Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 1 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 3 2019-11-05

Name

Selemani Said Bungara

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kusini

Primary Question

MHE. SELEMANI S. BUNGARA aliuliza:-

Kituo cha Afya Kilwa Masoko kinakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo uhaba wa watumishi, upungufu wa dawa, upungufu wa vitanda, magodoro, mashuka, vifaa tiba, kipimo cha sukari, kipimo cha damu, uchakavu wa majengo na pia kituo hicho hakina gari la kubebea wagonjwa hali ambayo ni kero kubwa kwa wagonjwa wanaohamishiwa Hospitali ya Wilaya iliyo umbali wa zaidi ya kilometa 25:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutatua changamoto zinazokabili Kituo hicho cha Afya ili kuondoa adha kwa wananchi?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Selemani Said Bungara, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Kilwa Masoko kilipatiwa kiasi cha shilingi milioni 500 katika mwaka wa fedha 2017/2018 kwa ajili ya ukarabati na upanuzi ambapo ujenzi na ukarabati wa majengo sita ya kituo umekamilika. Aidha, baada ya ujenzi na ukarabati kukamilika, kituo kimepokea vifaa tiba mbalimbali kwa ajili ya kuboresha huduma hususan za upasuaji ambapo hadi Oktoba, 2019 kituo kimepokea vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi 332,916,070/=. Hali ya upatikanaji wa dawa zote muhimu (Tracer medicine) katika Kituo cha Masoko ni asilimia 87.

Mheshimiwa Spika, kituo kina jumla ya watumishi 30 wa kada mbalimbali za Afya ikiwa ni upungufu wa watumishi 22. Kituo kina nafasi ya vitanda 55, vitanda vilivyopo ni 31 na mashuka 126. Idadi ya vitanda vilivyopo vinakidhi mahitaji kwani kwa sasa kituo kinapokea wagonjwa wa kulazwa angalau watano kwa siku. Kwa sasa Halmashauri ina gari maalum ambalo hutumika kubeba wagonjwa katika kipindi cha dharura.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutafuta rasilimali fedha za kutatua changamoto zilizopo ikiwa ni pamoja na kununua gari la wagonjwa kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Kilwa Masoko.