mishahara, hawalipwi marupurupu yao na changamoto hizo ambazo zipo. Wanakosa morali ya kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna zile call allowances walikuwa wanapata, tunaomba wawape; kuna postmortem allowance, wanafanya kazi kubwa mno hawa Madaktari wetu, kazi ni kubwa. Ukiwa mgonjwa ndiyo utajua kazi kubwa wanayoifanya hawa Madaktari; wawape hiyo allowance na motisha nyingine ambazo zinapaswa wapate hawa Madaktari, wanafanya kazi kwa weledi mkubwa na mazingira yao ni magumu, tunaomba wawape hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja katika kipengele cha wazee. Wazee wa nchi hii ni watu ambao wamechangia sana katika maendeleo ya nchi yetu, lakini pamoja na kuchangia maendeleo ya nchi yetu Serikali bado haiwatambui katika huduma ya afya. Wazee wanakwenda kwenye madirisha yale, tulisema kutakuwa na madirisha ya wazee, naomba Wizara ituambie ina madirisha mangapi mpaka sasa katika Halmashauri mbalimbali zilizopo nchini ya kupata dawa za wazee.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama haitoshi, Serikali imechukua hatua gani kwa wale ambao hawajatekeleza hilo agizo katika halmashauri zetu? Maana wazee wanakaa wanahangaika huko tunakotoka. Ni lini Serikali sasa itagharamia kuwapa bima ya afya wazee ili waweze kutibiwa. Tunajua wazee wanapofikia umri huo magonjwa na maradhi yanakuwa ni mengi mno; tunaomba Wizara ilitilie mkazo suala hilo la wazee.

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti wanayopata hii Wizara ya Afya ni ndogo sana na haitoki kwa wakati. Unakuta kwamba wamepewa asilimia chache sana kwa maendeleo….

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, muda wako umekwisha, ahsante sana.

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika hoja iliyopo mbele yetu ya Wizara ya Mambo ya Nje.

Mheshimiwa Spika, mimi naomba nianze kwa kuchangia katika Sera ya Mambo ya Nje na Diplomasia ya Kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, kuna mwanadiplomasia mahiri sana na alikuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa 38 wa Australia, Julie Bishop ambaye katika moja ya hotuba zake alizungumzia masuala haya; naomba niyanukuu kidogo na alisema; wakati diplomasia ya kizamani ililenga amani diplomasia ya uchumi inalenga ustawi kwa kukuza ustawi wa maisha ya watu, diplomasia ya kiuchumi inakuwa ndio msingi wa kudumisha amani, ikitekelezwa vizuri diplomasia ya kiuchumi ni lazima ilete matokeo ya kukua kwa uchumi, kuongezeka kwa ajira na kufunguka kwa vyanzo vipya vya uwekezaji wa ndani na wa kimataifa kuchochea ubora wa maisha ya watu na nchi husika. Kinyume cha matokeo hayo diplomasia ya kiuchumi itakuwa ni neno tu ambalo tunaweza tukaiga yaani copy and paste.

Mheshimiwa Spika, kwa nini nazungumza hivi; diplomasia ya uchumi itasaidia sana nchi yetu kuweza kutoka hapa tulipo. Itasaidia sana kuwa na mafanikio makubwa katika nchi yetu kwa sababu tunaposema diplomasia tunahitaji kuwa na wataalamu wazuri, tunahitaji mahitaji ya viongozi wenye maono, tunahitaji watu wenye ushawishi, tunahitaji mikakati madhubuti. Bila kuwa na hivi vitu tutapata changamoto kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kupata hii nafasi, najua wewe ni mbobezi na ni mzoefu. Tunakuomba uweze kuifanyia kazi tuweze kuipata hii sera na tuweze kufanyia yale ambayo Watanzania wanahitaji kuyaona katika kutafuta masuala mengi ambayo wameyasema wengine, napenda nisiyarudie. Ajira inatakiwa ipatikane kwa wenzetu ambao ni mabalozi wako kule waangalie fursa zilizopo ni zipi ili waweze kuzileta. Kwa hiyo, tunataka visionary leadership, strong negotiators, tunataka lobbyists na tunataka smart strategies ambazo zitasaidia nchi yetu iweze kutambulika na kupata yale ambayo mengi ambayo tunaweza kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa twende kwenye hadhi za balozi zetu, wamezungumza kuanzia Mwenyekiti wa Kamati ya Mambo ya Nje. Hadhi za balozi zetu zinasikitisha, balozi zetu ziko hohehahe, hatupeleki pesa za maendeleo, ndio mwanzo wa haya yote ambayo unayaona. (Makofi)

