Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Primary Question

MHE. JERRY W. SILAA Aliuliza:- Je, Serikali imefikia hatua gani katika utekelezaji wa Mradi wa Ujenzi wa Mwendokasi awamu ya tatu toka Gongolamboto mpaka Kariakoo ambao umeainishwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2020 – 2025?

Supplementary Question 1

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mradi huu katika mapendekezo ya awali ulikuwa ufike kwenye eneo la Pugu na kwa kuwa sasa mji umekua kwa kasi na wote mnafahamu Mkoa wa Dar es Salaam na Mkoa wa Pwani vimeungana, je, Serikali haioni ni wakati muafaka sasa kutekeleza mradi huu mpaka eneo la Pugu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kutumia historia ama matokeo ya mradi wa awamu ya kwanza kutoka Kimara mpaka Kariakoo na Posta wakati miundombinu imejengwa na sasa wafanyabiashara ndogo ndogo wanafanya biashara kwenye miundombinu hii mipya, je, Serikali haioni ni wakati muafaka sasa kuunganisha miundombinu ya mradi huu wa mabasi yaendayo haraka na masoko yatayoingiza wafanyabiashara kwenye maeneo haya ya vituo mlisho vya Banana, Mombasa na Gongolamboto? (Makofi)

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali ndugu yangu Mheshimiwa Jerry Silaa, Mbunge wa Ukonga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mawazo ni mazuri na tukifahamu kwamba Jiji la Dar es Salaam linazidi kutanuka, lakini design ya kwanza ilikuwa inatuelekeza tunaishia mahali fulani. Si hivyo tu, tulifikiria hata sehemu ya barabara inayoenda Mbagala, sasa hivi inaishia pale Mbagala Rangi Tatu, tulikuwa tunafikiria jinsi gani tutafanya tufike mpaka pale mbele ya Kongowe.

Kwa hiyo, haya yote ni mawazo mazuri, wataalam wetu wataendelea kuyafanyia kazi, lakini tuna phase one ya design, kama tutakuwa na variation yoyote tunaweza tukaifanya katikati ya kazi yetu lakini lengo letu ni kuhakikisha kwamba Watanzania wanapata huduma vizuri, hasa hii ya mwendokasi.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili la kuhakikisha haya mabasi yanapita katika vituo vya kutoa huduma; ni kweli na hata ukiangalia katika ujenzi wa soko letu la Kisutu pale Dar es Salaam, Ilala moja ya jambo kubwa ni kutengeneza daraja linalounganisha mwendokasi na kutengeneza soko. Wataalam wetu wa TANROADS na wale ambao wanafanya ujenzi walikuwa wanaendelea na kazi hiyo. Kwa hiyo, hilo jambo ni kipaumbele chetu kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, siyo hivyo tu, hata kuwa na pack maalum kwamba mtu akiondoka sehemu fulani anaweza akaacha gari lake na kuweza kusafiri. Hayo yote ni mambo ambayo tunayafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika awamu hii tutaenda kufanya maboresho makubwa kwa lengo kubwa miundombionu hii na usafiri wetu huu unakuwa safi na salama kwa wasafiri wote wa Jiji la Dar es Salaam.