Parliament of Tanzania

Kamati yaitaka MORUWASA kudhibiti upotevu wa Maji

KAMATI ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) imeitaka Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Mkoa wa Morogoro (MORUWASA) kuhakikisha inaweka mikakati thabiti ya kudhibiti upotevu wa maji.

Agizo hilo lilitolewa jana Mkoani Morogoro na Mwenyekiti wa Ujumbe wa Kamati hiyo, Shally Raymond wakati Kamati ilipotembelea miradi mbalimbali inayotekelezwa na Mamlaka hiyo.

Alisema Kamati imeshtushwa na upotevu wa maji wa asilimia 40 ambao ni mkubwa ukilinganishwa na Mamlaka nyingine za maji nchini.

"Tunataka mfanye jitihada za makusudi kupunguza upotevu huu wa maji kwa kuwa maji haya mnatumia gharama kubwa kwa ajili ya kuyazalisha na kuyatibu hivyo yanapokuwa yanapotea yanaleta hasara kwa Mamlaka," alisema.

Aidha, Mwenyekiti hiyo aliitaka Mamlaka hiyo kuchukua hatua za kuwaondoa wananchi wanaolima na kuishi milimani na karibu na vyanzo vya maji kwa kuwa wanasababisha uharibifu katika vyanzo hivyo.

"Waelimisheni kuhusu umuhimu wa kutunza vyanzo vya maji ili na wao pia waone kwamba wanawajibika kuvitunza vyanzo hivyo kwa ajili ya maisha yao ya sasa na ya baadae," alisema.

Kamati hiyo pia iliitaka Wizara ya Maji kuhakikisha inakamilisha miradi minne ya maji katika Miji midogo ya Gairo, Mvomero,Kilosa na Tuliani iliyotakiwa kukamilika mwaka 2012.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa MORUWASA Nicholaus Angubwike alisema Mamlaka hiyo inalitambua tatizo hilo la upotevu wa maji na kwamba imeanza mkakati maalum wa kukabiliana na upotevu wa maji.

"Hata sisi suala la upotevu wa maji ambalo pia linasababishwa na uchakavu wa mitambo linatuumiza, tumeanza mikakati maalumu ikiwemo kuwakamata wezi wa maji na kuwapeleka mahakamani," alisema.

Hon. Dr. Tulia Ackson

Speaker

Legislative Role

Profile

Ask the Speaker / Comments

Ms. Nenelwa J. Mwihambi

Clerk of the National Assembly

Legislative Role

Profile

Ask the Clerk / Comments

Member of the Parliament

View All MP's