Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Halima James Mdee (47 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nami kwa moyo mkunjufu kabisa japokuwa najua hawanioni, niwashukuru wananchi wa Jimbo la Kawe, kwa kunipa heshima kubwa, najua kuna watu walifikiria lile Jimbo nimeazimwa miaka mitano, sasa hii nguvu ya kuingia mara ya pili kwa tofauti ya kura 17,000 nadhani imetuma somo huko, mjue kwamba watoto wa kitaa wamenisoma vizuri na uzuri upande wa huko wengi ni wananchi wangu, kwa hiyo mtanivumilia kwa kipindi hiki cha miaka mitano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane kabisa na Mheshimiwa Peter Serukamba alivyozungumza asubuhi, baada ya Kamati ya Bajeti kuundwa, Chenge one na Chenge two, ilitoa mapendekezo ya kina baada ya Kamati kujadili, baada ya Bunge kujadili, na Kamati kwenda ku-compile, ilitoa mapendekezo ya kina ya vyanzo mbadala vya kodi vya Serikali. Leo tunakuja hapa, yaani ni kama vile akitoka Rais huyu, akiingia Rais mwingine, ni kama vile imetoka mbingu, imekuja dunia, hakuna connectivity.
Mheshimiwa Mwenyekiti, najua kuna Wabunge ma-junior hapa, tuko asilimia thelathini (30%) tumerudi ma-senior, lakini nawaambieni hii miaka mitano lugha ninayoizungumza leo mtakuja kuizungumza 2019. Serikali ya Chama cha Mapinduzi, mmechoka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana Zanzibar wamewakataa mnataka kulazimisha, ndiyo maana Tanganyika waliwakataa Tume ya Taifa ya Uchaguzi ikawabeba beba tu kindakindaki na ninyi mnajua. Nashukuru Mpango ametusaidia, katueleza yaani jinsi Serikali ya Chama cha Mapinduzi ilivyo-fail kwenye huu, alivyo review miaka mitano, anatuambia.
Mheshimwa Mwenyekiti, Reli mlipanga kukarabati, Reli ya Kati, kilometa 2,700, mmeweza 150 hivi hamuoni aibu? Halafu mtu anakuja hapa anasifia tu vyanzo tulishawapa Kambi ya Upinzani iliwapa miaka mitano iliyopita, kila mwaka tunawapa. Kamati ya Bajeti iliwapa mnakuja mnaumiza vichwa vya watu hapa for nothing.
Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mabehewa ya Mwakyembe, 274 tunaambiwa na yenyewe feki, yaani hayo yenyewe ndiyo yamenunuliwa basi na yenyewe Mheshimiwa Sitta katuambia siyo sisi, akaunda Kamati yake pale Chama cha Mapinduzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara Mzee Magufuli mwenyewe…
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Kuhusu utaratibu...
MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwakyembe ahsante kwa taarifa, tunaomba Mheshimiwa Halima Mdee uendelee.
MHE. HALIMA J. MDEE: Walikwambia wewe ni jipu? Sikiliza, mimi nimesema hivi, kwa mujibu wa Mheshimiwa Samuel Sitta alivyoenda Wizara ya Uchukuzi aliyasema hayo maneno. Sasa hayo mambo mengine wakamalizane wao wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara, alikuwa Mheshimiwa Magufuli. Walijipanga kujenga na kukarabati 5,204, wameweza kukarabari 2,700, na ni kati ya Mawaziri ambao walikuwa wanakuja na vitabu vikubwa sana na mikwara mingi, lakini kumbe hata nusu ya lengo haijatimia, Chama cha Mapinduzi.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu...
MWENYEKITI: Ahsante, naomba Halima uendelee.
MHE. HALIMA J. MDEE: Halafu hii biashara ya kufanya Rais hashikiki, wala hakamatiki wakati sisi jukumu letu ni kuisimamia Serikali ikome. Mimi hapa nimerejea…
MWENYEKITI: Naomba utumie lugha ya staha Bungeni kwa mujibu wa taratibu.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema hivi hii biashara ya kufanya Rais ni mtu ambaye hashikiki, hagusiki, hatajwi, hazungumzwi iishe kwa sababu jukumu la Bunge ni kuisimamia Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, rejea niliyoitoa hapa ni mafanikio ya …
MWENYEKITI: Mheshimiwa Halima naomba ukae, Mheshimiwa Waziri azungumze...
MWENYEKITI: Mheshimiwa Mdee naomba uheshimu Kanuni na katika mazungumzo.
MHE HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mpango wa Miaka Mitano iliyopita, wakati Mheshimiwa Magufuli ambae sasa ni Rais, alipokuwa Waziri wa Miundombinu hatimae Ujenzi na kila kitu, barabara zilizotakiwa kukarabatiwa na kujengwa ni kilomita 5,204 lakini sasa hivi tunaambiwa zilizokarabatiwa ni 2,775 kilometa. Kidumu Chama cha Mapinduzi! (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu kuna watu hapa wanazungumza utafikiria hii Serikali ni mpya, kumbe ninyi tokea mwaka 1961 mmepata dhamana kuanzia TANU mpaka CCM, watu tunaumiza brain tunatoa mawazo hamfanyi kitu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kilimo: Tukija kwenye sekta ya kilimo kimekua kwa asilimia 3.4 tuliokuja Bungeni miaka 10 iliyopita, kilimo kilikuwa kimekua kipindi kile kwa asilimia minne, tena malengo ya Serikali ilikua ni asilimia 10. Serikali ilivyoona inabanwa ikashusha mpaka asilimia sita. Leo tunaambiwa kilimo kimekua kwa asilimia 3.4 maana yake kwanza mmeshuka chini. Ile asilimia sita imekuja hapa chini mmeshindwa kui-balance, halafu mnasema eti mapinduzi ya kilimo! Hapa kazi tu! Yaani, kilimo cha umwagiliaji, wakati mkoloni anaondoka, tuna hekta za umwagiliaji 400,000, ninyi hapa mmetushusha mpaka 345,000 halafu mmnatuambia mmeongeza asilimia 46, wakati mnajua miaka mitano iliyopita tulikuwa tuna hekta 350,000. Yaani mnacheza na mahesabu, figure iliyokuwepo mnaongeza 5000 halafu mnajumlisha mnasema ni mafanikio. It is a shame! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka sijui 64 baada ya uhuru, asilimia 10 ya wananchi wana hati za kawaida na hati za kimila, hivi migogoro ya ardhi itaacha kuwepo? Miaka 64 sijui 54 baada ya uhuru, asilimia 20 ya ardhi yetu ndiyo ipo kwenye mipango, hivi mgogoro wa wakulima na wafugaji itaacha kuwepo? halafu inakuja Serikali hapa inaleta mpango, ime-adress vipi hivi vitu ambavyo ni critical, hakuna! Eti! mnaenda mnabomoabomoa Dar es Salaam, hivi tungekuwa na utaratibu wa kuwapa Watanzania maskini viwanja kwa gharama nafuu, kuna mtu anataka kwenda kujenga mtoni? Kuna mtu anataka kujenga mabondeni? Viwanja vya Serikali huna milioni sita, huna milioni saba hununui kiwanja, tena milioni 10, milioni 20 hununui kiwanja!
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni hivi, vipaumbele, miaka mitano iliyopita tulikuwa tuna miundombinu, tulikuwa tuna kilimo, tulikuwa tuna viwanda, tulikuwa tuna human development, tulikuwa tuna tourism, miaka mitano baadae majamaa yamegeuka, viwanda, kufungamanisha maendeleo ya watu, miradi mikubwa ya kielelezo, ujenzi wa maeneo wezeshi, yaani kilimo wameweka pembeni, kinaajiri asilimia 70 ya Watanzania, inachangia asilimia 30 ya pato la taifa, asilimia 40 ya fedha za nje umeweka pembeni, halafu unatuambia eti hivi vitu tulivyoviacha viporo vitajumuishwa, vinajumuishwaje kama havipo kwenye kipaumbele? Tutatengaje bajeti kama haipo kwenye kipaumbele?
MHE HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na Kamati ambayo imesema hivi ni muhimu kama kweli tunataka kuwasaidia Watanzania. Kama tunataka kuwasaidia Watanzania lazima tuingize kilimo kama kipaumbele cha msingi. Kamati ya Bajeti imesema na tukiingiza kilimo tutenge bajeti, mwaka jana tulikuwa tunasema hapa kwamba haiwezekani kitabu cha maendeleo cha Wizara ya Kilimo, fedha za maendeleo kwenye vocha ya kilimo imetengewa bilioni 40 wakati Jakaya Mrisho Kikwete ametengewa bilioni 50 kusafiri nje. Kwa hiyo, kama we mean business tuwekeze kwenye kilimo, tutapunguza Watanzania hao maskini kuwa wategemezi kwa Serikali.
MHE, HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo lazima miundombinu irejeshwe sababu kama tunataka viwanda, hivi viwanda bila uzalishaji kuna viwanda au kuna matope? Kwa hiyo lazima….
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru.
Mheshimiwa Spika, nikiwa Mbunge ambaye kwenye Jimbo langu kuna wanajeshi wengi wastaafu, ninawajibika kutoa sauti yao ili pale ambapo itatokea Serikali itasikiliza basi na wao waweze kupata neema.
Kabla sijaanza mchango wangu nitambue mchango wa masemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni. Vilevile nitambue mchango mzuri sana wa Mheshimiwa Nahodha na aliyewahi kuwa Waziri wa Ulinzi. Ni imani yangu kwamba Mheshimiwa Mwinyi utayasikiliza na Serikali hii Wizara na Taasisi zake na Idara mbalimbali za Serikali zione zina jukumu la kufanya kazi collectively kwa sababu Serikali ni moja na siyo kila mtu anaibuka na la kwake ndiyo maana kunakuwa na mkanganyiko wa aina hii. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuna hoja ambazo tulishazizungumza miaka miwili mitatu iliyopita. Imezungumzwa na Kambi Rasmi ya Upinzani, suala la migogoro baina ya Jeshi na wananchi. Ninaomba Mheshimiwa Waziri utakapokuwa unahitimisha leo naomba utueleze hatma ya mgogoro wa Kijiji cha Tondoroni kipo Kisarawe, mwaka jana, mwaka juzi nilizungumza kwenye hotuba ya ya Wizara ya Ardhi. Ningependa vilevile utupe hatma ya Kijiji cha Ihumwa, Dodoma, lakini vilevile Makuburi kwenye Kambi ya Jeshi wananchi sasa hii ni tofauti kwa sababu kwenye suala la Makuburi ni wananchi waliingia eneo la Jeshi kukawa na utaratibu ambao umefanyika Jeshi likaweka beacons upya. Sasa haieleweki hali ikoje sasa hivi ni muhimu vilevile ukatolea tamko ili wananchi wa maeneo yale waweze kukaa kwa amani.
Mheshimiwa Spika, hoja yangu ya pili ni pensheni ya wanajeshi wastaafu. Mheshimiwa Waziri huu ni mwaka wangu wa kumi na moja (11) Bungeni, katika kipindi chote hicho nikisimama kwenye hili Bunge Tukufu ninazungumzia suala la pensheni. Mheshimiwa Mkapa aliongeza kima cha chini kutoka shilingi 25,000 mpaka 50,000, Jakaya Kikwete akaongeza kima cha chini kutoka shilingi 50,000 mpaka 100,000, kima cha chini! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaambiwa Sir Major kwa waliostaafu kipindi cha mwaka 2009 kushuka chini analipwa shilingi 190,000 kwa mwezi, kwa maisha ya sasa hivi hawa wanajeshi wetu wanaishije? Mheshimiwa Waziri, tunajua Rais ana dhamana ya kuongeza vima vya chini, tunajua Rais ana dhamana ya kuangalia hivi viwango, tunaomba hili suala lifanyiwe kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ninamshukuru Mwenyekiti wa Kamati amesema kuna mapendekezo, kwa sababu tulikuwa tukisema hizi hoja, yanakuja maelezo kwamba kwa mwaka 2009 mpaka sasa kwasababu ya mishahara yao na blah blah nyingi. Lakini tunafahamu kwamba mwaka 2008 na 2009 utafiti ulifanywa mapendekezo yakatolewa, hivi kizungumkuti ni nini, hivi shida kweli ni fedha? Leo tunalalamika kuna uhalifu wa kijeshi, mabenki yanaibiwa, hivi kama mtu unalipwa laki tano kwa miezi mitatu kwa sukari ya shilingi 4,000, sukari tu, shilingi 4,000 mpaka 6,000 hivi utaacha kwenda kuiba benki? Wakati una uwezo wa kutumia silaha? Kwa hiyo, ninakuomba Mheshimiwa Waziri, hawa wastaafu wetu tuwaangalie kwa jicho pana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mwaka 2009 lilijibiwa swali hapa Bungeni, tunakumbuka kuna wanajeshi wetu hawa hawa wastaafu; mwaka 1978 walishiriki kwenye vita Uganda, mwaka 1978 na 1979. Serikali ya Uganda ikatoa kiinua mgongo cha shilingi bilioni 59; Mheshimiwa Khalifa aliuliza swali hapa 2009 miaka saba iliyopita, hii hela imetolewa. Serikali mkajibu hiki kifuta jasho kwa wanajeshi wetu tutawapa, miaka saba baadaye mmechikichia na mkwanja wa watu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tunaomba leo mtujibu kwamba hiyo shilingi bilioni 59 ambayo ilikuwa ni kifuta jasho cha wanajeshi wetu waliopambana usiku na mchana kuokoa nchi yetu kiko wapi? Naomba ujibu leo hapa usije ukatuambia ooh, muda hautoshi, nataka ujibu, kwa sababu wanajeshi wastaafu wanataka wajue ile fedha imekwenda wapi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, wanajeshi wetu wanasema kama Serikali imeamua kwamba mnawapa hiki kiinua mgongo, ama pensheni ya chini chini, hivi kweli Serikali hatuwezi kufikiria kuandaa mfumo wa bima ya afya? Bima ya afya kwa nini, kwa sababu tunaweza tukatumia utaratibu huo huo wa hiyo pensheni ndogo wakati tunajipanga kuongeza kwa makato hayo hayo, ili wanajeshi wetu wastaafu waweze kwenda kupata tiba. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, wanasema mmewaambia wakiugua wataenda watatibiwa Lugalo. Mimi wakazi wangu wanajeshi wananiambia wakienda Lugalo wengi wao wananyanyapaliwa, wanachokwa! Unahudumiwa bure siku ya kwanza, na unajua uzee ni maradhi, siku ya pili, siku ya tatu unanyanyapaliwa. Wanasema kabisa tunaona wenzetu wakienda mwingine ana kufa, wa pili ana kufa, wa tatu ana kufa; wanahisi labda ukienda pale unadungwa sindano kumbe mtu tu amekufa kwa ugonjwa wake wa kawaida. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo sisi tunaomba Serikali ifikirie, tunaweza tukaitumia pensheni hii ndogo, kuwakata makato kidogo kukawa kuna uhakika wa kupata tiba hawa wastaafu wetu na watoto wao. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, matumizi ya Jeshi Zanzibar. Mimi ni miongoni mwa watu ambao ninalipenda sana Jeshi letu, wanafanya kazi kubwa mno…
MHE. SULEIMAN M. NCHAMBI: Taarifa Mheshimiwa Spika.
SPIKA: Taarifa Mheshimiwa...
MHE. HALIMA J. MDEE: Nakushukuru kwa kumsaidia kwa sababu siyo size yangu. (Kicheko)
Mheshimiwa Spika, nilikuwa namalizia hoja yangu kwa kusema hivi, natambua kazi nzuri sana ya Jeshi letu, lakini ni muhimu ikaeleweka kitu kimoja, tukiendelea kutumia haya majeshi Mheshimiwa Waziri kwenye ukurasa wako wa 19 unasema ugaidi na uharamia. Ni muhimu tukaelewa ugaidi unatengenezwa ndani, watu wanapokuwa oppressed na kuchoka na kukata tamaa wanajengewa fikra za kufanya mambo ambayo walikuwa hawafanyi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo unapoona mwenzio ananyolewa wewe tia maji. Kina Al Shabab, kina Boko Haram hawakuanza out of nowhere, watu walikuwa suppressed. Sasa for the sake of this country, for the sake ya kizazi kichanga, average ya kizazi cha Tanzania ni miaka 18, kwa hiyo haiingii akilini watu wazima wenye tamaa ya mamlaka wanalazimisha kubaki Zanzibar wakati Wazanzibar hawajawachagua kwa kutumia Jeshi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Wabunge wa Zanzibar walikuwa wanakuuliza Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi, wakati wa maandalizi ya kinachoitwa uchaguzi wa marudio, Mheshimiwa Waziri kuna mazombi, mazombi wanaandikisha madaftari, mazombi wanapiga watu, Waziri unakataa hakuna mazombi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini kipindi cha uchaguzi, kipindi kuelekea uchaguzi tunaona watu na mask, tunaona mazombi wamepigwa picha. (Makofi)
SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Halima, nakushukuru muda haupo upande wako. Tunashukuru kwa mchango wako, huku Bara mnatuacha barabarani ninaposikia mazombi najiuliza zombi ndiyo nini? (Kicheko)
Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa hii nafasi. Niseme kwamba mimi ni Mjumbe wa Baraza la Madiwani la Jiji. Kwa hiyo, baada ya kuona suala la UDA limeingizwa hapa na mambo yanayohusiana na Jiji yanatajwa ninawajibika kuzungumza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nataka niweke rekodi sawa. Jana kuna mtu mmoja alikuwa anazungumza hapa, zamani tulikuwa tunawaita manjuka lakini siku hizi sijui tutawaita jina gani, wakasema kwamba hoja ya kutaka Jiji livunjwe ni kwa sababu ya kashfa ya Kiwanda cha Nyama, lakini anasahau kwamba kashfa hii ya Kiwanda cha Nyama ilitokea wakati Jiji likiwa chini ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
Kashfa hii ya UDA tunayozungumza leo imetokea wakati Jiji likiwa chini ya Chama cha Mapinduzi. Wakati sasa Jiji liko chini ya UKAWA tunataka tulisafishe ili Halmashauri zile zilizokuwa tatu na sasa hivi zimeongezeka tano ziwe sehemu ya kuboresha lile Jiji. Hawa wezi wanaotajwa kwenye ukurasa wa 31 na 32 wa hii Kampuni ya Nyama na UDA ni makada wao na wanawajua na hatujaona popote walipofikishwa mahakamani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme hivi, baada ya UKAWA kupata dhamana ya Jiji tumekwenda kubatilisha maamuzi yenye dhuluma yaliyopoka umiliki wa UDA Jiji na nitasema kwa nini?
Niliambie Bunge hili, msije mkathubutu, maana jana nilisikia wanasema kuna ile shilingi bilioni tano aliyolipwa Simon Group tuipangie matumizi, sisi kama Jiji tunatambua mamlaka yetu. Sasa kama sisi hapa hatujitambui Serikali inatuingilia sisi tunatambua mamlaka yetu. Tulisema hatuwezi kutumia hii shilingi bilioni tano kuhalalisha haramu kuwa kitu kitakatifu. Siyo kwamba haina matumizi, Halmashauri zetu zina changamoto nyingi sana, lakini tulisema hatuwezi kuwa sehemu ya haramu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwa bahati mbaya sana TRA baada ya kuona Azimio la Baraza la Madiwani linasema hii shilingi bilioni tano ya Simon Group hatutaitumia kwa sababu kuna ushenzi umefanyika kinyume kinyume kwa kutumia upungufu wa kisheria, wakaenda wakavuta kodi. Kwa hiyo, hayo makusanyo mnayosema yameongezeka miongoni mwao ni fedha za kifisadi za kuiibia nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la UDA, nitazungumza kihistoria tu. Hili shirika lilianzishwa mwaka 1974 ambapo Serikali ilikuwa na hisa asilimia 100. Mwaka 1985 Serikali iliamua kugawa hisa zake, asilimia 51 ikaipa Jiji na yenyewe ikabakia na asilimia 49. Ni muhimu mkaelewa, hisa kiujumla wake zilikuwa milioni 15 lakini katika hizo hisa milioni 15, hisa milioni 7.1 ndiyo zilikuwa zimelipiwa ama zimekuwa allotted hizo nyingine milioni 7.8 zilikuwa hazijalipiwa. Kwa hiyo, Serikali ilivyogawa hisa, asilimia 51 Jiji na yenyewe asilimia 49, Jiji likapata milioni 3.9 na Serikali ikabakia na milioni 3.4. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, figisu lilianzia wapi? Figisu lilianzia mwaka 2011 na wakati nasema haya naomba Serikali ielewe hivi, UDA kama ilivyo mashirika mengine ilikuwa chini ya uangalizi wa PSRC ama ilikuwa specified kwa Tangazo la Serikali Namba 543 la mwaka 1997. Kwa mantiki hiyo, kisingeweza kufanyika chochote mpaka iwe despecified na siyo kwa maneno maneno ila kwa Gazeti la Serikali. Mpaka sasa PSRC ilikuwa hai ikaisha, ikaja CHC ikaisha, haijawahi kuwa despecified. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tafsiri nyingine ni nini? Miamala yote kisheria iliyofanyika kuhusiana na UDA ilikuwa ni batili. Ndiyo maana katika muktadha huo, Jiji baada ya kwenda kwa UKAWA kwa sababu tunasoma na kujiongeza na kwa sababu wengine tulikuwa sehemu ya huu mchakato tukasema hili zoezi ni batili. Nilikuwa naelezea historia nikachanganya kidogo ili kuwaweka kwenye mstari ili mjue kwamba huu mchakato ulikuwa haramu from the beginning. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2011 kupitia hao hao makada wao, sitaki kuwataja majina maana ni wazee nawaheshimu sana, nimewatajataja sana mpaka wakawa wananipigia simu Halima vipi? Kwa hiyo, sasa siwataji kwa sababu mnawajua.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2011 Bodi ya UDA ikaenda kugawa zile share ambazo hazikugawiwa na wala hazikununuliwa milioni 7.8 kwa Simon Group. Kwa aibu wamemuuzia share moja shilingi 145 yaani ile UDA yote walikuwa wanataka kuigawa nusu kwa jumla ya shilingi sijui bilioni 1.5 wakati huo huo ukaguzi ama tathmini iliyofanyika inasema shirika kwa huo unusu wake tu ina thamani zaidi ya shilingi bilioni 18 alikuwa anapewa mtu kwa sababu amehonga honga. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya mwaka 2011, kwa hiyo Simon Group akawa sehemu ya wanahisa wa UDA kwa kununua zile unallotted shares ambayo ni kinyume na Articles of Associations za UDA. Nina maandiko hapa ya Serikali, ya Msajili wa Hazina, yako hapa. Kwa hiyo, Waziri wa TAMISEMI tikisa tu kichwa nitakupa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo akapata uhalali kama mwanahisa kwenda kuomba kununua hisa zingine. Serikali ilitaka kuuza hisa zake, lakini vilevile Jiji kukawa kuna dhana ya kuuza hisa. Serikali ikaachia pembeni lakini Jiji kwa rushwa hizi hizi ikapitisha Baraza la Madiwani, wakapitisha kinyume na utaratibu. Tunajua vilevile hata kama Baraza la Madiwani likipitisha lazima Waziri mwenye dhamana ya TAMISEMI ambapo kipindi hicho ni Waziri Mkuu aridhie. Hakuna sehemu hata moja ambayo Waziri wa TAMISEMI ameridhia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na huo ubovu wake sasa Simon Group akatakiwa alipe hiyo hela. Pamoja na ubovu wa mkataba ikakubaliwa mwisho wa kulipa fedha hiyo ni Septemba, 2014 kwa sababu hapa kuna fedha za unallotted lakini vilevile kuna fedha za Jiji baada ya Baraza kukaa, bilioni 5.4 hazikulipwa. Tukakaa kama Kamati ya Fedha, ni kwa bahati mbaya sana Kamati ya Fedha ya Jiji na Baraza tukaazimia mkataba ule ukabatilishwe mahakamani.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwa masikitiko na nasema hivi kwa sababu Kamati ya LAAC wakati Baraza lenye mamlaka linasema huu mkataba haramu tunaenda kuubatilisha, LAAC, sitaki kuamini LAAC ilihongwa kipindi kile, ikaja ikasema msibatilishe huu mkataba wakaelekeza Jiji waendelee na makubaliano na Simon Group. Kamati ya LAAC, kuna maelezo hapa na kibaya zaidi, kesho yake baada ya Kamati ya LAAC ilivyokuja kutoa ushauri kwenye Jiji, yale maneno waliyokuwa wanasema LAAC ndiyo hayo hayo maneno ambayo Simon Group aliandika kwenye barua kuhalalisha kwa nini aongezewe muda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme hivi, kwanza, fedha za hizo hisa zimekuja UKAWA tumeingia. Fedha iliyotakiwa ilipwe mwaka 2014 imelipwa mwaka 2016, tukasema huu mchakato ulikuwa batili kisheria kuanzia mwanzo. Hata kama Baraza la Madiwani la kipindi kile chini ya Masaburi na CCM lilipitisha sheria inasema lazima Waziri aridhie, Waziri hakuridhia na hii UDA ilikuwa iko chini ya PSRC, miamala yote ilikuwa ni batili. Kwa mantiki hiyo, ili kuondoa mzizi wa fitina kwa sababu TAKUKURU ilifanya kazi yake, CAG alifanya kazi yake, nitaomba Bunge hili kupitia Kanuni ya Bunge ya 120 tuunde Kamati Teule ili hili suala lifanyiwe uchunguzi, tujue kinagaubaga, tujue mbivu ni zipi, tujue zilizoiva zipi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, halafu eti tunasikia hapa watu wanazungumza, basi zile hisa ambazo Simon Group alikuja kukubali kuzirudisha milioni 7.8 tupewe Halmashauri tugawane. Hivi tunagawanaje wakati hivi tunavyozungumza, Simon Group wamekopa bilioni 50 NMB kwa ajili ya magari haya ya DART. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nashangaa eti Serikali inaitetea wakati ripoti ya Msajili wa Hazina hapa analalamika yeye mwenyewe kama mbia ambaye hakuuza hisa zake alikuwa hajui kama kuna kakampuni kingine kadogo cha uendeshaji wa magari ya mwendokasi kalikoundwa na Simon Group. Yaani Msajili ni mbia analalamika hajui halafu anatoka mbele anatetea huo upuuzi. Sisi UKAWA tunaoongoza lile Jiji hatutaruhusu. Hatutaki mtuingize kwenye choo cha kike na choo cha kiume kwa kutulazimisha. Eti twende kuwa mwanahisa wakati kuna huyu jamaa kivyakevyake ameenda kukopa shilingi bilioni 50 ambazo zenyewe hatujui kazifanyia nini, kuna vibasi pale vya Kichina tu vya kizushi, kwa hiyo tuingie tuwe wanahisa tuwe sehemu ya huo mzigo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme hivi kesho kutwa Baraza la Madiwani tunaenda kukutana kwa sababu hiyo ni mandate yetu, yaani ninyi hapa mnatushauri tu. Kwa hiyo, msije mkajidanganya kwa wingi wenu, hasa ninyi upande wa huku, maana nasikia sijui Jiji linavunjwa, sijui sasa share tupewe, sisi wenye mali ambao tunaongoza Jiji ndiyo tunaenda kuamua siyo ninyi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuongea hayo na nitaomba niungwe mkono kwenye kifuncgu cha 120 nitakapokileta hapo baadaye.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niongelee suala la Lugumi, nitaomba Mwenyekiti akirudi atuambie Lugumi walienda kufanya nini? Kwa sababu tunajua mliomba mkataba ambao ndiyo unaweza kuainisha haki na wajibu wa kila pande. Tunavyozungumza, na wewe Naibu Spika unajua nawe ulisaidiasaidia kulifunikafunika kuisaidia Serikali, unajua kwamba Bunge linapohitaji mkataba wa aina yoyote linatakiwa kupewa. Kamati yako imeomba mkataba kwa sababu CAG alisema vifaa vimefungwa 14 baada ya hoja ya Mheshimiwa Zitto alipokuwa Mwenyekiti wa PAC, mwezi Mei, 2016 CAG aliitwa tena na hawa kasema vimefungwa 14. Hivi ni miujiza gani imetokea tunaambiwa leo eti vimefungwa 153, ni miujiza gani?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunataka tujibiwe hapa kwa sababu imekuwa ni utamaduni wa nchi hii tunatumia Usalama wa Taifa, tunatumia Polisi, Ulinzi na Usalama excuse kuiibia nchi. Sasa leo Mwenyekiti…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Halima, malizia sentensi muda wako umekwisha.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Unajua leo nilikuwa na mizuka sana kwa sababu ya UDA hadi mbavu zinauma.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru.
Kwanza nimshauri tu Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, usiige utamaduni wa mtangulizi wako wa kutuletea vitabu vikubwa ambavyo mtu akisoma between the lines kuna maneno mengi kuliko uhalisia.
Ushauri wangu kwako tu, inawezekana huu ni mwaka wa kwanza bado una mihemko ya aliyekutangulia, kuanzia mwaka ujao uje na kitabu ambacho kinaeleza tumepanga nini na tutatekeleza nini kwa huo mwaka, hilo ni la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili watu ambao mnaongea sana, sijui Mheshimiwa Magufuli alivyokuwa Waziri kafanya nini, mwaka jana mwenyewe amekiri hapa, katika miaka kumi ya Ilani ya CCM, 2005 – 2015 ameweza kutekeleza asilimia 31 ya kile mlichotakiwa mkifanye. Sasa hivi nyie mtoto akifanya mtihani akipata 31 chini ya 100, hivi huyo amefeli amefaulu?
Kwa hiyo, tuache kujikomba, unafiki, tusaidie Serikali ndilo jukumu letu kama Wabunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina barabara zangu Jimboni, najua kuna wengine huko wanapata shida na barabara zao zimechokachoka, sisi wa town tuna nafuu kidogo. Lakini nimeahidiwa hapa, miaka mitatu iliyopita na Mheshimiwa Waziri, naomba utoe majibu. Kuna barabara za kupunguza foleni mkoa wa Dar es Salaam; barabara ambazo zinaunganisha Jimbo la Kibamba na Jimbo la Kawe; barabara ya Goba – Tanki Bovu; Goba – Wazo Hill –Tegeta, Gao – Goba – Makongo – Mlimani City.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba mkiwa mnanijibu hapa, msiniambie ujenzi umeanza, ninajua hizi ni barabara tatu tofauti zinazounganishwa na kipande kimoja. Sasa nataka leo msiniambie kwa sababu ukiangalia vitabu vya bajeti, na ndio maana nawaambia Waheshimiwa Wabunge,
tuwe tunasoma, tukiwa hatusomi Mawaziri hawa wanakuja wanatudanganya. Miaka mitatu mfululizo hizi barabara zimetengewa fedha, kipande cha kuunganisha Jimbo la Kibamba na Kawe, Goba – Mbezi, Goba – Wazo Hill, Goba – Mlimani City, lakini leo ni mwaka wa tatu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaona kuna hela zimetengwa hapa, zipo, kama ambavyo mwaka wa jana Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwa maneno haya haya kama ya kwako zilikuwepo lakini mwaka mmoja baadaye hakuna barabara. Sasa Waziri kesho ukiwa unajibu naomba uniambie kwa uhakika wananchi wa Kawe wasikie, kwa sababu wewe ni mwananchi wangu pia na Mbunge wako nikiwa nazungumza lazima usikilize hizi barabara zinakamilika lini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka wa juzi, wakati wanajenga hii barabara ya Mwenge – Tegeta – Kibaoni niliishauri Serikali nikaiambia wakati wa mvua kuna kiwango kikubwa cha maji kinachotoka ukanda wa Wazo huku juu Goba na ili barabara iweze kudumu kuna maeneo ambayo lazima mapokeo na matoleo ya maji yawe makubwa Ili tuweze kuelekeza maji baharini. Leo barabara imejengwa, mvua ikinyesha ukiwa pale Afrikana, Goigi ni majanga, hii barabara itakatika miaka mitano haitimii, kuna faida gani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi namuomba Mheshimiwa waziri akiwa anajibu, kwa sababu niliandika barua kama Mbunge nikiwaomba; mkasema ooh! huyu mjapani ambaye tumepewa msaada ana masharti tutatumia fedha za ndani kujenga mapokeo ya maji makubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa leo naomba niambiwe maana mvua ikinyesha yakitokea maafa Mheshimiwa Jenista Mhagama huyo, halafu mvua ikikauka na yeye anasepa, barabara iko vilevile. Sasa leo nataka mniambie mna mikakati gani, dhahiri, shahiri, kuweza kuokoa ile barabara ya mabilioni ya shilingi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu Rais ambaye watu tunaambiwa tusimtajetaje, tutamtaja tu kama alichemsha, msitutishe. Wakati tunapitisha bajeti ya barabara ya Mwenge – Tegeta ya shilingi bilioni 88 tuliambiwa hii barabara itajengwa vipande viwili, kwa matukio mawili. Moja ni Mwenge kwenda Tegeta ya pili ni Mwenge kwenda Morocco, bilioni 88. Sasa leo kuna uchafu unaendelea pale, kutoka Mwenge kwenda Morocco sijui mnatengeneza kichochoro, sijui mnatengeneza kitu gani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninataka nijui zile shilingi bilioni 88 ambazo Mheshimiwa John Pombe Magufuli, katika Bunge hili akiwa Waziri alisema kazi yake ni kujenga hizi barabara mbili, ziko wapi? Nataka majibu. Na ule uchafu mnaojisifia sijui fedha za Uhuru, sijui fedha za nini, ile barabara ilikuwa na pesa; kwa hiyo msitafute ujiko kwa kuwa mmezitafuna zile pesa mnatuletea uchafu. Si hadhi ya Dar es Salaam kujengwa ibarabara zile na kama mnatuambia mnajenga kwa muda, hilo pia ni tatizo linguine, misuse of resources. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mafuriko. TANROADS walifanya upembuzi yakinifu sijui mnavyoita ninyi, wakatengeneza na michoro kwa ajili ya mfereji mkubwa kuzuia mafuriko ukanda wa Kunduchi, miaka minne imepita. Mwaka juzi alienda Mheshimiwa Pinda, akaambiwa mchoro huo upo, wakati wananchi wanaelea kwenye bahari ya mafuriko, mkasema itajengwa, itatengewa fedha, hakuna kilichofanyika, naomba nipate majibu kesho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nyumba za Serikali. Naomba niseme hivi, haya majipu yanayotumbuliwa tutaona huyu bwana mkubwa ana maanisha akitekeleza Azimio la Bunge la mwaka 2008. Bunge lilisema nyumba ambazo zilipewa watu ambao si sahihi zirejeshwe, nyumba ambazo zilikuwa za maeneo ya kimkakati ya watumishi zirejeshwe. Sasa kuna maneno mengi ya mtaani yanasemwa kuhusiana na watu waliopewa nyumba hizi. Sasa tukiona bwana mkubwa anashindwa kufanya utekelezaji yale maneno ya mtaani tutaanza kuyaamini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka hatua zichukuliwe, ukaguzi ufanyike kwa kina, CAG aagizwe ili hizi nyumba 7,921 zilizouzwa, tujue mbivu zipi, mbichi zipi, na kama kuna watu walipewa kinyume na utaratibu nyumba zirejeshwe (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka wa jana Mheshimiwa Samuel John Sitta akiwa Waziri nilizungumza juu ya nyumba za TAZARA zilizouzwa kinyemela, kinyume na utaratibu. Kuna audited report ya mwaka 2014 aliniomba nakala nikampatia; nyumba zaidi ya 500 ziko hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa kuwa nyie kawaida yenu mnaendana na mihemko, maana kipindi kile aposhinda Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, ari mpya, kasi mpya, yaani kila mtu akija hapa ni swaga tu za ari mpya, maisha kwa Watanzania yamekuwa fresh. Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ameenda na ya kwake, Mheshimiwa John Pombe Magufuli ametengeneza asilimia 31 tunakuja huku, hapa kazi, story tu, yaani ninyi ni watu wa mapambio. Sasa mimi nitakupatia hii audited report ili umuulize na Mheshimiwa Samuel John Sitta aliifanyia nini, ili kesho unipe majibu juu ya hizi nyumba zilizouzwa. Kwa mtindo ule ule wa nyumba zile za Serikali utaratibu wake uko wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nikushukuru, lakini niwaombe Wabunge wenzangu mtanikumbuka miaka mitano ikiisha. Pitieni vitabu vya ujenzi mtanikumbuka maneno yangu. Ninyi kaeni, mnaona majina yenu hapa mnacheka cheka tu, itakula kwenu big time. Asanteni sana Mheshimiwa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nisema kwamba kwanza nasikitika na ninawashauri tu Wabunge wapya na vijana, jukumu letu sisi ni kuisaidia Serikali na kuisaidia nchi. Anasimama Mbunge anatoa pongezi kwa Wizara ya Kilimo kwa sababu ya hoja moja ya tozo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana Mheshimiwa Waziri katika hotuba yake anatumia robo tatu ya muda kusema tozo mbalimbali alizozikata badala ya kutuambia pamoja na hiyo tozo kukatwa tuna mikakati gani mipana ya kusaidia 75% ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tungewekeza kwenye kilimo ipasavyo kama ambavyo mipango ya miaka mitano mitano kwa miaka zaidi ya 30 iliyopita, kama ambavyo Ilani ya Chama cha Mapinduzi imekuwa ikisema kwa miaka zaidi ya 30 iliyopita, ajenda isingekuwa tozo yaani tungeongeza kodi Serikali ingepata mapato kwa sababu tumewekeza vizuri. Ni muhimu Wabunge wapya wakajua Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi iliahidi kuongeza…

T A A R I F A . . .

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ananipotezea muda. Ninachotaka kumshauri, mimi unajua natoka Jimbo la mjini, alright! Asilimia 85 mnatoka majimbo ya vijijini. Tukichukulia mzaha bajeti ya kilimo, mimi kwangu naathirika kwa sababu tu ya mfumuko wa bei.

Kwa hiyo, ni lazima nizungumze hapa kwa sababu mwaka 2016 mfumuko wa bei ulikuwa 5.4% sasa hivi ni 6.4% kwa mujibu wa ripoti ya BOT iliyotoka juzi. Kwa sababu chakula, mahindi, sukari, mihogo imepanda bei. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunapozungumza hapa, tunataka wenzetu wasikie. Hivi unapongezaje bajeti ambayo mlituahidi kilimo kitakua kwa 10% mwaka 2010; kikashuka, sasa hivi kilimo kinakua kwa asilimia 1.7%? Mwaka 2016 kilimo kilikuwa kinakua kwa 2.7%; mwaka 2015 kilimo kilikuwa kinakua kwa 4%! Kwa hiyo, kwa kadiri ambavyo siku zinakwenda, kilimo kinazidi kushuka chini; na tafsiri yake 75%



wa Watanzania wako hoi bin taabani! Hatuoni? Hivi tunapongeza nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya maendeleo inaniuma! Bajeti ya maendeleo, eti kati ya shilingi bilioni 101, zimepatikana shilingi bilioni 3.3, sawa na 3.31%. Hivi tunapongeza nini? Hivi Mheshimiwa Waziri huyu…

T A A R I F A . . .

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Chief Whip Kivuli! Aah, Mheshimiwa Chief Whip. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachosema ni hivi, labda nirudie, niweke vizuri. Kwa sababu sisi ni rahisi ku-propagate mambo. Nasema hivi 75% ya Watanzania ambao wanafanya kazi ya kilimo, ambao 80% ndani yake ni wanawake, wamefukarishwa na Serikali ya CCM kwa sababu ya mipango ambayo hawana mikakati ya kuitekeleza. Ndiyo maana…

MWENYEKITI: Hapana Mheshimiwa Mdee. Unaikubali taarifa au unaikataa?

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeikataa kwa sababu haina issue.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninachosema ni nini Wabunge? Nasema kwa nia njema kwamba kama leo bajeti ya maendeleo ya kilimo tumetoa 3%; mwaka 2016 tukasema utekelezaji, ndugu yetu ni mpya 15% tena kwenye shilingi bilioni 32 ikatoka shilingi bilioni tano, asilimia 15.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umwagiliaji, wakati anasoma Waziri wa Maji imepatikana 8% tu. Tume ya Umwagiliaji ina wajibu wa kuhakikisha kwamba Sera ya Umwagiliaji inatekelezwa ili miundombinu ya umwagiliaji iwekwe kule kwenye mashamba, halafu eti mtu anakaa anapongeza, unapongeza nini? Hatuisaidii Serikali! Hatuisaidii nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitegemea kwamba tutasimama hapa kwa sababu wengi tunawakilisha wakulima, tuweke mguu chini, tuiambie Serikali…

T A A R I F A . . .

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, siwezi kukubali, yaani haina mashiko. Siwezi kukubali hiyo taarifa, kwa sababu sisi tunasoma nyaraka ya Serikali. Tunasoma Taarifa za Kamati za Bunge. Sasa kama hizo taarifa



zinatuambia hivyo, hayo makandokando mengine ya kuombaomba huko, sisi hayatuhusu. Sisi tunazungumzia bajeti ya Serikali na tuko kwenye bajeti hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba wasiniingilie.
Mheshimiwa mh! Jana…

T A A R I F A . . .

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Wabunge wa CCM, vijana na watu wazima ambao wameingia, wametukuta sisi tukiwemo, mkasome vizuri Ilani ya CCM. Mimi huwa naipitia, kwa manufaa tu ya kujenga, kwa sababu mwisho wa siku, mafanikio ya Ilani yenu, ni mafanikio yenu na ni mafanikio ya Taifa. Kwa hiyo, hapa hatutafuti mchawi. (Makofi)



Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nawashauri wakasome Mipango ya Maendeleo mbalimbali. Yaani usije ukawa umekuja mwaka 2010, basi unachukua ule Mpango wa Maendeleo wa 2010 ama 2015; unakuja 15 kwenda mbele. Lazima tujue tumetoka wapi, tunakwenda wapi ili tuweze kushauri vizuri. Kwa hiyo, tusichukiane, dhamira ni njema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi kwa sababu watu wamezungumza suala la utafiti hapa, ni kweli! Tuliazimia na Serikali ikakubali kwamba 1% ya pato la Taifa itaenda kwenye utafiti kwa sababu dunia ya sasa hivi bila kufanya tafiti ili uweze kujua unataka nini, huwezi kupanga mipango yako. Isipokuwa mpaka sasa fedha zinazotolewa kwa tafiti zinatia aibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi Waziri wa Viwanda na Biashara, Mheshimiwa Mwijage amekuja hapa, kwa sababu tu ameandika kwenye hotuba yake viwanda ambavyo vimekuwa registered, yaani watu wameenda kusajili tu pale TIC! Kwa sababu ameandika kwenye hotuba yake viwanda
224. Kila Mbunge anapongeza anajua viwanda vimeshafanyaje? Vimeshajengwa! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana nimepitia hivi viwanda 224, si tuko kwenye hotuba ya kilimo! Sasa wamezungumza watu, hakuna kilimo bila raw materials, viwanda gani hivyo? Nimeangalia hapa viwanda 224, robo tatu viko mjini Dar es Salaam. Halafu viwanda vyenyewe basi ukienda kuangalia deep into details unaweza ukacheka, ufe mbavu, uzimie na ufe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana wamezungumza watu hapa suala la pamba, nikasema hebu ngonja niangalie, kwenye hivi viwanda 224 hivi kwenye hiyo mikoa, kwenye robo hiyo chache basi, hivi viwanda vya kuiongezea hadhi Pamba vipo? Hakuna hata kimoja!

Sasa unajiuliza hivi wale ndugu zetu wa Kanda ya Ziwa hususan mikoa ambayo inalima pamba, pamba



ambayo ni zao muhimu, akiwemo Mheshimiwa Mtemi Chenge, hamko kwenye mipango ya Serikali, halafu anasimama mtu hapa anapongeza, eti tozo. Yaani tozo isingekuwa issue kama wakulima wetu hawa tungewapa mitaji; kama tungeweza kuweka miundombinu na tungetoa fursa za kilimo! Tozo siyo issue! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hiki kitabu, mlisema juzi hapa kwamba hii Serikali ni moja, siyo kwamba Wizara ni ya huyu, ni wa huku, Serikali ni moja! Hivi iweje leo ukisoma kitabu cha Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara, ukisoma kitabu cha Mheshimiwa Waziri wa Kilimo…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila mpangilio)

MHE. HALIMA J. MDEE: Vipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma hivi vitabu viwili, moja ni mbingu, nyingine ni dunia. Hivi vitabu havikutani. Kwa hiyo, sasa sisi tunaiomba Serikali jamani, tuache kutumia, sijui tuliwanyima Watanzania elimu! Tuna-take advantage ya kuwanyima elimu, maana tumeambiwa 31% ya watu ambao hawajui kusoma na kuandika. Sijui tunafanya makusudi ili ukienda na hoja nyepesi unaijengea maghorofa kama vile hiyo hoja ndiyo ulikuwa umeahidi, kumbe ulikuwa umeahidi kitabu kinene hivi!

