Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 4 Sitting 1 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Wizara ya Kilimo 8 2016-09-06

Name

Marwa Ryoba Chacha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Serengeti

Primary Question

MHE. MARWA R. CHACHA aliuliza:-
Zao la tumbaku limekuwa likilimwa sana Wilaya ya Serengeti lakini kuna changamoto kubwa ya kukosa masoko.
Je, ni lini Serikali itasaidia upatikanaji wa kampuni zaidi ya moja kwenye ununuzi wa tumbaku ndani ya Wilaya ya Serengeti?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Marwa Ryoba Chacha, Mbunge wa Serengeti kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, majaribio ya kilimo cha tumbaku kibiashara Mkoani Mara yalianza mwaka 2008/2009 kwa lengo la kuwaelekeza wakulima kufuata mfumo wa Tanzania tofauti na hapo awali ambapo walilima tumbaku na kuuza kwa kufuata mfumo wa nchi jirani ya Kenya.
Kimsingi kilimo cha tumbaku mkoani Mara kulikuwa hakijaimarishwa na hivyo kutowanufaisha wakulima kama ilivyo katika maeneo mengine nchini. Aidha, kuendelea kulima tumbaku bila utaratibu maalum kulihatarisha kuenea kwa magonjwa ya tumbaku katika nchi hizi mbili.
Mheshimiwa Spika, msimu wa 2011/2012, Serikali kupitia Bodi ya Tumbaku ilirasimisha kilimo cha tumbaku mkoani Mara ikiwa ni pamoja na Wilaya ya Serengeti. Hatua ya kufunguliwa kilimo cha tumbaku mkoani humo ilitoa fursa kwa kampuni zilizopenda kununua tumbaku mkoani humo kufanya hivyo kwa kuzingatia kanuni na taratibu za zao hilo na pamoja na sheria nyingine za nchi. Hivi sasa Kampuni ya Alliance One ndio kampuni pekee inayonunua tumbaku mkoani Mara.
Mheshimiwa Spika, katika msimu wa 2013/2014 Serikali iliziandikia barua kampuni zote zinazonunua tumbaku nchini kuzijulisha uwepo wa fursa ya kuwekeza katika kununua tumbaku mkoani Mara. Hata hivyo, juhudi hizo hazijaleta matunda yaliyokusudiwa. Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wengine akiwepo Mheshimiwa Mbunge kuzishawishi kampuni hizo kuwekeza Wilayani Serengeti. Aidha, kwa kuwa Tanzania ina wanunuzi wachache, Serikali itaendelea kushawishi wanunuzi wengine hususan kutoka China kununua tumbaku ya Tanzania ikiwa ni pamoja na ya Wilaya ya Serengeti.