Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SUBIRA K. MGALU aliuliza: - Je, ni lini Hospitali ya Rufaa Tumbi na Hospitali za Wilaya za Mkoa wa Pwani zitapokea vifaa tiba ikiwa ni sehemu ya fedha za kupambana na UVIKO-19?

Supplementary Question 1

MHE. SUBIRA K. MGALU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwanza naishukuru sana Serikali kwa kazi nzuri iliyofanya kupitia fedha hizi za UVIKO na naishukuru sana Wizara ya Afya.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kwenye jibu la msingi ameeleza vifaa hivi vimefika zaidi ya asilimia 94 katika Hospitali ya Tumbi; je, Mheshimiwa Waziri anatuahidi ndani ya mwezi Oktoba kwamba CT Scan itafanya kazi, yupo tayari kuwaelekeza wataalam wake kuhakikisha kweli mwezi Oktoba vifaa hivi vitafanya kazi kwa kuwa ni jambo la kihistoria na halijawahi kutokea kuwa na CT Scan ngazi ya hospitali za rufaa za mkoa?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kwa kuwa kazi kubwa imefanywa ya ujenzi ya miundombinu ya afya ikiwemo vituo vya afya Mkwakwani tuna vituo vya afya 10 kutokana na tozo na hospitali za wilaya na zahanati.

Je, Serikali haioni ipo haja sasa ya kupunguza ujenzi wa miundombinu mipya ili ijielekeze kuhakikisha miundombinu hii ambayo imejengwa kwa kasi inapata vifaa tiba kwa kuwa pia inakuja na mpango wa bima ya afya ili mpango huu ukianza kutekelezeka hospitali zote na vituo vya afya viweze kuwa na vifaa tiba? Ahsante sana. (Makofi)

Name

Ummy Ally Mwalimu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Tanga Mjini

Answer

WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Subira Mgalu kwa maswali yake mazuri na hususan kusema kwamba suala la ununuzi wa vifaa tiba ni jambo la kihistoria ambalo limefanywa na Rais Samia Suluhu Hassan haijapata kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa CT Scan kama nilivyosema itafungwa by October, 2022 lakini kabla ya kuanza kufanya kazi lazima pia tufanye testing (tufanye majaribio) na watu wa Tume ya Atomic Energy lazima pia watoe kibali cha kuanza kutumika. Kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Subira Mgalu kwamba suala hili kwetu ni la kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, suala la pili kuhusu je, kwa nini sasa Serikali isijielekeze katika kuimarisha huduma za afya? Nakubaliana nawe Mheshimiwa Subira na mimi nilishatoa maelekezo kwa wenzangu Wizara ya Afya, lakini kwa Ofisi ya Rais – TAMISEMI. Tumejenga zahanati nyingi, tumejenga vituo vya afya vingi, tumejenga hospitali za wilaya nyingi. Sasa hivi tujikite kuhakikisha kwamba huduma zinatolewa zenye ubora katika hospitali tulizojenga.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kipaumbele cha Wizara ya Afya au kwa sekta ya afya sasa hivi ni mambo mawili; ubora wa huduma, kuhakikisha huduma zinapatikana, dawa zinapatikana, tunao watumishi wa kutosha lakini pamoja na lugha ambazo wataalam wetu wa afya wanawahudumia wananchi. Kwa hiyo, hiki ndiyo kipaumbele cha sekta ya afya katika kipindi hiki.

Mheshimiwa Spika, sisemi kwamba hatutajenga zahanati na vituo vya afya kwa sababu Waheshimiwa Wabunge wengi mnataka, lakini tutajikita katika maeneo ya kipaumbele ambayo tunadhani labda kuna umbali mrefu, kuna idadi kubwa ya wananchi, lakini pia mzigo wa magonjwa bado ni mkubwa katika eneo hilo husika. Nakushukuru sana.