Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Hafidh Ali Tahir

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dimani

Primary Question

MHE. HAFIDH ALI TAHIR (K.n.y. MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN) aliuliza:- Suala la raia kupigwa na kuharibiwa mali zao kwa upande wa Zanzibar limekuwa likiongezeka siku hadi siku; Je, Serikali inatambua tatizo hili na kama inatambua inachukua hatua gani?

Supplementary Question 1

MHE. HAFIDH ALI TAHIR: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana pamoja ya kuwa sauti ilikuwa ndogo lakini nashukuru sana majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, amezungumzia suala la wakati wa kampeni.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa kampeni ya uchaguzi na baada ya uchaguzi kule Zanzibar nyumba ya Kamishna wa Polisi ilichomwa moto, lakini mikarafuu mingi kule kisiwani Pemba ilikatwa, mazao machanga nayo yaliharibiwa.
Je, Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na mambo yote yaliyotokea haya hivi sasa umechukua hatua gani ya kukomesha vitendo kama hivi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa sababu hivi sasa kuna mambo mengi yanatokea na kwa kuitikia wito wa Rais Magufuli ambaye amesema sasa hivi uchaguzi umekwisha tunataka maendeleo.
Je, utawachukulia hatua gani wale ambao watatekeleza ukorofi katika siasa badala ya kuleta maendeleo ndani ya Tanzania?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Hafidh Ali Tahir anataka kujua kwamba ni hatua gani zimechukuliwa dhidi ya watu ambao wamevunja sheria baada ya uchaguzi, akataja matukio mawili specifically, moja linahusu kurushwa bomu kwenye nyumba ya Kamishna na mambo ambayo yamekuwa yakijitokeza siku za karibuni ya ukataji mashamba ya mikarafuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimjulishe tu Mheshimiwa Hafidh Ali Tahir kwamba mpaka sasa hivi Polisi imeshafanya kazi ya kuwakamata watuhumiwa, mimi binafsi juzi nilifanya ziara na nilikuatana na Viongozi wa Polisi Zanzibar pamoja na Makamanda wa Polisi wa Mikoa ya Kusini na Kaskazini Pemba. Dhamira ya ziara ile ni kuweza baada ya kupata taarifa mbalimbali ambazo tumekuwa tukizipata kila siku juu ya hatua ambazo tunachukua, lakini kujionea wenyewe jinsi hatua hizo zilivyofikiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninachoweza kusema ni kwamba mpaka sasa hivi kuna watuhumiwa kadhaa wameshakamatwa na katika watuhumiwa waliokamatwa ni matukio mawili ambayo yamefikishwa Mahakamani, matukio mengine bado kesi zao zipo kwa DPP. Nilijaribu kutoa wito kwa DPP kuweza kufanya kazi kwa karibu kabisa na Polisi ili kuharakisha kesi hizo ili watu hao waweze kuchukuliwa hatua kali za kisheria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na swali lake la pili ambapo alitaka kujua kwamba baada ya kauli ambayo ameizungumza Mheshimiwa Rais, nataka nisisitize kwamba Jeshi la Polisi ndiyo chombo pekee chenye dhamana ya kuweza kutathmini hali ya usalama katika nchi yetu. Kama ambavyo imefanya kupitia Kamishna wake wa operation walitoa agizo kwamba kulingana na hali ya usalama nchini wamezuia mikutano ya kisiasa. Nataka nitoe wito tu kwamba wananchi ama vyama vya siasa vitii agizo hilo la Polisi, kama kuna yeyote ambaye hatii agizo hilo basi sheria ichukue mkono wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumewahi kuzungumza mara nyingi hapa kwamba hakuna mtu ambaye yuko juu ya sheria, kwa hiyo basi tunataka na mamlaka husika, kwa maana ya kwamba viongozi wa Jeshi la Polisi wa ngazi za chini wahakikishe kwamba wanatekeleza maelekezo ya ngazi za juu. Kwa hiyo, watu ambao wanahusika kutoka vyama vya siasa watii sheria hiyo, lakini watu ambao wanapaswa kuisimamia sheria hiyo waisimamie ipasavyo katika maeneo yote ya nchi yetu ikiwemo Pemba, Zanzibar na maeneo ya Tanzania Bara mpaka pale mamlaka husika ama Jeshi la Polisi watakapoamua vinginevyo kwa mujibu wa taarifa zao za ki-intelijensia na taratibu zao za kazi na utaalam ambao wanao.

Name

Maida Hamad Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HAFIDH ALI TAHIR (K.n.y. MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN) aliuliza:- Suala la raia kupigwa na kuharibiwa mali zao kwa upande wa Zanzibar limekuwa likiongezeka siku hadi siku; Je, Serikali inatambua tatizo hili na kama inatambua inachukua hatua gani?

