Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 50 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 433 2019-06-21

Name

Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. QAMBALO W. QULWI (K.n.y. MHE. SUSAN A. LYIMO) aliuliza:-

Je, Serikali inasema nini kuhusu ucheleweshaji wa kupata hati za kumiliki ardhi?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Susan Anselm Lyimo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa hapo awali kulikuwepo na malalamiko ya ucheleweshaji wa upatikanaji wa hatimiliki za ardhi. Sababu kubwa iliyosababisha changamoto hiyo ni kuwepo kwa Kamishna mmoja tu kwa nchi nzima aliyeruhusiwa kutia saini hati kwa nchi nzima, hali hiyo ililazimu rasimu zote za hati kuwasilishwa Makao Makuu ya Wizara. Hata hivyo, tangu mwaka 2018 mpaka sasa Wizara imefanikiwa kuanzisha jumla ya Kanda 8 za usimamizi wa ardhi kwa ajili ya kutoa huduma mbalimbali ikiwemo hiyo. Utoaji wa hatimiliki za ardhi, upelekaji wa huduma za ardhi katika Ofisi za Ardhi za Kanda pamoja na kutumia mfumo wa kielektroniki katika utoaji wa huduma zimeondoa kwa kasi kubwa changamoto ya kuchelewesha utoaji wa hatimiliki kwa wanachi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na kuanzishwa kwa Ofisi za Kanda, Wizara imejenga Mfumo Unganishi wa Kutunza Kumbukumbu za Ardhi (Integrated Land Management Information System). Mfumo huu unalenga kurahisisha, kuharakisha na kupunguza gharama za utoaji huduma za ardhi. Kwa sasa tayari mfumo huo umeanza kutoa hatimiliki za kielektroniki katika Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni na Ubungo. Aidha, Serikali imekamilisha ufungaji wa mfumo huo katika Ofisi za Ardhi za Manispaa ya Ilala, Kigamboni na Temeka na utaanza kutumika kuanzia Julai 01, 2019. Serikali inaendelea na utaratibu wa kusimika mfumo huu katika halmashauri zote nchini kwa awamu.