Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Ali Hassan Omar King

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Jang'ombe

Primary Question

MHE. ALI HASSAN OMAR KING aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kufungua Ofisi Ndogo ya Hazina Zanzibar kama ilivyo kwa taasisi nyingine za Muungano ili kurahisisha huduma kwa wastaafu wa Jamhuri ya Muungano wanaoishi Zanzibar?

Supplementary Question 1

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, ahsante; humu mna jibu hakuna jawabu, kwa sababu nilichoomba kwamba ni lini Serikali itafungua Ofisi ya Hazina Ndogo lakini jibu lililokuwemo humu wamesema watafanya mashirikiano na Wizara ya Fedha ya Zanzibar kitu ambacho hakiwezekani kwamba taarifa za Serikali ya Jamhuri ya Muungano zikawepo katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Hawa wazee taarifa zao zipo Wizara ya Fedha ya Muungano, wanapokuwa na matatizo wanakwenda Dar es Salaam na wanachukua muda mwingi hadi wengine wanasamehe mafao yao. (Makofi)

Sasa nataka jawabu Serikali ina mpango gani wa kuwa na ofisi kama ilivyokuwa ofisi nyingine? Mpango wa kuwa na ofisi, hilo lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, je, hawa wazee wanaokuja mpaka wakakata tamaa wakarudi wakasamehe mafao yao Serikali itachukua hatua gani?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ali Omar Hassan King, Mbunge wa Jang’ombe kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza hatujapokea malalamiko ambayo yanaonesha kuna usumbufu wa malipo ya wastaafu kupitia utaratibu ambao tunao sasa hivi wa kushirikiana kati ya Wizara za Fedha za pande mbili za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hivyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge kama ana malalamiko mahususi ambayo pengine hayajatufikia sisi, basi ayawasilishe tutayashughulikia haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na lini tutajenga ofisi, masuala ya ujenzi wa ofisi ni masuala ambayo yanahitaji bajeti na uwezo wa kifedha na maandalizi. Kwa hiyo, kutoa kauli hasa ni lini kwa sasa hivi inaweza ikawa sio rahisi sana hata hivyo Mheshimiwa Mbunge nimhakikishie kwamba kwa sababu ofisi hizi ndogo zilizopo mikoani kwa upande wa Tanzania Bara ambazo zimejengwa huwa zinafanya kazi kwa mujibu wa Sheria ya Fedha ya Umma na Kanuni zake ambayo pamoja na mambo mengine, zinahudumia Ofisi za Makatibu Tawala wa Mikoa pamoja na Idara za Serikali ya Muungano ambazo kwa upande wa Zanzibar Ofisi za Tawala za Miko ana hizi Idara za Serikali shughuli zake zinafanywa na Wizara ya Fedha ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. Kwa hiyo, shughuli zile hazijakwama kwa upande wa Zanzibar kwa sababu zinasimamiwa na Wizara ya Fedha ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ambayo sio masuala ya Muungano.

Mheshimiwa Spika, zipo taasisi ambazo tayari zimeshajengwa majengo huko kama BOT na TRA zina Ofisi Zanzibar, kwa hiyo, masuala mengine ya ujenzi wa miundombinu ni masuala ambayo hayaendi kwa wakati mmoja, yanakwenda hatua kwa hatua.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba concern yake Serikali tunaitambua na pale ambapo hali itaruhusu basi tutakamilisha utaratibu huu ambao amependekeza.