Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Dr. Pius Stephen Chaya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Primary Question

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kuhuisha vigezo vya mfumo wa miradi ya kimkakati kupitia maandiko ya miradi ili iweze kusaidia Halmashauri kubuni miradi ya kiuchumi?

Supplementary Question 1

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, ninayo maswali mawili ya nyongeza. Swali langu la kwanza; ni lini sasa Serikali itatoa huo mwongozo mpya ili tuweze kusaidia zile halmashauri ambazo zina uhitaji mkubwa wa kuwekeza kwenye miradi ya kimkakati?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; katika Jimbo la Manyoni Mashariki hatuna stendi ya mabasi. Sasa nini commitment ya Serikali kuhakikisha kwamba kwa kupitia huu mfumo itakuwa tayari kusaidia Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni kujenga stendi ya mabasi ili itumike kama kitega uchumi kwa halmashauri?

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Pius Stephen Chaya, Mbunge wa Manyoni Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na mwongozo mpya ilitokana na mapendeezo ambayo Mheshimiwa Mbunge amewasilisha. Kwa hiyo pale ambapo utakuwa umekamilika kwa kuzingatia haya mapendekezo ambayo ametupatia tutampatia. Hata hivyo, kwa huu mwongozo ambao tunaendelea nao na tunadhani mpaka sasa hivi haujaleta changamoto kubwa, ninao hapa na nitampatia baadaye.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili; niwapongeze kwanza yeye Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wake wa jimboni kwake kwa jitihada ambazo wameanzisha, lakini nimhakikishie kwamba kama ambavyo tumekuwa tukifanya siku zote kuhakikisha tunasaidia ujenzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika halmashauri zetu mbalimbali ikiwemo miradi ya stendi za mabasi, basi na jimbo lake na lenyewe tumelichukua tutaangalia tuingize katika mpango wetu wa utekelezaji pale tutakapofanya upembuzi wa kina kubaini kwamba ni utaratibu gani muafaka wa kuweza kuendelea na mradi huo na bajeti itakapokuwa imeruhusu.

Name

Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Primary Question

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kuhuisha vigezo vya mfumo wa miradi ya kimkakati kupitia maandiko ya miradi ili iweze kusaidia Halmashauri kubuni miradi ya kiuchumi?

Supplementary Question 2

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kuniona. Kwa kuwa suala la kujenga uwezo wa halmashauri na hasa katika miradi hii ya kimkakati linakwenda sambamba na suala la kuinua hali za wananchi kiuchumi ili waweze kushiriki vizuri katika miradi hii, nini hatua ya Serikali mpaka sasa katika kilio kikubwa cha wananchi cha kupunguza riba za mabenki?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Kilumbe Ng’enda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka hapa wakati wa mjadala wa bajeti, Mheshimiwa Kilumbe alikuwa miongoni mwa Waheshimiwa Wabunge ambao walilizungumzia sana tatizo hili la ukubwa wa riba katika mabenki yetu ya biashara. Muda mfupi Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan alitoa maelekezo kwa Serikali kuangalia jinsi gani ambavyo tutapunguza riba hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo basi, kama ambavyo nilikuwa nimeeleza jana wakati najibu swali, naomba nirudie kuwahakikishia kwamba yale maeneo matano ambayo Benki Kuu ya Tanzania iliyaainisha kuwa kama ni njia ya kuweza kufikia malengo hayo tayari yameshaanza kufanyiwa kazi. Kwa hiyo, nimthibitishie Mheshimiwa Kilumbe Ng’enda kwamba, wakati wowote kuanzia sasa mabenki kadhaa tayari yameshaanza kupeleka maombi yao kwenye Benki ya Tanzania kwa ajili ya kutumia fursa hizo zilizotolewa zenye dhamira ya kufikia malengo haya ya kuhakikisha kwamba riba inakuwa nafuu kwa kiwango kisichozidi asilimia kumi.

Name

Justin Lazaro Nyamoga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilolo

Primary Question

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kuhuisha vigezo vya mfumo wa miradi ya kimkakati kupitia maandiko ya miradi ili iweze kusaidia Halmashauri kubuni miradi ya kiuchumi?

Supplementary Question 3

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa moja kati ya vigezo vilivyopo katika mwongozo ni halmashauri iwe na hati safi kwa miaka mitatu mfululizo; na kwa kuwa kigezo hiki ni kandamizi kwa wananchi kwa sababu wanaosababisha hati kuwa chafu au safi siyo wananchi bali ni watumishi wa halmashauri.

Je, Serikali haioni kwamba hata kama kuna marekebisho yanafanywa kigezo hiki kiondolewe mara moja ili halmashauri zote zipate haki ya kuomba miradi hii ya kimkakati? (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Justin Nyamoga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inapoandaa miradi hii ya kimkakati moja katika dhamira zake kubwa ni kuhakikisha kwamba miradi hii inakuwa na tija kwa ujumla wake. Ndiyo maana miongoni mwa vigezo, ukiachilia mbali hicho ambacho Mheshimiwa Mbunge amekizungumza, ni kuangalia mtiririko mzima wa fedha katika mradi ili kuona kwamba mradi ule utaweza kujiendesha kwa faida na baadaye uweze kuwa na tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hati chafu inapokuja inatoa kiashiria hasi juu ya ufanisi wa mradi husika. Hata hivyo kwa kuwa jambo hili ni la kitaalam, naomba nilichukue halafu tukaiwasilishe hoja yake kwa wataalam, tuone jinsi gani inaweza ikafanyika bila kuathiri lengo halisi la kuona tija inapatikana katika mradi ule, lakini wakati huohuo isiathiri dhamira njema ya wananchi kwa makosa ambayo hayawahusu.