Kwa hiyo, tunaishauri Serikali, tunamuona Waziri wa Fedha yupo apeleke pesa ili balozi zetu ziendane basi angalau hata na balozi za nchi za Afrika ambazo zipo maeneo hayo, tunatia aibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yaani balozi zetu unaangalia zina majengo yanavuja, balozi zetu zimechoka huko, majengo ya balozi zetu yanatia uchungu. Kwa hiyo, naomba nisiyaelezee sana haya, kuna maeneo mengi viongozi wetu wakuu walikwenda wakaahidi, lakini bado mpaka leo hatujajenga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende kwenye suala la uraia pacha; mimi nazungumza kwamba uraia pacha ni fursa kimkakati. Tunaangalia nchi za wenzetu wameweza kufanya hivyo, watu wanapata uraia pacha. Tuchukulie mfano tuna wachezaji wanacheza nchi za wenzetu, kuna mchezaji anaitwa Rashford yuko kule anacheza Manchenster United, yule inasemekana wazazi wake ni Wazanzibari, sasa angekuwa na uraia pacha angeweza kurudi akachezea nchi yetu na wengine wengi ambao wako huko wakipata hii fursa kwetu inasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wenzetu Wakenya diaspora yao imechangia dola za Kimarekani bilioni 2.7 kwa mwaka 2018 na ambayo ni asilimia tatu ya pato la Taifa ambayo imetokana na uraia huo pacha. Kwa hiyo, sisi tukiweza tusikae kama kisiwa, tuwaangalie wenzetu wanafanya nini na sisi tuangalie pale ambapo italeta tija na sisi tuifanyie kazi hivyo kwa sababu hii tunajikosesha wenyewe mapato kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano kuna nchi moja inaitwa Estonia. Hii nchi wana uraia wa kidijitali, kwa hiyo, hapo ulipo unaweza ukapata uraia, unaweza kuomba una kampuni uweze kuwekeza kule na wanaendesha nchi inakwenda, wanakwenda kidijitali, lakini sisi kuna vitu ambavyo tunavifinya. Kwa hiyo, kama kuna mambo ambayo tunataka tuyaweke sawa basi Mheshimiwa Waziri aangalie ni mambo gani ambayo tuyaweke sawa, lakini tuweze kuwafikia wenzetu ili na sisi tuweze kusonga mbele tunyanyue uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatutumii vizuri diaspora zetu. Kwa nini nasema hivi; balozi zetu zikiangalia Watanzania walioko katika nchi ile, tuwe na kanzidata, tujue kabisa kuna wanafunzi wangapi na wanasoma masomo gani na yatasaidiaje kwa nchi yetu? Wapi wanafanya kazi gani? Kama ni watu wa kufanya kazi za majumbani tufahamu, itambulike kabisa na hizi ni fursa wafanyabiashara wangapi? Wanafanya biashara zipi?

Mheshimiwa Spika, sasa tukitambua hivyo mabalozi hawa watatusaidia kuona fursa ziko wapi. Tuna watu wako kule wanasoma nini? Wanafanya nini? Kwa hiyo, sisi kama nchi itatusaidia kutambua kwamba tuwekeze wapi kwa zaidi kwa sababu tunakuwa tuna data kamili ya watu ambao wako nje ya nchi ambao tunaweza kuwa-supervise na kuona nini ambacho wanaweza wakakifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nije kwa mabalozi; mabalozi wana wajibu mkubwa sana wa kutafuta fursa za ajira kwa nchi yetu. Fursa za ajira watatutafutia mabalozi wetu, kama kweli tutawachukua wale ambao wamefuzu, wamesoma diplomasia, wanaelewa ni kitu gani wafanye katika nchi hizo.

Kwa hiyo, wanapokuwa pale wanaweza wakaziona fursa, amesema Mheshimiwa Balozi Pindi Chana hapa. Watu tuna mazao mengi yako kule tunakosa masoko, lakini balozi ambayo itaona kwamba hapa pana fursa hii ndio kazi yao kubwa ya kuhakikisha inashirikiana na nchi hii kujua kwamba mkoa fulani wazalishe hiki ni fursa huku na tunaweza tukaipelekaje hiyo.

Mheshimiwa Spika, lakini pia sisi tunakuwa hatuangalii, wenzetu wa Kenya wana-market strategies ambazo wanatangaza utalii. Unakuta wanatangaza kabisa kwamba pengine Mlima Kilimanjaro uko kule kwa sababu sisi tuna vitu ambavyo ni vikwazo. Mimi kuna jamaa yangu alikuwa yuko huko Sweden, lakini ametaka kuja, kwenda kwenye ubalozi wetu wanasema hawatoi visa ya East Africa. Sasa anakwenda kwenye ubalozi wa Kenya na nchi nyingine anapata visa, anakuja kupitia Kenya, kule anatoa pesa inabaki kule, sisi tumezuwia, lakini atafika Tanzania kapitia Kenya. (Makofi)

Kwa hiyo, kuna fursa kama hizo zipo sisi tunazizuia kwa vikwazo ambavyo kwa kweli kama kuna msingi mkubwa ambao tunauona hauna manufaa basi turekebishe ili na sisi tuweze kupata pesa kutoka kwa watalii wengi wanaotaka kuja kwetu. Kwa hiyo, hayo ndio mambo ambayo ninaya-insist.

