Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Masache Njelu Kasaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupa

Primary Question

MHE. MASACHE N. KASAKA aliuliza: - Je, ni lini Serikali itapunguza ukubwa wa Msitu wa Mbiwe na kurudisha kwa Wananchi?

Supplementary Question 1

MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Pamoja na majibu ya Serikali lakini bado nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hifadhi ya Msitu wa Mbiwe ilianza rasmi mwaka 1995, wakati shughuli za kibinadamu za kiuchumi katika mamlaka ya Mji Mdogo Makongolosi hasa kilimo zilikuwa zinafanyika: -

Je, Serikali haioni haja sasa kwa kipindi hiki kuweza kuweka utaratibu maalum kama ilivyofanya kwenye uchimbaji wa madini ili na hawa wananchi wanaoshughulika na shughuli za kilimo waweze kufuata hizo taratibu waweze kufanya shughuli zao za kilimo kwenye maeneo yanayofaa kwa kilimo?

Swali la pili, Wilaya ya Chunya imekuwa muhanga wa kupokea wahamiaji wengi waliotoka maeneo mbalimbali walikofukuzwa huko hasa maeneo ya Usangu pamoja na Wilaya ya Songwe: -

Je, Serikali haioni haja sasa kuweza kuona utaratibu maalum hawa wananchi ambao wametoka kwenye maeneo hayo, wanafika Wilaya ya Chunya na kuharibu mazingira hasa na mifugo yao kuweza kuingia kwenye maeneo ya mashamba kuweza kutoa tamko rasmi ili wananchi wetu wale wasiweze kuathirika na mifugo hiyo inayoingia ndani ya Wilaya ya Chunya.

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Masanche Njeru Kasaka Mbunge wa Rupa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu utaratibu wa kuruhusu shughuli za kilimo ndani ya hifadhi, taratibu na kanuni zinaelekeza kwenye uapnde wa misitu ya TFS kwamba kunapokuwa na uchimbaji wa madini basi wale wachimbaji wanaruhusiwa kuchimba na wakati huohuo kurudishia miti ili kuendelea kuhifadhi maeneo hayo. Kwa hiyo, sheria na taratibu zinazoongozwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania ni kwamba hairuhusiwi kufanya shughuli za kilimo isipokuwa uchimbaji wa madini, ambalo ni eneo maalumu lililo ndani ya hifadhi ya misitu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu wahamiaji, binadamu au wananchi kulingana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haimzuii mwananchi yoyote kuishi eneo lolote analohitaji. Katiba inaruhusu mtu yoyote kuishi pale ambapo anaona panafaa, isipokuwa kwa wale ambao wanavamia maeneo ya hifadhi sheria na taratibu zitafuatwa ikiwemo kuwakamata na kuwachukulia hatua za kisheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo nawaomba wananchi waheshimu maeneo ya hifadhi kwa mustakabali wa Taifa letu na kwa faida ya wananchi wenyewe.

Name

Condester Michael Sichalwe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Momba

Primary Question

MHE. MASACHE N. KASAKA aliuliza: - Je, ni lini Serikali itapunguza ukubwa wa Msitu wa Mbiwe na kurudisha kwa Wananchi?

Supplementary Question 2

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa vijiji vya Twentela, Mbalwa, Ntungwa, Mbawo, Moraviani na Itumbula wamezungukwa na hifadhi, hapo nyuma wananchi hao wenyewe kwa ridhaa yao walitoa maeneo hayo ya hifadhi ambayo yalikuwa ni ya kwao.

Je, Serikali haioni ipo haja ya kumega kipande kidogo tu cha hifadhi kuwasaidia wananchi hawa wapate eneo la kulima kwa sababu wamezaliana na hawana sehemu nyingine ya kwenda kwa ajili kuendesha shughuli zao, lakini kwa kufuata utaratibu na kutoa elimu bila kuathiri sheria zetu. Ahsante sana.

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Condester kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali hili pia aliwahi kuuliza Mheshimiwa Mbunge na taratibu nilimwelekeza kwamba, maombi yanatakiwa yaletwe na sisi tutaangalia tathmini, kama kuna umuhimu wa kumega eneo hilo basi tutapeleka mapendekezo kwa Mheshimiwa Rais, lakini pale ambapo tutaona kuna haja ya kutunza vyanzo vya maji basi wananchi wataelimishwa na maeneo haya tutayahifadhi kwa ajili ya kizazi hiki na kinachokuja.

Name

Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Primary Question

MHE. MASACHE N. KASAKA aliuliza: - Je, ni lini Serikali itapunguza ukubwa wa Msitu wa Mbiwe na kurudisha kwa Wananchi?

Supplementary Question 3

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kuuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunatangaza Hifadhi ya Nyerere, National Park tayari kuna maeneo ya WMA, mfano kama Wma ya Magingo katika vijiji vya Mpigamiti, Barikiwa na Mlembwe tayari vimechukuliwa na TANAPA.

Je, ni lini Serikali itakuja kuhakiki hiyo mipaka ili yale maeneo yaliyokuwa yamehifadhiwa na vijiji yaendelee kuwa yanahifadhiwa na vijiji?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kuchauka, Mbunge wa Liwale, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu wananchi wa Liwale niwaahidi kwamba kwa kuwa taratibu za kuainisha mipaka ni kazi inayoshirikisha Wizara ya Ardhi pamoja na Wizara ya Maliasili na Utalii, tutaenda kuhakiki hiyo mipaka ili kuruhusu wananchi watambue maeneo yao na kisha yaendelee kuhifadhiwa vizuri.

Name

Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Primary Question

MHE. MASACHE N. KASAKA aliuliza: - Je, ni lini Serikali itapunguza ukubwa wa Msitu wa Mbiwe na kurudisha kwa Wananchi?

Supplementary Question 4

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itamaliza mgogogro wa mpaka kati ya TANAPA na wananchi wa Momela ambao unatokana na TANAPA kutwaa mashamba Namba 40 na Namba 41 bila kushirikisha Serikali ya Kijiji.

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Pallangyo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimuahidi Mbunge tutaenda kuzungumza na wananchi nikishirikiana na wataalamu tupate maelezo ya kutosha.