Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 4 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 46 2021-11-05

Name

Jeremiah Mrimi Amsabi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Serengeti

Primary Question

MHE. JEREMIAH M. AMSABI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupunguza Viwanja vya Ndege ndani ya Hifadhi ya Serengeti kwa kujenga Uwanja wa Ndege katika Mji wa Mugumu nje kidogo ya Hifadhi pamoja na kukamilisha ujenzi wa barabara ya lami ya Makutano Sanzate Natta na ile ya Tarime Mugumu Natta?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri na Ujenzi na Uchukuzi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jeremiah Amsabi Mrimi, Mbunge wa Jimbo la Serengeti, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa lengo la kujenga Kiwanja cha Ndege cha Serengeti katika eneo la Mugumu, kitakachotoa huduma za usafiri ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti. Aidha, kiwanja hicho kitakapojengwa na kukamilika kitapunguza matumizi ya viwanja vya ndege ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti kwani ndege nyingi zitakuwa zikitumia kiwanja kitakachokuwa kimejengwa nje ya hifadhi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu barabara ya Makutano – Sanzate – Natta yenye urefu wa kilometa 90, ujenzi kwa kiwango cha lami unaendelea na umegawanyika katika awamu mbili. Sehemu ya kwanza ni Makutano – Sanzate yenye urefu wa kilometa 50; kazi za ujenzi kwa kiwango cha lami zinaendelea na hadi Oktoba 2021 ujenzi ulikuwa umefikia asilimia 90 na unatarajiwa kukamilika mwezi Februari, 2022. Aidha, sehemu ya pili ni Sanzate – Natta yenye urefu wa kilometa 40; ujenzi kwa kiwango cha lami unaendelea. Hadi Oktoba, 2021 kazi za ujenzi zilikuwa zimefikia 7% na zinatarajiwa kukamilika mwezi Julai, 2022.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Barabara ya Tarime – Mugumu – Natta yenye urefu wa kilometa 122.97 itajengwa kwa awamu. Zabuni kwa ajili ya kupata Mkandarasi wa kujenga sehemu ya Tarime - Nyamwaga yenye urefu wa kilometa 25 zimefunguliwa mwishoni mwa Oktoba, 2021 na uchambuzi unaendelea ili kumpata Mkandarasi wa ujenzi. Serikali itaendelea na ujenzi wa sehemu iliyobaki kadiri ya upatikanaji wa fedha. Ahsante.