Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Flatei Gregory Massay

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Vijijini

Primary Question

MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Chuo cha VETA katika Jimbo la Mbulu Vijijini ili vijana wapate ujuzi?

Supplementary Question 1

MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Elimu, kutoka Mbulu Vijijini sehemu ya Haydom kwenye Mbulu Mjini ni kilometa 90 na kwenda Babati ni zaidi ya kilometa 130. Kwa majibu yake haoni kwamba atakuwa amewaondolea fursa vijana wa Mbulu Vijijini kupata uzoefu na ufundi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Mbulu Vijijini hatuna kabisa chuo, je, yuko tayari kutenga fedha sasa ili bajeti ijayo tuweze kupata chuo katika Jimbo la Mbulu Vijijini? (Makofi)

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Flatei, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kutoka Mbulu Mjini mpaka Mbulu Vijijini ni kilometa 90 lakini kama nilivyojibu katika swali langu la msingi kwamba Serikali inafanya juhudi mbalimbali za kutafuta fedha ili kuendelea na mpango wake wa ujenzi wa vyuo hivi vya VETA katika kila wilaya na mkoa. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itakapopata tu fedha tutahakikisha kwamba maeneo yote ikiwemo na Mbulu Vijijini yatajengewa vyuo hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivi sasa naomba kumtaarifu Mheshimiwa Mbunge kuwa tuna vyuo vingi ambavyo viko katika Wilaya ile ya Mbulu kiujumla. Tuna Vyuo vya Ufundi Stadi Mbulu, Haydom, Masieda, Jiendeleze, Integrity na St. Jude Yuda Thadei. Vyuo hivi vyote vinaweza kutumika kwa ajili ya vijana wetu kupata uzoefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, vyuo nilivyovitaja mwanzo vile vya Manyara vina nafasi ya wanafunzi kulala pale pale chuoni. Kwa hiyo, wanafunzi wetu hawa wanaotoka mbali wanaweza kupata fursa ya kupata ujuzi wao pale na kuondoa usumbufu huu wa kutembea au kwenda umbali mrefu.

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Primary Question

MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Chuo cha VETA katika Jimbo la Mbulu Vijijini ili vijana wapate ujuzi?

Supplementary Question 2

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na shukrani nyingi kwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, napenda kufahamu juu ya Chuo cha VETA ambacho kimejengwa Wilayani Nyasa. Nafahamu kimeshafikia zaidi ya asilimia 95, ni nini mpango wa Serikali kuanza kutoa mafunzo ili vijana waweze kunufaika na chuo hicho?

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Tunafahamu kwamba vyuo hivi ambavyo tayari ujenzi wake umekamilika, tuko katika mpango wa kuanza kutoa mafunzo mara moja. Suala lililokuweko mbele yetu sasa ni kuhakikisha kwamba tuna vifaa kwa ajili ya kufundishia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tuko kwenye mchakato wa manunuzi ya vifaa hivyo na pindi tu manunuzi hayo yatakapokamilika, program zile za ufundishaji katika maeneo haya zitaanza mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.