Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Issa Ally Mchungahela

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Primary Question

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA Aliuliza:- Mradi wa maji wa Chipingo uliopo katika Jimbo la Lulindi ambao umegharimu Shilingi Bilioni 3.9 ni wa muda mrefu tangu mwaka 2013, lakini umekuwa hauna tija kwa kuwa hautoi maji; mabomba kupasuka mara kwa mara na mpaka sasa bado haujakabidhiwa kwa Serikali:- Je, Serikali inatoa kauli gani juu ya mradi huo?

Supplementary Question 1

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, ninayo maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikipoteza pesa nyingi sana, hasa kwenye miradi na miradi ya maji ikiwapo hasa huu mradi wa Chipingo. Hii imetokea mara nyingi kutokana na watendaji ambao sio waaminifu wakishirikiana na wakandarasi kuhujumu Taifa kwa kutotimiza majukumu ya mikataba yao. Je, Serikali ina tamko gani kuhusiana na suala hili? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, sina shaka na utendaji wa Wizara hii; Mheshimiwa Aweso pamoja na timu yake wanachapa kazi sana lakini wale watendaji wenu kule wanawaangusha. Je, Mheshimiwa Waziri au Naibu Waziri anakubali kuambatana na mimi kwenda kuangalia hali halisi mkajiridhisha kisha mkatatua changamoto hii kwa umakini kabisa? (Makofi)

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge Issa Mchungahela kutoka Jimbo la Lulindi, kama ifauatvyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara kwa sasa hivi tumekuwa tukifanya jitihada za kuona kwamba watendaji wanaendana na kasi ya hitaji la Wizara yetu kwa sababu, madeni yote na miradi ambayo imekuwa ya muda mrefu awamu hii tunaelekea kuikamilisha.

Mheshimiwa Spika, hivyo, napenda kumtoa hofu Mheshimiwa Mbunge kwa hawa watendaji ambao wanakiuka maadili yao ya kazi na kuweza kuwa wahujumu katika shughuli zao tayari tunawashughulikia na tayari tuna mkeka mpya wa Wahandisi ambao wanashindwa kutekeleza majukumu yao kadiri ambavyo tunahitaji watuvushe.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusiana na suala la kuambatana, Mheshimiwa Mbunge aondoe hofu. Hiyo ndiyo moja ya majukumu yangu na ninamhakikishia baada ya kukamilisha ziara yangu kwenye maeneo mengine, basi na hata huko Masasi pia nitakuja na nitajitahidi kufika kwenye majimbo yote kuona suala la maji linakwenda kupata muarobaini.