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba kwa dhamira nzuri kabisa, tuisaidie nchi! Yaani naomba kwa nia njema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri wa Kilimo alituambia mwaka 2013 kulikuwa kuna sera mpya ya kilimo. Hivi ni vitu gani ambavyo viko kwenye Sera ya Kilimo ya 2013 ambavyo vimekuwa reflected huku, yaani inauma! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa tunazungumzia masuala ya migogoro ya wakulima na wafugaji. Mwaka 2011 tulileta hoja binafsi hapa, miaka saba kama siyo sita iliyopita, tukaiambia Serikali tufanye land auditing nchi nzima ili tuweze kujua kila kipande cha ardhi cha nchi yetu anayo nani? Kama ni mwekezaji, kama ni mkulima, kama ni mfugaji ili tuweze kupanga matumizi bora ya ardhi, Bunge hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka sita iliyopita nilitoa hiyo hoja, Bunge likaunga mkono, likawa Azimio la Bunge na aliyekuwa Waziri wa Ardhi akafanya mabadiliko kidogo. Tukasema tukifanya hivi, tutaweza kutatua migogoro ya wakulima na wafugaji, tutaweza kujua mashamba makubwa ambayo yako chini ya wawekezaji ni mangapi. Tutaweza kujua wakulima wetu wadogo na wafugaji wakoje, ili tuweze kupanga mipango kama nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka sita baadaye Azimio la Bunge ambalo nadhani lilikuwa ni la kihistoria kwa pande zote; Waheshimiwa Wabunge wa Chama Tawala na Upinzani tuliungana tukasema…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa. Muda wetu ndiyo huo. Ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami niungane na wote ambao walisema kuna umuhimu kama Taifa kupima ardhi yote. Wakati wa Uchaguzi Mkuu CHADEMA tulisema is very possible kupima ardhi na kutoa hati kwa wananchi kwa sababu kuna potential kubwa sana kupitia kodi ya ardhi kwa nchi kuweza kupata mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na wote ambao wanaitaka Serikali ije na mpango mahsusi wa kuhakikisha sekta binafsi ya Tanzania inashamiri. Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mpango kwenye tathimini ya mpango wake wa 2011-2015 na mpango unaokuja anakiri kuna changamoto ngumu sana kwenye sekta binafsi, ushiriki wao hauridhishi. Lazima tujiulize maana lazima unapofeli ufanye tathmini kwa nini ni ngumu kwenye eneo hili muhimu tunalotarajia lichangie zaidi ya 40 trilioni kwenye mpango wetu huu mpya tumeshindwa kulivutia kuwa ni sehemu muhimu wa maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilimsikia ndugu yangu hapa akisema wasiosikia na wasikie, wasioona na waone, ndugu yangu tunapofanya tathmini ni muhimu tuwe wakweli pia. Mimi niwashauri Wabunge hawa kwa sababu ni mkongwe kidogo, tukija na mentality ya kusifia SGR, Stigler’s Gorge na madaraja ya Dar es Salaam, hatuwezi kulisaidia taifa kwa sababu hivyo vitu vitatu is no longer breaking news. Stigler’s Gorge ilianza kuzungumzwa miaka mingi sasa hivi inajengwa asilimia 25, SGR tulianza kuzungumza tokea enzi hizo iko kwenye mipango imeanza kutekelezwa kidogo na nyienyie Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kikubwa, Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mpango katika Kitabu chake cha Maendeleo; tathmini yake mwenyewe kwenye kitabu chake, amekiri kwa maneno yake na nitarejea na mengine jana walirejea Waheshimiwa Wabunge. Katika ukuaji wa uchumi bado hatujafika, pato la kila mtu bado hatujafika, mapato ya kodi ya Serikali kwa mwaka vis-à-vis pato la taifa bado hatujafika, uwiano wa mapato kwa pato taifa bado hatujafika, kiwango cha umaskini bado hatujafika, uwekezaji wa mitaji kutoka nje bado hatujafika, uzalishaji wa umeme bado hatujafika, usambazaji wa umeme bado hatujafika, vifo vya kina mama na watoto na huduma za maji vijijini bado hatujafika, kilimo bado hatujafika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Serikali, Mheshimiwa Mwigulu tuliza mzuka, kama Serikali yenye wataalam wa uchumi na wa kupanga wanaweka mipango, wanashindwa kutimiza malengo, afadhali mengine wanaweza wakawa wamefika kidogo, inakaribia lakini mengine ni mbingu na ardhi then tuna shida na wataalam wetu. Wakati tunaelekea kwenye Mpango wa Tatu lazima tufanye tathmini, nimesema hivi mimi ni mkongwe unanisoma vizuri, Wabunge hapa wakati wa maswali asubuhi, swali la maji ulitoa maswali ya nyongeza mpaka unataka kutoa maswali ya ziada ya nyongeza huku umesimama lakini mimi niliyekuwepo wakati wa Mpango wa Kwanza huu wa miaka mitano (2011-2016) kati ya mwaka 2012-2014 asilimia 27 ya manunuzi ya nchi yalikwenda kwenye maji. Fedha iliyotumika kwa miradi ya maji kwa CCM hii hii kwa kipindi hicho tu na siyo maneno yangu mimi, ni maneno ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali aliyefanya special auditing akasema kati ya shilingi 2.7 trilioni zilizokuwa injected 49 percent ya miradi haifanyi kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mnapokuja hapa SGR, Stigler’s Gorge, what is that! Ndiyo maana watu wanatushangaa, lazima tu-move. Serikali ikiwa madarakani aidha umechaguliwa au umeingia kiunjanja, ni jukumu lako wewe kuhudumia wananchi. Kuhudumia wananchi siyo hisani viongozi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukianza kuamini na kuwa na mentality kwamba kuhudumia Watanzania ni hisani, ndiyo maana kuna vijana wadogo hapa wanatushangaa tokea wako primary wanaona wazee wazima tunaongelea Stigler’s Gorge, wanakuja secondary wanaona tunazungumzia SGR, wanakuja Bungeni wanakuta ngoma ile ile, wanajifunza nini kutoka kutoka kwetu?

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, (SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Umeshaanza Mheshimiwa Jenista.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Halima Mdee, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Jenista Mhagama.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, (SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, sijui tumsaidieje Mheshimiwa Halima Mdee, hii miradi yote ambayo ya vielelezo, ni miradi ambayo kwa maamuzi thabiti ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi, utashi wa kisiasa wa Rais John Pombe Joseph Magufuli, ndani ya miaka mitano tu ya Serikali yake miradi hii imeanza kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama ilikuwa haijatekelezwa siku za nyuma si imeanza sasa kutekelezwa! Kuanza kutekelezwa kwa miradi hii kunaonyesha ni kwa kiasi gani Serikali ya Awamu ya Tano imejipanga kuleta maendeleo endelevu ya Taifa la Tanzania. Kwa nini Mheshimiwa Halima asikubali jambo hilo? (Makofi/Kicheko)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Halima Mdee, unaipokea taaria hiyo.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza Jenista alikuwepo kwenye Serikali zote hizi, Magufuli alikuwepo kwenye Serikali zote hizi…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Halima Mdee, ngoja kidogo, kwa Kanuni zetu hawa ni Waheshimiwa kwa hiyo wataje vyeo vyao.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Jenista alikuwepo kwenye Serikali zote hizi, Mheshimiwa Magufuli alikuwepo kwenye Serikali zote hizi na Serikali ya Awamu ya Tano iliahidi kwenye Mpango uliopita kupunguza kiwango cha umaskini kutoka asilimia 28 mpaka asilimia 16, mmeweza kupunguza kwa asilimia 2 tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nachotaka kusema hapa mentality ya kufikiria unapotoa ama unapotekeleza wajibu ni hisani, ndiyo haya unafikiria likijengwa daraja pale eti wananchi wa Tanzania wamesaidiwa, hawajasaidia kwa sababu mnakusanya kodi. Ninachowashauri hapa tukiwa tunaelekea Mpango wa Tatu tufanye tathmini tuone tumekosea wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kila mtu anajisifia, ooh, kuna ujenzi, sikiliza miaka mitano ya Mpango huu ujenzi imepewa trilioni 8 sasa kwa nini sekta ambayo mmewekeza trilioni 8 isikue? Hiki kilimo ambacho kila mtu anakizungumzia hapa na jana amezungumza aliyekuwa Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Muhongo kwamba kama tunataka hiki kimuhemuhe cha kusema nchi yetu ni tajiri kiwe reflected kwa wananchi kule chini tuwekeze kwenye maeneo yanayogusa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kilimo average ya kutoa bajeti ya maendeleo ni 17 percent kwa miaka mitano iliyopita. Hotuba ya Mheshimiwa Dkt. Mpango mwenyewe anasema eti miaka mitano kwenye kilimo tumetoa shilingi bilioni 188, hatusemi Serikali ilime, hapana, tunasema itengenezwe miundombinu wezeshi. Nchi hii ina utajiri wa umwangiliaji, hivi tutapoteza nini kwa mfano, hawa wakulima wetu wadogo wadogo tukisaidia kuweka mifumo thabiti ya umwagiliaji? Leo ni aibu asilimia 90…

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, (SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Halima Mdee, kuna taarifa.

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Bashungwa, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Jenista.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, (SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee, Halima ni Mbunge mbobezi na mzoefu na anajua uchambuzi wa bajeti unavyokwenda. Uchambuzi wa bajeti unavyokwenda na unavyopangwa kwa utaratibu wa circle lakini utaratibu wa Serikali, bajeti ya kilimo haihesabiwi kwenye fedha zinazopelekwa kwenye Wizara ya Kilimo peke yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bajeti ya Kilimo, Halima anajua, ningemwomba Halima anapoweka hii hoja mezani aeleze bajeti ya kilimo iliyokuwa budgeted kwenye Wizara ya TAMISEMI, Ofisi ya Waziri Mkuu, achukue bajeti zote za kisekta zinazoenda kuzungumzia sekta ya kilimo kwenye sekta mtambuka fungamanishi, akizichukua zile zote atakuja kupata bajeti halisi ya kilimo ambayo ilikuwa imetolewa na Serikali katika kipindi anachokisema.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Halima Mdee, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, siwezi kuipokea kwa sababu mimi nafanya rejea ya hotuba ya Mchumi mwenyewe wa nchi, Waziri Mpango. Sasa kama Mchumi wa nchi anasema tumetenga shilingi bilioni 188 mimi ni nani? Mheshimiwa Jenista Mhagama ni nani wa kubishana na Mchumi? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nachoshauri kupanga ni kuchagua. Tuna nia ya kusaidia Watanzania wenzetu lazima tuangalie sekta zinazogusa wananchi walio wengi.

MBUNGE FULANI: Muda hauishi? (Kicheko)

MHE. HALIMA J. MDEE: Sekta hii tumeipuuza sana lakini bado kwa heshima kubwa inachangia pato la Taifa kwa asilimia 26.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Halima, hiyo ni kengele ya pili.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa taarifa Mheshimiwa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Gwajima tulia.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa taarifa kabla hajamaliza.

MWENYEKITI: Ngoja, ngoja. Mheshimiwa Halima Mdee, kengele ya pili imeshagonga.

MHE. HALIMA J. MDEE: Sawa namwambia atulie.

MWENYEKITI: Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiwa natoa mchango wangu nitambue mchakato unaoendelea Chasimba, wananchi wangu wameanza mchakato wa kupatiwa hati, kwa hiyo kwa hili mnyonge mnyongeni haki yake mpeni, nampongeza sana Mheshimiwa Lukuvi kwa hili, kwa sababu wananchi wale takribani elfu ishirini walikuwa wanatakiwa kuondoka, lakini sasa hivi wameanza kupata matumaini na wanapatiwa hati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile natambua mradi mkubwa wa Shirika la Nyumba unaoendelea Jimbo la Kawe, eneo lililokuwa la Tanganyika Packers, baada ya mapambano ya muda mrefu, kuokoa lile eneo kutoka kwa wanyang‟anyi wanchache, tumefanikiwa limerudishwa chini ya Shirika letu la Nyumba. Vile vile wako pamoja na mwekezaji, kuna maendeleo wanafanya pale, kwa hiyo na hiyo pia natambua mradi mkubwa unaoendelea pale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutamsifu sana Mheshimiwa Lukuvi hapa, lakini tusipompatia fedha ni sawa na bure, Mheshimiwa Lukuvi mwaka jana bajeti yake ya maendeleo aliyopata bilioni tatu point tano mwaka huu anaomba bilioni ishirini, kumi za nje kumi za ndani. Wakati Lukuvi anaomba hii fedha taarifa ya review ya miaka mitano ya Mpango wa Miaka Mitano inatuambia ni asilimia 10 tu ya Watanzania ama nyumba ambazo zina hati za kimila na hati za kawaida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia 10, miaka 54 baada ya uhuru, tunampa huyu jamaa bilioni 20. Inawezekana ana dhamira njema, lakini hiyo dhamira njema, haiwezi kuishia kwa kutatua migogoro, jukumu la Waziri sio kutatua migogoro, ndiyo maana tuna vyombo mpaka ngazi ya kijiji, huyu anatatua migogoro kwa sababu mfumo umefeli, anakwenda kufanya kazi ambayo kimsingi siyo yake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka 54 baada ya uhuru asilimia 20 tu ya ardhi ya Tanzania, imewekewa mpango, iko planned. Hivi kweli migogoro ya ardhi itakwisha? Hivi kweli wakulima na wafugaji wataacha kuuana. Mtakumbuka miaka minne iliyopita, alipokuwa Waziri mama Tibaijuka nilileta hoja, nikasema sasa hivi tumepewa hivi vitabu, lakini nitawaambia hizi takwimu zilizokuwa humu na uhalisia uliopo kule chini, ni vitu viwili tofauti, tunafanya kuhisia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikasema kwa nia njema kusaidia nchi hii, naomba Mheshimiwa Lukuvi anisikilize na alifanyie kazi, tunahitaji kufanya land auditing, ili tujue kila kipande cha ardhi ya nchi hii kinafanya nini, nani ana nini, kiko wapi, kinafanya nini, mali ya Serikali Kuu ni ipi, mali ya vijiji ni ipi, mali ya halmashauri ni ipi. Ili tukishajua thamani ya kila kipande, tutajua na juu ya kila kipande kuna nini, kuna majengo gani, hayo majengo yanasaidia nini katika uchumi wa nchi. Kwa hiyo, tukitumia fedha nyingi, tukafanya kitu kimoja, kitu kikawa kina tija kwa Taifa; kitajibu kodi ya ardhi, kitajibu mipango ya nchi, kitajibu property tax, tutajikuta biashara ya kuzungumzia mapato haipo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kikaenda kikarudi, zikapigwa danadana, miaka minne baadaye, hakuna kitu kinachoendelea. Sasa swali linakuja Mheshimiwa Lukuvi kazi yakoeitakuwa ni kutatua migogoro? Hivi nikimuuliza leo kama Waziri wa Ardhi ni vipande gani vinafaa kwa ajili ya kilimo cha kumwagilia maji atakuwa anaotea, nikimwambia nani ana nini, atakuwa anaotea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nikimuuliza Mheshimiwa Mwijage hapa anazungumza eti biashara ya viwanda na yeye kwenye ukurasa wa 45, amezungumza utengaji wa maeneo ya viwanda. Tunajua, juzi kwenye hotuba yake ya viwanda na biashara, alivyobanwa kwenye maeneo ya EPZ na SEZ alikuwa anang‟atang‟ata meno. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunaambiwa Tanzania ya viwanda, ardhi ya EPZ ya SEZ karibu hekta 31 hakuna fidia iliyolipwa, elfu kumi ndiyo inafanyiwa tathmini, hiyo elfu kumi Serikali ilitakiwa ilipe bilioni 60, Serikali haina fedha, sasa hivi katika zile elfu kumi Serikali mnatakiwa mlipe bilioni 190, bilioni 130 zaidi. Hivi hizo kweli ni akili jamani, hapo bado zile hekta elfu ishirini na moja bado hazijafanyiwa tathmini. Halafu tunasema oooh Tanzania ya viwanda, ardhi yenyewe huna, hujalipa fidia, Sheria za nchi zinamlinda Mtanzania dhidi ya kulipwa fidia ili aweze kuondoka, tunapigana maneno. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwombe sana Mheshimiwa Lukuvi, tuisaidie hii nchi, tufanye land auditing, let us do that. Tulivyopendekeza aliyekuwa Waziri akaenda akakagua hayo mashamba yaliyokuwepo. Sijui mashamba 964, ekari karibu laki tisa sijui na ngapi mwenyewe anakuja kugundua yale mashamba kwamba kwa wastani wageni wanamiliki ekari, 6,300, wazalendo wanamiliki ekari 280 kwa wastani. Wageni 6,000 wazalendo 200, kwa hiyo tukiwa na hizi taarifa tutajua tunaipeleka wapi nchi, tukiwa hatuna hizi taarifa, tutabakia tu tunafikiria hapa puani, hatufikirii kizazi cha sasa, kijacho na cha kesho kutwa. Nimwombe tena tutasaidia mpango wetu wa kilimo, tutasaidia mipango yetu ya viwanda, tutasaidia mambo ya kodi, tutaweza kuisogeza nchi mbele, tutakuwa na takwimu ambazo ni tangible. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Nyumba, hili shirika tumshukuru kijana wetu ameli-transform, Waswahili wanasema mnyonge mnyongeni, haki yake mpeni na Watanzania tujifunze kuwalipa watu kutokana na uwezo wao wa akili, tuache fikira za kimaskini. Nchi za wenzetu wako tayari kumlipa mtu hela nyingi kama ataweza kurudisha kitu chenye tija, sasa leo tunawalaumu Shirika la Nyumba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitaje tu kodi wanazolipa na naomba nitaje tu, hili shirika tunaambiwa wajenge nyumba za maskini. Asilimia 10 ya mapato yao ya mwaka yanatakiwa yapelekwe Mfuko Mkuu wa Hazina, wanatakiwa walipe kodi ya makampuni asilimia 30, wanatakiwa walipe gawio milioni 300, wanatakiwa walipe riba ya mikopo wanayojengea asilimia 16 hakuna cha ruzuku ya Serikali. Wanatakiwa walipe kodi ya ardhi, kodi ya jengo, kodi ya zuio, kodi za Halmashauri Civil Service Levy, kodi ya VAT, hawa hawa wananunua ardhi kwa bei ya soko, hivi kutakuwa kuna nyumba ya bei nafuu hapo? Hakuna! Wenzetu huko mnakokwenda kutembea kila siku, haya mashirika yanawezeshwa na Serikali zao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu huko mnakoenda kutembea kila siku haya mashirika yanawezeshwa na Serikali zao kama kweli hizi lugha mnazosema, tunataka ooh, tusaidie maskini, Waziri atujibu hapa, ana mpango gani wa kupunguza huu mzigo kwa shirika, ili hao maskini wasaidiwe tunaojifanya tunaimba kwa maneno wakati kwa vitendo hatulisaidii Shirika letu. (Makofi)
Mheshimimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri, tuwape moyo lakini tuwasaidie huu mzigo wote wa haya makodi kumi niliyoyataja hapa, yote yanabebwa na mlaji. Mwaka 2014 hawa mapato yao ya mwaka yaliyokuwa bilioni 176 ukitoa tu asilimia 10 ya withholding wanatakiwa wapeleke Serikalini bilioni 17, wanasema ile pesa walioipeleka Serikalini walikuwa na uwezo wa kupata mkopo wa bilioni 101 ya kujenga nyumba nyingine. Yaani badala mfikirie vyanzo vipya vya kodi mkiona tu amekuwa creative pesa zinaingia mnataka mvune, hebu jiongezeni basi. Nimewaambia fanyeni land auditing, msifikirie uchaguzi, yaani shida yetu sisi Watanzania huwa tunawaza uchaguzi na tukiwa tunafanya mambo kwa kuwaza uchaguzi tutakuwa tunawaza puani, hatuwazi mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri asijali hata kama itam-cost ten million kufanya auditing nchi nzima, anaweza akaziagiza hata halmashauri kwa sababu ndiyo maana tunakuwa tuna mfumo wa utawala, aagize halmashauri tunataka mtupe taarifa kwenye halmashauri zenu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naomba nawakilisha.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, na mimi mchango wangu utaongezea yale ambayo yamezungumzwa kuhusiana na dawa za kulevya; na nitarejea ukurasa wa saba na wa nane wa taarifa ya Kamati, naomba kunukuu inahusiana na mwenendo wa bajeti ya Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya, ukurasa wa saba unasema; “Hata hivyo katika kipindi cha mwaka 2015/2016, 2016/2017 bajeti za Tume zilishuka hadi kufikia sifuri kwa miradi ya maendeleo kwa mwaka 2016/2017 kutokana na ukomo wa fedha za wafadhili na kubadilika kwa vipaumbele vya Bajeti ya Serikali.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati hotuba ya Kamati inasema haya leo Mheshimiwa Rais wakati anamuapisha Mkuu wa Majeshi amesema kinaga ubaga kwamba anaunga mkono vita ambayo kwa mtazamo wake yeye imeanzishwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam na kwamba hakuna atakayepona na kwamba wote wawekwe ndani na haangalii umaarufu. Ifike kipindi hii nchi yetu tuache kuiendesha kwa sanaa. Ninarudia, ifike kipindi hii nchi yetu tuache kuiendesha kwa sanaa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya mwaka 2016/2017 ambayo Rais Magufuli anayetoa tamko la kumuunga mkono Makonda ndiyo alikuwa ameshakuwa Rais; bajeti ya maendeleo ni sifuri, na bajeti ya maendeleo ndio tunatarajia ikafanye hizi shughuli; leo anasimama Ikulu anadai eti anaunga mkono hii vita. Isipofika kipindi kama nchi tukaamua kutembelea ama kusimamia maneno tunayoyasema ama kutembelea kauli zetu haya majanga hayawezi kuisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, President Nickson mwaka 1971 wakati anaanzisha vita dhidi ya madawa ya kulevya Marekani mpaka sasa Taifa la Marekani limetumia si pungufu ya dola trilioni moja na bado wanapambana. Kwa mwaka mmoja Taifa la Marekani linatumia sio pungufu ya dola bilioni moja angalia GDP yetu halafu linganisha na dola bilioni 51; lakini vita bado ni kubwa. Leo bajeti sifuri halafu anasimama mkuu wa nchi anasema eti vita ipiganwe; tutapigana kwa viboko? Tutapiganaje? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwahiyo ifike kipindi tuache kutafuta headlines na tuache kucheza na vichwa vya Watanzania kwa kutengeneza headlines kwa sababu hii vita si ya jana, si ya leo na wala si ya juzi na wala si ya mtu mmoja.
Kwa hiyo, lazima tuwe na political will na dhamira ya kisiasa haipimwi zaidi ya kwenye maandiko, huna pesa huwezi kufanya kitu, tuache usanii, tuache sanaa na tulisaidie hili Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ninyi hatuwaji wauza unga sisi? Hatuwajui wanaoagiza unga sisi? Si ndio wanaotuchangia kwenye kampeni sisi? Hatuwajui? Si ndio tunakula nao sisi? Si ndio tunalala nao sisi? (Makofi)
Leo tunaenda tunakamata vitoto vya watu eti vinatumia unga; Rais anasema kamateni hao watumiaji watatusaidia kutuambia wanaouza, mzee kama hawajakwambia ukweli inawezekana kampeni zako ulichangiwa na hawa watu, hii vita ni kubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, inawezekana Rais amezungukwa na watu ambao anadhani anawaamini, mimi naamini hili Baraza lina watu makini, lakini naamini kuna watu anaowasikiliza zaidi na wengine anawapuuza. Tuanze kupima na kuangalia Rais anazungukwa na watu gani. Kwa hiyo, kama leo kwa sababu kuna mtu amesema hapa inawezekana Rais ametuma tu, labda Makonda ndiyo msemaji wake siku hizi anaambiwa tangulia halafu mimi nafuata, kwa sababu haiwezekani ikawa ni coincidence. Yaani anatokea anasema kitu halafu Mzee anafuata! Hii vita if we are serious, waliokuwepo kwenye Bunge lililopita, mnakumbuka Mheshimiwa Lukuvi alipokuwa Waziri anayeshughulika na masuala ya Bunge, alituingiza kule akatuonesha sinema, anasema watu wanawajua, iko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kikwete alisema anawajua na sisi tunaamini Rais akiondoka Ikulu mafaili yanabaki Ikulu, kwa hiyo, tusikimbie vivuli vyetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais John Pombe Magufuli na wasaidizi wake mnanisikia, list ya waagizaji siyo watumiaji, waagizaji, wafanyabiashara wa dawa za kulevya wanaotuma watu huko nje unayo Ikulu, tunaomba fanyia kazi list iliyokuwa Ikulu, tusicheze na akili za Watanzania kwa kutafuta headlines.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kila siku tunakwepa masuala ya msingi, wanaona uchumi unadorora wanamwambia mzee toka na hiki ili tu-divert minds za Watanzania, wanaona kuna njaa wanasema toka na hiki tu-divert akili za Watanzania, msitupotezee muda. Mmepewa hii nchi kwa dhamana, more than 50 years now, jana wametimiza 40 years kama chama, watu wazima yaani 40 years maana yake mtu mzima, shababi. Tu-behave kama watu wazima, tulisaidie hili Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba, niambiwe kabisa na Waziri wa Afya, kwa hizi mbwembwe mnazoanza hizi, hii kutoka zero itakuja ngapi ili tuweze basi kuanza kupambana na hili tatizo. Akina Amina Chifupa walizungumza sana humu wakaja akina Mheshimiwa Ester Bulaya na hoja zao binafsi wakaungwa mkono na Waziri Mheshimiwa Jenista, tukatunga sheria, sheria ukiisoma ni kali kwelikweli, na ile sheria ukiisoma between the lines inalenga wale mashababi, ambao inawezekana wengine, ndiyo maana yule dogo alikuwa yuko Marekani siku 20, hakuna anayejua nani kamfadhili Marekani siku 20, hana ubavu wa kuishi Marekani siku 20. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana hawa wauza unga ndiyo wanampeleka huko, anakuja anamkamata Wema, Wema kweli! Alizunguka na ninyi kwenye kampeni mlikuwa hamjui, alikuwa na Makamu wa Rais miezi mitatu, sijui Mama na Mtoto, mkapata kura za ma-teenagers kwa kumpitia huyo dogo. Kwa hiyo, siku zote yuko na Makamu wa Rais kumbe ananusa kitu Makamu wa Rais hajui, acheni usanii. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetumia muda wangu mwingi kulizungumzia suala hili, nirudie tumuogope Mungu, tuache usanii. Tunadhamira ya kuwasaidia watoto wetu hawa, tuwasaidie watoto kwa kuwapa tiba tukamate majambazi na majangili wanaoharibu Taifa letu, tumechoka maneno, tunataka vitendo sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la HIV…….
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Mdee.
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwanza niungane na hoja ya mwisho ambayo amezungumza Mheshimiwa Matiko kuhusiana na Bandari ya Bagamoyo, lazima ifanywe uchunguzi wa kina wa kimkataba ili kama mkataba uliopo huko kwa lugha ambayo hayati Magufuli alizungumza ambaye alikuwa ni Rais highest authority then. Kwa hiyo, niungane na wewe kwamba lazima kama Taifa, tutulie, tuweze kufanya uchambuzi wa kina, tuje na kitu kitakachosogeza Taifa mbele, hilo la kwanza.

Mheshimiwa Spika, nasema hivyo kwa nini, majuzi CAG kazungumza kuhusiana na ATCL, nimesoma hapa kuhusiana na usafiri wa anga, taarifa Mheshimiwa Mwigulu, anasema tulikuwa tuna ndege moja katika utekelezaji huu wa mpango, sasa hivi tuna 11, lakini tulivyokuwa ndege moja miruko ya ndege ndani na nje ilikuwa 225,000 mwaka 2015, maandiko ya Waziri wa Fedha. Tulivyokuwa na ndege 11 miruko imekuwa 292,105 ndani ya miaka mitano. Kwa hiyo tumetoka ndege moja kuja 11 katika kipindi cha miaka mitano tulichofanikiwa ni miruko yaani ndege kuruka ni elfu 67 pekee. Sasa vitu kama hivyi vinakupa swali ama tathmini ndogo tu. Naomba tuangalie abiria waliosafiri walitoka 4,207,000 mpaka 4268,000, ndege moja as against ndege 11, maandiko ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha. Sasa kama kulikuwa kuna walakini atakuja kuyasema yeye.

Mheshimiwa Spika, wakati tunahoji uwekezaji wa fedha kwenye shirika la ndege sio kwamba tulikuwa hatutaki shirika letu lifufuliwe, tulisema uangaliwe upungufu ambao umezungumzwa na wataalam. Wakati tunatoa fedha mara ya kwanza 2016, mara ya kwanza tumetoka kwenye ripoti ya CAG Utoh wakati huo, ameelezea masuala ya msingi zaidi ya 15 juu ya ubovu wa ATCL, akapendekeza yafanyiwe kazi kwanza, hatukuyafanyia kazi tukaanza ku-inject five hundred billion, miezi mitatu kabla ya taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Msajili wa Hazina akaenda akatoa taarifa PIC, akasema shirika hili hali ni mbaya, halina mpango wa biashara, kama uliandaliwa ulikuwa ni wa kukurupuka, haina mpango wa uwekezaji kama ulikuja kuandaliwa ulikuwa ni wa kukurupuka, halina mahesabu, halijafanyiwa mahesabu; hali ya shirika haijulikani kwa sababu hakuna ukaguzi wa kimahesabu uliofanywa. Tumezungumza hapa kama ndugu zangu kama nyie hapo wakapiga makofi wakasema hewala.

Mheshimiwa Spika, CAG Profesa Assad ripoti yake ya kwanza, huyu wa juzi amesema hasara ya miaka mitano, Profesa Assad ripoti yake ya kwanza baada ya kuteuliwa kuwa CAG alisema shirika limepata hasara kwa miaka kumi mfululizo. Sasa Waheshimiwa Wabunge, tukiwa tunapanga vitu kwa ajili ya Taifa hili, tuangalie namna njema ya kulisaidia. Leo hii ripoti ya juzi…

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa ipo upande gani? Sawa, nimekuona.

T A A R I F A

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba, tunapokuwa tunajaribu kuangalia performance ya shirika la ndege mara nyingi sana huwa hatuangalii number of tourists ambao wamesafiri kutoka sekta moja kwenda sekta nyingine.

Mheshimiwa Spika, tunapojaribu performance ya shirika la ndege mara nyingi tunajaribu kuangalia amount of money which has been spends by the tourists katika sekta moja mpaka sekta nyingine katika kipindi cha mwaka. Kwa mfano, sisi Tanzania tunajua katika kipindi cha mwaka 2015 tuliweza, watu waliweza kuja na kutumia fedha walitumia fedha dola milioni moja, milioni mia tisa na ishirini na nne mwaka 2016 dola bilioni mbili milioni mia moja arobaini na tisa mwaka 2017 dola bilioni mbili, milioni mia mbili na sitini na tano elfu, mwaka 2018…

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, sasa nilichotaka kuwa kusema ni kwamba tusije kupoteza Taifa…

SPIKA: Ahsante. Taarifa inakuwa fupi.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, ahsante.

SPIKA: Ahsante sana, nafikiri umeeleweka. Unaipokea taarifa Mheshimiwa Halima.

MHE. HALIMA J. MDEE: Tatizo la hawa manjuka, ndio maana nawaambia watulie, unajua ukiwa form one inabidi utulie kwanza. Nimesema hapa kwamba hakuna anayepinga shirika la ndege kufanyiwa ama kuwekewa fedha, hakuna anayebisha…

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa Mheshimiwa Musukuma.

T A A R I F A

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, kuna kauli ameitumia Mbunge mwenzetu ya njuga, sasa sisi wengine tunatoka kijijini, sijui njuga ni nini, hatuelewi labda afafanune.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa…

SPIKA: Haina shida Mheshimiwa Msukuma unajua yeye ni darasa la saba, sasa hii lugha hawezi kuielewa kidogo. Endelea Mheshimiwa Halima.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru njuka ni form one, sasa Msukuma si unajua ameishia darasa la saba mwanangu. Kwa hiyo njuka ni form one, hukufika kule.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunachofanya hapa, ni kujaribu kusaidia yaani huwa nawaambia watu sisi ni Watanzania, tunaishi Tanzania, pasipo kujali umetoka chama gani, yaani vyama ni njia ya kusaidia Taifa, kwa hiyo tukizungumza tusionane maadui.

Mheshimiwa Spika, ninachosema taarifa ya Kichere ambayo watu wanajifanya wanaifanyia rejea na wengine kutoka huko sio mambo mapya. Yalizungumzwa CAG Bwana Utoh aliyazungumza, CAG Profesa Assad, tena Profesa Assad aliyazungumza kipindi ambacho ndio tumekuja hapa na Serikali inatuambia jamani tutenge bilioni mia tano, tunafufua ndege. Kazungumza hapa Mheshimiwa Aida, ni muhimu as a nation tuwe na vipaumbele vinavyo tu-guide ili CCM ikichukua sawa, ACT ikichukua anakuwa guided, CHADEMA ikichukua anakuwa guided. Sasa leo tunapanga kipaumbele kilimo, kesho Alhamdulillah Mheshimiwa Jenista anakuwa Rais, anakuja hapa anasema, mie nadhani nilikuwa napenda sana ndege nilivyokuwa mtoto, hapana. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, tuweke kuji-guide, tutafanya mambo na kuweza kuyamaliza ndio hoja waliokuwepo wanajua kama sio wanafiki, suala la ndege halikuwa priority namba moja, you know it, tulikuja tu tukalichomeka, leo tunaambiwa trilion 1.2 zimemwagika, CAG anatuambia shirika lina madeni ya bilioni 412, this is…

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa nilikuwa ninaishauri Serikali na namshauri Waziri wa Fedha…

SPIKA: Mheshimiwa Mpembenwe tena, Mheshimiwa Halima kaa, kuna taarifa.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, pamoja na u-form one uliyepo, nataka kusema tu sisi Wabunge tusijekupoteza wananchi. CAG sisi ndio tumempa kazi na kazi tuliyompa ya kwenda kuangalia mashirika tofauti, hasara iliyokuwa imepatikana, naomba nimpe tu taarifa mzungumzaji ni kwamba, shirika ambalo lina-operate kwa hasara kubwa sana Afrika kwa sasa hivi ni shirika letu ambalo ni majirani zetu hapo karibu wa Kenya, lakini kwa nini hawapigi kelele kuna sababu.

Mheshimiwa Spika, kwenye economics kuna kitu kinaitwa complimentary goods. Mheshimiwa Rais Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli wakati amechukua maamuzi ya kununua ndege hizi tafsiri yake ni kwamba alikuwa anaenda ku-compliment na sekta nzima ya mambo ya tourism na ndio maana tourism sekta kwetu sisi imepanda sawasawa na watu wa Kenya tourism sekta ilivyokuwa imepanda japokuwa wanapata hasara. Ahsante sana.

SPIKA: Mheshimiwa Halima, pokea taarifa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Nafasi za uteuzi zimejaa. CAG ameambiwa aseme ukweli kulisaidia Taifa, CAG amesema shirika la ndege halifanyi kazi vizuri, lazima tuliangalie, tuangalie watu wameshauri nini, ndege zishakuwa hapa, hatuwezi kusema tukazitupe ama kuzichoma moto, tuangalie kwa makini tujirekebishe pale tulipojikwaa.

Mheshimiwa Spika, tunasema haya kwa nini? Unajua, nilikuwa nasikiliza hapa Wabunge wachanga, tunakaa tunajiaminisha eti miradi tunajenga kwa hela zetu za ndani my friend nchi yenu inakopa, kukopa sio tatizo, lakini kopa wekeza kwenye miradi ambayo…

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Namtafuata anayesema taarifa.

MHE. ELIBARIKI I. KINGU Nipo hapa, Kingu.

SPIKA: Haya bwana endelea, Mheshimiwa Kingu.

T A A R I F A

MHE. ELIBARIKI I. KINGU Mheshimiwa Spika, pamoja na mchango mzuri wa dada yangu hapa Halima, lakini naomba nimpe taarifa ifuatayo: -

Mheshimiwa Spika, most ya carrier za mataifa mbalimbali hasa kwa Afrika, kazi ya mashirika ya ndege mengi duniani ukisema ripoti za shirika linalosimamia mashirika ya ndege duniani, kazi kubwa ya mashirika ya ndege duniani ni kuchochoa uchumi mwingine, si lazima kutengeneza profit. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukienda na mentality ya kutegemea ATC siku moja itengeneze faida tukataka ku- discourage juhudi zilizofanywa za kufufua shirika la ndege tutakuwa hatulitendei haki Taifa la Tanzania. Natoa mfano, Kenya Airways mwaka 2016 na 2017 ilirekodi loss ya dola millioni 249, mwaka uliofuata wa 2018 wakapata loss kutoka dola milioni 249 kwa asilimia 51 zikaenda dola 97 milioni, hasara. South African Airways…

SPIKA: Malizia taarifa yako.

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Spika, South African Airways mwaka 2017 shirika la ndege la South Africa lili-accumulate loss ya dola milioni mia moja hamsini na tatu, lakini uchumi mwingine kwa mashirika haya ulikuwa unachochowewa. Naomba tusibeze juhudi za kufufua ATCL.

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Ahsante kwa taarifa, nafikiri ataipokea taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Halima taarifa hiyo.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, ninavyomwona senior naye anaingia humohumo, unakuwa unaona kwamba naye dogo anataka kupotea.

Mheshimiwa Spika, ni hivi ndege tukianza kuzungumza katika zile ndege zilizo-park pale airport tukiuliza tu kati ya hizo nane zilizopo au 11, ngapi zinaruka tutaanza kupotezana. Wamenunua ndege, hawana business plan zina-park pale. Kwa hiyo ndege ziki-park kama hasara kama hii inazungumzwa, lazima mtoe justification kwa nini hasara kama hii inapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tusitake kwenda huko wala tusipotezeane muda, wataalam waliochaguliwa na Rais wamesema tumekurupuka kwenda kudandia treni kwa mbele wakati hatujajiandaa, hilo ndilo tatizo. Inawezekana tungejiandaa, sisi tungekuwa ni mifano yaani Kenya ingekuwa inaturejea sisi, South Africa ingekuwa inaturejea sisi, yaani wewe unajivunia vipi kuanza kufanya rejea failures, yaani unajivunia vipi, kwa nini usijivunie kwamba umejipanga vizuri wale failures wanakutumia wewe kama rejea. CAG amezungumza, mama Samia amesema, CAG funguka, maana yake mama Samia kawaambia na nyie fungukeni, acheni unaa, tulisaidie Taifa.

Mheshimiwa Spika, deni la Taifa linakua kwasababu, kwa makusanyo wanayokusanya TRA tunaweza kufanya mambo makubwa matatu; tunaweza tukalipa deni lenyewe, tunapitisha hapa trilioni nane mpaka kumi, tunaweza tukalipa mishahara watumishi kwa mantiki ya wage bill; tunaweza tukalipa OC – matumizi ya kawaida ya ofisi ili watu waweze kwenda ofisini. Ukiacha mambo makubwa hayo matatu, TRA ama sisi kama Taifa kama kuna salio linabaki labda trilioni moja, tukijitutumua sana trilioni mbili. Kwa hiyo mkija kupitisha hapa trilioni 36 mjue kwenye 36, 22 ndiyo tuna uwezo nazo, 12 tunakopa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwa kuzingatia kwamba miradi yetu ya maendeleo tunaendesha kwa mikopo ndiyo maana tunatoa mapovu hapa. Tufanye vitu vyenye tija. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninyi mnajua wakati Dkt. Magufuli anaingia mwaka 2015 – Mungu amlaze mahali pema peponi Mheshimiwa Rais – deni la Taifa lilikuwa 41 trillion. Now, Ripoti hii ya BOT ya Februari, 2021 deni la Taifa ni trilioni 71, public and private. Kwa mantiki hiyo – msije mkasimama hapa mkaanza kusema tunajenga kwa hela zetu, hakuna hela, tena tunakopa mikopo ya biashara. Kwa hiyo, kila jambo tukilipitisha hapa tulipitisha kwa wivu mkubwa kwa kuangalia kizazi cha sasa na kijacho.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunivumilia. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi hii, la kwanza, mchango wangu utajikita kwa Taarifa ya Kamati ya Katiba na Sheria, kuhusiana na Hifadhi ya Jamii na niipongeze sana kamati kwa kufanya kazi nzuri na nitaongezea hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mifuko ya Hifadhi imeanzishwa sababu moja kubwa, ni kuangalia mustakabali wa wafanyakazi wetu pale wanapokuwa watu wazima na kustaafu na kulinda maslahi yao baada ya umri wa kustaafu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naamini mifuko hii iliwekwa chini ya ofisi ya Waziri Mkuu, kwa kutambua nafasi ya Waziri Mkuu mwenyewe na unyeti wa mifuko hii na ikitarajiwa, Waziri Mkuu pamoja na wasaidizi wake waweze kusimama kidete, ili kulinda mifuko kwasababu ukilinda mifuko, umelinda watumishi wa Taifa hili. Tunavyozungumza Hifadhi ya Jamii na hii Mifuko maana yake tunazungumzia watumishi wa sekta ya umma na tunazungumzia watumishi wa sekta binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mifuko huwa inafanya uwekezaji, na mifuko duniani kote inawajibu wa msingi wa kuisaidia Serikali kuweza kushiriki katika shughuli za maendeleo. Hilo halina ubishi duniani kote, lakini, changamoto iliyokuwa hapa kwetu Tanzania na ambayo ninaomba sana, Mheshimiwa Jenista utujibu sio umjibu Halima hapana, jibu wafanyakazi wa Taifa hili ili wapate matumaini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninasema hivi kwanini? Mifuko inawekeza katika mazingira mawili, zingira la kwanza kuikopesha Serikali na Taasisi zake kwa riba. Serikali inakopa kwa ajili ya kuingiza kwenye shughuli za maendeleo inadhamini Taasisi zake zinakopa, inatakiwa ilipe kwa riba. Lakini la pili, inashiriki katika uwekezaji kwenye maeneo mbalimbali ya ujenzi ama wao binafsi ama kwa kushirikiana na Sekta Binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mdudu mkubwa, donda ndugu, zito, ilililo sugu kabisa ni upande wa Serikali. Pesa inazokopa, inazotakiwa ilipe kwa riba, pesa ambazo Serikali inadhamini taasisi zake zikope kwenye Mifuko ya Hifadhi ambayo inatakiwa ilipe, hailipi! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 2018, mtanisahihisha kama nimekosea, tuliunganisha mifuko tukaambiwa kwamba hii mifuko inaunganishwa ili ufanisi uwe bora zaidi. Nimeona hotuba ya Waziri Mkuu imesema wamepunguza gharama za uendeshaji, yes! Lazima ipungue kwa sababu watu wamekuwa wachache, mifuko ni miwili lakini usugu upo! Zile fedha mlizokopa mna kigugumizi gani kurudisha? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Ester Bulaya amezungumza juzi, kwamba madeni yale ya kawaida kwa taarifa zenu wenyewe kupitia Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ni 2.7 trilioni. Pia mnafahamu kuna fedha zingine shilingi trilioni 7.1 ambazo pia PSPF walipewa jukumu kulipa wastaafu ambao walikuwa wamekidhi umri lakini hawajachangiwa, almost ten trillion! Kwenye mifuko hatulipi. Kama Serikali ina uwezo kila Mwaka wa Fedha kutenga shilingi trilioni 8 mpaka 10 kulipa madeni ya nje ya Serikali ama ya mabenki, tuna ugonjwa gani kushindwa kutenga hata shilingi trilioni moja moja basi kila mwaka tuisaidie mifuko yetu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bahati mbaya sana na inauma madeni mengine yalikuwa yameiva toka 2007, 2008, 2010, 2014 Serikali inatoa ahadi hapa, haitekelezi! PSPF ikachoka, ikafilisika, tukaunganisha ili kuziba mashimo. Hatuwezi kwenda hivi!

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi niombe…

T A A R I F A

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Taarifa, Mheshimiwa Kimei.

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, mimi ningeshukuru au ningemuomba Mbunge anayezungumza aelewe kwamba Serikali ni mdhamini wa mifuko hii. Serikali ina namna nyingi ya kupata fedha wakati wowote, hawezi kusema kwamba hii mifuko imefilisika. Haiwezi kufilisika kwa sababu Serikali ina uwezo wa kutengeneza fedha saa yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nataka nimhakikishie kwamba deni analosema yeye hamna tofauti na deni ambalo linalipwa kwa wakati na Serikali ina namna yake kwa sababu inaweza ikatu-tax sisi saa yoyote ile. Kwa hiyo, hakuna sababu ya kuogopa kwamba iko siku Serikali itashindwa kulipa hiyo mifuko. Hivyo ndivyo ilivyo duniani kote kwamba fedha ya mifuko inatumika na njia salama kabisa kutumia fedha ya mifuko ni kwa Serikali kutumia zile fedha kwa kufanya miradi ya muda mrefu.

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, niseme kwamba Serikali haikosei chochote.

SPIKA: Ahsante sana. Taarifa hiyo ipokee Mheshimiwa Halima.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, ninamheshimu sana Mheshimiwa Kimei na ametumikia nchi hii muda mrefu sana. Sitaki kumjibu kwa sababu nikimjibu naweza, ngoja niendelee. (Makofi/Kicheko)

MBUNGE FULANI: Msamehe.

MHE. HALIMA J. MDEE: Namsamehe. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, niseme hivi, Serikali imekopa fedha, iliingia makubaliano na mifuko, tutakopa hizi fedha, tutarudisha ndani ya muda fulani, tutakopa hizi fedha kwa kuzidhamini taasisi tutarudisha ndani ya muda fulani tena kwa riba. Navyozungumza Mkurugenzi mstaafu mpaka sasa
Serikali inadaiwa zaidi ya shilingi trilioni 10 kwa vitabu vyenu wenyewe! Sasa hiyo shilingi trilioni 10 basi hata lipa kidogo kidogo watu wapate matumaini, hulipi unakauka tatizo ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunajenga nyumba moja, yaani wala tusigombee fito. Tunawakilisha wastaafu wa nchi hii. Leo Mbunge aniambie kwenye Jimbo lake sasa hivi kutokana na Serikali kutokurudisha fedha, kuna matatizo makubwa sana kwa wastaafu kulipwa ndani ya muda. Zamani ilikuwa mtu anastaafu, ndani ya miezi sita pesa zimeshaingia. Sasa hivi kuna wengine wanastaafu mpaka wanakufa fedha hazijaingia. Hii mifuko ingekuwa ina hela mambo yangeenda mswano. Nashauri Mheshimiwa Kimei akasome…

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mzee naomba utulie basi. Please!

