Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Selemani Said Bungara

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kusini

Primary Question

MHE. SELEMANI S. BUNGARA aliuliza:- Kituo cha Afya Kilwa Masoko kinakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo uhaba wa watumishi, upungufu wa dawa, upungufu wa vitanda, magodoro, mashuka, vifaa tiba, kipimo cha sukari, kipimo cha damu, uchakavu wa majengo na pia kituo hicho hakina gari la kubebea wagonjwa hali ambayo ni kero kubwa kwa wagonjwa wanaohamishiwa Hospitali ya Wilaya iliyo umbali wa zaidi ya kilometa 25:- Je, Serikali ina mkakati gani wa kutatua changamoto zinazokabili Kituo hicho cha Afya ili kuondoa adha kwa wananchi?

Supplementary Question 1

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Mheshimiwa Spika, kwanza nakushukuru sana na ninakupongeza kwa kutupatia tablet hizi. (Makofi)

Pili, hili swali niliuliza mwaka 2016, lakini naishukuru Serikali leo wamejibu kwa vitendo. Kweli Kituo cha Afya Masoko sasa hivi utasema upo Ulaya, nashukuru sana. Pamoja na shukrani hizo; je, ni lini Serikali itatimiza au itakamilisha wafanyakazi 22 waliobakia ili kituo kiendane sawasawa na kilivyo? Swali la kwanza hilo.

Swali la pili; kwa kuwa hakuna gari maalum ya wagonjwa hiyo unayosema, lakini kwa kuwa umenipa matumaini kwamba mtatafuta gari nyingine: Je, lini hiyo gari ya Kituo cha Afya cha Kilwa Masoko itapatikana?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, niruhusu nipokee pongezi za Mheshimiwa Bungara, maana huwa zinatolewa mara chache sana. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la kwanza anauliza ni lini upungufu wa watumishi 22 utatatuliwa ili hadhi ya Kituo cha Afya ambacho anasema ni sawa na kuwa Ulaya kitaweza kutoa huduma kukiwa na ikama ambayo inatakiwa?

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kama ambavyo ameendelea kuiamini Serikali ya CCM ikiahidi inatekeleza na utekelezaji ni pamoja na swali ambalo aliliuliza, nami nampongeza kwa kuuliza swali na Serikali tumemjibu kwa vitendo. Naomba nimhakikishie ni azma ya Serikali kuhakikisha maeneo yote ambayo Vituo vya Afya vimefunguliwa tunapeleka watumishi kwa kadri nafasi za ajira zinavyopatikana na Kilwa hatutasahau.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili anaulizia suala la kuwepo gari. Gari lililopo aina ya Maruti linafanya kazi, lakini kama tulivyokiri katika majibu yetu kwamba ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba tunapata gari zuri zaidi kwa kushirikiana Halmashauri yake, ni vizuri nao katika bajeti; maana kama kuna Halmashauri ambayo inafanya vizuri katika makusanyo ni pamoja na Halmashauri yake maana zao la ufuta linaingiza fedha nyingi. Ni vizuri nao Halmashauri wakatenga na sisi Serikali tukashirikiana ili gari ziweze kupatikana kwa ajili ya wananchi.