Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Primary Question

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kuimarisha biashara kupitia Diplomasia ya Uchumi kati ya Tanzania na Malawi kwa kutumia meli ya MV Mbeya II?

Supplementary Question 1

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Kwa kuwa imethibitika kwamba Wilaya ambazo ziko mpakani zinanufaika sana kupitia biashara na majirani zao wa nje, na kwa kuwa katika Wilaya ya Nyasa, kwanza kuna uasilia wa kindugu lakini vilevile kuna changamoto kubwa za kukuza biashara na Malawi ingekuwa ni mkombozi mkubwa.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mheshimiwa Waziri ameonesha kuwa na uwezo mkubwa wa kidiplomasia kwa jinsi ambavyo amenijibu swali langu, namshukuru sana, je, Waziri una mpango gani wa kwenda kuongeza nguvu ya kupeleka ushawishi katika nchi ya Malawi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa…

SPIKA: Ushawishi wa nini?

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ushawishi wa kuhakikisha kwamba suala hilo ambalo tumelizungumzia la kibiashara linafanyika kwa kutumia meli na nyenzo nyingine.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ninapenda pia kumualika Mheshimiwa Waziri au Naibu Waziri kuja Wilaya ya Nyasa ili kuwafahamu wananchi wa kule na shughuli wanazozifanya na kuona namna bora zaidi ya kukamilisha kushughulikia suala hili la kibiashara. (Makofi)

Name

Amber. Mbarouk Nassor Mbarouk

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Engineer Stella Manyanya, Mbunge wa Nyasa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki itafanya kila jitihada kwa kushirikiana na mamlaka husika nchini Malawi ili kuwezesha meli ya MV Mbeya II ianze safari zake kati ya Malawi na Tanzania pale taratibu zote zitakapokamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili ambao ni mwaliko, naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba nitakuwa tayari, kwa idhini yako, kufanya safari hiyo ili kuona fursa mbalimbali ambazo ziko katika Wilaya ya Nyasa. Ahsante sana. (Makofi)