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, Taarifa tena. Hilo analosema lote ni sehemu ya Deni la Taifa.

SPIKA: Mheshimiwa Kimei sijakuruhusu bado. (Kicheko/ Makofi)

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi nachoshauri…

SPIKA: Sasa nakuruhusu Mheshimiwa Kimei.

WABUNGE FULANI: Aaaaa. (Kicheko)

T A A R I F A

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nataka nimuelimishe kwamba hilo analosema kwamba Serikali haijalipa ni sehemu ya Deni la Taifa ambalo kila siku tunasema linakua. Ukweli ni kwamba Deni la Taifa ni kidogo sana kwa sababu ya assets Serikali ilizoweka. Net worth ya Serikali ni kubwa hasa ukiangalia miradi hii ya muda mrefu ya kujenga reli, kununua ndege na kadhalika hizo ni assets zipo. Ukweli ni kwamba ukiondoa liability na assets tulizonazo ni kama zina-balance. Kwa hiyo, hakuna tatizo. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Halima pokea Taarifa hiyo, hakuna tatizo.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, napokeaje? Tatizo lipo kwa sababu yeye anasema haya madeni ni sehemu ya Deni la Taifa, si ndiyo? Deni la Taifa hapa kila mwaka na mtaona kwenye bajeti ya mwaka huu maana naye ni mpya, sitaki kutumia lile jina lingine, utaona katika bajeti ya mwaka huu tunatenga shilingi trilioni 8 mpaka 10 lakini ujiulize…

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri nimekuona, Taarifa.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Spika,
nilikuwa nafikiri kwamba ningesubiri wakati wa kujibu hoja na nilikuwa nimejipanga kutoa maelezo ambayo yangeweza kusaidia Bunge lako Tukufu na wafanyakazi kuendelea kuwa na matumaini na usimamizi wa sekta kiujumla.

Mheshimiwa Spika, kwa ufupi lakini nitakuja kutoa maelezo baadaye, tunakubaliana na utaratibu wa Kiserikali wa CAG (Mdhibiti wa Fedha za Serikali) kufanya ukaguzi na kutoa taarifa ya hali ya sekta zote ikiwemo sekta hii ya Hifadhi ya Jamii. Hayo madeni anayoyasema Mheshimiwa Halima, yako madeni ambayo yana uhalali, yanajionesha wazi lakini anapoongeza yale madeni mengine yanayofika karibu kama shilingi trilioni kama saba anazozisema nadhani angerudi akafanye uhakiki vizuri.

Mheshimiwa Spika, lakini nachotaka kusema hapa tulipoamua kufanya merging ya mifuko ilikuwa ni kazi ya Serikali kwa sababu iligundua kuna tatizo kwenye sekta na ndiyo maana ikaamua kufanya merging ya mifuko. Kama Serikali iliona kuna tatizo na kufanya merging nadhani ilikuwa ni hatua mojawapo ya kusaidia na anachokizungumza Halima ni ile pre 99 ili isiue sekta nzima ya hifadhi ya jamii.

Mheshimiwa Spika, naomba nikuhakikishie sasa hivi tumeamua kutekeleza takwa la kisheria la kufanya actuarial ili kupata taarifa sahihi za hali ya mifuko jinsi ilivyo. Actuarial ndiyo itakayotusaidia kujua hali ya mifuko na nini kifanyike kwenye madai, madeni na kuboresha sekta ili iweze kuwa sustainable.

Mheshimiwa Spika, kwa hali ya haraka haraka tu, wastaafu wa PSSF ambao ni takriban kama 132,670 wamekwishakulipwa mafao na tulitoa taarifa kwenye Kamati. Tunabakiwa na hayo madeni ya nyuma ya wastaafu kama 6,793. Kwa hiyo, hao sasa ndiyo tunaendelea nao. Juzi Hazina wametupa shilingi billioni moja ili tuweze ku-clear hawa wengine waliobakia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo matatizo yapo lakini yako manageable kwa sababu Serikali inasimamia na kuhakikisha kwamba inatafuta suluhu.

SPIKA: Ahsante. Mheshimiwa Halima, pokea Taarifa hiyo.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Jenista amesema anakubaliana na lile la shilingi trilioni 2.7, hili la shilingi trilioni 7.1 ana mashaka nalo. Namshauri mambo yafuatayo, nenda kasome Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali ya mwaka 2013/2014 labda nirejee. Ukurasa wa 96, inasema hivi; kwa mujibu wa Ripoti ya Kikosi Kazi na Ripoti ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali TK/02/Januari 2015 ya mwaka unaoishia tarehe Juni 2013, Deni la Serikali ni shilingi za Kitanzania, kwa kipindi hicho kabla halijafika sasa hivi shilingi trilioni 2.7 lilikuwa shilingi trilioni 1.8. Anasema deni hilo halijajumuisha jumla ya shilingi za Kitanzania trilioni 7.1 ambalo ni deni la Serikali linalodaiwa na PSPF tangu 1999 ambapo PSPF iliwalipa mafao wastaafu waliokuwa hawachangii lakini wanatakiwa kulipwa mafao kwa mujibu wa sheria. Hii ni kwa mujibu wa Taarifa ya Mkaguzi Mkuu na hizi shilingi trilioni 7.1 hamjawahi kuzilipa. Mimi ni mkongwe nimekuwa kwenye hili Bunge na ripoti hizi za CAG ni endelevu. Hamuwezi kutuambia ripoti ya mwaka huu inaziba ile nyingine wakati hamkutekeleza ile nyingine. (Makofi)

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Spika, Taarifa ndogo.

SPIKA: Mheshimiwa Halima, Mheshimiwa Waziri amesimama tena.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Spika,
nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Halima kwamba hiyo ripoti amesema ni ya mwaka 2013/2014. Ndiyo maana tuliamua mwaka 2016, 2017 na 2018 ili kuhakikisha kwamba tunaondoa tatizo la pre 99 hiyo anayoizungumza kwa kufanya merging. Unapofanya merging unaunganisha mifuko, assets zote na kila kitu. Ukishaunganisha hiyo mifuko inakusaidia sasa ku-treat yale matatizo ambayo yalikuwa siku za nyuma. Mheshimiwa Halima essence ya kufanya merging ilikuwa ni sustainability ya sekta kwa kuzingatia hiyo pre 99 ambayo umesema ni Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nachotaka kumshauri, aache tufanye hiyo actuarial valuation, itatusaidia kujua hayo yote yameshafanyika kiasi gani? Naomba niliambie Bunge lako Tukufu tayari PSSF imeshafanyiwa utathmini na ripoti sasa hivi ndiyo inaletwa Serikalini ili iweze kusomwa na kuona hayo mawanda yote na namna sasa ya kuweza kuitendea kazi ripoti hiyo.

SPIKA: Mheshimiwa pokea taarifa hiyo.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, namshukuru Waziri kukiri kwamba ile shilingi trilioni 7.1 ilikuwepo lakini yeye anafikiria kwa ku-merge ndiyo unaondoa tatizo. Unapo- merge kitu unachukua zile assets na liabilities. Sasa moja kati ya liabilities zilikuwa ni madeni ya shilingi trilioni 7.1. Jamani, kiroho safi tu, yaani mimi hapa wala sina beef na mtu, nachotaka ni tuangalie kwa namna gani mifuko yetu hii, nakiri kwamba Serikali haiwezi kulipa kwa mkupuo lakini basi turudishe kidogo kidogo ili kuifanya iwe sustainable. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, leo Kamati inatuambia, kuna miradi ya ujenzi zaidi ya minne ya Tungi, Tuangoma, Kijichi, Mzizima I na II ambayo inagharimu shilingi bilioni 495 za wastaafu wetu watarajiwa zimekuwa injected ile miradi imeshindwa kuonesha multiplier effect. Nyumba zimejengwa, hakuna nyumba iliyouzwa tunaishia kupangisha tena tunapangisha bila mikataba ambapo haikuwa lengo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo kaka yangu Wakili kapendekeza tunaomba kuja na mkakati tufanye mortgage financing, tushirikiane na BoT ambayo ndiyo ina jukumu la kusimamia masuala ya uwekezaji kwa kushauriana na hii mifuko. Tushirikiane na BoT na mabenki, uzuri Tanzania tuna sheria ya mortgage financing, tufanye huo utaratibu, wananchi waweze kukopeshwa na mabenki kununua zile nyumba, zile nyumba zitumike kama collateral. Jambo limeshatokea kama tulivyosema juzi kwenye ATCL, zimeshakuja hatuwezi kuzichoma lazima tupange utaratibu wa kufanya mambo yaboreke zaidi. Kwa hili naomba tuangalie utaratibu wa mortgage financing, tushirikiane na BoT kwa sababu inasimamia mabenki yetu, wananchi wapate nyumba kwa sababu sekta ya nyumba kwa Tanzania bado iko chini sana; Serikali ipate na mashirika yetu yaweze kwenda mbele.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba tupate majibu, siyo kwa sababu Halima amezungumza bali tupate majibu wa nini muelekeo wa mifuko yetu kwa mustakabali wa Taifa na watumishi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho lakini sio kwa umuhimu...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Nadhani ni wakati muafaka kwa Waziri wa Fedha kutuambia kwamba kama makusanyo ya mapato yetu ni mazuri kwa kiwango hicho, asilimia 82 tunaambiwa mpaka sasa, inakuwaje ni changamoto kubwa sana inapokuja kwenye suala la utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, kwangu haiingii akilini kama tunajisifu performance ya makusanyo yetu, lakini ukija kwenye bajeti ya Kilimo utekelezaji ni less than fifty percent, ukija Viwanda na Biashara, ukija Maji, ukija Ujenzi, yaani tunakusanya vizuri, lakini ikija kwenye utekelezaji wa maeneo ambayo ni muhimu na nyeti, kwa mustakabali wa Taifa letu performance hairidhishi kwa nini?

Mheshimiwa Spika, la pili, niungane na hoja ya Kamati kwamba, kichaka cha uhakiki kinaumiza sana wakandarasi wetu wa ndani, kinaigharimu sana Serikali kwa sababu ya riba ama kwa sababu ya adhabu kwa kutekeleza mikataba nje ya muda.

Mheshimiwa Spika, protocol ya Afrika Mashariki kama ambavyo imeelezwa, ilielekeza wazi kwamba uhakiki ukishafanyika, wananchi ama wakandarasi weather ni wa ndani ama wa nje wanatakiwa walipwe ndani ya siku 90 baada ya uhakiki. Kama hawatalipwa ndani ya hizo siku 90, hilo deni litaenda ama hayo madai sasa yaliyohakikiwa yatatoka kwenye madai, yataingia kwenye deni la Serikali ili hawa wakandarasi wawe na uhakika wa kulipwa kwa sababu kwa taratibu za nchi yetu, deni la Serikali ni first charge, yaani lipo la kwanza. Kama tukipitisha bajeti la deni la Taifa, tumekadiria linaenda kulipwa trilioni nane mpaka 10, kama tumeweza kukusanya trilioni 20 ama 30 kitu cha kwanza cha kulipa ni deni la Serikali ikifuatiwa na mishahara ya watumishi na vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Spika, sasa leo ni bahati mbaya sana Serikali badala ya kutimiza wajibu wake kuweza ku- encourage wafanyabiashara, wakandarasi wa ndani ili biashara ziweze kukua ama waweze kukuza mtaji, Serikali ndiyo inaminya. On very serious note Kamati ya bajeti imeona lakini tunaomba leo Waziri atuambie commitment ya Serikali ya kukubaliana na mapendekezo ya Kamati ya Bajeti kwamba kuwe na deadline ya uhakiki.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naangalia tu kwa mfano madeni tu ya kawaida katika Sekta ya Ujenzi, ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ambaye amefanya ukaguzi maalum wa miradi ya maendeleo, anatuambia madai ya wakandarasi ambao hawajalipwa kwenye ujenzi peke yake ni trilioni 1.03, ikijumuisha milioni 224 riba ya adhabu kwa Serikali kushindwa kutekeleza mkataba kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa unajiuliza common sense ya kawaida, tuna Wachumi nchi hii wabobezi, tuna Wanasheria nchi hii wabobezi, hivi ni akili kweli, unaingia mkataba kujenga barabara ukijua uwezo wako wa kifedha, unashindwa kulipa ndani ya muda, unatozwa adhabu kwenye Sekta ya Ujenzi milioni 200, yaani hii ni adhabu, hivi hizo ni, yaani najiulizaga nasema ni akili au, nikitumia lile tope watu wanakasirika, lakini tujiulize hii milioni 200 sijui na nne, ingejenga kilometa ngapi za barabara. Huu ni mfano mmoja kwenye ujenzi; tukienda kwenye maji habari ndiyo ile ile; tukienda kwenye kilimo, habari ndiyo ile ile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, REA, Serikali inadaiwa na wakandarasi mpaka mwaka 2020, tunajisifu hapa umeme vijijini, umeme vijijini, tunapiga swaga kama vile kila kitu ni perfect, kumbe huku wakandarasi wanaumia. Tunadaiwa kwenye REA trilioni moja, umeme vijijini, hapa sijazungumzia kabisa wakandarasi wanaotoa huduma kwenye Wizara zetu matrilioni.

Mheshimiwa Spika, kitu ambacho Kamati ya Bajeti inasema, hivi viporo vinatokana na the so called uhakiki, Serikali inajua, wakihakiki wanatakiwa ndani ya siku 90 walipe. Kwa hiyo wanachoamua wanakauka hawahakiki huku wanaumiza watu. Mbaya zaidi tunakuwa hatupati taarifa sahihi ya deni la Serikali. Tunadangayana hapa deni la Taifa lilikuwa trilioni 59 juzi la Serikali siyo la Taifa, maana tukiweka huko la Taifa tunafika trilioni 70 la Serikali.

Mheshimiwa Spika, juzi nasika Waziri Mheshimiwa Mwigulu jana ameingia mkataba, maana tunaenda tirioni 60 point kadhaa, lakini madeni kama haya yangeingizwa kwenye utaratibu waliokubaliana kwenye protocol, tungejua Taifa tunadaiwa nini, matokeo yake tunajidanganya, deni letu ni himilivu, lakini tuna madeni yaliyojificha kwenye kichaka. Naomba Mheshimiwa Waziri atujibu seriously hiyo siyo ajenda yangu, ni haja ya Kamati ya Bajeti, Kamati ya Mheshimiwa Spika.

Mheshimiwa Spika, la pili, dhuluma iliyojificha kwenye kichanga cha kusafisha. Wakati sisi tunakuwa enzi hizo ilikuwa ni jambo la kawaida kabisa na ambalo lililindwa na mfumo, Halima nimemaliza zangu form four nina ndugu yangu pale, ndugu yangu anakuja kutumia cheti cha Halima. Akishatumia cheti cha Halima, anaenda kusoma diploma, degree ama masters, anasoma PhD ndiyo ilikuwa life style. Kwa sababu kiteknolojia tulikuwa hatuna mfumo wa kufanya tracking, siyo kwamba sasa hivi DNA tu unaweza kujua nani kafanya nini, mfumo ambao Serikali iliutekeleza ikaulinda yenyewe.

Mheshimiwa Spika, kilichotokea, maskini ya Mungu, watu wameenda wakaenda wakasoma degree zao, wengine wakaenda wakasoma PhD professionals lakini ametumia cheti cha Halima. Leo wanaitwa wenye vyeti fake, yes is true kwa sababu alitumia cheti change, lakini Serikali inadhani ni fair kibinadamu. Unajua saa nyingine unaweza ukajikuta unapata laana kwa kudhulumu tu. Serikali inadhani ni fair, watu kama hawa kufukuzwa kazi na kunyimwa hata shilingi mia, is it fair kibinadamu? Yaani mfumo tumeutengeneza wenyewe, kwa kutumia mfumo tumeenda tumewasomesha wenyewe licha ya kwamba alichukua cheti cha Halima cha PhD anatumia lakini ni hapana, ni kwamba alichukua cheti changu na wengine tulikuwa nao wanasiasa, lakini wakachuniwa tu kwa sababu wana political influence, hivi Serikali inadhani ni fair?

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia nia njema ya Mheshimiwa Mama Samia aliyoionyesha kwa wale waliomaliza darasa la saba wakatolewa kwenye mfumo kwamba walipwe stahili zao, naomba Mheshimiwa wa Fedha atuambie mustakabali wa watumishi hawa waliolitumikia Taifa hili kwa jasho na damu ukoje? Hivi wako tayari kudhulumu mtu ambaye ametumia muda wake wote wa maisha yake kufanya kazi ya utumishi Serikalini, akabakiza miaka miwili astaafu, mshahara wake wenyewe ni tia maji tia maji...

T A A R I F A

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Taarifa, ndiyo Mheshimiwa Mpemenwe.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji, Mheshimiwa Mdee yeye ni Mwanasheria mzoefu na anajua kwamba sheria huwa haina excuse, huwezi ukatoka ukaenda ukaibah ukasema nimeiba kwa sababu nilikuwa na njaa.

Kwa kuwa ameshakiri yeye mwenyewe kwamba hawa watu walitumia vyetu ambavyo siyo vya kwao, halafu anakuja mbele ya Bunge lako kuja kuzungumza kitu cha namna hii na ukizingatia kwamba yeye ni Mwanasheria, naomba aifute tu hiyo kauli.

SPIKA: Mheshimiwa Halima, taarifa hiyo unaipokea.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, si unajua tena nanilii anajua, mimi naomba niendelee. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nimesema hivi kibinadamu sheria tuna tunga binadamu, watu wametengeneza mfumo ambao ulikuwa unaruhusu hayo mambo kufanyika, watu wakaenda kusomea taaluma kwa kulipiwa na Serikali hii hii, wamehudumia Taifa hili kwa miaka 10, 15, 20,30 wanawatoa kapa, siyo ubinadamu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la tatu, huduma za Mfuko Mkuu Fungu la 22, pamoja na mambo mengine unawajibka kusimamia na kulipa malipo na michango ya mwajiri kwa watumishi wote wa Serikali pamoja na taasisi zake. Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Wizara yake ndiyo ina jukumu la kuhakikisha kwamba michango ya wastaafu watarajiwa inapelekwa kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii.

Mheshimiwa Spika, sasa leo nataka Mheshimiwa Waziri anieleze, maana juzi Mheshimiwa Mhagama alipiga mkwara mzito na nilimkubali, akasema waajiri wote na nitafanya ukaguzi mahususi na mkirejea waajiri ambao ni wa vyombo vya habari na waajiri wengine ambao hawapeleki michango ya watumishi. Sasa leo nataka Serikali iniambie hivi kwa nini na yenyewe haipeleki michango ya watumishi wao? Hivi uhakiki ule wataufanya kwa sekta binafsi ama watafanya na kwao?

Mheshimiwa Spika, ni aibu CAG anatuambia kwa sababu ndiyo amepewa mamlaka ya kukagua kwamba kwa mwaka wa fedha ulioishia mwaka 2019 ambao ripoti ilitoka mwaka 2020, walikuwa hawajapeleka michango shilingi bilioni 171; PSSSF milioni 61, NHIF milioni 24, WCF bilioni 85.

Mheshimiwa Spika, taarifa aliyoitoa juzi inaonesha kwamba hamkuwasilisha Taasisi za Umma zaidi ya shilingi bilioni 20.9 na michango ya PSPF ikiwa ni shilingi bilioni 7.7. Sasa sisi tunajua namna gani kwanza hii mifuko inaumizwa sana kwa Serikali kukopa, lakini hailipi. Hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, tunajua namna gani hii mifuko inaumizwa sana; kwa sasa hivi tumeanzisha utaratibu tunasema tunajenga viwanda, lakini tunajenga viwanda kwa kutumia mabilioni ya hii mifuko, hatukatai. Bahati mbaya viwanda sasa hivi vinatangeneza hasara; hiyo ni ajenda nyingine tutakuja kuizungumza. Ila tunatujua tusipopeleka fedha, tunaathiri ukwasi wa mifuko na tunaathiri wastaafu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nami naomba Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, rafiki yangu, ukija hapa, maana hili siyo tatizo la Mheshimiwa Jenista, hili tatizo ni lako mtoa pesa. Mheshimiwa Jenista yeye anawasimamia tu hawa. Utuambie Mheshimiwa Mwigulu Nchemba ni kwa nini hupeleki fedha za wastaafu? Utuambie ni lini hizi fedha za wastaafu zitalipwa kwa ukamilifu wake? Zamani ilikuwa mtumishi akistaafu, ndani ya miezi sita amepata kwake anatulia nyumbani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi mtumishi akistaafu, yaani anakufa kabla hajapata. Akifa ndiyo warithi sijui wanaitwa nani hao, watu wa mirathi hawa; kwa hiyo, naomba sana, hili jambo ni nyeti, zito, linaumiza wananchi wetu, tuambiwe haya madeni yataenda kulipwa lini? Kubwa zaidi Mheshimiwa Jenista nilikuwa nakuomba, ile fimbo uliyokuwa unaenda kuwachapia waajiri wale ambao hawapeleki michango yao, isiishie sekta binafsi. Tunaomba upite humo humo Serikali ili utuletee ripoti hapa Bungeni, maana uliji- commit hapa kwenye Serikali hii, watu sugu wa kutoa hii michango ni akina nani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho siyo la umuhimu limezugumzwa na Kamati hapa, ukomo wa kuajiri ama ikama ya ajira. Kuna maeneo ambayo watumishi wakiwa wamepungua, yanaweza yasiwe na madhara makubwa sana, lakini kuna maeneo ambayo Serikali mnatakiwa mhakikishe idadi ya watumishi inakuwa kama ambavyo wanahitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi kweli ni akili pale ambapo mamlaka iliyopewa jukumu la kukusanya mapato, tumekaa hapa tunasema hatuna vyanzo vya mapato, mapato hatukusanyi ipasavyo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie.

Mheshimiwa Spika, ni akili kwa TRA kuwa na upungufu wa wafanyakazi? Hivi ni akili kwa Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali anayekagua pesa zetu na matumizi yake kuwa na upungufu wa wafanyakazi?

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, naomba hili liangaliwe kwa umakini na tupate majibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwanza ninarejea hotuba ya Waziri ambapo katika ukurasa mmojawapo ulihamisha jukumu la uwekaji vinasaba kwenye mafuta ya petroli kutoka kwa Mkandarasi binafsi na jukumu hili ukalipa Shirika la Viwango la Tanzania. Sasa Mheshimiwa Waziri nataka wakati unajibu utueleze namna gani fikra kama hii ambayo kutokana na mikata mibovu na hovyo kabisa ilisababisha Mkandarasi binafsi kwa mwaka kupata zaidi ya bilioni 68 kwa miaka nane aliyokuwepo zaidi ya bilioni 490. Umefanya jambo la busara kuondoa hilo jukumu kuipa taasisi ya Serikali ili haya mapato basi yaweze kuingia Serikalini na hata mkipunguza gharama yakiwa kwa kiwango kidogo vilevile yaweze kuingia Serikalini, hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka uniambie Mkandarasi huyu ambaye amepewa jukumu la kubandika stempu za ki-electronic ama ETS, kwenye bidhaa zinazozalishwa Nchini kwa ajili ya kutoza ushuru wa bidhaa mkataba wake utakoma lini ili hili jukumu ambalo amepewa Mkandarasi huyu kipewe ama chombo cha Serikali ama mfanye ushindani upya aweze kupatikana Mkandarasi kwa bei nafuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumezungumza juu ya mafuta, sasa nitazungumza juu ya ETS. Kwa maelezo ya Serikali huu utaratibu ulianza mwaka 2018, maana tunaofikiria kipindi kile mambo yalikuwa perfect sana, lakini siyo kila kitu ni perfect kuna sehemu tunakosea na lazima tujirekebishe. Lengo lake lilikuwa ni jema kuweza kutambua bidhaa, kuzuia watu wasikwepe kodi, Serikali iweze kupata kodi yake stahiki, jambo ni jema. Lakini gharama, tunaambiwa mpaka sasa hivi wazalishaji ambao wamefungiwa hizo mashine wako 245, waagizaji 86. Sasa mafanikio ni nini! Kwa sababu kwa petroli ilikuwa akiweka kale kadude lita moja shilingi nane, huku kwenye bidhaa za vinywaji, vinywaji vikali na vyepesi na masigara na kadhalika kuna shilingi nane kwa mantiki ya dola nane na dola 20 kutegemeana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mafanikio ni nini kabla ya ETS na baada ya ETS. Kwa maelezo ya TRA kabla ya ETS tulikuwa tunakusanya shilingi bilioni 237 baada ya ETS tumekusanya shilingi billioni 246. Tafsiri yake ni nini, tofauti ninyi mnajua bilioni 46 toa bilioni 37 ni bilioni nane. Sasa gharama ambazo Makampuni yetu yanaingia kutokana na huu mchakato ni nini? Taarifa ya TBL ambao ni walipa kodi wakubwa nchini, wanasema katika kipindi cha miaka mitatu wanatarajia, kuanzia mwaka 2019 mpaka 2021 watamlipa Mkandarasi shilingi bilioni 94 kampuni moja, hapo nimesema makampuni ambayo ama viwanda viliunganishwa ni zaidi ya 250, wakati TRA nyongeza yao ni kutoka bilioni 237 mpaka bilioni 246 different ya eight billion. TRA wakatupa data zao za mvinyo wa ndani, kabla mtambo wa ETS shilingi milioni 657 baada ya ETS on average imeongezeka mpaka bilioni 3.4. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda cha pili ni cha sigara, mmeshataja TBA hapo. Mkandarasi binafsi kalipwa na TBA bilioni zaidi ya 90. Serikali nyongeza mlifikiria kuna cheating kubwa mmepata shilingi bilioni nane. Hivi, tukisema hii ni busara, hii ni busara…

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa, taarifa!

MHE. HALIMA J. MDEE:… TCC...

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Halima Mdee kuna taarifa kutoa kwa Mheshimwa Kenneth Nollo.

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Naibu Spika, mi nataka nimpe taarifa mzungumzaji. Nadhani anajaribu kutoa opinion, tangu kule alivyosema kwenye mafuta na hata huku. Na kitendo cha kuanza kutaja kampungi hii inalipa this amount, this amount ni kama anataka kusema kama kuna uonevu. Kwa hiyo hoja yake ya msingi hapa angejaribu kusema hapa labda alternative kwamba tutafute kampuni nyengine lakini anachokifanya hapa ni kwamba hawa wanalipa kiasi hiki, as if watu wanaonewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka tu nimpe taarifa, anajua mchakato mzima tulivyompata mtu wa kuweka stamp za TRA na lilivyokuwa jambo gumu. Kwa hiyo kinachotakiwa aelewe kwamba hiyo opinion anayoitoa ni kutafuta suluhu ya namna nyingine na asifanye kama kuna kuibiwa. Ahsante sana.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Halima Mdee unaipokea taarifa hiyo?

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, ninachokizungumza hapa sina tofauti na alichokizungumza Mheshimiwa Tabasam the other day kuhusiana na utaratibu huu huu kwenye mafuta; hakuna tofauti na alicho zungumza mbunge wa Gairo, kuhusiana na utaratibu huu huu kwenye mafuta. Na tunazuzngumza hapa ili kuiambia Serikali kupitia wataalamu wetu; na nilisema hapa, dhamira ya ilikuwa ni nini njema, kuweza kujua bidhaa zinazozalishwa, lakini dhamira njema mkijua kwamba mlichemka mnatakiwa mnakaa mnajitathmini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimetoa mfano kwamba, tulimchukua mkandarasi …

MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Halima Mdee kuna taarifa kutoa kwa Mheshimwa Stanslaus Nyongo.

MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimwai Naibu Spika, napenda tu kumtaafu Mheshimiwa Mbunge, kwanza kabisa yeye mwenyewe ni mjumbe wa Kamati ya Bajeti, na haya yote yamepita kwenye kamati ya bajeti. N kuhusu suala la ETS imekuwa raised kwenye Kamati ya Bajeti na Serikali imekuwa ikisimamia na kupambana na suala hili ili kuhakikisha kwamba inakuwa na faida.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine na cha mwisho, ameonesha kama kuna difference ya eight billion, difference ilikuwa ni kubwa, nia ilikuwa ni njema kama anavyosema, sema kiwango kimekuwa kidogo. Yeye akubali, na yeye ni mjumbe wa Kamati ya Bajeti aendelee kuishauri Serikali vizuri kuliko kushutumu watu wengine wamechemka ilhali na yeye mwenyewe ni sehemu ya kuchemka. Ahsante sana. (Makofi/ Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Halima Mdee unaipokea taarifa hiyo?

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza mimi sikuchemka kwa sababu mimi sikuwa sehemu ya mkataba uliotengenezwa wala hata siujui. Pili kuwa mjumbe wa Kamati ya Bajeti hakunizuii mimi kuchangia bungeni, na nimelichangia hili ili kutambua hatua ambayo Serikali imechukua kwa kuondoa jukumu la vinasaba kwa mtu binafsi, imerudishwa Serikalini, kwa hiyo pesa inarudi Serikalini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi ninaitaka Serikali; na uzuri Mheshimiwa Mwigulu anasikiliza, nataka Mhesnishiwa Mwigulu hili la ETS ulitoe huko kwa mkandarasi aliyepo sasa, kwa sababu tumeshapigwa vya kutosha, turudishe ama Serikalini, na kama Serikali haina teknolojia ya kutosha tufanye ushindani watu waje tupate mtu mwenye gharama nafuu. (Makofi)

Meshimiwa Naibu Spika, kiwanda cha pili cha sigara, kwa mwaka mmoja kimelipa bilioni 14, kiwanda kimoja. Tukizungumza hivi viwanda vidogo vidogo ni bilioni tatu biloni nne, bilioni nane; ukijumlisha unaweza ukakuta wakati TRA mmeongeza si pungufu ya bilioni 20, mwenzenu huku kwa vile viteknolojia vya kudonoa donoa tu na kuweka nembo, amepata bilioni 400 labda, hivi hii ni busara. Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, nitakuomba tu unijibu kwa sababu kiukweli tunapigwa pigwa sana, na si busara kukubali kuendelea kupigwa pigwa, na mimi najua wewe hupendi tupigwe pigwe. (Makofi)

Meshimiwa Naibu Spika, la pili. Mpango wa kwanza na wa pili tulifeli kwa sababu, kwanza hatukuwa na mtiririko wa fedha za kutosha, pili hatukuwa na takweimu za kutosha. So, mimi ninasikiliza ndugu zangu Wabunge hapa, kila mtu anasema Bungeni hapa, ooh sijui jimboni kwangu inakuja milioni 500, tunapiga makofi, yaani tunawahisha shughuli. Lakini Nheshimiwa Mwigulu unajua, kwamba kwenye bajeti yako wewe ambayo tunaimaliza sasa ni ya mtangulizi wako. Tulipanga kwa miaka hii yote kwa mikopo kwa mambo yetu yote ya ndani tuweze kukusanya trilioni 34. Juzi hapa unatusomea hotuba yako umeweza kukusanya trilioni 24, kuna deficit ya trilioni 10. Hivi kweli nisaidie; ni muujiza gani huu utakufanya Mheshimiwa Mwigulu na Serikali muweze kukusanya 10 trillion ndani ya miezi miwili? Pili, kama unajua ulishindwa mwaka jana hivi kweli ni busara kwenda kusema kwamba unaweza kukusanya trilioni 36, hivi ni busara?

Meshimiwa Naibu Spika, ndugu zangu Wabunge wadogo zangu asilimia 70 hapa ni wageni, hizo 500 msipige kofi, tutakutana mwakani hapa tutaanza kutoana macho. Kwa sababu kwa mtindo wa ukusanyaji wa aina hii, naomba Waziri uje utuambie kuna miujiza mengine itakayokuja, lakini kwa utaratibu huu, siku zote nawaambieni tukiwa wakweli kama unauwezo wa shilingi mia, jipangie kwa shilingi mia yaki ili sasa tuendelee kuishi kwa matumaini, sio unaweka shilingi mia unakusanya buku unasema mimi naweza kukusanya elfu moja, wakati unajua ndugu yangu mia ndio saizi yako…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: haya ahsante sana Mheshimiwa Halima Mdee muda wako umeisha ahsante sana.

MHE. HALIMA J. MDEE: …. Kwa hiyo tuwe wakweli tuweze kulisaidia taifa hili. Nitaomba majibu mahsusi kwa ETS…

NAIBU SPIKA: Muda umekwisha Mheshimiwa Halima Mdee, ahsante sana, shukran.

MHE. HALIMA J. MDEE:… nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwanza nianze na jambo ambalo nisingelianza, lakini kwa sababu kuna mtu amegusa inabidi niseme. Kuna mchangiaji mmoja alizungumzia Msemaji wa Kambi ya Upinzani kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu ambaye ni Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, kuzungumza ni kwa namna gani bajeti za Serikali hii zimekuwa hewa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa bahati mbaya akatolea mifano ya hela ndogo wakati sisi tulikuwa tunaongelea mambo mazito, tulikuwa hatuongelei mambo peanut. Sasa nimuoneshe tu ni kwa nini Kiongozi wa Upinzani Bungeni amesema ni hewa, nitanukuu hotuba yetu. Mosi,
Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ilipewa shilingi bilioni 2.2 kwenye Wizara ya Kilimo ambayo ni sawa na asilimia 2.2 ya bilioni 101 ilizotakiwa ipewe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Kitengo cha Mifugo na Uvuvi ilitengewa shilingi bilioni 1.2 sawa na asilimia 7.9 kati ya shilingi bilioni 15.8. Amekiri mwenyewe muongeaji kwamba kilimo kwa mwaka huu kimekuwa kwa asilimia 2.9 badala ya asilimia sita iliyokuwa ikitarajiwa na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani akaenda mbele zaidi, akasema tunashangaa kwamba asilimia 70 ambayo inaajiri Watanzania wengi wamepewa asilimia 2.2 wakati eti tumenunua ndege ama kupeleka advance payment ya bilioni 128 ambayo inahudumia watu 10,000 tu. Sasa naona kuna Wabunge wanakaa wanalalamika hapa halafu wanashindwa kuiambia Serikali ukweli. (Makofi)
Wizara ya Viwanda na Biashara tunaambiwa huu ni mwaka wa viwanda, hii ni Serikali ya viwanda, hii Wizara inatakiwa iratibu wawekezaji waweze kuja, hivi viwanda viweze kupatikana, wawekezaji waweze kuwekeza nchini, imepewa shilingi bilioni 7.2 sawa na asilimia nane ya shilingi bilioni 40 zilizoidhinishwa na Bunge.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Miundombinu ilipewa shilingi trilioni 1.7 sawa na asilimia 58.7 ya shilingi trilioni 2.1 ambayo Bunge hili lilipitisha; Wizara ya Uchukuzi asilimia 30; Wizara ya Nishati na Madini asilimia 36 na Wizara ya Afya asilimia 25. Hivi mkiambiwa hewa ndugu zangu siyo kweli kwa bajeti nzima ya maendeleo kwa wastani kwa mwaka huu unaoisha ni asilimia kati ya 26 na 34 ambazo zimetolewa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ndugu zangu kama kweli zaidi ya asilimia 70 ya fedha za maendeleo hazijapatikana, mkiambiwa bajeti yenu ni hewa mnakasirika nini? Kupanga ni kuchagua, tujue uwezo wetu ni upi, tujipange kutokana na uwezo wetu ili tujue tunaendaje
mbele kama Taifa. Ndugu zangu niwaombe wanaopitapita huko mbele wanaambiwa nenda katetee ni hivi, hapa hakuna cha kutetea, hatetei mtu hapa, yaani huu mwaka mmoja wa Mheshimiwa Magufuli na Serikali yake kwenye bajeti ya maendeleo mmechemka, tukubali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Halmashauri zetu, tukiacha kuwa wanafiki hapa ni vilio, mwaka jana Serikali ilikuja kwa mbwembwe hapa tunachukua property tax, tumejipanga vizuri wakijua kwenye Halmashauri nyingi za miji hicho ndio moja ya vyanzo wanavyovitegemea, kwa
mbwembwe nyingi huu mwaka umeisha. Mimi nimetoka juzi kwenye Baraza letu la Madiwani, tunapoenda bajeti nyingine ya mwaka huu hakuna hata shilingi moja iliyotoka Serikali Kuu kwa property tax. Wakati wenyewe tulikuwa tuna uwezo wa kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 10, tulikusanya mwaka mmoja ule uliopita, tumepanga kukusanya mwaka huu Serikali imechukua pato hamjaturudishia pato, shughuli za maendeleo zinakwama. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa sisi ni wa Mjini ambao japo tuna vyanzo vingine, sasa wenzangu na mimi wa vijijini mkikaa hapa mnapiga makelele, mnapiga makofi, oyaoya hatutawanyoosha hawa Mawaziri ili waweze kuwajibika vizuri kwa Bunge. Kwa hiyo, mimi niombe kati ya kipindi ambacho Wabunge tunatakiwa tuwe wamoja kuisaidia nchi yetu na siyo kulinda Serikali yetu, kuisaidia nchi yetu ni kipindi cha bajeti hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya pili, suala la mauaji na utekaji unaoendelea. Asubuhi ilitolewa hoja hapa na Mheshimiwa Hussein Bashe, ukaikatiza hoja, mimi ninaamini kwamba Spika wetu huko anasikiliza. Ninaamini mtu mwingine akija akitoa hoja hiyo hiyo Spika wetu akija ataweza kulitendea haki hili jambo. Nadhani umeona ni jambo zito sana ukasema ngoja kwanza nimsikilizie bosi wangu akija atasema nini, inawezekana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kauli zinapotolewa na watu wazito na ninashukuru hili suala halina chama, linatoka upande wa CCM na linatoka kwa upande wa Kambi ya Upinzani. Kwa sababu CCM wanaamini miongoni mwa watu wa Serikali hii kuna watu wana nia njema na Taifa hili, vilevile wanajua kuna watu miongoni mwa Serikali hii hii wanafikiria wao wako juu ya sheria, kwa sababu fulani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana tunasema haya mambo lazima tuyajadili, kama Bunge lisipojadili, kama Bunge linaogopa kujadili leo, nani ajadili. Nilimsikiliza Mheshimiwa Nape akiongea Mtama, alikuwa ni Waziri Mheshimiwa Nape alitoa kauli nzito, kauli ambayo inaonesha kwamba kuna watu ndani ya Serikali wanatumia genge la Usalama wa Taifa kuteka watu, kufanya mauaji. Huyu ni former Minister, siyo mtu mdogo, wiki mbili zilizopita. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo Mheshimiwa Bashe amezungumza, mimi kwangu Mbunge wa CCM akizungumza ni kama Serikali inazungumza, that is my opinion kwa sababu ninaamini hakuna Mbunge yeyote makini wa kutoka Chama Tawala akasema kitu ambacho hana uhakika nacho.
Mheshimiwa Bashe amerudia amesema kuna genge ndani ya Usalama wa Taifa linashirikiana na bahati mbaya anatajwa dogo sijui Bashite yule, wamekuwa wakimtajataja kwamba Bashite ndiyo anaongoza hili genge. Sasa tunajiuliza sasa kama Bashite anaongoza genge, kama Bashite anasemwa hachukuliwi hatua, juzi ambaye alimtolea Mheshimiwa Nape silaha lile gari lililombeba limeonesha limesajiliwa kwa namba ya Ikulu, halafu watu wanakauka tafsiri yake ni nini?
Mheshimiwa Naibu Spika, je, Rais anajua? Sisi hatutaki ionekane Rais anajua, ndiyo maana tunasema hili Bunge likaondoe mzizi wa fitina, kwa sababu inaoneka Mheshimiwa Mwigulu ngoma imeshamshinda na ndiyo jukumu letu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunaambiwa kuna Wabunge 11 ni wanted, hivi kweli viongozi wetu mnaambiwa kuna Wabunge 11 wanted na imetoka kwenye proper authority, hakuna mtu yeyote aliyesimama hapa akamwambia thibitisha, futa kauli yako sisi tunajuana, yaani huku ndani tunajuana, sindano ikigusa pale pahali pake inabidi kila mtu anakaa chini anatulia, hakuna mtu aliyepinga kile kilichosemwa. Kwa hiyo, je, tusubiri aanze kufa Mbunge mmoja mmoja ndiyo tuunde hii timu? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Ben Saanane kijana wetu amepotea, zikaanza kupigwa propaganda eti CHADEMA tunajua alipo. Sasa kama mnajua sisi wauaji kwa nini msitukamate mtuweke ndani? Kwa nini maisha ya watu tunachukulia simple?
Mheshimiwa Naibu Spika, Ben Saanane aliandika waraka tarehe 8 Septemba, 2016 naomba ninukuu, kaandikiwa na namba ifuatayo; “Ben Saanane unachokitafuta ndani ya Serikali hii utakipata kwa elimu na uwezo wako hatukutarajia ungefikia hatua ya ajabu kwa namna uliyofikia hujiulizi kwa nini upo huru hadi muda huu, your too young to die. Tunajua utaandika na hii, andika lakini the next force hutaandika ukiwa na uhuru wa kutosha. Andika but your days are numbered, unajua kuna rafiki yako alipuuza na hatutaki kuandika kuhusu yeye labda kwa kuwa alitangulia, andika Ben, andika sana, ongea sana lakini utajikuta mwenyewe.”
Mheshimiwa Naibu Spika, namba iliyomwandikia ni 0768 79982 hii namba polisi wanaijua, Serikali mnaijua, mkitaka ku-trace watu...(Makofi)
NAIBU SPIKA: Haya ahsante Mheshimiwa Halima Mdee.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurasa wa 22 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri inazungumzia upanuzi wa barabara ya New Bagamoyo (Morocco JCT) – Mwenge – Tegeta (12.9 kilomita). Barabara hii ilishakamilika na kuzinduliwa katika kipindi cha mwaka 2010/2015. Kwa maelezo ya Mheshimiwa Waziri barabara hii iko katika kupindi cha uangalizi kinachotarajia kukamilika 30 Julai, 2017. Ni ushauri wangu kwa Mheshimiwa Waziri na timu yake, wapite na kufanya uhakiki katika barabara husika kutokana na ukweli kwamba kuna maeneo ambayo tayari yameshaharibika (hayako katika hali nzuri).

