Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZAYTUN S. SWAI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kupima na kuchimba visima virefu Mkoani Arusha hasa Wilaya ya Longido katika Vijiji vya Noondoto, Matale, Wosiwosi na Ngereani ambapo kuna uhaba wa vyanzo vya maji safi na salama?

Supplementary Question 1

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali madogo ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, leo hii ukienda Longido kwenye vijiji vya Noondoto, Matale, Wosiwosi na Ngereani, utalia kwa jinsi wananchi wanavyopata shida ya maji na hususan akina mama; wanalazimika kutembea umbali mrefu wa zaidi ya kilomita 10 kutafuta maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile, akina mama hawa mara nyingine wanalazimika kwenda kulala kwenye vyanzo vya maji kusubiria maji yanayochuruzika. Swali langu kwa Serikali: Je. Waziri yuko tayari kwenda Longido kuona hali halisi ya maeneo haya? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kwa kuwa changamoto ya Wilaya ya Longido linafanana kabisa na changamoto walizonazo akina mama wa Monduli hususan kwenye Kata za Moita, Lekruko na Naalarami: Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia akina mama wa Monduli haki yao ya msingi ya kupata maji safi na salama? Nakushukuru. (Makofi)

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

MHE. NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa kufika Longido ni moja ya majukumu yangu na tayari maeneo yale nilishatembelea nikiwa na Mbunge wa Jimbo na nimeshawasiliana naye kwa kirefu sana. Hata hivyo nitajitahidi kufika tena kuona namna gani tutaendelea kusaidiana na wananchi waweze kupata maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, mipango ya Wizara ni kuhakikisha maeneo yote yanafikiwa na maji bombani. Tupo kwenye mkakati kabambe wa kuhakikisha kwamba maeneo yote ambayo yamekuwa na matatizo ya vyanzo rahisi kama chemchemi, basi visima vinaendelea kuchimbwa na tayari Wizara wataalam wake wako huko wanaendelea, hata sasa hivi hapo Chemba tayari visima vinachimbwa na maeneo mbalimbali katika Majimbo yote.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, namwondoa hofu Mheshimiwa Mbunge, akina mama tuna lengo jema la kuhakikisha tunawatua ndoo kichwani; Wizara tuna lengo jema kuhakikisha tunaokoa ndoa hizi ambazo akina mama wanalala kwenye vyanzo vya maji; tunahitaji akina mama walale nyumbani na familia zao. (Makofi)

Name

Catherine Valentine Magige

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZAYTUN S. SWAI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kupima na kuchimba visima virefu Mkoani Arusha hasa Wilaya ya Longido katika Vijiji vya Noondoto, Matale, Wosiwosi na Ngereani ambapo kuna uhaba wa vyanzo vya maji safi na salama?

Supplementary Question 2

MHE. CATHERINE MAGIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza tunaishukuru Serikali kwa mradi mkubwa wa maji wa shilingi bilioni 520 katika Jiji la Arusha. Mradi huu changamoto yake kubwa unapita katika maeneo ya mjini, lakini maeneo ya pembezoni kwenye Kata kama Olmoti, baadhi ya sehemu za Muriet, Moshono na Olasiti hazifiki. Je. Serikali haioni sasa kuna umuhimu mkubwa wa mradi huu wa maji kuhakikisha unapita katika Kata za pembezoni mwa Jiji la Arusha? (Makofi)

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mji wa Arusha una bahati kubwa sana, kwa sababu una mradi wenye fedha nyingi sana na ni mradi ambao tunautarajia umalize kero ya maji katika Jiji la Arusha. Katika maeneo haya aliyoyataja, ni jana tu nimekuwa nikiongea na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Arusha, aliyeongozana na timu iliyotoka kule ikiwa pamoja na Mheshimiwa Diwani Miriam, tayari nimeshafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, maeneo ambayo yako pembezoni, wenzetu wa Mamlaka ya Maji ya Arusha, pale tayari na wenyewe wanaendelea kuweka mikakati mbalimbali ya kuona namna bora ya kuendelea kutanua mitandao ya mabomba kuwafikia wananchi. Hili nalo tutalisimamia kwa karibu kabisa kuhakikisha maeneo yote ya pembezoni, Mamlaka pamoja na RUWASA wanawajibika ili maji yaweze kuwafikia wananchi. (Makofi)

Name

Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Primary Question

MHE. ZAYTUN S. SWAI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kupima na kuchimba visima virefu Mkoani Arusha hasa Wilaya ya Longido katika Vijiji vya Noondoto, Matale, Wosiwosi na Ngereani ambapo kuna uhaba wa vyanzo vya maji safi na salama?

Supplementary Question 3

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona. Nitumie fursa hii kumwomba Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba maji ya Ngaresero hayataweza kufika katika Wilaya ya Longido, kwa hiyo, nafikiri kuna haja ya kurekebisha hapo. Hata hivyo, nashukuru kwa jitihada ambazo Serikali inaenda kufanya katika kutupatia maji kwa gharama yoyote, iwe ni mabwawa au chemichemi ama chanzo chochote cha maji salama katika eneo la Wilaya ya Longido.

Mheshimiwa Spika, naomba tu kutumia fursa hii kuikumbusha Serikali kwamba, kuna ahadi ambayo imerudiwa tena na tena ya kutoa tawi la maji ya Mto Simba ambayo yamekwenda mpaka Mjini Longido na sasa hivi yanaelekea Namanga. Naiomba sana Serikali Kijiji cha Eilarai eneo la Motong’ wapate maji maana ni Kijiji cha kwanza kilichopitiwa na bomba hilo kubwa na wananchi wale wameendelea kunikumbusha kwamba ahadi imetolewa na Mawaziri watatu hadi sasa; Mheshimiwa Waziri Mbarawa, Mheshimiwa Waziri Kamwelwe na huyu aliyeko sasa hivi wakati ule akiwa Naibu Waziri. Kwa hiyo, ni lini Serikali itakwenda kuwapelekea watu wa Imotong’ maji safi na salama ya Mto Simba?

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kuhusu maji ya Mto Simba, ni mpango mkakati wa Wizara kwenda kutumia mito, maziwa na vyanzo vyote vya maji kuhakikisha maeneo yote tunayafikia. Kwa upande wa Longido, Mheshimiwa Mbunge tuna mpango wa kuendelea kuona chanzo hiki cha maji cha Mto Simba kinakwenda kutumika katika mwaka wa ujao wa fedha.