Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 8 Water and Irrigation Wizara ya Maji 63 2021-04-13

Name

Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZAYTUN S. SWAI aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kupima na kuchimba visima virefu Mkoani Arusha hasa Wilaya ya Longido katika Vijiji vya Noondoto, Matale, Wosiwosi na Ngereani ambapo kuna uhaba wa vyanzo vya maji safi na salama?

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zaytun Seif Swai, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kutokana na Wilaya ya Longido kuwa na uhaba wa vyanzo vya maji hasa chemichemi, Serikali imeendelea na jitihada mbalimbali ikiwemo kufanya utafiti wa maji chini ya ardhi na kuchimba visima virefu, ambapo katika Kijiji cha Matale B, uchimbaji wa kisima unaendelea kupitia Bajeti ya mwaka 2020/2021 na unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Juni, 2021.

Mheshimiwa Spika, Kijiji cha Noondoto, kinapata huduma ya maji kupitia mradi wa maji wa Kijiji cha Elang’atadabash unaohudumia vijiji vitano vya Elang’atadabash, Sokoni, Olchonyorokie, Noondoto, Losirwa na Naadare. Katika Kijiji cha Wosiwosi kisima kilichochimbwa, maji yake yalibainika kutofaa kwa matumizi ya binadamu kutokana na kuwa na kiwango kikubwa cha madini chumvi ukilinganisha na kiwango kinachokubalika.

Mheshimiwa Spika, hivyo, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali itatumia vyanzo vya Mto Engaresero kutekeleza mradi wa kufikisha maji Kijiji cha Matale na Wosiwosi. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 kwa ajili ya kijiji cha Wosiwosi, tumeweka bajeti ya kujenga bwawa litakalosaidia mifugo na wananchi.

Mheshimiwa Spika, Kijiji cha Ngereani kinapata huduma ya maji kupitia Mradi wa Maji Tingatinga Ngereani. Serikali itaendelea na jitihada mbalimbali za kuhakikisha wananchi wa Wilaya ya Longido wanapata huduma ya maji safi na salama kwa kutumia vyanzo mbalimbali vitakavyoonekana vinafaa ikiwemo mito, visima na mabwawa.