Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 7 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 88 2021-02-10

Name

Jafari Chege Wambura

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rorya

Primary Question

MHE. JAFARI W. CHEGE Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Daraja la Mto Mori kwani mto huo umekuwa ukisomba watu na kusababisha vifo kwa wananchi wanaofuata huduma upande wa pili?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, Mbunge wa Rorya, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mto Mori unakatisha katika barabara ya Kirogo-Nyamaguku yenye urefu wa kilomita 15, ikiunganisha Tarafa za Luo-imbo, Suba na Nyancha katika Wilaya ya Rorya. Barabara hii ilifunguliwa mwaka 2008 kwa nguvu za wananchi kupitia Mpango wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).

Mheshimiwa Naibu Spika, Mto huu umegawanyika katika matawi mawili ambayo ni Mto Mori Mkuu wenye upana wa mita 43 na Wamala wenye upana wa mita 16 ambapo madaraja mawili (2) yanahitajika kujengwa. Hivyo, kwa sasa, barabara hii haipitiki kutokana na kutokuwepo kwa madaraja hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na umuhimu wa barabara hiyo, Halmashauri ya Wilaya ya Rorya imewasilisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI, maombi maalum ya Shilingi bilioni 1.54 ambayo ni makisio kwa ajili ya ujenzi wa daraja katika Mto Mori na matengenezo ya kawaida katika Barabara ya Nyamaguku- Kirogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali itatenga fedha kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kwa ajili ya usanifu wa madaraja mawili ya Mto Mori ili kufahamu mahitaji na gharama halisi za ujenzi wa madaraja hayo na kisha kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi. Aidha, ujenzi wa madaraja na miundombinu ya barabara hizi utatekelezwa kadri ya upatikanaji wa fedha.