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo ambayo wakati wa ujenzi wa barabara mapokea na matoleo ya maji hayakujengwa katika kiwango ambacho kinakidhi. Kiwango cha maji wakati wa mvua kinachotoka maeneo ya Goba ni kikubwa na hatari zaidi iko Tangi Bovu maeneo ya Mbuyuni, Kunduchi, Africana pamoja na Salasala. Kutokana na ufinyu huu kuna hatari ya barabara kupasuka na kuharibika. Ni ushauri wangu kwa Mheshimiwa Waziri na kwa Wizara kuchukua hatua za dharura ili kunusuru kazi iliyokwishafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua kwamba kuna kazi inayoendelea ya Ujenzi wa service road katika barabara husika. Kwa muktadha huo huo, ningependa kujua kwamba ni lini taa za barabarani zitakamilika kwa kuwa ajali nyingi zinasababishwa na kutokuwepo kwa taa barabarani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba ya Mheshimiwa Waziri katika ukurasa wa 22 na 23 inaonesha kwamba kipande cha Morocco – Mwenge kitajengwa kwa kiwango cha dual carriage way. Baada ya kupata msaada wa fedha kutoka Serikali ya Japan kupitia Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Japan (JICA). Hata hivyo, hotuba za bajeti za miaka minne iliyopitia ilionesha kwamba Serikali ya Japan ilitoa bilioni 88 ambapo pamoja na mambo mengine ingejenga barabara ya Mwenge – Tegeta (first phase) na Mwenge – Morocco (second phase)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kupata ufafanuzi juu ya utata uliojitokeza kutokana na kauli mbiu zinazotofautiana kutoka kwa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imekuwa ni utamaduni kwa Mfuko wa Barabara kutoa kiasi fulani cha fedha kwenda halmashauri, lengo likiwa ni kuziwezesha halmashauri zetu ambazo zina uwezo mdogo. Hata hivyo, kwa mwaka wa fedha 2016/2017, Manispaa ya Kinondoni ilitarajia kupata Shilingi bilioni 10.5 kutoka Mfuko wa Barabara. Mpaka kikao chetu cha mwisho cha Baraza la Madiwani taarifa tulizopewa ni kwamba hakuna hata shilingi iliyowasilishwa Halmashauri, hali ambayo imeathiri kwa kiwango kikubwa utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Naomba ufafanuzi ni lini fedha husika zitaletwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, TAZARA. Kwa muda wa miaka miwili/mitatu mfululizo nimekuwa nikizungumza juu ya uuzwaji wa nyumba za TAZARA kinyume na utaratibu halikadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uvamizi wa maeneo ya TAZARA yaliyofanywa pasipo hatua zozote kuchukuliwa. Mheshimiwa Samwel Sitta (marehemu) akiwa Waziri mwenye dhamana ya Wizara ya Uchukuzi nilimpatia Audit Report ikizungumzia kwa kina suala tajwa hapo juu lakini hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa mpaka sasa kuhusiana na suala husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua hatua zilizoanza za ujenzi wa barabara za Tegeta kibaoni – Wazo Hill – Goba. Taarifa zinaonesha kwamba kumpata mkandarasi kwa ajili ya sehemu ya Maendeleo – Goba (kilometa tano) zinaendelea. Ni imani yangu ahadi hii ya muda mrefu, itaanza kufanyiwa utekelezaji katika hatua ya kwanza kuelekea kukamilisha ujenzi mpaka Kibaoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kupata ufafanuni wa barabara kuu kuelekea Ruaha National Park itajengwa?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda kupongeza kazi nzuri inayofanywa na Jeshi letu ya kuhakikisha inalinda mipaka ya nchi yetu kwa weledi, uaminifu na uzalendo wa hali ya juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kuna matukio ambayo yameanza kujitokeza hivi karibuni ya Jeshi kujiingiza au kuingizwa kwenye siasa za vyama. Mambo haya yanatakiwa kukemewa na kila Mtanzania makini anayeipenda nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitendo kilichofanywa tarehe 23 Septemba, 2017 wakati Maafisa Wanafunzi wakitunukiwa Kamisheni na Rais na Amiri Jeshi Mkuu cha kupokea wanachama wapya wa CCM hakitakiwi kurudiwa tena. Ni udhalilishaji wa Jeshi na nchi. Jeshi letu lina wajibu wa kulinda nchi na siyo chama cha siasa. Tanzania ikiwa ni nchi yenye mfumo wa vyama vingi, chama chochote cha siasa kinaweza kushinda uchaguzi na kuunda Serikali. Tukiona Jeshi linalotakiwa kuwa neutral linaegemea upande wa chama fulani linashusha hadhi ya Jeshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe, Jeshi la Polisi limeshachafuka na kushuka hadhi yake. Jeshi pekee tunalolitegemea limejijengea heshima kubwa ni Jeshi letu la Ulinzi. Tunaomba hadhi hii isivurugwe na watu wachache wenye maslahi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ya pili ni kuhusu ajira. Kuna malalamiko kutoka kwa vijana wa Operation Kikwete ambao wamefanya kazi na kulitumikia Jeshi kwa takriban miaka mitatu, wanashiriki operation mbalimbali ndani ya nchi yetu ikiwemo Operation Kibiti. Mbali na ushiriki wa operation zote na kulitumikia Taifa kwa moyo, wameambulia kurejeshwa nyumbani na nafasi zao kuchukuliwa na vijana ambao hawana uzoefu (wengine hata mwaka wa uzoefu hawana). Malalamiko yanahusu ajira mbalimbali zikiwemo ajira mpya za Jeshi la Polisi zilizotangazwa hivi karibuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana waliochukuliwa inasemekana hata usaili wa JWTZ walikuwa hawajafanya. Kwa lugha nyingine, kumekuwa na ubaguzi wa ajira baina ya vikosi vya Operation Kikwete na Operation Magufuli. Kuna sintofahamu kubwa sana ya vijana walioko mtaani. Tunaomba Waziri azungumzie hili na kutoa ufafanuzi wa sintofahamu hii na hisia za vijana ambao wanadhani hawajatendewa haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wanasema ajira zilizotolewa ndani ya JWTZ kupitia Mheshimiwa Rais akiwa Arusha hazikufuata utaratibu. Waliopata nafasi hizo ni watoto wa wakubwa Jeshini. Tunaomba ufafanuzi ili kuondoa sintofahamu hii.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Mimi leo nitajikita Jimbo la Kawe zaidi, kwa sababu naona kama Kawe kuna kaombwe hivi, sasa ninaomba Mheshimiwa Waziri unisikilize kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, katika ukurasa wako wa 78 umezungumzia miradi ya 711 na umesema kwamba utakamilisha miradi mikubwa iliyosimama ya Kawe 7/11 na Golden Premium Residence. Vilevile wataendeleza mradi wa Samia Housing Scheme Kawe. Sasa nilitaka unipe maelezo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu seven eleven one ilikuwa na thamani ya Shilingi bilioni 142, na Seven eleven two Shilingi bilioni 103. Nilitaka kufahamu ukamilishaji una lengo la kukamilisha asilimia 100 ama kiwango gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, Ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ya Mwaka ulioishia Juni, 2018, alisema wazi kabisa kwamba kutokana na miradi hii kukwama likelihood 2018 nazungumza; likelihood ya Serikali kupata hasara ya Shilingi bilioni 99.9 kipindi kile, lakini kuna hasara nyingine ya Shilingi bilioni 2.6 kwa sababu kuna wananchi ambao tayari walikuwa wameshalipia yale majengo lakini hakuna kilichoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri akija naomba anijibu kwa ufanisi kabisa ili tuweze kujua ni hasara kiasi gani ambayo nchi na Serikali imepata kutokana na mradi huu kukwama toka mwaka 2017 mpaka sasa na hasa ukizingatia kwamba Shirika la Nyumba la Taifa lilikuwa linatumia mikopo ya kibiashara kwenda kukopa ili kufanya hii kazi. Uzembe huu na hasara hii kwa nchi imetokana na Serikali kuinyima kibali kwa miaka zaidi ya saba kwenda kukopa wakati ikijua hili jambio ni la kibiashara. Hilo ni la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni migogoro ya ardhi. Nashukuru leo amezungumza Mwenyekiti wa Kamati, naunga mkono hoja yake. Mwaka jana 2022 nilisema hapa, migogoro ya ardhi nchi hii, Mawaziri na watendaji wa Serikali, kwenu ninyi mnatuimia kama dili la kuzunguka kufanya ziara. Hamna dhamira hata kidogo ya kuhakikisha nchi yetu inapangiwa mipango ya matumizi bora ya ardhi ili ifike kipindi tuachane na migogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2022 tuliambiwa kuna mkopo tukajinasibu sana. Leo Kamati inatuambia eti katika ule mkopo shilingi bilioni 47 ni ya posho na uratibu na kuzurura zurura huko, halafu Tume ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi, wanapewa chini ya shilingi bilioni 10! This is nonsense! (Makofi) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Mwenyekiti, this is lack of seriousness. Haya mambo yanauma. Jimbo la Kawe Mheshimiwa ninakuomba sana, tuitatue migogoro ya ardhi kwa Mwenyekiti wa lile Jimbo. Nimeondoka siku mbili tatu, kunalipuka. Kata ya Mabwepande, Mtaa wa Mbopo, kwa ndugu yangu kule wa Kibamba, Tegeta A, Isumi, eneo lingine la Madale Jimbo la Kawe, kuna mgogoro unaofukuta wa huyu mdudu anaitwa DDC. [Neno “mdudu” Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina nyaraka hapa Mheshimiwa Waziri toka mwaka 1980 eneo ambalo DDC inadai ni la kwake lilikuwa ni eneo la Kijiji, nyaraka zote ziko hapa. Kijiji kiliwaambia kitawapa hekta 500 kwa masharti kadhaa. DDC wakaenda wakakaa kikao na Wizara ya Ardhi, wakatengenezea hati mezani, wakaja na hati ya hekta 5,000. Ndiyo maana leo tunatoka kwenye Kijiji cha Jimbo la Kawe cha Mabwepande, tunaenda kwenye mtaa mwingine wa Mabwepande wa Kata ya Kawe ambao…

Mheshimiwa Mwenyekiti, samahani, napata mzuka yaani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaenda kwenye kata nyingine ya Jimbo la Kawe inaitwa Kata ya Wazo Mtaa wa Madale. Mabwepande ilipo ni kata tofauti, Wazo ilipo ni kata tofauti. Tunaenda kwenye Jimbo la Kibamba la ndugu yangu kata ya Goba. Taasisi za Serikali, hiki kimdudu kinaitwa DDC toka mwaka 1980 waliambiwa tufanyieni hawa mje mlipe wananchi fidia, hawajaja. [Neno “kimdudu” Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2004 wakaja wakapiga sound. Wananchi wakawaambia makubaliano yetu yako wapi?

Juzi bahati mbaya sana wamekwenda na Mkuu wa Mkoa. Nina barua za toka mwaka 1980 hapa. Wameenda na Mkuu wa Mkoa Makala na maaskari Polisi na mitutu ya bunduki, wanatisha wananchi wa Jimbo la Kawe eti na kuwaambia tunawapora, tuwapimie ardhi upya. Yaani mimi nimeshanunua ardhi, nimejenga, unakuja kuniambia unipimie nyumba yangu nikulipe tena!

That is nonsense, that is nonsense. [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge].

MWENYEKITI: Mheshimiwa Halima, jaribu kutumia maneno ya Kibunge ambayo ni ya heshima.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, yanauma. Haya nafuta.

MWENYEKITI: Hata kama yanauma. Haya.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi vitu vinauma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkuu wa Mkoa kaenda na jeshi lake, analazimisha wananchi, anaongea na wananchi lugha za kejeli, dharau na kiburi. Sasa nakuomba Mheshimiwa Waziri, kwanza kaa ukijua wananchi pale tumeshajipanga, hakilipwi kitu.

Pili, tunazungumza kwa eneo la Mabwepande peke yake, ni kaya zisizopungua watu 39,000. Hako kaeneo kamoja, sijamzungumzia ndugu yangu wa Kibamba, sijamzungumzia suala la kata ya Wazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna shule za Umma ziko pale, kuna hospitali za Umma ziko pale, kuna miradi ya maji eneo la Tegeta A, limejengwa tanki kubwa la Umma linalohudumia Jimbo la Kibamba na Jimbo la Kawe. Leo kuna kajitu kamoja kalikuja kuomba shamba la mifugo, hajawahi kutuletea hata mbuzi, hajawahi kuleta hata kuku, miaka 40 baadaye mmempiga nyie sijui bili ya ardhi ya Shilingi milioni 4.5 anafikiria atakuja kuponea kwa wananchi? Over my dead body, hilo ni la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, Bunda Mjini; Nyatwali. Ni hivi, sheria za nchi zinasema hivi, ukitaka kuchukua ardhi ya mwananchi, lazima ufidie kikamilifu na usimwache kwenye ufukara, umpeleke katika hatua aliyokuwanayo ama hatua ya juu ya zaidi. Ukisoma Katiba hiyo hapo, ibara ya 24(2) imesema, ukisoma Sheria ya Ardhi hapa part two imesema, ukija Sheria ya Utwaaji wa Ardhi imesema. Hivi kweli ni akili leo, wananchi wa Nyatwali wako pale zaidi ya miaka 700, Serikali mnakuja mnataka kutengeneza njia ya Wanyama, yaani jinsi ambavyo mnapenda wanyama kuliko watu. Mnahamisha kata nzima ya watu 13,000 unaenda unamwambia mwananchi ninakulipa fidia square meter moja shilingi 495! Halafu unasema kama una hati ninakulipa square meter moja shilingi 704! Halafu mbaya zaidi unatoa hayo makadirio yako…

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

TAARIFA

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge kwamba mchakato wa Nyatwali tunaenda kunusuru maisha ya wananchi ambapo kumekuwa na changamoto kubwa sana ya wanyama wakali na waharibifu. Kwa hiyo, wananchi wanaoondolewa pale, siyo kwa sababu eneo lile Serikali inalitaka, ni kwa sababu tunaokoa maisha ya Watanzania.

MWENYEKITI: Unapokea taarifa?

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana nasema hivi, kwanza wananchi wa Nyatwali ni wastaarabu sana. Wamekaa pale miaka 700…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Halima, umeipokea hiyo taarifa kwanza? Subiri kwanza. Mheshimiwa Halima umeipokea taarifa ya Mheshimiwa?

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ngoja kwanza, dakika zangu zinahesabiwa kwake sasa.

MWENYEKITI: Najua. Umeipokea hiyo taarifa ya kwanza au hujaipokea?

MHE. HALIMA J. MDEE: Taarifa ya kwanza nimeipokea na reservations. Kwa nini nimeipokea? Nimeipokea kwa sababu kwa maelezo yao hao wenye meno, wananchi wanatakiwa wahame. Wananchi wamesema sawa, tumekaa hapa miaka 700, tutahama, lakini lipeni fidia kwa matakwa ya sheria za nchi yanavyosema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu Nyatwali ni Bunda Mjini, halmashauri hiyo hiyo watu wanalipwa square meter kwa vipimo ni shilingi 6,000, halmashauri hiyo hiyo Kata ya jirani basi, tufanye sawa, kata nzima inaondoka. Huyu mwananchi hawezi kubaki kata hiyo, lazima anunue ardhi eneo la jirani. Eneo la jirani square meter moja ya ardhi ni shilingi 2,000 kwenda juu mpaka shilingi 3,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachosema ni hivi, ni bahati mbaya, halafu nasikia kuna jamaa mmoja sijui anaitwa mtathmini huyu; mtathmini mmoja anaitwa Sanga. Chief Valuer anapambana na wananchi wanafurahia sana Chief Valuer anavyopambana nao, lakini kuna haka kajitu huko kanaitwa Sanga, kanawapeleka wananchi mpera mpera. Sio Sanga wewe, siyo Sanga wewe, tulia. (Kicheko/Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Halima, muda wako umeisha. Malizia dakika moja.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa usahihi na kumalizia na kwa msisitizo, mmepewa dhamana. Ninarudia, ardhi ni mali ya Watanzania. Rais amepewa dhamana yaani ni trustee kwa niaba yetu. Sheria zizingatiwe, haki itendeke. Sitaki mjibu hili suala emotional. Don’t personalize matters. Don’t personalize issues. Jibuni kwa mustakabali mpana wa wananchi wa Taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni hayo tu. (Makofi)
Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwenye hili nichangie kama ifuatavyo; kwanza ni muhimu ikaeleweka kwamba watu wanaokosoa jambo wana nia njema kuliko watu wanaoona jambo na kulichukulia kama lilivyo, hilo la kwanza. (Makofi)

La pili tuna Watanzania wenzetu wako huko nje wana akili nyingi sana, pia inawezekana kutuzidi hata sisi tuliokuwa huku ndani. Kwa hiyo, ni muhimu sana kama Taifa tukajenga utamaduni wa kuheshimu kila mchango wa Mtanzania, vilevile tukauchuja pale ambapo tunaona hauna maslahi mapana kwa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja hazijibiwi kwa ukali, hoja inajibiwa kwa upole,…

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU (MHE. UMMY H. NDERIANANGA): Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Nani amesimama kwa ajili ya taarifa? Aah Mheshimiwa Halima Mdee kuna taarifa kwa Mheshimiwa Ummy Nderiananga.

TAARIFA

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU (MHE. UMMY H. NDERIANANGA): Mheshimiwa Spika, napenda kumpa taarifa dada yangu Mheshimiwa Mdee kwamba hamna mchango ambao umedharauliwa au kupuuzwa ila ambacho tuna mashaka nacho ni michango ambayo ni ya upotoshaji na tunaendelea kuelimishana katika eneo hilo, ahsante. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Halima Mdee unaipokea taarifa hiyo.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, Taarifa ya Kamati imesema kwamba makubaliano hayo kwa sababu tukipitisha kama Bunge maana yake yanaenda kuwa makubaliano ya Kimataifa yaani Sheria ya Kimataifa inaenda kuwa International Law. Sasa tunaambiwa makubaliano yanaweka msingi wa kisheria na sio mkataba na sisi ndio tunazungumza hapa hapa kwamba kama msingi una mashaka, kama msingi una matobo, kama msingi hauna madhara kitaifa hiyo mikataba mnayosema tutaletewa hapa Bungeni lazima iendane na sheria hapa. (Makofi)

Kwa hiyo, ni kama vile hii Katiba ya Jamhuri ya Muungano hapa, Katiba ni msingi mama wa sheria zote. Haya makubaliano hapa ndugu zangu ndio msingi wa kitakachokuja. Nitatoa mfano scope Ibara ya nne inasema; “Scope of this agreement is to facilitate the implementation of areas of co-operation set out in an Appendix I of this agreement.”

Mheshimiwa Spika, Appendix I ni sehemu pacha ya huu mkataba ama haya makubaliano. Appendix I ina phase mbili; ina phase i na ina phase II. Phase I inahusu yale magati ya bandarini ambayo pamoja na mambo mengine yanahusisha magati ambayo Tanzania tulikopa almost trilioni moja kuyafanyia maboresho. Ndugu yetu wa TPA kwa haya maelezo anapewa terminal ya maboti na anapewa na terminal ya passengers ya abiria, hilo la kwanza.

Mheshimiwa Spika, la pili phase II inahusisha ku-develop, ku-manage na ku-operate mind you kwa sheria ya sasa hivi ya bandari ya 2014 na kama tulivyofanya marekebisho mwaka 2019, majukumu haya ni ya bandari. Kwa hiyo, tunasema kama nia ni njema kwa nini aspect ya PPP isionekane kwenye makubaliano yanayokuja kuwa sheria ya Kimataifa? Makubaliano haya bandari ni facilitator tu wa mazungumzo makubaliano haya hata umiliki wa ardhi, bandari hajulikani yuko wapi. Kwa hiyo nilisema phase II…

SPIKA: Mheshimiwa Halima subiri muda wako unalindwa, Waheshimiwa Wabunge kama nilivyosema, maana tuko hapa tunataka kujua vifungu vipi vina shida humu ndani. Umeeleza kuhusu scope of co-operation and implementing entities ukasoma kifungu kidogo cha kwanza, hebu kirejee tena.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, kidogo cha kwanza si ndio phase I project?

SPIKA: Ndio ulioisoma, irejee tu.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, imesema development, management and operation of General Cargo Berth one to four in container terminal berth five to six. Development Dhow Wharf Terminal and Passengers Terminal of Dar es Salaam Port to be operated by TPA. This two ndio anapewa TPA ku-operate kwa mujibu wa hii hapa.

SPIKA: Kwa hiyo, kwa ulivyosoma umeanzia huku article 4 ukasoma sub-article one, ukatupeleka huku kwenye appendix I. Umetueleza kwamba Serikali ilishawekeza pesa trilioni zaidi ya moja na hilo eneo ndilo analopewa huyu DP World. Hebu nieleweshe mimi hapo anapewa kufanya nini? Kwa vifungu hivi tulivyonavyo mbele yetu anapewa kufanya nini?

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, naomba unilindie muda wangu.

SPIKA: Unalindwa kabisa usiwe na wasiwasi.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nimesema hivi article 4 ni scope of co-operation ambayo article 4 inaenda sambamba na appendix I. Appendix I imeelezea maeneo ya ushirika ambayo katika appendix I specific eneo naomba niruhusu…

SPIKA: Nakusikiliza, umenisikia nimeongea, nakusikiliza. (Kicheko)

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo appendix I katika moja, mbili, tatu mpaka saba kwenye appendix I TPA amepewa namba two, ndio atakayo…

SPIKA: Sawa sasa twende hapo mimi nataka pale kwenye pesa ya Mtanzania ambayo ili…

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, pesa ya Mtanzania...

SPIKA: Subiri kwanza, mimi si nakusikiliza, tunasikilizana kwa sababu jamani leo sio michango ya kawaida humu ndani, ni michango kwa ajili ya hili azimio hili. (Makofi)

Mmi nisaidie jambo moja kwenye lile eneo ambalo pesa zimetumika za Mtanzania, si ndio? Hapa phase I project na wewe uko hapo inasema hapo kwenye moja; “development, management and operation” hapo. Huku mwanzoni kwenye article 4 inasema; “The scope of this agreement is to facilitate the implementation of areas of the co-operation set out in appendix I to this agreement, co-operation between this two entities” kama hivyo ndivyo na yale maelezo ambayo umeyatoa mwenyewe kwamba Serikali imeshawekeza pale. Kwa nini wewe, mimi nauliza ili nielewe maana tunataka tujue vifungu gani tupitishe, vingine vipi tukatae.

Kwa nini usifikiri lile eneo anaenda kwenye operation maana hapa yako mambo matatu, kuna development, management and operation?

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, mimi siwezi kufikiria kwa niaba ya Serikali kwa sababu hoja…

SPIKA: Ehe sasa ngoja hapo hapo umemaliza vizuri.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, kwa sababu hapa…

SPIKA: Ngoja niweke sasa vizuri hoja yangu ili nikupe muda uendelee kumalizia. Ndio maana Waheshimiwa Wabunge sasa hivi tunatoa maoni yetu ili Serikali yale ambayo wanaenda kuingia kwenye hiyo mikataba wakayatazame. (Makofi)

Huu mkataba haujaweka msingi kwamba kwenye eneo hili la zero mpaka berth sijui saba huu mkataba hauwezi kusema anaenda kufanya nini pale, wala hausemi. Unaeleza maeneo ambayo anaweza kupelekwa sio anapelekwa. Kwa nini anaweza kupelekwa? Kwa sababu kifungu cha tano ambacho kimetajwa sana huko nje kimeweka misingi ya hayo ili waweze kukubaliana, lazima wakubaliane kamoja kamoja ambayo hawakubaliani anaweza kupewa mtu mwingine au akaendelea yeye mwenyewe TPA. (Makofi)

Sasa Mheshimiwa Halima nilitaka mimi mwenyewe nielewe vizuri maana leo lazima tuongozane vizuri humu ndani, nje mambo ni mengi. Nilitaka nielewe pale kwenye uwekezaji na maadamu umesema kwamba huwezi kujua Serikali inapeleka wapi, haya endelea na mchango wako.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, huu mkataba ni baina ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Dubai na DP World ametajwa hapa specifically. Kwa hiyo, hata kama tutazunguka mbuyu kwa kiwango gani tunachozungumza hapa hivi vitu vyote viwe vitatu, kiwe kimoja, viwe viwili lazima apewe. Kwa hiyo, tukipitisha mkataba atapewa hilo ni la kwanza.

SPIKA: Lazima apewe unaitoa wapi Mheshimiwa Halima? Maana lazima tukae sawa leo ile lazima apewe yeye umeitoa wapi? (Makofi)

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, unajua kwa nini naitoa kwenye haya makubaliano, wamekubaliana ushirika wa mambo yote yaliyozungumzwa hapa.

SPIKA: Hapana twende vizuri, vifungu humu ndani vimetaja mambo mahususi kwamba ni lazima yeye apewe; wapi pamesema?

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa taarifa.

SPIKA: Twende tu vizuri mimi na wewe ni mwanasheria, ingawa wengine wote watatutaka sisi wanasheria tukae sawa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru wewe ni Mwanasheria tena mbobevu. Haya makubaliano Bunge leo likipitisha whether pameandikwa ni lazima apewe, ama asipewe haya makubaliano yametoa ulazima yakipitishwa kwamba chochote kitakacho…

SPIKA: Huo ulazima ndio nataka kujua unapoutoa mwanasheria mwenzangu, huo ulazima unatokea wapi? (Makofi)

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, ni hivi labda…

SPIKA: Mimi naweza kukuelewa sana ukisema kwamba yaani huu mkataba ama haya makubaliano yanaweka msingi ili umalizie hoja yako kwa maana ya kwamba kwa sababu haya yanaweka msingi, naishauri Serikali inapoenda kuingia mkataba itazame hapa na hapa na hapa. Ukisema inaweka ulazima hilo mimi siwezi kukukubalia kwa sababu sijapaona humu ndani panapoweka ulazima, sijapaona.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa taarifa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, aah come on Mheshimiwa…

SPIKA: Nani anataka kuzungumza?

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Jerry Silaa.

SPIKA: Sasa taarifa unanipa mimi au Mheshimiwa Halima?

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Halima Mdee.

SPIKA: Ngoja tumalize kwanza hoja yetu, kabisa ni uhuru wa maoni ila leo Bunge hili ni la tofauti linatoa maoni na linatoa elimu kwa umma kwa sababu kumekuwa na upotoshaji mkubwa sana. Kwa hiyo, tunajadiliana kwa uhuru kabisa leo lazima tutoke humu ndani sisi wenyewe tukiwa tumeelewana, Mheshimiwa Halima. (Makofi)

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, kwa maneno yako mwenyewe kwamba mkataba huu ama makubaliano hayo yakipitishwa yanaweka msingi, na naweka msisitizo yanaweka msingi na huo msingi unatakiwa uzingatiwe kwenye sheria ama mikataba mingine yoyote midogo midogo itakayokuja. (Makofi)

Kwa mantiki hiyo kama msingi una matatizo na nashukuru Profesa hapa wakati anazungumza amesema kama kuna matatizo maana yake tunajua kuna matatizo…

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, tunapaswa kukubali kwamba…

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, hilo la kwanza, la pili,…

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie.

SPIKA: Inatokea wapi taarifa?

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie.

TAARIFA

SPIKA: Aah Mheshimiwa Patrobass Katambi.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kumkumbusha na kumpa taarifa Mheshimiwa Halima msomi mwenzangu katika kile kwenye suala la msingi ambalo anausema, ni vizuri akajua all contracts are agreements, but not all agreement are contracts. Kwa sababu msingi wake ni kwamba ukisoma hayo anayoyaeleza, ukisoma article one ya sheria hii ambayo itasomwa pamoja na kifungu cha tano utaangalia pia na huku kwenye appendix kwenye phase I ndipo utapata tafsiri ya pamoja kwenye hili. Hata kwenye eneo ambalo amezungumza kuhusu ardhi ukienda kwenye interpretation inaeleza kwamba excluding…

SPIKA: Haya ahsante sana kwa sababu taarifa ni moja, umechagua ile ya sehemu ya kwanza, hii ni sehemu ya pili ahsante sana. Mheshimiwa Halima Mdee unaipokea taarifa hiyo.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, kwenye appendix hiyo hiyo ambayo inatokana na hiyo scope phase II imejumuisha ports zingine imejumuisha maziwa na vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Spika, nazungumza mawanda…

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU (MHE. UMMY H. NDERIANANGA): Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa bandari ama taarifa ya bandari.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU (MHE. UMMY H. NDERIANANGA): Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, tuna bandari kadhaa, kama hamtaki tuchangie basi mseme.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, tusikilizane tusikilizane, tusikilizane taarifa hiyo itakuwa ni taarifa ya tatu nafikiri sio, ni taarifa ya tatu na ya mwisho.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, ya pili hujanipa.

SPIKA: Sasa siwezi kuwapa wote wawili; Mheshimiwa Naibu Waziri.

TAARIFA

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU (MHE. UMMY H. NDERIANANGA): Mheshimiwa Spika, analolizungumza Mheshimiwa Halima la scope ya nafasi ya pili maana yake ni kwamba sisi tukishaingia makubaliano Tanzania na Dubai, tukishawapa hawa DP World wakifanya, tukijiridhisha, tukatathmini, tukajua wanaweza kufanya vizuri, tuna uwezo wa kuwapa nafasi. Tukiona hawawezi tuna uwezo wa kuwapa kampuni zingine zikafanya kazi hiyo, kwa hiyo asipotoshe, aseme vizuri. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Halima Mdee, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, analolisema yeye analisema yeye, halipo hapa. Nimesema article four inazungumzia scope imerejea appendix I, appendix I ina phase mbili; phase ya kwanza ni hiyo niliyozungumza, phase ya pili, two inasema; development, management and operation of additional sea and/or lakes ports.

Mheshimiwa Spika, mawanda yamekuwa mapana kwa bandari ambazo tunazo, Bahari ya Hindi ukiacha hiyo ya Dar es Salaam, kwa sababu hili suala sio la Dar es Salaam, ni Dar es Salaam na bandari nyingine, Bahari ya Hindi tuna bandari 12, Ziwa Victoria tuna bandari 24, Ziwa Tanganyika tuna bandari 19, Ziwa Nyasa tuna bandari 11 hizi ni zile ambazo zimekamilika kisheria. Kwa hiyo, tukisema hili jambo ni la nchi linahusisha bandari, maziwa 66. Kwa hiyo, iko mbele kwa kisheria, ukija ambazo… (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Halima, hayo maeneo yote ni katika huu mkataba, yaani kwa maana ya kwamba Tanzania na Dubai moja?

MHE. HALIMA J. MDEE: Yes, mkataba huu…

SPIKA: Wapi pamesema?

MHE. HALIMA J. MDEE: Hawaja mention, wametoa ruhusa ya jumla...

SPIKA: Sasa unaona hiyo ndiyo changamoto? Kama hawajataja mbona una-speculate?

MHE. HALIMA J. MDEE: Nina speculate kwa sababu mimi ninaona mbele. Ninaona mbele kwa sababu gani? No, no, no naomba tusikilizane, naomba tusikilizane. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Halima ngoja, ngoja, ngoja muda ninaozungumza na wewe naulinda usiwe na wasiwasi, muda ninaozungumza na wewe ninaulinda.

Waheshimiwa Wabunge, tuelewane vizuri hili kwa sababu nilishasema mwanzo kwa hiyo nitazungumza nikiwa nimekaa. Kanuni zetu, Kanuni ya 111 inasema hivi; “Majadiliano wakati wa kujadili hoja ya kuridhia mkataba yatahusu masharti ya mkataba husika.” (Makofi)

Kwa hiyo, hakuna mkataba nje wa haya unaoweza kuzungumziwa kwenye ngazi hii, lakini nimwelewe yeye anasema kwamba anaona mbali. Kwa hiyo, anatoa maoni yake Waheshimiwa muyasikilize upande wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Halima Mdee.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nisikilize, unajua vitu vingine vinachosha. (Kicheko)

Kwa hiyo, mimi niseme tu mkataba huu tofauti na wengi wanavyosema kwanza haufanani kabisa na Mkataba wa TICTS, wala usifananishe, kwa sababu wa TICTS zilikuwa zinahusu zile berth nne, hii ni kubwa na ni pana kuliko TICTS. Sasa kama huu mkataba unagusa Mtwara, unagusa Dar es Salaam, unagusa Tanga, unagusa Mwanza, unagusa Kigoma na Lake Tanganyika ipo na Lake Nyasa, Lake Victoria ipo kwa nini lisizungumzwe kwa mapana yake? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pili kuna hiki kitu kinaitwa Exclusive Economic Zones,kwa taarifa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Halima, nilikuwa najishawishi kukuongeza muda lakini sasa namna unavyosema mkataba huu unahusisha hizo bandari na kifungu huna, unasema unawaza baadaye kwa kweli kengele ya pili imeishagonga sekunde thelathini malizia sentensi.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, ulisema unanilindia muda wangu...

SPIKA: Nimeshaulinda.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nasema hivi mkataba huu hili suala serious sana, na nilisema wakati ninaanza tukipitisha leo tuna nafasi ya kubadilisha, lakini hatutabadilisha, tukipitisha leo maana yake huu unaenda kuwa mkataba ama makubaliano ya Kimataifa ambayo yako legally binded. Kwa hiyo, chochote kilichotajwa humu kiujumla jumla kwa sababu kimetajwa kiujumla jumla, kinachohusu ports zetu zote kinahusika…

SPIKA: Mheshimiwa Halima, muda wako umekwisha, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. HALIMA J. MDEE – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI ZA MITAA (LAAC): Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi niliyopata ya kuweza kufanya majumuisho. Lakini vilevile nichukue nafasi hii kuwashukuru Waheshimiwa Wajumbe/Wabunge mliochangia ambao mliochangia kwa kuzungumza ni zaidi ya 78 na wengine ambao mmechangia kwa maandishi.

Mheshimiwa Spika, nitajibu hoja kadhaa halafu nitakuja kwenye Maazimio. Jambo la kwanza ambalo nilikuwa nataka kulizungumza ni kuhusiana na haja ya upande wa Serikali na watendaji kuchukulia Taarifa za CAG kwa uzito wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, umesema hapa mwezi Juni tulikuja hapa kupitia utekelezaji wa Serikali wa maagizo ya CAG. Kwa upande wetu sisi Serikali za Mitaa mpaka tunatoa taarifa hapa, kulikuwa hakuna agizo hata moja lililotekelezwa kwa ukamilifu wake. Kwa hiyo tunavyosema Serikali muwe makini tunasema muwe makini na muwe serious kwa sababu sisi tunakutana na maafisa masuuli kwenye vikao vya Kamati. Ni muhimu ikaeleweka kwamba majibu ambayo yataua ama kumaliza hoja za kaguzi siyo majibu ambayo Mawaziri mnatupa hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, majibu yatakayomaliza hoja za kaguzi ni majibu ambayo Mkaguzi atayapata kwenye vikao lakini vile vile wakaja kufanya verification kwamba tumesema tumekwama hapa, Serikali mnajibu hapana hatujakwama tumeenda hapo; unayetakiwa kumpa uthibitisho ni Mkaguzi wa hiyo hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mantiki hiyo maelezo waliyokuwa wanayatoa Mawaziri hapa na sisi ambao tulikuwepo kwenye vikao mpaka juzi, mock LAAC za mwisho kwenye LAAC, mock LAAC yaani vikao kati ya Ofisi ya CAG na upande wa Serikali vilifanyika kuanzia Oktoba 3, Oktoba 2, Septemba majibu yaliyokuja ndiyo yamepelekea Taarifa zetu hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivyo basi ndugu zangu; kama kweli tuna dhamira ya kusaidia hii nchi iende, hayo majibu mnayoyasema kwa sasa hayana maana mpaka CAG aka-verify. Kwa hiyo, ni muhimu mzingatie hilo Mawaziri na mimi kwenye Kamati yetu wamekuja Mawaziri wa TAMISEMI, wawili Naibu Mawaziri wanamuwakilisha Waziri wanakuja na Makatibu Wakuu. Kwa hiyo, ninashangaa Waziri anasimama hapa anasema yeye kwake anakuja anakuta hapa ni kitu kipya, hili ni jambo ambalo mnatakiwa mjue wote. Waziri aje na Katibu Mkuu wake aje; akituma mtu aje akupe mrejesho. Ndiyo tunasema hakuna connectivity ya kazi au utendaji kazi hakuna connection. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni bahati mbaya sana watu waliopewa dhamana ya kusimamia fedha za nchi hii hawana uchungu wa kusimamia fedha za nchi hii. Kunahitajika nguvu ya ziada, kunahitajika mkono wa chuma kusimamia watu waliopewa dhamana ya kulinda fedha zetu; kwa nini nasema hivi? Tunataarifa hapa ya madeni kwa mfano ambayo hayakupelekwa kwenye mifuko ya hifadhi (makato).

Mheshimiwa Spika, unakuta Halmashauri ya Mpanda kwa mfano, hawakuwasilisha shilingi milioni 56.52 lakini kwa sababu mifuko yetu inavifungu vya adhabu vya faini inayotolewa kila mwezi kwa watu ambao hawapeleki michago; leo Mpanda adhabu ni shilingi milioni 514. Tuje Bunda, walitakiwa wapeleke shilingi milioni 56, hawakupeleka; faini shilingi milioni 114. Shinyanga, walitakiwa wapeleke shilingi milioni 205 hawakupeleka. CAG anasema eti faini imeenda mpaka shilingi bilioni 45, sisi tunajiuliza hawa watu walizembea muda gani mpaka faini zika-accumulate to this sum? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watu wamepewa dhamana. Hivi ni vitu ambavyo kama chain ya Serikali inafanya kazi ipasavyo, kuanzia Wakurugenzi, kuanzia Wakuu wa Mikoa, kuanzia Mawaziri wangeviona hivi vitu; huwezi kukaa usubiri CAG aje aone hivi vitu. Nilisikia hapa watu wakizungumza kuhusiana na CAG jukumu la controllership la CAG kwa mujibu wa Ibara ya 143(2)(a) ya Katiba kwa sababu kuna maeneo matatu ambayo ni majukumu ya CAG.

Mheshimiwa Spika, udhibiti wake uko kwenye (a) kuhakikisha kwamba fedha zozote zinazokusudiwa kutolewa kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali matumizi yake yameidhinishwa na kwamba zitatolewa kwa mujibu wa masharti ya Ibara ya 136 ya Katiba hii na iwapo watatosheka kwamba masharti hayo yatatekelezwa ipasavyo basi ataidhinisha hizo fedha zitolewe. Hiyo ndiyo udhibiti, role aliyopewa CAG. Sasa mnataka CAG akafanye kazi ambazo wanatakiwa wafanye Wakurugenzi huku ya kukimbizana hela? Come on! (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, hivi tunsema tumeajiri watu wa kazi gani? Ndiyo maana nikisikiaga eti imeundwa task force, nasema task force ya nini? Yaani mmeajiri watu, mnalipa watu mishahara, wamesababisha tatizo, kuenda ku-rectify tatizo mnaunda task force? For what? For what? Kuna tatizo kubwa sana la mfumo ambao lazima wafanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili; ni bahati mbaya natakiwa nijibu zangu tu, yaani ningekuwa nachanganya na nyingine watu hawajali. IPTL, hizi fedha hizi wanazoenda kulipwa ni za watu kutokujali, ni deal tu, kwa sababu Serikali ilienda kuweka fedha kwenye Escrow Account. Ule mkopo ulitakiwa ulipwe Escrow Account haikulipiwa. Si mfuate maneno ya mtaani wakati ana watu. Nimesema tu nachanganya; watu hawajali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, SYMBION katika taarifa ya mwaka jana alilipwa zaidi ya milioni 300 ambazo hakutakiwa apewe, watu hawajali. Tunataka mjali. Siyo sifa kupanda VX na kuwa Waziri pekee, siyo sifa kupanda VX na kuwa Katibu Mkuu, sifa tendea haki nafasi yako.

Mheshimiwa Spika, Kamati yako ya LAAC, nawashukuru wajumbe wangu tunafanya kazi mpaka saa sita usiku. Siku moja niliwaambia, wa TAMISEMI niliwaambia kazi inayofanywa na LAAC basically ni kazi iliyotakiwa ifanywe na wakurugenzi, ni kazi iliyotakiwa ifanywe na TAMISEMI. Sasa mnatuletea vitu ambavyo vimeshindikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi vitu vinauma, vinakera, vinachefua. Nawashukuru Waheshimiwa Wabunge mmechangia vizuri. Hivi nchi hii wakurugenzi tunawapataje? Yaani mtu ambaye mmempa dhamana ya kwenda kusimamia halmashauri kitendaji kuwa accounting officer kupokea mabilioni ya shilingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo kule kwenye halmashauri zinaenda billions of money, ukiuliza mkurugenzi amepatikanaje? “Kashindwa kura za maoni”, wapambe. Maana nimegundua nchi hii yaani ukishakuwa kiongozi, yaani kabla hujawa mtu mkubwa wapambe hawapo ukishapata nafasi zenye uteuzi wapambe wanakuzunguka. Mamlaka ya uteuzi inawezekana group hili la wakurugenzi ninaamini linavurugwa na wapambe zaidi.

Mheshimiwa Spika, naomba sana, kama nchi tuangalie upya namna wakurugenzi wetu wanavyopatikana. Nilikuwa napitia kitu kinaitwa the local government financial memorandum ya mwaka 2009. Kuna kitu kinaitwa responsibilities of the director. Yaani kuna responsibilities hapa kama 12, ni nzito ambazo zinahitaji mtu mwenye weledi na taaluma na uzoefu wa hali ya juu katika usimamizi wa fedha, katika kusimamia watu, katika utawala na mambo mengine.

Mheshimiwa Spika, tumeshuhudia wakurugenzi tuliokutana nao huko unakuta kakurugenzi yaani katoto, DT ni kama baba yake. Ukiuliza umetokea wapi? “Nimetokea sekta binafsi”, hasemi sekta binafsi wapi. Kwa hiyo, ukiangalia hata wage bill, muulize Mheshimiwa Mwigulu hapo. Wage bill inaongezeka kwa kiwango kikubwa kwa sababu moja kubwa, tunaokota watu nje ambao hawakuwa kwenye mfumo, tunampa nafasi ya kulipwa mshahara mnono. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, turudie utaratibu wa kila wenye vigezo vilivyowazi watu washindanishwe. Mimi nina mifano yangu hapa, mtiririko wa makusanyo ya mapato. Unakuta halmashauri kama Kigoma DC, nadhani, ilikadiria kukusanya shilingi milioni 700 ikakusanya shilingi milioni 688. Kigoma DC, OC iliyotoka Serikali Kuu; yaani hapa kuna watu wameshiba, watu wazima na akili zao, shilingi milioni 688 mwaka mzima. Yaani akili zao zote zile milioni mia 688 makusanyo ya ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukija kiasi cha OC, matumizi ya kawaida walichochopewa na Serikali Kuu ni shilingi bilioni 16.3. Yaani kuna watu wazima wamekaa kule chini wanalipwa mshahara. Hiyo ni OC, sijazungumzia miradi ya maendeleo fedha ilivyoshushwa. Sasa unajiuliza hivi kuna faida gani ya kuwa na wakurugenzi, maafisa mipango na ma-DT kule chini ambao hawako creative ku-deal na vyanzo vya mapato, ama kuhakikisha vilivyopo vinatosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unakutana na mkurugenzi anakwambia kwamba sisi tunafanya shughuli ya kilimo. Kwa kuwa mvua hazijanyesha mapato yetu yameshuka, mkurugenzi! hivi hizi ni akili? Kwamba ameweka pale kusubiri mvua? Sawa, si lazima uwe mbunifu, kama unasubiri mvua kuwa mbunifu na umwagiliaji. Kama huna, tafuta vyanzo vingine, tengeneza fedha itengenezwe. Tuna wakurugenzi ambao hawana uwezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana Serikali iweze kutekeleza wajibu wake ipasavyo. Madeni ya wazabuni, tumeweka maazimio yetu naamini hayajabadilika, ni yale yale tu, kwa hiyo, tutayapitisha tu haraka haraka.

Mheshimiwa Spika, madeni ya wazabuni ni crisis nyingine, alisema Mheshimiwa Hawa Mwaifunga hapa, kwamba hii ni sampling. Si mkaguzi amesema bilioni nane point kadhaa, sisi tumekutana na halmashauri takriban 79 kwenye hii mikutano miwili. Hii juzi tumekutana na 39. Kwa fedha tu za ndani za halmashauri pekee hii taarifa ya CAG inazungunguka mara mbili. Si alisema shilingi bilioni nane, tunazungumza hizi halmashauri ambazo tumekutana nazo sasa hivi, na hazifiki 40; hamlipi fedha za wazabuni. Sasa tumeingia sisi kufanya kazi ya Serikali. Mnajua mlichofanya? Mkiambiwa mdawaiwa shilingi ngapi na wazabuni? shilingi kadhaa, mwaka huu mmefunga kiasi gani? Wakasema hapana tumetenga kidogo. Ndiyo allocation mnaenda kufanya Disemba? Ndiyo; fanyeni reallocation, mwaka ujao shilingi ngapi.

Mheshimiwa Spika, yaani sisi tunaweza kuwa na vikao vya Kamati kuwafanyia mambo ambayo mlitakiwa mfanye ninyi. Kwa hiyo, kila mkurugenzi aliyekuja kwenye Kamati yetu tumeshampa mpango wa kwenda kulipa wazabuni wote. Lakini najiuliza; kwa nini sisi wajumbe wako tukeshe, yaani sisi tukeshe halafu jamaa wapo hapo, haiwezekani. Natambua kazi ambayo Mchengerwa ameanza nayo, natambua, lakini tunasema hivi, kama Mheshimiwa Mchengerwa hamtatatua dudu la wakurugenzi wa hovyo wanaopatikana, wasiokuwa na uwezo; siyo wote, kuna ambao wanaweza, niseme neno baadhi, wasiokuwa na uwezo. Nakwambiaje, utaishia kutumbua. Yaani itakuwa miaka yako inaisha unatumbua, ukimaliza kutumbua huyu, unakuja unatumbua mwingine halafu fedha ya umma imepotea. Tuanze kutibu tatizo from the core tuangalie source.

Mheshimiwa Spika, sasa nashauri, yeye ni Waziri bwana, mimi sina access na Mheshimiwa Rais; akamshauri Mheshimiwa Rais ili aliangalie hili eneo kwa mapana na mawanda yake kwa sababu kuna impact kubwa sana tukiwa na wakurugenzi wazuri kule chini. Yaani impact kubwa ya kimapato ya kiutendaji na kiufanisi. Tufikirie nje ya box. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni la madai ya wafanyakazi, bilioni 119. Sasa ndugu yangu Simbachawene naona hayupo; amekuja hapa katutajia figure zake kaondoka. Sasa hajatwambia katika figure zake zile Serikali Kuu ni ngapi, halmashauri ni ngapi. (Kicheko/Makofi)

SPIKA: Usiwe na wasiwasi Waziri Mkuu yupo.

