Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 6 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 38 2021-04-09

Name

Deodatus Philip Mwanyika

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Primary Question

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA Aliuliza:-

Je, Serikali inachukua hatua gani kumaliza tatizo la upungufu wa Walimu nchini, hasa shule zilizopo maeneo ya vijijini?

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deodatus Phillip Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kukabiliana na changamoto ya uhaba wa walimu katika shule za msingi na sekondari, kuanzia Disemba 2015 hadi Septemba 2020, Serikali imeajiri walimu 10,666 wa shule za msingi na walimu 7,515 wa shule za sekondari na kuwapanga kwenye maeneo yenye uhitaji mkubwa. Aidha, kuanzia mwezi Desemba 2015 hadi Septemba 2020, Halmashauri ya Mji Njombe imeajiri walimu 21 wa shule za msingi na walimu 111 wa shule za sekondari. Vilevile Ofisi ya Rais-TAMISEMI kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais-Utumishi na Utawala Bora na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia itaajiri walimu wapya 6,000 wa shule za msingi na sekondari ifikapo Juni 2021 ili kujaza nafasi zilizoachwa na walimu waliofariki ama kustaafu kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, kupitia ofisi za wakuu wa mikoa imekuwa ikifanya uhamisho wa ndani kwa kuwahamisha walimu waliozidi hasa kwenye maeneo ya mijini na kuwapanga kwenye shule zenye uhaba mkubwa wa walimu ambazo nyingi zipo maeneo ya vijijini. Serikali itaendelea kuajiri na kuwapanga walimu kwenye shule za msingi na sekondari hasa zenye mahitaji makubwa kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.