Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Deodatus Philip Mwanyika

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Primary Question

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA Aliuliza:- Je, Serikali inachukua hatua gani kumaliza tatizo la upungufu wa Walimu nchini, hasa shule zilizopo maeneo ya vijijini?

Supplementary Question 1

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya swali la msingi lakini niulize swali la kwanza. Kwanza tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa maamuzi aliyoyatoa siku ya Jumatatu ya kuruhusu kuajiriwa kwa walimu 6,000 kwa haraka, tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ni ukweli kwamba walimu 6,000 wanaokwenda kuajiriwa bado wanakwenda kufanya replacement; mahitaji ya walimu katika shule bado ni makubwa sana. Maamuzi ya Serikali ya kutoa elimu bure kwa nia njema yamefanya kuwe na uhaba mkubwa sana wa walimu katika maeneo hasa ya vijijini. Kwa hiyo, pamoja na mipango ambayo imeelezewa lakini bado kuna tatizo kubwa na ninapenda kujua, je, Serikali inaweza bado ikatoa commitment kwamba itaajiri walimu wa kutosha? Kwasababu hii namba iliyotajwa hapa bado haitoshi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; naelewa kuna vigezo ambavyo vinatumika kwenye ugawaji wa walimu kwenye maeneo mbalimbali. Ni ukweli usiopingika kwamba kwa yale maeneo ambayo ni miji ambayo iko ndani ya halmashauri vigezo ambavyo vinatumika kwa kweli havina uhalisia kwasababu maeneo hayo unakuta yanaangaliwa sana kwasababu yana miji lakini vilevile yana maeneo mengi sana yenye shule nyingi sana ambayo wananchi wamejitoa wakajenga shule ambazo zipo katika maeneo ya vijijini. Wanapoangalia vigezo vya reallocation unakuta kwamba hawaangalii hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa swali; je, Wizara itakuwa tayari kupitia upya vigezo vya ku-allocate walimu ili maeneo ya halmashauri za miji ambayo yana maeneo makubwa ya zaidi ya kilometa 25 yaweze kupata walimu ili elimu yetu iwe na tija? Ahsante. (Makofi)

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikiri wazi kabisa kwamba alichozungumza Mheshimiwa Mbunge ya uhaba wa walimu nchini pamoja na replacement ya walimu 6,000 ambayo tunakwenda kuifanya hivi karibuni bado upo. Na Serikali imeji-commit hapa katika statement yangu ya awali kwamba tutaendelea kuajiri kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Na mpango huo upo na ni endelevu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge ondoa wasiwasi kwenye hilo kwa sababu Serikali iko makini, na Serikali ya Rais wa Sita, mama Samia Hassan Suluhu, imejipanga kuhakikisha tunaondoa kabisa tatizo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, amezungumzia kuhusu Wizara kama tutakuwa tayari kupitia vigezo vya ugawaji wa walimu upya. Nikubali kabisa hilo tumelipokea, moja, ni kama ushauri, lakini pili, tutaendelea kulizingatia kuhakikisha kabisa ugawanyaji wa walimu wote nchini unafuata usawa na haki katika maeneo yote. Ahsante sana.

Name

Masache Njelu Kasaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupa

Primary Question

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA Aliuliza:- Je, Serikali inachukua hatua gani kumaliza tatizo la upungufu wa Walimu nchini, hasa shule zilizopo maeneo ya vijijini?

Supplementary Question 2

MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Tatizo ambalo linaikumba Njombe Mjini la uhaba wa walimu, ndilo tatizo hilohilo ambalo linaikumba Wilaya ya Chunya kwa uhaba wa walimu. Ajira mara ya mwisho iliyopita Wilaya ya Chunya tulipata takribani walimu 26 tu ambao ni idadi ndogo ukilinganisha na ukubwa wa Wilaya ya Chunya.

Je, Serikali inatuhakikishia vipi kwamba kwenye awamu hii ya ajira itakayokuja tutapata walimu wa kutosha, hasa maeneo ya vijijini, ili kuweza kukidhi mahitaji ya watu wa Wilaya ya Chunya? Ahsante.

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, moja, nikubaliane na yeye kwamba kweli hata Chunya nakufahamu vizuri. Eneo ni kubwa na kuna idadi ndogo sana ya walimu. Lakini kwa sababu ameleta hapa ombi na sisi kama Serikali kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumelipokea hilo ombi na katika mgawanyo wa walimu 6,000 tutalizingatia hilo. Ahsante sana.

Name

Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Primary Question

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA Aliuliza:- Je, Serikali inachukua hatua gani kumaliza tatizo la upungufu wa Walimu nchini, hasa shule zilizopo maeneo ya vijijini?

Supplementary Question 3

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kumekuwa na tatizo kubwa la walimu katika nchi nzima, na kuna walimu ambao wanajitolea kufanya kazi za kufundisha katika maeneo mbalimbali nchini, zinapojitokeza ajira walimu hawa hawapewi nafasi; je, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha walimu wanaojitolea wanapewa kipaumbele pale nafasi zinapotoka? (Makofi)

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya vigezo ambavyo sasa hivi Serikali imekuwa ikitumia katika kuajiri walimu ni pamoja na kuzingatia walimu wote ambao wamejitolea kwa muda mrefu katika shule wanazofundisha. Kwa hiyo, hata katika hizi nafasi 6,000 ambazo tunakwenda kuzijaza zitazingatia vigezo hivyo. Na tumetoa maelekezo kwa maafisa elimu wote ngazi za wilaya kuleta taarifa za walimu wote wanaojitolea katika shule zao ili tuweze kuwazingatia katika ajira mpya. Ahsante sana. (Makofi)

Name

Rose Cyprian Tweve

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA Aliuliza:- Je, Serikali inachukua hatua gani kumaliza tatizo la upungufu wa Walimu nchini, hasa shule zilizopo maeneo ya vijijini?

Supplementary Question 4

MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Mheshimiwa Naibu Waziri katika majibu yako ya msingi ameonesha kabisa changamoto ya walimu pamoja na kuajiri hawa waliopo bado changamoto itakuwepo, hasa kwenye walimu wetu wa sayansi. Na technology inakua, hasa matumizi yetu ya simu. Sasa kama Serikali, mna mkakati gani wa kuhakikisha sasa tuna-link, hasa zile shle zilizopo vijijini tukatumia hii mitandao ili wakawa na access ya wale walimu wanaofundisha wenzao mjini wapate elimu sawa na kule vijijini? Nakushukuru sana.

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa kwamba kwenye masuala haya ya TEHAMA bado kuna changamoto kubwa sana hususan vijijini, na hata kwenye mitandao ya simu sisi wote ni mashuhuda kabisa kwamba networking ya mjini na vijijini ni tofauti kabisa. Lakini sasa hivi Serikali tuna mitandao, tuna mfumo ambao unawezesha walimu wa vijijini na mijini kuwa na access iliyo sawa. Kwa hiyo, pamoja na kwamba ameleta kama moja ya mapendekezo ama maoni na ushauri, basi sisi tutalipokea na moja ya kazi kubwa tutakazozifanya ni kuboresha mifumo iliyopo ili kuondoa hii changamoto ambayo ipo kwa sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.