Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SUBIRA K. MGALU aliuliza:- Je, kuna mpango gani wa kujenga nyumba za walimu Shule za Msingi katika Kata za Salale, Kiongoroni, Mbuchi na Maparoni Kibiti?

Supplementary Question 1

MHE. SUBIRA K. MGALU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika,pamoja na jibu zuri la Serikali lenye kuleta matumaini lakini kwa kuwa hii Tarafa ya Mbwera ipo visiwani na changamoto kubwa ya upungufu wa nyumba za walimu zaidi ya 35, hasa katika maeneo ya Twasalie, Kiongoroni, Mbuchi na Saninga. Je, Serikali inatupa matumaini gani kwa mwaka wa fedha wa 2024/2025?

Swali la pili kwa kuwa Tarafa hii ya Mbwera siku za nyuma huko ilijengewa sekondari moja tu kwa ajili ya Kata zote tano lakini kwa sasa Mheshimiwa Mbunge Twaha Mpembenwe na wananchi wa Tarafa hizi hasa Kata ya Mbuchi na Msala wamejenga sekondari imefikia ngazi ya lenta. Je, Serikali ina mpango gani wa kuchangia jitihada hizi za Mheshimiwa Mbunge na Madiwani na wananchi wa maeneo haya ili kukamilisha hizi sekondari? ahsante.

Name

Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Subira Khamis Mgalu Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la kwanza nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba upatikanaji wa bajeti ndiyo kigezo kikubwa kinachoweza kusaidia shule hizo kujengwa. Hivyo nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wananchi wa Kata hizo za pembezoni hatutowaacha isipokuwa Serikali yao inaendelea kutafuta fedha na itaendelea kuweka fedha ili kujenga shule hizo.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kwanza nataka nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa jinsi ambavyo anashirikiana na Mbunge wa Jimbo Mheshimiwa Mpembenwe kwa jinsi anavyofuatilia maendeleo ya wananchi wetu. Nataka nimhakikishie kwamba pamoja na kujengwa kwa shule ambapo kumekwama katika Kata hizo za Mbuchi na kule alikosema nataka nimhakikishie kwamba Serikali itaendelea kutenga bajeti katika mwaka ujao wa bajeti kama ilivyofanya katika mwaka huu kwa kutenga bilioni 55.75 ili kuendelea kusaidiana na wananchi kuweza kufikia malengo makubwa ya kuwapelekea elimu wananchi wetu.