Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:- Je, ni kwa namna gani Wakala wa Misitu (TFS) inashirikiana na Mamlaka za Serikali za Mitaa, hususan Wilaya katika kusimamia misitu hapa nchini?

Supplementary Question 1

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Baada ya kusema hayo, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, misitu ni uhai na kama misitu ni uhai, kila mmoja wetu ana jukumu la kulinda misitu. Pamoja na jitihada nzuri za Serikali, ningependa kufahamu kwamba kumekuwepo na utaratibu wa kusafirisha magogo kwenda nje ya nchi; hii pia ni mojawapo ya chanzo cha uharibufu wa mazingira.

Mheshimiwa Spika, nataka kufahamu jitihada za Serikali katika kuhakikisha kwamba inalinda misitu yetu na misitu hii iendelee kutulinda na sisi Watanzania.

Mheshimiwa Spika, itakapofika mwaka 2022 tunafahamu kwamba bwawa la Mwalimu Nyerere la kuzalisha umeme litakamilika na ni dhahiri kwamba litapunguza gharama kubwa za umeme. Vile vile tukitumia gesi yetu itakuwa ni njia mojawapo pia ya kupunguza uharibifu wa mazingira.

Mheshimiwa Spika, nataka kufahamu mkakati wa Serikali katika kuhakikisha kwamba gesi tuliyojaaliwa na Mwenyezi Mungu hapa nchini inafanya jitihada gani kuhakikisha kwamba wananchi wanaingia katika zoezi zima la kutumia gesi kuweza kulinda mazingira yetu? Nini jitihada za haraka za Serikali?

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri sana kwa mwuliza swali. Pia nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge kufuatilia matumizi ya gesi katika mkakati wa kupunguza uharibifu wa mazingira.

Mheshimiwa Spika, ni kweli, kwanza mkaa unaoingia katika Jiji la Dar es Salaam kwa kila siku ni zaidi ya magunia 400,000 mpaka 500,000 na hiyo yote inahusisha ukataji wa miti na kuharibu mazingira. Vile vile kuni zinazotumika vijijini pamoja na mkaa ni zaidi ya wananchi zaidi ya asilimia 71. Sasa mkakati ulipo kwa sasa ni kuhakikisha kwamba gesi hii inatumika katika shughuli za majumbani ili kupunguza ukataji wa miti unaoharibu mazingira.

Mheshimiwa Spika, hivi sasa kwa niaba ya Watanzania wanaosikiliza, zaidi ya wananchi 600 wameshaanza kutumia gesi na wiki iliyopita nimeunganisha gesi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa wafanyakazi 110 na cafeteria nne zimeanza kutumia gesi. Huu ni mkakati mzuri sana wa kupambana na mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongeze tu, awamu ya pili tunakwenda katika mikoa yote ya Tanzania Bara kwa kuanza kusafirisha mitungi iliyoshindiliwa na gesi na kujenga mabomba katika mikoa hiyo ili nako kuanza kusambaza katika vijiji vyote ikiwa ni harakati ya kupunguza uharibufu wa mazingira.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la kwanza la Mheshimiwa Amina Mollel. Kwanza naomba nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Amina Mollel ambaye ni Balozi wetu wa Utalii kwa kazi nzuri sana ambayo anaifanya. Mheshimiwa Amina Mollel alipata hati ya kutambuliwa kama Balozi wa Utalii wakati wa Maadhimisho ya Miaka 60 ya Ngorongoro na Serengeti na anafanya kazi nzuri sana yeye pamoja na wenzake. Nampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Amina Mollel ametaka kujua, kwa nini Serikali inaendelea kuruhusu usafirishaji wa magogo nje ya nchi wakati usafirishaji huu ni chanzo kikubwa sana cha uharibifu wa mazingira? Ni kweli kwamba hapo awali Serikali ilikuwa ikiruhusu usafirishaji wa magogo ya miti migumu nje ya nchi lakini kwa takribani miaka mitatu sasa, Wizara ilizuia usafirishaji wa magogo ambayo hayajaongezewa thamani kwenda nje ya nchi. Ni nia ya Wizara kuona kwamba mauzo yoyote ya mazao ya misitu nje ya nchi yanakuwa ni mauzo ya mazao yaliyoongezewa thamani. Kwa hiyo, jitihada hizo katika Wizara zinaendelea na sasa hivi tumefunga uuzaji wa magogo hayo na tutakapofungua tutatoa masharti na maelekezo ya namna ya kufanya biashara hiyo. Ahsante sana. (Makofi)