Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Priscus Jacob Tarimo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Mjini

Primary Question

MHE. PRISCUS J. TARIMO aliuliza:- Je, Serikali imejipangaje kusimamia ubora wa nguo na viatu vya mtumba vinavyotoka nje ya nchi ambavyo havina ubora na bei ni kubwa?

Supplementary Question 1

MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini kwanza niseme tu wamejibu upande mmoja, upande wa quality, yaani ubora lakini upande wa bei hawajagusia. Ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu sisi ambao tuko field tumeona kabisa utaratibu huu wa kukagua haufanyi kazi, kwa maana marobota yanayokuja sasa nchini yamejaa nguo chakavu ambazo haziwezi hata kuuzika; je, Serikali haioni namna ya kutafuta utaratibu mwingine wa kuhakikisha wanafanya ukaguzi mzuri? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili. Kwa kuwa bei imeonekana bado ni kubwa kutokana na kuwepo kwa madalali, lakini pia ubora unakuwa compromised kutokana na zile nchi nazo zimepigwa na uchumi: Serikali haina mpango mwingine wa kudhibiti biashara hii ili tusiwe dampo? (Makofi)

Name

Sagini Jumanne Abdallah

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Butiama

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ufanisi wa ukaguzi wa mawakala tuliowapa kazi hiyo kwa mujibu wa maelezo ya Mheshimiwa Mbunge ambaye naamini anawakilisha wafanyabiashara wanaofanya biashara hii ni kwamba ziko chini ya kiwango. Wizara ya Viwanda na Biashara kupitia TBS itafanya uthamini juu ya utendaji wa mawakala waliopewa na kama itathibitika kwamba wanaleta mavazi ambayo yako chini ya kiwango kwa maana ya ubora, lakini na uchakavu hatua zitachukuliwa ikiwa ni pamoja na kuwafutia hizo leseni na kuwatafuta watu wengine wanaoweza kufanya kazi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu bei kubwa ya bidhaa inayotoka kwenye hizo nchi alizozibainisha ambako ndiko wafanyabiashara wetu huchukua mizigo, Serikali kupitia Wizara hii ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji itafanya tathmini na kuangalia masoko mengine kwa maana ya nchi nyingine zinazozalisha bidhaa kama hizo zinazotafutwa na wawekezaji au wafanyabiashara kutoka Tanzania ili wale ambao watakuwa na bei nzuri, basi mwelekeo uwe katika nchi hizo kuliko kuendelea kutumia masoko ya zamani ambayo bei yake ni kubwa, nashukuru.