Mheshimiwa Spika, wenzetu kule kuna lugha ya Kiswahili, lugha ya Kiswahili nje wanaofundisha wengi ni Wakenya wanafundisha Kiswahili, sisi tupo na ndio waanzilishi na wenye Kiswahili hapa, hatufanyi hivyo. Ukiangalia kwenye mtandao unakuta kuna translation za Kiswahili wamefanya Wakenya, wameingia mkataba na google, wanapata fedha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sisi tuzione hizo kama ni fursa na sisi tuweze kutumia mabalozi wetu na wengine kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunaitendea haki Wizara hii, tunaitendea haki nchi yetu ili tuweze kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini cha mwisho sio kwa umuhimu, basi angalau hawa mabalozi wabakiziwe maduhuli yale ambayo badala ya kupeleka Serikalini wabaki nayo mabalozi yawasaidie kwa ajili ya ujenzi wa balozi zao, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kupata fursa hii. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu; vile vile niwashukuru Mheshimiwa Waziri na Manaibu Waziri pamoja na watendaji wa TAMISEMI kwa usikivu wenu. Usikivu huo muuendeleze kwa kuu-transform kwa watendaji ili waweze kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachangia Wizara hii nikijielekeza katika fedha za maendeleo ambazo zinatolewa. Wizara hii inagusa moja kwa moja wananchi kule ngazi za chini. Wizara hii ni nguzo kabisa, ni kama uti wa mgongo wa Wizara zote katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninazungumza hivi kwa sababu, fedha za maendeleo zimekuwa zikipelekwa tofauti kwa Halmashauri tofauti. Kuna Halmashauri zinapata fedha zaidi ya asilimia 100 waliyoomba, kuna Halmashauri ambazo zinapelekewa fedha za maendeleo chini ya asilimia 50 ya zile fedha ambazo wameziomba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri anapohitimisha atueleze nini kinasababisha hivyo? Kwa sababu, tumeona kuna Halmashauri ambazo zina uhitaji mkubwa na hazipati fedha kwa wakati. Kwa mfano, Halmashauri ya Wilaya ya Momba imekuwa inapata fedha ndogo sana ukilinganisha na Halmashauri nyingine ambazo zipo. Kwa hiyo, tunapenda kuwe angalao na msawazo, Halmashauri zipate fedha ambazo zitawakwamua katika miradi yao ya maendeleo, ili waweze kufanya maendeleo ya Watanzania kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kukosa usimamizi wenye weledi na uratibu mzuri katika Wizara hii. Ninazungumza hivi kwa sababu, kumekuwa na miradi ya maendeleo ambayo imeratibiwa toka miaka mingi na mpaka sasa haijakamilika. Miradi ambayo inakamilika lakini haitumiki na miradi ambayo inakamilika lakini katika ubora wa chini sana. Sasa hivi vyote vinaleta changamoto kubwa katika utekelezaji wa miradi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni bora mkawa na miradi michache mizuri, ikamilike kwa wakati ndipo tutaona thamani ya fedha ambazo tunazipeleka katika Halmashauri zetu. Kupeleka miradi mingi ambayo haimaliziki kwanza inaongeza fedha nyingi kwa sababu wakandarasi waki-stop kuna pesa wanakuja wanadai, na hii fedha wananchi wanaigharamia pia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda nitoe mfano. Kamati yetu ya LAAC, tulikwenda Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali; ninavyosema usimamizi, ni kwa sababu gani? Halmashauri ya Mbarali, ina mradi wa muda mrefu, lakini tumekwenda pale, kwa sababu tulitoa taarifa, ndiyo kwanza walianza kuchonga barabara, walikwenda kuchoma moto, kwa sababu kuliota nyasi nyingi sana. Wamechoma moto hadi gutters ziliungua; ujue hizo nyasi zilikuwa na urefu gani? Maana yake ni kwamba, usimamizi haupo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa nini usimamizi haupo? Wenzangu wamezungumza hapa, kuna Wenyeviti wa Vijiji, Watendaji, na Madiwani. Hawa wote ni wasimamizi katika zile ngazi. Kama hatuwawezeshi, hawawezi kuangalia hii miradi vizuri kwa ufasaha.

Kwa hiyo, tuangalie namna ambavyo hawa watawezeshwa kwa namna moja au nyingine, na kuwe na mfuko wa ufuatiliaji. Huu mfuko wa ufuatiliaji utasaidia wale ambao wako katika kufuatilia waweze kwenda na kuona fedha zinazowekwa pale. Mradi wa takribani shilingi bilioni nne na zaidi haukaguliwi, hakuna anayeufuatilia! (Makofi)

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa, Mheshimiwa Asenga Abubakari.

T A A R I F A

MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naomba kumpa taarifa mzungumzaji, ukweli katika Mradi wa Hospitali ya Mbarali anaouzungumzia ni mradi very serious ambao umeharibiwa na wasimamizi wa mradi ule. Namkumbusha tu kwamba, tulikuta hata bohari ya dawa imewekwa dawa ikiwa kuna joto kali sana. Hakuna vipooza joto. Kwa hiyo, anachosema ni sahihi, namwongezea taarifa hiyo.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Grace Tendega, unapokea taarifa?

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa kwa sababu, bohari ya dawa iliwekwa sehemu za joto na wanaharibu dawa nyingi sana ambazo ni fedha za wananchi na ni dawa ambazo zingeweza kutumika. Kwa hiyo, hivi ndivyo vitu tunavyovizungumza kwamba usimamizi hakuna. Kwa hili niko serious kwa sababu, kama hamtasimamia hizi fedha takribani shilingi trilioni nane zinakwenda kule chini, tutakuta madudu makubwa yako kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninazungumzia pia manunuzi yasiyozingatia sheria. Haya manunuzi hayazingatii sheria, lakini vilevile sheria yetu ina changamoto; unakuta bati linalouzwa shilingi 30,000/= wananunua kwa shilingi 110,000/=. Kwa hiyo, hizi ndiyo changamoto. Namwomba Mheshimiwa Waziri waangalie, kama hizi sheria zina shida walete turekebishe humu ndani ili tunusuru Watanzania pesa zile zitumike vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ya CAG inasema, Halmashauri 40 zilifanya manunuzi yenye thamani ya shilingi bilioni 5.37 bila ushindani. Halmashauri 59 zilifanya matumizi ya shilingi bilioni 8.86 bila idhini ya Bodi ya Zabuni na Halmashauri tatu zilitekeleza miradi isiyokidhi viwango na kusababisha hasara ya shilingi milioni 32.64. Hii maana yake ni kwamba, kama…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Hitimisha hoja yako, muda wako umekwisha Mheshimiwa.