MHE. HALIMA J. MDEE – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA Bunge YA HESABU ZA SERIKALI ZA MITAA (LAAC): Mheshimiwa Waziri Mkuu yule kijana wako; amekuja ametutajia figure zake kaondoka, si ndiyo? Sasa mimi na timu yangu kwa taarifa ambayo mpaka tunawasilisha taarifa yetu Bungeni na kwa Spika na ambayo Mock LAAC zilivyokaa zimethibitisha ni kwamba kwenye halmashauri kuna bilioni 119 hazijalipwa. Hii taarifa imeeleza kila halmashauri inadai kiasi gani. (Kicheko/Makofi))

Mheshimiwa Spika, wanakuja watu wa Wizara tunawaambia okay, Wizara ya fedha ninyi si mmesema mmelipa bilioni ngapi, wanatutajia figure za kutisha ili kukupoteza confidence. Sawa basi twambie hivi, halmashuri hii mmelipa nini, halmashauri hii mmelipa nini, wanakimbia, hawana majibu. Sasa sisi tunasema hivi, mpaka sasa licha ya majibu aliyoyatoa kaka yangu Simbachawene hapo, ya kwake, ambayo hayajawa verified, Serikali inatakiwa ilipe madai ya watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Jesca amezungumza hapa, tulikuwa Kigoma nadhani kama siyo Kigoma ni halmashauri moja wapo. Yuko DT…

(hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie. Halmashauri mojawapo, Kigoma DT amekaa pale anatujibu maswali amenyong’onyea. Sasa Jesca akafanya utundu kidogo, akachukua kile kitabu akaanza kuchambua baada ya kusikia watu wamejitambulisha. Kumbe yule jamaa DT anaidai Serikali shilingi milioni 40, yaani amekaa pale ndiye DT halafu ndiyo tunategemea yeye atupe majibu, kalipeni watumishi wa umma. Kujisifu kwa mbwembwe hakusaidii, mbwembwe zitajijibu zenyewe kwa matendo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa sehemu ya tatu, tunaomba sasa Bunge likubali mapendekezo yale ya Kamati kama nilivyoyasoma na kama ambavyo Hansard imeyaingiza. Baada ya kusema hayo nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa kunisikiliza.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja ili mapendekezo yetu ya Kamati yaweze kupita. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Awali ya yote nitumie nafasi hii kumpongeza Waziri na timu yake kwa kazi nzuri ambayo amefanya Jimboni kwangu, anajua mimi siyo mtu wa kusifia sifia lakini pale ambapo mtu anakuwa anaonesha kitu cha maana lazima tumpe credit zake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunavyozungumza eneo la Chasimba ambalo lilizungumzwa sana Bunge hili, sasa hivi wananchi wameshapimiwa, Wataalam wa Wizara walikaa pale siku 30 wameweka kambi, hawakulipwa posho, walikuwa wanapika kama vile wako shuleni. Kwa hiyo kwa kweli nashukuru sana na wananchi wa Chasimba, Mtaa wa Basihaya wana-appreciate kazi nzuri mliyoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na sifa hizo ambazo nimezitoa Jimbo la Kawe bado lina changamoto nyingi sana, kuna migogoro ya ardhi mingi bado na Mheshimiwa Waziri nimpongeze kwa sababu hotuba yake ime-reflect maoni ya Waziri Kivuli wa miaka mitano iliyopita. Naona anachokifanya hapa ndicho kile ambacho tulikuwa tunamshauri afanye na ndiyo maana anapewa credit kwa sababu alijua kwamba Tanzania inajengwa na watu wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa namwomba katika muktadha huo huo wa kuchukua mawazo yetu kwenye masuala ya kuchukulia hatua watu ambao wanamiliki maeneo makubwa ya ardhi na hawayaendelezi asiwe na double standard. Kama kuna kada wa CCM haendelezi achukue, kama kuna kada wa CUF haendelezi achukue, kama kuna kada wa CHADEMA haendelezi achukue. Asipofanya hivyo na sisi tutakuja hapa tutamsulubu kwa ubaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi yalizungumzwa masuala ya migogoro ya wakulima na wafugaji, tunategemea Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha hapa, atatueleza kwa sababu Wizara yake ndiyo Mama, hizi Wizara nyingine zinamtegemea yeye katika kuonesha mwelekeo. Kwa hiyo, tunatarajia majibu yake yeye yatatoa mwelekeo wa Taifa kwa kushirikiana na Wizara zingine, ili tujue tunaendaje kutatua migogoro hii kwa kuhakikisha tunaweka ama tunapanga matumizi bora ya ardhi. Kwa hiyo, nategemea atakuja na hayo majibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanja 20,000 ama mradi wa viwanja 20,000. Nasisitiza kama ambavyo nilisisitiza miaka kadhaa iliyopita, tunaomba ifanyike audit ya vile viwanja, kwa sababu tunajua sekta ya ardhi ilikuwa imegeuzwa sehemu ya wajanja wachache kujinufaisha kwa maslahi yao. Tukiweza kufanya audit katika hivi viwanja, tutajua nani anamiliki nini, tutajua viwanja vya wazi ni vipi na tutajua viwanja vya huduma za jamii ni vipi. Kuanzia hapo tutaweza kujua Serikali iliweza kufanikisha ama ilishindwa na turekebishe nini. Kwa hiyo, naomba sana atueleze kama hiyo audit itaanza kufanyika na ifanyike lini, atagundua madudu mengi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulizungumza suala la migogoro ya Jimboni kwangu, eneo la Nyakasangwe, Kata ya Wazo. Huu mgogoro ni wa muda mrefu, utatuzi wa huu mgogoro ulishaanza kufanyiwa kazi toka mwaka 1998 na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mheshimiwa Makamba. Kuna nyaraka zote tumezipeleka Wizarani kwake na barua ya mwisho tumepeleka tarehe 20 Januari, 2017.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro huu unahusu wananchi wasiopungua 4,000, tunamwomba Mheshimiwa Waziri, tulimaliza hatua mbalimbali za kisiasa na za kitaalam, tukafikia hatua ya kuanza kutambua wananchi kwa kushirikiana na MKurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni, kwa sababu tunajua yeye ndiyo mamlaka yenye uwezo wa kushughulika na masuala ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunataka kufikia mwisho, hawa Viongozi vijana mnaowateua teua hawa wanaopenda kuuza sura, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, akaja akataka kuvuruga mambo wakati Ofisi ya Mkurugenzi na Viongozi waliopita wote wa Mkoa na Wilaya tulikuwa tumeanza kufika sehemu ya mwisho. Sasa yule dogo sishughuliki naye kwa sababu siyo saizi yangu, mimi nakwenda kwa Mheshimiwa Waziri. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu mimi na Mkurugenzi tumeshafika sehemu nzuri na wananchi, tumekaribia kumaliza tulete Wizarani, dogo anataka kuingilia, sasa tumemwandikia barua tarehe 20 Januari, 2017 tumeambatanisha nyaraka zote, tunaomba Ofisi yake ilitafutie ufumbuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunataka kulimaliza, juzi amekuja mtu ama Mtaalam Mshauri anazunguka eneo la Nyakasangwe, Kampuni ya Nari, anasema yeye ametumwa na Kiwanda cha Wazo na kwamba Kiwanda cha Wazo kilipewa mamlaka ya kufanya utafiti ama leseni ya kufanya utafiti na kwamba lile eneo inasemekana lina madini, kwa hiyo wameanza kufanya survey na kuweka alama na kuzua taharuki kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hili suala nimeshakabidhi Wizara ya Nishati na Madini. Kwa hiyo, wakati Mheshimiwa Waziri ananipa majibu yake kama Waziri wa Ardhi natarajia vilevile Waziri wa Nishati na Madini anayekaimu ambaye ni Naibu sasa, atatoa majibu ili wananchi wangu waache kuishi kwa taharuki, hilo la Nyakasangwe nimemaliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Boko kwa Somji, nimesema leo naenda Kijimbo jimbo zaidi kwa sababu wananchi wa Kawe ndiyo wananiweka mjini. Suala la eneo la Boko na lenyewe liko Wizarani kwake ni mgogoro wa muda mrefu sitataka kuongea kwa kina hapa, lakini tokea mchakato wa upatikanaji wa hili eneo, toka kipindi kile cha sheria za Mkoloni, taratibu hazikufuatwa. Nitampelekea Mheshimiwa Waziri kabrasha ili aweze kulifanyia kazi kwa sababu kuna matapeli pale wanazunguka, wanasema ooh, tunataka tulipwe fidia, sisi ni wamiliki halali wakati mmiliki halali alishakufa, wakati Serikali iliishataifisha eneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa namwamini Mheshimiwa Waziri katika kufanya maamuzi wala sina shaka katika hilo na ardhi ni mali ya umma, tusiruhusu wajanja wachache ambao walitumia ombwe lililokuwepo, wakati watu wengine wanaongoza Wizara ya Ardhi kuweza kuvuruga mustakabali wa wananchi. Kwa hiyo, naomba suala la Boko kwa Somji tulimalize ili basi kama ambavyo tulivyopima Chasimba, tupime Nyakasangwe, tupime Boko kwa Somji maisha ya wananchi wangu yaende kuwa mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana tulikuwa tunazungumza kuhusiana na suala la ardhi, umiliki wa ardhi na nafasi ya mwanamke katika umiliki wa ardhi, nimwombe Mheshimiwa Waziri wanawake wanatengeneza asilimia zaidi ya 80 ya labour force ya kilimo, tunaomba sheria zinazowakandamiza hawa wanawake, zisipofanyiwa marekebisho Sheria za Kimila, hata kama tuwe na sheria nyingine nzuri kwa kiwango gani hawa wanawake hatutawasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuomba kwa dhati, kweli Sheria ya Ardhi Namba 4 inasema haki, Sheria Namba 5 inasema haki, lakini sheria zetu zinatambua Sheria za Kimila. Sasa kama haya mambo ambayo yanamilikiwa kimila yasipokuwa formalized, tutakuwa tunafanya biashara kichaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, tuangalie haya mambo kwa kina, tusaidie wanawake ili tuweze kujenga Taifa letu kwa usawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, leo nimekuwa mpole kidogo, nashukuru na nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi anayoifanya.
The Written Laws (Miscellaneous Amendments) (no. 6) Bill, 2021
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru na mimi kupata nafasi ya kuchangia Sheria ya Mabadiliko ya Sheria Mbalimbali, Namba (6) ya Mwaka 2021. Nikianza na Sheria ya Kodi ya Mapato, Sura Namba 332, (The Income Tax Act) ambayo pamoja na mambo mengine inafuta Kifungu cha 83(b) ambayo ilianzisha Kodi ya Zuio ya Asilimia Mbili.

Mheshimiwa Spika, naungana na wote ambao wametambua umuhimu wa kipengele hiki kufutwa, lakini siyo sifa sana pale Bunge linapotunga sheria halafu baada ya miezi minne Bunge hilohilo linakuja kurekebisha sheria, siyo sifa sana. Kamati ya Bajeti inayofanya kazi kwa niaba ya Bunge tuliliangalia hili jambo tukaelekeza Serikali namna ya kufanyia kazi, Serikali ikapiga chini lakini na Bunge letu sisi hapa, tuliwajibika na sisi kuangalia kwa kina ili tusimame imara kama Bunge kuzuwia sheria za namna hii.

Kwa hiyo, ninakiri kwamba, kuna uzembe kwa upande wa Serikali kutokufanya tafiti na kujua kwamba, tukianzisha kodi ipi, itakuwa na faida ipi, lakini vilevile na sisi kama Bunge tunatakiwa Kamati za kisekta ama Kamati mahususi zikileta mapendekezo tuyaangalie, tuyadadavue na tuyafanyie kazi kwa ufanisi kwa maslahi mapana ya wananchi tunaowawakilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niungane na maoni ya Kamati ambayo yamependekeza, na ninaomba Serikali ilichukulie hili kwa umakini sana kwamba Serikali iimarishe vitengo vya utafiti.

MWENYEKITI: Nimekuona Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango. Taarifa.

T A A R I F A

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba nimpe Taarifa mchangiaji. Pamoja na mawazo mazuri na yeye ni Mjumbe wa Kamati, tunashauriana kuanzia kwenye Kamati.

Mheshimiwa Spika, jambo hili kufika hatua hii Bunge halijafanya uzembe wala Serikali haijafanya uzembe, isipokuwa Mheshimiwa Rais aliona umuhimu wa kufanya jambo hili kwa sababu, katika majira haya sekta ya kilimo imepigwa na majanga mbalimbali yakiwemo mambo ya mbolea, yakiwemo mambo ya bei, akaona kwa sababu, sekta hii pia haikufaidika na fedha za Covid licha ya kwamba, na sekta hii imeathiriwa na Covid basi iweze kupata nafuu ya kupunguza baadhi ya kodi ambazo zilikuwa zimekusudiwa kukusanya fedha na fedha hiyo ipatikane kutokea maeneo mengine ili wananchi waweze kupata nafuu.

Kwa hiyo, si kwamba, ni uzembe wa Serikali ama uzembe wa Bunge, bali ni huruma ya Mheshimiwa Rais kwamba kwa sababu tumeshapata fedha sehemu nyingine na sekta hii haikunufaika basi tuna sehemu ya kufidia fedha hii tuondoe hii kodi ambayo inaweka maumivu kwa wananchi. (Makofi)

MWENYEKITI: Taarifa hiyo, unapewa Mheshimiwa Halima.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, siwezi kuipokea kwa sababu Rais ni kichwa kimoja, Bunge ni vichwa vya watu wengi tunaowakilisha wananchi. Ni jambo la aibu Mheshimiwa Mwigulu ukisema kwamba ni sahihi Bunge kupitisha kifungu ambacho ni kibovu na kukiri kwamba mpaka Rais akaone kifungu kibovu ndio alete. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana nasema collective responsibility, hata mimi ni Mjumbe wa Kamati, sasa ukitaka tuzungumze ya Kamati na wewe ulituambia nini na ulikuja kufanya nini, hatutaki kufika huko. Tunasema uwajibikaji wa pamoja sisi kama Bunge tulitakiwa tuwe na jicho la ziada ili mambo yasitokee. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, lakini nilikuwa nazungumza suala la utafiti wa sera.

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mwenye taarifa endelea.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, naomba uulinde muda wangu.

SPIKA: Muda ulindwe Katibu.

T A A R I F A

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, kwa unyenyekevu mkubwa napenda nimpe taarifa Mheshimiwa Halima Mdee kwamba kwa mujibu wa Ibara 63 Kifungu cha kwanza, Rais ni sehemu ya Bunge ikiwa nusu ya Bunge. Ukija kwenye sehemu ya pili, ndiyo inatoa madaraka sasa kwa Bunge kufanya kazi zake na sehemu ya tatu. Kwa hiyo, Rais kufanya intervention ni kitu ambacho ni muhimu kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu. Ahsante sana.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, naomba niachane naye, kwa sababu nahisi ananipotezea muda.

SPIKA: Pokea taarifa hiyo Mheshimiwa Halima.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, siwezi kuipokea kwa sababu hakuna popote kwenye Katiba ambako kumesema Rais ni nusu ya Bunge. Yeye ni sehemu ya Bunge kwa sababu tukitunga sheria ana nafasi yake ya ku-assent ile sheria ili iweze kufanyiwa kazi. Kwa hiyo, kila mmoja ana role yake independently. Kwa hiyo, tusichanganyane hapa.

Mheshimiwa Spika, suala la tafiti, nitasoma mambo kadhaa ili Serikali ielewe. Tumetolea mifano mbalimbali kwa ajili ya maeneo gani yanahitaji udharura, lakini kwa sababu ya suala la research tulipitisha Sheria ya Tozo hapa. Sasa ngoja nikusomee taarifa ya TCRA imesemaje? Kwa sababu tunapopitisha mapato, sisi tunafurahi Serikali wamefanya utafiti, kile ambacho Serikali ilikadiria kupata ipate ili huduma ziweze kupatikana. Serikali inapopitisha kodi, halafu kodi badala ya kuongezeka inapungua, tafsiri yake kulikuwa hakuna utafiti.

Mheshimiwa Spika, ngoja nikusomee, maana naona muda umeshaenda, wameshanipotezea muda. Uchambuzi wa miamala ya kifedha kwenye mitandao ya simu kabla na baada ya tozo, jumla ya miamala ya fedha imeshuka kwa asilimia 12 kutoka shilingi milioni 352 mwezi Juni hadi shilingi milioni 307 mwezi Septemba baada ya tozo.

Mheshimiwa Spika, miamala inahusisha kutuma na kutoa fedha inaendelea kushuka wakati miamala isiyokuwa na tozo za Serikali inahusu malipo ya huduma inaendelea kupanda. Idadi ya miamala pamoja na tozo zimeendelea kupungua badala ya kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili, uchambuzi wa miamala kifedha kwenye mitandao ya simu kabla ya tozo inatuambia, kuanzia…

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Halima upokee taarifa kutoka kwa Waziri wa Nchi.

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika,
naomba tu kumpa taarifa Mheshimiwa Halima Mdee kwamba, nadhani amejisahau kidogo kwamba hoja tunayozungumza sasa ni marekebisho ya Muswada Maalum na una vifungu maalum ambavyo havitoi ufafanuzi na haviendani na Sheria ya Kodi ambayo ilizungumzia tozo katika miamala. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba tu nimwamshe arudi kwenye hoja ambayo iko Mezani. Hiyo ya tozo za miamala tutakuja nayo siku nyingine kwa sababu hiyo ilishapita na shughuli zake zilishaanza kuendelea huko tulikotoka. (Makofi)

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa…

SPIKA: Sijakuruhusu Mheshimiwa Halima. Umesikia taarifa ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi? Unaipokea hiyo taarifa?

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, mimi najadili uchambuzi uliofanywa na Kamati ya Bajeti, uchambuzi ambao umejadiliwa na Wabunge katika context ya kuishauri Serikali. Sasa aniache nimalizie tu, atulie. Unaogopa nini?

Mheshimiwa Spika, kuanzia mwezi Julai, 2020 tozo za miamala zilipoanza, jumla ya tozo zitokanazo na miamala ya fedha zimekuwa zikishuka kwa wastani wa 9% kwa mwezi kutoka shilingi bilioni 94 kwa mwezi Julai hiyo, mpaka shilingi bilioni 78 mwezi Septemba. Kodi zilizokuwa zinalipwa Serikalini kutoka kwenye mapato ya watoa huduma, zimeshuka kwa asilimia 39 kutoka wastani wa shilingi bilioni 28 kwa mwezi mpaka wastani wa shilingi bilioni 16 kwa mwezi. Mapato ya watoa huduma yameshuka kwa wastani wa 39% kutoka kwa wastani wa shilingi bilioni 88,500 mpaka…

SPIKA: Hizo data tumeshazisikia. Hoja yako nini yaani?

MHE. HALIMA J. MDEE: Hoja yangu ni kwamba Serikali zingatieni ushauri wa Serikali kuimarisha vitengo vya utafiti wa Sera ya Mapato ili kuiwezesha Serikali kuwa na taarifa za uhakika. Siyo sifa kwenye suala hili la miamala tulitarajia kupata 1.3 trillion tunakuja tunaambiwa utekelezaji wake Serikali inapata nusu.

SPIKA: Sasa Mheshimiwa Halima, huko kwingine KABISA.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti,…

SPIKA: Utanipa taabu.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, hapana, hapana. Namalizia. Nivumilie kama ulivyomvumilia Mheshimiwa Reuben.

WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

T A A R I F A

SPIKA: Ndiyo. Kuna taarifa. Ooh, Mheshimiwa Waziri wa Habari na Teknolojia ya Habari.

WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA
HABARI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba kumpa taarifa msemaji. Taarifa anayoi-cite nilitamani sana aseme mwisho wa taarifa hiyo kwenye mjadala nini kilielezwa? Nayo ilikuwa kushuka kwa miamala hii ni jambo la kawaida kunapokuwa na introduction ya kodi mpya. Sasa naomba nimwambie, wakati tunaanza kukusanya tozo hii ya miamala anayoieleza, idadi ya miamala ilikuwa 12,330,223 na leo taarifa ya tarehe 27 mwezi wa Kumi, miamala ambayo ilirekodiwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) ni 13,489,119.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba apokee taarifa hii kwamba hili ni jambo la kawaida kwamba kuna kupanda na kushuka tunapokuwa na introduction ya kodi mpya. Ahsante.

SPIKA: Hivi sasa miamala iko juu.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nilitarajia kwenye taarifa yake angeniambie miamala ilivyokuwa juu, implication yake ya kimapato kwa fedha ikoje? Ukinipa story za miamala kuwa mingi, inaweza ikawa mingi lakini wamefanya shilingi mbili mbili. Hizi ni data ambazo sisi tumepewa na wao wenyewe. Kama kampuni za simu zinazolipa kodi zinapata hasara kwa 39 percent...

SPIKA: Mheshimiwa data zako zimeishia mwezi Septemba.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, hizi data tumepewa juzi kwenye Kamati.

SPIKA: Waziri amekupa current.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, naona unamsaidia kujibu. Sisi tunaangalia hapa…

SPIKA: Ndiyo ukweli wenyewe, yaani umechagua ile miezi miwili ya mwanzo ile; mwezi wa Nane na wa Tisa ambapo huko ni kweli, lakini ungeendelea hadi sasa ambayo anakwambia Waziri, ni kwamba ilikuwa ime-trip chini sasa imerudi pale pale na imepanda juu hata ya pale ilipokuwa. Ndicho anachosema. (Makofi)

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, tunazungumzia mapato. Kwa hiyo, ninachotaka anipe majibu kimapato, asinipe majibu kimiamala. Miamala inaweza ikawa mingi lakini isi-reflect mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme hivi kwa kumalizia; ushauri wa bure tu wa Kamati jamani, msini-mind, kwamba fanyeni utafiti kwa sababu siyo sifa, unatunga sheria leo halafu kesho; yaani tatizo unalitengeneza mwenyewe, halafu unataka uonekane kwamba wewe ni mkombozi kwenye hilo tatizo. Siyo sifa. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, tuvumiliane Mheshimiwa haya mambo yanahitaji ngozi ngumu tu. Ahsante sana. (Kicheko)
Muswada wa Sheria ya Ununuzi wa Umma wa Mwaka 2023.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru.

Mheshimiwa Spika, Sheria hii tukipitisha leo maana yake tunaachana na Sheria ya Ununuzi wa Umma Namba 7 ya mwaka 2011, kama ilivyorekebishwa mwaka 2016 na Kanuni zake za mwaka 2013, kama zilivyorekebishwa mwaka 2016. Nimeanza haya na ukiongezea pale ambapo Mheshimwa Nahodha amemalizia kwa kuonesha kwamba kulikuwa na sheria ambayo tunayo sasa, hii sheria haikuwa mbaya yote ndiyo maana mara ya mwisho tumeifanyia marekebisho 2016 ambayo ni kama miaka Saba hivi iliyopita.

Mheshimwa Spika, changamoto kubwa tuliyonayo ni kuwa na watu wenye weledi, watu wenye uzalendo, watu wanopenda Taifa lao, kutekeleza wajibu waliopewa kuutekeleza kisheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini ninasema hivi? Nashukuru wachangiaji wote waliopita wameelezea changamoto ambazo tumetoka nazo. Ukisoma ripoti zote za Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali za mwaka huu, ama miaka miwili ama mitatu iliyopita, nitatoa mfano wa mwaka huu ambao chimbuko lake ni matokeo ya tulikotoka.

Mheshimiwa Spika, kuna eneo maalumu linalohusu usimamizi wa manunuzi na mikataba. Kwa Serikali za Mitaa peke yake, eneo hili lina gharama ya shilingi bilioni 100.4. Serikali za Mitaa peke yake. Kwa mujibu wa Bajeti ya Serikali za Mitaa zenyewe mtanielewa, kama kwenye shilingi bilioni 600 au 700, shilingi bilioni 100 inahusu eneo la manunuzi, challenge ni kubwa. Ripoti ya Mashirika ya Umma iliyotoka sasa hivi, eneo la mikataba na manunuzi ni shilingi bilioni 600. Ukija Serikali Kuu ambayo ndiyo tunaiita baba lao, eneo la mikataba na manunuzi ni shilingi trilioni 8.12. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini nimesema hivi? Katika hii shilingi trilioni nane, shilingi trilioni 3.4 ni madeni ya wazabuni. Sasa tuje kwenye kanuni tulizonazo tuone zinasema nini? Kanuni ya 44.1 ya Kanuni ya Ununuzi wa Umma ya mwaka 2013, inaeleza, “kwa madhumuni ya kusaidia ukuaji wa makampuni ya ndani na kuwezesha makampuni hayo kutimiza wajibu wao kimkataba, taasisi zinapofanya ununuzi, zitahakikisha kuwa malipo yanafanyika kwa wakati kwa wazabuni.” Hii ni Kanuni ya mwaka 2013 ambayo ipo sasa, lakini tunapozungumzia madeni ya wazabuni wanaotoa huduma nchi hii, ni crisis kwa miaka nenda miaka rudi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nakubaliana na Mheshimiwa Nahodha kwamba tatizo kubwa siyo sheria zetu, tatizo kubwa watekelezaji wa sheria waliopewa jukumu la kufanya hizi sheria ziende kwenye utekelezaji ukoje? Taratibu za zabuni; mikataba ikifanyika; kazi zikifanywa; nani anatakiwa aidhinishe malipo; malipo yanaidhinishwa kwa wakati; hili ndilo tatizo.

Mheshimiwa Spika, tukisema hapa kwamba eti huu ndiyo msahafu utaondoa matatizo na wakati tuna mentality ya watumishi wale wale, wenye akili zile zile, wasiotaka kubadilika, wasiochukuliwa hatua na mamlaka zinazotakiwa ziwachukulie hatua, tutakuja tena. Amesema Mheshimiwa Nahodha, tutakuja tena. Natoa rejea kwa senior, tutakuja miaka mitatu ijayo, tutasema eti tubadilishe sheria. Kwa hiyo, we should change, we must change our mentality. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama tunadhani watu wetu wanahitaji kusaidiwa, wana upungufu, tuwasaidie, tuwajengee uwezo. Kama tunadhani watu wetu wanafanya hujuma za makusudi kwa Serikali na kwa Taifa, tuchukue hatua. Kinyume na hapo, we are just wasting muda wa Bunge, tutakuja tutabadilisha tena na tunapoteza rasilimali za Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, ukubwa wa hili eneo kwa bajeti ya nchi, tuchukulie mfano bajeti za miaka miwili; 2021/2022 katika shilingi trilioni 37, shilingi trilioni 23 zilikuwa za matumizi ya kawaida. Tunaposema matumizi ya kawaida, maana yake unalipa deni la Taifa, unalipa mishahara na matumizi mengine (other chargers). Kwenye mwaka 2021/2022, shilingi trilioni 14.9 zilienda kwenye maendeleo, mwaka 2022/2023, shilingi trilioni 15.06 zilienda kwenye maendeleo.

Mheshimiwa Spika, tunavyozungumzia shughuli za maendeleo, tafsiri yake ni kwamba, tunazungumzia miradi mbalimbali ya ujenzi ama miradi mingine yoyote ile inayohusu manunuzi. Kwa hiyo, tunavyozungumzia asilimia 36 ya bajeti, ninazungumzia kipengele cha maendeleo. Kama huku kwenye matumizi ya kawaida hii asilimia 60 na kitu, ina manunuzi, hilo ni jambo lingine. Mimi nazungumzia specifically fedha ambazo zimetengwa kwa ajili ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, hatuwezi kuchukulia shilingi trilioni 15 kimzaha mzaha. Ndiyo maana nakubaliana kabisa na Muswada kama ulivyoletwa awali. Ulisema, Taarifa ya Mwaka ya Tathmini ya Utendaji Kazi wa Ununuzi wa Umma na Thamani Halisi ya Fedha, ikisema kwamba taarifa ikishawasilishwa kwa Rais italetwa Bungeni. Dhumuni ya hili ilikuwa ni nini? Kwa sababu PPRA ina majukumu mengi, inafanya chunguzi kubwa. Chunguzi za shilingi trilioni karibu 16. Mwanasheria Mkuu na timu yake kwa busara kubwa wakasema, Rais akishakabidhiwa hiyo ripoti tarehe 30 Machi, mchakato ufanyike kwa Waziri mwenye dhamana kuileta taarifa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, taarifa ikiletwa Bungeni ni Taarifa ya Umma. Wabunge wanajua, tunaweza tukaijadili, tukajua shida ni nini, turekebishe tunachokijua. Namshukuru Mheshimiwa Dkt. Kimei kafunguka, hakujua mimi nilikuwa nam-note. Mheshimiwa Waziri umeenda kushawishi Kamati ya Bunge, eti hii ngoma isiletwe kwa sababu ipo kwenye sehemu ya taarifa ya CAG, wakati mnajua Taarifa ya CAG inajumuisha mambo mengi! Kwa hili akalizungumza kwa ufupisho, (in summary form), Lakini ikiletwa hiyo taarifa yote, tutajua hizi shilingi trilioni karibia 16 ambazo tunapeleka kwenye manunuzi zimeendaje?

Mheshimiwa Spika, licha ya kwamba Kamati ya Bajeti ni Kamati yangu, imenikuza sana, lakini katika hili nitaomba nilete mabadiliko ili nikubaliane na spirit ya Serikali. Serikali imesema inataka kuwa wazi, inataka kuonekana, inataka kujinyumbulisha. Sasa tunataka hii spirit ya Serikali isiwe iliingia bahati mbaya kwa mkono huu, walivyoona kama vipi, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu alitumwa ama alijituma mwenyewe? Ninaamini kwa sababu spirit ilikuwa ni njema, na kwa sababu CAG hataainisha mambo kwa mapana yake, na sheria hii imeipa mamlaka makubwa sana PPRA ili iweze kufanya udadavuzi wa mambo, nitaleta marekebisho kesho ili hiki kipengele kiweze kurudi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naona kengele imelia, nimalizie mambo mawili; hili la mabehewa, kifungu cha 79(1). Ununuzi wa vichwa na mabehewa ya treni ya ndege mitumba. Sawa, inawezekana spirit ya ununuzi wa vitu vipya tumeiona ina faida na hasara zake, lakini mashaka yangu, unapozungumiza ndege mtumba, unapozungumzia mabehewa mitumba, tafsiri yake ni kwamba, na hapa bahati mbaya sana tunasema hivi vitu kwa mapana yake vitaelezwa kwenye kanuni ambazo Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana amepewa jukumu la kwenda kuziandaa.

Mheshimiwa Spika, juzi tulikuwa na Kamati hapa ya Kanuni ya Bunge, imelalamika kwa namna gani Bunge linapokwa mamlaka yake kwenye mambo muhimu. Nilikuwa naangalia gharama ya Airbus ikiwa mpya, karibia shilingi bilioni 500. Tufanye mtumba basi kwa ndege moja, labda tufanye shilingi bilioni 200. Uamuzi mmoja wa namna hii una kishindo kikubwa kuliko maamuzi 1,000 ya Serikali zetu za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haiwezekani Bunge hili likaruhusu Waziri apewe mamlaka makubwa namna hiyo. Tumejenga reli ya SGR kwa mikopo, kwa trillions of money, halafu tunaruhusu mtu aje mwenyewe kivyake vyake kwa kanuni zake akatuelekeze namna ya kununua mitumba. Hapana. Tukubaliane mitumba itakuwaje humu humu ili tukishajua mitumba itakuwaje, tumwambie akatekeleze mitumba yetu. Sio tumruhusu yeye akajichimbie kule, ukizingatia taarifa iliyoelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia, naenda pamoja na kifungu cha 128. Maeneo 28 ya sheria hii muhimu amepewa Waziri akatunge kanuni. Haiwezekani. Otherwise tukubaliane kwamba akitunga hizo kanuni zake, alete kwenye Kamati ya Bunge ya Bajeti plus Kamati ya Bunge ya Sheria Ndogo, kabla hazijafanya chochote. Kama ndiyo tumeamua maeneo 28 muhimu ya sheria hii muhimu tumpe Mheshimiwa rafiki yangu, kaka yangu Dkt. Mwigulu akatungie kanuni, kwa mambo nyeti, tusifanye chochote paka ziende Kamati ya Bajeti na Kamati ya Sheriia Ndogo, nakushukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, jana nimefurahi sana nilipoona Wabunge wa CCM wakilia kwamba halmashauri zao hazina fedha. Nimesema hivyo kwa sababu, miezi sita iliyopita wakati tunapitisha bajeti ni Wabunge hao hao ambao walikuwa wanasema bajeti hii ya 2017/2018 ni bajeti ambayo haijawahi kutokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bajeti mbadala ya Kambi ya Upinzani tulisema wazi kabisa kwamba kwa kitendo cha Serikali kupitia Wizara ya Fedha kunyang’anya vyanzo vya mapato vya halmashauri zetu, vikusanywe na TRA kutoka kwenye halmashauri zetu ni mwanzo wa kuvunja miguu halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni bahati mbaya sana mmetoa muda mchache; kwa sababu ukiangalia hotuba ya Mwenyekiti wa Kamati anaonesha kama vile fedha za kawaida zilizopelekwa kwenye halmashauri zina-range kwenye asilimia 90; lakini ukipitia hili kabarasha ukiangalia fedha za kawaida, including mishahara yake. Matumizi ya kawaida kwenye fedha ambazo zinaonekana ama zimezidi asilimia 100, ama zimezidi asilimia 150, utakuta ni kwenda kulipa madeni ya wazabuni ya watumishi, ukiwaambia tenganisheni zijulikane za utendaji wa kawaida wa halmashauri na madeni ni zipi, hawasemi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma hiki kitabu, bajeti ya kilimo tunatakiwa tupelekwe bilioni 150 lakini zimepelekwa bilioni 11 nusu ya mwaka. Viwanda tunatakiwa tupeleke bilioni 74 zimepelekwa bilioni saba asilimia tisa. Ndiyo maana mnatupatia dakika saba, tutazungumza nini.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kodi ya majengo ni mbaya sana pale ambapo Mheshimiwa Waziri unavunja sheria ya bajeti kwa makusudi na nimeleta mabadiliko. Kwa nini nasema hivi; kwanza ufanisi mmeshindwa kukusanya kodi mnatudanganya kwamba mmefanikiwa. Nitakupa mfano wa halmashauri yetu; 2016/2017, Kinondoni tulikusanya bilioni 10 tukiwa na Ubungo. Bilioni 10 a hundred Percent tulikuwa tunapanga kuongeza, mkapata tamaa mkachukua. Mwaka 2016/2017, mmechukua mmeleta bilioni hii, moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunaweza kukusanya 10 asilimia 100 mnaleta bilioni moja, hivi huo ni ufanisi? Mwaka 2017/2018, tulikuwa baada ya halmashauri kugawanywa Ubungo ikaenda 2.5, Kinondoni 7.5, tulikuwa tunauwezo wa kukusanya asilimia 100. Wamechukua; sasa hivi miezi sita imepita hata shilingi haijaja. Ninyi mnajua hivi ndivyo vyanzo vyetu vya mapato kisheria, tuliwapa nyie mtukusanyie siyo mchukue mwondoke nazo.

Mheshimiwa nyie mnajua, wamechukua kodi ya mabango. Tulikuwa tuna uwezo wa kukusanya 4.5, a hundred percent billion kwa mwaka uliopita tulikusanya bilioni 3.5 tukaweza kukusanya kwa asilimia 100. Tukasema mwaka huu makadirio yetu tukiongeza tutakuwa na uwezo wa kukusanya mmechukua hamrudishi. Kwa manispaa yangu ninavyozungunza Kinondoni, Iringa, Arusha, Morogoro, hiyo ndiyo mifano. Halafu mnakuja hapa mnasema ufanisi Kinondoni tunashindwa kufanya chochote. Tuna deficit of twelve billion. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Bajeti iko hapa, tulifanya mabadiliko kifungu cha 65 kazi kununua Madiwani tu. Kifungu cha 65 kinasema hivi tulifanya marekebisho mwaka 2016/2017, tukasema, Waziri wa Fedha atashirikiana na Waziri wa TAMISEMI ili wagawane. Wizara inakusanya vipi kupitia TRA halmashauri inakusanya vyanzo vipi vya Property.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2017/2018 mkabadilisha mkamtoa Waziri wetu wa TAMISEMI mkajiweka wenyewe mkasema 65(2) kwamba hizi Property Tax zitakazokuwa collected zitakuwa deposited kwenye Consolidated Fund. Pili 65(2)(a) inasema mgawanyo na msambazo wa zitakazokunywa zinatakiwa zipelekwe halmashauri kutokana na bajeti, ndiyo sheria inavyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanajua hawa. Mchakato wa Bajeti huwa unaanzia ngazi ya halmashauri inapitishwa Hazina, inakuja Bungeni. Hizi bajeti za halmashauri tulishazipitisha tokea mwaka jana, inakuwaje leo Mpango eti watatoa kutokana na sisi tutakavyowaambia mahitaji yetu ni nini. Huo siyo utaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hili tutamtaka Mpango. Tunaomba na Bunge lako Tukufu tuweze kuungana pamoja kwenye azimio ambalo litasema mmeomba mtukusanyie kwa niaba kwa sababu ya ufanisi japokuwa ufanisi hakuna tumekubali; na kwa kuwa tukiwaambia mturudishie tunajua kwa wingi wenu mtakataa lakini tunasema…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzunguzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwanza nataka Mheshimiwa Waziri anisaidie kupata majibu kuhusiana na barabara za Jimbo la Kawe ambazo ni barabara za kupunguza foleni ya Makongo, Chuo Cha Ardhi, Makongo Juu kwenda Goba. Nimesoma kitabu cha hotuba hapa kinaonesha kwamba, kilometa nne zimekamilika. Sasa kilometa nne zilizokamilika ni kutoka Goba na kilometa moja imeingia Makongo.

Mheshimiwa Spika, sasa nataka nifahamu, kwa sababu zoezi sasa hivi ni kama limesimama na haijulikani kama kuna fedha ya fidia kwa sababu hapa fidia sijaona; na corridor ya barabara ina changamoto kidogo. Sasa nataka nipate majibu kwa mustakabali wa barabara ya Makongo.

Mheshimiwa Spika, pili, nataka vile vile anisaidie majibu ya barabara ya Wazo-Tegeta Kibaoni-Wazo-Madale, kuungana na Goba; kuna ujenzi unaendelea sasa hivi, lakini nikiangalia hiki kitabu kinazungumzia kilometa tano zinazojengwa sasa hivi, hakizungumzii kilometa sita ambazo zitaunganisha Madale kwenda Wazo. Kwa hiyo, naomba anipe hayo majibu kwa sababu hii barabara ni very strategic.

Mheshimiwa Spika, la tatu lakini sio kwa umuhimu; tunafahamu kwamba kuna upanuzi wa barabara ambao unatakiwa ufanyike kati ya Tegeta kwenda Bagamoyo. Sasa pale ni kati ya maeneo ambayo yanakumbwa na mafuriko miaka yote. Tutakumbuka katika utawala wa Awamu ya Nne viongozi wote walikwenda pale, mpaka aliyekuwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Pinda na tukakubaliana kuna mfereji wa chini utakaojengwa, ili kuondoa yale mafuriko na kumwaga maji Mto Nyakasangu.

Mheshimiwa Spika, sasa mfereji ulichorwa na watu wa TANROADS Mkoa wa Dar-es-Salaam, lakini mpaka sasa hivi hakuna hatua zozote ambazo zinafanyika. Sasa nataka tu nifahamu kwa sababu wananchi wanaumia sana kipindi hiki cha mafuriko, kwamba ule mpango wa ujenzi wa mfereji upo? Ama kwa sababu kuna mpango wa kuipanua hii barabara kutoka Tegeta kwenda Bagamoyo basi ndio utajumuishwa katika huo mradi wa upanuzi wa barabara?

Mheshimiwa Spika, baada ya kumaliza hayo ya ufupi ya jimboni kwangu, naomba nije kwenye suala la kitaifa la ATCL. Nikiangalia randama ukurasa wa 11 tunaambiwa kwamba kwa mwaka huu wa fedha Serikali inatarajia kufanya ununuzi wa ndege mpya kwa ajili ya Kampuni ya Ndege ya Tanzania (ATCL), shilingi bilioni mia nne tisini na tano. Tunakumbuka vile vile mwaka jana Serikali kupitia Waziri wa Fedha ilitenga vile vile bilioni zisizopungua mia tano kwa ajili ya ununuzi wa ndege.

Mheshimiwa Spika, ni muhimu ieleweka hapa na Wabunge waelewe, kwamba hoja hapa si kupinga ununuzi wa ndege. Hoja hapa ni hizi fedha ambazo tunaziwekeza ambazo ni matrilioni ya shilingi zinaenda kuzalisha ama tunaenda kuzitupa chini na zinapotea kama fedha nyingine? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina taarifa ya Msajili wa Hazina hapa. Msajili wa Hazina ndiye amepewa dhamana ya kusimamia mashirika yote ya Tanzania, anasema hivi, ukurasa wa nne wa taarifa yake:-

“Imekuwa vigumu kwa ofisi yangu kuweza kufanya uchambuzi wa kina wa utendaji wa ATCL kutokana na kutokuwepo taarifa za kutosha za kampuni. Kwa mfano, mahesabu ya kampuni yaliyokamilika ni ya mwaka 2014/2015 tu yaliyofanywa na PWC. Hata hivyo mahesabu hayo hayajatizamwa wala kupitishwa na Bodi. Hali hii imesababisha Ofisi ya Msajili wa Hazina kutoweza kuchambua na kubainisha hali halisi ya uwekezaji ilivyo hadi sasa kuhusu madeni na mali za kampuni,”

Mheshimiwa Spika, vile vile wanasema wanashindwa kujua hali ya ukwasi wa kampuni kwa sababu ya kampuni kutokuwa na mahesabu kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukija kwenye taarifa yenyewe ya ATCL wanasena kwamba, shirika halikuwa na mpango wa biashara. Yaani tunawekeza bilioni mia tano 2016/2017, 2017/ 2018 tukawekeza bilioni mia tano, 2018/2019 tunataka tuwekeze bilioni mia nne tisini na tano halafu hatuna mpango wa biashara. Hivi unaenda kuanzaje kufanya biashara wakati huna mpango? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hakuna business plan, tunawekeza trillion shillings. Tunakuja hapa wanasema inabidi tuanze kuajiri management yenye uwezo kwa sababu sasa hivi shirika halina wataalam wenye uzoefu wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Bunge lako mwezi Januari, walitoa taarifa za Kamati, kwa niaba ya Bunge wameita wataalam wa Serikali wanaosimamia mashirika yetu. Wamesema kwamba shirika letu mpaka sasa lina hali dhoofu na lina madeni ya shilingi bilioni mia tano kumi na saba. Sasa shirika lina madeni, shirika halina mpango wa biashara, shirika halina wataalam, tunaweka trilioni mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niliombe hili Bunge tutekeleze wajibu wetu. Hivi inaingia akili timamu, kwamba kwenye kilimo ambacho mkinaajiri asilimia zaidi ya 75 ya Watanzania tumeweza kuweka bilioni 11 tu, kwenye ndege ambayo tuna uhakika kwamba hii pesa tunaenda kuimwaga chini, tuna uhakika, tumeweka trilioni moja.

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Waziri akija hapa atujibu. Ni muhimu akajua wasije wakafikiria watakuwa salama, hizi pesa wanakumbuka akina Mramba, mnakumbuka akina Yona, hizi pesa tukigundua wameziwekeza kinyume na utaratibu, kama ambavyo nyaraka zinaonesha, tutawachukulia hatua.

Mheshimiwa Spika, ni muhimu Mheshimiwa Rais akajua pia, hiyo kinga aliyonayo ya Kikatiba inaangalia kama kuna masuala yalifanywa kwa makusudi kwa kuona kwamba kuna hasara mbele tukajiingiza kichwa-kichwa, huo usalama ama hiyo kinga ya Katiba haipo, tutamshughulikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haiwezekani. Naongea kwa dhamira ya dhati na najua Wabunge wengi wanajua, wengi wakiwa huko nje wanalialia, tukija huku ndani…

KUHUSU UTARATIBU . . .

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, Rais alichaguliwa na Watanzania. Hili Bunge ni la wawakilishi wa Watanzania. Rais lazima akosolewe na jina la Rais lazima litajwe kama anaenda kinyume na utaratibu. Lazima hii perception kwamba, Rais ni untouchable, lazima iishe. Bunge likiogopa kumtaja Rais wakati sisi tunapitisha bajeti, Rais ni sehemu ya Bunge, tutakuwa tunalifanyia makosa makubwa sana aifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi sijatumia jina la Rais kwa kebehi, nimesema hivi, tuna taarifa mbili hapa; tuna taarifa ya Msajili wa Hazina, tuna Taarifa ya ATCL. Taarifa ya Msajili wa Hazina inasema, nataka…

T A A R I F A . . .

