Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Jafari Chege Wambura

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rorya

Primary Question

MHE. JAFARI W. CHEGE Aliuliza:- Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Daraja la Mto Mori kwani mto huo umekuwa ukisomba watu na kusababisha vifo kwa wananchi wanaofuata huduma upande wa pili?

Supplementary Question 1

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na pia kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, lakini nataka niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa daraja hili linaunganisha tarafa zaidi ya tatu kwa maana Tarafa ya Suba, Nyancha pamoja na Luo- imbo na ni muhimu sana kwenye uchumi wa muunganiko wa watu wanaoishi ndani ya tarafa hizi.

Je, Mheshimiwa Waziri haoni kuna umuhimu wa kuharakisha daraja hili kwa kuwa si tu linaharakisha uchumi, lakini pia ni sehemu ambayo wananchi wengi wamekuwa wakipoteza maisha wanapovuka kutoka upande mmoja kwenda upande wa pili?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, Mheshimiwa Waziri haoni sasa baada ya Bunge hili, kuna umuhimu sasa wa kuongozana mimi na yeye ili kwenda pamoja kule ndani ya jimbo kuona namna gani tunaweza tukatatua pamoja changamoto hii ili angalau wananchi hawa waweze kupata huduma hii kwa uharaka?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, Mbunge wa Rorya, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba daraja hilo ni muhimu sana kwa kuwa linaunganisha vijiji vingi na tarafa tatu katika Halmashauri ya Rorya na kiungo muhimu sana katika shughuli za kiuchumi na shughuli za kijamii katika eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoongea katika majibu yangu ya msingi kwamba Serikali inatambua sana umuhimu wa daraja hilo na ndiyo maana katika mwaka wa fedha ujao 2021/2022 Serikali itatenga fedha kwa ajili ya kufanya tathmini na usanifu ili kutambua shughuli ambayo inahitaji kutekelezwa na gharama za daraja hilo ili kadri ya upatikanaji wa fedha daraja hilo liwezwe kujengwa na kutatua changamoto hizo kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na suala la Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kuambatana na Mheshimiwa Mbunge naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tuko tayari wakati wowote kufika kushirikiana naye Mheshimiwa Mbunge. Baada ya kikao hiki tutapanga tuone ratiba bora zaidi ya kwenda kupita eneo hilo na kuona namna gani tunakwenda kuwahudumia wananchi.

Name

Joseph Kasheku Musukuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita

Primary Question

MHE. JAFARI W. CHEGE Aliuliza:- Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Daraja la Mto Mori kwani mto huo umekuwa ukisomba watu na kusababisha vifo kwa wananchi wanaofuata huduma upande wa pili?

Supplementary Question 2

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Matatizo yalioko katika Daraja la Rorya ni sawa kabisa na matatizo yaliyoko kwenye Jimbo la Geita Vijijini kwenye Daraja la Blengete, Kata ya Isilobutundwe na tumeshaandika maandiko mengi lakini hatujawahi kupata majibu. Je, Wizara au Waziri yuko tayari sasa baada ya Bunge hili kuongozana nami kwenda kuona ili aone umuhimu wa kutupatia pesa hizo?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kasheku Musukuma, Mbunge wa Geita Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge ameelezea daraja katika eneo hilo ni muhimu sana katika shughuli za kiuchumi za wananchi, lakini pia kwa shughuli za kijamii. Niwapongeze sana akiwemo mwenyewe Mheshimiwa Musukuma kwa jitihada za kufuatilia daraja hilo liweze kujengwa ili wananchi waweze kupata huduma. Naomba nimhakikishie kwamba, kadri ya upatikanaji wa fedha Serikali itaendelea kulipa kipaumbele eneo hilo la daraja na litaanza ujenzi pale bajeti itakapotengwa na fedha itakapopatikana.

Name

Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Primary Question

MHE. JAFARI W. CHEGE Aliuliza:- Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Daraja la Mto Mori kwani mto huo umekuwa ukisomba watu na kusababisha vifo kwa wananchi wanaofuata huduma upande wa pili?

Supplementary Question 3

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Naibu Spika, Ahsante Sana. Naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri swali la nyongeza. Daraja lililopo Jimbo la Moshi Vijijini lilisombwa na maji mwaka mmoja uliopita na daraja hili ni muhimu, linaunganisha kata nne katika Jimbo la Moshi Vijijini. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa daraja hili? Ahsante sana.

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Moshi Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua maeneo yote korofi ambayo madaraja yetu kwa namna moja ama nyingine yameathirika na mafuriko kutokana na mvua ambazo zimeendelea kunyesha hapa nchini. Serikali imeweka mkakati wa kwenda kufanya tathmini ya mahitaji katika maeneo hayo korofi ili kulingana na upatikanaji wa fedha, fedha ziweze kutengwa na madaraja hayo yaweze kujengwa au kufanyiwa marekebisho ili kuwezesha wananchi kupata huduma kama Serikali inavyodhamiria.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Moshi Vijijini kwamba eneo hilo Serikali inalitambua na tutakwenda kadri ya upatikanaji wa fedha kutenga bajeti kwa ajili ya usanifu, lakini pia kutenga bajeti kwa ajili ya ujenzi wa daraja hilo ili tuweze kurahisisha shughuli kwa wananchi.