Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 4 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 53 2021-09-03

Name

Jonas Van Zeeland

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mvomero

Primary Question

MHE. JONAS V. ZEELAND: Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaondoa wanyama wakali hasa tembo katika Tarafa ya Mlali na kuwarudisha kwenye Hifadhi ya Taifa Mikumi kwa kuwa wamekuwa kero kwa wananchi?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jonas Van Zeeland, Mbunge wa Mvomero, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kutoa pole kwa wananchi wote wanaokutana na changamoto ya wanyamapori wakali na waharibifu hususan tembo. Wizara imeendelea kudhibiti wanyamapori hawa katika Wilaya ya Mvomero, Mkoani Morogoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jitihada za kukabiliana na matukio haya, Wizara kwa kushirikiana na viongozi wa Mkoa iliweka mkakati wa pamoja ambapo kutakuwa na vikosi maalum vya kudhibiti tembo. Vikosi hivyo vimeendelea kutoa msaada wa haraka pale inapotokea tatizo katika Mkoa wa Morogoro na maeneo mengine ikiwemo Wilaya ya Mvomero. Vikosi hivyo vimewezeshwa kwa kupatiwa vitendea kazi muhimu vinavyohitajika katika zoezi la kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu. Vifaa hivyo ni pamoja na magari, risasi za moto, risasi baridi na mabomu maalum ya kufukuzia wanyamapori hususan tembo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na jitihada hizo, Wizara imenunua na kusambaza simu zenye namba maalum katika maeneo 14 nchini kwa ajili ya kuhakikisha wananchi wanatoa taarifa za matukio ya wanyamapori wakali na waharibifu, kwa haraka bila malipo na kwa wakati ili ziweze kushughulikiwa mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)