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nimesema hivi, siwezi kumjibu Dokta Shika bidhaa ya Kichina, umenielewa; nikimjibu nitakuwa najidhalilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja yangu iko wazi kabisa. Nimesema hivi na naomba nirudie kwa sababu, najua kengele itagonga; nina nyaraka mbili za Serikali, nina nyaraka ya Msajili wa Hazina, nina nyaraka ya ATCL yenyewe; wanasema kwamba, mosi, tumewekeza bilioni…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa katika Mkutano wa Kumi na Kumi na Moja wa Bunge
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Niseme kwamba ni miongoni mwa Wajumbe wa Kamati ya Sheria Ndogo na wakati Kamati zinapangwa watu tuliopangwa Sheria Ndogo tulionekana kama vile watoto yatima kwa sababu inaonekana kama madaraja ya Kamati. Nimhakikishie Mheshimiwa Spika anayepanga Kamati kwamba nimepata nafasi ya kujifunza vitu vingi sana na ninamshukuru sana na kama Mungu atajalia niendelee kupangwa Kamati hii milele na milele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili wamezungumza Wabunge hapa, la kwanza ambalo ni muhimu kwa Serikali, taasisi na vyombo mbalimbali kujua kwa mujibu wa Katiba na ninataka nirudie ili lieleweke. Bunge ndiyo lina jukumu la kutunga sheria kwa mujibu wa Ibara ya 64 ya Katiba. Kwa sababu Bunge tunakutana mara nne kwa mwaka na kwa sababu tuna majukumu mengine mengi zaidi ya kutunga sheria ndiyo maana Ibara ya 97(5) ya Katiba tumefanya delegation kwa mamlaka mbalimbali kutunga sheria ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni muhimu Mawaziri, Halmashauri na Mahakama zetu kupitia Chief Justice zifahamu kwamba kazi hii tumeishusha. Vilevile kupitia Kamati hii ndogo baada ya hizo sheria ndogo kuwa gazetted tuna wajibu wa kuja kuziangalia kama zimeenda kinyume tuna wajibu na haki ya kuzirekebisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu sana mkaelewa kwamba sheria hizi ndogo zinapuuzwa kwa sababu ya jina lake sheria ndogo. Sheria hizi ndogo ndiyo zinagusa maisha ya wananchi wetu mmoja mmoja kule chini kila siku. Kwa hiyo, kama kuna kanuni, by law, miongozo, kanuni za mahakama, amri, taarifa na tangazo maalum lolote lile linalohusu watanzania, wawekezaji na taasisi mbalimbali hizo zote ni sheria ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana watu walikuwa wanasema ooh, mnaenda kutunga sheria za mbuzi na ng’ombe sijui, hapana. Ndiyo maana ningependa hicho kitu kinachoitwa semina hata Wabunge wapewe kwa sababu kazi tunayoifanya hapa tunafanya nusu, halafu ile nusu nyingine wanaenda kufanya watu wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, amezungumza Mwenyekiti wetu wa kamati hapa kwamba kuna tatizo la Mawaziri wakipewa dhamana ya kwenda kutengeneza sheria ndogo wanatengeneza sheria ndogo ambazo zinakinzana na sheria mama. Juzi nimeshtuka sana wakati Kamati ya Katiba na Sheria ilipoleta suala la kuanzishwa mahakama (mobile courts) Waziri akalazimika kuliondoa kwa sababu Kamati ilikuwa haiungi mkono. Waziri anakuja anasema kwamba eti kifungu cha 4 cha JALA na kifungu cha 10 cha Magistrates’ Courts Act kinampa mamlaka Jaji Mkuu kuunda mahakama, jambo ambalo ni la uongo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu cha 4 cha JALA kama ambavyo nimesema Jaji Mkuu ana uwezo wa kutengeneza rules za jinsi mahakama zinavyotakiwa ziendeshwe, lakini siyo kuunda chombo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia Magistrates’ Court Act, JALA na Sheria ya Tafsiri inayotoa tafsiri ya Magistrate hakuna popote ambapo Jaji Mkuu amepewa ruhusa ya kuunda mahakama nyingine, lakini ana uwezo wa kusema hii Mahakama ya Wilaya ikajisogeze iende sehemu fulani ambayo haina Mahakama ya Wilaya ili wananchi wasogezewe huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mazingira kama haya tukahoji hizi shilingi bilioni 48 mmezitumia mkanunua hayo mabasi kwa ajili ya mobile courts/special courts zinaenda kufanya nini? Tunajibiwa eti Jaji Mkuu anaweza kuunda mahakama mpya. Sasa vitu kama hivi vinatisha na vinaogopesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, amezungumza Mheshimiwa Aida hapa, Sheria Ndogo za BASATA. Mwenyekiti wangu wa Kamati yaani ingekuwa ni amri yangu azimio hili la leo liseme kanuni hizi zisiende kutekelezwa mpaka Waziri alete marekebisho mengine. Kanuni hizi zinaua wasanii wetu, kanuni hizi hazijengi wasanii wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, naomba nikisome kifungu cha 64 na Wabunge mnisikilize, kinasema; makosa na adhabu; haya makosa yote ninayosoma hapa ndiyo msanii anaweza akatozwa yote siyo moja moja.

Moja, Msajiliwa wa Baraza au mtu yeyote atakayebainika kuvunja au kukiuka masharti ya kifungu chochote cha kanuni hizi atakuwa anafanya kosa na atachukuliwa hatua zifuatazo;-

(i) Atatozwa faini ya papo kwa papo isiyopungua shilingi milioni moja;

(ii) Kufungiwa kazi husika na kutozwa faini ya papo kwa papo isiyopungua shilingi milioni tatu;

(iii) Kufutiwa usajili;

(iv) Kufungiwa kujishughulisha na kazi za sanaa kwa kipindi kisichopungua miezi sita;

(v) Kuzuiwa kujishughulisha na kazi za sanaa maisha kwa kubainika kulingana na ukubwa wa kosa;

(vi) Kutozwa faini na adhabu yoyote stahiki wakati wa utendaji wa kosa husika;

(vii) Kufungiwa kujishughulisha na kazi za sanaa kwa kipindi kisichopungua miezi sita; na

(viii) Kuzuiwa kujishughulisha na kazi za sanaa maisha kwa kubainika kulingana na ukubwa wa kosa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sub-section 2 inasema adhabu zilizotajwa hapo juu katika kanuni ya 64(1) zinaweza kutolewa moja moja au kwa pamoja kulingana na uzito wa kosa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu fikiria zisipungua milioni moja, mbili na tatu. Ukiangalia sheria inayoanzisha BASATA hapa inawapa majukumu mengi ya kuweza kutafutia wasanii masoko, kuwajenga wasanii na kuwapa mafunzo, hawatekelezi kanuni hizi ila wameona wasanii wawili/watatu maskini wa Mungu wametoka, wanataka kuminya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nisisitize Mwenyekiti wetu ukija ku-wind up, namshukuru Mheshimiwa Mwakyembe alikuja akawa na busara ya hali ya juu akasema kamati ninaomba hii kitu niondoke nayo nikairudie upya niiangalie, ni busara ya hali ya juu na kwa sababu ya busara hii azimio letu pamoja na mambo mengine lielekeze hizi kanuni batili zisitumike mpaka pale ambapo zitaletwa mpya na kamati ijiridhishe kwamba imeendana na hizi sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya ripoti ya CAG kutoka Machi, 2018, Naibu Spika alirekodiwa akisema hapa Bungeni kwamba kuzungumzia taarifa ya CAG ni suala halali na kila mtu ana haki ya kuzungumzia ripoti ya CAG. (Makofi)

Kwa mantiki hiyo, ruling ya Spika ni kwamba Wabunge tuna haki ya kujiachia kwenye ripoti ya CAG na kwa mantiki hiyo tunamtaka Waziri wa Fedha akijibu hoja zake atuambie shilingi trilioni 1.5 iko wapi. Tunamtaka Waziri wa Fedha akijibu hoja zake atuambie shilingi bilioni 200 mliyopeleka Zanzibar iko wapi, ilipelekwa lini, kwa usafiri gani na ilifanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa anapoteza muda hana mpya bwana, anarudia kulekule anapoteza muda…

KUHUSU UTARATIBU . . .

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, namwambia hivi Mheshimiwa Dkt. Magufuli ameshakusikia unavyopambana tulia kashasikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mtindo wa makusanyo kutolewa yakiwa pungufu, ukirejea hata ripoti ya CAG ya mwaka iliyotolewa Machi, 2017 ukurasa wa 42 unatuambia walikusanya Serikali shilingi bilioni 21.1 wakatumia shilingi bilioni 20; kwa hiyo, hii inatupa tafsiri gani kwamba ni utamaduni wa Serikali hii ya CCM wanakusanya mapato, wanafanya matumizi halafu kuna kachenji kanabaki wanajua wanakafanyia nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasisitiza Waziri wa Fedha ndio unadhamana za fedha za nchi hii 2015/2016 ripoti iliyotolewa Machi, 2017 kuna katrilioni moja kalikuwa hakaelewiki kako wapi, mwaka 2017/2018 ripoti imetolea Machi 18 shilingi trilioni 1.5 mtatujibu leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili tunataka Waziri wa Fedha akija atuambie zile fedha za makinikia ziko wapi? Mnakumbuka mwaka 2017 Rais aliunda Tume mbili nchi ikasimama tv zote live, tukawaambia Watanzania kwamba ACACIA Mining hawajalipa kodi wamejificha kwa kuibia Serikali kuanzia mwaka 2000 mpaka mwaka 2017.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkaliambia Taifa tuna idai ACACIA shilingi trilioni 424 kodi. Leo mpaka sisi tukawaambia jamani hapa shida siyo ACACIA, shida ni Serikali ya CCM na mikataba mibovu ambayo inaimaliza nchi. Mwaka mmoja baadae mbele ya Bunge hili Tukufu anasimama Mheshimiwa Profesa Kabudi mwalimu wangu na mpaka naona aibu kuwa na mwalimu kama yeye, anasema, anatuambia eti hatuwezi kutoa siri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Mheshimiwa Magufuli ilisema unaidai ACACIA Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi trilioni 400 leo Waziri wa Sheria anatuambia eti anaona aibu wakisema wanaotudai watakuja kutudai. Hivi wakati mnatangaza hiyo shilingi trilioni 400 waliokuwa wanatudai hawakujua, sasa ni hivi Serikali muwaambie watanzania kwamba mliwadanganya.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya ripoti ya CAG kutoka Machi, 2018, Naibu Spika alirekodiwa akisema hapa Bungeni kwamba kuzungumzia taarifa ya CAG ni suala halali na kila mtu ana haki ya kuzungumzia ripoti ya CAG. (Makofi)

Kwa mantiki hiyo, ruling ya Spika ni kwamba Wabunge tuna haki ya kujiachia kwenye ripoti ya CAG na kwa mantiki hiyo tunamtaka Waziri wa Fedha akijibu hoja zake atuambie shilingi trilioni 1.5 iko wapi. Tunamtaka Waziri wa Fedha akijibu hoja zake atuambie shilingi bilioni 200 mliyopeleka Zanzibar iko wapi, ilipelekwa lini, kwa usafiri gani na ilifanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa anapoteza muda hana mpya bwana, anarudia kulekule anapoteza muda…

KUHUSU UTARATIBU . . .

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, namwambia hivi Mheshimiwa Dkt. Magufuli ameshakusikia unavyopambana tulia kashasikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mtindo wa makusanyo kutolewa yakiwa pungufu, ukirejea hata ripoti ya CAG ya mwaka iliyotolewa Machi, 2017 ukurasa wa 42 unatuambia walikusanya Serikali shilingi bilioni 21.1 wakatumia shilingi bilioni 20; kwa hiyo, hii inatupa tafsiri gani kwamba ni utamaduni wa Serikali hii ya CCM wanakusanya mapato, wanafanya matumizi halafu kuna kachenji kanabaki wanajua wanakafanyia nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasisitiza Waziri wa Fedha ndio unadhamana za fedha za nchi hii 2015/2016 ripoti iliyotolewa Machi, 2017 kuna katrilioni moja kalikuwa hakaelewiki kako wapi, mwaka 2017/2018 ripoti imetolea Machi 18 shilingi trilioni 1.5 mtatujibu leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili tunataka Waziri wa Fedha akija atuambie zile fedha za makinikia ziko wapi? Mnakumbuka mwaka 2017 Rais aliunda Tume mbili nchi ikasimama tv zote live, tukawaambia Watanzania kwamba ACACIA Mining hawajalipa kodi wamejificha kwa kuibia Serikali kuanzia mwaka 2000 mpaka mwaka 2017.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkaliambia Taifa tuna idai ACACIA shilingi trilioni 424 kodi. Leo mpaka sisi tukawaambia jamani hapa shida siyo ACACIA, shida ni Serikali ya CCM na mikataba mibovu ambayo inaimaliza nchi. Mwaka mmoja baadae mbele ya Bunge hili Tukufu anasimama Mheshimiwa Profesa Kabudi mwalimu wangu na mpaka naona aibu kuwa na mwalimu kama yeye, anasema, anatuambia eti hatuwezi kutoa siri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Mheshimiwa Magufuli ilisema unaidai ACACIA Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi trilioni 400 leo Waziri wa Sheria anatuambia eti anaona aibu wakisema wanaotudai watakuja kutudai. Hivi wakati mnatangaza hiyo shilingi trilioni 400 waliokuwa wanatudai hawakujua, sasa ni hivi Serikali muwaambie watanzania kwamba mliwadanganya.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati Hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nitaanzia kuchangia kamati ya PIC, ukurasa wa 25 ambao unazungumizia mashirika ambayo yanafanya matumizi kuliko uwezo wake wa kukusanya na vilevile uwezo ama faida ya shirika kupungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajielekeza kwenye Shirika la Nyumba hasa ukizingatia kwamba mimi ni Mbunge wa Jimbo la Kawe na katika kipindi cha mwaka 2000 – 2015, kulikuwa kuna miradi mingi sana ya ujenzi ambayo ilikuwa inasimamiwa na Shirika la Nyumba la Taifa na kama miradi husika ingefanikiwa Serikali ingeweza kupata mapato mengi; mosi kwa kutumia property tax, lakini pili kwa kutumia uuzaji wa nyumba ama kupangisha nyumba na shughuli zozote za kijamii zilizokuwa zikiendelea ama ambazo zingeendelea katika eneo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiangalia taarifa ya PIC inaonesha kwamba Shirika la Nyumba la Taifa mwaka 2016/2017, mapato yalikuwa bilioni 154 matumizi 122; mwaka 2017/2018 mapato milioni 116, matumizi bilioni 83.2. Hata hivyo, ukiangalia taarifa ya Kamati inaonyesha kwamba ina dhamira ya kulaumu shirika zaidi pasipo kuangalia shirika limefikaje hapo. Sote tunajua kwamba mpango wa ujenzi wa nyumba Regent, ujenzi wa nyumba Morocco, ujenzi wa nyumba 711 (I) Kawe na ujenzi wa nyumba 711 (II) Kawe zimekwama kwa sababu Waziri wa Fedha amegoma kutoa kibali cha Shirika la Nyumba kuweza kukopa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa Waziri wa Fedha atujibu hili kwa sababu jana wakati Mwenyekiti wa PAC alipokuwa akizungumza na hili Bunge alisema, kutokana na miradi kukwama miradi yote mwaka 2017 Serikali inalazimika kumlipa mkandarasi kila siku ya Mungu shilingi milioni 20, kila siku ya Mungu. Hapa tunapozungumza project hizi nne tofauti kuna wakandarasi wanne tofauti. Sasa hii milioni 20 inalipwa kwa mkandarasi mmoja ambaye yupo kwenye project moja ama inalipwa kwa wakandarasi wanne, ama kila mkandarasi kati ya hawa wanne analipwa hiyo hasara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni bahati mbaya sana huu mradi tunaelezwa mimi ni jimboni kwangu 711(I) ulianza kufanyiwa kazi kwa 20% imewekezwa pale milioni 26.3, mradi ambao umekwama. Kwa hesabu ambazo Mwenyekiti ametuambia jana, kama kwa siku wanalipwa milioni 20 kwa project kwa mkandarasi. Tafsiri yake kwa mwaka wanaojua mahesabu zinakaribia bilioni saba kwa mwaka. Kwa miaka mitatu kuanzia mwaka 2017 mpaka sasa hivi tafsiri yake kuna bilioni karibu 21 ama 26, mimi nimesoma sheria mambo ya hesabu hesabu siyajui 21.6 nimeambiwa hapa na wachumi, zinadondoka chini kwa sababu tu kuna Waziri wa Fedha mmoja ambaye hata kama shirika limefikia ukomo lakini lilikuwa lina business mind, fedha ingeweza ikarudi zaidi ya kile ambacho kimekopwa na faida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka mitatu mfululizo, mradi umekwama, juzi kama miezi kadhaa iliyopita niliuliza swali hapa Wizara ya Ardhi akajibu Naibu Waziri wa Ardhi, nikauliza ni kwa nini Mradi wa Kawe, Kawe 711 (I) 711 (II) Morocco na Regent imekwamba; akaniambia eti ni kwa sababu Serikali imehamia Dodoma, kwa hiyo nguvu zote zilizokuwa zifanyike kwenye zile project zimehamia Dodoma. Serikali isiyokuwa na vision, Serikali isiyokuwa na mipango, anayeibuka anaibuka na jambo lake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake ni nini? Mradi wa phase II ambao ulikuwa unagharimu bilioni 103 na wenyewe, ile ni phase I, umefanywa kwa 30% tu, umetumia bilioni 34.8 mradi umelala. Kwa hiyo tafsiri nyingine na huyu mkandarasi wa pili na yeye analipwa milioni 20 yake kwa siku amekaa tu anakula bata halafu leo wanasema wana uchungu wa Watanzania, wana uchungu na matumizi ya fedha, we can‟t allow this. Nina ripoti ya CAG hapa, naomba ninukuu CAG amesema nini kuhusiana na hayo mamlaka ambayo Mheshimiwa Waziri anayo lakini ameamua kuyakalia. Anasema hivi

“Ikiwa NHC haitapata kibali cha kukopa na kushindwa kukamilisha miradi yake itapaswa iwalipe wakandarasi jumla ya shilingi bilioni 99.99 kutokana na uvunjaji wa mkataba.” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii fedha ni extra ya zile bilioni 21 ambazo tunazimwaga chini kwa sababu tu ya maamuzi ya kisera ya kukurupuka. Pia anasema:

“Pia itawapasa kufanya marejesho ya shilingi bilioni 2.6 kwa wateja walioanza kulipia malipo ya awali ya ununuzi wa nyumba hizo.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kawe ama lile eneo ni very strategic yaani NHC walikuwa wanapata wateja kabla hata hawajamaliza ujenzi. Kwa hiyo kulikuwa kuna uhakika wa fedha upo hapa mkononi, kulikuwa kuna uhakika wa kodi za majengo, Mheshimiwa Mpango aliamua kutunyang’anya halmashauri property tax ili lile kapu lake linenepe. Kwa akili yangu iliniambia kama kweli yeye ni Mchumi maana sisi wengine ni Wanasheria makanjanja, uchumi hatujui, uchumi wake ungemwelekeza kwamba kuwekeza kwenye zile nyumba kungeweza kulisaidia hili Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaomba nipate majibu ya uhakika kutoka Serikalini project za Shirika la Nyumba, nimeamua nisimame nizungumze nyumbani kawe na nilizungumze shirika letu ambalo chini ya akina Mchechu tulikuwa tunaliangalia kama shirika la mfano. Halafu wanakuja watu wanasema, hatuwezi kukulipa milioni kadhaa. Lazima awalipe watu mamilioni kutokana na brain, kama brain yao inaleta trillions wawalipe kwa thamani hiyo. Wanakaa wanawaza kimaskini halafu wanataka productivity, hakuna vitu kama hivyo. Hata wenzetu waliotangulia huko brain yako ndio inaangalia kipimo chako cha mshahara. Kama wewe ni kilaza utapata hivi, kama Mungu amekujaalia kuwa hivi utapata hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri tupate majibu ya haya mashirika na waache kusakizia ama kutupa mzigo kwa wetendaji wetu, wakati kinyumenyume wao ndio wanaovuruga na kuyanyonya mashirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nashukuru sana na natarajia Mwenyekiti anatanipa majibu. Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati msilembelembe hizi taarifa. Nimeaangalia jana taarifa ya PAC, ukiangalia CAG ana hoji mambo mengi ya muhimu, wanakuja hapa wanachagua vieneo vichache ili kuonyesha Serikali imefanya wonders kumbe kwenye hizi taarifa kuna mambo ya ajabu, mambo ya hovyo ambayo Bunge tunatakiwa tusimamie kwa maslahi mapana ya nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, Mheshimiwa ndio nimerejea kama hivyo, msiyempenda amekuja. Ahsante sana.(Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kiukweli mimi kama mkongwe kwenye Bunge hili Wizara hii ilikuwa kati ya Wizara moto sana kipindi hicho palikuwa hapakaliki, lakini sasa hivi naona moto umepoa sana. Kwa hiyo hicho ni kiashiria kwamba Mheshimiwa Lukuvi na timu yake wamekuwa wakifanya kazi kwa viwango vyema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, mwaka 2010 mpaka 2015 mimi nilikuwa Waziri kivuli wa Ardhi na nilitumia muda huo kufanya utafiti mkubwa sana wa migogoro ya ardhi na sikuwa mchoyo nika-share na Mheshimiwa Lukuvi ma-book yangu yale, akayafanyia kazi na anapata kiki kutokana na kazi ambayo nilitumia brain yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Mheshimiwa Bashiru yuko hapa, aliyekuwa Katibu Mkuu wa CCM na yeye nilikuwa namsaidia tafiti nilizokuwa nikifanya na yeye wakati huo akiwa ni Mhadhiri akifanya maandiko yake huko na atakubali kama hatakuwa mchoyo wa fadhila. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa leo nitakuwa local kidogo, nitakuwa Jimbo la Kawe, kwa sababu inaonekana kama vile kumepoa Kawe kidogo. Mheshimiwa Lukuvi, mimi na yeye wakati niko Mbunge wa lile Jimbo tulifanikiwa kutatua migogoro mingi sana na nimshukuru kwa hilo. Tulitatua Nyakasangwe, tukatatua Kunduchi, tukatatua Bunju kwa Somji, tukatatua kile kimgogoro cha miaka kumi na tano Basihaya pale, kuna Mtaa wa Chatembo, cha Chui na cha Simba. Hayo majina yenyewe yanaashiria watu gani wanakaa kule. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, lile eneo lina wakazi 4,000, lile eneo tarehe 13 Juni, 2015, tulienda pale kumaliza mgogoro, alikuwepo Waziri, alikuwepo Katibu Mkuu wakati huo Kidata ambaye sasa hivi ni Kamishina wa TRA, alikuwepo Naibu Waziri kipindi hicho, Anjella Kairuki, Wakurugenzi na timu yake yote walikuwepo. Tukatatua mgogoro husika na wananchi wa eneo lile na alikuwepo pia aliyekuwa Mkurugenzi wa kile kiwanda anaitwa bwana Alfonso Rodriguez kwa niaba ya kiwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu tuna roho nzuri siku 60 ambazo wataalam wa Wizara walikaa pale, wananchi walijigharamia, wakahakikisha wanakaa sehemu nzuri hili upimaji ufanyike. Nini tulikubaliana kwenye kikao na nasema haya Mheshimiwa Lukuvi anajua yeye ni rafiki yangu, tumefanya mengi pamoja, lakini akiona nimeamua kuja kufunguka hapa nataka arekodiwe na Hansard sasa akijigeuka mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maazimio tulikubaliana nini? Kikao cha wananchi kilikuwa na maazimio saba, nitayasoma kwa ufupi:-

(i) Eneo ambalo limekaliwa na wananchi kwa muda mrefu libadilishwe matumizi kuanzia leo tarehe 13 Juni, 2015, kutoka matumizi ya uchimbaji wa madini na kuwa eneo la makazi;

(ii) Wananchi waliotambuliwa wakati wa zoezi la uthamini ndiyo watakaohusika na zoezi zima, wananchi ambao hawakuwepo na walikuja baada ya zoezi hawatatambulika;

(iii) Wakati wa umilikishaji Wizara itatoza tozo ya mbele premium kwa kila kiwanja itakachomilikisha. (Makofi)

(iv) Wizara imekubali sehemu ya malipo ya premium yataenda katika kiwanda na kitasaidia kujenga miundombinu na huduma za jamii kwa zahanati;

(v) Wananchi kwa kushirikiana na Serikali ya Mtaa wataunda Kamati ya Utekelezaji na Usimamizi wa Mpango huo;

(vi) Kazi za uchimbaji mchanga na kokoto hazitaruhusiwa na atakayefanya hivyo atakamatwa; na

(vii) Kazi ifanyike haraka mwezi Oktoba, 2015, mambo yatakamilika, wananchi watakabidhiwa maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri akafunga kikao, akadondoka signature hapa, Mheshimiwa Lukuvi pembeni, Mheshimiwa Kidata pembeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazungumza Mheshimiwa Jerry hapa, sisi Wanasheria katika nyaraka ukishadondoka ukaji-commit huwezi kuja uka-change kote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nini kimetokea na majina haya signature za wananchi waliohudhuria kikao. Ameondoka Mtendaji Mkuu wa Twiga, akaja Mtendaji Mkuu mwingine, anaanza kuivimbia Serikali, anakuja na terms nyingine, wakati tulikubaliana hapa wananchi watachangia premium, premium kidogo itaenda kwenye kiwanda na nyingine itakuja kurekebisha miundombinu. Mheshimiwa Waziri alienda juzi, Mheshimiwa Tibaijuka alienda akaondoka akasahau kiatu, nashukuru Mheshimiwa Waziri walimstahi, anawaambia wananchi kutoka premium ambayo kawaida ni one percent kama ikiwa Serikali imesimamia mpaka three percent haiwezi kuzidi hapo ya thamani ya ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo wanaenda wanawaambia wananchi watoe 35 percent ya thamani ya ardhi. Kwa sababu, wamethaminisha wakasema square mita pale ni Sh.20,000/=, wakasema wananchi walipe Sh.6,500/= kwenda Sh.7,000/= mwanzoni ilikuwa Sh.8,000/= wakapunguza kidogo kwamba walipe Sh.6,500/= hii nyingine watafidiwa na mwekezaji. Square mita moja Sh.7,000/= wakati tulikubaliana tunalipa premium ambayo ni asilimia moja ya thamani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, kile alichokifanya ni kutaka wananchi wanunue ardhi almost upya. Wananchi wanaokaa eneo lile ni wananchi wa kipato cha chini, wananchi maskini, inakuwaje leo Mheshimiwa Waziri anageuza maneno yake na nimwambie tu kama hafahamu, wananchi wamesema hivi nikufikishie ujumbe, hawatatoka ila wako tayari kulipa premium tuliyokubaliana. Hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naamini Mheshimiwa Waziri ana burasa ya kuamua kulimaliza hili kwa sababu tulienda vizuri tukagota.

Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Nyumba la Taifa; juzi niliuliza swali hapa, Mheshimiwa Naibu Waziri akajibu, akasema mradi huu utakuwepo kwenye bajeti mwaka huu wa fedha tunaoanza kuutekeleza. Sasa mwaka wa fedha Wizara si lazima kwenye maandishi huku nione. Waziri alisema utekelezaji wa Mradi 7111 ambayo thamani yake ni shilingi bilioni 142; na Mradi 7112 shilingi milioni 103, miradi yote miwili ina thamani ya shilingi bilioni 245 ambazo Shirika la Nyumba la Taifa liliingia mikataba na wakandarasi wawili toka mwaka 2014. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo mradi mmoja umetekelezwa kwa asilimia 20 na mwingine asilimia 30. Mkataba wa kwanza ulikuwa 2014 mpaka 2017 waka-extend mpaka 2019, leo kazi imelala. Mheshimiwa Naibu Waziri atakwambia tulihamishia Makao Makuu Dodoma tukagota. Waziri akasema kulikuwa kuna mikataba haijakaa vizuri tunaifanyia kazi toka mwaka jana hawajajibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na watu wa PAC wako hapa ni mashahidi, anasema ule mkataba na sababu ya nini kukwama, Shirika hivi linavyojiendesha kibiashara limegota limeshindwa kupewa fedha kwa sababu, wamekopa, mwisho wa ukomo wao shilingi milioni 300, wakaenda kuomba kibali Wizara ya Fedha toka 2017. Kwa sababu mradi huu ni viable, unakaa eneo ambalo ni prime, tunaomba mtupe kibali mradi huu utalipa. Toka mwaka 2017 mpaka leo hakuna ambacho kimetokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna wananchi wamewekeza zaidi ya shilingi bilioni tatu pale wameshanunua nyumba kabla hazijajengwa, Waziri anatuambia kuna process, ni kweli? Tafiti zinaonyesha tuna upungufu wa nyumba kwenye majiji zaidi ya milioni tatu na kila mwaka nyumba laki mbili zinahitajika, halafu wanakaa hapa wanasema hatuna mapato, yaani hatuna mapato wakati pale Kawe New City iliyokuwa inatarajiwa kuwa na wakazi 50,000, wangeingiza property tax mpaka Mheshimiwa Waziri angekimbia. Hivi kwa nini tunafikiria kimaskini (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie; tusipotekeleza huu mkataba Wizara inaenda kulipa bilioni 100, wakati wamekataa kuipa ruhusu Shirika la Nyumba yaani shilingi bilioni 100 unaenda kumpa mkandarasi bure kwa kuvunja mkataba jamani hii ni akili ama nini? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Halima kengele ya pili imeshagonga.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimwombe Waziri anipe majibu yenye mantiki kwa maslahi mapana ya nchi na Jimbo la Kawe. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi hii. Nikiwa sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Bajeti nitachangia mambo kadhaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, Kamati ya Bajeti imependekeza kwamba Shirika letu la Ndege (ATCL) liangaliwe ili liweze kuboreshwa zaidi ili liweze kufanya kazi kwa ufanisi. Lakini nikiwa naunga mkono hiyo hoja nitazungumza mambo kadhaa kwa sababu lazima tujue tulikotoka ili kuweza kujua tunakwendaje mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunavyozungumza sasa ATCL ina madeni yenye thamani ya bilioni 472, thamani ya mali za ATCL ni bilioni 256. Tafsiri yake ni kwamba ATCL ina mtaji hasi wa shilingi bilioni 216. Na unapokuwa na mtaji hasi tafsiri yake ni kwamba umekufa tu lakini upouopo tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kingine, malengo ya biashara ya ATCL wakati tunaifufua, na watu tulizungumza tukasema tunaingiza fedha lakini wakati tunaingiza hizi fedha nyingi lazima tuhakikishe shirika liko tayari, Taifa liko tayari, wananchi wako tayari. Zikapigwa porojoporojo hapa, mambo yakaenda, tumefika hapa tulipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, malengo yalikuwa bilioni 600, malengo ya kibiashara, kutengeneza, wamefanikiwa bilioni 157; asilimia 24 tu ya lengo. Naunga mkono tui-boost, tuifufue, sikatai, ila lazima tujue tulitoka wapi, tumeteleza wapi, tunakwenda wapi na tusifanye maamuzi yanayohusu pesa za Umma kimihemkohemko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa 2015/2016 – 2021/2022 malengo kwa ATCL peke yake ilikuwa ipewe trilioni 3.39, mpaka sasa imefanikiwa kupata trilioni 1.9 kwenye hiki kipindi cha miaka mitano. Sasa nikiwasikiliza ndugu zangu hapa wanazungumza kilimo, mkongwe hapa, tumepiga hizi sound za kilimo tu kwenye mipango, tumezipiga yaani hawasikii. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kilimo ambacho tunajua kinachangia asilimia 26 ya GDP, Pato la Taifa, yaani kwenye zile trilioni 163, kilimo anachofanya mkulima mmojammoja kwa support kiduchu ya Serikali inachangia trilioni 44. Tumeipenda sana tumeipa bajeti 294, ukija utekelezaji utakuta wamebajeti bilioni 100, ikizidi sana bilioni 60. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ndugu zangu hawa wa ATCL wamepigwa trilioni zao 1.9, ukiuliza hivi inachangia pato la Taiifa kiasi gani, sidhani kama asilimia moja inafika. Kuna wenzangu na mimi hapa walikuwa wanajifanya, oh, wanaleta watalii; ndege gani ya ATCL inatoka Mpanda inaleta watalii Bongo? Nendeni Kilimanjaro pale, nendeni huko Mwanza muangalie kuna ndege gani ya ATCL inaleta Wazungu kutoka Ulaya kuja Tanzania kwa utalii? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, angalia safari za ndani ufanye analysis ujue kama hizi ndege zina mchango kwenye utalii. Nazungumza tujitathmini. Tujitathmini. Sina nia mbaya. Kwa sababu midude iko hapa, yalikuja 11 yameshalipiwa mengine sasa hivi tunaambiwa 16 halafu hadi kuelekea ule uchaguzi zitatimia 19. Yaani hili ni eneo pekee ambalo mtatekeleza bajeti kwa asilimia mia lakini output ikoje, productivity ipo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima na taadhima, hili shirika tunavyozungumza limepewa asilimia 600 ya bajeti ya kilimo kama ikipelekwa kwa ukamilifu. Hebu tujiulize tu, hiki kilimo hiki kingepewa hata trilioni moja, ingekuwa boosted kwenye mifumo ya umwagiliaji. Hatusemi muwape hela mfukoni, wakulima wetu wanahitaji miundombinu wezeshi, wanahitaji kupewa channels za masoko. Kupanga ni kuchagua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi mna-enjoy nini kwa mfano. Ndiyo, tuna ndege 19, taarifa ya ATCL wenyewe wanatuambia eti wanahudumia abiria 60,000; halafu eti wamepungua kwa sababu ya Covid mpaka 11,000 halafu watu wazima tunakaa hapa tunapitisha mpango. Tumetoka kulipa bilioni 500 juzi, ndege nyingine mpya tano. Hatuoni aibu, tupo tu, hatuoni aibu.

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu… msinichanganye jamani, acheni nina uchungu.

MWENYEKITI: Ni upande gani hiyo taarifa? Endelea, nakuruhusu. Nimekuona Mheshimiwa Shigongo.

T A A R I F A

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa taarifa mzungumzaji, Mheshimiwa Mdee, namheshimu kwa sababu ni mtu anayeelewa vitu vingi lakini natofautiana naye sehemu moja tu; katika biashara kuna suala linaitwa trading na investing.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapo-trade unachukua kitu unauza na unapata faida immediately, tunapozungumzia investing kuna incubation period ya kusubiri ndiyo uanze kupata faida. Itachukua muda ATCL ianze kutupa faida, lakini finally ATCL will pay. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, biashara ya ndege siyo trading ni investing. Let’s be patient, ATCL itatulipa. (Makofi)

MWENYEKITI: Taarifa hiyo unaipokea Mheshimiwa Halima?

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Shigongo naye anajua biashara mwenyewe hayuko vizuri sasa hivi, kwa hiyo atulie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachosema ni nini? Sipingi ndege kununuliwa, napinga maandalizi. Nitawasomea kitu kimoja hapa, taarifa ya ATCL wenyewe, wanasema hivi; Serikali inakabiliwa na mashauri ya kesi zilizokwishaamuliwa mahakamani, utekelezaji wa maamuzi ya kesi hizo haujafanyika na hivyo madeni haya yanaweka mali za Serikali katika hatari ya kukamatwa kwa ajili ya kukazia utekelezaji wa hukumu. Hatari hii inafanya tuogope kupeleka ndege zetu nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu fikiria sisi watu wazima tumenunua ndege, tumetumia trilioni 1.9, tunaogopa kulipa madeni ya kesi za Wazungu huko kwa hiyo ndege tuko nazo nyumbani. Hivi hizo ni akili ama nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulisema tunapenda sana shirika letu changamoto iliyopo kulikuwa hakuna business plan, ndiyo maana leo madeni ya ATCL mwaka 2014 ilikuwa ni bilioni 74, ilikuwa haifiki hata milioni 100 mwaka 2014/2015, leo bilioni 400 pamoja na ku-inject 1.9 trillion, hivi hamuoni?

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia, wanao mtindo wa kuninyima michango yangu nikichangia, ninashtaki kwako leo ili wanipe, tunasaidia Nchi jamani hatutafutani mchawi hapa. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Nyongeza ya Bajeti ya Mwaka 2021/2022
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru na naunga mkono hoja kwa sababu mimi ni mjumbe wa Kamati ya Bajeti, lakini pili nitambue suala la mkopo wa trilioni 1.3 ambao ulifanywa kwa uwazi, Watanzania wakaelewa. (Makofi)

Kwa hiyo tuombe huu utamaduni wa hii mikopo tunayokopa kwa sababu wananchi ndio wanalipa, uendelee kuwa wazi huko tunakoendelea; uwe mkopo wa biashara, ama uwe mkopo usio na riba, ama uwe mkopo wa riba nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nitazungumzia eneo dogo tu; uzuri Waziri ameji-commit hapa kwamba hizi fedha zitafuatiliwa mpaka mwisho na CAG atafanya kazi yake kwa ufanisi. Kwa hiyo tunategemea tunakoelekea tutapata taarifa mahususi kabisa jinsi hizi fedha zilivyotumika.

Mheshimiwa Spika, lakini mchango wangu utajikita kwenye shilingi bilioni 693 ambazo tunakwenda kukopa mkopo wa biashara kuziba nakisi. Mpaka sasa hivi kwa mujibu wa taarifa ya Wizara ya Fedha, deni la Serikali ni shilingi trilioni 68.5, maana yake huu mkopo wa shilingi bilioni 693 unakwenda kuongezea deni la Serikali. Tukijumlisha na wa sekta binafsi ni trilioni 85. Kwa hiyo hapa tunazungumza deni la Serikali kwa taarifa za Wizara ni trilioni 68.5.

Mheshimiwa Spika, tunakwenda kuongeza bilioni 693, ambayo mimi siipingi kwa sababu ni sehemu ya timu ya Bajeti. Lakini bado kuna trilioni mbili za hati fungani ambazo tumeingia mkataba kwa ajili ya kulipa mifuko ya hifadhi, sehemu ya deni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tafsiri yake ni nini; kwamba hivi karibuni deni letu la Taifa lita-shift from the current 68 trillion to almost 70 trillion. Sasa ni jambo ambalo ni muhimu sana kama Taifa tuendelee kujifanyia tathmini na ili tuweze kwenda mbele vizuri.

Mheshimiwa Spika, majuzi hapa Kamati zako za Kisekta na Kamati za Fedha zimeileza Serikali ni maeneo gani ambayo kuna mianya ya fedha za umma kupotea ama kwa makusanyo mabovu au kwa mifumo kutokusomana, kwa hiyo watu wanatumia hayo madhaifu kupiga deal. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mimi ninatarajia Serikali ichukue yale maazimio ya Bunge kama sehemu ya kuongeza mapato yetu, siyo tukiwa tuna gap tunakimbilia kwenda kukopa. Kukimbilia kukopa inawezekana ni kujifinyisha uwezo wa kufikiri na uwezo wa kufanyia kazi changamoto zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tarehe 8 Februari, CAG alituletea taarifa kwenye Kamati yetu ya Bajeti akielezea; na ninashukuru Dada Subira juzi alizungumza hapa kiujumla jumla. CAG akatuambia, juzi, tarehe 8 Februari, makusanyo gani ama mapato gani ambayo hayajakusanywa na Serikali ambayo ameelekeza kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, CAG anasema mapato ambayo hayajakusanywa ni shilingi trilioni 356. Na ukiangalia uchambuzi wa CAG…

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa inatokea upande gani?

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, kwa Hussein Nassor.

SPIKA: Mheshimiwa Hussein Amar.

T A A R I F A

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ninataka nimpe taarifa mzungumzaji kwamba yule ni Mheshimiwa Subira, siyo Bwana Subira. Ahsante.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nimesema dada yangu Subira jamani, mbona ananitoa kwenye pozi.

SPIKA: Mheshimiwa Halima Mdee, malizia mchango wako.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nimesema Dada Subira, na yeye anajua yule ni Balozi wa Kodi, namzungumzia hapa Balozi wa Kodi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tuna trilioni 356 ambazo Serikali imezikalia haijazikusanya, na CAG anasema sababu ya fedha kutokukusanywa; mosi, anasema kuchelewa utatuzi wa mapingamizi ya kodi. Kwa nini? Anasema kuna watumishi wachache ambao wanatakiwa wawepo kwenye zile Mamlaka za Rufaa za Kikodi. Liko ndani ya uwezo wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, CAG anasema TRA, wakusanyaji mapato, wana watumishi wachache.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie.

SPIKA: Dakika moja.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, namalizia.

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali mkifanyia kazi kwa ufanisi hoja za Kamati za Bunge, hoja za CAG, biashara ya kwenda kukopa nje tutaiacha, tupunguzie nchi mizigo isiyokuwa na sababu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 1 Machi, 2022 kupitia barua yenye kumbukumbu namba JA.9/ 259/01A/45 lilitolewa Tangazo la kuitwa kazini kwa waombaji wa kazi wa nafasi mbalimbali waliofanya usaili kati ya tarehe 29 Desemba, 4 – 29 Januari, 2022 na tarehe 7-10 Februari. Miongoni mwa kada zilizoitwa kazini ni Shirika la Reli Tanzania (TRC). Vijana 359 walishachukua barua na kupangiwa kituo cha kazi. Walipopeleka TRC HQ waliambiwa watapigiwa simu. Mpaka sasa hakuna mawasiliano yoyote, wanaomba ufafanuzi.

Pia kumekuwa na malalamiko kwa kutoka kada ya Maafisa Tarafa kwamba majukumu yameongezeka, huku mshahara umeshuka. Hivi sasa Afisa Tarafa anazidiwa mshahara na Watendaji wa Kata anaowasimamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ufafanuzi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Bulaya anapitia shirika letu la ATCL nimejaribu kupitia taarifa ya CAG ambayo imedondoshwa asubuhi hii, unajua tunajaribu kuwa current kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, CAG anasema mapitio yangu ya utendaji wa kifedha wa Mashirika ya Umma yalibaini kuwa masharika 10 niliyoyakagua mwaka huu, yakiwemo mashirika mawili ya kibiashara katika sekta ya umma, kampuni ya ndege na kampuni ya … yalikuwa na mtaji hasi kama inavyooneshwa kwenye Jedwali Namba 6.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaenda kwenye jedwali Na. 6 anasema, ni maoni yangu kuwa kuwa na madeni mengi kuliko mali kuna tia shaka iwapo mashirika hayo yanaweza kuendeleza huduma zao na kutimiza wajibu wao katika siku zijazo. Ukienda Jedwali la Sita mashirika ya umma yenye mtaji hasi katika mashirika yote kampuni yetu pendwa ya ndege iko Namba Moja, jumla ya mali Milioni 295, jumla ya madeni Milioni 535, mali hasi Bilioni 239.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni shirika ambalo kati ya maeneo ambayo naweza nikasema manne wakati wa Awamu ya Tano na ya Sita yaliyotengewa fedha nyingi sana kuliko maeneo mengine. Kwa tuliokuwepo kipindi hicho tulisema tumeanzisha shirika hili, tumenunua ndege wakati shirika halina mpango wa biashara!

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulisema tukapuuzwa lakini leo taarifa za Serikali zinaonyesha bayana kwamba wakati tunatoa Shilingi Trilioni 1.5 mwaka 2016 ndiyo wakati ule huo huo mpango wa muda mfupi wa biashara unatengenezwa. Matokeo yake ni nini? Mtaji hasi aliouzungumzia. Tunanunua ndege Serikali kama Mwanahisa Mkuu haweki capital halafu unategemea eti ndege ndiyo zijiendeshe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huo huo, unajiuliza kuna maneno nikiyatumia hapa sipendi kukera watu. Unamtumia wakala wa ndege eti mapacha wawili mnapangia dili ya biashara! Yaani wewe na mtoto wako, Serikali ATLC ni mali ya Serikali, wakala wa ndege ni mali ya Serikali, eti wakala wa ndege ana mkodisha ATLC ndege ambayo iko dhoofu bin hoi! Sasa matokeo yake ni nini? Matokeo yake ni kwamba huyu mtu ambaye hamjampa mtaji, huyu mtu ambaye ana madeni nimesema hapa zaidi ya Shilingi Bilioni 500 sasa hivi, anaongezewa madeni mengine eti na mtoto mwingine wa Serikali anaitwa wakala wa ndege, jamani hizi ni akili jamani! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaongea kwa sababu Mheshimiwa Rais alihutubia Bunge hapa na wengine tulisema tulipinga from the beginning siyo ufufuzi wa shirika ila namna lilivyofufuliwa. Mheshimiwa Rais akasema, tutafanya utaratibu Mheshimiwa Samia tufanye maboresho ya shirika letu tulipunguzie mzigo, sasa leo deni nimezungumza hapa Shilingi Bilioni zaidi ya 500.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mpango wa biashara wa ATLC, ngoja niwatajie safari zake walikuwa na mpango wa kwenda Johannesburg, safari za kimkakati za biashara Nigeria, walikuwa wanataka kwenda London na maeneo mengine ya Bara la Ulaya, lakini sasa ukija huku ndugu zangu kwa mujibu wa hotuba ya Waziri Mkuu sasa Arusha, Geita, Mtwara, Songea, Bunjumbura, Entebe, Harare, Lusaka, halafu wameanzisha vituo vitatu vya kimagumashi hivi Lumbumbashi, Guangzhou, Mumbai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, why tuna-divert kwenye mpango wa biashara? tunaogopa kwenda mbele watakamata ndege zetu, with due respect ni kweli ni faida kuwa na ndege 16 hadi zinapaki pale airport good! Yaani we are so proud, very proud lakini unakuwaje na ndege ambazo hazikuletei tija? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema hapa hivi unafikiria kwa sababu eti mmempa wakala wa ndege ambaye anamuongezea mzigo ATLC ndiyo mkienda ‘mtoni’ hamkamatwi? Hizi ni mali za Tanzania. Tutibu tatizo tulipe madeni, Serikali ndiyo mwanahisa Mkuu wa Shirika, weka mtaji maisha yaendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna viwanja 15 vya ndege nchi hii, katika viwanja 15 viwanja Vinne ndiyo vinaweza kufanya kazi masaa 24 my friend!

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo tunapozungumza haya …

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Waziri wa Fedha.

T A A R I F A

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mchangiaji kwamba utaratibu unaotumika wa Wakala, Serikali pamoja na Shirika hauhusiani na masuala ya madeni. Serikali ilishalipa madeni, ndege zetu hazina risk ya kukamatwa popote duniani, haya mambo yanayohusiana na madeni madeni yote yalishalipwa. Hakuna sehemu ndege ya Tanzania itaenda ikamatwe kwa ajili ya madeni na zitakuja na ndege za mizigo zitafanya safari zote za mizigo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kama kuna eneo lolote, ndege ya Tanzania haijaenda zitakuwa ni logistics tu za mambo ya kufungua anga kutokana na mambo ya COVID-19 yaliyokuwa yanatokea, lakini siyo kwa masuala ya madeni, madeni yote yalishalipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna deni lolote ambalo linaiweka nchi yetu kwenye risk ya kukamatiwa mali yeyote ya Tanzania, na taarifa zingine hizo zitakuwa taarifa ambazo zinaendelea kukamilisha taratibu tu ambazo ni za masuala ya kianga na maeneo tofauti baada ya pandemic ya covid.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mdee unapokea taarifa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nina taarifa hapa ya shirika lenyewe kwa Kamati ya PAC inasema hivi ukurasa wa 10, naweza nikakupatia Mheshimiwa Waziri, inawezekana ulitoa hela zikaishia katikati. Inasema madeni ya ATCL na Serikali yanaathiri biashara na utendaji wa ATCL kwa kushindwa kutekeleza mipango ya kibiashara na kuhofia kukamatwa kwa ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano safari zilizoanzishwa za Johannesburg zilisitishwa wakati mipango ya kuanzisha safari za kimkakati za kibiashara za Nigeria, London na maeneo mengine. Hii ni nyaraka inaonesha ukurasa wa Kumi nitakupatia hii nyaraka.

