Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Jeremiah Mrimi Amsabi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Serengeti

Primary Question

MHE. JEREMIAH M. AMSABI aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kupunguza Viwanja vya Ndege ndani ya Hifadhi ya Serengeti kwa kujenga Uwanja wa Ndege katika Mji wa Mugumu nje kidogo ya Hifadhi pamoja na kukamilisha ujenzi wa barabara ya lami ya Makutano Sanzate Natta na ile ya Tarime Mugumu Natta?

Supplementary Question 1

MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni sote tumeona jitihada kubwa sana za Rais Samia za kuvutia watalii katika nchi yetu, lakini pia sasa hivi tayari Mkuu wa Mkoa wa Mara Mheshimiwa Ally Hapi, pamoja na Wizara ya Maliasili na Utalii walianza jitihada za pamoja, wameanza vikao vya kuona namna ya kujenga uwanja ule. Hii ni kuzingatia pia kwamba kuna ushindani mkubwa kwa wenzetu, watu wa Masai Mara kule Kenya ambao wana-share ikolojia moja na Serengeti.

Mheshimiwa Spika, sasa namwomba sana Mheshimiwa Naibu Waziri nipate nafasi ya kukutana naye kwa mazungumzo maalumu kuona ni namna gani tutapata mwelekeo wa pamoja wa kuweza kujenga uwanja huu kwa viwango vikubwa kabisa.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, barabara hii ya Sanzate mpaka Natta, na ile ya Tarime – Mugumu – Natta, barabara hizi hazi-connect Makao Makuu ya Wilaya ya Serengeti pale Mugumu. Mwaka wa jana, 2020 aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano alitupa ahadi ya ujenzi wa kilometa 30. Kwa hiyo, namwomba sana…

SPIKA: Unasema Tarime – Mugumu – Natta, haifiki Mugumu tena!

MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Spika, Tarime – Mugumu – Natta halafu kuna ile ya Makutano na Sanzate – Natta. Sasa zote hizi kwa jinsi ya ule mpango wa ujenzi, zitachukua muda mrefu kuja kuunganisha Makao Makuu ya Wilaya. Kwa hiyo, tukawa tumemwomba aliyekuwa Rais Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwamba kipande cha Natta – Mugumu kiweze kupewa fedha kijengwe haraka ili barabara ile ya Makutano – Sanzate – Natta sasa itoke pale Natta mpaka Mugumu. Halafu na ile inayotoka kule Tarime – Nyamwaga – Mugumu iweze kuungana nayo mapema zaidi.

Mheshimiwa Spika, sasa ni lini Wizara inaweza kutekeleza mpango huu na ile ahadi ya Rais? Ahsante sana.

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Amsabi Jeremiah, Mbunge wa Serengeti kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza ameomba tufanye mazungumzo namna bora ya kupata fedha ya kujenga uwanja wa ndege wa Serengeti.

Mheshimiwa Spika, naomba tu nitumie nafasi hii kusema kwamba kwa sasa pia Mheshimiwa Rais ameshatoa fedha za kutosha za kuanzia ujenzi wa uwanja wa ndege wa Musoma na mkandarasi ameshapatikana, yupo site anafanya kazi, lengo ni kuboresha huduma katika Hifadhi ya Serengeti.

Mheshimiwa Spika, tangu anazungumza Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa, walifanya kazi nzuri sana pamoja na Wizara ya Maliasili ya kufanya mjadala. Sisi tunaona kwamba uwanja ambao walipendekeza kujenga ni uwanja ambao unamilikiwa na TANAPA na Halmashauri, ambao ni uwanja mdogo. Sisi tunataka tujenge uwanja mkubwa wa Kimataifa ili tushindane na wenzetu wa Kenya ambao wanajenga kule Masai Mara uwanja mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumewaelekeza watu wa Maliasili Uongozi wa Mkoa wa Mara watuletee andiko maalumu, tukae pamoja na Wizara ya Ujenzi, tujenge Uwanja wa Ndege wa Kimataifa ili tusigawane watalii wanaotaka kupata huduma katika mbuga yetu ya Serengeti. (Makofi)

SPIKA: Huo uwanja mnataka kujenga wapi?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, tunafikiria kujenga uwanja wa ndege Serengeti pale Mugumu, wanalo eneo pale la kutosha.

SPIKA: Haya endelea.

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, sawa, ahsante.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni kweli kwamba barabara ya Sanzatte inajengwa na ameleta ombi la kilometa 30, tumepokea ombi hilo na linafanyiwa kazi. Wakati huo huo, kilometa 25 zinajengwa kutoka eneo la Tarime kwenda Serengeti ili wananchi wa eneo hilo waweze kupata huduma.

Mheshimiwa Spika, mawazo yote ni mazuri, lakini kupanga ni kuchagua. Kadri tunavyopata fedha za kutosha, barabara hizo zitakamilika kwa wakati ili huduma iweze kupatikana katika eneo la Serengeti. Ahsante. (Kicheko)