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nahitimisha. Nawaomba Ofisi ya Rais, TAMISEMI, muwe mnazingatia usimamizi kwa mali za Umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
Hoja ya Dharura (Changamoto ya Kupanda kwa bei za Mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa)
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi, mimi naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Kigua kama alivyoitoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia changamoto hii ya mafuta tukianzia Machi. Machi petrol ilikuwa Shilingi 2,459 hii ni kwa Dar es Salaam, Aprili ilikuwa Shilingi 2,642 na Mei ilikuwa Shilingi 3,148, ina maana kumekuwa na ongezeko la asilimia 28. Ukija diesel ilikuwa Shilingi 2,500 natolea kwa Dar es Salaam, Aprili, Shilingi 2,644 na Mei Shilingi 3,258 ongezeko la asilimi 30; mafuta ya taa ilikuwa Shilingi 1,811 mwezi Machi, Aprili ilikuwa Shilingi 2,173 na Mei imekuwa Shilingi 3,112. Sasa hii trend ya kuongezeka mafuta kiasi hiki inakwamisha hata maendeleo ya Watanzania kwa ukubwa, kwa maana nyingine hili ni janga kama lilivyokuwa janga la UVIKO. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiangalia Watanzania asilimia kubwa kule vijijini mafuta ya taa ndiyo wanayoyatumia, hii imeleta changamoto kubwa wananchi kwa ongezeko la zaidi ya asilimia 71 ya mafuta ukiangalia toka Machi mpaka Mei. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mimi ninaliona tatizo hili ukiangalia wale wananchi waliokuwa wakipanda bodaboda kwa Shilingi 1,000 hivi sasa hivi ni shilingi 3,000, wale waliokuwa wakipanda bajati kwa shilingi 5,00 sasa hivi ni shilingi 1,500 inakwenda hadi shilingi 2,000 kwa Mtanzania wa hali ya chini imekuwa ni changamoto kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Serikali, kwa sababu kwa sababu nimesema hili ni janga ni kama lilivyokuwa la UVIKO tunaweza kukopa pia mikopo ya bei nafuu ikasaidia kuweza kupunguza changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine tukiangalia kama tuliweza kutoa ruzuku kwa pembejeo, basi tufanye hivyo pia hata kwa sekta hii ya mafuta ili tuone jinsi ambavyo wananchi itawapunguzia mzigo mkubwa wa kuendesha maisha yao. Unaona wananchi wanapata shida, kwa kweli hali ni mbaya. Usafiri bei zimepanda mno na kila mtu anakuja na bei zake, kwa hiyo, Watanzania wanapata changamoto kubwa ya mafuta haya yalivyopanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine tuweze kuondoa tozo nyingine, tunaweza tukaancha hizi za REA na mambo mengine lakini hizi tozo nyingine tuziondoe kwa muda wa mpito, tukikaa sawa tutakuja kuona huko mbele. Lakini kwa wakati huu, hizi tozo tupunguze ili wananchi waweze kufanya hivyo, lakini Serikali kwa kweli ipate muda wa kuyatafakari haya na kuja na majibu kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, tumeona kwa nchi ya Kenya, walitoa ruzuku lakini hata jana wameendelea kutoa ruzuku, wametoa ruzuku ya shilingi za Kenya bilioni 34.4 ambayo ni sawasawa na shilingi bilioni 691.2 za Tanzania. Hii inawasaidia wananchi wa Kenya kuweza kupunguziwa ukali wa Maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru lakini niombe Serikali kwa kweli ikae, itafakari ije na majibu ambayo yatawasaidia Watanzania. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nina hoja zifuatazo; kwanza Mkoa wangu wa Iringa tuna wafugaji na wavuvi kwenye Bwawa la Mtera. Bajeti ya mwaka 2021/2022 Wizara iliahidi mikakati ifuatayo:-

(a) Kutengeneza vichanja vya kukaushia dagaa na Samaki;

(b) Wataongeza uzalishaji wa barafu na kujenga cold rooms. Hadi sasa wananchi wavuvi mkoani kwangu wanasubiri cold rooms kwa ajili ya kuhifadhia Samaki; na

(c) Mliahidi kununua boti za uvuvi, hatujapata bado.

Mheshimiwa Naibu Spika, mifugo mingi malisho yake ni changamoto kiasi kwamba mazao yake yanakuwa kidogo. Ushauri wangu:-

(a) Wizara ihimize uandaaji wa malisho ya mifugo. Tuelimishe wananchi kilimo cha majani kwa mifugo na tuwawezeshe wafugaji kuwa na malisho ya mfano.

(b) Wizara itafute soko kwa wavuvi na wafugaji wetu ili wavue na kufuga kisasa.

(c) Wizara itoe mafunzo, ihimize wananchi kuwa katika vikundi na kuwawezesha ufugaji wa mifugo na samaki pia mshirikiane na Halmashauri zetu katika mikoa yote ili kuinua wananchi na kuwaunganisha na taasisi za kifedha.

(d) Wizara itengeneze vichanja kwa ajili ya kukaushia Samaki.

