Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Dr. Paulina Daniel Nahato

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO aliuliza: - Je, ni lini Serikali itawalipa Wahadhiri wote nchini malimbikizo yao ya miaka ya nyuma?

Supplementary Question 1

MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, Serikali imeweka mkakati gani wa kuhakikisha malimbikizo hayaendelei tena kutokea katika kipindi kijacho?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, je, Serikali ipo tayari kulipa riba katika malimbikizo ya malipo yaliyochelewa kulipwa kwa Wahadhiri kama inavyofanya kwa wakandarasi wanaochelewa kulipwa malipo yao? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Paulina Nahato, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoeleza kwenye majibu ya msingi, kwamba Serikali hulipa malimbikizo pamoja na stahiki nyingine za watumishi kulingana na bajeti. Kwa hiyo, mkakati wetu kama Serikali jambo la kwanza ni kuhakikisha kwamba tunaweka bajeti stahiki na toshelezi ili malimbikizo kwanza yasitokee na pili watumishi wanapokuwa na madai yao yaweze kulipwa kwa wakati. Huo ndiyo mkakati wetu kama Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo la pili la riba, naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge kwamba malipo haya hulipwa kwa mujibu wa kanuni, sheria taratibu na miongozo na kwa kanuni tulizonazo hivi sasa, hazina eneo ambalo linaonesha kwamba malipo yatakapochelewa yalipwe na riba. Kwa hiyo, halipo na badala yake tunasimamia utaratibu wa kawaida ambao ni bila riba.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.