Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Tumaini Bryceson Magessa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busanda

Primary Question

MHE. TUMAINI B. MAGESSA aliuliza: - Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya kutoka Geita kupitia Nyarugusu kwenda Bukoli hadi Kahama ambapo upembuzi yakinifu ulishafanyika?

Supplementary Question 1

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu yale yale ambayo alinipatia mwaka 2021 leo yamejirudia tena. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza kwenye swali hili. Kwa vile mazungumzo ya ahadi yaliyotolewa na Barrick yamechukua muda sasa na hayana mafanikio: Nini kauli ya Serikali kwa ujenzi wa barabara hii bila kuhusisha Barrick ili iweze kufanyika? Kwa sababu wale waliotoa ahadi wanaonekana kama hawapo tayari kutekeleza ahadi hiyo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa vile upembuzi yakinifu wa barabara hii umeshafanyika toka mwaka 2017, lakini nasikitika kwamba nyumba zilizoko barabarani zote hazina alama: -

Je, nini mpango wa Serikali kuonyesha wananchi kwamba nyumba hizi zitabomolewa kama barabara itajengwa hivi karibuni?

Name

Eng. Godfrey Msongwe Kasekenya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ileje

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Magessa, Mbunge wa Busanda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, bado mazungumzo yanaendelea na yako kwenye hatua nzuri. Kama yangekuwa yamekwama, tungeacha na kutafuta utaratibu mwingine. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mazungumzo yanaendelea kati ya Barrick na hizo Wizara ambazo nimezitaja.

Mheshimiwa Spika, swali la pili; tunapoweka alama za kuanza kubomoa, ni pale ambapo taratibu zote za kuanza ujenzi zimeanza na fedha ya kutoa fidia imeshapatikana. Tukishafikia hatua hiyo, basi tutaanza kuweka alama kuonesha wananchi ambao watapisha barabara hiyo. Ahsante. (Makofi)

Name

Salma Rashid Kikwete

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mchinga

Primary Question

MHE. TUMAINI B. MAGESSA aliuliza: - Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya kutoka Geita kupitia Nyarugusu kwenda Bukoli hadi Kahama ambapo upembuzi yakinifu ulishafanyika?

Supplementary Question 2

MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kuuliza kuhusu barabara ya Ngongo - Milola na Michiga. Hii barabara ina urefu wa kilomita 82. Tuliambiwa itajengwa kwa kiwango cha lami, lakini mpaka leo bado hatujaiona hiyo lami. Kibaya zaidi kwenye barabara hii, sasa hivi mvua hizi zinazonyesha, hii barabaraba imekatika yote na wakaweka mchepuko, diversion ya pili; na hata ile diversion ya pili nayo imekatika; na barabara hii ni kiungo muhimu baina ya Majimbo matatu; Jimbo la Lindi, Jimbo la Mchinga na Jimbo la Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, tunaomba kauli ya Serikali, lini barabara hii itarekebishwa? Kama siyo kurekebishwa ina maana kwamba Majimbo haya yote yatakuwa yamejifunga. Ahsante. (Makofi)

Name

Eng. Godfrey Msongwe Kasekenya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ileje

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI – (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Salma Kikwete, Mbunge wa Mchinga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Salma kwa jinsi ambavyo anafuatilia hii barabara ya Ngongo - Milola - Michiga yenye kilometa 82. Barabara hii inapita kwenye miinuko mikali; na kama alivyosema pia kuna maporomoko mengi ya maji.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa barabara hii imekatika, naomba kutumia nafasi hii kumwangiza Meneja wa TANROAD ahakikishe kwamba kesho anafika maeneo yote na kuhakikisha kwamba anapeleka Wakandarasi kwa ajili ya kurekebisha hii barabara na nipate taarifa kuanzia kesho ambapo pia atawasiliana na Mheshimiwa Mbunge kuona kwamba hili suala linafanyika ili kuhakikisha kwamba barabara hii inapitika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu ujenzi kwa kiwango cha lami, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ina azma ya kuijenga na fedha bado zinaendelea kutafutwa. Basi zikipatikana, tunaanza kuijenga hii barabara kwa kiwango cha lami. Ahsante.(Makofi)

Name

Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Primary Question

MHE. TUMAINI B. MAGESSA aliuliza: - Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya kutoka Geita kupitia Nyarugusu kwenda Bukoli hadi Kahama ambapo upembuzi yakinifu ulishafanyika?