(e) Wafugaji wakubwa kama ASAS Iringa azidi kupewa wataalamu ili aweze kufanya vizuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipoa fursa ya kuchangia Wizara hii ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naanzia na ukusanyaji wa maduhuli, kama ulivyoona, lipo tatizo la ukusanyaji wa maduhuli ambalo limeoneshwa katika Taarifa ya Wizara lakini Taarifa ya Kamati. Niungane na Taarifa ya Kamati kama walivyosema, unaona kabisa wao walikadiria kukusanya bilioni 126.1 lakini wamekusanya milioni 600 tu, asilimia 0.48. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, nawaona bado vijana, wana uwezo mkubwa kabisa. Hivi mmekwama wapi? Mtueleweshe mnakwama wapi kukusanya kiasi hicho, kiasi kwamba sisi hapa leo tuwapitishie bajeti nyingine wakati mmeshindwa kukusanya asilimia hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kabisa jinsi ambavyo wameweka, kwamba makadirio ya mwaka 2023/2024 ni bilioni 10, basi wangeenda waweke makadirio hata iwe bilioni moja ambayo mtaifikia kuliko kuweka bilioni 10 ambayo hamtaifikia kama mlivyokuwa hamjaifikia hiyo mliyoifanya. Sasa Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa niombe atupe maelezo; nini kinaleta utofauti huo mkubwa wa ukusanyaji wa maduhuli? Ama makadirio hayako kiuhalisia? Mnakwama wapi? Ningependa hilo aweze kuja na utuambie changamoto iko wapi ama hawana uhakika wa vyanzo vyeo vya makusanyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye Tume ya Umwagiliaji. Mheshimiwa Waziri wakati anasoma taarifa yake katika ibara ya 247 ameeleza kuwa tuna hekta milioni 29.4 zinazofaa kwa kilimo cha umwagiliaji, zinazotumika sasa ni hekta laki 727.2, tu ambayo ni asilimia 2.5 tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kati ya hekta 29.4 tunatumia asilimia 2.5 tu kwa umwagiliaji. Ndiyo maana unakuta kwamba tunaenda kuagiza ngano nje, tunakwenda kuagiza bidhaa zingine kule kwa sababu hatujaweza kutumia vizuri ipasavyo sekta hii. Ukiangalia kwa mwaka wa fedha uliopita tulipitisha bajeti, na tunamshukuru Mheshimiwa Rais aliongeza ile bajeti ikawa kubwa sana. Sasa twende kwenye sekta ya umwagiliaji ilivyopata fedha. Katika mwaka huu tume iliidhinishiwa jumla ya shilingi bilioni 257.5 kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa umwagiliaji. Hadi Februari 2023 bilioni 46.687 tu ambazo ni sawa na asilimia 18 ndizo zilikuwa zimetolewa kwa ajili ya kutumika, asilimia 82 hazijatolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika hii maana yake nini? Hii maana yake ni kwamba, tunapitisha bajeti na tukishapitisha bajeti zile fedha hazitoki, matokeo yake huko nje tunaonekana tuna bajeti kubwa, Waziri wa fedha yuko hapa lakini fedha hazijaenda, Kwa hiyo ndio maana unakuta kwamba miradi mingi haitekelezwi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nishukuru, kuna Skimu ya Mkombozi ambayo iko Isimani katika Mkoa wangu wa Iringa ambayo mmeipa shilingi bilioni 55 na kwa kweli inaenda vizuri, hii skimu mmeipa fedha. Lakini skimu nyingine zote zimekosa, ni kwa sababu hizo fedha hazikutolewa zote. Ni ombi langu, Skimu ya Magozi ambayo iko Pawaga Jimbo la Isimani naomba nayo muipe fedha, Skimu ya Nyabula naomba nayo muipe fedha ili wananchi waweze kufanya kazi ya umwagiliaji wapate mazao kwa sababu ndiyo wanayoyategemea katika uzalishaji mali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kikubwa ambacho ninataka nikizungumzie hapa ni nini? Usipopeleka hizo fedha wananchi wanakuwa na hali ngumu ya maisha, wanakosa vyakula kwa sababu kule wanategemea sana hizo skimu, kwa hiyo wananchi wetu wametutuma tunaomba fedha ziende kwa ajili ya umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende katika changamoto ya watumishi katika sekta hii, hasa maafisa ugani. Tuna mahitaji ya watumishi 20,000 waliopo ni 6,000, tuna upungufu wa asilimia 67 wa maafisa ugani. Sasa hii ukiangalia na namna ambavyo Waheshimiwa Wabunge wengine ambavyo wamezungumzia kuhusu uzalishaji, unaona jinsi ambavyo tunashindwa kufikia targets zetu za kilimo. Kwa maana hiyo hatuwezi kuchangia pato la taifa vizuri kama hatuna maafisa ugani.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati sisi tuko huko vijijini tunakua ilikuwa maafisa ugani wakija pale kijijini kwa ajili ya kutoa maelekezo wanaitisha mkutano, wananchi wanakwenda kwenye shamba moja lililochaguliwa na wanatoa malekezo. Ningependa kujua, utaratibu unaotumika sasa hivi ukoje? Ili tuweze kuutambua. Kwa sababu kweli mmewagawia pikipiki na kwenye bajeti yenu mmeonesha kwamba mtawapa magari. Tunataka kujua utaratibu uoje ili wananchi wale wa chini waweze kutumika vizuri…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante, kengele ya pili.

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie. Kuna vijana tumewapeleka Israel, wanarudi wakiwa na ujuzi mkubwa. Niwaombe muwaunganisha katika mradi wa BBT ili waweze kuwa saidia vijana wetu kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nichangie katika bajeti hii. Nianze kwa kumpongeza Waziri, kwa kweli nampa pongezi kubwa kwa sababu ya usikivu na uvumilivu na utendaji kazi katika Wizara hiyo, hongera sana. Pia nampongeza Katibu Mkuu Doctor Faraji Mnyepe kwa kazi kubwa anayofanya pamoja na watendaji wote katika Wizara hii. Watendaji hawa wanafanya kazi kwa weledi mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze na Jeshi la Wananchi Tanzania, napenda kuwapongeza pia nao kwa utendaji mkubwa wa kazi zao uliotukuka na kwa gharama ya uhai wao. Hapa tulipo tunapumua na tuna starehe kabisa, lakini wenzetu wapo kazini wanafanya kazi bila kuchoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ndiye Amir Jeshi Mkuu kwa kutufanya tuwe na amani hii katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizo na utendaji wote wa Jeshi wanaoufanya, lakini kwa kweli fedha wanayopata ya maendeleo ni kidogo. Laiti wangepata fedha nyingi za maendeleo wangefanya vitu vikubwa sana. Tumetembelea maeneo mengi ambayo wanafanyia kazi, wanafanya kazi kubwa, kwa weledi mkubwa na kazi zao zinaonekana ukilinganisha na maeneo mengine ambayo tunakwenda. Kwa hiyo, niiombe Serikali iweze kutoa fedha wamepata asilimia 30.11 tu ya fedha za maendeleo. Kwa hiyo wangepata asilimia mia moja wangeweza kufanya kazi kubwa Hivyo, niombe Serikali itoe fedha kwa asilimia mia moja bila kuleta mzaha kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jeshi letu ili liendane na ubora hasa kama ubora wa kimataifa, lazima bajeti yao inayotengwa, iliyoidhinishwa itolewe kwa wakati na itolewe kikamilifu. Ikitolewa hivyo, wanajeshi wetu watafanya kazi kwa uhakika, lakini pia Serikali ihakikishe kwamba maslahi ya wanajeshi wetu wanapata bila changamoto zozote.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano tunaona kuna wanajeshi ambao wanaenda kwenye kozi mbalimbali sasa wanakwenda kule wanatoa fedha zao mfukoni za mshahara, ningependa kama ingekuwa Jeshi linapata asilimia mia moja fedha za maendeleo, hawa wangeweza kulipiwa kwa sababu kuna kozi ambazo ni za kuongeza teknolojia na mambo mengine ambayo ni ya kiubunifu ambayo wanatakiwa waweze kulipiwa. Kwa hiyo Serikali isifanye masihara katika kutoa fedha hizo.