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimtaarifu mchangiaji ya kwamba taarifa anayoisema ni ya hesabu za fedha za mwaka 2019/2020, na tayari Kamati ya PAC mimi nikiwa mjumbe wa Kamati ya PAC deni la awali lilishalipwa Shilingi Bilioni 120 ambazo ziliripotiwa katika mwaka wa fedha husika.

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Halima Mdee unaipokea hiyo taarifa?

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa niliyonayo mimi ni ya tarehe 31 Januari, 2022 juzi na imesainiwa na Afisa Mtendaji Mkuu Mhandisi Ladislaus Matindi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema haya unajua mimi nashindwa kuelewa tunapozungumza haya mambo hakuna anayemvizia mwenzie hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa natamani huo uchungu ambao wote tunao huo wa kupanda kwa mafuta na natarajia kipindi cha bajeti ya Nishati hapa ama kipindi cha Bajeti Kuu hapa, kama mzizi wa fitina wa mafuta, kama mzizi wa fitina wa vyakula kupanda bei, haujatafutiwa ufumbuzi pachimbike na ndiyo nitajua kweli sisi ni Wawakilishi wa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiroho safi Tanzania ni yetu, siyo kwa ubaya! kwa hiyo ninaposema wakati wa taarifa ya Waziri Mkuu inaonesha tuna miruko ya ndani, katika viwanja 15 vya ndani, vinavyoweza kuruka masaa 24 basi hata tutendee haki ndege zetu ni viwanja Vinne my friend! Nilidhani Waziri wa Fedha ataniambia, Halima wakati tunaanza kupata kwenda huko mbele tutahakikisha viwanja vyote 15 vya ndani vinafanya kazi masaa 24. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Na mimi niungane na wote ambao wanazungumzia utumishi wa umma, wanazungumzia wafanyakazi wanapoajiriwa, suala la umri; ukisema umri miaka 25 wakati Wabunge wengi hapa wanasema tuwaangalie wale ambao walikuwa wameshaanza kujitolea, then nadhani itakuwa hai-make sense. Kwa hiyo, naamini Waziri wakati anajibu yale masharti ya umri yatakuja kutolewa kulingana na mazingira yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili, yamekuwa yakizungumzwa masuala mengi sana kuhusiana na kustaafu. Waziri Jenista atasema yeye anahusika na watumishi wa umma, lakini vilevile atasema masuala ya kustaafu yako Wizara ya Vijana kwa sababu inasimamia mifuko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ni ukweli hivi vitu haviwezi kutenganishwa. Nimesema mtumishi anaanza pale anapoajiriwa, pale anapofanya kazi, pale anapostaafu. Sasa unapokuwa na mtumishi sasahivi yuko kazini halafu hajui mustakabali wake baada ya ajira, akiwa mtu mzima wakati viungo vya mwili vimechoka hana uwezo wa kufanya kazi, hiyo si sawa. Na kwa sababu Serikali ni moja ninatarajia kabla Mheshimiwa Jenista hajajibu Waziri anayehusika na mifuko atueleze Watanzania hali ya mifuko ya umma ikoje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana kazungumza Mheshimiwa Bulaya hapa, akasema, tathmini iliyofanyika inaonesha mfuko wa PSSF uko below average, una hali mbaya. Unatakiwa kwa wastani kwa kiwango cha chini iwe asilimia 40, leo iko asilimia 22, tunataka mtujibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipitia Taarifa ya CAG kidogo. Shirika la Reli, kwa mfano, unaambiwa makato ya Mfuko wa Pension kwa Watumishi wa Umma ya thamani ya shilingi bilioni 99.6 hayajapelekwa PSSF. Yani kuanzia mwaka 2015 mpaka mwaka 2021 watumishi wa Shirika la Reli, shirika la umma, makato yao hayajapelekwa. Hivi mtasema hamtakiwi kujibu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunajenga reli ya SGR. Reli ya SGR ikikamilika na matawi yake yote ambayo hili Shirika la Reli ndilo linasimamia itaigharimu Taifa shilingi trilioni 32, SGR na matawi yake yote. Hivi kweli tukiwaambia kwa nini msiwajibike kutoa taarifa hapa ili watumishi wa nchi hii wajue hali yao? Tunataka Waziri wa Kazi ukija hapa, hii ni Serikali, tunazungumza na Serikali, mmelipa trilioni mbili sijui point moja hatifungani sio cash. Tunataka ile trilioni 2.58 iliyobaki ilipwe sasa ili mfuko uwepo kwenye uhai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Jenista niliwahi kuuliza hapa, kwa sababu mfuko huu unalipa wale wafanyakazi kabla yam waka 99 waliokuwa hawachangii. Kwa hiyo, hatushangai Wabunge wanavyosema wastaafu wanastaafu mafao yanachelewa kwa sababu lile kapu halina hela, huo ndio ukweli.

Kwa hiyo tunataka Mheshimiwa tujibiwe, hiki kikombe ulikikimbia ulivyoondoka ile Wizara, hiki kikombe tunataka kijibiwe leo na Serikali kwa sababu tunazungumza na Serikali. Hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, Wakala wa Ndege Mheshimiwa Jenista. Wakala wa ndege uko chini yako, ATCL wanasema sababu ya kushindwa kufanya kazi ni kwa sababu wanawalipa Wakala wa Ndege tozo ya kukodi na pesa ya marekebisho ya ndege, ukarabati wa ndege. Na wanasema zimelipwa milioni 159, wanasema hivi wanawalipa nyie fedha za ukarabati, lakini ikija kwenye ukarabati hamtoi pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Jenista ukurasa wa 41 wa hotuba yako inasema wazi kabisa…

MWENYEKITI: Unaongea na Kiti ee.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naongea na…

MWENYEKITI: Unaongea na Kiti. Usimu-address Waziri.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naongea na wewe ndiyo, huku namu-address Mheshimiwa Jenista Mhagama. Unasimamia Wakala wa Ndege, kwenye mipango yako ya mwaka huu, unasema wazi kabisa utafanya matengenezo ya ndege ya viongozi wakuu, utafanya matengenezo ya ndege ambayo ni aina ya Forker 50, hakuna ndege yoyote kati ya hizi ambazo ni zile ndege 16 za ATCL, hapa ndipo ulipo mzizi wa fitina.

Sasa nataka ukinijibu uje ueleze kwa namna gani zile fedha ambazo kwa akili ambayo kwa kawaida hai-make mantiki mmekodisha ndugu zenu shilingi bilioni 159 ambazo kati ya hizo milioni 59.4 ni za matengenezo ya ndege. Kwa nini mnaliachia shirika la ndege likarabati na kufanya matengenezo ya ndege zake peke yake? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mwisho, na si kwa umuhimu. Tunaambiwa kwamba…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa hotuba ya Waziri, ukurasa wa 28 Serikali imelipa madai ya malimbikizo ya mishahara ya watumishi 14,398 yenye jumla ya shilingi 25,655,898,954.61 hadi Machi, 2023. Vilevile madai ya malimbikizo ya mishahara ya watumishi wa umma 2,942 waliokoma utumishi wao yamelipwa, na kwamba kwa kipindi cha mwaka mmoja kuanzia Februari, 2021 hadi Machi, 2023 Serikali imelipa madai ya malimbikizo ya mishahara 119,098 yenye thamani ya shilingi 204,420,741,285.25.

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Waziri alieleze Bunge hili tukufu madai hayo inayosemekana yamelipwa yanatokana na kiasi gani kinachodaiwa na cha muda gani? Na kiasi gani bado hakijalipwa na kina muda gani? Hii inatokana ukweli kwamba bado madai ya watumishi ambayo hayajalipwa ni mengi na malalamiko yamekuwa mengi sana.

Mheshimiwa Spika, moja ya jukumu ambalo Wakala wa Ndege za Serikali iliongezewa mwaka 2016 ni jukumu la kuratibu ununuzi wa ndege na kukodisha kwa Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL), halikadhalika kusimamia mikataba ya ukodishwaji wa ndege hizo kwa niaba ya Serikali. Ningependa kufahamu kwa mwaka wa fedha 2023/2024 tunatarajia kutumia kiasi gani kwa ununuzi wa ndege? Lakini pia kumekuwepo na malalamiko toka ATCL, moja ya sababu linalolifanya shirika husika kujiendesha kwa hasara ni mkataba mbovu wa ukodishaji na matengehezo ya ndege. Nini kauli ya Serikali kuhusiana na hili na hatua gani inatarajia kulichukua kunusuru shirika letu la ndege?

Mheshimiwa Spika, naomba nipate ufafanuzi wa kina kwenye maeneo hayo mawili.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, na mimi nitachangia kwa uchache. Mosi nikitambua maelekezo aliyoyatoa Mheshimiwa Waziri Mkuu katika mahitimisho yake Tarehe 13, Mwezi wanne mwaka 2023, kuhusiana na asilimia kumi ya mikopo ya Vijana, wanawake na watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika utambuzi huo nilidhani Waziri wakati anajibu atusaidie mambo kadhaa. Kwa sababu siku zote huwa nasema hii ni Wizara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; ninyi hapo mmepewa dhamana ya kumsaidia. Katika mazingira ya kawaida, Wizara ambayo ni ya Rais inategemewa iwe ni mfano kwa Wizara nyingine kuiga. Sasa, tumeambiwa kwenye taarifa mbalimbali za Mkaguzi Mkuu; ya mwaka jana, ambapo mwaka jana pamoja na mambo mengine ilifanya majumuisho ya fedha ambazo hazijarejeshwa katika kipindi cha miaka mitano ya mfuko wa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu. Kwa hiyo ukijumlisha za mwaka jana ambayo ilikuwa ni bilioni 47.1 na za miaka ya nyuma yake minne inaenda kama bilioni 100 plus, ukijumlisha na za mwaka huu ambazo ni bilioni 88 maana yake unaenda 188 billion plus.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shida yangu ni moja, nimesoma maelekezo yako mahsusi ambayo umepeleka kwenye mamlaka za Mikoa na Halmashauri, maelekezo 14, hatuoni popote ulipotoa maelekezo kwa Wakuu wa Mikoa, kwa Wakurugenzi kuhakikisha kwamba hizi fedha ambazo zimepotea huko chini inasemekana zimepotea huko chini, ziweze kupatikana zote. Sasa unapotoa maelekezo 14 lakini elekezo la upotevu wa billions of money hamtoi maelekezo mahsusi, unatupa jibu gani? Kwamba inawezekana kabisa hili jambo hamlichukulii serious, inawezakana kabisa hiyo miezi mitatu ikiisha ukaja mfumo mwingine mambo yatakuwa yale yale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaitaka Serikali kabisa na nikutake Waziri, ukiwa unajibu hapa utoe maelekezo ya fedha hizi zilizopotea huko chini kwa wajanja, zikusanywe. Ulizungumza hapa Bungeni ukiwa unajibu swali lakini kujibu swali hapa Bungeni ni jambo lingine, kutoa maelekezo mahsusi kuhusu suala la kibajeti ni jambo lingine, hamjaliona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapopitia Kanuni za utoaji wa asilimia 10, unagundua kwamba hizi fedha hazijapotea, hizi fedha zimepotezwa. Sasa kama fedha zimepotezwa kuna element ya jinai hapa, lazima watu wawajibike kama wamehujumu uchumi, haiwezekani!

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu mnasimama hapa mnasema Rais wetu anazunguka mataifa kwenda kuomba fedha, hivi hamuoni aibu Rais anahangaika, fedha zinakuja halafu wajanja huko chini wanapiga? Kwa sababu ni kweli hizi ni mapato ya ndani ya Halmashauri yes, lakini ni sehemu ya mapato ya ndani ya Halmashauri ambayo kutokana na Halmashauri zetu kutokuwa na uwezo wa kimapato tunategemea mikopo ya nje kuendesha mambo mengine ya kule chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kanuni hii nitarejea tu kwa mfano, Kanuni ya Saba inawataja Watendaji wa Kijiji, Watendaji wa Mitaa na Watendaji wa Kata kama watu wa kutawakilisha vikundi, kuanzia Kijiji. Kanuni ya 13 Afisa Maendeleo ya Jamii anatajwa yeye ni usajili na uratibu, Kanuni ya 14 kuna Kamati ya Huduma ya Mikopo kuna Mkurugenzi wa Halmashauri na timu yake yeye anachambua na anajadili na kufuatilia vikundi. Kanuni ya 17 inataja Kamati ya Kudumu ya Fedha na Mipango ya Halmashauri zetu, wao wanaidhinisha mikopo, wako Madiwani, tuko Wabunge huku ndani, Kanuni ya 18 ni Mkutano wa Halmashauri kupitisha kile ambacho Kamati imepitisha. Kanuni ya 20 Sekretatarieti ya Mkoa wana jukumu la ufuatiliaji, Kanuni ya 21 Ofisi ya Rais - TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Bunge lituambie hapa eti kuna vikundi hewa huko chini? Nchi hii ilivyokuwa na cheo mpaka huko chini? Nchi hii mtu ukifanya hata uhalifu wa kawaida unavyoweza kutafutwa, kwa nini hapa kuna kitendawili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi ninapendekeza, CAG afanye kitu kinachoitwa Forensic Auditing yaani ukaguzi wa kiuchunguzi ili tuangalie kama kuna udanganyifu, kuna wizi ama kuna rushwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi vitu hatuwezi kuviacha viende hivi. Mimi niseme wazi kabisa ili mradi Kiongozi wetu wa Muhimili Mheshimiwa Spika ametuamini kwenye Kamati ya LAAC tutafanya kazi yetu kwa uaminifu na kwa uadilifu mkubwa kulisaidia Taifa hili. Haiwezekani unaenda kuomba omba huko halafu unakuja Bilioni zaidi ya 100 zinadondoka chini halafu na wewe unacheka cheka tu! No, no, no! Mambo hayaendi hivyo. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Halima muda wako umeisha.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria mbalimbali (Na. 2) wa Mwaka 2019 (Toleo la Kiingereza).
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwanza kwa kuongeze hapo uliposema, naamini Serikali itaacha ubishi ama itapokea ushauri wa Kamati ambao ulitaka ipunguze masharti magumu na mazito ya kifungu cha 86A na 86B ili kuruhusu minerals ziweze kutoka maeneo mengine ziingie nchini, then sisi kama nchi tu-export. Kwa hiyo, naamini Serikali licha ya kwamba Kamati tulishauri kwa muda mrefu wakaja na msimamo wao mkali baada ya kauli za Spika watalegeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, ni muhimu kupitia Muswada huu Serikali ikiri kwamba wakati wa Bunge la Bajeti ina wajibu
wa kusikiliza, kwa sababu ukiangalia mambo yanayohusiana na 18% ya wachimbaji wadogo, 5% ya withholding tax na 18% ya VAT kuondoa kwa wachimbaji wadogo, hili suala la zabibu lilizungumzwa kwenye bajeti, Kamati ya Bajeti ikaleta, Kambi Rasmi ya Upinzani ikashauri, Serikali ikakataa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa swali linakuja, je Serikali imeleta mabadiliko haya ya Finance Bill, actually ukisoma between the lines tunafanya marekebisho ya Finance Act lakini kwa sababu haiwezi kuletwa katikati, tunatumia miscellaneous. Sasa Serikali imeona imepanua wigo wa kodi ngumu na nzito, fedha zimekosekana, tumeamua kuchenjia gia hewani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni ushauri tu Serikali ilenge kusikiliza sababu pale ambapo tumeweka kodi mpaka zinakuwa kero, tunafanya watu wakwepe kodi. Tunafanya watu badala ya kutumia rasilimali za ndani, wa-import kutoka nje. Walisema juzi kwamba Mheshimiwa Dkt. Mpango ameanza kusikiliza, naona kwa mabadiliko haya Mheshimiwa Dkt. Mpango ataanza kusikiliza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la tatu, suala property tax, kodi za majengo, dhamira ya uanzishaji wa vyanzo vya mapato ya halmashauri mbalimbali ni kuziwezesha kujiendesha. Ndio maana Serikali Kuu ina vyanzo vyake na Serikali za Mitaa zina vyanzo vyake. Tunatambua kwamba TRA ndio custodian wa makusanyo, lakini pale ambapo wanakusanya kodi ya majengo Kawe, spirit ya kodi ya majengo ni Mama Mollel alipe kodi, halmashauri ikamrekebishia barabara yake, hiyo ndio spirit. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa leo Serikali inakusanya vyanzo vya halmashauri, inaweka kwenye kapu kuu pesa ambayo wananchi wake ambao wanatozwa kodi zingine, hizi zinazotozwa na halmashauri hawa -feel mchango wao kwenye halmashauri zao. Sasa katika spirit ya kusikiliza na ninyi mnajua kwamba Serikali Kuu, halmashauri inacholeta kikubwa ni mishahara ya watumishi na miradi michache mikubwa. Ujenzi wa madarasa, zahanati, ununuzi wa madawati na utengenezaji wa barabara ni wa halmashauri. Pamoja na kwamba TARURA imeanzishwa inategemea halmashauri, tutaendeshaje hizi halmashauri? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikuombe na nimwombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwamba hatuwezi kuua decentralization iliyojengwa for more than 20 years. Kama nchi lazima tuwe tuna vitu vinavyotu-guide, haya mambo ya kila awamu ikija inakuja na mambo yake tunalipoteza Taifa. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Mwaka 2022 tulipokuwa tukijadili Wizara ya Ardhi, moja kati ya mjadala mkubwa ni kwamba nchi yetu mpaka sasa haina mpango wa matumizi bora wa ardhi uliokamilika. Mwaka jana 2022 tulikuwa tunapigana hapa kuomba Tume ya Taifa ya Mipango ipate Shilingi bilioni 10 tu ili ifanye mipango tujue ardhi ya kilimo na ardhi ya wafugaji, ili tuweze kuepukana na migogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu Waziri wa Kilimo ambaye hana dhamana kwenye masuala ya ardhi, ana jukumu la kugawa hekta milioni moja za ardhi ya nchi hii wakati hatuna taarifa za hali ya ardhi ikoje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku zote nasema, tuangalie kizazi kinachokuja, tusiangalie sasa. Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yako unasema, 2050 tutakuwa na Watanzania milioni 136 kutoka milioni 61 ya sasa hivi. Tunapozungumza sensa ya makazi, asilimia 44 ni ya watoto chini ya miaka 18; sijazungumza chini ya miaka 21, sijazungumza chini ya miaka 35. We have a very young generation. Tunagawiana ardhi. Sipingi vijana kupata ardhi, napinga concept ya Wizara kutafuta wakulima kama ambavyo tunatafuta ma-nurse na walimu. Ndiyo shida yangu kubwa na ninyi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha kwa sababu, hata hayo mashamba yenyewe, nilisoma tangazo lenu, hizo block farms bila kuwa na mwekezaji mkubwa, hii program haiwezi ku-take off; kwa mujibu wa tangazo lenu na kwa maelezo yenu. Unahitaji mwekezaji mkubwa ambaye atapewa kuanzia heka 1,000 mpaka 20,000 na vijana wetu ambao watapewa kuanzia hekta moja mpaka hekta 10.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasikitika kwa sababu, Waziri anasema, katika hizi hekta milioni moja atakazozigawa, wastani wa kusafisha hekta moja ni shilingi 16,800,000; kusafisha, kusawazisha udongo, kuweka miundombinu ya umwagiliaji. Hapa tuna wakulima. Hivi kweli mkulima anaweza kusafisha heka moja, kusawazisha kwa Shilingi milioni 16 na kuweka miundombinu ya umwagiliaji? Mheshimiwa Waziri anasema mpaka 2025 – 2030 wanatarijia kutumia Shilingi trilioni 16.8. Hiki ni kilimo cha iPad, hiki ni kilimo cha mjini. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumza kusaidia nchi. Mheshimiwa Mama Kilango anazungumza vizuri hapa. Majimbo 188 ni ya wakulima, tena wakulima wanaolisha nchi hii ni wakulima wadogo wadogo, wanasaidia 26 percent ya GDP ya nchi hii miaka yote. Hivyo, tujiulize basi, Mheshimiwa Bashe, kama ni wakulima wadogo given the fact kwamba Tanzania ni young generation, vijana wakulima wako kule; wakike wakiume wako kule. I can assure you my friend, najua you guys are working hard, lakini lazima tushauriane. Hii Shilingi trilioni 16 mkienda mki i-pump in kwa wakulima tuliokuwanao, I can assure you GDP ita-move from 26 to 50 even to 60 percent. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikiliza. I am very disappointed! Tusifanye kilimo cha politics, tusifanye kilicho cha kusema tunaangalia uchaguzi 2025. Tufanye kilimo kwa kuangalia the coming generation. Mheshimiwa Bashe nakuomba, hao watoto wa watu hapa umeshawakusanya, ndiyo hivyo, umeshawapa matumaini, huna namna. Ninachokisema ni hivi, hii tuitumie tu kama case study, kuwamba ngoma, ndiyo imeshapanuka hivyo, huwezi kuwakatisha tamaa, lakini kuanzia mwaka ujao wa fedha 2023/2024 tunataka utuambie ni kwa namna gani hayo mafungu mengine yaliyobaki mnaenda ku-inject kwa wakulima wadogo tuliokuwanao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ni akili ya kawaida! Nasikia Wabunge wenzangu hapa wanashukuru ruzuku, hivi unafikiri wakulima wetu wangekuwa na hela wangekuwa na njaa ya mbolea? Poor commonsense! Yaani tuko hapa, kila mtu anashukuru eti ruzuku, sijui kimeenda, kimerudi, ruzuku hiyo ni ya mbolea, for God’s sake, that is poverty! That is poverty! Kwa hiyo, tunafurahia wakulima wetu waendelee kuwa masikini halafu tunakuja kuwapa mbolea, halafu mbolea zenyewe za Wazungu tunazoagiza huko kwa billions of money. We should use our brains.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi, mmeanza hapa, mmeshaita Watoto, mmeshawakusanya huko, sawa hao wapoozeni. Mwaka ujao wa bajeti tunataka tuambiwe mnawasaidiaje wakulima wadogo wa nchi hii? Mheshimiwa Bashe, kingine, hivi mazao ya kimkakati ya nchi hii ya kutuingizia foreign currency ni vipi? Huwezi kuridhisha kila mtu my friend. Wamezungumza juzi hapa, wamesema ngano kila mwaka more than five hundred billion tunatumia; na sita nimesoma ripoti ya CAG ya ufanisi kwa miaka minne tumetumia 2.7 trillion kuagiza nje. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, parachichi, OUSB na FAO wanasema, by twenty thirty thamani ya soko la parachichi duniani ni fourteen trillion. Bashe, nchi hii ina mikoa zaidi ya nane, inalima parachichi tena inayotakiwa Ulaya huko, inayotakiwa Asia huko. Why aren’t you using common sense? This is fourteen trillion, tungeenda kuwasaidia wakulima wa parachichi, wakulima wa ngano, wakulima sijui kwenye maeneo strategic, nchi ingepata fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme tu ndugu yangu, we should think of the next generation. Unagawa hekta milioni moja, hivi ninyi mnajua hekta milioni moja! Hivi mnazijua, ama ni kwa sababu huko Wizarani hakuna wakulima! Kenya kwa parachichi pekee, kwa sababu Kenya ndio a leading country kwa ku-export parachichi kwa Afrika. eighty five percent ya export za parachichi zinachangiwa na wakulima wadogo wa Kenya. The remaining fifteen percent ndio wakulima wakubwa. Kwa hiyo, ni vizuri kuwa na wakulima wakubwa, lakini tusijipe utumwa wa wakulima wakubwa, tusaidie wakulima wetu, nchi itasogea. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, na mimi nitatoa mchango wangu. Nitambue humbleness ya Waziri na timu yake, hamna shida na mtu, mnasikiliza. Lakini kama kawaida mimi nitashauri na tukishauri naomba msichukulie personal badala ya kujibu hoja mnafanya personal attacks, tunashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya kwanza miradi ya barabara. Mheshimiwa Waziri nilipitia randama yako ambayo imeanisha miradi mbalimbali ambayo mnataka kuitekeleza.Nimefanya uchambuzi wa miradi 69 ya barabara yenye urefu wa kilometa 11,696.88. Kiwango cha fedha ambacho kimetengwa kwa mwaka huu wa fedha kujenga barabara mlizozianisha kwa mwaka huu wa fedha ni shilingi bilioni 434.66, miradi hii 69, sizungumzii miradi yote kiujumla wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukizungumzia gharama ya ujenzi wa kilometa moja ya lami, kilometa moja ya lami ni kati ya bilioni moja ama bilioni mbili. Kwa shilingi bilioni 434 zilizotajwa inatuambia, kama gharama za ujenzi ni bilioni moja kilometa moja maana yake katika kilometa 11,699 mlizozianisha zitajengwa kilometa 434 tu kwa hii miradi 69. Kama ni bilioni mbili mbili kwa kilometa moja ambayo ndio standard ya sasa hivi zitajengwa kilometa 217.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku zote nimekuwa nikisema kwamba Wabunge tunakuwa tunaleweshwa tukiona barabara zetu zimetajwa, lakini tukienda kuangalia unaweza ukakuta, kuna hii Barabara ya Kibireshi unakuta kilometa 450 imepewa milioni tano. Sasa, bilioni tano ni kilometa mbili na nusu ama kilometa tatu. Sasa fikiria, ninazungumzia randama yenu. Kama nimekosea mtanisahihisha, lakini kibireshi imetengewa bilioni tano, na ni kilometa mbili. Sasa nawashauri wenzangu (colleagues), nendeni mkapitie randama halafu utoke ujue ulivyoambiwa umepewa kilometa 50 hela kwa mwaka umepangiwa kiasi gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana Waheshimiwa Wabunge hawaishi kulalamika CAG..

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unilindie muda wangu.

MWENYEKITI: Taarifa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, atajibu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa mwache tu, mpe taarifa hiyo, Mheshimiwa Waziri.

TAARIFA

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mchango mzuri anaosema Mheshimiwa Halima, naomba kumpa taarifa kwamba miradi yote mikubwa ukiondoa darasa ambalo linajengwa kwa force account au zahanati miradi mingine yote inayojengwa kwanza time frame yake inazidi mwaka mmoja wa bajeti. Kwa mfano barabara ya kutoka Karatu kwenda mpaka Maswa haitarajiwi ijengwe ndani ya mwaka mmoja barabara ya kutoka Mikumi kwenda Lumecha mpaka Londo kule Songea haitarajiwi ijengwe mwaka mmoja.

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Waziri…

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: …Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya kutoka Handeni, Kibireshi mpaka Singida haijengwi mwaka mmoja...

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa ananipotezea muda wangu. ulipewa dakika mbili Mheshimiwa Mwigulu utanijibu…

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: ...Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachofanyika inatolewa down payment na baada ya hapo certificate zinaanza kutolewa na kulipiwa kadri kazi inavyotekelezwa…

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa amesha kuelewa huyu. Mheshimiwa Halima.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Waziri wa Fedha anaona ni value for money kwa barabara moja kwa mwaka mmoja kujengwa kilometa mbili nina mashaka. CAG katika ripoti yake amesema hivi TARURA na TANROADS, hawa hapa, wana madeni kutokana na kwanza tunakuwa na project nyingi hatuna fedha za kulipa hatulipi wakandarasi kwa wakati matokeo yake ni nini? Tunaambiwa kutokana tu na madeni haya ya bilioni 673 tumetoa riba, malipo shilingi bilioni 69. Sasa common sense bilioni 69 unajenga kilometa 69 za barabara, kama thamani ni bilioni moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilikuwa nasema, na uzuri Kamati ya Bunge ya Bajeti, Mwenyekiti wangu yupo hapa, Mheshimiwa Sillo, mwaka jana 2022/2023 wakati tunatoa hotuba yetu ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa 2022/2023 tulisema masula yafuatayo; kwanza tulishauri barabara zijengwe chache zisiibuliwe mpya ili kazi ikifanyika ifanyike kwa ukamilifu wake. Tulipendekeza mapendekezo mengi sana, tukaishauri Serikali, hamsikilizi, matokeo yake ni nini? riba 70 million, can you see? Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili bandari yetu. Nitaomba nizungumze masula haya machache, la kwanza, hakuna mtu yoyote atakayepinga sekta binafsi isishirikiane na Serikali kwa uwekezaji, hayupo, kwa sababu bila sekta binafsi mambo hayaendi. Lakini muhimu ni kujiuliza sekta binafsi hii ambayo tunataka kwenda kuichukua tumejifunza tulikotoka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na TICTS for 20 years. TICTS ilikuwa ni mwiba sugu Waheshimiwa Wabunge wa mwaka 2008 wako hapa. Baada ya Serikali kuingia chaka 2008 tukaweka resolution, kwamba ikavunje mkataba, ilishindikana, TICTS imekuwa donda ndugu mpaka mkataba ulivyoisha. Ndiyo maana leo Mheshimiwa Waziri unatueleza faida ya TICTS kuanzia 2012 mpaka 2021; hujatuambia, tangu mwaka 2001, mpaka 2010, Taifa limepata nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nashauri, ushauri, mtasikiliza mtaacha, tusikurupiuke, tufanye tathmini ya kina tulikosea wapi tunaendaje, tusije tukajikuta ndugu zangu makosa ya TICTS yanajirudia. Mmepewa dhamana lakini nchi hii ni ya Watanzania ninyi mnapita tu. Kwa hiyo whichever decision itakayofanyike ifanyike tathmini ya kina. Siyo tayari tunawawekezaji wetu kapuni tunakuja hapa Waheshimiwa Wabunge tunachangia hapa halafu tunashindwa kwenda kuisimamia Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hili la bandari, bandari ni usalama wa nchi, bandari ni roho ya nchi, bandari ndiyo future ya watoto wetu, tusifanye makosa, kukurupuka kwa sababu tuliamini miaka 20 iliyopita.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru nikiongezea kwa hoja ya Mheshimiwa Mhagama kuhusiana na eneo la Bunge, nakumbuka wakati wa hotuba ya Waziri Mkuu, Kamati ya Bajeti ilieleza suala hili kwa kina na tukaambiwa kwamba hoja hii imepelekwa Wizara ya Ardhi, kwa mantiki ya dhamira ya kutwaa maeneo. Sasa nilikuwa nadhani kwa sababu Wizara yenyewe mko hapa ni wakati muafaka wa kulitolea majibu hili ili kama kuna namna ya hatua za ziada kama ambavyo imependekezwa na Mheshimiwa Mbunge, iweze kufanyika kwa haraka, kwa sababu siku hazigandi na thamani ya ardhi inapanda kila siku kwa hiyo lazima uamuzi ufanyike na ufanyike haraka kwa maslahi mapana ya Taasisi ya Bunge lakini na wananchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili jana nilisikiliza kwa makini Wizara ya Mifugo, migogoro ya ardhi ilizungumzwa ikashikwa Shilingi hapa ikapigwa juu kwa juu kimtindo, lakini dhamira ilikuwa ni kuwapa somo wajifunze tunakoelekea inakuwaje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo nikisoma hotuba ya Waziri, migogoro ya ardhi vilevile imezungumzwa na Waziri anasema kabisa kwamba katika mwaka 2021/2022 walitarajia kutatua migogoro 1,000 lakini wakatatua migogoro 1,800. Sasa ukimsoma nae Waziri wa Mifugo jana anasema alifanya mikutano 28 kwa ajili ya kutatua migogoro baina ya wafugaji na watumiaji wengine, yaani ni kama vile kutatua migogoro ni sifa. Mawaziri wameacha kufanya shughuli zao za msingi wanaenda kutatua migogoro. Tumesikiliza taarifa ya Kamati ya Ardhi imesema…

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU (MHE. UMMY NDERIANANGA): Mheshimiwa Spika, taarifa.

TAARIFA

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU (MHE. UMMY NDERIANANGA): Mheshimiwa Spika, ahsante naomba kumpa taarifa Mheshimiwa Dada yangu Halima Mdee kwamba kati ya majukumu mengine ambayo Waheshimiwa Mawaziri walipewa, wamepewa kwa mujibu wa kanuni na utaratibu waendelee kufanya zoezi hilo. Kwa hiyo, asiseme kwamba wameacha majukumu yao ni kati ya sehemu ya majukumu yao kufanya shughuli hizo. Ahsante. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Halima Mdee, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. HALIMA J. MDEE: Siwezi kuipokea, mdogo wangu alitakiwa asubiri kwanza niendelee ajue najengaje hoja. Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati amesema hapa, kuna tatizo kubwa sana la kibajeti kwenye Tume inayowajibika kupanga nchi. Hili tatizo tunalizungumza leo kwa sisi wakongwe ni mwaka wa 15, sasa Mheshimiwa kama tusipojua principle moja kama Taifa, wananchi tunaongezeka ardhi haiongezeki. (Makofi)

Mheshimiwa kwa takwimu za Wizara yenyewe wakati tunapata uhuru mwaka 1961 watu walikuwa Milioni 10.3, ukigawa maeneo ambayo tunatakiwa tutumie ukiacha hifadhi na mambo mengine, ilikuwa gawio la ardhi kwa kila mtu ni wastani wa eka 8.4 mwaka 1961. Sensa 2012 tunaambiwa tulikuwa Milioni 43, kwa takwimu ya ardhi gawio ni hekta Mbili kwa kila mmoja tunazidi kudondoka, leo tunaenda sensa 2022 possibly ya Watanzania kufika Milioni 100 ni kubwa tutafika wapi? Mipango ya matumizi bora ya ardhi mifugo tunazungumza migogoro ya mifugo na wakulima, tunaambiwa 1978 tulikuwa tuna mifugo Milioni 21, mwaka 2012 tuna mifugo Milioni 43. Jana nimejumlisha kwa mujibu wa Waziri wa Mifugo ukichanganya ng’ombe, kondoo, mbuzi, kuku na kitimoto tuna jumla ya mifugo 1,165,000. Ninasema hivi nchi square meter ni zile zile square kilomita zile zile 945,000 lakini tume-shift from 10 Milioni Mungu anajua sensa itatuambiaje.

Mheshimiwa Spika, tume-shift from 20 and so now tuko 1,165,000, tunaambiwa hapa tumepitisha sisi wenyewe mpango wa miaka mitano, Tume yetu inahitaji Bilioni 15 tu kwa mwaka kuweza kufanikisha baada ya miaka mitano tuweze kupima vijiji 6,160. Bilioni 10 hivi leo kweli eneo hili muhimu ambalo tumejipangia kupima vijiji 719 kila mwaka tutimize target ya miaka hivi hatuna Bilioni 10? Halafu mnatuambia kwenye hotuba zenu hapa eti mnapiga maziara hivi hizo ziara mlizozipiga nyie wakubwa, tokea tumeanza kutatua migogoro ya ardhi nchi, hii hivi mmetumia shilingi ngapi? Au kwangu mimi kwa tafsiri yangu tu ya kawaida, ni hivi migogoro ya ardhi tunatumia kama dili kimtindo na kuweza kupata shughuli za kufanya.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu huwezi kuniambia tunakosa 10 Bilioni ambayo mimi nahakika Lukuvi pale kwa uzoefu wake, kwenye akaunti yake ana Bilioni 10 kama mimi ninayo kidogo dogo yeye anakosaje? Kwenye eneo ambalo tunatakiwa, nasema na nasisitiza kama kuna eneo ambalo tunaiomba Kamati ya Bajeti on a very serious note iende ikaliangalie katika mtindo huo huo wa maeneo ya Bunge tuliozungumza, kama tunaweza tukaenda tukafanya mambo ninaomba tumsaidie Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, najua Waziri anaandika lakini anachekelea si tunamtafutia hela, tumsadie Waziri apate Bilioni 10 tuondokane na matatizo ya migogoro ya ardhi nchi hii, wananchi wetu wanateseka, wakulima wanateseka, wafugaji wanateseka, lazima tuonyeshe leadership for once, haiwezekani Mkapa akashughulikia migogoro, Mzee wetu Mwinyi kashughulikia migogoro, Kikwete kashughulikia migogoro, Marehemu Magufuli kashughulikia migogoro na Mama Samia naye? Sasa si tumepiga Azimio leo asubuhi si ndiyo?

MBUNGE FULANI: Yes!

MHE. HALIMA J. MDEE: Tukamsifu Mama anaupiga mwingi si ndiyo? Sasa kuupiga mwingi siyo kwa mabarabara, kuupiga mwingi ni kwa agenda zinazogusa Watanzania. Wafugaji walio wengi, wakulima walio wengi, wachimbaji madini walio wengi na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ninaomba sana nimelizungumza hili kwa sababu it pains, watu wanaumia halafu vijisenti vidogo vidogo tunashindwa kuvitoa ili kusaidia hili tatizo litatuliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho ni suala la mradi wa Kawe. Kwanza nitambue baada ya kuhangaika sana hatimaye project ya National Housing 7111, 7112 ya Shilingi Bilioni 45 inaenda kufanyakazi. Kwa hiyo, niwapongeze Wizara japokuwa tulizembea nchi ikapata hasara Bilioni 100, tusifanye uzembe wa namna hii tunaliumiza Taifa kwa kuchelewa kufanya maamuzi makini kwa wakati makini na kwa dhamira njema kusaidia nchi.

Mheshimiwa Spika, ninashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru na mimi nichangie Wizara hii muhimu na nilikuwa nadhani kwamba ni muhimu Mheshimiwa Waziri akatufanya Watanzania tukajua kwamba hii ni Wizara muhimu; mosi, inahusika na maendeleo ya jamii kwa mantiki ya kwamba jamii nzima ya Tanzania; pili, ni jinsia maana yake ni (ke) na (me) maana kuna watu wanafikiria ni Wizara ya Wanawake; tatu, wanawake wenyewe na makundi maalum ambayo ndio vijana, watoto, watu wenye ulemavu na wazee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesema niyaseme haya kwa sababu yamezungumzwa hapa na wachangiaji wengi sana, namna gani kumekuwa na ongezeko la ubakaji na kulawitiwa kwa watoto wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nilikuwa napitia taarifa za UNICEF ambazo zinatuambia ili Waziri najua hizi taarifa unazo lakini ni msisitizo tu, ili ujue jukumu lililokuwa mbele yako kwa sababu watoto wako chini yako. Watanzania kwa idadi yetu tuliyonayo sasa hivi watoto chini ya umri wa miaka 18 kwa mujibu wa UNICEF ni milioni 29.7; kwa hiyo, kwa lugha nyingine population ya Tanzania asilimia 50 ya Watanzania wote ni watoto chini ya miaka 18. Sasa tunaambiwa huyu mtoto tusipomlinda akiwa mtoto ndio anavyokuwa mtu mzima kuna vituko mbalimbali huko vinatokea, alizungumza Profesa hapa asubuhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Wizara hii tusiichukulie kama Wizara ya mzaha mzaha, ni Wizara ambayo mmepewa majukumu makubwa ya kulea Taifa. Katika hao watoto milioni 29 mimi leo nitamzungumzia mtoto wa kike ambao wako milioni 14.7. Tunaambiwa kati ya nchi ambazo zina kiwango cha juu cha ndoa za utotoni Tanzania tunaongoza, ni miongoni mwa nchi ambazo tuna kiwango cha juu cha ndoa za utotoni. Tunaambiwa kati ya watoto watano wa kike; wawili wanaolewa kabla hawajatimiza miaka 18. Sasa tujiulize katika hawa watoto milioni 14.7 kwa mnaojua mahesabu kama ndani ya watano hao ukiwagawanya kiwatano/watano kila watano wawili wanaolewa chini ya miaka 18 Taifa linakwenda wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unajua maendeleo ya Taifa yanahitaji jinsia ya (me) na jinsia ya (ke) zifanye kazi kwa pamoja tuweze kwenda mbele. Waziri unajua kizazi cha sasa sio kama kizazi cha mababu zetu na mabibi zetu, vijana wa sasa tunataka mtoto wa kike ajitume na mtoto wa kiume ajitume mnawaza nini kwa watoto hawa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaambiwa mikoa mitatu bora takwimu zinatufanya tuangalie namna gani tunakwenda kutatua tatizo. Mikoa mitatu bora ambayo kati ya wasichana watano wawili wanaolewa chini ya miaka 18, Shinyanga asilimia 56, Tabora asilimia 58, Dodoma asilimia 51 tunakwenda wapi?

Mimi niiombe Serikali juzi nilikuwa napitia maana Tanzania ni Mjumbe wa Baraza la Umoja wa Mataifa wa Haki za Binadamu katika hilo Baraza ni la Kidiplomasia ndio, lakini mnajitathmini kwa namna gani haki za binadamu zinatekelezwa kwenye nchi husika? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Halima Mdee, dakika moja, malizia. (Makofi)

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, ni masikitiko yangu dakika moja; katika maeneo ambayo tunataka Waziri hili ulijibu katika maeneo ambayo Tanzania imeweka pending, haijakubali bado kuyafanyia kazi; mosi, ni eneo la ndoa za utotoni; pili, ni eneo la masuala ya mirathi sote tunajua wakina mama wanavyoumia kuhusiana na mirathi; tatu, ku-deal na sheria hizi Customary Laws (Sheria za Kimila) zinazonyima wanawake wa Kitanzania kumiliki ardhi. (Makofi)

Sasa kwa sababu ninajua Waziri unajua nataka uniambie kwa nini Watanzania kwenye vikao vya Kimataifa huko vya haki za binadamu masuala ya mtoto wa kike na masuala ya wanawake sio kipaumbele; na kama jibu ni tofauti niambie mna taarifa gani tofauti na hii taarifa ya Umoja wa Mataifa ya Baraza la Umoja wa Mataifa linalohusiana na haki za binadamu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na mimi nianzie hapa ambapo ameishia Mheshimiwa Dkt. Samizi kuhusiana na TANESCO. CAG amesema ni miongoni mwa mashirika yanayoendeshwa kwa madeni, ina madeni zaidi ya mtaji kama ambavyo mwezangu aliyetangulia amesema na katika mashirika 16, shirika la TANESCO ni Namba Mbili, deni Trilioni 13, mtaji Trilioni Tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa jana Mheshimiwa Waziri umesema kwamba haya madeni ya TANESCO ni ya makaratasi, sasa ni muhimu kwa sababu hili ni shirika letu muhimu na tunapenda lifanyiwe reform, utuchambulie kinagaubaga kiwango kipi ni madeni ya makaratasi, kiwango kipi ni uzembe wa baadhi ya watu na kukosa kuwajibika. Ninasema hivi kwa sababu ukisikia deni linalozungumzwa na TANESCO sana ni lile Bilioni 500 la TPDC, lakini madai ya TANESCO kwa watu wengine nadhani ni kama zaidi ya Bilioni 400. Sasa hapa katikati kuna nini, na anayejua huo mzizi siyo mwingine ni wewe, lakini pili tumeambiwa hivi karibuni na nilikuwa napitiapitia hapa kwenye Mafungu yako nikifikiria kwamba nitaona sijaona, kwamba tunatakiwa kuilipa Symbion Shilingi Bilioni 355, kwa sababu gani, kuna jamaa mmoja tu pale TANESCO baada ya mkataba wa Symbion wakati 2011 na 2013 ulipoisha, yeye mwaka 2015 alisaini mkataba lakini 2016, Tarehe 24, Mei Serikali ikasitisha mkataba. 2017 wenzetu wakaenda Mahakama za Kimataifa, 2019 wakaendelea kwenda Mahakama za Kimataifa 2021 hatimaye Serikali mkakubaliana na TANESCO mkaingia mkataba na symbion kuilipa Bilioni 325. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu tu kuna watu wamefanya maamuzi, ya kuingia mkataba whether ilikuwa ni kwa dili ama siyo kwa dili lakini Serikali hiyohiyo na baada ya miezi kadhaa ikasitisha mkataba, halafu Serikali hiyohiyo inakuja inaingia makubaliano na symbion kulipa kodi za wananchi Bilioni 355. Sasa unajua kuna wakati unakaa unafikiri hivi hizi hela za Watanzania, hizi pesa za walipa kodi hizi hivi tuna uchungu nazo kweli kama tunavyosema?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali nnamshukuru Mwanasheria Mkuu yuko hapa, majuzi rafiki yangu Mheshimiwa Reuben wa Muheza alisema hivi kwa nini Mawakili wetu Wanasheria wetu hawapelekwi kwenye mafunzo ya kuwa wabobezi kwenye mikataba? Yaani kwenye mambo muhimu pesa hatutengi leo tunaambiwa nchi yetu eti tukamlipe symbion Bilioni 355 kwa kuvunja mkataba wa kizembe! Wanasheria wa nchi wako wapi Mwanasheria Mkuu tunaomba majibu haya! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo watu wanalia umeme hapa hivi tujiulize tu….

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Ndiyo Mheshimiwa wa Mbunge wa Tabora, taarifa.

T A A R I F A

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa taarifa Mheshimiwa Halima Mdee anapouliza wanasheria wa nchi wako wapi sijui, yeye mwenyewe ni Mwanasheria ameuvua lini uanasheria? (Kicheko/Makofi).

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mdee unapokea taarifa?

