Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Primary Question

MHE. QAMBALO W. QULWI (K.n.y. MHE. SUSAN A. LYIMO) aliuliza:- Je, Serikali inasema nini kuhusu ucheleweshaji wa kupata hati za kumiliki ardhi?

Supplementary Question 1

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, pamoja na majibu hayo ya Serikali ninayo maswali mawili ya nyongeza. Changamoto kubwa ya upatikanaji wa hatimiliki za ardhi ni pamoja na gharama kubwa zinazohusu upimaji wa maeneo. Jambo ambalo wananchi wengi wanalishindwa hasa pale ambapo upimaji unatakiwa ufanyike kwa kundi kadhaa kubwa la wananchi ili yapimwe kwa pamoja. Kwa nini Serikali isipunguze gharama hizo ili wananchi waweze kupata fursa ya kumiliki ardhi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Waziri wa Ardhi Mheshimiwa Lukuvi alipokuwa Karatu tarehe 07 Machi, mwaka huu aliagiza kufutwa kwa hatimiliki ya ekari 20 katika Kitongoji cha Ngorongoro, Ayalabe, Kata ya Ganako ambayo ilitolewa kinyemela kwa mtu binafsi. Hadi leo ni takribani miezi minne eneo hilo bado halijarudishwa kwa umma;

Je, nini kauli ya Wizara kwa Kamishna wa Ardhi Kanda ya Kaskazini ili kutekeleza agizo hilo la Waziri ambalo wananchi walilishangilia sana? Ahsante.

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza amezungumzia kwamba gharama za upimaji ni kubwa na hivyo wananchi wengi wanashindwa kulipa na wakati mwingine wanakuwa wako kundi kubwa wanaopimiwa. Naomba tu nimkumbushe Mheshimiwa Mbunge ya kwamba gharama za upimaji zimepunguzwa sana katika kipindi hiki cha miaka mitatu na huu mwaka wa nne tumeanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukikumbuka wakati tunaanza mwaka 2015/2016, gharama za upimaji zilikuwa juu sana zilikuwa wanachaji kwa ekari moja shilingi 300,000. Premium ilikuwa asilimia 15, ikapunguzwa ikawa asilimia 7.5 mwaka wa fedha uliofuatia. Kama hiyo haitoshi mwaka wa fedha uliofuatia 2017/2018 ikapunguzwa ikawa asilimia 2.5 na sasa hivi imepunguzwa ikawa asilimia moja. Maana yake ni kwamba zinakwenda zinapungua kutegemeana pia na uhitaji kama walivyosema.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tukumbuke hapa katikati tumekuwa na zoezi kubwa la urasimishaji ambalo limechangia katika kupima maeneo mengi sana. Wakati wanaanza gharama zilikuwa kubwa, zilikuwa kwenye kama 250,000 mpaka 300,000 lakini kwa sasa kuna watu wanapimiwa kiwanja kwa shilingi 60,000; kuna watu wanapimiwa kwa 150,000; kuna watu wanapimiwa kwa 90,000, mifano tunayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda Halmashauri ya Chemba nadhani wako kwenye 90,000; ukienda kwenye Halmashauri ya Mkinga wako kwenye 90,000; kwa hiyo zinakwenda zinashuka pia kutegemeana na uhitaji wa watu, kadri unavyokuwa na volume kubwa ya kazi na bei inapungua. Maeneo mengi sasa hivi yamepimwa kwa njia ya urasimishaji lakini katika kaya zinazopimwa kwa taratibu za kawaida gharama bado siyo kubwa kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amelalamikia.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili amezungumzia kufutwa kwa hatimiliki katika eneo la shamba moja katika Eneo Lake. Naomba niseme Mheshimiwa Waziri kutamka kwamba hati hiyo ifutwe ni jambo moja, lakini jambo la pili ni process pia kuhakikisha inafutwa na umiliki wake unaanza tena upya kwa namna itakavyokuwa. Unapofuta zile hatimiliki haina maana kwamba basi hapo hapo wanaanza kugawiwa, kuna utaratibu ambao lazima Mheshimiwa Rais aidhinishe na ikiidhinishwa inarudi kwa halmashauri husika na kuwekewa mpango maalum kwa ajili ya matumizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, haufutwi tu ukaletwa kwa wananchi moja kwa moja, unakuwa pia na maelekezo ya namna ya kupanga matumizi kutegemeana na mahitaji yalipo. Kwa hiyo, naomba nikuhakikishie tu kwamba ahadi iliyotolewa na Mheshimiwa Waziri iko pale pale na muda utakapokamilika basi tutawaletea utaratibu wa matumizi mtakayokuwa mmejiandalia.