Supplementary Question 2

MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa, Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba watachukuliwa hatua kali za kisheria wale wote walioshiriki vitendo hivi, lakini pia kuna wengine ambao tayari sasa hivi wameshakamatwa, yaani watuhumiwa wameshakamatwa, je, Serikali itakubaliana nami kwamba baada ya kugundulika watu hawa waliofanya vitendo hivi kwa raia wa Zanzibar, Serikali iko tayari pamoja na hatua kali zitakazochukuliwa za kisheria, iko tayari kuwataka walipe fidia kwa wale wote waliowafanyiwa vitendo hivi?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na uamuzi wa hatua gani za kuchukua baada ya kubainika na makosa ni maamuzi ya Mahakama. Kwa hiyo, pale ambapo Mahakama itaamua kulingana na sheria za nchi yetu basi nadhani ndivyo ambavyo inapaswa kutekelezwa. Siyo jukumu la Jeshi la Polisi kuamua hukumu gani ambayo watuhumiwa hawa wachukuliwe.

Name

Munira Mustafa Khatib

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HAFIDH ALI TAHIR (K.n.y. MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN) aliuliza:- Suala la raia kupigwa na kuharibiwa mali zao kwa upande wa Zanzibar limekuwa likiongezeka siku hadi siku; Je, Serikali inatambua tatizo hili na kama inatambua inachukua hatua gani?

Supplementary Question 3

MHE. MUNIRA MUSTAFA KHATIBU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa wanaoathirika zaidi ni wanachama wa CCM kwa kule Pemba; Je, Serikali haioni umuhimu wa chama hiki cha CUF kukifutia usajili na kuweza kupata amani ndani ya Tanzania yetu?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kwa upande wa Pemba matukio haya, wakati wa uchaguzi wa marudio na baada ya uchaguzi kumalizika, Pemba kulikuwa na amani, ambapo mpaka sasa hivi amani ipo. Matukio haya ya kihalifu ya kukatakata mikarafuu na kufanya mambo mengine ya hovyo zaidi yalijitokeza baada ya viongozi wa CUF, kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge alivyosema, kufanya ziara kule Pemba. Ndiyo maana nikasisitiza kwa Jeshi la Polisi kuhakikisha kwamba wanachukua sheria kali kwa Kiongozi yeyote wa chama chochote kiwe cha CUF au chama kingine ambacho kinahatarisha ama kinachochea amani ya nchi yetu.
Kuhusiana na suala la kukifutia usajili chama hiki nadhani hayo ni mamlaka ya Msajili wa Vyama vya Siasa kuona kama kuna haja hiyo kulingana na taratibu na sheria za nchi yetu zilivyo. Si jukumu la Serikali ama Jeshi la Polisi kuamua.

Name

Tauhida Cassian Gallos Nyimbo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HAFIDH ALI TAHIR (K.n.y. MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN) aliuliza:- Suala la raia kupigwa na kuharibiwa mali zao kwa upande wa Zanzibar limekuwa likiongezeka siku hadi siku; Je, Serikali inatambua tatizo hili na kama inatambua inachukua hatua gani?

Supplementary Question 4

MHE. TAUHIDA CASSIAN GALOSS NYIMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii ya kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa, toka tumalize Uchaguzi Mkuu Zanzibar imekuwa na baadhi ya watu wakitoa kauli za vitisho, hususan wakati huu wa sikukuu wanatoa kauli za vitisho kupitia mitandao ya kijamii;
Je, Serikali inawaambia nini wananchi wa Zanzibar, hususan vijana na watoto ambao wanatarajia kusherehekea sikukuu ya Eid al-Fitr.(

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inachoweza kuwaeleza wananchi wa Zanzibar na Watanzania kwa ujumla ni kwamba wasiwe na wasiwasi wowote, nchi yetu iko salama na itaendelea kuwa salama. Ninyi ni mashahidi kwa kazi nzuri ambayo imekuwa ikifanywa na Jeshi la Polisi. Kwa matukio ya hivi karibuni jana na juzi mmejionea. Pia kwa upande wa Zanzibar juu ya hawa watu ambao wanajaribu kutaka kutuletea mrafaruku katika nchi yetu, tumewadhibiti. Nataka nitoe tu wito kwa wananchi kuacha kukubali kuchochewa na baadhi ya wanasiasa, wahakikishe kwamba wanaendelea kufuata sheria za nchi yetu, yeyote ambaye atakiuka sheria hiyo kama ambavyo tumekuwa tukizungumza kila siku, kwamba ikiwa ni mwanachama wa chama cha siasa, ikiwa ni kiongozi basi hatua kali za kisheria zitachukuliwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nisisitize tu kwamba wananchi wasiwe na wasiwasi, waendelee kusherehekea siku ya Eid-al-Fitr bila wasiwasi wowote. Serikali yao ipo itaendelea kuwalinda wao pamoja na mali zao.