Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Primary Question

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA aliuliza: - Je, Serikali ina mkakati gani wa kupeleka watumishi na vifaa tiba katika Kituo cha Afya Majengo?

Supplementary Question 1

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, pamoja na majibu ya mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; upungufu uliopo katika kila Kituo cha Majengo tuna upungufu huo katika Kituo cha Afya Jinyecha, Kiromba na Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Nanyamba na kupelekea kuwa na upungufu wa watumishi 610; je, Serikali ina mpango gani wa dharura kupunguza tatizo hilo la watumishi katika Halmashauri ya Mji wa Nanyamba? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; Wizara ya Afya imetoa mwongozo wa wanachuo wa kada ya afya ambao wamemaliza waweze kujitolea katika vituo vya kutolea huduma.

Je, Serikali haioni sasa ni muda muafaka wa kutenga fedha kiasi ili wahitimu hawa sasa waanze kufanya kazi katika maeneo yenye upungufu mkubwa wa watumishi? Kwa sababu kwanza itasaidiia tatizo la watumishi, lakini pili watakuwa wanatumia ujuzi wao wakati wanasubiri ajira za kudumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Abdallah Dadi Chikota, Mbunge wa Jimbo la Nanyamba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Halmashauri ya Nanyamba ina upungufu wa watumishi takribani 610 ambayo Mheshimiwa Mbunge amewataja na Mpango wa Serikali ni kuendelea kuajiri watumishi, lakini pia kupeleka watumishi wengi zaidi kwenye maeneo yenye changamoto kubwa zaidi ya watumishi hao kama ilivyo katika Halmashauri ya Nanyamba. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge hasa kwenye hizi ajira ambazo tayari zimetangazwa tutahakikisha halmashauri zote ikiwemo Nanyamba ambazo zina upungufu mkubwa zaidi wa watumishi zinapewa kipaumbele zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, Serikali ni kweli kupitia Wizara ya Afya, lakini pia Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumetoa mwongozo wa namna ya watumishi wa kada za afya kujitolea kwenye vituo vya huduma zetu. Tumeelekeza Wakurugenzi kutenga fedha za angalau posho kwa ajili ya wanaojitolea katika vituo vyetu, niendelee kusisitiza kwamba suala hili ni muhimu Wakurugenzi wafanye hivyo ili kuendelea kupunguza upungufu wa watumishi katika sekta hizo, ahsante. (Makofi)