Supplementary Question 3

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu imefanya kazi kubwa sana ya kujenga barabara nzuri kutoka Ndondo mpaka Kigoma. Tatizo kubwa linalotukabili sisi Urambo ni kwamba kona ya kuingilia Urambo Mjini inasababisha ajali kubwa sana. Sasa kwa kuwa nilishaomba Serikalini kujengewa round about na Serikali imeshafanya utafiti wake, imeshapata na gharama: Je, Serikali iko tayari sasa kujenga hiyo round about. (Makofi)

Name

Eng. Godfrey Msongwe Kasekenya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ileje

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Sitta, Mbunge wa Urambo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama alivyosema kwamba kama tathmini ilishafanyika, maana yake ni kwamba Serikali ina dhamira ya kuijenga. Naomba baada ya hapa, nimwombe Mheshimiwa Margaret Sitta tuweze kuona ni wapi tumekwama ili tuweze kuamua, kwa sababu kama kazi imeshafanyika, maana yake ni kwamba Serikali imeshaona kuna umuhimu wa kujenga.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)

Name

Halima James Mdee

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. TUMAINI B. MAGESSA aliuliza: - Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya kutoka Geita kupitia Nyarugusu kwenda Bukoli hadi Kahama ambapo upembuzi yakinifu ulishafanyika?

Supplementary Question 4

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Miradi mingi ya Serikali ya barabara ina mwaka kati ya mmoja, kumi na mingine hadi 15 na changamoto kubwa ni kwa sababu tunaahidi barabara nyingi, lakini tuna fedha kidogo, hali inayosababisha tunagawana kilometa moja moja, matokeo yake barabara hazikamiliki, lakini tunatumia fedha nyingi sana kulipa interest kwa wakandarasi kwa sababu hatulipi fedha zote kwa wakati. Sasa Kamati ya bajeti ilishauri kwamba kwa nini Serikali isianze kumaliza barabara zote ambazo ziko kwenye mpango, kisha ndiyo tuanze upya?

Je, wazo hili la Kamati ya Bajeti ambalo Bunge limeridhia kwamba tumalize viporo vyote vikamilike, barabara ikamilike; Serikali imelipuuza ama inalifanyia kazi? (Makofi)

Name

Eng. Godfrey Msongwe Kasekenya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ileje

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Halima Mdee, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali haiwezi kupuuza ushauri wa Kamati ya Bajeti. Pia nataka nimhakikishie Mheshimiwa Halima Mdee kwamba tunaendelea kuufanyia kazi ushauri wa Kamati ya Bajeti na tutakuja kulileta kama Serikali, tuone namna tutakavyofanya kuhusu kuhamua ni barabara zipi zijengwe na kwa wakati upi?

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Primary Question

MHE. TUMAINI B. MAGESSA aliuliza: - Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya kutoka Geita kupitia Nyarugusu kwenda Bukoli hadi Kahama ambapo upembuzi yakinifu ulishafanyika?

Supplementary Question 5

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri ambayo yamekuwa ni yale yale kila mwaka, lakini mwaka wa fedha ulioisha, barabara ya Geita - Kahama ilitengewa shilingi bilioni tatu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa nini Wizara isitangaze kumpata mkandarasi na kuanza na fedha hizo zilizotengwa ili kipande hicho kitakachoanza kujengwa kianze kuanza kazi?

Name

Eng. Godfrey Msongwe Kasekenya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ileje

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye jibu la msingi, fedha iliyotengwa hii ni pamoja na fedha tunayotegemea kuipata kama mazungumzo yatakamilika na wenzetu wa Barrick. Kwa hiyo, mara fedha itakapopatikana, basi kazi hizo zitaanza kwa pamoja. Ahsante. (Makofi)