Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 7 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 89 2020-02-05

Name

Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-

Je, ni kwa namna gani Wakala wa Misitu (TFS) inashirikiana na Mamlaka za Serikali za Mitaa, hususan Wilaya katika kusimamia misitu hapa nchini?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Taarifa ya Tathmini ya Rasilimali za Misitu Tanzania (National Forest Resources Monitoring and Assessment - NAFORMA) ya mwaka 2015, Tanzania ina rasilimali za misitu zinazokadiriwa kufikia hekta milioni 48.1 ambapo asilimia 34 inasimamiwa na Serikali Kuu, asilimia 6.5 inasimamiwa na Halmashauri, asilimia 45.7 inasimamiwa na vijiji, asilimia 7.3 inasimamiwa na Sekta Binafsi na asilimia 6.0 ya misitu iko katika ardhi huria (general land). Kulingana na taratibu za Serikali, misitu ya Tanzania inasimamiwa kwa mujibu wa Sheria ya Misitu Na. 14 ya Mwaka 2002.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria hiyo, Mamlaka za Usimamizi wa Misitu Nchini zipo katika Wizara mbili, nayo ni Wizara ya Maliasili na Utalii ambayo imekasimu mamlaka hayo kwa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) ambapo una jukumu la kusimamia misitu ya Hifadhi ya Serikali Kuu na misitu mingine yote ambayo haijahifadhiwa kisheria; na Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) inayosimamia misitu iliyopo chini ya Mamlaka za Serikali za Mitaa (Halmashauri na Vijiji).

Mheshimiwa Spika, kwa tafiti zilizopo, misitu ya Tanzania inakabiliwa na changamoto kubwa mbili; kwanza, uharibifu mkubwa wa misitu ambao kwa sasa umefikia kiasi cha hekta 470,000 kwa mwaka; na pili, mahitaji ya mazao ya misitu yanayozidi uwezo wa misitu kwa zaidi ya meta za ujazo millioni 19.5. Ili kukabiliana na changamoto hizo, Serikali imeendelea kufanya jitihada za pamoja kati ya Wizara hizi mbili zinazosimamia rasilimali za misitu. Kupitia ushirikiano huo, Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia taasisi yake ya TFS imekuwa ikishirikiana na Mamlaka za Serikali za Mitaa katika kutatua changamoto hizo.

Mheshimiwa Spika, kupitia mpango huo wa pamoja, Wizara ya Maliasili na Utalii na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa tumekubaliana kushirikiana katika maeneo mbalimbali ambayo ni pamoja na kuimarisha usimamizi wa misitu na ufuatiliaji wa miradi inayofadhiliwa na Mfuko wa Misitu Tanzania. Ushirikiano huo unashirikisha ngazi ya wilaya ambapo Mwenyekiti wa Kamati ya Uvunaji wa Mazao ya Misitu katika Wilaya ni Mkuu wa Wilaya.

Mheshimiwa Spika, aidha, Afisa Misitu wa Halmashauri ya Wilaya ni Mjumbe wa Vikao vya Uvunaji na ndiye anayetoa leseni za uvunaji wa mazao ya misitu katika Wilaya husika. Vilevile, ushirikiano mwingine upo katika kutoa elimu kwa Umma, kuhifadhi misitu kwa njia shirikishi, kuanzisha magulio ya mkaa na kusimamia doria za kudhibiti uvunaji na usafirishaji haramu wa mazao na bidhaa za misitu.

Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha ushirikiano huo, tarehe 26 Mei, 2016 Wizara ya Maliasili na Utalii ilisaini Mkataba wa Makubaliano na Ofisi ya Rais, TAMISEMI ya kuimarisha zaidi ushirikiano katika usimamizi wa misitu nchini na utawala bora. Kufuatia makubaliano hayo, vikao vya pamoja katika ngazi ya wilaya vya kujadili utekelezaji vimekuwa vikifanyika kila mwaka ili kuchambua changamoto mbalimbali.

Mheshiwa Spika, kwa ujumla utunzaji na uendelezaji wa misitu nchini unakabiliwa na changamoto mbalimbali kulingana na mazingira ya mikoa na wilaya husika.

Hata hivyo, Serikali kupitia Wizara hizi mbili itaendelea kuweka mikakati mbalimbali ili kuwezesha rasilimali za misitu kuendelea kutumika kwa kufuata taratibu zilizopo ili rasilimali hizo zinufaishe vizazi vya sasa na vijavyo.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)