Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 8 Water and Irrigation Wizara ya Maji 110 2021-02-11

Name

Issa Ally Mchungahela

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Primary Question

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA Aliuliza:-

Mradi wa maji wa Chipingo uliopo katika Jimbo la Lulindi ambao umegharimu Shilingi Bilioni 3.9 ni wa muda mrefu tangu mwaka 2013, lakini umekuwa hauna tija kwa kuwa hautoi maji; mabomba kupasuka mara kwa mara na mpaka sasa bado haujakabidhiwa kwa Serikali:-

Je, Serikali inatoa kauli gani juu ya mradi huo?

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ally Mchungahela, Mbunge wa Jimbo la Lulindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Maji wa Chipingo upo katika Jimbo la Lulindi, Wilaya ya Masasi. Mradi huu ulianza kujengwa Aprili, 2013 na ni miongoni mwa miradi ambayo haikukamilika kwa wakati kulingana na mkataba. Katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi, Serikali ya Awamu ya Tano imefanya jitihada za kukamilisha mradi huu na hivi sasa mradi huo unatoa maji na upo katika hatua za majaribio ambapo vijiji 6 kati ya 8 ambavyo ni Manyuli, Chipingo, Mnavira, Chikolopora, Namnyonyo na Mkaliwala vinanufaika.

Mheshimiwa Spika, Vijiji viwili vya Rahaleo na Mapiri vya mradi huo bado havijaanza kupata huduma ya maji ambapo ujenzi wa mtandao wa maji kwa ajili ya vijiji hivyo unaendelea na unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa Machi, 2021.

Aidha, kuhusu suala la upasukaji wa mabomba katika kipande cha bomba kuu chenye urefu wa kilomita 1.2, Serikali inaendelea kusimamia maboresho yanayofanywa na mkandarasi kipindi hiki cha majaribio ya mradi ili wananchi waweze kupata huduma ya maji kama ilivyokusudiwa. Utekelezaji wa mradi umefikia asilimia 90.