Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Jonas Van Zeeland

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mvomero

Primary Question

MHE. JONAS V. ZEELAND: Aliuliza:- Je, ni lini Serikali itaondoa wanyama wakali hasa tembo katika Tarafa ya Mlali na kuwarudisha kwenye Hifadhi ya Taifa Mikumi kwa kuwa wamekuwa kero kwa wananchi?

Supplementary Question 1

MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na niishukuru Serikali kwa majibu mazuri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, kwa kuwa tuna vijiji ambavyo vimepakana moja kwa moja na Hifadhi ya Mikumi. Je, Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kuweka kila kijiji angalau kuwe na game ambaye ataweza kuzuia tembo mara tu anapotoka kwenye hifadhi na kutaka kuingia kwa wananchi?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la pili, kwa kuwa tuna wananchi zaidi ya 28 wameshapoteza maisha kwa sababu ya tembo, lakini wananchi zaidi ya 2,000 mazao yao yameharibiwa na tembo.

Je, ni lini sasa Serikali itaenda angalau kuwafuta machozi na kuwafuta jasho kwa kupata uharibifu na tembo katika Wilaya yetu hii ya Mvomero? Ahsante.

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jonas Van Zeeland, Mbunge wa Mvomero kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge ameomba kuwepo na askari maalum kwa ajili ya kuweka usalama wa wananchi wanaozunguka maeneo ya hifadhi vikiwemo vijiji ambavyo amevielezea, nimuahidi tu Mbunge kwamba Serikali inatambua changamoto hii na ndio maana tumekuwa tukitoa ushirikiano wa karibu sana na wananchi kuhakikisha kwamba wananchi wanalindwa na mali zao pia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuombe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba atuvumilie lakini tutaandaa eneo maalum kwa ajili ya kuweka askari game ambao watakuwa standby kwa ajili ya kufanya patrol katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tuna upungufu wa askari kwa maana ya kuweka kila Kijiji, nimuombe aendelee kutuvumilia, lakini tutahakikisha tunaimarisha eneo lile ili wanyama wakali na waharibifu wasiendelee kuvamia wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kifuta machozi nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge hili Tukufu nitazunguka kwenye maeneo yote ambayo hayajapata kifuta machozi. Nimuahidi kwamba nitalisimamia zoezi hili mimi mwenyewe kuhakikisha kwamba wananchi wanalipwa kwa wakati. Ahsante. (Makofi)