Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Hasna Sudi Katunda Mwilima

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kigoma Kusini

Primary Question

MHE. HASNA S. K. MWILIMA aliuliza:- Vijana wengi wa maeneo ya Nguruka na Uvinza kwa ujumla biashara zao ni pikipiki na Polisi wamekuwa wakiwakamata na kuwatoza faini nyingi vijana hao bila utaratibu:- Je, Serikali haioni kuwa sasa ni wakati wa kulielekeza Jeshi la Polisi kuacha mara moja kuwasumbua vijana hao wa bodaboda ambao wanajipatia kipato kupitia bodaboda?

Supplementary Question 1

MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini, sambasamba na majibu yake ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, tunatambua kwamba bodaboda baadhi yao ni kweli huwa wanafanya makosa barabarani na wanapofanya makosa barabarani wanatozwa faini ya Sh.30,000, lakini hata magari pia wanapofanya makosa barabarani ambako ni matairi manne pia hutozwa faini ya Sh.30,000. Sasa kwa kuwa tozo hizi zinatokana na Kanuni na Mheshimiwa Waziri anayo mamlaka ya kubadilisha Kanuni wakati wowote, swali langu, kwa nini sasa Waziri asibadilishe Kanuni ili bodaboda yenye matairi mawili pamoja bajaji yenye matairi matatu waweze kupunguziwa tozo hii ya Sh.30,000 na hatimaye ishuke chini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, tunafahamu kwamba SUMATRA huwa wanatoza tozo ya Sh.22,000 kwa bodaboda, lakini Sh.25,000 kwa hiace na Sh.120,000 kwa mabasi. Ada hii imekuwa ni kubwa sana kwa watu wa bodaboda ukigawanya 25,000 kwa hiace abiria wako 15, ukigawanya hiyo unaipata kila abiria mmoja wa hiace analipa 1,666 lakini kwa bodaboda wanalipa 22,000, ukiigawanya kwa dereva na abiria inakuwa analipa 11,000 sasa swali langu, ni kama hili la kwanza, kwa nini sasa hizi Kanuni zisibadilike ili SUMATRA waweze kuwatoza angalau 10,000 kwa mwaka badala ya 22,000? (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili muhimu ya nyongeza ya Mheshimiwa Hasna Mwilima, Mbunge wa Kigoma Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nataka nichukue nafasi hii kulitaarifu Bunge lako Tukufu na umma kwa ujumla kwamba tupo katika hatua za mwisho katika Marekebisho ya Sheria ya Usalama Barabarani na tunatarajia mchakato huo utakapokuwa umekamilika sheria hiyo italetwa hapa Bungeni ili Waheshimiwa Wabunge tuweze kuijadili na hatimaye kuipitisha na sheria hiyo itakapokuwa imekamilika itapelekea vilevile kutoa fursa kwa Mheshimiwa Waziri kufanya mabadiliko ya Kanuni kulingana na Sheria itakavyokuwa imepitishwa na Bunge. Katika mambo ambayo tumeona kwamba ni muhimu kuyabadilisha katika Sheria ya Usalama Barabarani, moja, tumeona kwamba Sheria iliyopo sasa hivi inachangia ama inakwaza mapambano dhidi ya kupunguza ajali za barabarani nchini na moja katika jambo ambalo tuliona kwamba tutalipendekeza katika sheria hiyo ni juu yenu Waheshimiwa Wabunge kuona kama linafaa au halifai ni kuziangalia hizi tozo ambazo zinatozwa kwa hawa watu ambao wanafanya makosa ya usalama barabarani.

Mheshimiwa Spika, kama wataona kwamba tozo zilizopo sasa hivi ni ndogo na hivyo zinapaswa kuongezwa na kufanya hivyo pengine itasaidia kuwafanya waendesha vyombo hivi waogope, basi ni juu ya Waheshimiwa Wabunge na huo ndiyo mtazamo ambao nauona ni sahihi. Kwa mtazamo wangu mimi, nahisi kwamba baadhi ya waendesha vyombo vya moto wamekuwa wakifanya makosa kwa sababu wanaona wanaweza wakalipa hizi faini kwa kuwa ni kidogo na wanaweza wakalipa mara moja na wakaendelea na shughuli zao. kwa hiyo hili niseme kwamba kwa kuwa litakuja hapa Bungeni, tulipatie muda.

Mheshimiwa Spika, hili linakwenda sambasamba vilevile na swali lake la pili ambalo lilikuwa linazungumzia vilevile masuala ya tozo, ingawa hili la pili linahusiana na masuala ya SUMATRA ambayo kwa kuwa Serikali ni moja, basi nina hakika tutakaa pamoja na Wizara ya Uchukuzi ili kuona kwamba mambo haya mawili tutakwenda nayo vipi kwa pamoja.