Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Cecil David Mwambe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ndanda

Primary Question

MHE. CECIL D MWAMBE K.n.y. MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza: - (a) Je ni lini mikataba ya miradi mbalimbali ya migodi ya madini, ujenzi wa Bandari Bagamoyo, ujenzi wa Reli (SGR), ujenzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere, Bomba la Mafuta na Mradi wa Bomba la Gesi kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam italetwa Bungeni ili kupata ufahamu wa miradi hiyo? (b) Je, katika mikataba hii ni mingapi imewahi kukaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali?

Supplementary Question 1

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama utakumbuka mwaka jana mwishoni, Mheshimiwa Spika aliunda Kamati Maalum kabisa ambayo ilikuwa ni Kamati ya Viwanda na Biashara pamoja na Kamati ya Bajeti na tulikaa kwa nia ya kutaka kupitia mambo mbalimbali kwa sababu tulipokea taarifa za malalamiko kutoka kwa wafanyabiashara kuhusiana na bei kubwa za stamp za kielektroniki. Lakini nimesimama hapa nikwambie tu kwamba pamoja na mazungumzo yale Serikali au TRA waliendelea kusaini mkataba huo ambao umekuwa wa kinyonyaji kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimuulize Waziri wetu wa Katiba kwamba je, yupo tayari sasa kuleta mkataba kati ya SICPA na Serikali unaohusisha masuala ya stamp za kielektroniki ili tuweze kuwasaidia wananchi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, pamoja na hiyo mikataba mingi uliyoisema na sisi kama Wabunge wengi tunatamani kujifunza na wengine siyo wahudhuriaji kwenye Kamati hizo ulizozitaja. Hauoni sasa ni wakati mikataba hiyo kwa mfano hiyo SGR, mkataba wa Bandari ya Bagamoyo, mkataba wa gesi wa kule Mtwara na mingine mingi kuwa wazi kwa Wabunge wote kuisoma na kupata uelewa wa kina kuweza kuishauri Serikali? (Makofi)

Name

Geophrey Mizengo Pinda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kavuu

Answer

NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na swali la nyongeza la kwanza la Mheshimiwa Mwambe hili linalohusu stamp, nadhani tutafanya mawasiliano na taasisi inayohusika ili tuweze sasa kujiweka sawa katika eneo hili ambalo limeonesha mashaka ya mkataba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili kuhusu suala la kuwasilisha mikataba katika Bunge lako tukufu kama nilivyoeleza mwanzo, mikataba hii huwa inapita kwenye Kamati kwa sababu ndiyo taratibu zilizowekwa. Kama Bunge lako tukufu litataka mkataba ufikishwe mbele ya Bunge lote basi maamuzi yanatoka kwenye Kamati baada ya kupitia zile taarifa zinazowasilishwa. Ahsante.