Mheshimiwa Spika, niende katika mashirika yetu ya kimkakati, Nyumbu pamoja na Mzinga. Mashirika haya ni mashirika ya kimkakati yapo. Tumeona Nyumbu juzi tu hapa yametengeneza magari ya zimamoto na magari haya yamekuwa ni magari mazuri kabisa. Dunia yenyewe inatuona tumetengeneza magari ya zimamoto kwa fedha zetu hapa ndani. Sasa hawa Nyumbu wakiweza kupewa fedha za kutosha, wakiweza kupewa teknolojia za kisasa, wanaweza wakatengeneza vitu vingi vikiwemo vipuri mbalimbali wakauza ndani ya nchi na hata nje ya nchi. Wanaweza wakashirikiana na shirika la reli, wakasaidiana kuona wanatengeneza vipuri mbalimbali vikasaidia katika kupunguza mapato ambayo tunakwenda kununua katika nchi nyingine, tunatumia fedha za nje badala ya kutumia fedha zetu.

Mheshimiwa Spika, Nyumbu ilitoa mafunzo katika Nchi ya Uganda na Rwanda, lakini wenzetu wameshatupita,wako mbali kwa sababu ya kutekeleza azma ambayo Baba wa Taifa alikuwa anaitaka, kwa hiyo tuombe Serikali mweze kuchukulia kwa uzito, shirika hili linaweza likatutoa likatupeleka mbali sana kwa kutengeneza vifaa mbalimbali vya kisasa na hii itatusaidia kuweza ku-serve fedha za ndani badala ya kutumia fedha za nje kwenda kununua labda chuma nje, tunaweza tukasaidia Jeshi letu likapata Mchuchuma na Liganga wakaweza kuona kuna kitengo gani wawape ili waweze kuvuna chuma kile kikatumika kwenye Shirika la Nyumbu ambalo litasaidia katika kuleta masuala mbalimbali ya kimaendeleo.

Mheshimiwa Spika, pia kuna changamoto ya ikama ya watumishi. Kuna watumishi wapo lakini kuna wale ambao ni hitaji katika shirika hilo ambao wana sifa ambazo zinatakiwa katika shirika hilo. Nimwombe Mheshimiwa Waziri na niiombe Serikali waweze kupeleka watumishi wa kutosha katika shirika hilo ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa, kwa sababu wanafanya kazi kwa weledi mkubwa. Ukifika pale unashangaa ni Tanzania ama sio Tanzania, ni kweli kabisa kwa kweli wenzetu wanajitoa, wanafanya kazi kwa weledi lakini tuwape fedha, Serikali wapeleke fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikienda katika suala la JKT; Jeshi la Kujenga Taifa ni jeshi ambalo linaweza likatusaidia sana kututoa katika hali ya kiuchumi hasa tukishirikiana na vijana. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa mawazo ya kuona kwamba vijana wanatakiwa kusimamiwa kimaadili na mambo mengine yoyote, lakini bila fedha bado ni changamoto. JKT wametengewa asilimia sita tu ya fedha za maendeleo, itafanya nini? Tumeona wanajenga majengo mazuri. Tumeona wanashindwa hata kupeleka vijana JKT wengi kwa kukosa fedha za kuwahifadhi pale. Kuna vijana wengi wanatamani kwenda Jeshi la Kujenga Taifa hapa Wabunge wengi tunapigiwa simu kutoka huko, tunaomba vijana waende, lakini Mkuu wa Jeshi anashindwa awaweke wapi, hakuna hata sehemu ya kuwaweka. Kwa hiyo fedha zikienda, fedha nyingi za maendeleo tunaweza tuka-accommodate vijana wengi kwenda katika Jeshi hilo lakini wakafanya kazi nyingi za kilimo, za kiuchumi na za kuleta maendeleo katika Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Waziri aangalie kabisa kwamba target kubwa katika fedha ya Wizara JKT inachangia asilimia 73.3, hizo ndio fedha zinazochangiwa na JKT. Pale ambapo wanachangia fedha nyingi na Serikali ione namna ya kuwekeza zaidi ili kuweza kuongeza fedha nyingi Zaidi, kama tutawekeza kwa Jeshi la kujenga Taifa. Nimwombe Mheshimiwa Waziri aweze kufanya hivyo kwa Jeshi letu la Kujenga Taifa.

