Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Khalifa Mohammed Issa

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Mtambwe

Primary Question

MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA aliuliza: - Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha uwepo wa marubani wawili kwenye ndege ndogo za abiria?

Supplementary Question 1

MHE. KHLAIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza namshukuru Waziri kwa majibu yake ya kina, lakini hata hivyo nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali langu lilihusu hasa usalama wa raia wanaporushwa katika ndege. Usalama wao huu siyo kwa sababu ya uchache na udogo wa ndege. Ndege nyingi takribani ndogo ndogo hizi ambazo tunaruka nazo ni chini ya kilogramu 4,000, lakini bado ni abiria: Je, Serikali itabadilisha sheria hata kuwa ndege ni ya watu watatu, kilogram 3,000 kuleta marubani wawili?

Mheshimiwa Spika, la pili, kuhusu marubani kufanyiwa uhakiki wa afya zao miezi sita au 12; mgogoro wa afya unaweza kutokea wakati wowote akiwa ndani ya anga. Sasa unaonaje, unanusuru vipi abiria wale ambao rubani wao amepata changamoto ya afya akiwa angani peke yake? Ahsante.

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA
M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, nakushukuru. naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Khalifa, Mbunge wa Mtambwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza Mheshimiwa Mbunge anataka kujua, ni kwa nini ndege ambazo zinabeba watu chini ya kilo 3,000 haziwezi kutumia marubani wawili?

Kwanza, ndege inapokuwa inatengenezwa, yule mtengenezaji anatoa maelekezo marubani wangapi wanapaswa kuitumia hiyo ndege.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, ni kweli kwamba kutumia marubani wawili kwenye ndege moja ndogo pia ni gharama, maana yake huyo rubani inabidi alipwe. Ila sisi kisheria tumeruhusu kwamba unaweza ukatumia marubani wawili, lakini waendeshaji wadogo kwenye ndege zao hawazuiliwi kisheria kutumia marubani wawili.

Mheshimiwa Spika, la tatu, wanaangalia pia ile ndege aina ya mitambo na vipuri vinavyotumika. Ndege hizi ndogo zinabeba chini ya abiria 19 na haziendi umbali mrefu zaidi na hazitembei kwa saa nyingi na haziendi juu ya anga kwa maana ya kupata mikikimikiki ile ya mawimbi makubwa. Hata hivyo ikitokea kuna viashiria vya hali ambayo siyo nzuri kwa afya, kwa kuchukua tahadhani wanaweza kuongeza rubani wa pili katika ndege hiyo.

Mheshimiwa Spika, la pili ni uhakiki wa afya za marubani kwamba wale ambao wana miaka chini ya 40 ni mizei sita, lakini wale zaidi ya miaka 40 ni miezi 12. Hii ni ukweli kwamba kisayansi kwa mazoea ni kwamba hawa wenye chini ya miaka 40 ni vijana, tunaamini kwamba wana afya na nguvu ya kuweza kufanya kazi zaidi. Ila ikitokea kwamba kuna viashiria vya hali ya usalama kiafya wanaweza kufanyiwa utaratibu wa kupimwa afya zao hata chini ya miezi mitatu. Ni jambo ambalo linawezekana.

Mheshimiwa Spika, tunafanya mambo yote haya kwa kuzingatia Sheria ya Anga ya Kimataifa.

Mheshimiwa Spika, ahsante.