Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 59 East African Co-operation and International Affairs Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 497 2021-06-25

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Primary Question

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuimarisha biashara kupitia Diplomasia ya Uchumi kati ya Tanzania na Malawi kwa kutumia meli ya MV Mbeya II?

Name

Amber. Mbarouk Nassor Mbarouk

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mhandisi Stella Martin Manyanya, Mbunge wa Nyasa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, meli ya MV Mbeya II yenye uwezo wa kubeba abiria 200 na tani 200 za mizigo ilizinduliwa rasmi na Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tarehe 5 Januari, 2021. Meli hii kwa sasa inafanya safari kati ya Bandari za Tanzania tu za Kyela na Mbambabay.

Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa Sera ya Diplomasia ya Uchumi ni miongoni mwa majukumu makubwa ya Wizara yangu. Kutokana na umuhimu mkubwa wa kukuza biashara kati ya Tanzania na Malawi na katika kuhakikisha kuwa meli ya MV Mbeya II inatumika ipasavyo, Ubalozi wa Tanzania nchini Malawi, ukishirikiana na Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) imeanza mawasiliano na Serikali ya Malawi na taasisi zake kupitia Wizara ya Mambo ya Nje ya Malawi ili kuweka mazingira mazuri ya kuwezesha MV Mbeya II kufanya safari zake nchini Malawi.

Mheshimiwa Spika, ubalozi wetu uliopo Lilongwe, Malawi pia unafuatilia kwa karibu kufikia makubaliano (MoU) baina ya Serikali ya Tanzania na Malawi kuhusiana na uanzishaji wa Ofisi za TPA mjini Lilongwe ambazi zitasimamia utekelezaji na uendeshaji wa shughuli zote za kibiashara zinazotumia huduma za bandari za Tanzania. Hii inatokana na maazimio ya Marais wa Tanzania na Malawi wakati wa ziara ya Mheshimiwa Rais wa Malawi nchini Tanzania iliyofanyika tarehe 7 - 8 Oktoba, 2020.

Mheshimiwa Spika, kukamilika kwa taratibu hizo na kukamilika kwa kipindi cha majaribio ya meli hiyo na hivyo kuanza safari zake nchini Malawi, ni dhahiri kuwa biashara kati ya Tanzania na Malawi kwa kutumia Ziwa Nyasa itaimarika. Ahsante sana.