Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Primary Question

MHE. LOLESIA J. M. BUKWIMBA aliuliza:- Je, ni lini miradi ya usambazaji wa umeme katika Kata za Kamena, Nyamalimbe, Busanda, Nyakamwaga, Nyakagomba, Nyaruyeye, Kaseme, Magenge, Nyalwanzaja na Bujula katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita utaanza rasmi?

Supplementary Question 1

MHE. LOLESIA J. M. BUKWIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Kwanza nianze kwa kutoa shukrani kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa sababu utekelezaji utaanza mara moja mwaka huu Julai, 2016. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, kuna hizi huduma za jamii, shule za sekondari, zahanati, vituo vya afya ambavyo pia ni muhimu kuweza kupatiwa umeme. Napenda kujua sasa, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba pia vituo vya afya pamoja na zahanati na shule za sekondari zinapatiwa umeme huu? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, katika Bunge lililopita, la Kumi, Serikali iliahidi kwamba ingehakikisha vile vijiji vyote ambavyo vinapitiwa na nguzo za umeme juu, zinapatiwa umeme, lakini mpaka sasa hakuna hatua zozote zinazoendelea kuhakikisha wanapatiwa umeme. Katika Jimbo la Busanda pia kuna vijiji ambavyo vimepitiwa na nguzo juu lakini hazina umeme. Napenda kujua:-
Je, Serikali ina mpango gani sasa kuhakikisha kwamba vijiji hivi ambavyo vikiwemo Kijiji cha Buziba, Bunekezi na Naruyeye vinapatiwa umeme ili wananchi waweze kunufaika na huduma ya umeme? (Makofi)

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa kuna maeneo mengi ya ustawi kwa jamii ambayo pia yangepewa kipaumbele cha umeme kwenye mpango huu.
Niseme tu kwamba kwenye awamu ya kwanza na awamu ya pili ya (REA-Phase I na REA-Phase II), maeneo mengi sana ya Shule za Sekondari pamoja na hospitali yamepitishwa umeme. Hata hivyo kwenye REA-Phase III inayoanza mwezi Julai, naomba tu niungane na Mheshimiwa Bukwimba kwamba kama kuna shule za sekondari pamoja na vituo vya afya ambavyo havimo kwenye mpango huo na havikufanyiwa kazi kwenye awamu ya pili, naomba tufuatane naye baada ya Bunge lako ili tukabainishe maeneo hayo. Ahsante sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba sasa nijibu swali la pili la Mheshimiwa Lolesia Bukwimba, kuhusu vijiji vilivyopitiwa na nyaya za umeme lakini hazina umeme. Namhakikishiae Mheshimiwa Lolesia Bukwimba kwamba kwenye awamu inayokuja awamu REA-Phase III, kuna underground REA-Phase III. Maeneo ambayo yalipitiwa na nguzo za umeme lakini hayakupata umeme na yamo kwenye mpango wa umeme, yamekadiriwa kwenye nguzo za umeme under REA- Phase III, under REA Line, ambao pia ambapo itahusisha Vijiji vya Buziba, Bunekezi na maeneo ya jirani.
Mheshimiwa Spika, pia namwomba Mheshimiwa Bukwimba, kwa sababu tumeshirikiana naye sana kwenye masuala ya umeme kwenye Mkoa wa Geita, kama kuna vijiji vingine ambavyo havimo kwenye mpango huu, kadhalika baada ya Bunge hili, nionane naye ikiwezekana tukae sisi wawili tu, tujifungie, kuainisha maeneo hayo. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Kicheko)