Mheshimiwa Spika, tumeona kwamba katika Jeshi la Kujenga Taifa kuna miradi ya kilimo ambayo inafanywa, lakini wanashindwa kuitekeleza kwa ukosefu wa fedha. Changamoto kubwa ni hiyo ya ukosefu wa fedha. Kwa hiyo niombe Serikali, Wizara ya Fedha wapeleke fedha kwa Wizara hii, hatuwezi kuwa salama bila ulinzi wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa miongoni mwa viongozi wenye ushawishi mkubwa Duniani na kupewa Tuzo ya mafanikio ya ujenzi wa miundombinu
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii. Na mimi kwa niaba yangu binafsi lakini kwa niaba ya Watanzania nipende kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais Samia Suluhu Hassan kwa kweli kwa utekelezaji wa majukumu yake na hasa kwa tuzo kubwa aliyoipata. Tunaweza kuwa na changamoto ndani ya nchi lakini tunavyotoka nje hili ni la kupongeza kwa kweli kwa kupata tuzo hii. Ni sifa kubwa ametuletea Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuzo hiyo ya miundombinu ambayo ameipata; wananchi wengi mnaona changamoto ambazo tunazipata katika usafirishaji hasa wanawake katika kutatua changamo zao. Kwa hiyo tunapongeza sana kwa kupata hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hiyo amekuwa miongoni mwa viongozi mashuhuri 100. Kwa kweli ni kitu ambacho ni cha kupongeza sana, haijawahi kutokea. Lakini mama huwa anajali familia na anajali nje ya familia. Tunaona kwa vitendo jinsi ambavyo anafanya, tumeona Mheshimiwa Rais amejielekeza katika maendeleo ya watu, na tunaona katika sekta ya afya Rais anakwenda kujenga hata hospitali kubwa kwa ajili ya akina mama na Watoto. Hili ni jambo la kupongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwenye elimu ameangalia kila mkoa kwa kuhakikisha kwamba tunapata shule za wasichana. Hii itasaidia sana wanawake kuwa kuwa katika maamuzi katika maeneo mbalimbali. Tumeona pia kwenye sekta ya maji miradi mingi ya maji imeanzishwa, mingi inalenga kutimiza ile asilimia 85 vijijini na asilimia 95 mijini. Lakini pia mama ameleta mapinduzi katika kilimo, tumeona katika bajeti hii jinsi ambavyo amefanya. Cha muhimu ni kwamba fedha zikitoka tutaona matunda yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, licha ya hivyo tumeona mahusiano yake na mataifa ya nje. Ameonesha katika ziara zake anazokwenda ametoa fursa mbalimbali za kiuchumi na tunaona fursa za kiuchumi zinakuja katika nchi yetu. Ameimarisha mahusiano na nchi za nje, kwa mfano tumeshuhudia amehudhuria Mkutano wa Umoja wa Mataifa ambako alikwenda kuhutubia kwa umahiri mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia tumeona alihudhuria Mkutano wa Glasgow ambako kuna masuala ya mabadiliko ya tabianchi. Huku tunaona ndiko gumzo kubwa sasa linalotokea katika mabadiliko ya tabianchi. Amehudhuria pia katika maonyesho ya kibiashara ya Dubai (Dubai Expo) ambapo wafanyabiashara wakubwa ulimwenguni wanakuja. Hili nalo limeleta umaarufu wa nchi yetu lakini tunajitoa kibiashara ili wananchi waweze kuja kuwekeza nchini kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini alifanya ziara nchi za Ulaya, Ufaransa, na Ubelgiji. Hii yote ni kutanua wigo kuhakikisha wananchi wanaiona hiyo. Vilevile, umaarufu wa Royal Tour; kwa wale ambao wanaangalia sinema, ile tamthilia ya revenge kwenye king’amuzi cha Azam, jana Mellan alimwambia mchumba wake nikufanyie nini? au nikupeleke Tanzania. Kwa maana hiyo inaonyesha jinsi ambavyo ziara hii jinsi ambavyo ziara ya Royal Tour ilivyozaa matunda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ninadhani kwa miaka ijayo Mheshimiwa Rais pamoja na kwamba alienda Marekani akakutana na Makamu wa Rais, lakini miaka ijayo mwakani labda anaweza akapata tuzo ya watu 20 hivi chini ya hapo, ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia na mimi bajeti hii kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023. Bajeti hii ukiingalia kwenye karatasi ni nzuri, lakini kazi ipo kwenye utekelezaji. Utekelezaji ndiyo changamoto kwa bajeti nyingi, hatujawahi kufikia asilimia 80 ya utekelezaji wa bajeti. Kwa hiyo, hata kama Mama alishasema kwamba yeye hawezi kuzungumza kwa kufoka, lakini tujitafsiri sisi kama Serikali na kama Watanzania kuhakikisha kwamba bajeti hii inatekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nianze kwa kuangalia; hii ni bajeti ya pili kwa mpango wa miaka mitano ambayo ni 2021/2022 – 2025/2026. Dhima yake ilikuwa ni kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu. Hiyo ndiyo dhima kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuweka vipaumbele vyake ambapo ameweka kilimo, mifugo, uvuvi, nishati, uwekezaji na biashara. Hivi alivyoviweka kama kipaumbele, kama kweli vitafanyiwa kazi, tuna miaka siyo miwili au mitatu, tutakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niunge mkono suala la mkakati wa kubana matumizi ya Serikali. Naunga mkono kwa sababu Watanzania kwa kweli wana hali ngumu na tumeona. Kwa mfano, masual ya magari, utaona jinsi magari anavyotumika ndivyo sivyo. Tukiangalia wenzetu tu nchi ya Jirani; Uganda, wanatumia magari yao binafsi na wanakwenda wanafanya kazi vizuri. Cha muhimu, lazima kuwe na utaratibu mzuri wa kuhakikisha kwamba wale ambao umewaweka katika categorization zenu za uongozi basi wawekewe mkakati