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sijatumika tu rafiki yangu, tatizo mkiona tunafunguka mnafikiria sisi ni enemies hapana sisi ni Watanzania tunapigania Tanzania hii, kwa hiyo, Wanasheria ninaowazungumzia hapa na waliopewa dhamana na nchi hii kwa kusomeshwa kwa kodi za nchi hii, kusimamia mikataba ya nchi hii, kwamba leo tunaenda kuilipa Symbion Bilioni 355. Sasa naamini Mheshimiwa January utakuja kunijibu vizuri kwanza huo mpunga huko wapi maana hapa siuoni kwenye bajeti yako siuoni na kwenye bajeti iliyopita hatukuona.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Halima Mdee kwa hiyo taarifa umeipokea au umeikataa?

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeikataa taarifa kwa mantiki niliyoieleza hilo la kwanza. Pili, ningependa kujua vilevile hawa watu wote walioshiriki katika mnyororo hadi Taifa limefika hapa, wanawajibika kiasi gani, wameshachukuliwa hatua, kama hawajachukuliwa hatua, mna mpango gani wa kuchukuwa hatua? Haiwezekani watu ‘wanavijikesi’ vya hovyo hovyo huko wako ndani, wakati kuna watu wenye kesi makubwa ya uhujumu uchumi tumekaa nao tu haiwezekani! Huwezi kutofautisha hili jambo uhujumu uchumi, kwa hiyo naomba nipata majibu sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika muhtadha huohuo Bwawa la Julius Nyerere, katika mradi ambao Serikali imewekeza asilimia 100 kwa pesa za ndani ni mradi huu kutokana na maandiko yenu, 6.5 trilion. Mradi huu ulitakiwa ukamilike tarehe 14 Juni, kwa mujibu wa mkataba wa awali. Leo tunaambiwa umefikia asilimia 57, tunajua kwenye mkataba kuna sura mbili, Mwanasheria Mkuu yuko hapa, kwamba upande mmoja ukiwa na uzembe upande mwingine lazima ufidiwe, ninaomba Waziri ukija kutujibu hapa utuambie hasara ambayo Tanzania imeipata kwa Mkandarasi huyu kutokumaliza Tarehe 14 Juni, tunalipwa kiwango gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya nimesoma taarifa ya Kamati, taarifa ya Kamati ya sasa na taarifa ya Kamati ya Mwezi wa Pili vinatofautiana. Mwezi wa Pili Kamati ya Nishati na Madini imeeleza sababu Tisa za msingi, hizo sababu Tisa ni uzembe wa Mkandarasi. Eti leo wanatuambia UVIKO wakati Mheshimiwa Naibu Waziri unakumbuka ulikuja Kamati ya Bajeti ukatuambia Mkandarasi anasema UVIKO, ninyi kama Serikali mmegundua tatizo siyo UVIKO ila Mkandarasi alikosea, alitakiwa ajenge matuta mawili, kajenga tuta moja wakati wa mafuriko mchezo mzima ukavurugika ninyi mlisema! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nataka leo haiwezekani kila siku sisi tunapigwa haiwezekani! Sasa leo tunampa mtu kazi tena tunamlipa vizuri, yaani kama kuna mtu analipwa kiroho safi ni huyu jamaa, yaani hana hata stress! Sasa nataka hivi, huyu mtu anayekula pesa zetu bila stress,s hajamalliza ujenzi kama mkataba unavyotaka, sababu zake alizozitoa ni za uwongo, sababu za Kamati ya Bunge zilikuja hapa zikabaini, Waziri ulikuja ukatuambia kabisa tena hamkutaka kuzikubali tena, tukakuambia subiri mwezi wa Sita si bado? Hasa mwezi wa Sita ndiyo huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Taifa lipate majibu kiroho safi, mimi sina bifu na ninyi, wote tunajenga nyumba moja kiroho safi. 6.5 Trillion ambazo tunampa huyu kwa heshima kubwa, nchi inapata nini kutokana na uzembe ili tujue kumbe bado tunashida mikataba, ili tujue Wanasheria wetu bado hatujajifunza kutokana na makosa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo sina mengi sana leo hayo mawili tu, naomba nipate majibu kwa nia njema na nisipojibiwa tutakamata Shilingi tu ili tuweze kujiachia zaidi. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Kulitangaza Jiji la Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi wa Mwaka 2018
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza na mimi naungana na hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani na niseme kwamba na kwenye hotuba yetu tumeandika, hakuna mtu anayepinga kuhamia Dodoma, hakuna mtu anayepinga Dodoma kuwa Jiji. Hoja zetu hapa ni utaratibu wa kisheria, hoja zetu hapa ni mipango ya Taifa kupangwa na itekelezwe kwa mujibu wa Katiba na kwa mujibu wa Mpango ya Miaka Mitano na mwaka mmoja mmoja, hizo ndiyo hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, isije ikajengwa propaganda hapa kwamba kuna mtu yeyote anapinga. Kwa sababu sasa hivi siasa zetu zimetoka kwenye hoja zimeenda kwenye vihoja yaani watu wakizungumza hoja inafanyiwa spin na kupotosha watu bila sababu za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru Mbunge wa Mtwara amezungumza huu Muswada hapa una mambo mawili na yamechomekewa strategically na nitarudia kusoma. Kwenye preamble hapa kuna maneno yafuatayo:-

“WHEREAS on the 26 April, 2018 His excellence JOHN POMBE MAGUFULI, the President of the United Republic of
Tanzania officially declared Dodoma to become the City to be developed and administered by the Dodoma City Council”.

Mheshimiwa Spika, hiyo ya kwanza, ya pili, inasema, nanukuu:-

“AND WHEREAS consequent to the declaration of the City of Dodoma by His Excellence JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, the President of the United Republic of Tanzania, the Government has determined to establish and develop the City of Dodoma as the Capital City of the United Republic of Tanzania”.

Mheshimiwa Spika, hii sheria inazungumzia vitu viwili, inazungumzia Makao Makuu na inazungumzia Jiji. Hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani, sijui mlikuwa mmejipanga, naona mkawa mna m-crush pale kumchanganya, hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani imesema hivi, hii document kuna Jiji hapa na kuna Makao Makuu. Imesema Rais wakati anatangaza Jiji ambalo mmelichomekea hapa kwenye sheria hakuzingatia matakwa ya kisheria, that was our basic question. Sasa nyie badala mjadili hoja mmeingia kwenye kichororo cha Makao Makuu, mmekuja mmehalalisha Bunge kunyang’anywa mamlaka yake ya kisheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, it’s so unfortunate, mimi ni Mbunge wa Awamu ya Tatu, Viti Maalum, Jimbo, Jimbo; sijawahi kuona I am sorry to say that, Bunge ambalo linapelekwa pelekwa na Serikali kama Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina Sheria ya Mipango Miji ya 2007, Sheria Na.8 inasema vigezo vya Jiji, minimum population 500,000, self sustenance at least 95 per cent of annual budget halafu kuna kipengele cha mwisho kinasema the power to bestow a municipality the status of a City shall be vested in the National Assembly, and this is the National Assembly. Sasa mtuambie ni lini Bunge hili lililetewa lililetewa Muswada ukainyanyua Dodoma. Ni lini Bunge hili lilifanya kazi yake kwa mujibu wa Sheria?

Mheshimiwa Spika, nina taaarifa hapa; nyaraka ya Serikali ambao walitoa taarifa kwa umma baada ya hoja kutolewa kwamba jamani, tunakubali kwamba Dodoma ina haki ya kila kitu lakini taratibu zimefuatwa? Wakajibu hapa ukurasa wa pili, kwamba; baada ya maombi haya kuwasilishwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mheshimiwa Rais ambaye pia ndiye Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa alitafakari na kujiridhisha kwamba Manispaa ya Dodoma imekidhi vigezo vya kupandishwa hadhi kuwa Jiji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Rais hana Mamlaka automatic ya ku-declare kwa sababu declaration ni kitu kingine, kuipa legal status ni kitu kingine. Rais anaweza akasema, lakini Mamlaka ya Bunge sasa kuipa uhalali lazima itekelezwe. Sasa nilitarajia kwa nia njema kabisa angekuja Waziri hapa na Muswada wake, angesema jamani, tuna- declare Makao Makuu, ndani ya Sheria hii tumechomekea Jiji kuna vigezo moja, mbili, tatu, nne, tano vimefikiwa, hakuna! We just do politics. Hapa kwenye maandishi hapa ya Serikali yanaeleza wazi kabisa kwamba ni kweli Rais amesema lakini tutaleta Bungeni, waliileta lini? Haya ndiyo majibu tunayotaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni wajibu wako wewe kulinda heshima na hadhi ya Bunge lako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni kweli hili jambo la Makao Mkuu siyo jipya, amezungumza hapa Mheshimiwa Msigwa mipango. Wakati tarehe Mosi Oktoba, 1973 baada ya referendum kufanyika nchi nzima na kuamua kwamba Makao Makuu ya Serikali yawe Dodoma kulikuwa kuna bajeti kwamba itatugharimu paundi milioni 186 na itachukua miaka 10, mwaka 1973 wakati huo shilingi moja dola ni 0.5

Mheshimiwa Spika, nasema hivi, nchi haiwezi kuendeshwa bila mipango. Mwaka 1973 kulikuwa kuna mpango wa miaka 10, kuna fedha ambayo ilikuwa iko allocated, sasa tunataka watuambie wakati wanajibu hapa; hii kuhamisha Dar es Salaam kuja Dodoma namsikia eti Waziri anasema kuna Ofisi, kuna Ofisi wakati wanaweka Ofisi zenu kule UDOM!! Sasa hivi watoto wetu watapata mimba, watapata maradhi kwa sababu kuna mchanganyiko wa watu wazima na watoto, hizo ndizo ofisi hizo? We have to be serious kuweka mipango ya nchi.

Kwa hiyo, maana yake unavyosema hivyo unahalalaisha sisi watu wazima kutembea na watoto, siyo? (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ninachosema ni hivi, naomba ninukuliwe vizuri, kwamba mipango ya nchi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 3) wa Mwaka 2018
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwanza, napongeza taarifa ya Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria kwa kitendo chake cha kuzuia Sehemu ya Tano ambayo ilikuwa inafanyia marekebisho The Magistrate Court Act na kuruhusu Jaji Mkuu kwa mapendekezo yake ama kwa maslahi ya umma kwa kadri atakavyoona inafaa kuanzisha Mahakama Maalum na Mahakama za kuhamishika. Ni imani yangu kwamba hii Sehemu ya Tano iliyoondolewa ambayo kwa bahati mbaya sana ilikuwa inampelekea Jaji Mkuu kuunda Mahakama kupitia regulations mbalimbali na kusema kabisa hizi Mahakama zitamsimamia nani kwa utaratibu gani?

Mheshimiwa Spika, kama Bunge litaruhusu kwa njia ya pembeni, kwa sababu tumeambiwa hapa leo asubuhi kwamba tayari magari husika yameshanunuliwa, zimetumika shilingi bilioni 48, kila gari shilingi milioni 350 na fedha hizi ni mkopo kutoka Benki ya Dunia. Swali langu kwa Mheshimiwa Waziri, Kamati ya Bunge imesema hii Sehemu ya Tano isipitishwe, hivyo vifaa vilivyonunuliwa vinaenda kufanya kazi gani? Isije ikawa tumepigwa changa la macho kama Bunge, tunaambiwa hili suala tumelitoa, lakini linaenda kuingilia kwa upande wa nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa Mheshimiwa Waziri atuambie kwa sababu Mwenyekiti wa Kamati amesema hapa kwamba magari yameshanunuliwa. Mjumbe wa Kamati amesema hapa kwamba magari yameshanunuliwa. Mkopo wa Benki ya Dunia siyo bure, ni mkopo ambao Watanzania tunaenda kuulipa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wote tunajua tokea Awamu ya Tano imeingia madarakani, kiwango cha kukopa cha nchi hii kimeongezeka katika kiwango ambacho haijawahi kutokea katika historia ya nchi hii. Kwa hiyo, haiingii akilini, wananchi wanaonyeshwa vitu, hivyo vitu vinaonekana kama vina tija tukijiaminisha kwamba tunatumia fedha zetu za ndani, kumbe watoto, wajukuu na vitukuu watalipa mzigo mkubwa sana. Sasa tunataka Mheshimiwa Waziri atuambie kwa cost benefit analysis, hii shilingi milioni 350 kwa gari ambalo life span yake ni miaka mitano tu au miwili, kwa sababu ni magari tu yanayo-move, huu mzigo wa matumizi mabovu ya fedha za umma ataubeba nani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikija kwenye hoja nyingine kuhusiana na hii Sheria ya Takwimu. Kwa mtu yeyote mwenye akili timamu anajua mabadiliko haya ya kuongeza kifungu cha 24A na kufanya mabadiliko ya kifungu cha 37, malengo yake ni udhibiti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanasema kwamba utafiti hauwezi kutolewa kwa umma bila approval ya Bureau. Wakati TWAWEZA walivyokuwa wakimsifia Mheshimiwa Dkt. Magufuli, kwamba anakubalika kwa asilimia 90, anakubalika kwa asilimia 77, hakuna mtu aliyeona kwamba ni shida hizi tafiti. Mara moja tu baada ya TWAWEZA kusema Rais ameporomoka kutoka asilimia 90 huko mpaka asilimia 50 imekuwa nogwa. Hivi imefika nchi hii sasa hivi watu inakuwa kutoa maoni kwamba mtazamo wa nchi, Watanzania mmoja, mmoja wanaona ni hivi, imekuwa ni nogwa! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili Bunge ni kwa bahati mbaya sana na sisi tumezubaa tunaingiliwa. Juzi Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti amebadilishwa. Yeye atasema kwamba ameamua.

Mheshimiwa Spika, Bunge ndiyo chombo cha kusimamia Serikali. Hii sheria imeletwa, narudia, lengo ni kudhibiti ili ukiletwa utafiti wowote ambao unaenda kinyume na maslahi mapana ya Serikali ya Awamu ya Tano, utafiti hautatoka kwa umma. Ni kwa bahati mbaya sana wameleta hapa haya mabadiliko hawajasema kama hii Bureau isikubali huu uchapishwaji utolewe, remedy ni nini kwa huyu mtu au kwa hiki chombo kilichofanya utafiti? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi narudia, Bunge lako limedhibitiwa, linaingiliwa. Sasa hivi Katiba ya nchi inavunjwa, vyama vya siasa vimedhibitiwa, sasa hivi Mahakama zimedhibitiwa.

Mheshimiwa Spika, ngoja niseme hivi, tumeshuhudia juzi Mwenyekiti wa Kamati ya bajeti, Mheshimiwa Hawa Ghasia, yeye najua atasema kwamba amejiuzulu kwa matamanio yake mwenyewe, lakini sisi wenye akili timamu tunajua ni kwa sababu alivyosimama na korosho. Tunajua akaletwa Mjumbe mwingine kutoka kwenye nje ya Kamati, akawekwa pale.

Mheshimiwa Spika, hoja yangu ni ndogo tu, kwamba sisi kama Bunge tuna jukumu kubwa la kuisimamia Serikali. Tuna jukumu kubwa la kuhakikisha kwamba, sheria zinazoletwa kwenye Bunge hili zina lengo siyo la kulinda mtu ambaye yuko kwenye madaraka, siyo kusaidia chama ambacho kiko kwenye madaraka, ila ni sheria ambazo zitaisaidia nchi. Hiyo ndio hoja yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama Bunge tutashindwa kusaidia nchi, hii nchi ikivurugika, hakuna atakayepona, ndiyo hoja yangu hapa. Hoja yangu hapa ni kwamba huu Muswada wa Takwimu tunaambiwa kwamba, kwa mfano, mtu yeyote ambaye atachapisha bila ruhusa atakuwa amefanya kosa na adhabu yake siyo pungufu ya shilingi milioni kumi au kifungo kisichopungua miaka mitatu au vyote viwili.

Hebu firikia tuna taasisi hii, ina vigezo vyake imeenda kuomba kibali, imepata kibali imefanya utafiti, imeenda kusema utafiti huu, mwenye mamlaka amekataa kutoa ruhusa… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi wa Mwaka 2018
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kwanza jana wakati naandaa hii hotuba nilimsikia Profesa Kabudi akifanya upotoshaji wa kiwango kikubwa na ningependa niweke mambo clear kwa ajili ya Hansard.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana kuna wanasheria wengi tulichangia humu ikaonekana kwamba wengine tukaambiwa kwamba marks zetu itabidi zifukuliwe lakini mimi niseme hivi, Kabudi alinifundisha Family Law (Sheria ya Familia), Constitutional Law nilifundishwa na Profesa Mwinuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana kulikuwa kuna upotoshwaji ionekane kwamba Taifa hili kuna total separation of power. Tunafahamu kuna mihimili Mitatu. Kuna mhimili wa Bunge unaotunga sheria, kuna mhimili wa Executive unao- enforce sheria, kuna mhimili wa Judiciary unao-interprete sheria. Kwa mfumo wetu Tanzania hii mihimili inaingiliana na hii mihimili inachekiana kuna (checks and balance) ndiyo maana leo unakuta tuna Mawaziri ni sehemu ya Bunge, ndiyo maana leo unakuta tuna Rais anachangua Jaji Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri kusimama na kusema kwenye Serikali kuna Mawaziri watatu tu na kwamba eti fedha ambazo tunazitoa kwa mhimili wa Judiciary kama Bunge hatuwezi kuhoji wakati CAG anakagua kila hesabu na Bunge tunachambua kila kinachoandikwa na CAG na ku-recommend. Kwa hiyo, namshauri Profesa Kabudi akasome vizuri Katiba, ajue separation of powers zinafanyikaje katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija hoja ya pili sasa kwenye muswada, nitaanzia pale ambapo Mheshimiwa Msigwa ameishia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 11 kuhusiana na utatuzi wa migogoro. Tunasema kwa nia njema kabisa, na tunasema kwa nia njema. As long as sheria yetu ya PPP inakaribisha na inatambua kutakuweko na wawekezaji wa ndani na kutakuwepo wawekezaji wa nje, lazima hii sheria tuifanyie maboresho ili tuweze ku-accommodate hayo makundi mawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna anayepinga kwamba option mojawapo ya kutatua hiyo migogoro iwe kutumia mifumo yetu ya arbitration ya ndani, hakuna anayepinga. Sambamba na hilo lazima kuwe na option kuwe na option ya hizi sheria zingine ambazo Mheshimiwa Chenge ulikuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Tanzania kama nchi hatuishi in isolation, kama nchi tumesaini mikataba ya kimataifa, kama nchi tumesaini multilateral na bilateral agreements na baadhi ya nchi kuhusiana na masuala ya wawekezaji na nitatoa baadhi ya mifano michache tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza Tanzania ni wanachama wa International Centre for Settlement of Investment Dispute, chombo hiki kinakuwa funded na UN ama kwa lugha nyingine tunaita ICSID. Katika mfumo wetu wa arbitration tuna maeneo ambayo tuna arbitration na multilateral agreement katika investment protection kati ya nchi na nchi. Sisi ni wanachama wa MIGA amezungumza Mheshimiwa Msigwa hapa. Sisi ni signatory to the New York Convention on the Recognition and Enforcement of Arbitration Awards. Kwa hiyo, katika mazingira kama haya ambayo Taifa letu linataka kukaribisha wawekezaji serious, kwa sababu hapa hatuzungumzii wawekezaji uchwara. Tunazungumzia wawekezaji serious ambaye anataka akija anakuta kuna neutral ground kwamba yeye atakuwa salama, lakini vilevile na mbia atakuwa salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Mahakama yetu kwa mfano, Majaji wanateuliwa na Rais, Rais wetu ndiyo Magufuli huyu! Chief Justice anateuliwa na Rais, Rais wetu ndiyo Magufuli, Principal Judge anateuliwa na Rais, Rais wetu ndiyo Magufuli, halafu hawa watu ndiyo wanatakiwa wawe wanashusha maelekezo ama kutengeneza regulations mbalimbali za mifumo uendeshaji za mahakama zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nia njema tunaipenda nchi ndiyo, lakini lazima tuwe realistic hatuishi kwenye kisiwa. Mwanasheria Mkuu wa Serikali of all people unatakiwa umsaidie Rais, Mheshimiwa Kabudi mwalimu wangu wa Family Law alitakiwa amsaidie Rais, sasa bahati mbaya na yeye anakuwa sehemu ya upotoshaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kabudi, Waziri wa Katiba na Sheria sasa hivi, ni mwalimu wangu mzuri kweli wa Family Law, hawa wanamsaidia kumshauri Rais kwa kiwango gani, kama tumezidiwa tuna watalaam wengi wa sheria ndani ya Serikali tusaidie tujenge nchi hii. Ninachotaka kusema hatuishi na in isolation. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu ikaeleweka vilevile Mheshimiwa Mpango najua una uchungu sana na nchi hii na una uzalendo na ile uliyoipiga Dar es Salaam nilikukubali, ulivyomshughulikia dogo kule Dar es Salaam safi. Ni muhimu ukajua kwamba mgogoro wa TANESCO na Standard Charted hauna uhusiano wowote na ICSID wala MIGA. Mgogoro wa Bombardier ilitaka kushikiliwa juzi kwa mkataba ambao Rais alivyokuwa Waziri wa Miundombinu aliuvunja kienyeji kampuni ikaenda huko ikafungua mashitaka ikashinda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro wa ACACIA mnabisha hapa, sisi tupo ACACIA anaenda kule na atatuchapa, mtatuambia sisi siyo wazalendo kumbe ninyi ndiyo ambao siyo wazalendo mmeingiza nchi kwenye shida na hamtaki kukubali ukweli. Kwa dhamira njema sawa, mfumo wa arbitration ndani ya nchi yetu upo tuuweke, lakini tuweke mifumo mingine tupate wawekezaji mahiri watakaoisaidia nchi, huu uzuri wote ama baadhi ya uzuri robo tatu ama nusu ya hii sheria unavurugwa na hiki kipengele, hiki kipengele ndiyo kinafanya huu muswada unakuwa ni wa hovyo kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nilitaka Waziri wa Fedha anisaidie kwenye madhumuni tunaambiwa kwamba muswada huu unapendekeza kwa ajili ya kuwezesha Waziri wa Fedha kusimamia utekelezaji wa sera, sheria na kanuni za ubia. Mapendekezo ya marekebisho yanakusudia kurekebisha mfumo wa kitaasisi na kisheria katika usimamizi wa miradi ya ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi. Ukienda kwenye madhumuni Waziri unatajwa, ukija huko kwenye vifungu vingine vya sheria haupo. Sasa huyu Waziri ambaye kwa tafsiri tunaambiwa anahusika na masuala ya PPP hii Wizara ambayo kwa tafsiri tunaambiwa anahusika na masuala ya PPP mbona haipo kwenye sheria, lakini kwenye madhumuni ipo, kitu gani kinafichwa? Isije baadae tukaletewa sheria tunaambiwa Waziri wenye dhamana ya TAMISEMI bwana mkubwa mwenyewe namba moja, ndiyo atakuwa ana dhamana ya PPP. (Makofi/Kicheko)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Siasa wa Mwaka 2018
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwanza niweke sahihi upotoshwaji ambao umefanya na mdogo wangu Mheshimiwa Mhagama pale. Kambi ya Upinzani katika hotuba yetu, hakuna mahali popote ambapo tumepinga ukaguzi wa Hesabu za Serikali asifanyie ukaguzi fedha za Umma. Ni muhimu Mheshimiwa Mhagama akajua kuna shida ya kukaririshwa vitu vya kusema.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni muhimu Mheshimiwa Mhagama akajua; na rekodi za Bunge hili za mwaka 2009, ni Kambi ya Upinzani kupitia Mheshimiwa Zitto Zuberi Kabwe tulileta mabadiliko hapa ya Sheria ya Vyama vya Siasa kutaka Mkaguzi akague ruzuku. Tena CCM walikuwa wanapinga. Usilete upotoshaji hapa, eti tunapinga hii sheria ama Muswada wa Vyama vya Siasa kwa sababu tunaogopa kukaguliwa. Hatujawai kuogopa kukaguliwa jana, juzi, leo na kesho. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuache kudanganya Watanzania kwamba tuna uchungu na tuna mapenzi na kinachoitwa fedha za Umma. CCM mmepewa dhamana nchi, hii lakini leo Hazina (hati chafu), Serikali ya Jamhuri ya Muungano (hati chafu) na Jeshi (hati chafu). (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunasubiri taarifa ya ukaguzi maalum kuhusiana na 1.5 trillion, utaona vituko vya kiwango gani Hazina haitulii, inachezewa na Chama cha Mapinduzi. Tusitumie propaganda zisizokuwa na kichwa wala miguu kuweza kuhalalisha masuala ya msingi yenye maslahi ya Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mtu amezungumza hapa kwamba ni mambo madogo. Tunajadili mambo madogo madogo. Hivi suala la Katiba ni jambo dogo? Suala la kuvunja Katiba ya Nchi, ni jambo dogo? Unatambua kuna kazi imefanywa na Kamati vizuri, wala hatupingi. Tunatambua kuna kazi zimefanywa na Serikali ndani na nje vizuri. Tunachotaka turekebishe Muswada uwe bora, tusije tukajidanganya hata siku moja kwamba hii Miswada mnaitungia CUF, CHADEMA, ama ACT ama NCCR-Mageuzi. Hamjui lini mtakuwa wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Katiba, ibara ya 8(c) kuna uvunjaji wa Katiba, naungana na hoja ya Mheshimiwa Msemaji wa Kambi. Kifungu cha 8(c) kinasema, vyama vinatakiwa viweke register mpaka ngazi ya Uongozi, sawa. Tunasema, Msajili anaweza akataka register, anasema, anafikiria chama chenye wanachama milioni sita, unataka kiwe kina register ya kila mwanachama, wanachama ambao wanaingia leo au wanaoingia kesho. Kwa maana hiyo wanaingia na kutoka. Hicho chama kitakuwa hakina kazi nyingine zaidi ya kuweka kumbukumbu za wanachama milioni sita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kifungu cha 8(c)(3) uwezekano siyo shida, kwa sababu vyama makini vina viongozi mpaka kule chini. Mnasema eti Msajili wa chama kinachoweza kushindwa ku-comply 8(c)(3) hakijarekebishwa mpaka sasa, labda mniambie Serikali imerekebisha usiku, maana tumepata Amendments saa 4.00. Yaani tumepata Amendment mpya saa 4.00 asubuhi na saa 4.00 hiyo hiyo mnataka tuchangie na kujumuisha mabadiliko ya Serikali. Wakati wote tumepeleka Amendments saa 2.30 mmekazana kutaka kuona huyu bundi, this is nonsense. Kifungu hiki kinasema eti chama kikishindwa kupeleka nakala ya wanachama wake Msajili akifute. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wewe ni Mwanasheria, Mwalimu wangu uliyenisimamia Thesis. Ibara ya 20(2) ya Katiba (a) - (e) na Ibara 20 (3) inasema mazingira ambayo Msajili anaweza akakinyima chama usajili ama kukifutia, suala la register ya mwanachama siyo sehemu ya Katiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninatambua Kamati mlifika Kifungu cha 5B mlifika Kifungu cha 8, tunaomba Serikali kwa mantiki hiyo hiyo hiki Kifungu cha 8C(3) kifutwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ibara ya 13 ya Katiba kuna jamaa hapa anasema mambo madogo madogo; usikubali kukaririshwa someni Muswada. Ibara inasema, “ni marufuku kwa sheria yoyote iliyotungwa na mamlaka yoyote na Jamhuri ya Muungano kuweka sharti ambalo ni la ubaguzi. Kasema hapa Mheshimiwa Bulaya, mabadiliko ya Serikali yanasema kwamba “a person is citizen of the United Republic by birth and birth parents of that person are citizens of United Republic.” Katiba inatuambia uraia wa kuzaliwa tu. Hizi story za wazazi Katiba haitambui, uvunjwaji wa pili wa Katiba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uvunjwaji wa Katiba siyo jambo dogo. Tunataka Mheshimiwa Waziri Jenista akija afanye marekebisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la vikosi kwa ulinzi wa chama, hivi nani asiyejua leo, kama ni wakweli wanajiamini, kwamba Jeshi la Polisi la nchi hii linafanya kazi ya Chama cha Mapinduzi kwenye uchaguzi. Nani asiyejua? Safari hii kwenye nchi hii tumefika hatua, mimi nimeshuhudia askari wanaiba kura wanaiba mabox ya kura.

Mheshimiwa Naibu Spika, hiki kifungu kisingekuwa na shida kama majeshi yetu yangesimama katikati. Hiki kifungu kina shida. Kama Kiongozi wa Kambi ya Upinzani, Mnadhimu anapigwa risasi Dodoma Makao Makuu kwenye ulinzi, Serikali imeshindwa kulinda.

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Kuhusu Utaratibu.

KUHUSU UTARATIBU

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, sawa na ninashukuru kwa kumwelewesha. Nadhani akienda kusoma vizuri Katiba atanielewa nilikuwa namaanisha nini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kifungu kama ambavyo Serikali imeleta mabadiliko imefanya ubaguzi kwa sababu Katiba yetu inatoa ruhusa ya kugombea nafasi yoyote kushiriki shughuli yoyote ukiwa raia wa Tanzania wa kuzaliwa, haizungumzii biashara ya wazazi. Sasa ubaguzi wa kipengele hiki kinagusa wazazi kinyume na Katiba. Kwa hiyo, kohoa kidogo kidogo. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu nilikuwa namalizia kwamba ni muhimu Mheshimiwa Waziri akaeleza hiki kifungu kinagaubaga kwamba je, vyama vya siasa haviruhusiwi kuwa na ulinzi binafsi? Tafsiri ya walinzi ni nini? Kwa sababu tuna Waziri wa Jeshi hapa, tuna Waziri wa Mambo ya Ndani hapa, wanajua taratibu za kumiliki silaha nchi hii zikoje. Siyo rahisi chama cha siasa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2020 (Toleo la Kiingereza)
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Naunga mkono alichokizungumza Mheshimiwa Jerry Silaa kuhusiana na transfer price. Sitataka kukirudia kwa sababu amekizungumza vizuri na kwa kina. Natumaini Waziri atakuja na majibu ya kina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kwa sheria hii maana yake ni kwamba itakuwa ni marufuku sasa hivi kwa Bodi ya Mikopo kuweka tozo mbalimbali zinazotokana na Mikopo ya Elimu ya Juu na kwa kweli ni ushindi kwa wote waliopigania kero ya asilimia sita ya retention fee na vile vile asilimia 10 ya penalty ambayo ilikuwa inatozwa kwa watu ambao wamevuka miwili ile ya muda ambao walikuwa wamepewa wa kuweza kulipa deni. Kwa hiyo nitambue kazi ambayo imefanya na vijana huko nje lakini hapa nitambue kelele nzuri sana zilizopigwa na Mheshimiwa Matiko kuhusiana na vijana hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nitazungumza hoja ambayo imekuwa raise na Kamati, lakini ambayo vile vile imezungumzwa na Mheshimiwa Njeza ambaye ni Mjumbe wa Kamati, kuhusiana na ushuru wa bidhaa; yale marekebisho ya Sheria ya Ushuru wa Bidhaa ambayo yanahusu vinywaji vikali. Hii inawahusu wote ambao wanatumia whisky, wanapiga ma-Gin, wanapiga ma-Vodka. Malengo ya kuweka ushuru ambao haukuwa mkali sana kwa vinywaji ambavyo vinazalishwa nyumbani ililenga ku-encourage watu wetu watoke kwenye vinywaji ambavyo havijachujwa. Vinywaji ambavyo havijapita kwenye mnyororo wa kuhakikiwa ili wasiweze kupata maradhi na vitu vingine. Kwa lugha za gongo na mapombe mengine yanayofanania hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nazungumza hivi kwa sababu tumepata nafasi ya kukutana na wadau ambao ndio walipa kodi wa nchi hii na wameonesha concern zao kuhusia na hili. Kubwa zaidi hili ni jambo la kisheria; sababu Sheria ya Ushuru wa Bidhaa imezungumza masuala mawili makubwa; kwamba bei ama ushuru utaongezwa kutokana na mfumuko wa bei tarajiwa ama shughuli zingine za kiuchumi. Sasa sisi tunatumia taarifa zetu kutokana na taarifa za Serikali ambazo inatupa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa mujibu wa taarifa ya Serikali ambayo imesomwa na Waziri wa Fedha, mfumuko wa bei kwa kipindi kilichopita ilikuwa asilimia tatu na mfumuko wa bei tarajiwa ni asilimia tano kwa mwaka ujao wa fedha. Sasa leo wanatuletea ushuru wameongeza kwa level ya asilimia 30 na wamepunguza sasa hivi baada ya Kamati kwenda asilimia 20. Sasa unajiuliza kwa mwaka ujao wa fedha, unaoanza kesho kutwa; hivi mfumuko wa bei tarajiwa ni asilimia tano ambayo wameisema ama ni asilimia 20 ambayo wametumia kutoza ushuru wa bidhaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu sasa Serikali ikalijibu hili kwa sababu wazalishaji wa bidhaa hii na taarifa na tafiti zinaonesha kwamba kwanza kuna utitiri mkubwa wa bidhaa haramu zinaitwa, bidhaa ambazo hazikidhi vigezo. Vile vile tunaambiwa asilimia 51 ya Watanzania ama ya bidhaa za pombe kali mitaani; kuna asilimia 51 za bidhaa za pombe kali haramu ambazo TRA wameshindwa kuzi-track, hivyo basi hazilipi kodi. Sasa kutokana na kutengeneza mazingira magumu ya kikodi, tutapelekea sasa, Watanzania watatoka kwenye bidhaa ambazo zipo kwenye mfumo rasmi watakwenda kwenye bidhaa ambazo haziko kwenye mfumo rasmi; wao wataathirika lakini zaidi Serikali itakosa mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ukiangalia Serikali yenyewe inatuambia uchumi wetu kwa kipindi kilichopita tulitarajia ungekua kwa asilimia saba, lakini ume-drop kwa asilimia tano. Tunaambiwa pato la Taifa ambalo ndio mkusanyiko wa shughuli mbalimbali za kiuchumi za Taifa, tulitarajia lingekua kwa asilimia saba, limekua kwa asilimia 4.8. Sasa shughuli za kiuchumi zime-drop, sasa inakuwaje leo tunatunga sheria ambayo inakwenda kinyume na sheria yenyewe. Mosi, nimesema mfumuko wa bei uko chini, lakini Wizara wame-estimate very high. Pili, shughuli za kiuchumi zime-drop kwa sababu pato la Taifa lime-drop drastically sasa hivi vitu mbona havi-relate.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema mosi nilizungumze hili, kwa sababu wadau wamesema Serikali itakosa mapato.

Mfano tu mmoja wa mdau mmoja wa Mega ambaye anazilisha K-Vant na najua huku wapenzi wa K-Vant mko wengi kweli kweli, amesema kutokana na tozo hii mpya maana yake ni kwamba wao wenyewe kikodi watapunguza bilioni 19, yaani kwa hiyo hiyo kampuni moja tu. Kutokana na introduction ya huu ushuru mpya maana yake Serikali itakosa bilioni 19. Kwa hiyo, natarajia vilevile Serikali ije itupe majibu mazuri na yenye tija ili tuweze kuangalia, lakini zaidi kama Kamati ilivyosema ni busara na Serikali inatakiwa itunge Sheria ama ileta mapendekezo mapya ya kodi kutokana na sheria siyo kinyume na sheria inavyosema. Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni suala la sekta ya huduma ya fedha. Kwa mujibu wa mapendekezo ni kwamba, kutakuwa kuna tozo kati ya Sh.10 mpaka Sh.10,000. Sasa nina taarifa ya mjumuiko wa wamiliki wa makampuni ya simu, wanaoitwa TAMNOs wametoa uchambuzi ufuatao, kwa transaction za chini kabisa na transaction za juu. Watanisahihisha na watatoa mwongozo sahihi ili Taifa liweze kusikia kwa namna gani wataathirika na hili jambo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamesema kwa sasa kwa mfano; mtu akituma Sh.10,000 kwa mtu mwingine anatozwa Sh.350, mtu akipokea Sh.10,000, anatozwa Sh.1,450, anapokea 8,550 kwa hali ilivyo sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, anasema kwa tozo mpya; Halima nikimtumia pesa mtu mwingine, kwa mfano Sh.10,000 nitatozwa 550, nikipokea ile fedha nitatozwa Sh.1,650 ambayo inajumlisha levy ya Sh.200 kutokana na huo mchanganuo walioutoa, nitapokea Sh.8,050. Kwa hiyo natumiwa Sh.10,000, napokea Sh.8,050. Sasa tulianzisha huduma za simu ili kuweza kusaidia watu ambao hawawezi kufikia mabenki waweze kupata fedha kwa gharama nafuu. Sasa kwa utaratibu huu nadhani inaleta tatizo kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia akasema kwa watu wanaotuma fedha nyingi kwa mfano, akimtumia A, akimtumia B Sh.3,000,000 kwa sasa anatozwa Sh.5,000; B akipokea anatozwa Sh.10,000; maana yake akipelekwa Sh.3,000,000 anapata katika hatua ya mwisho 2,990,000 kwa sasa. Baada ya levy pamoja na tozo zote, naenda kwa summary sasa, mtu katika Sh.3,000,000 anapata 2,980,000 yaani 20,000 yote hii ni kwa mujibu wa TAMNOs.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama hivi ni sahihi, nadhani kuna sehemu tunakosea, maana yake dhamira yote ambayo ilifanya Tanzania tukasifika kama watu ambao tumeweza ku-simplify huduma ya fedha, mwananchi wa kawaida kule akaweza akapata, inakuwa defeated na mabadiliko haya. Kwa hiyo, naomba Waziri na Serikali ikija ifanye uchambuzi wa kina ili tujue implication ya hii gharama kwa sababu sasa hivi mzigo ni mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, ambalo nitatoa dogo kama ushauri kuhusiana na kodi ya majengo. Kwa mabadiliko hayo, nusu dakika nimalizie. Kwa mabadiliko haya wamelazimisha mtu awe analipa kwa mwezi, kwa mabadiliko haya, yaani ama Shilingi elfu tano, tano, kama kwa mwaka ni Sh.60,000 ama shilingi elfu moja, moja kama kwa mwaka ni Sh.12,000. Nashauri, kama mtu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante muda wako umekwisha.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, basi iwe kama mtu anataka kulipa kwa pamoja waweke provision, kama anataka kulipa Sh.60,000 yote alipe yote, msilazimishe kulipa...

MWENYEKITI: Mengine andika kwa Waziri.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Kudhibiti Utakatishaji wa Fedha Haramu wa Mwaka 2022
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nami nikiwa kama Mjumbe wa Kamati, kiukweli nitambue utayari wa Waziri pamoja na Mwanasheria Mkuu wa Serikali na timu yake kukubali mapendekezo ya mabadiliko ambayo tulikuwa tumependekeza kwenye Kamati ili kufanya huu Muswada uwe bora zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia kwenye maeneo yafuatayo: Kwanza, ni muhimu sana kwa Waziri sasa ikawa ni kipindi muafaka kuleta sera, kwa sababu ni aibu sana pale ambapo tunatunga sheria, wakati tukijua kwa taratibu za nchi, lazima uanze kuwa na sera ambayo ndiyo inaleta misingi, kisha unakuja kutunga sheria wakati tayari umeandaa misingi na mifumo iliyo bora katika utekelezaji wa sheria husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna hoja kwamba hili jambo ni la dharura; ninakubali kwa ajili ya maslahi ya nchi tu. Kwa sababu ni aibu pale nchi inapokuwa chini ya uangalizi kwa kutokuwa na mifumo thabiti ya kudhibiti utakasishaji wa fedha haramu. Ni jambo la aibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile, kwa sisi ambao hii sheria ya kwanza kabisa ya utakasishaji wa fedha; na Mwanasheria Mkuu anajua; ya kwanza kabisa ilikuwa ni 2006 si ndiyo! Act Na. 12, 2006 ya kwanza kabisa; ya pili ni Act Na. 6, 2008; ya tatu tulikuwa tunafanya Amendment Na. 1, 2012; Na.1, 2013; Na. 14, 2015; Na.4 2016; na hii hapa Na. 2, 2022. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, katika mazingira ya kawaida, hili jambo siyo jipya, ni jambo ambalo kama nchi tulikuwa tunalifahamu. Sasa tunapokuja na kufanya mabadiliko, kwangu mimi ni tafsiri ya kawaida tu; imefanywa tathmini na mabosi huko, Wazungu wanaotufadhili chenji mbili tatu, wameona kwamba kuna ukakasi ambao hauendani na vigezo vya wanaotusaidia huko, kwa hiyo tunakuja faster faster kufanya mambo mazito. Kwa hiyo, naomba sana, kama tuko serious kama Taifa, kwenye hili jambo, nami wanajua kwenye Kamati tumeshirikiana vizuri tu, wala sina bifu, ni kuhakikisha kwamba tunakuja na sera. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona Mheshimiwa Jenista anahangaika pale. Mwache Mheshimiwa Dkt. Pindi atulie. Mheshimiwa Jenista, cheo kimeshaondoka hicho, mwache Mheshimiwa Dkt. Pindi. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni aibu pale nchi tunayojivunia kama Tanzania kuwa chini ya uangalizi. Tulikuwa na matatizo mwaka 2009, tukawa chini ya uangalizi mpaka 2014, tukaonekana tunapumuapumua kidogo baada ya kuwa chini ya uangalizi. Kutoka 2014 sasa tukaachiwa kidogo, tathmini ikafanywa 2015/2016, ripoti ikatoka 2019, lakini imechapishwa rasmi 2021. Tumeonekana tunafanyaje? Tunachechemea, tunataka kuwa chini ya uangalizi. There is something wrong somewhere. Something big and very very wrong iko sehemu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba kiroho safi kabisa, tulete sera ili baada ya kutimiza haja ya leo tusiwe tena chini ya uangalizi. Ni aibu kwa Taifa kama letu la Tanzania. Hilo ni la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, suala la ugaidi; na katika hili ni -appreciate sana mabadiliko ambayo mliyaleta baada ya Kamati kushauri, kwamba ulivyokuja ilikuwa kama suala la ugaidi ni kosa la kawaida, wakati ni jambo zito ambalo lina maumivu makubwa sana ya watu. Mpaka suala liwe la ugaidi, lazima liwe la kutisha sana; liwe na madhara makubwa sana, kwa kutenda ama kutokutenda, kwa kupanga ama vinginevyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika busara yako hiyo hiyo, nashauri sana, sheria yetu hii inaeleza tukio la ugaidi, makosa ya kigaidi viashiria vyake ni nini? Kwa busara hii, hii tukumbuke mashehe wetu wa Uamsho walikaa sana ndani kwa makosa ya ugaidi, ushahidi ukashindwa kupatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Mwenyekiti wa CHADEMA, Mheshimiwa Freeman Mbowe ana kesi. Sitaki kujadili mambo ya Mahakamani, lakini ninaamini busara yako, kutokana na vigezo hivi ambavyo sheria imeainisha, haya mambo myamalize kwa haki na kisheria. Kwa sababu ugaidi is not a joke, ugaidi siyo jambo la kitoto, ugaidi ni jambo ambalo linaonyesha viashiria vya wazi vya madhara makubwa kwa mwananchi mmoja mmoja, kwa jamii na kwa jamii ya Kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hizi tuzitunge na tuzitekeleze tukifahamu kwamba leo sheria hii itamkamata Halima, kesho sheria hii itamkamata Jenista. Tukifanya mambo haya, tutazirahisishia Mahakama zetu kazi ili zi-deal na kesi za maana na zenye tija. Huo ni mchango wangu wa pili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa tatu, tumepanua wigo wa watoa taarifa, wigo ambao umeingiza magari na vile vile wameingiza watu wa clearing and forwarding. Najua dhamira ni njema kwamba sawa hawa watu, kuna watu wengine anapiga fedha chafu huku, anaenda ananunua magari, anahalalisha hela. Ni jambo jema. Hata hivyo, kuna majukumu makubwa sana ya kisheria ambayo hao watoa taarifa wameongezewa, na Mwanasheria Mkuu wa Serikali unajua na Mheshimiwa Waziri unajua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilichokuwa ninaitaka Serikali, jukumu la msingi la kuhakikisha watoa taarifa wote; inawezekana wa zamani mlishafanya utaratibu wakawa wanajua wajibu wao vizuri, hao watoa taarifa wapya ambao ni wafanyabiashara tu wa kawaida, vijana wanapambana huko (clearing and forward agents), hao wengine dealers wa magari, mhakikishe mnatoa mafunzo mahususi kwa sababu sheria hii imetoa adhabu ya fedha na kifungo. Kwa hiyo, kama dhamira ni kusaidia kuweza kudhibiti fedha chafu, basi ushauri wangu kwenu wa bure tu ili kuepusha kutokuwa na kesi Mahakamani zisizokuwa na maana na kuwachosha Mawakili, Mahakimu na Majaji, waende Mahakamani watu wanaostahili, lakini siyo watu waende Mahakamani kwa nia ya kutokutekeleza wajibu wenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tu kwa kuendelea kutambua kiukweli kabisa, Mwanasheria Mkuu wa Serikali na timu yako, mimi ni mkongwe kwenye hili Bunge; na Mheshimiwa Waziri kwa sababu huu ndiyo Muswada wake kwa kusaidiana nawe, mmekuwa flexible sana, sana. Kinyume na hapo, yaani leo hapa pangekuwa na kitimtimu. Mmekuwa flexible, ninaamini sasa mtatekeleza sheria hizi kwa haki, bila upendeleo na bila kuonea watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)