Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Marwa Ryoba Chacha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Serengeti

Primary Question

MHE. MARWA R. CHACHA (K.n.y. MHE. AGNESS M. MARWA) aliuliza:- Nyumba nyingi za Vijijini hazikuwekewa umeme wakati wa usambazaji japo baada ya kuweka umeme kumekuwa na ongezeko la ujenzi wa nyumba na uzalishaji mali kama ujasiriamali. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha nyumba zote zilizobaki zinapata umeme kabla mradi wa REA haujamaliza muda wake?

Supplementary Question 1

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Spika, ahsante naomba kwanza nichukue nafasi, nimshukuru Mheshimiwa Waziri, na Naibu wake Waziri wanafanya kazi nzuri sana, na ni kazi ambayo itaisaidia sana CCM 2020 tunakoenda kwenye uchaguzi.

Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza, swali la kwanza Mheshimiwa Waziri wa Nishati alipokuja Serengeti mwaka huu mwanzoni alihaidi maeneo ya yafuatayo yatapa umeme; shule ya Sekondari Inagusi ilipo Kata ya Isenye, Kijiji cha Nyamatoke na Mosongo vilivyopo Kata ya Mosongo pamoja na Kiyakabari Kata ya Stendi Kuu.

Ni lini maeneo haya yatapata umeme ambao ulihaidiwa na Mheshimiwa Waziri?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni lini TANESCO au REA watapeleka umeme Kata ya Morotonga katika Vitongoji vya Mutukura na Romakendo?

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza tupokee pongezi zake, lakini naamini pongezi ni kuhitaji zaidi huduma. Kwa hiyo, tumepokea kwa ahadi kwamba tutaendelea kufuatilia hiyo miradi. La pili pia nimpongeze yeye Mheshimiwa kwa namna ambavyo anavyofuatilia masuala ya nishati katika Jimbo lake na sekta mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, lakini masuala yake mawili yamejielekeza kwanza kwenye ziara ambayo imefanywa na Mheshimwia Waziri wa Nishati katika Jimbo la Serengeti na ahadi aliyoitoa katika shule ya Sekondari Nagusi na maeneo ya Kiyabakari. Nataka nimthibitishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Mheshimiwa Waziri wa Nishati alipotoa ahadi hii alikuwa na uhakika wa utekelezaji wa mradi wa REA Awamu ya III mzunguko wa kwanza unaoendelea na kwamba mkandarasi Derm wa Mkoa wa Mara ni miongoni mwa wakandarasi wanaofanya vizuri tulivyo wa-rank na kwamba inatarajiwa itakamilisha kazi kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, maeneo aliyoyataja mara tu Julai 2019 mradi wa REA Awamu ya III unaanza na kazi ndiyo itafanyika. Kwa hiyo nimthibitishie Mheshimiwa Mbunge kwa kipindi hiki cha kuendelea 2019 maeneo haya yote ataiona kazi inaanza na nguzo zitapelekwa na ninaomba nimuelekeze mkandarasi Derm azingatie maelekezo ya Mheshimiwa Waziri pamoja na Meneja wa TANESCO wa Mkoa wa Mara na msimamizi wa mradi wa REA katika Mkoa wa huo.

Mheshimiwa Spika, swali la pili Mheshimiwa Mbunge ameulizia masuala la kwa mfano Marotonga na eneo ambalo umelitaja Mgumu Mjini, yanaonyesha haya maeneo ni ya ujazilizi. Kama nilivyosema kwenye jibu la msingi Mheshimiwa Agnes Serikali baada ya kuona pana changamoto baada ya miradi ya REA kukamilika na kwa kuwa lengo lake Serikali ni kusambaza umeme palikuwa na changamoto ya gap ya usambazaji wa umeme. Na ndiyo maana ikabuni mradi wa ujazilizi na bahati nzuri Mkoa wa Mara ulikuwemo katika ujazilizi Awamu ya kwanza ambao ulikuwa kama mradi wa majaribio.

Mheshimiwa Spika, na Serikali imekuja na mradi wa ujazilizi Awamu ya pili, Awamu ya II(a) ambayo itakuwa na Mikoa tisa na Awamu ya II(b) itakuwa na Mikoa 16, ikiwemo Mkoa wa Mara na kwa kweli tunauhakika Awamu ya II(a) utafadhiliwa na Serikali za Norway, Sweden na Umoja wa Ulaya na hela zake tunazo bilioni 197 na Awamu ya II ya ujazilizi two (b) itafadhiliwa na Serikali ya Ufaransa mpaka sasa tunauhakika wa kiasi cha bilioni 270 kati ya bilioni 400 ambazo zitaanzia kazi na mchakato tupo hatua ya manunuzi na mradi huu utaanza 2019/20 kwa ajili ya kufikisha umeme katika maeneo ya Vitongoji ili kuweza kusambaza umeme, nikushukuru sana.