Madhubuti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia suala la kupunguza ukubwa wa uwakilishi, nalo naliunga mkono katika vikao kusafiri umbali mrefu, kutumia TEHAMA, ni vitu ambavyo ni muhimu, hata alipokuja Mheshimiwa Rais hapa Bungeni tarehe 22/4/2022 alihimiza mambo kama hayo, TEHAMA itumike, na ndiyo vitu ambavyo tunaomba Mheshimiwa Waziri akafanyie kazi vizuri. Pia kufanyia kazi huko kuendane na kuboresha wafanyakazi ambao watakuwepo katika sekta mbalimbali za maeneo ya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tujiulize, mfumo wa kuendesha uchumi wa nchi yetu ni upi? Hamjawahi kututanabaisha kwamba mfumo wetu ni upi? Ni ujamaa na kujitegemea? Ni mfumo gani? Hatuna mfumo ambao tunaufahamu. Kwa sababu kama huufahamu vizuri, utapanga na utatekeleza vitu ambavyo hujui unakwenda wapi? Tujipambanue na tutafsiri mfumo wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa kujibu hoja, atuambie tuko wapi sasa hivi ili tuweze kujua tunafanya nini? Kwa sababu kila aina ya uchumi inajipambanua. Hata kama ni Bima ya Afya ya Ujamaa ni tofauti na Bima ya Afya ya Ubepari au Bima ya Afya ya kitu kingine. Kwa hiyo, tukijipambanua tutajua tunawekaje mambo yetu yaende sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme, Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere alizungumza kwamba, naomba ninukuu: “Maendeleo lazima yawe na uhusiano na watu.” Pia Hayati Rais Benjamin Mkapa, alisema katika kitabu chake, naomba ninukuu, anatamani mfumo wa uchumi ambao ni shirikishi. Hii ina maana gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya asilimia 67 ya watu nchini ni vijana. Kati ya hiyo asilimia 67, asilimia 13 ya hao hawazalishi hata Shilingi 100/=. Tupo kwenye majimbo yetu, tupo katika nchi yetu, nayo ni nguvu kazi. Sasa ni heri kuibua kichwa kimoja chenye ubunifu kuliko madini tuliyonayo. Kwa sababu tunaweza tukayaibua hayo madini lakini watu wa kuja kuyatumia wasiwepo. Tunataka uzalishaji wenye tija. Kama hatujawekeza vizuri kwa vijana hawa, uzalishaji utakuwa ni ndoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji mfumo wa kuinua sekta binafsi ili tuibue mabilionea wengie. Hebu tujiulize Tanzania, tuna mabilionea wangapi Mheshimiwa Waziri wa Fedha? Tunao wangapi? Nchi kama Finland, Ghana, Norway, Ujerumani, zimeweza kuwatumia wazawa wao, zimewawezesha na mpaka wameweza kufanya uchumi wao unakuwa stable. Sasa sisi tunajipambanuaje kwa hilo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo wa soko huria la kijamii (social market economy) ni mfumo unaochukua mazuri ya Ujamaa na mazuri ya Ubepari kwa pamoja, kisha wanapata mfumo mmoja wa kuhakikisha uchumi wa mtu mmoja mmoja unakua. Sasa hiki ndiyo kitu ambacho kama Serikali itaweza kutumia mfumo huu, tunaweza tukafika mbali. Ila mfumo huu ni endelevu, misingi yake mikubwa, lazima kuwe na sera na sheria zinazotabirika kwa wawekezaji. Hatuna sera zinazotabirika kwa wawekezaji. Rais amejitahidi sasa hivi, lakini tunaomba matokeo ya utekelezaji wa sera hizo. Vile vile kuwe na ushindani, uwajibikaji, soko, umoja, motisha na ushindani mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Tanzania anayeanza biashara leo, mtu kama anataka kuanza biashara leo, anaanza kulipa lini? Tujiulize wote, anaanza kulipa lini? Lazima tuwatengenezee mazingira ambayo huyu mtu anayeanza biashara leo tumpe muda wa kuuza kulipa. Hiyo ndiyo changamoto tunayopata. Pia, kodi kiasi gani? Hiyo kodi atakayolipa itakuwa ni kiasi gani? Lazima tuwashike mkono hao wote ambao watakuja kutaka kuwekeza. Tusipofanya hivyo itakuwa ni changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo ni wazo langu la mwanzo. Naenda katika kipengele cha Bodi ya Mikopo. Katika taarifa ya Mheshimiwa Waziri, sijaona mahali ambapo amezungumzuzia kabisa kuongeza posho ya wanafunzi wa vyuo vikuu. Ni jambo jema kwa wanafunzi wa Kidato cha Tano na Sita kusoma bure, sawa; lakini kule chuo kikuu, toka miaka hiyo wanapewa Shilingi 8,500/= wakati Dola bado ni Shilingi 1,600/=, mpaka leo Dola imepanda kuwa Shilingi 2,300/= mpaka Shilingi 2,400/=, bado wanapata kiasi kile kile, Hapana. Tuwaboreshee na hao. Pia mishahara imepanda. Kwa hiyo, tuangalie na hawa vijana tuweze kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine tuwaongezee pia ile capitation grants, tulipanga Dola moja, Shilingi 10,000/= tukawa tunawapa, tuwaongezee nao angalau ifike Shilingi 25,000/= kwa Primary School na Secondary, tuwaongezee hata ifike Shilingi 50,000/=. Hii itawasaidia watoto wetu kuweza kupata huduma bora za kielimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nizungumzie sasa kuhusu usimamizi na udhibiti wa upotevu wa mapato. Kama tunatenga hizi pesa lakini hazina udhibiti mzuri, tunatwanga maji kwenye kinu. Namshukuru Mheshimiwa Waziri, ameweza kumwongezea fedha Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali, na vile vile ameweza kuwapa vote wale internal auditors. Nashukuru kwa sababu kumekuwa na changamoto kubwa katika uwasilishaji wa taarifa za masuala haya. Tukifanya hivyo, ndipo uwajibikaji tutauona, uwazi tutauona, tutaona tija ya fedha zetu ambazo tunazipeleka katika sekta mbalimbali huko katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Ahsante sana. (Makofi)