Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Christopher Kajoro Chizza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buyungu

Primary Question

MHE. ENG. CHRISTOPHER K. CHIZA Aliuliza:- Serikali ilitoa zaidi ya shilingi bilioni mbili kwa ajili ya ujenzi wa miradi ya maji ya Nyabibuye, Gwanumpu, Muhange, Kiduduye, Nyangwijima na Kakonko Mjini. Miradi hiyo sasa inahitaji ukarabati mkubwa hata kabla ya kuanza uzalishaji na mingine utekelezaji upo chini ya asilimia 10:- (a) Je, ni kasoro gani zimesababisha miradi yote sita kutotekelezwa kwa mwaka uliopangwa? (b) Serikali imechukua hatua gani kuhakikisha miradi hiyo inakamilika?

Supplementary Question 1

MHE. ENG. CHRISTOPHER K. CHIZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza niishukuru sana Serikali kwa kuanza kutekeleza ahadi yak. Baada ya Waziri kutembelea na kusikia kilio cha wananchi imetenga shilingi milioni 300 na tayari wamepeleka shilingi milioni 20 na wataalam wameanza kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza. Katika lot ya miradi ya Kiduduye, Nyagwijima na Muhange, kwa kuwa tayari mradi wa Muhange unatekelezwa: Je, ni lini sasa Serikali itapeleka wataalam na fedha kwa ajili ya miradi miwili ya Nyagwijima na Kiduduye kuanza kutekelezwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Wakati Mheshimiwa Waziri wa Maji akihitimisha hotuba yake ya Bajeti ya mwaka huu, alituhamasisha Wabunge wote kupeleka orodha ya visima vinavyofaa kuchimbwa katika Majimbo yetu, nami nilikuwa wa kwanza kumkabidhi orodha ya visima 15 vilivyofanyiwa utafiti: Je sasa, Mheshimiwa Naibu Waziri anaweza kuniambia au kuwaambia wananchi wa Buyungu ni lini sasa ligi itapelekwa katika Jimbo la Buyungu kuanza kuchimba visima hivi 15? (Makofi)

Name

Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa ambayo anaifanya kwa muda mfupi tangu amechaguliwa na wananchi wake. Kikubwa amekuwa mfuatiliaji, nasi kama Wizara hatutakuwa kikwazo kum- support kuhakikisha tunatatua tatizo la maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya changamoto kubwa sana kusuasua kwa miradi ya maji kulikuwa kunatokana na wakandarasi wababishaji. Sisi kama Wizara ya Maji, tumejipanga, sasa hivi tumeanzisha Wakala wa Maji kwa maana ya RUWASA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie, kwa miradi ile ambayo imekuwa ikisuasua, tutaitekeleza kwa kutumia wataalam wetu wa ndani ili kuweza kukamilisha miradi ile kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, miradi hiyo tutaifanya kwa wataalam wetu na tutawa-support kuwapatia fedha ili miradi iweze kukamilika na wananchi wako, waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la ahadi ya visima, ahadi ni deni. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tukutane tufanye mazungumzo na wenzetu wa DDC ili tuwatume waende kuchimba visima kwa wananchi wake waweze kupata huduma hii muhimu ya maji safi na salama.