Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Yahaya Omary Massare

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Magharibi

Primary Question

MHE. YAHAYA O. MASSARE aliuliza: - Je, ni lini ukarabati utafanywa katika njia ya umeme kutoka kituo kikubwa kuelekea Ikungi, Manyoni, Itigi, Mitundu hadi Mwamagembe?

Supplementary Question 1

MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana ninayo maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Manyoni inapata umeme kutoka Singida na kutoka Singida – Ikungi – Manyoni lakini Itigi – Mitundu hadi Mwamagembe, kutoka kituo kikubwa kinachopoza umeme ni karibu kilometa 400. Serikali ilikuwa na mpango wa kujenga vituo vya kupoozea umeme substation katika Mkoa wa Singida ikiweo Iramba na hiki cha Manyoni ambacho amekitaja kwenye majibu na cha Mitundu.

Je, ni lini sasa wanaenda kujenga vituo hivi katika Mkoa wa Singida? (Makofi)

Swali la pili, nguzo za zege sasa hivi tunaziona katika maeneo mengi zikiwekwa, njia hii ndefu ya kutoka Singida kama nilivyoitaja na umbali wake kutoka Manyoni lakini kutoka Itigi kwenda Mitundu mpaka Mwamagembe kilometa ni nyingi. Ni lini wataweza kuweka sasa nguzo za zege kwa sababu maeneo haya kuna maeneo chepe chepe, maeneo ya misitu lakini maeneo yenye acid yanakula sana nguzo hizi za miti.

Je, ni lini sasa Serikali itaanza kufanya hilo zoezi ili kufanya maisha yawe mazuri, umeme ni maisha. (Makofi)

Name

Stephen Lujwahuka Byabato

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, mojawapo ya sababu ya umeme kukatika katika maeneo mengi ni kusafiri kwa umbali mrefu. Serikali kupitia TANESCO ilifanya upembuzi yakinifu na kubaini mahitaji ya vituo vya kupooza umeme takribani 88 katika Halmashauri zetu zote, imetafuta fedha kupitia mradi wetu wa Gridi Imara na tukapata karibia shilingi trilioni nne na shilingi bilioni mia mbili ambazo zitakuja kwa awamu nne. Awamu ya kwanza tumepata shilingi bilioni 500 na tutajenga vituo 15 katika Wilaya mbalimbali. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Massare pamoja na Waheshimiwa wengine kwamba itakapofika miaka mitano, sita ijayo baada ya mradi wa Gridi Imara kukamilika, kila wilaya tunatarajia iwe na kituo cha kupoaza umeme ili umeme usisafiri umbali mrefu na kuweza kukatika katika humo njiani.

Mheshimiwa Spika, sasa vituo alivyovitaja vya Iramba, Mkalama na maeneo mengine vitajengwa pia katika awamu hizo kulingana na wale ambao wana hali ngumu zaidi kufuatia wenye hali nzuri kidogo.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la nguzo za zege ni kweli Serikali inafanya jitihada za kuhakikisha inabadilisha nguzo za miti kuweka za zege katika maeneo chepe chepe, yenye wadudu waharibifu na maeneo ya mapori ambapo hatuwezi kuingia mara kwa mara kufanya marekebisho. Maeneo aliyoyasema ni ya kipaumbele na tutaenda kuyatazama ili tuyaweke kwenye mpango wa kuyabadilishia kutoka nguzo za mbao kuweka za zege ili umeme upatikane kwa wakati wote katika maeneo hayo na maeneo mengine pia. Ninakushukuru.