Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Marwa Ryoba Chacha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Serengeti

Primary Question

MHE. MARWA R. CHACHA aliuliza:- Zao la tumbaku limekuwa likilimwa sana Wilaya ya Serengeti lakini kuna changamoto kubwa ya kukosa masoko. Je, ni lini Serikali itasaidia upatikanaji wa kampuni zaidi ya moja kwenye ununuzi wa tumbaku ndani ya Wilaya ya Serengeti?

Supplementary Question 1

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza.
Wilaya ya Serengeti ni Wilaya ambayo kimsingi tunazungukwa na wanayama kila kona na zao pekee ambalo kimsingi Tembo hali ni tumbaku, Mheshimiwa Spika, unakumbuka nimekuandikia barua kuhusu issue ya Tembo wamehamia Serengeti wamekula mazao yote; wananchi kwa sasa hawana chakula, zao ambalo kimsingi lilikuwa likiwanufaisha na kuwaokoa wananchi wa Serengeti ni tumbaku, kwa sasa tumbaku haina soko hata kampuni ya Alliance One iliyopo nasikia mwakani inaondoka.
Sasa swali Mheshimiwa Waziri Serikali hii ya Awamu ya Tano kipaumbele chake ni viwanda ni lini mtajenga kiwanda cha ku-process tumbaku Tanzania?
La pili, uko tayari wewe Waziri na mimi Mbunge wa Jimbo la Serengeti kuambatana na wewe kwenda kuwasikiliza wakulima wa tumbaku wa Serengeti na kuwatafutia hayo makampuni uliyosema?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwanza nakiri kabisa kufahamu changamoto inayoletwa na wanyama waharibifu kwa wakulima wa Serengeti kama ilivyo katika maeneo mbalimbali katika nchi yetu. Mimi nafahamu maeneo ya Serengeti kwa sababu ni jirani zangu, sisi Ngorongoro tulichokifanya ni kwamba wanyama tumewatumia kama fursa ili hata pale wakituletea taabu tuone kwamba tunaweza vilevile tukanufaika na hao wanyama.
Hata hivyo changamoto ya tumbaku kama zao la biashara wote tunafahamu, tumbaku ndio zao la pekee duniani ambalo hata wale wanaotaka wanufaike nalo hawakubali kulipigia debe linunuliwe. Leo hii nina hakika Mheshimiwa Mbunge na hata wale wanaotoka maeneo mengine wanaolima tumbaku nikiwaambia twendeni nje tukapige debe ili watu wanunue sigara nina hakika hawataungana na mimi, ndio changamoto ya tumbaku, ni zao ambalo limeshetanishwa duniani yaani limekuwa demonized.
Mheshimiwa Spika, ni zao ambalo pamoja na kwamba tuko tayari kunufaika nalo lakini dunia nzima inapiga vita tumbaku na hii imesababisha bei ya tumbaku iendelee kudorora na wanunuzi wa tumbaku wameendelea kuwa wachache siku baada ya siku. Leo hii nchini tuna wanunuzi wanne tu kampuni hiyo anayosema ya Alliance One, tunao Premium, TLTC na GTI na duniani kote makampuni makubwa hayazidi manne yanayonunua tumbaku. Kwa hiyo, ni shida ambayo ni ya dunia nzima lakini pamoja na changamoto hiyo Serikali inaendelea kutafuta fursa katika masoko ambayo yanaelekea kuanza kujitokeza hasa soko la China. Wizara inaendelea na majadiliano na Ubalozi wa China tuone ni namna gani tunaweza tukapata fursa katika soko la China.
Mheshimiwa Spika, lakini vilevile tunaangalia uwezekano wa kupata fursa katika soko linaloibukia la shisha katika maeneo ya Uarabuni, nchi kama Misri lakini kwa sasa wananchi wetu tunaendelea kuwaeleza umuhimu wa kuangalia uwezekano wa kulima mazao mengine kwa sababu inavyoelekea soko la tumbaku duniani litaendelea kushuka kwa sababu ya aina ya zao lenyewe, ni zao ambalo linapigwa vita, zao ambalo lina madhara kiafya, kwa hiyo, tunaendelea kuwashauri kwamba tutafute mazao muafaka.
Mheshimiwa Spika, kuhusu ujenzi wa kiwanda cha kuchakata tumbaku nchini nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ya Awamu ya Tano inaweka mazingira wezeshi pamoja na kushawishi sekta binafsi kujenga viwanda vya tumbaku.
Mheshimiwa Spika, tuna baadhi ya viwanda vya tumbaku, kuna kiwanda kikubwa kipo Morogoro lakini tunaendelea kuwahamasisha sekta binafsi kama wanaweza wakaanzisha kiwanda cha kuchakata tumbaku sina hakika kama hata nikiandamana na Mheshimiwa Mbunge kwenda Serengeti kwamba mimi ninaweza nikapeleka kiwanda kule lakini tutaendelea kuwahamasisha sekta binafsi.
Mheshimiwa Spika, kuhusu Serikali inafanya nini kuhusiana na uharibifu ambao unaendelea, nilishaongea na Mheshimiwa Mbunge kwamba mimi niko tayari kuongea na Wizara ya Maliasili ili kuangalia ni namna gani Serikali inaweza ikawafidia wananchi ambao mazao yao yanaharibiwa na Tembo.